Malaika Wa Shetani

Malaika Wa Shetani

17.
“Unamfikiriaje?”

“Nani?”

“Rais.”

Joram akatabasamu kidogo kabla hajaongeza, “Sikia Nuru, Rais wa Kiafrika sio mtu wa kujadiliwa na mtu kama mimi na wewe mahala kama hapa. Tunaweza kesho tukajikuta mahabusu, badala ya hotelini, kujibu maswali yasiyoeleweka.”

Nuru naye alicheka. “Usinidanganye Joram,” alisema baada ya kicheko hicho kizuri. “Najua unahitaji muda wa kufikiri. Ameivuruga akili yako. Ulichotegemea sicho ulichokikuta. Akasita tena. Alipomwona Joram yuko kimya akaongeza, “Hata mimi sina budi kusema kuwa amenishangaza. Tulivyopokelewa nyumbani kwake badala ya Ikulu nilidhani ameamua kutusimulia hicho alichotuitia. Sasa utafanyeje, Joram?”

Kama alitegemea jibu, basi alikosea sana. Badala yake Joram alimshika mkono na kumwongoza kwenye lifti ambayo iliwapandisha hadi ghorofani kilikokuwa chumba chao. Chumbani aliendelea kuyakoroga maswali yote ya Nuru juu ya Rais huyo. Ulipofika wakati wa mlo walikuwa wa kwanza kufikia





chumba cha maakuli. Walikula huku wakitazama televisheni ambayo ilikuwa ikionyesha kikundi cha utamaduni kilichokuwa kikiwatumbuiza wageni fulani uwanja wa ndege. Wageni hao walipopita baada ya kuwatazama wachezaji kidogo, kikundi hicho kilisahauliwa na umuhimu kuhamishiwa kwa wageni. Historia zao za nchi zao zilisimuliwa, zikafuatiwa na majibu yao kwa waandishi wa habari. Joram aliyatazama yote hayo ilihali hayaoni. Mara baada ya mlo na bia mbilimbili za kuteremshia aliushika tena mkono wa Nuru na kumwongoza chumbani, ambako sasa alitulia kama awali; akiendelea kutafakari.

Kwa muda aliusahau mkasa huo na kujifikiria mwenyewe. Alikosa nini kwa Mungu hata apewe moyo huu wa kufuatilia mambo yasiyomuhusu ambayo mara zote uifanya roho yake iponee chupuchupu? Kitu gani kilichomwambukiza ugonjwa huu hatari? Tamaa ya kufichua kila siri, kiu ya kumfichua kila mwenye hatia, njaa ya kumpokonya silaha kila mwenye nia mbaya unapochanganyika na uroho wa kushuhudia mibabe iliyokubuhu ikilia hadharani; kama si ugonjwa ni nini?

Joram hakuweza kukumbuka ni lini na nani alimwambukiza maradhi hayo. Yako magonjwa mengine ambayo mwanaume huzaliwa nayo. Pengine Joram ni mmoja wao.

Baba na mama yake wasingesahau jinsi mtoto wao huyu pekee alivyokuwa machachari tangu alipokuwa na umri wa miaka mitatu. Akiwa mtoto aliyepatikana baada ya miaka saba ya kutafutwa kwa namna zote, madaktari na wahenga walishirikishwa, alipopatikana alikuwa kama mboni ya jicho kwa baba na yai la dhahabu kwa mama. Kila mmoja alipenda kumlea kutwa. Lakini iliwashangaza kuona kwamba mtoto huyu hakupenda kabisa kubebwa. Kila aliposhikwa mikononi alisumbua kwa kurusha viteke na vigumi hata akarejeshwa kitandani ambako alitulia.
 
18.
Hayo yalifuatwa na jinsi alivyoanza kutambaa, kusimama na hatimaye kutembea akiwa katika vikundi vya watoto wakubwa zaidi akishiriki katika michezo na maongezi. Alikuwa hodari katika kila kitu, jambo ambalo lilimfanya apendwe na watu mbalimbali, shuleni na mitaani. Katika vikundi hivyo mara nyingi alionekana kama kiongozi na msemaji mkuu. Hata katika timu zao za mpira, mchezo ambao hakuumudu kama mingine, bado alichaguliwa kuwa kiongozi.

Huyo ndiye Joram Kiango utotoni, utoto ambao aliupitisha





katika mitaa ya California nchini Marekani ambako baba yake alikuwa akifanya kazi kwa Mzungu mmoja aliyeondoka naye hapa nchini kukimbia ‘adha ya uhuru’ mara tu ulipopatikana. Shule zilimpa Joram elimu nzuri. Alijipatia shahada ya M.A katika historia, fasihi na siasa. Mara akaliacha somo hilo na kuanza kusomea Sayansi. Kabla ya kuhitimu aliamua kuacha masomo na kutulia nyumbani, muda wake mwingi akiutumia katika mazoezi ya kareti, ngumi na sarakasi. Haya pia aliyaacha na kukaa bure.

Hakuwa mzigo kwa wazazi wake. Kwa kweli walipenda sana mtoto wao akae nao muda wote, hasa baada ya daktari kuwahakikishia kuwa Joram alikuwa yai pekee lenye uhai katika tumbo la mama yake. Hata hivyo, iliwashangaza kuona kuwa pamoja na mtoto wao kuwa mtu mwenye hekima na uwezo wa hali ya juu katika mambo mbalimbali, bado alikuwa kama mtu ambaye hakujua alihitaji nini katika maisha yake. Hata kati ya wasichana wengi ambao alikuwa akiwaleta nyumbani hakuonyesha dalili ya kumpenda yeyote. Aidha, kila aliyediriki kuzidisha dalili za mapenzi Joram alimwepuka mara moja. Hilo lilimtia hofu mama yake. Hakuona kama Joram angekuwa mtu wa kuoa na kutulia kama watu wengine. Asingependa kufa kabla ya kumwona mjukuu. Zaidi angependa Joram achukue jukumu ambalo yeye alishindwa kulitekeleza, aijaze nyumba kwa watoto.

Hakubahatika kuishi hadi hilo litokee.

Siku moja Joram alikwenda disko ambako alichelewa hadi saa nane za usiku. Aliporudi nyumbani alishangaa kukuta taa zinawaka, wazazi wake wakiwa nje wakimsubiri. Baba yake alikuwa akivuja damu puani na mdomoni.

“Kuna nini?” aliwauliza. “Tumeibiwa,” walimweleza.
 
19.
Majambazi manne yenye silaha yaliivamia nyumba yao na kumpiga baba yake, kisha yakamlazimisha kutoa pesa zote alizokuwa nazo humo ndani. Yalipozipata yalichukua pia televisheni na kinyago chao kikubwa, kinyango ambacho kilimshangaza kila mtu mjini hapo kwani kilikuwa mwanzo wa uchongaji wa vinyago dhania vya mashetani. Mmakonde huyo alikuwa amechonga binadamu mwenye vichwa sita, akiwa ameinama kulipapasa tumbo lake. Hiyo ilikuwa amali yao pekee ambayo iliwapa sifa katika mtaa huo kiasi cha kuwafanya





wajivunie nchi yao, kila walipoulizwa msanii gani aliyeweza kuchonga kitu kama hicho na alitumia vifaa gani.

Joram aliyasikiliza maelezo ya wazazi wake kwa makini. Aliwauliza maswali mawili, matatu kwa nia ya kuelewa dalili za watu hao. Wazazi wake hawakuwa na maelezo marefu. Lakini huo haukuwa mwisho wa maswali ya Joram. Alipeleleza kwa urefu katika majumba ya sanaa, kuulizia kama kuna watu waliokuwa wakiuza aina fulani ya kinyago. Majibu yalimjia toka New York, kwa simu kuwa kinyago alichohitaji kililetwa hapo na wauzaji ambao hawana ujuzi na vinyago wala sanaa kwa ujumla. Alipaa hadi mjini hapo. Aliporudi alikuwa na anuani kamili ya watu aliowahitaji. Usiku wa siku iliyofuata aliwatembelea ghafla. Aliwakuta wawili kati yao. Walipomwona, kijana mdogo kiumri, akiwa mikono mitupu walimcheka na kumdhihaki. Lakini walishangaa kuona akidiriki kuwarushia makonde yaliyokuwa mazito kuliko umri wake. Walishangaaa zaidi kuona akikwepa kila konde walilomrushia. Muda mfupi baadaye, walijikuta hoi, hawajitambui. Hivyo, hawakua na upinzani Joram alipowaburura hadi nyumbani kwao, wakiwa wamekibeba kinyago hicho. Nyumbani aliwalazimisha kuwapigia magoti na kuwalamba miguu wazazi wake. Baada ya hapo aliwafukuza.

