Wakuu, kwanza kabisa nikiri kuwa sijasikiliza kile alichokisema Malinzi kwenye mkutano wake na waandishi wa habari. Lakini pamoja na hilo, ziko hoja kadhaa ambazo zinanifanya niamini kuwa Malinzi hana tena sifa za kuongoza TFF.
1. BILA ACADEMY HATUFIKI POPOTE
Kwa mpenzi yeyote wa soka hii si hoja ngeni kwa nchi yetu. Jambo hili limeongelewa sana hata kabla Tenga hajaanza kuiongoza TFF.
Wakati ni kweli kwamba academies ni msingi mzuri na wa uhakika kwenye soka, si kweli kwamba bila hizo hatuwezi kupata matokeo mazuri. TFF si shirikisho jipya, kipya ni jina tu. Na kama mtakumbuka wakati maalim Muhidin Ndolanga anang'olewa kwa mbinde TFF (enzi hizo FAT), timu yetu ya taifa ilikuwa katika kipindi kibovu sana. Alipoingia Tenga alianza na mtazamo wa kuinua soka la vijana na ndipo hapa tukapata Serengeti boys iliyofuzu michuano ya vijana Africa lakini ikapokonywa ushindi.
Tofauti na kina Malinzi, rais Tenga alitumia mfumo sahihi wa kukuza soka la vijana kwa kuzijengea uwezo klabu la ligi kuu. TFF ilibaki kuwa msimamizi mkuu wa soka la Tanzania ikiwemo kupanga sera. Ni wakati huu ndipo tulipoona hata soka la wanawake likiinuka kwa kasi sana.
Jamal Malinzi na vigogo wenzake wanatumia mfumo opposite na huo ulioanzishwa na akina Tenga. Leo hii vilabu ndio vinatoa pesa kwa TFF kuchangia maendeleo ya soka la vijana ambayo kimsingi hulelewa na vilabu. Swali ninalo jiuliza: TFF ina mpango wa kuanzisha timu zake binafsi? Ama kuna mpango wa kuanzisha Akademi za TFF? Kwani jukumu la TFF hasa ni nini?
Je, Rwanda waliotufunga wana Akademi ngapi? Vipi Uganda, Kenya, Burundi, DRC? Zambia ziko Akademi ngapi? Sipingi hoja ya kuwa na Academy la hasha, ila tu katika taasisi yoyote huwa kuna malengo ya muda mfupi na muda mrefu. Kina Tenga walifaulu kwa kiasi kikubwa sana kwenye malengo ya muda mfupi. Kwa TFF hii mambo ni shagala bagala, hakuna kinachoeleweka. Mapesa yanamiminika TFF halafu wimbo ni ule ule, bila Academy hatufiki popote. Hivi huyu Malinzi amewekwa TFF ili akatafiti sababu ya taifa stars kufanya vibaya, au alete suluhisho la matokeo mabovu?
2. WACHEZAJI HAWAFUNDISHIKI
Kuna mahali nilisoma kuwa Cameroon ni mojawapo ya nchi zenye academies bora kabisa barani mwetu. Nakumbuka nyakati za Malcio Maximo na taifa stars yetu isiyo na Academy. Jinsi tulivyiwanyesha wahitimu wa Academy ambapo almanusuru tufuzu kwa michuano afrika. Ni wakati huu tulipothubutu kuwatunishia msuli miamba wa soka Brazil, huku timu moja ya Academy toka ulaya iliyofuzu world cup tukiinyoa kwa mabao manne.
Nabaki kujiuliza, kutofundishika kwa wachezaji wetu kumeanza lini? Kwa akili ya Malinzi waganda wanafundishika lakini si watanzania. Je, hatukuwa na akina Dani na Simon Sserunkuma hapa Tz? Je, walifua dafu kwa hawa maimuna wetu? Tatizo letu ni nini hasa?
Kwa mtazamo huu wa Malinzi nitashangaa sana kama mchezaji yeyote wa ligi kuu ataitwa timu ya taifa akaitikia wito. Hii ni dharau kubwa sana kwa vijana ambao wanacheza soka la kitabuni wawapo kwenye vilabu vyao.
3. HAMASA YA SOKA KWA TAIFA
Bila kupepesa macho tunarudi zama za giza. Wakati Tenga anaingia madarakani watanzania tulishajitenga na timu ya taifa. Ilibidi ifanyike kampeni kubwa kujaribu kurejesha hamasa ya watanzania kuipenda timu yao. Hili lilifanikiwa kwa kiasi kikubwa sana. Lakini leo tunarudi tulikotoka kwa kasi kubwa ajabu. Watu wamesusa timu ya taifa. Mpira umebaki ngazi ya vilabu ingawa wachezaji inasemekana hawafundishiki.
MTAZAMO WANGU
Kwa kuzingatia haya,sasa ninaamini kuwa Malinzi aliingia TFF pasipo kuwa na maono yoyote. Ameingia akiwa haelewi msingi wa timu kufanya vibaya. Ameingia kwa sababu tofauti na kukuza soka letu.
Namshauri bwana
Jamal Malinzi aachie ngazi kwa amani kuliko kuzidi kulididimiza soka letu. Sasa inatosha, tunahitaji viongozi wenye maono sahihi.