Marehemu Ayubu Kiguru: Shabiki mkubwa wa Sunderland football club miaka ya 1960

Wewe mzee unapenda sana muunganiko na wafu, eti? Haya Moo kapeleka milioni 100 nenda ukasome khitma mle ubwabwa. Ujue kwa imani za watu wengine ibada za wafu ni dhambi. Mbona unakuwa ni mwenye kuchanganya kila kitu na imani yako?
Mnaharibu uzi hii ni sport na ameshawajibu wengine vizuri tu,heshima kwa watu wazima hasa wanaojibu kiungwana namna hii hauhitaji wazaz wakuambie
 
SIMBA ni ile ya kina Juma Mzee
Kilomoni
Msomali
Kulikuwa Na Dreva Taxi alikuwa anapark club ya SIMBA pembeni alikuwa anaitwa Mzee Mwinyigumba aka Under line
Hiyo SIMBA Mbwiga hawezi kuijua
 
Mzee Mohamed Said, yule kijana aliyetoa kitabu chake cha historia ya soka la Tanzania hivi majuzi angepata faida sana kama angebahatika kukutembelea
 
Sergio,
Maktaba imechoka kwa ajili ya kuhamahama.
Maalim Mohamed Said kwanza natoa salamu kwako pili uniwie radhi kwa kurudisha nyuma uzi wako kwani nimechelewa kuuona,tatu usiwe mnyonge hata siku moja kwa kusema Maktaba yako imechoka ukweli ni kuwa Maktaba iliyochoka ndiyo iliyosheheni hazina ya kumbukumbu
Guasa,
Hii ya Kitwana Popat sijui lilikujaje.
Mwinda Ramadhani ''Maajabu,'' ni ile ''good football,'' yake.
Maalim wangu
Kitwanna Popat na kitwana Douglas ni wachezaji wawili tofauti.
Kitwana Popat ni kitwana Manara na ndiye aliyekuwa Golikipa na akaja kuwa center forward akicheze timu ya Yanga.
Kitwana ni kaka yake Sunday Manara (computer) na Kassim Manara wote walichezea Yanga. Nyogeza ya habari ni Baba yake Mkubwa Hajji Manara Msemaji wa simba kwa sasa!!
Kitwana Douglas huyu ni mchezaji mwingine na alikuwa anachezea Cosmo.
Guasa,
Juma Chogo, ''Mluya'' jitu la Kenya.
Chogo alikuwa akifahamika kwa Chogo Chemba au Chogo Mluya,
Hii Chemba ilikuwa ni aina yake ya kupiga mpira, kwanza mpira anauputa unapaa juu kisha anabutua kwa kuruka juu sasa huo urukaji ndiyo ukitwa Chemba. Huu urukaji wake wakati anafanya hivyo vituko mashabiki wa Simba hulipuka kwa kushangilia sana.
Hivyo ukaigwa na kujulikana kama kupiga Chemba.
 
Maalim Wangu Abdulrahaman Juma ni kweli hakuwa Center half au Mkoba, aliyekuwa akicheza Mkoba ni *Mwamba Kapera,* sikuwahi kumuona hata siku moja Mwamba kapera akicheka hovyo uwanjani!
kitu kimoja naomba nikukumbushe kuhusu Captain Abdulrahrahman Juma mbali na kuitwa cashier alijulikana zaidi kwa jina la LINK MAN ilikuwa kila mpira kona anaenda kupiga yeye na hapo sisi mashabiki wa Yanga tulikuwa tunashangilia kwa sababu alikuwa anapiga kona mpira unakuwa hatari ya kufugwa wapizani wetu.
Sikuwahi kumuona Link man apige kona itoke nje au iwe fyogo wala short corner.
 
Mbetini,
Nashukuru sana kwa kunikumbusha hili jina la Link Man mimi nililisahau.