Kuwafukuza badala ya kuwapeleka polisi, kama wazazi wake walivyomshauri, lilikuwa kosa ambalo Joram atalijutia hadi siku ya kwenda kaburini; kwani usiku wa siku ya pili yake nyumba yao ilitembelewa na majambazi hayo. Safari hii hayakuja kwa mzaha. Yaliifunga milango yote kwa nje na kuimwagia petrol nyumba nzima, kisha yakailipua moto. Ulikuwa moto mkali ambao uliwachukua zima moto saa kadhaa kuuzima. Hata hivyo, hawakufaulu kuyaokoa maisha ya baba na mama Joram Kiango. Walikutwa wamefia bafuni baada ya juhudi zao za kuzima moto kwa maji ya bomba kutozaa matunda.
 
20.
Joram hakuyaamini macho yake alipofika nyumbani toka kokote alikokuwa na kukuta maiti mbili zilizoungua zikibebwa na polisi kupelekwa katika gari la wagonjwa lililokuwa nje. Wala hakuelewa chochote pindi majirani walipoanza kumpa pole na kumkaribisha nyumbani kwao. Kwake ilikuwa kama moja ya zile ndoto mbaya ambazo humtukia mtu kushuhudia jambo la kusikitisha. Hivyo, alijitoa katika mikono yenye huruma ya majirani hao na kuendelea kuitazama ‘picha’ hiyo ya kutatanisha.





Tahamaki fahamu zake zilioana na hali halisi. Akaanza kulewa. Ikampambazukia kuwa miili iliyokuwa ikipakiwa katika gari hilo ilikuwa ya wazazi wake.

Bado hakujisikia chochote. Damu yake ilikuwa imetulia, fahamu zikiwa kimya. Chochote alichotegemea kuwa humwingia au kumtoka mtu ambaye amewahi kushuhudia kifo cha aina hiyo kwa wazazi wake yeye hakukihisi. Ubaridi ambao amesoma vitabuni kuwa humwingia mtu hadi rohoni yeye hakuusikia. Machozi ambayo ameyaona mara nyingi katika macho ya watu yeye hayakumtoka. Alikuwa kimya kama alivyokuwa. Angeweza kucheka, angeweza kulia, lakini hakufanya lolote zaidi ya kutulia kimya, akitazama.

Ukimya na utulivu wake uliwashangaza majirani na kuwatisha polisi ambao walikuwa wakisubiri kuzungumza naye. Jirani walizoea mtu anayeomboleza, si huyu asiyeeleweka. Askari wangependa kumtupia maswali mtu anayebabaika, si aliyetulia kama huyu. Hata hivyo, askari mmoja alimshika mkono na kumwongoza mtaa wa pili ambako kulikuwa na baa. “Listen, you need a drink,” alimwambia akimwagizia pombe kali. Joram aliipokea na kuinywa taratibu. Kisha, askari alianza kumwuliza maswali ambayo yalikuwa yakimtatiza muda wote huo. “Unaweza kukisia nani aliyetenda kitendo cha kinyama kama hiki?” Aliuliza kwa upole. Joram hakumjibu. “Au hujawa tayari kuzungumzia suala hili… unajua, tungependa kuwakamata mapema.” Aliongeza. Joram hakumjibu. Badala yake aliaga kwamba anakwenda kujisaidia.

Askari huyo alisubiri hapo kwa dakika ishirini. Hakuamini. Wasiwasi ulipomzidi alimfuata Joram maliwatoni. Hakumkuta. Wanywaji aliowauliza kama wamemwona hawakuwa na la kumjibu. Alihangaika huko na huko bila mafanikio. Ikamlazimu kurudi kituoni kutoa taarifa.

Alfajiri hiyohiyo maiti mbili ziliokotwa nyuma ya nyumba moja ambayo iliungua moto. Marehemu waliuawa kwa mikono baada ya kupigwa na kuvunjwavunjwa viungo. Mwuaji hakuonekana. Lakini uchunguzi ulionyesha kuwa marehemu walikuwa miongoni mwa magaidi manne yaliyokuwa yakiisumbua sana wilaya hiyo kwa wizi na mauaji. Mara mbili tatu yaliwekwa ndani kwa makosa madogomadogo. Ushahidi mzuri wa kuyaweka kizimbani au kitanzini ulikuwa haujakamilika. Hivyo, kufa kwa
 
21.
wawili kati yao haikuwa habari mbaya sana kwa polisi japo wangependa zaidi kumfahamu mtu aliyewasaidia kazi hiyo.

Mtu wa tatu katika kikundi hicho aliokotwa siku chache baadaye, akiwa maiti; katika kitongoji fulani. Yeye pia aliuawa kwa mikono ingawa alikuwa na majeraha mengi mwilini. Polisi waliwaagiza wafungwa kumzika, kisha walianzisha upelelezi mkali kumtafuta mtu aliyehusika na mauaji hayo. Haikuchukua muda kugundua kuwa mwuaji alikuwa Joram Kiango ambaye alikuwa akilipiza kisasi dhidi yao kwa madai kuwa ni wao waliwateketeza wazazi wake kwa moto. Msako mkali ukaanzishwa dhidi ya Joram. Vyombo vya habari vikapewa jina na picha na kumtangaza kama mtu hatari.

Polisi hawakuwa na haja ya kujisumbua kumtafuta. Siku chache alionekana katika kituo cha treni akiwa na mateka wake ambaye alifungwa kamba. Wote walikuwa mahututi. Joram alikuwa taabani kwa majeraha mengi ya visu na risasi, ambayo yalianza kuvunda kwa kutopatiwa matibabu halisi. Mateka wake pia alikuwa hoi kwa kipigo ambacho alikipata tangu walipoanza mapambano. Walivutana hadi katika kituo cha polisi ambapo Joram alimwamuru mateka wake kujieleza kwa mara nyingine jinsi walivyoshoriki kuwaangamiza wazazi wake. Mbele ya polisi jambazi hilo lilijaribu tena kukataa, jambo ambalo liliamsha hasira za Joram. Pamoja na udhaifu wake, aliwashangaza polisi alipopaa angani na kutua katika uso wa jambazi hilo kwa kichwa, kitendo ambacho kiliufumua uso huo na kuchafua sakafu kwa damu. Walimkamata Joram na kumpeleka hospitali chini ya ulinzi wa polisi.

Joram alitibiwa hapo kwa wiki nzima. Japo alijisikia nafuu, lakini aliendelea kujifanya mahututi akisubiri siku na wasaa aliouhitaji. Hatimaye, uliwadia. Mchana askari wa zamu alikuwa mmoja tu. Daktari aliingia katika chumba chake na kuyachunguza majeraha yake. Kisha, akamshauri Joram kwenda katika chumba cha X-ray kuzipima tena mbavu ambazo alidai kuwa zinamwuma sana ingawa picha hazikuonyesha madhara yoyote. Ni chumbani humo ambamo Joram aliamua kuchukua uhuru wake. Alimshangaza daktari kwa kumtia mweleka ambao ulifuatiwa na kufungwa kamba zilizotokana na shuka ya kijitanda cha chumba hicho. Kabla hajaamua la kufanya alisokomezwa tambara mdomoni kwa namna ambayo
 
22.




ilimfanya asiweze kupiga kelele. Kisha, alivuliwa nguzo zake, ambazo Joram alizivaa harakaharaka huku akitamka kitu kama ‘samahani.’ Mara akatoka kuelekea nje.

Safari yake iliishia benki ambako alichukua akiba yake yote. Toka hapo alikwenda uwanja wa ndege ambako alikata tiketi ya New York. Alijificha kwa muda katika mji huo akisubiri vyombo vya habari vichoshwe na suala lake ambalo lilipambwa mambo mengi ya uongo. Idd Amini alipojiita Mungu, Mugabe alimng’oa Ian Smith na kuiita nchi Zimbabwe na mambo mengine. Habari hizo zilimeza nafasi ya jina la Joram katika magazeti ya Marekani. Akasahauliwa. Ni hapo aliponunua hati ya usafiri ya bandia na kupanda ndege ambayo ilimchukua hadi Afrika, Dar es Salaam; Tanzania.

Jiji la Dar es Salaam halina hiana. Pamoja na ukweli kwamba Joram alikuwa mgeni sana nchini hapa, isipokuwa kwa safari chache alizokuja alipokuwa likizo; bado lilimlaki kama Mtanzania mwingine yeyote. Alieleweka alipoomba kufungua ofisi ya upelelezi binafsi, ingawa haikueleweka kama taifa au yeye angepata faida kutokana na kazi hiyo. Ikiwa kazi ngeni hapa nchini haikumchukua muda kupata kibali cha ofisi na kile cha kumiliki bastola kwa ajili ya kujilinda.

