Babu wa Loliondo ageuzwa mradi
Imeandikwa na Marc Nkwame na Veronica Mheta, Arusha; Tarehe: 17th March 2011
WAKATI miundiombinu ikizidi kuharibika Loliondo, Mkuu wa Wilaya ya Ngorongoro, Elias Wawa Lali ameagiza magari kutozwa ushuru na kupiga marufuku waandishi wa habari kumhoji Mchungaji mstaafu Ambilikile Mwaisapile bila kibali.
Marufuku hiyo aliyoitangaza jana, inahusu pia upigaji picha za Mchungaji huyo maarufu kama Babu ambaye anatoa dawa ya magonjwa mbalimbali yakiwamo ya kisukari, Saratani, Kifafa na Upungufu wa Kinga Mwilini (Ukimwi).
Kwa uamuzi wa Lali, magari binafsi hivi sasa yanatozwa Sh. 2,000 wakati makubwa na ya biashara kama mabasi, malori na pick-up, yanayobeba abiria yanatozwa kati ya Sh. 5,000 na Sh. 10,000 na fedha hizo ni kwa ajili ya kuboresha mazingira ya eneo la tiba.
Kwa sasa wateja wa Mchungaji huyo wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), wamekuwa wakilalamikia kuzagaa kwa takataka na uchafu kikiwamo kinyesi cha binadamu huku mvua zikianza kunyesha na kuzua hofu ya magonjwa ya mlipuko.
Kuhusu waandishi wa habari kumwona Mchungaji Mwasapila na hata kumpiga picha, alisema itabidi kwanza kupata kibali kutoka ofisi ya Mkuu wa Mkoa.
Hivi sasa mwandishi yeyote anayetaka kumhoji au kupiga picha yake, lazima aende Arusha katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa kupata kibali maalumu, Lali alisema.
Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Isidori Shirima alipoulizwa alihoji, hakuna kitu kipya, Mchungaji Mwasapila amekwishaeleza kila kitu kuhusu dawa yake sasa ahojiwe nini tena?
Aidha, Mamlaka ya Udhibiti wa Usimamizi wa Usafiri wa Nchi Kavu na Majini (Sumatra) imesema haijaandaa utaratibu wa kudhibiti viwango vya nauli kwa ajili ya magari yanayokwenda Loliondo kupeleka wateja wa Mchungaji huyo, kwa kuwa suala hilo ni la dharura.
Mkurugenzi wa Sumatra wa Mkoa wa Arusha, Ahmadi Kilima, alisema , walikuwa wamesajili mabasi sita yanayofanya safari kati ya Loliondo na Arusha, lakini kutokana na kugundulika kwa dawa hiyo, magari ya aina mbalimbali yamejitokeza kusafirisha abiria.
Alisema, Mamlaka hiyo sasa haiwezi kupanga kiwango cha nauli ya Loliondo kwa magari mengine isipokuwa yaliyosajiliwa, ambayo nauli halali ni kati ya Sh. 13,500 na Sh. 35,000.
Hata hivyo, alisema uongozi wa Arusha na wadau wa usafirishaji, wanalifanyia kazi suala la kupanda nauli ya Loliondo ili kuja na kiwango kimoja.
Alisema, ni vyema suala hilo likafanyiwa kazi haraka ili abiria wajue wanatozwa kiasi gani, kwani suala hilo liko kiholela zaidi kwa kila mmoja kutangaza bei yake.