Hakika Abdulrahman Juma ndiye alikuwa ''corner taker,'' wa Yanga na
kitu kimoja ni kuwa ile mipira yake ilikuwa inaangukia kwenye kichwa
cha Kitwana Manara.

Kumbe wewe Yanga!
Aha!

Hakuna neno bila nyinyi sisi hatuwezi kuwepo na mpira utakuwa hauna
ladha yoyote.

Mara ya mwisho nimekutana na Abdulrahman Juma ilikuwa Mtaa wa
Congo na Uhuru baada ya hapo sikumuona hadi alipofariki.

Allah amrehemu.
 
Mbetini,
Kitwana
wote wawili nikiwafahamu.

Kitwana Douglas tukifahamiana yeye alianza mpira Young Kenya
pamoja na akina Jamil Hizam (Denis Law), Twaha (Briyson)
mdogo wake Jumanne Masimenti, King Kodo, Kesi Kibuda,
Saleh Yongo
...

Kitwana Douglas alikuwa na sura jamil na akivaa vizuri toka udogo
wake na akivaa jezi akipendeza sana.

Iko siku katika miaka ya 1980s nimekutana na Kitwana Douglas
nikamuuliza mbona umeacha kucheza mpira akanijibu kuwa hana tena
''interest,'' na soka.

Nilisikitika.

(Siku hiyo niko Immigration nalipa nipate passport cashier anaepokea
fedha namuona King Kodo kichwa kimejaa mvi).

Kitwana Douglas na Jamil wote baadae wakaenda Cosmo.

Nakuwekea hapo chini picha ambayo pamoja na watu wengine niko mimi,
Saleh Yongo na Adam Juma:


Waliosimama kushoto aliyevaa miwani ni Mwandishi, Saleh Yongo na Adam Juma wote walicheza club za
mitaani pamoja na Mwandishi katika miaka ya katikati 1960 tukiwa shule za msingi.


Saleh Yongo na Adam Juma walikuwa na soka la kupendeza sana na kwa
Yongo yeye katika Young Kenya ndiye alikuwa na umri mdogo sana lakini
aliweza kupata namba kikosi cha kwanza.

Nilikuwa sijamuona Yongo kwa kipindi kirefu sana ingawa mara moja moja
tukiswali pamoja Kichangani.

Siku moja namuuliza Yakub Mbamba (tukimwita Gowon) mmoja wa vijana
wa Kariakoo waliokuwa na soka zuri pia, Saleh sijamuona yuko wapi?

Yakub akanambia Saleh amefariki siku nyingi.
Hili jina la ''Yongo,'' lilikuwa la mchezaji wa Kenya akiitwa James Yongo.
 
SIMBA ni ile ya kina Juma Mzee
Kilomoni
Msomali
Kulikuwa Na Dreva Taxi alikuwa anapark club ya SIMBA pembeni alikuwa anaitwa Mzee Mwinyigumba aka Under line
Hiyo SIMBA Mbwiga hawezi kuijua
Boxboy,
Jina lake ni Habib Segumba.
Alikuwa Patron wa Sunderland.

Msomali alikuwa Yanga kisha Cosmo.
 
Mbetini,
Ahsante kwa kuisifia hii maktaba iliyo mbetembete.
Asubuhi nililkuwa naangalia kitu nimekuta hii:


Kushoto: John Limo, Mbwana Abushiri (Director), Hemed Seif (marehemu) na Saleh Zimbwe wote wamecheza
Timu ya Taifa katika miaka ya 1960 na 1970 na wote wanatoka Tanga.

Wapenda Soka Barzani,
Hao wote nawafahamu vizuri na wakati niko Tanga walikuwa wazungumzaji
wangu.