Wateja wakaanza kumjia. Wengi wakiwa na matatizo madogomadogo ambayo aliyatatua mara moja. Yale ambayo hayatatuliki aliyatupa kapuni. Kuna waliotaka msaada wa ushahidi wa vitendo vibaya katika ndoa, kuna wale ambao walidhulumiana; wengine ni wale ambao walipotelewa na mali au amali zao; n.k. yote hayo Joram aliyafanya shingo upande kwa ajili ya kujipatia kitu cha kutia tumboni. Zaidi, alihitaji mikasa mizito ambayo inatisha na kutatanisha.

Ni hilo lililomfanya ajitume kwa hiari katika mkasa wowote uliotokea. Na ni katika moja ya mikasa hiyo alipokutana na Neema ambaye aliondokea kuwa mwenzi wake wa kudumu hadi kifo kilipowatenganisha, mkasa ambao uliyafikia masikio ya waandishi wa habari na kupambwa sana na gazeti la Kiongozi ni ule wa mauaji ya Ngarenaro, Arusha, ambao waliuita Lazima Ufe… Baada ya huo ndipo macho na masikio ya watu wengi yalielekezwa kwake, jambo ambalo lilifanya mikasa na maafa yaanze kumwandama kila anapopita.

Kwa ajili ya njaa, kijana mmoja anayejifanya mwandishi
 
23.
aliibuka na tabia ya kuandika kila mkasa uliomkumba. Matokeo ya kazi hiyo ni msululu wa vitabu kama Dimbwi la Damu; Najisikia Kuua Tena; Mikononi mwa Nunda; Salamu Toka Kuzimu na Tutarudi na Roho Zetu, Mikataba ya Kishetani na vingine vingi. Jambo ambalo lilimzidishia umaarufu ndani na nje ya nchi na kumfanya ajikute katika nchi hii ya Pololo ambayo hakutegemea kuitembelea katika maisha yake.



***

Naam, huyo ndiye Joram Kiango, Joram ambaye sasa, kwa mara ya kwanza maishani mwake, alijikuta akiilaani kazi yake na kuilaumu bahati yake. Mungu alimpa au kumnyima nini mpaka akapenda kuhangaika vichochoroni na makuburini akipeleleza mambo ya watu wengine badala ya kutulia katika ofisi moja yenye kiyoyozi nyuma ya meza kubwa yenye fomica na kufanya shughuli zake kwa utulivu? Afrika imeipa nini roho yake wakati nchini mwake hakuwahi kupewa walao ujumbe wa nyumba kumi?

Alitulia kwa muda akiitazama dari. Hapana. Alikuwa haioni. Alikuwa mbali zaidi, nje kabisa ya chumba hicho; akiyatazama mengi ambayo yamepata kumtukia, mengi ya kutisha na kutatanisha. Yote yaliifanya roho yake iponee chupuchupu. Lakini hakuna kilichomfurahisha zaidi ya kuwa mshindi kati ya yote hayo. Na ni hilo ambalo lilimsumbua, kuona pamoja na ushindi wake wa kila mara, leo hii ameondokea kuonekana mtu wa kwanza kwa ujuha; utoke kwenu, ulipe nauli, hadi nchi ya watu, mbele ya Rais wa watu na kudai madai yasiyoeleweka wala kuelekeza kama si ujuha ni nini? Ujuha huu umemwanza lini? Na utaendelea hadi lini?

“Utafanya nini Joram?” Sauti ilimzindua.

Joram akageuka kumtazama. Nuru alikuwa amelala kando yake. Mikono yake ilikuwa imekizunguka kiuno cha Joram, uso wake ukimtazama. Joram alikuwa amemsahau. Wakati wote ambao alikuwa nje ya chumba hiki kimawazo, alikuwa amesahau kabisa kuwa alikuwa mikononi mwa msichana mzuri, pengine kuliko wote duniani katika karne hiyo, kwani imedaiwa mara nyingi kuwa Nuru alikuwa mmoja kati ya wale wanawake ambao huja duniani kwa makosa, wakiwa wamekusudiwa kuwa
 
24.
malaika, kosa ambalo Mungu hulifanya mara moja tu katika kila miaka mia moja.

Nuru, akiwa anaufahamu uzuri wake na jinsi uzuri huo unavyowasumbua wanaume wengine wote, awali Nuru alishangazwa kuona kuwa hauna madhara yoyote katika akili za Joram Kiango. Mwanzoni, hilo lilimwudhi sana. Kisha, alilisamehe. Ilikuwa baada ya kujiuliza kuwa pengine Joram pia sio binadamu wa kawaida. Kama ni kweli, wanavyotania waandishi wa habari kuwa yeye alikusudiwa kuwa malaika basi pengine Joram pia alitayarishwa kuwa malaika wa kiume.

Kwa kweli, huo ulikuwa mzaha tu uliokuwa ukipita katika kichwa chake katika vipindi kadhaa ambavyo kichwa hakikuwa na kazi nyingine muhimu, kama wakati huo alipokuwa ametulia na kujaribu kumtoa Joram katika dimbwi la mawazo lililokuwa limemmeza gubigubi. Alipomwona kazama kabisa, utulivu usio wa kawaida ukiwa umemkumba, macho yake yakiwa wazi kama maiti, ndipo Nuru akaamua kutulia, ili asivuruge mkondo wa mawazo yake, hadi alipomwona Joram akirudi chumbani humo toka kokote alikokuwa. “Utafanya nini?” alilirejea tena swali lake. Joram aligeuka kumtazama. Akatabasamu. Tabasamu hili lisingeweza kumlaghai Nuru. Lilikuwa tabasamu la uchungu lililobeba hasira na maumivu makubwa. Badala ya kutoa jibu Joram alitoa ulimi na kuusogeza kinywani mwa Nuru ambaye aliukwepa kwa kumsukuma pembeni akisema, “Usijisumbue.

Hujisikii kustarehe. Akili yako yote imevurugika kwa kukosa kazi ya kufanya kama ulivyotegemea.”

Tabasamu la Joram liligeuka kuwa halisi, kama alivyotaka Nuru. “Nadhani hujanielewa mpenzi,” alimwambia.

“Kinachonisumbua siyo kazi ya kufanya. Tanzania ina misitu mingi ambayo inahitaji jasho langu kugeuzwa mashamba. Kama shida yangu ingekuwa kazi, ningerudi kufanya hivyo mara moja. Kinachonisumbua ni marehemu ambaye alitutafuta usiku na mchana, na hatimaye kufia mikononi mwetu, baada ya kufikisha ujumbe ambao niliondokea kuuamini. Unadhani alikufa akifanya mzaha? Kuna mzaha wa aina ile? Mtu ufanye utani hata dakika ya mwisho wa maisha yako?”

“Sasa utafanya nini? Rais ame…”

“Hilo ndilo tatizo langu,” Joram alimkatiza. “Nitafanya nini?

Nifanye nini?”
 
25.


ILIKUWA usiku usio na furaha kwa Joram na Nuru. Walilala ndiyo, wakiruhusu miili yao kustareheshana kama kawaida, mikono ikijifariji kwa kugusa hapa na

pale; miguu ikiburudika kwa mguso huo. Hata hivyo, faraja hiyo haikufikia kiwango cha kuzifuta chembechembe zisizoelezeka ambazo zilienea katika fikra za Joram. Akijua hayo Nuru alifanya kila alilolifanya kwa dhamira ya kumsahaulisha msiba wake walau kwa muda. Alipoona havitimizi wajibu alijaribu kutumia maneno, kwa sauti yake laini, iliyopenya katika kiza kilichotanda chumbani humo baada ya kuzimwa taa zote, Nuru alimwambia. “Mpenzi nadhani hakuna asiyejua kama wewe ni shujaa.”

“Wanakosea wanaonifikiria hivyo,” lilikuwa jibu la Joram kwa

sauti nzito yenye dalili ya uchovu.

“Hivyo, inanishangaza kuona ukivunjika moyo kwa tatizo dogo kama hili. Unautia dosari ushujaa wako.”

Joram alikohoa kidogo kabla ya kumjibu. “Yaleyale ya waoga wanaodai, ‘Asiyekubali kushindwa si mshindani.’ Sikiliza Nuru…” Lolote alilokusudia kulisema lilikatizwa na mlio wa simu iliyokuwa kando yao. Simu hiyo iliwashangaza kidogo kwa sababu nyingi. Wakiwa wageni ambao hawakujulikana kabisa katika nchi hiyo, hawakuwahi kupigiwa simu na mtu yeyote, toka nje. Wala wafanyakazi wa hoteli hiyo hawakuwahi kuitumia kwa jinsi walivyokuwa wageni wasio na madai mengi. Zaidi ya





yote hayo saa hizi ilikuwa yapata saa saba za usiku? Maswali hayo ndiyo yaliyomfanya Joram aidake mara moja na kuitika.

“Samahani bwana,” sauti toka upande wa pili iliitika. “Tafadhali unaombwa kufika mapokezi kuna mgeni wako ambaye anakusubiri.”

‘Mgeni wa saa hizi! Anatoka wapi? Anataka nini?’ Joram alitamani kumuuliza hivyo operata huyo. Lakini alihairisha maswali hayo kwa kumjibu kuwa angefika mara moja. Akawasha taa na kujitupia mavazi ambayo yalikuwa karibu.

“Vipi?” Nuru alimtupia.

“Kuna mgeni hapo nje. Naenda mara moja.”

Nuru hakuelekea kulifurahia wazo hilo. “Kwa nini humkaribishi hapa ndani?” alimwuliza. “Nahisi wito huo hauna wema.”

“Nadhani hatukufuata mema huku, Nuru. Tungeyataka mema tungeendelea kuishi Dar es Salaam katika mahoteli ya Embassy na Kilimanjaro,” alimjibu huku akimaliza kuvaa na kuanza kutoka.

“Nisubiri basi,” Nuru aliita akikurupuka toka kitandani. “Usijisumbue. Nitarudi mara moja.”

Pengine Nuru hakumsikia, kwani Joram alisema huku akiufunga mlango nyuma yake.

Aliiendea lifti na kuisubiri. Ilipofika aliingia ndani ambamo alimkuta abiria mmoja tu, ambaye alikuwa amelewa. Alimsumbua Joram kwa harufu ya pombe kali ambayo ilijaa chumba hicho kila alipopumua. Joram alipofika chini alikwenda moja kwa moja katika chumba cha mapokezi.

Alikuwemo mgeni mmoja tu. Alikuwa ameketi juu ya kochi, sigara mdomoni; kitabu wazi mkononi. Uso wake ulimezwa na ndevu nyingi zilizoyafunika
 
26.
masikio. Alivaa mavazi ya kawaida kuliko ilivyo kwa watu wengi wa umri wake katika nchi hiyo; shati jeusi, ambalo halikuchomekewa na suruali ya kijivu. Joram alimkisia kama mtu mwenye umri wa kati ya miaka sitini na sabini. Macho yake yalikuwa yamezama katika kitabu cha riwaya ya kiingereza, Fear to Live alichokuwa akikisoma. Hisia zilimwambia Joram kuwa huyo ndiye mgeni wake. Hivyo, alimsogelea na kuketi naye.

“Natumaini hujambo,” alimsalimu.

Mgeni huyo aliinua uso mara moja na kumtazama Joram. Kisha, alikikunja kitabu chake na kumsogelea Joram zaidi.





“Joram Kiango?” aliuliza bila ya kuzijibu salamu za mwenyeji wake. Sauti yake haikuwa ngeni masikioni mwa Joram. Alijaribu kujiuliza aliisikia wapi. Hata hivyo, mgeni wake hakumpa nafasi ya kuendelea kufikiria. Alikuwa amenaza maelezo kwa sauti ndogo ambayo ni dhahiri ilikusudiwa kuishia katika masikio ya Joram peke yake.

“Nina ujumbe wa siri sana,” alieleza. “Rais ameomba radhi kwa jinsi alivyopuuza habari ulizomletea jana. Baada ya kufikiria kwa makini ameona kuwa yawezekana kweli marehemu alikuwa na habari muhimu ya siri ambayo alikusudia kukuletea. Hivyo, anakuomba uendelee na upelelezi wako kwa siri sana kuchunguza jambo lolote ambalo lilikusudiwa kutendwa dhidi ya taifa. Ameahidi kukupa msaada wowote ambao utahitaji pamoja na ulinzi kwa maisha yako kwa lolote litakalotishia usalama wako.”

Joram alikuwa akimsikiliza kwa makini. Sasa sauti hiyo haikumtatanisha tena. Alijua anaongea na nani. Aliupenda sana mchezo wa aina hiyo. Kwa kuufanya mchezo uendelee alisema, “Nadhani ningependa kumsikia Rais mwenyewe akinipa maagizo hayo badala ya mtu mwingine. Kama sikosei, iwapo kuna lolote linalotisha katika mashaka haya basi litakuwa suala linalotishia maisha ya Rais zaidi ya mtu yeyote mwingine.”

“Ukinisikiliza mimi umemsikiliza Rais,” alijibu. “Wewe ni nani kwake?”

“Msiri wake mkuu.”

Joram alitabasamu kidogo. “Nadhani umri wako ni mkubwa sana, kuwa nje ya nyumba yako usiku kama huu na katika baridi kali kama hii. Ungeniita tu, mzee…”

“Usijali,” alijibiwa baada ya kumjibu Joram kwa tabasamu lake lililochanua na kutoweka mara moja. “Usijali,” aliongeza. “Wazee vilevile tunapenda kujikumbusha matembezi ya usiku yanavyoburudisha. Zaidi suala hili ni la siri sana. Rais asingeweza kumwamini mtu mwingine zaidi yangu.”

Wakatazamana na kucheka tena katika hali ya kuelewana. “Unaelekea kijana mwepesi sana wa kuona,” aliongeza.

“Natumaini hutasahauu kuwa nimekutembelea usiku huu na kukupa ujumbe mzito kama huu. Nadhani inafaa tuagane. Utapokea mahitaji yako yote kesho mchana. Usisite kuomba msaada mwingine wowote ule.”





Waliinuka pamoja na kupena mikono.

“Itakuwa siri,” Joram alimwambia. “Nani atakayeniamini katika dunia hii nikijitia kutamba kuwa niliwahi kutembelewa na Rais katika hoteli yangu?”

Rais yupi?” mgeni huyo aliuliza akiondoka.
 
27.
Mara moja akamwona yule mlevi waliyeshuka naye katika lifti akichomoza toka katika kimoja kati ya vyumba vya hoteli hiyo na kumfuata mgeni huyo kwa mwendo ambao ulitangaza yeye ni nani katika duia hii. Hata chembe moja ya ulevi haikuwemo tena mwilini mwake. Koti lake lilituna kidogo mgongoni kuonyesha kuwa alikuwa kamili. ‘Kidogo nishangae,’ aliwaza kimoyomoyo. ‘Nilidhani hatimaye nimekutana na mmoja wao anayejiamini. Hawajiamini walo kwa dakika moja.’ Taratibu aligeuka kuiendea lifti.

Alishangaa kumkuta Nuru nje ya lifti hiyo. Hakushangaa alipoulizwa kwa sauti ndogo, “Ni nani yule mzee aliyekutembelea saa hizi? Na alitaka nini?”

“Kwa nini hukulala hata ujisumbue kunifuata kwa siri?

Ulidhani naitwa na mwanamke? Ulitaka kunifumania?”

“Acha mzaha, Joram,” Nuru alisisitiza. “Ulitegemea kuwa ningestarehe juu ya kitanda wakati wewe umeitwa usiku wa manane na mtu mwenye madevu ya kutisha kama yule?” alipoona hajibiwi aliongeza, “Ni nani lakini yule Joram?” Lifti ikafika. Wakaingia.

“Mbona hunijibu Joram?”

“Kukujibu nini?” aliuliza akipapasa mfuko na kutoa sigara. “Yule mzee. Ni nani na alitaka nini?”

Joram alikuwa akishughulikia sigara yake. Alivuta mara moja, ikazima. Akaiwasha tena. Lifti ikawafikisha. Wakashuka na kufuatana chumbani kwao.

“Ni nani? Au hutaki kunijibu?” lilikuwa swali la kwanza mara walipoingia chumbani kwao.

“Kwani hukumwona?” Joram aliuliza. “Nimemwona, sikumtambua.” “Alikuwa Rais.”

“Rais yupi?” “Abdul Shangwe.”

Nuru alitabasamu kwa hasira. “Naona hutaki kuniambia

ukweli, Joram. Tumeanza lini kufichana mambo?”





“Tangu ulipoanza kutoniamini.” Alipoona Nuru hajamwelewa, aliongeza, “Kwa nini huamini kuwa Rais wa nchi hii ametutembelea? Nuru ninayemjua mimi hawezi kudanganywa na madevu yale ya bandia na mavazi ya kubabaisha aliyoyavaa.”



***

Moyo wa Joram ulijaa furaha alipoingia katika baa ya tatu kati ya nne ambazo aliambiwa kuwa hayati Patauli Kongomanga alizipendelea, baa iliyojulikana kwa jina la Glamour Site ikiwa moja kati ya zile maarufu sana katika mji huu wa nchi ya Pololo, Baubu.