Alipofariki Hemed Seif niliandika taazia hiyo hapo chini:
HEMED SEIF MTAALAMU WA MASHUTI AMEFARIKI


Hemed Seif


Timu ya Taifa 1960s Kushoto Kwenda Kulia: Hemed Seif, Mbwana Abushiri,
Awadh Matesa, (sina jina lake), John Limo, Mathias Kissa, Abdallah Aziz,
(sina jina), Miraji, (sina jina) Chaki


Waliosimama wa Kwanza Kutoka Kulia Hemed Seif


Hemed Akida Seif

Kushoto Kwenda Kulia: John Limo, Mbwana Abushiri, Hemed
Seif na Salehe Zimbwe


Kushoto ni Marehemu Salim Kajembe na Kulia ni Hemed Seif

Zimenifikia taarifa hivi punde kutoka Tanga za kifo cha Hemed Akida Seif. Hemed Seif amefariki jana baada ya kuugua kipindi kifupi akalazwa hospitali kasha akatoka. Hemed Seif amezikwa leo asubuhi, Jumapili tarehe 13 Aprili 2014 sawasawa na tarehe 12 Mfungo Tisa 1435 na kazikwa kwenye makaburi ya familia yao Magaoni Tanga ambako ndiko alikozaliwa na kuishi maisha yake yote. Huenda leo pakawepo wengi ambao hawamjui Hemed Seif ni nani.

Hemed Seif alikuwa mchezaji mpira maarufu katika miaka ya 1960 na siku zote akivaa jezi na. 10. Hapakuwahi kutokea mchezaji akamnyang'anya jezi hiyo wakati yeye alipokuwa bado anacheza. Jezi namba 10 ilikuwa imegongewa misumari mgongoni kwake. Hemed Seif alikuwamo katika ile timu ya taifa iliyochukua Kikombe cha Gossage mara mbili mfululizo mwaka 1964 na 1965 chini ya kocha Myugloslavia, Celebic.

Sifa kubwa ya Hemed Seif ilikuwa ni kufunga magoli kutoka mbali, yaani nje ya kumi na nane au nje ya ''box,'' kwa mashuti mazito na hapa ndipo palipokuwa na ''uchawi'' wake. Hemed Seif alikuwa mwembamba mrefu na anapokuwa uwanjani ikiwa humjui, picha itakayokujia ni kuwa ni mchezaji ambae mabeki watamzoa kwa vibuyu kirahisi na kumwangusha chini kwa wembamba wake. Lakini haikuwa hivyo kwani ingawa alikuwa mwembamba Hemed Seif alikuwa na kasi na ujanja wa kuwatoka mabeki kirahisi. Zaidi ya hayo miguu ya Hemed Seif ilikuwa ikibeba mabomu na mizinga mizito.

Free-kick'' zote pamoja na ''penalty'' iwe katika timu yake ya Tanganyika Planting Company (TPC) kutoka Moshi au Timu ya Taifa alikuwa anaachiwa Hemed Seif kupiga na kwa hakika mara nyingi sana nyavu ilikuwa lazima zitikisike. Hemed Seif alikuwa mtaalam wa magoli. Mikwaju yake ilikuwa gumzo kwa timu pinzani na magolikipa wote wa Afrika ya Mashariki wakati akicheza katika mashindano makubwa ya wakati huo ya Taifa Cup na Kombe la Gossage. Kombe ambalo likishindaniwa na nchi zote za Afrika ya Mashariki, Kenya, Uganda, Tanganyika na Zanzibar. Hemed Seif katika timu ya taifa alikuwa akicheza na ‘’Director’’ Mbwana Abushiri kuliani kwake na John Limo akiwa mbele katikati ‘’centre forward,’’ au ‘’half back’’ wa kulia. Wingi wa kulia akiwa Sembwana na kushoto Abdallah Juma Aziz.