Katika baa zilizotangulia Joram alidokezwa na mtu mmoja kuwa alipata kumwona marehemu akifuatana na msichana mmoja aliyefanya kazi hapo Glamour Site katika hali ya mtu na mpezi wake. Hayo aliyapata baada ya maswali mengi, uongo mwingi na ahadi zisizo na idadi kwa wafanyakazi mbalimbali; hasa wa kike, katika baa mbalimbali. Haikuwa kazi ngumu kwa mtu kama Joram kupata mwanya wa kumfikisha hapo. Jina la marehemu Kongamanga likiwa bado moto masikioni mwa watu, hasa kwa waandishi wa habari; ilimchukua dakika chache tu kupenya toka baa hadi baa hata kufikia hii ambayo aliamini ingekuwa kichochoro ambacho ama kingemwongoza katika barabara kuu au msitu mkuu wa chochote alichokuwa anakitafuta.

Alianza upelelezi rasmi baada ya ile ziara ya Rais usiku wa manane. Kutembelewa na Rais wa nchi! Usiku kama ule! Katika hali kama ile kulimzidishia ile njaa aliyokuwa nayo rohoni, kutaka kujua ni kitu gani kinapikika sirini, katika nchi; kiasi cha kuyapoteza maisha ya kijana asiye na hatia kama Kongomanga. Na nani mpishi wa chungu hicho.
 
28.
Nuru aliondokea kuwa tatizo dogo lililojitokeza mwanzoni mwa uchunguzi wake. Hakuafiki kuachwa nyuma. Joram akijua kuwa suala hilo kama lilikuwa lianze katika mabaa; basi ingekuwa toka katika midomo ya wanawake, ambao wasingejisikia kumkaribisha endapo angekuwa akifuatana na msichana, kisha mzuri kama Nuru. Alijaribu kumshawishi Nuru kubaki nyuma, haikusaidia. Siku ya kwanza ilibidi wafuatane. Matokeo yake Nuru mwenyewe aliyaona. Siku ya pili alikubali kubaki hotelini kwa masharti ya kufahamishwa ratiba nzima ya mienendo ya





Joram. Ni siku hiyo ambayo Joram alifaulu kuzungumza kwa mapana na watu mbalimbali, akianzia mbali na kuishia katika maongezi ya marehemu Kongamanga.

Hata hivyo, baada ya maongezi yake, alimwona Nuru akiingia na kuketi meza ya mbali sana. Joram alijaribu kumsalimu kwa macho lakini Nuru akajifanya hamwoni wala hamsikii. Badala yake aliyaona macho yake yakimtia moyo kwa tabasamu la kumvutia mzee mmoja ambaye tangu alipoingia hakuchoka kumtazama, kinywa wazi; ulimi nje; kila dalili ya tamaa ikiwa wazi katika macho yake. Baada ya muda mzee huyo alihamia katika meza ya Nuru na kuanza kumwaga vinywaji na maongezi kama aliyepagawa. Joram alihisi wivu kiasi. Lakini mara moja alijicheka kwa wazo la kuwa na wasiwasi na ‘zee’ kama lile. Akaendelea na shughuli zake. Akayapata anayoyataka. Alipotosheka aliaga na kutoka nje ambako aliita teksi. Wakati akifungua mlango na kuingia aliisikia sauti ya kike ikimsemesha. “Samahani,” ilisema kwa upole. “Kama unaelekea Golden View Hotel naomba lifti.”

Joram alimtazama kidogo kisha akatabasamu kabla ya kuuliza, “Na yule bwana wako?”

“Achana naye.”

Wakainggia na kuondoka. Hawakuzungumza chochote hadi chumbani kwao ambako Joram alimgeukia tena Nuru na kumwuliza, “Umeanza lini dada yangu, tabia ya kujiuza kwa wanaume katika mabaa?

Ilikuwa sauti yenye mzaha, Nuru alijibu kimzahamzaha. “Unadhani nitakuruhusu ukaukwae Ukimwi kwa wanawake

wa baa?”

“Utafanyaje kunizuia?”

“Nikiona maongezi yanakuwa si ya kawaida nitaanzisha fujo na kukupora wewe na huyo hawara yako.”

Wakacheka na kujitupa kitandani.

***

Naam, hayo yalikuwa ya jana. Leo Joram yuko katika baa yenye matumaini makubwa. Alikuwa tayari kununua habari kwa bei yoyote ile, hata kwa kutazamana na Ukimwi ana kwa ana. Asingekubali Nuru alete wivu au mzaha ambao ungevuruga uchunguzi wake. Hivyo, alifanya hima kuvaa lile tabasamu lake ambalo huwaloga wanawake, tabasamu ambalo mara





nyingine humletea matatizo bila ya kutegemea kwa kutafsiriwa vibaya na wanawake ambao hakuwakusudia. Leo alilielekeza kwa kila mwanamke. Macho yake yakiwa kazini kutafuta uso wa mwanamke aliyekuwa akimhitaji. Isingekuwa kazi ngumu kumfahamu mwanamke ambaye amepoteza mpenzi siku mbili, tatu, zilizopita.
 
29.
Tabasamu lilifanya maajabu. Haukupita muda, mara akawa nyota katika baa hiyo, macho ya kila mwanamke yakimwelekea; kila mhudumu akitaka kumhudumia. “Samahani, nimekwishahudumiwa,” alieleza kwa mara ya tatu.

Kinywaji chake kilipoletwa alikunywa kwa utulivu, akiendelea kutupa jicho lake huku na kule. Haukupita muda alipouona uso aliouhitaji, uso wenye furaha ya bandia na tabasamu lililokusudiwa kufunika msiba ulokuwa moyoni. Ulikuwa uso wa msichana mzuri wa sura, mwenye umbo dogo lililokatika kike kiunoni na kujaza tosha nyuma, nywele zake ndefu zilizosukwa kileo zikiwa zimeuzunguka uso wake mzuri na kuufanya kama kisiwa cha kupendeza katikati ya bahari nyeusi. Msichana huyu, aliyekuwa katika mavazi yake ya kikazi; alikuwa akipita hapa na pale katika meza za wanywaji.

Joram alimkonyeza. Akajifanya haoni. Akamkonyeza tena. Bado alijifanya haoni. Joram akaamua kumwacha kwa muda. Akaichoma na kuishughulikia sigara yake. Alipoinua uso, msichana huyo alikuwa kasimama mbele yake akiuliza kwa upole, “Naweza kukusaidia?”

“Eh! Ndiyo. Bia mbili, moja kwa ajili yako.”

Msichana huyo alimtazama Joram kama anayetafuta kitu katika macho yake. Kama ambaye alikipata au hakukipata alinong’ona, “Ahsante, lakini bado niko kazini. Kama unanitaka kwa maongezi zaidi naweza kumwomba ruhusa msimamizi wetu. Ghorofa ya pili toka hii kuna vyumba vya mapumziko. Nenda kapate chumba, kisha nipigie simu, naitwa Betty.”

Baada ya nusu saa nitakupigia simu,” Joram alijibu.

Alikunywa bia yake taratibu. Alipomaliza alimtupia Betty jicho la kumuaga, kisha akainuka kuelekea mlangoni. Ndio kwanza akamwona Nuru aliyekuwa ameketi katika meza ya tatu tu nyuma yake, pamoja na wanaume wengine wanne. Nuru alikuwa amevaa katika hali ambayo isingekuwa rahisi mtu yeyote aliyemwona jana kumfahamu. Alikuwa katika suruali ya degrizi,





fulana nyeusi na nywele za bandia. Matiti yake yalisimama wima kama yanayowaringia wanawake wote katika baa hiyo na kumdhihaki kila mwanaume. Sura yake nzuri, yenye macho maangavu ilikuwa kama bahari tulivu ambayo iliwatia wivu wanawake wazuri wa kuvutia wanaume machachari. Kwa muda, Joram alijikuta amesahau kwamba huyo alikuwa Nuru wake, akimsubiri; na badala yake moyo wa tamaa na wivu ukamshika. Akajikuta akitamani kumwendea na kumtoa katika kundi hilo la wanaume wenye kiu kubwa kumgusa. Lakini alipomtazama Nuru na kutoiona dalili yoyote ya kutofahamiana na mwanaume yeyote kati yao akakumbuka kuwa yuko kazini. Akatabasamu kimoyomoyo na kuendelea na safari yake.

Alijipatia chumba kidogo ambacho kiti pekee chumbani humo kilikuwa kitanda. Kando ya kitanda kulikuwa na kijimeza ambacho Joram hakuona kama kilikuwa na kazi nyingine zaidi ya kuwekea nguo. Hewa chumbani humo ilikuwa nzito kiasi kwamba Joram aliifikiria kama hewa iliyojaa dhambi. Kadhalika, kulikuwa na harufu kali ya ukahaba. Ilimchukua dakika mbili tatu kabla ya kuubatilisha uamuzi wake wa kumwalika Betty chumbani humo.

Betty aliingia kikazi. Alikuwa katika mavazi tofauti na yale ya kazi. Hili lilikuwa vazi jepesi, fupi ambalo Joram hakujua aliite gauni au sketi. Liliruhusu mwili wake wa ndani, ngozi inayomeremeta kwa rangi yake ya kunde, na mapaja laini, mekundu, yawe kama siri isiyohitaji kuwa siri katika mavazi hayo. Sura yake nzuri ilizidi kuwa nzuri kwa tabasamu lililochanua ghafla usoni mwake. “Bwana wangu mzuri… una bahati wewe?... utafurahi…” Betty alisema huku akijifungua fundo moja nyuma ya mgongo wake ambalo lilifanya gauni hilo lifumke na kuwa kipande kimoja cha kitambaa kilichoteleza toka mwilini mwake na kumwacha kama alivyozaliwa. “Siku ya leo… hutaisahau…” alisema akimsogelea Joram.
 
30.
Naam, ilikuwa sura ambayo ilitosha kabisa kuufariji ubongo uliochoka kwa kusoma aina mbalimbali za vitabu, uso ambao ulibebwa na umbo ambalo ni burudani kamili kwa fikra za mtu ambaye muda mwingi wa maisha yake aliutumia kuandika burudani za watu wengine, mtu kama hayati Patauli Kongomanga. Hayo yalipita katika kichwa cha Joram pindi akiendelea kujiuliza ama hisia zake zilikuwa kweli kuwa huyo ndiye





aliyekuwa hawara au mpenzi wa Patauli. Kadri anavyowafahamu waandishi walivyo watu wanaoishi katika ndoto za ajabuajabu, na wanaopenda kufanya maisha halisi kuwa ndoto na dunia sehemu tu ya ndoto hiyo; aliamini kuwa hata mapenzi kwao ni ndoto ya mahaba, ndoto isiyo na upande wa pili ambao ni dhiki na maudhi. Nani ambaye angefaa kuikamilisha ndoto hiyo zaidi ya mwanamke, mzuri aliyehitimu katika kila fani ya kumstarehesha mwanaume? Mwanamke ambaye kula yake inategemea jitihada na mafanikio yake kitandani. Na ni yupi mwanamke huyo katika baa hiyo zaidi ya Betty?

Betty ambaye sasa alikuwa kajilaza chali kitandani, macho kayalegeza huku kwa sauti ndogo ya huba akinong’ona, “Njoo… Nadhani naweza kukuamini… Malipo baadaye…”

Ilikuwa picha ya aina yake, picha inayotisha na kupendeza kwa wakati mmoja, picha inayoshawishi na kuvutia, moja kati ya zile picha ambazo hufanya akili ya mwanaume ihamie kisogoni na kujikuta ikifuata matakwa ya mchezaji katika jukwaa, badala ya akili yake timamu. Hata hivyo, haikuwa picha mpya kiasi hicho kwa Joram Kiango. Alichofanya ni kuendelea kusimama katikati ya chumba hicho, akiimalizia sigara yake. Kisha, kwa sauti tulivu alisema, “Vipi Betty… sikujua kama nawe hu shemeji kula.”

“Kwani vipi jamani?” Betty aliuliza kwa mshangao kidogo. “Mimi ni shemejio,” alieleza. “Nilichohitaji ni kuzungumza

nawe tu.”

“Kuzungumza!” Betty alifoka kike. “Kuzungumza! Wakati wenyewe wanasubiri nusu ya chochote utakacholipa! Wewe vipi kaka! Unajua niliondokea kukuheshimu sana?” akasita kidogo. Kisha, “Kwanza yamekuaje hayo ya shemeji! Kwa nani?”

“Hayati Patauli… alikuwa rafiki yangu mpenzi…”

Betty alimkatiza kwa ukali kidogo, “Mwongo! Nipishe niende zangu. Kumbe nawe u mmoja wao! Hamchoki kunifuatafuata? Nipishe…”

Kiasi Joram alishangaa kidogo. Hakutegemea kama ingekuwa rahisi kiasi hicho. Alichotegemea hasa ungekuwa ubishi mwingi na Betty kujifanya hamfahamu kabisa marehemu. Baada ya ubishi huo angeambulia kununua ukweli au uongo ambao angeuchambua na kuungaunga hata apate uchochoro aliokuwa akiuhitaji. Hata hivyo, hiyo pamoja na urahisi huo, hisia fulani zilimfanya Joram ahisi kuwa ukali katika sauti ya Betty ulikuwa





wa bandia na hata maneno hayo aliyatamka kama aliyeyakariri kwanza. Hivyo, alimtazama kwa makini pindi akijifunga vazi lake taratibu na, hatimaye, kuanza kutoka.

“Usiwe na haraka kiasi hicho bi Betty,” Joram alimshika mkono. Akamwambia taratibu, “Nimekuita tuzungumze tu juu ya marehemu, mpenzi wako. Nipo tayari kuilipia kila dakika ambayo nitakupotezea. Au hujui kuwa alikupenda sana?”

Betty alimbetulia macho na kumtazama Joram kwa makini zaidi, “Alinipenda ndiyo… mie pia nilimpenda… lakini wewe ni nani? Watu wengi sana wamekuwa wakinifuatafuata kwa maswali ambayo hata sielewi yanaelekea wapi. Hata nahofia maisha yangu sasa. Sijui wanataka kuniua kama walivyomwua yeye…”

Ilikuwa nafasi ambayo Joram asingeipoteza. “Unadhani ni kweli walimwua?”

“Bila shaka,” Betty alifoka. Kisha, dalili za hofu ziliurudia uso na sauti yake alipouliza tena, “Wewe ni nani? Sijisikii vizuri kuzungumza na mtu nisiyemfahamu.”
 
31.
Hisia ziliendela kumfanya Joram ajione kama anayechezewa akili zaidi ya anavyomchezea yeye. Bado Betty alikuwa kama anayeigiza mchezo ambao alikwishaufanyia mazoezi kwa muda mrefu. Hilo lilimfanya Joram aamue kujitokeza toka kichakani na kuingia hadharani. “Sikia Betty. Mimi ni mgeni katika nchi hii. Nimetoka nchi ya mbali sana kukufuata wewe ili unieleze chochote unachojua juu ya maisha na kifo cha mpenzi wako, Patauli. Unaonaje ukiketi chini na kunieleza kwa tuo?”

Betty alitabasamu kidogo kabla ya kumjibu, “Sura yako inanifanya nijisikie kukuamini ingawa roho hainiruhusu. Nadhani hujui, tangu alipofariki nimekuwa nikifuatwa na watu mbalimbali na kuulizwa maswali tofautitofauti. Wote huanza kwa kunitaka mapenzi na tunapofikia chumbani huishia kunitupia maswali mazitomazito. Wote hujifanya rafiki wa hayati Patauli. Wengine wamediriki hata kunitisha kwa sababu nisiyoielewa. Hata nimekuwa simjui nani rafiki nani adui yake.” Akasita na kumtazama Joram kwa wizi. “Kwa hiyo, kaka, nashindwa kujua nikuweke katika kundi lipi.”

‘Mwanzo mzuri!’ Joram aliwaza. “Huitaji kuniweka katika kundi lolote. Kama nilivyokwambia mimi ni mgeni tu nchini, ambaye niliondokea kuvutiwa na mtindo wake wa uandishi. Kifo





chake cha ghafla, nchini mwetu, kilinifanya niwe na shahuku

kubwa ya kuelewa kilivyotukia.” “Umetokea Tanzania?” “Hujakosea.”

“Unaitwa Joram Kiango?”

“Hauko mbali sana na ukweli.” Kisha Joram aliliweka usoni tabasamu lake ambalo anaamini ni moja kati ya silaha zake kali kwa wapenzi na maadui. “Ndiyo. Wananiita Joram Kiango. Bila shaka marehemu alikuwa akinitaja sana katika maongezi yake.”

“Hapana, alikutaja katika ndoto,” Betty alimfahamisha. “Sijakuelewa… ndoto vipi?” Joram aliuliza.

“Aliwahi kukutaja usingizini,” Betty alifafanua. “Wakati ule ambapo alikuwa mtu aliyebadilika sana na kuwa mkimya, msiri, mwenye wasiwasi sana. Katika usingizi wake wa mchana aliwahi kuweweseka akitamka mambo mengi. Mojawapo lilikuwa jina lako.”

“Alisemaje?”

“Sikumbuki vizuri. Lakini ilikuwa kitu kama… nitakwenda Tanzania… Joram kiango anafaa…” mambo kama hayo. Sikuelewa maana yake hadi baada ya kusikia kuwa amefia Tanzania.”

Joram alimtazama kwa makini zaidi. Maongezi hayo yalimvutia kuliko alivyotegemea. Alijihisi kama anayekunywa chai iliyozidi sukari. “Mambo gani mengine aliwahi kuongea ndotoni Betty?”