Nakumbuaka kama jana vile jinsi tulivyokuwa tukilisubiri basi la TPC liingie uwanjani na sisi watoto tukimbilie kuwaangalie wachezaji nyota wa zama zile kama Hemed Seif mwenyewe na kaka yake Marshed Seif, Mbwana ''Director'' Abushiri, Sembwana, John Limo, Awadh Maseta, Ishaka Mzee, Dracula, Emil Benadicto Kondo, Shariff Salim, Hospitali, Okoth ambae alikuwa golikipa wa timu ya taifa Kenya kasha akaja kucheza TPC. Enzi zile takriban timu nzima ya TPC ilikuwa ikichaguliwa katika timu ya taifa. Wachezaji hawa mimi nimewafaidi sana katikia utoto wangu wakija kucheza Ilala Stadium katika miaka ya 1960 katikati.

Lakini kabla ya hapo niliwaona akina Hemed Seif wakati nikiishi na wazee wangu Moshi. Niliwaona wachezaji hawa wakicheza timu ya TPC ikija Moshi, King George Memorial Stadium, Lukaranga kuja kupambana na timu kama Kahe au Tanganyika Coffee Curing Company (TCCC) timu ambazo ndizo zilizokuwa zikishiriki katika ligi Moshi mjini. Kahe ndiyo timu angalau ikijitahidi kutoa upinzani mkali kwa TPC lakini bila mafanikio. Kahe ilikuwa timu ya wafanyakazi katika shamba la mkonge la Kahe na walikuwa na wachezaji vijana wa Kijaluo kutoka Kenya.

Wachezaji hawa wa Kahe walikuwa wakitegemea nguvu zao zaidi ya ujuzi wa mpira. Hapo ndipo palipokuwa na raha kuangalia mpira wa TPC na Kahe wakati nguvu zilipogeuzwa zikawa kichekesho wakati wachezaji wa TPC wakigonga pasi kuanzia nyuma hadi mbele kisha ikapigwa ''back pass na Mbwana wakati mwingine kwa kisigino na Hemed Seif kama vile simba aliyekuwa akisubiri mawindo akapokea pasi bila kutuliza na ghafla nyavu zinacheza.

Mwaka 2000 nilikwenda kufanya kozi Nairobi na mmoja wa walimu wangu alikuwa mchezaji wa timu wa zamani wa timu ya taifa Kenya Mohamed Abdilkadir. Alipojua natokea Tanga akaniuliza kama namjua Hemed Seif. Nilipomweleza kuwa Hemed Sief nikonae barazani kila siku na tunafanya kazi pamoja bandarini alifurahi sana ndipo akanipa kisa chake kuhusu Hemed Seif. Alinambia kuwa yeye katika miaka ya 1960 alikuwa mwanafunzi Chuo Kikuu cha Nairobi na alikuwa akicheza timu ya taifa ya Kenya akiwa katika safu ya ulinzi kama ''half back.'' Anasema siku ilipojuliikana kuwa Kenya watakutana na Tanzania, kocha na wachezaji wenzake walimuonya kuwa awe makini sana na Hemed Seif, amwangalie sana asimuachie hata kidogo kwani ni mfungaji mabao hatari mno.

Mohamed Abdilkadir anasema ikawa sasa kwake ni vitisho wenzake wakimtisha kwa kumpigia makelele, ''Mohamed, Hemed Seif huyo nyuma yako...'' Basi katika mazoezi ikawa ni vicheko na vitisho kwake kuhusu Hemed Seif na mashuti yake. Maelezo haya yakanitia hamu nikamuuliza nini kilitokea Nairobi City Stadium siku ya mechi ya Kenya na Tanzania. Mohamed Abdilkadir alitingisha kichwa akasema,''Bwana ilikuwa kazi. Mimi nilimpania Hemed Seif. Sikuwa nabanduka nyuma yake. Nilikuwa kama kivuli chake, kila anapokwenda niko mgongoni kwake...wapi bwana. Kama walivyonitahadharisha wenzangu kitambo...Hemed Seif alifunga bao kama kawaida yake. Nikakumbuka maneno ya wachezaji wenzangu kuwa Hemed Seif hatoki uwanjani bila ya kutingisha nyavu.'' Hemed Seif alikuwamo katika timu ya Tanzania ilipocheza na timu kali ya daraja la kwanza kutoka Uingereza, West Bromwhich Albion ilipokuja nchini na kucheza na timu ya Tanzania Uwanja wa Taifa (sasa Uwanja wa Uhuru). Kama kawaida Hemed Seif aliwatoka mabeki wa West Bromwhich na kufunga goli. Picha yake ilitoka kwenye ''Tanganyika Standard'' ikimuonyesha Hemed Seif akifunga bao hilo. Huyu ndiye Hemed Seif aliyekuwa msakata kabumbu maarufu.