“Mengi tu,” Betty alieleza, “Alikuwa kama anayeropoka tu, kama ambaye alianza kuharibikiwa na akili. Siku hiyohiyo alisema vitu kama … Waziri Mkuu…. Kumwaga damu… kwa ajili ya mapenzi… hapana… nani ataamini… Joram’ “Maneno kama hayo kisha ghalfa Betty aliinuka na kumtazama Joram kwa hofu. “Nafanya nini?” aliuliza. “Haya ninayoyazungumza kwako sijapata kumwambia mtu yeyote. Nadhani ni haya yaliyomwua. Tafadhali usiniulize zaidi.”

“Sikiliza Betty,” Joram alimwambia. “Bado nahitaji sana kuzungumza nawe. Nadhani utanisaidia sana.”

“Basi sio hapa,” lilikuwa jibu la Betty. “Waonaje nitakapomaliza kazi tukilala wote tuzungumze kwa urefu. Nina chumba changu ambacho hakina bugudha wala kupigiwa hodi.”
 
32.
“Leo si rahisi, Betty. Labda tukutane kesho wakati huko kazini, tupange kwa ukamilifu na kuzungumza kwa marefu na





mapana.”

“Vizuri… saa ngapi? Unajua sisi tunaoishi kwa kuuza miili yetu hatuna muda wa kutosha? Lazima uwe na ahadi za kiungwana. Ukichelewa hunikuti, ukiwahi hunipati. Saa ngapi?”



***

Saa nne ya asubuhi hiyo ilimkuta Joram akiwa mtaa wa pili toka hotelini hapo. Alisimamisha teksi ya kwanza ambayo ilisimama na kumchukua. Akampa dereva jina la mtaa na namba ya nyumba aliyohitaji. “Mapalala, jengo la Edward namba 104. Fanya mwendo wa kiume rubani,” alimweleza.

Haikuwa kazi kubwa kwa Joram kumtoroka Nuru. Alimwacha kitandani, akaingia bafuni ambako alioga na kupiga simu kwa wahudumu akiomba chai iletwe chumbani humo. Kisha, alifanya kama aliyekumbuka kitu, akainuka na kutoka. Akawa ameondoka. Nyendo za mchana zikiwa nje ya kawaida yao tangu walipofika katika mji huo Nuru hakuwa na sababu yoyote ya kushuku kuwa anaachwa.

Uamuzi wa kumtoroka Nuru ulimjia usiku wa jana baada ya kumaliza maongezi yake na Betty kwa ahadi ya kukutana mchana huo na kurudi ambako alimkuta Nuru katika kundi la wanaume walewale. Wakiwa wamelewa kiasi, kila mmoja alianza kuonyesha dalili ya kumtaka Nuru kwa heri au shari, hali ambayo ilimfanya Nuru ainuke na kutoka zake nje. Joram alimfuata huko na kumshika mkono huku akimwambia, “Leo mwisho kujiuza kwa bei rahisi kiasi hicho.”

Nuru alimgeukia na kumwambia kwa mzaha, “Nimekubali baada ya kushuhudia ukiukataa mwili mzuri wa msichana mzuri kama yule. Nimeanza kukuamini Joram…”

Ndiyo kwanza Joram akafahamu kuwa Nuru alimnyemelea na kumchungulia. Pamoja na kwamba Nuru hakuwa na nia mbaya, bado Joram alifahamu madhara mengi ambayo yangeweza kusababishwa na mzaha au mapenzi katika kazi kwa visingizio vya “Usalama wako.” Ndipo akaamua kumtoroka Nuru katika kila safari ambayo ingekuwa na umuhimu katika upelelezi wake, alikuwa na hakika kuwa angejifunza mengi ambayo yangemsaidia kujua kitu gani anatafuta.

Gari lilimteremsha robo saa kabla ya muda alioahidiana na

Betty. Hakuwa tayari kufuata matakwa ya Betty ya kufika kwa





muda uliopangwa kama angekwenda msikitini au kanisani, kwani moja kati ya mambo ambayo anayathamini katika maisha ya mpelelezi ni tabia ya kutomwamini mtu yeyote na kumshuku kila mtu, hata marehemu. Kupanga muda ni kati ya makosa makubwa. Unaweza kuwa unashirikishwa kupanga muda wa kifo chako. Hivyo, ni vizuri kukifumania kifo kikijiandaa kukuchukua au kukichelewesha kidogo. Ubovu wa gari na uzembe wa dereva kwa kutojua vyema ramani ya mji huo ndio uliomfanya aipoteze robo saa nyingine.

Kilikuwa kitongoji ambacho kilikuwa na haki ya kumshukuru Meya wa Jiji hilo kwa kukikumbukakumbuka. Mitaro ilikuwa safi, barabara ya kuridhisha na taa za barabarani zilienea kila upande. Nyumba nyingi katika mtaa huo zilikuwa za kuridhisha. Hata wakazi wake walikuwa na dalili nyingi za “Hatujambo” kuliko vingine vya mji huo ambavyo Joram aliwahi kuvitembelea. Watu hao, wake kwa waume, walipita katika shughuli zao, bila kumtupia jicho la pili Joram ambaye tayari alikuwa akipiga hodi mlango wa nyumba aliyoihitaji.
 
33.
Ilikuwa nyumba kubwa, yenye zaidi ya vyumba ishirini. Mlango ulifunguliwa na msichana ambaye kitabia alikuwa ndugu yake Betty. Lakini baada ya Joram kumtaja msichana huyo alilimeza tabasamu ambalo alikuwa amekwishaliumba usoni mwake. Kwa sauti ya kebehi alilalamika, “Kila mtu anamtaka Betty… mgejua alivyo malaya wala msingejisumbua. Mwanamke gani ambaye halali bila ya wanaume kumi kumshughulikia?” baada ya maneno hayo alirudi chumbani kwake na kufunga mlango wake kwa nguvu.

Kabla Joram hajajua afanye nini mlango mwingine ulifunguka. Uso mwingine wenye dalili za mapigo ya Betty ukachungulia. “Ni wewe unayemtaka sio?” aliuliza bila ya kusalimu. “Sijawahi kukuona hapa. Utawezana naye? Sasa hivi ameingia ndani na mwanaume. Kama utasubiri zamu yako njoo chumbani. Huwezi nenda zako… haturuhusu watu kukaa ukumbini. Mtatufukuzia baraka.”

Ilimlazimu Joram kutabasamu. Alishindwa kufahamu ni mtu gani au shirika lipi hili lililojenga nyumba kama hii na kuwapangisha watu ambao kitabia walifanana kama pacha. Badala ya kujibu alifuata mlango ambao wote walikuwa wakielekeza macho yao na kugonga. Hakuitikiwa. Akagonga





tena. Bado hakuitikiwa. Alipoitazama saa yake ilikuwa dakika tano kabla ya muda ambao waliahidiana na Betty. Akaujaribu. Mlango ukafunguka taratibu na kumruhusu kuingia chumbani, chumba ambacho pia kilitumika kama ukumbi wa maakuli na maongezi.

Picha kubwa, iliyoegemezwa ukutani ikiwa katika fremu ya kioo, ilimhakikishia Joram kuwa hakupotea. Katika picha hiyo Betty alikuwa kavaa sidiria na chupi peke yake, akiwa kakalia mwamba wa jiwe kando ya mto mkubwa. Kwa mbali, wavuvi wawili wakiwa ndani ya mtumbwi wao, walionekana wamesimama wakimwangalia. Ikiwa picha ya miaka miwili au mitatu iliyopita, akiwa hana madoido mengi ya kuongeza uzuri mwilini mwake, Joram aliona jinsi Betty alivyowahi kuwa msichana mzuri. Kama madoido yalikuwa yamemuongezea kitu mwilini, basi nyongeza hiyo haikuwa chochote zaidi ya kuutia dosari uzuri wake.

Macho ya Joram yalipoikinai picha hiyo yalitambaa chumbani kote, yakapima hiki na kile. Ziara ya macho hayo ilipokoma, ilimfanya Joram kubakiwa na hakika kuwa Betty hakuwa akifanya biashara ya kujiuza kwa shida, labda alikuwa na silika ya kupenda wanaume. Kitanda chake kiligharimu pesa za kutosha kuwekea msingi wa nyumba, redio yake ilimeza mishahara ishirini ya kima cha chini, makochi yangetosha kabisa kumfanya awe na pikipiki na zulia lingemwezesha kumiliki gari dogo. Juu ya kijimeza cha kando kulikuwa na simu, kando yake kabati ambalo lilikuwa limefunikwa na vitabu anuwai. Kwa mbali, Joram aliweza kuyaona majina ya waandishi kama James Hadley Chase; Harold Robbin; Mario Puzo na wengine.