Hemed Seif alistaafu kazi Tanzania Ports Authority (TPA) Tanga kiasi cha kama miaka kumi iliyopita na tofauti na wenzake wengi aliochezanae mpira wakati mmoja, Hemed alikuwa na maisha mepesi ya kupendeza na alikuwa akicheza mpira na utu uzima wake kila alipopata nafasi. Mmoja wa marafiki zake na mwanabaraza nilipompigia simu kumpa mkono wa pole akanambia kuwa,’’Hemed Seif siku zote alikuwa mwanamichezo hadi umauti ulipomfika.’’ Nilikuwa nikimtania Hemed Seif kuhusu gari zake nzuri za kupendeza alizokuwa akiendesha pale mjini. Yeye alikuwa siku zote akinipa jibu kuwa, ''Ah! Sheikh Mohamed watoto hao wananiletea.''

Nyakati za jioni Hemed Seif alikuwa anapenda kukaa kwenye baraza yao ya ''watoto wa mji,'' akina Said Bembea, Saleh Makubeli na nduguye Athmani Makubeli, Salim Mohamed Kajembe, Mzee Ali ''Ma-White,'' ambao wote ukimtoa Said Bembea wameshatangulia mbele ya haki. Baraza hii ilikuwa kwenye kituo cha kuuza mafuta cha Agip karibu sana na Mkwakwani Stadium ambapo hadi leo napakumbuka maana palikuwa na chai nzuri sana jioni ambayo nikisimama kusalimia wanabaraza watanilazimisha kunywa angalau kikombe kimoja kabla sijashika hamsini zangu. Kituo hiki cha mafuta kilikuwa kikimilikiwa na marehemu Saleh Makubeli. Baraza hii ya Hemed Seif na wenzake ilikuwa baraza ya manufaa ikipigwa adhana wote wananyanyuka kwenda msikiti wa jirani maarufu Msikiti wa Maalim Jumbe kwenda kusali. Hemed Seif alikuwa mtu wa ibada na ukiangalia picha yake na Salim Kajembe utaiona sijda yake jinsi ilivyomuenea usoni.

Allah amsamehe sahib yangu na kaka yangu dhambi zake na amweke mahali pema peponi.
Amin.




Kushoto Kewnda Kulia: Kitwana Manara, Rashid Seif Hemed Seif,
Abdallah Luo


Waliosimama wa Kwanza Kushoto: Hemed Seif


 
Muungwana ni vitendo na huyo ndio Alhaji sheikh Muungwana mzee wngu Mohamed Said ninaye mjua mie safi sna mzee wngu ila naomba nikupe kisa ambacho umewahi kukiandika na kunieleza mara nyingi japo sikumbuki vzuri nafikiri ilikuwa kwenye kikao cha TANU kupitasha wagombewa wao kuna mtu alimuuliza Sir George Kahama swali naweza kusema la kizushi juu Mali zake na kumfananisha na bepari lkn kwa hekima za mwalim nyerere alimkataza Sir George Kahama kujibu swali ilo kutoka na yy mwenyewe mwalim kumjua vzuri Kahama na historia yao nami pia na kuomba sna usiwe unawajibu watu wajinga wajinga na malofa km hao mzee wngu maana kwanza anaonekana ni mgeni mpili uzi unazungumzia mambo mengine na yy analeta mambo mengine unajua dunia yetu ya leo hii chizi au mwenda wa zimu sio mpk avue nguo mzee wngu nina hakika huyo kijana wenzangu Akili zake hazipo sawa
 
Maalim wangu
Allah awa rehemu waasisi wa hizi klabu na wachezaji waliotangulia mbele ya Haki.
Maalim la Uyanga naam mi Yanga damu tena Kwala!,kwenye ukoo wetu wote sisi Yanga kasoro ndugu yangu mmoja ndiyo Abijo.
Maalim katika kuzurura kwangu nimeokota picha ya watani zangu naiweka hapa ili kama kuna mtu anawatambua atujuze,mi nimemtambua mchezaji mmoja tuu ni khamisi Kisiwa.
 
Mbeteni,
Yanga mie ''nawapenda,'' kwa namna yangu ya ajabu kabisa.

Rafiki zangu wengi hadi wachezaji walikuwa ''Kuala Lumpa,'' kama
Elias Michael, Sunday Manara, Juma Matokeo, Leonard
Chitete
lakini tukielewana vizuri sana.

Hili jina Yanga watani zetu tuliwapa kwa sababu Kuala Lumpa kulitokea
machafuko na kila radio katika taarifa ya habari inaanza na habari za
huko.

Sasa tukapatapo silaha ya kuwapigia watani wetu tukawapa jina hilo
Kuala Lumpa.

Elias na mimi sote tulikuwa wapenda kusoma vitabu kwa hiyo
tukiazimana vitabu.

Ahsante kwa picha.

Kuna wengi nawatambua na wengine ni walikuwa wazungumzaji
wangu kama Said Walala, Adam Athmani, Hamisi Kisiwa,
Mbaraka Salum Rwando, Hamisi Kilomoni, Arthur Mambeta,
Hamisi Fikirini, Hamisi Kibunzi
na Emmanuel Mbele.

Wengine hapo ni Haji Lesso Simba wakimuita ''Kiuno,'' Lased,
Mustafa Choteka...

Enzi hizo tukiwapa Yanga bao nne kila wakitia pua Ilala Stadium
sasa sisi tukawaongezea watani wetu jina lingine, ''four, four,'' sawa
na Peugeot 404.

Katika picha yuko na mshabiki mkubwa sana wa Sunderland -
Jumanne Kisukari.

Kisukari
siku za mwisho za uhai wake alikuwa muadhin wa msikiti
wa jirani na nyumbani kwake Magomeni.

Udongo unameza watu.

Kisukari alikuwa akichangamsha na kuweka morali ya wachezaji
juu maana yeye anatangulia mbele na bendera ya Simba kuingia
uwanjani kuanzia enzi ya Ilala Stadium hadi Uwanja wa Taifa.

Bendera yetu ilikuwa na maneno haya, ''Daima Mbele Nyuma Mwiko,''
maana yake sisi tutapambana haturidishi majeshi yetu nyuma.

Hili Yanga wakilijua sana.

Kuna wakati alinunua ''sports car,'' nyekundu.
Yanga walipata sana shida na gari ile.

Na unajua kuwa unazi wa enzi zile ulikuwa wa kufanyiana vitimbi
wala hakuna chuki ndani ya nafsi maana wote wakijuana toka utoto
wao.

Siku moja Yanga wamepigwa mbao na Sunderland na Salum Ali
Sunderland wakimuita, ''Jini,'' alitingisha nyavu kama mara mbili hivi.

Hiyo kombe uwanjani Ilala Stadium.

Siku hizo Yanga wapo Mtaa wa Sukuma karibu na chuo cha Sharif
Abdulrahman
.

Usiku Yanga wako club pale wamejikunyata, wanawaza mabao
tuliowapiga.