Vitabu vyote humo vilikuwa katika hali ya vuruguvurugu ambayo ilimfanya Joram ahisi kwamba Betty alichelewa kuamka na hivyo, hakuwa mbali. Akajituliza juu ya kochi kumsubiri. Subira yake ilipungua baada ya kuteketeza sigara mbili bila ya kumwona mwenyeji wake. Akainuka na kuanza kuchungulia huko na huko. Jikoni hakukuwa na mtu. Akagonga mlango wa bafuni. Haukuitikiwa. Akasita kabla ya kuufungua na kuchungulia. Macho yake yalivutwa moja kwa moja na beseni la kuogea.

Kama angekuwa mtoto mdogo angecheka kwa kumwona mtu akioga katika maji ya rangi, maji mekundu. Lakini utu uzima wake ulimfanya agutuke kidogo na kisha kulisogelea sinia hilo.
 
34.


Yeyote yule aliyeifanya kazi hiyo alikuwa hodari sana wa kazi yake. Betty alikuwa na jeraha moja tu, dogo sana, katika ubavu wake wa kushoto. Kitu chochote kilichoingia katika jeraha hilo kiliufikia moyo na, hivyo, kufanya damu itoke nyingi kuliko ilivyohitajika. Ustaarabu mwingine wa mwuaji huyo ni jinsi alivyomlaza marehemu katika sinia lake kwa uhakika hata tone moja la damu lisidondokee sakafuni.

Kiasi, Joram alisikia kichefuchefu. Haikuwa picha ambayo aliitarajia hata kidogo. Akamtazama marehemu kwa muda, kisha akarudi sebleni ambako aliduwaa akijiuliza kwa nini Betty ameuawa. Ni kweli kuwa maongezi yake ya jana usiku na ahadi yao ya kuonana leo ndiyo kisa cha mauaji hayo? Betty alikuwa na lipi la haja? Na ni nani huyo ambaye alikuwa akizichunguza nyendo zake kiasi hicho hata kumwua mtu pekee ambaye alielekea kuwa nyota pekee katika anga hii yenye kiza cha kutisha?

Hasira zikachemka katika ubongo wa Joram. Kwa hasira hizo akatabasamu. Sasa asingelala usingizi hadi amegundua jambo gani linatukia katika nchi hii. Mara akainuka na kuanza kupekuapekua katika makabati na masanduku ya Betty. Alikuwa na hakika kuwa mwuaji asingeacha kuharibu kitu ambacho kingemsaidia katika upelelezi wake. Hata hivyo, aliendelea kutafuta, ingawa hakujua anatafuta nini. Aliangalia hiki akaacha, akasoma kile na kuacha akashika hiki. Mara simu ikalia na kumkatiza. Aliitazama kwa mashaka kidogo, moyo ukimshauri aache kuipokea. Moyo mwingine ulimshawishi kupokea. Pengine ingemsaidia kuisikia sauti ya binadamu yeyote ambaye alihitaji kuzungumza na Betty.

Akainua mkono wa simu na kuitikia akiitaja namba iliyoandikwa kwenye simu hiyo.

“Nani mwenzangu?” sauti iliuliza. “Wewe unamtaka nani?”

Kimya kifupi kilifuata. Kisha, sauti hiyo ilizungumza tena. “Wewe ni Joram Kiango?”

“Kama ndiye?”

“Sikiliza…” sauti hiyo ilinguruma. “Unasikia, Joram? Unajua unachokitafuta? Unatafuta kifo chako.”

Baada ya maneno hayo simu ilikatwa. Joram akatua yake na kutabasamu kidogo. Hili lilikuwa tabasamu la furaha. Ilikuwa





hatua moja mbele, hatua ya ushindi. Kama aliyepiga simu hiyo alikusudia kumtisha, basi alikosea sana. Alichofanya ilikuwa kumtia ari na matumaini zaidi. Adui anapoanza kukutisha ameanza kukuogopa.

Akarudia upelelezi wake. Hakupata chochote cha haja. Wakati akikaribia kukata tamaa, karatasi moja ilidondoka toka chini ya matandiko aliyokuwa akiyafunua. Alipoigeuza alishangaa kukuta ni picha. Ilikuwa ni picha yake ya siku mbili tatu zilizopita. Hilo lilimshangaza. Vipi Betty ambaye wamefahamiana jana tu awe na picha yake? Na vipi aifiche kiasi hicho? Zaidi alipigwa lini picha hii bila ya yeye mwenyewe kujifahamu?
 
35.
WAZIRI Mkuu… kumwaga damu… kwa ajili ya mapenzi… Hayo yalikuwa maneno pekee ya haja kati ya yote ambayo hayati Betty aliyatamka. Kama angekuwa hai

hadi sasa, au endapo kifo chake kingekuwa cha kawaida maneno hayo pia yangeweza kuwa ya kawaida au uzushi tu. Lakini sasa amekufa. Hapana, ameuawa! Yawezekana kuwa maneno hayo au mengine ambayo angeweza kutoa yakawa ndiyo kisa cha kifo chake? Haiwezekani kuwa amechinjwa na mwuaji wa kawaida kwa sababu zake binafsi? Wangapi ambao wameua hata wana wao bila ya sababu? Lakini, kuna ile simu… na ile picha…

Hayo yalielea katika kichwa cha Joram wakati akirudi nyumbani baada ya kuiacha nyumba hiyo ya maafa kwa siri. Aliamua kutembea kwa miguu ili apate wasaa wa kuyatafakari hayo yaliyokuwa yakitendeka. Jitihada zake zote za kuwaza na kuwazua zilizidi kumdidimiza katika shimo lenye kiza kizito lisilo na nuru wala mwanga wa kutokea.

Kwanza, mtu atoke mbali aje kufia mikononi mwako, akuambie kuwa unaitwa na Rais! Rais akatae, kisha akuombe uendelea na upelelezi. Mtu wa kwanza mwenye uwezekano wa kukupa habari auawe dakika chache kabla hujamfikia. Kisha, ije simu, ikikutishia ili uache uchunguzi wako. Katika upekuzi wako uikute picha yako ikiwa imefichwa humo ndani. Hujui ilifika vipi.





Kitu pekee ambacho kilimtia Joram moyo katika suala zima ni simu hiyo. Ilimdhihirishia kuwa sio bure, liko jambo. Na asingestarehe hadi angelifahamu. Kwamba maisha yake yangekuwa hatarini, hatari zilikuwa ladha na burudani zake pekee. Zaidi, usalama wake ulikuwa katika kugundua ukweli wa jambo hilo kuliko kuukimbia kwani, kwa namna moja au nyingine, aliwishajiingiza katika mkasa huo. Mtu yeyote angefanya mauaji hayo kumchinja kama alivyomfanyia Betty, hawezi, wala kumpa sumu kama Patauli sio rahisi, lakini asingesita kumzawadia risasi ya kichwa wakati wowote atakapoona hana budi. Zaidi, kifo cha Betty yeye, akiwa mtu wa mwisho kuonekana akiingia kwake, kabla maiti yake haijagunduliwa, kwa tabia ya polisi angekuwa mtu wa kwanza kushtakiwa. Na asingekuwa na lolote la kujitetea, wala muda wa kukaa mahabusu kwa miaka kusubiri polisi hao wavivu wampate mwuaji wa kweli au Rais akutetee. Kwa kila hali alilazimika kuanza msako kwa nguvu zaidi. Dawa ya moto ni moto.

‘Waziri Mkuu… kumwaga damu….’ Aliyakumbuka tena maneno ya Betty. Bado hakuona kama yalikuwa na kichwa au miguu. Wala hakujua kama ‘Waziri Mkuu’ lilikuwa jina la mtu, jina la kikundi cha majambazi au cheo cha mkuu wa kikundi cha majambazi. Pengine Betty angeweza kumsaidia kupata walao fununu, lakini amekufa! Joram alifahamu Waziri Mkuu mmoja tu katika nchi hii. Mtu wa pili kwa madaraka serikalini, mtu mkubwa sana. Ni yeye anayeweza kuwa tishio kwa Rais na taifa lake? Ni yeye ambaye anaweza kuwa nyuma ya mauaji haya ya kinyama? Anachotaka ni kipi? Ukuu wa nchi?

Yalikuwa maswali yaleyale ambayo yalimfanya apige hatua moja mbele moja nyuma, maswali ya kupoteza muda. Mtu ambaye angemsaidia alikwisha kufa. Iliyobaki ni yeye mwenyewe kupambana. Njia ilikuwa moja tu, kumwona Waziri Mkuu. Lakini mtu huenda vipi kwa mtu mkubwa kama huyo na kumshutumu kwa mauaji? Na kama kweli ni mwuaji kiasi hicho si atakuwa anajipeleka mwenyewe katika domo la simba lililo wazi, likimsubiri?

Hapana… lazima aende. Walao kumwona tu.
 
Back
Top Bottom