Salium Ali kachukua kikombe anakuja kwa miguu hadi Sukuma.
Sunderland siku hizo club yao iko Mtaa wa Kongo.

Kushtuka, Yanga wanamuona Salum Ali huyu hapa keshawasimamia
mbele yao kama jini aliyetumwa.

Salum Ali anawaambia Yanga, ''Nyie Makwala haya nimekuleteeni
kikombe hiki chukueni...''

Yanga wako kimya wanajifanya kama hawamsikii vile.

Basi Salum Ali katamba sana pale na jamaa sasa wamejazana pale
club wanacheka.

Kisha huyo kabeba kombe lake anaondoka anawaambia, ''Haya kama
hamkitaki kikombe mimi nakwenda zangu.''

Jamaa mmoja wa Yanga akasema, ''Wallahi leo Jini katuweza kweli
kweli lakini huyu Salum wewe mwachie tu siku tukiwafunga mimi
nitakwenda kukesha nyumbani kwake namuudhi kama alivyotuudhi
sie leo.''

Washabiki wapenda mpira hawa leo hawapo na Dar es Salaam ile pia
imekwenda zake.

Miaka mingi imepita na nimepoteza mapenzi ya mpira.

Jirani yangu kuna rafiki yangu anaitwa Kambi Kilago, Mzaramo
na sijui kwa nini Wazaramo wanapenda Yanga labda kwa kuwa
viongozi wa juu enzi zile walikuwa Wazaramo kama Kondo Kipwata
kisha Mangara Tabu.

Kambi ana genge jirani yangu anauza matunda na mimi mteja wake
mkubwa.

Nikifika pale namuona Kambi anavyowagaragaza Simba wenzangu
anawafunga mdomo hawana majibu.

Anavyotunanga roho inaniuma lakini nikasema nasubiri hawa Yanga
wafungwe nakwenda kwa Kambi kuweka ligi na yeye, huyu hanijui
mimi.

Basi siku ya siku nikenda kumkomesha.
Weee!

Kafunga mdomo.
Vijana wa mtaani walijazana pale kunisikiliza.

Siku hizi rafiki yangu Kambi kaja na mpya akiniona yuleee nakuja
anajidai anasikiliza simu.

Sikumuacha nikenda kwanza nikapiga wito kuwaita jamaa wanisikize
ninavyomtoa raha Kambi Kilago.

''Kambi rafiki yangu kipenzi ongea na simu lakini najua hiyo ni geresha
unanisikia vizuri sana.

Kama ulivyosema kuwa sisi Simba hatuna mpira wala hatutakwea pipa
kwa muda mrefu na mechi zetu tutaishia na Mtibwa.

Sawa nimekubali lakini nakupa taarifa kuwa tumeagiza majoho mekundu
na vuvuzela nyekundu kutoka bondeni hizi makhsusi kwa kukuzomeeni kila
mkicheza na lazima mfungwe tu.''

Sasa nikimaliza hasira zangu namuuliza Kambi bei ya ndizi.
Ananitajia huku machozi yanamtoka kwa kucheka.

''Kambi mbona unanifanyia aghali mtani wangu au ndiyo haya maneno
yangu?

Usiwasikize hawa jamaa fitna wanataka kutugombanisha mbwiga...''
 
Rubawa,
Mimi sijashangazwa na swali lile kwani haya ni mambo ambayo
nakutananayo kila siku.

Jamaa kilichomsukuma ni udhaifu wa nafsi tu.

Ananisoma na ananielewa lakini akili yake ndiyo inakataa inasema,
''Haiwezi kuwa.''

Hii, ''Haiwezi kuwa,'' inazaa donge katika moyo wake na hili donge
haliwezi kuondoka hadi mimi nipatikane na kasoro.

Yeye kaona hakuna kitu ambacho mimi nitakuwa sina ila hilo la
kisomo.

Ndipo akataka kujua wapi nilipata elimu yangu.
Yeye angetumia akili yake kidogo tu asingetabika.

Mimi maneno yale ya kwenda kiwanjani kucheza mpira huku nina
kitabu,ile mimi na Jumanne Masimenti umri wetu kama miaka 14
au 15 ni watoto wadogo.

Mimi nilimpuuza...

Yule aliyeulizwa swali la kumfedhesha ni Paul Bomani si George
Kahama.


Kisa hiki kilitokea Diamond Jubilee Hall wakati wa uchaguzi wa Kamati
Kuu ya CCM na Bomani alikuwa anagombea.

Muulizaji akataka kumuonyesha Bomani kama mtu tajiri bepari asingefaa
kupewa nafasi ya uongozi katika chama.

Bomani aliposimama kutaka kujibu Nyerere ambae ndiye aliyekuwa
Mwenyekiti akaingilia kati akasema kwa ukali, ''Paul, usijibu...''

Kweli Bomani alikuwa tajiri lakini hakutajirikia katika siasa.

Alikuwa kiongozi wa TAA Kanda ya Ziwa na TANU ilipoasisiwa ilimkuta
na utajiri wake.
 
Mzimu...
Amin kwa sote.

Bahati niliyokuwanayo mimi ni kuwa nilizaliwa hapa Dar es Salaam
kwa hiyo haya yote nimeyaona kwa macho yangu mwenyewe.

Na mimi napenda kuieleza Dar es Salaam kama ninavyoijua.
Maalim wangu jana kwenye baraza yetu nilikuwa nasimulia habari hizi za Marehemu Ayoub Kiguru jinsi ulivyomuelezea humu JF kuna mmoja wa jamaa zangu pale Barazani akaniambia hebu muulize Maalim kuwa unakikumbuka kisa cha marehemu alifungiwa kuingia uwanja wa mpira Ilala Stadium kwa sababu ya maneno lilimtoka kombora kumbe mgeni wa heshima kwenye huo mchezo alikuwa Marehemu mzee karume! Maalim wangu hebu tujuze kidogo hiki kisa.
 
Mbetini,
Nacheka peke yangu nakuomba ruksa niwageukie wanabarza niwaulize swali.
Wanabarza mmeamini kuwa Ayubu Kiguru alikuwa kibiko ya Yanga?

Mnaona huyu Yanga anavyomkumbuka katika barza yake na bila sha hiyo barza
ya watani wangu.

Kisa hiki maarufu.
In Sha Allah nitarejea.
 
Mkuu unafahamu mambo mengi sana kuhusu historia ya nchi yetu kwenye siasa na michezo. Umeshawahi kuandika vitabu kuhusiana na haya? Je, kama vipo vinapatikana wapi na title zake ni zipi? Kama havipo basi fanya hima uandike ili wengi tuweze kuvisoma vitabu hivyo na kujifunza mengi yanayohusu historia ya nchi yetu.
 
Maalim wangu usemacho hakina ubishi hakika Yanga na Simba ni watani wa jadi ila wapenzi wa kila timu tulikuwa na mapenzi ya dhati kwa timu zetu,bahati nzuri Barza yetu ni mseto lakini ukikuta tunavyo interact kwenye Ukwala na Uabijo ni raha tupu.
Maalim sitaki ubishi na wewe lakini Marehemu kiguru haiwezekani awe kiboko yetu,hata kwetu kuna watu ambao walikuwa kiboko kwenu kwa uchache tuu kulikuwa na Marehemu Mnuwili,Samuel Copper,Zoom bila kumsahau Marehemu Tokyo (aliacha kazi UDA kujakuendesha Bus Yanga)! Kwa kumalizia Amiri Mgido Abijo mlikuwa hamuoni ndani.
[emoji3] [emoji2] [emoji3] [emoji1]
 
Cookies are required to use this site. You must accept them to continue using the site. Learn more…