Pole sana mdau, hapa nitaeleza namna ninavyoelewa juu ya swala hili lakini ningekushauri pia upate kupitia
Thread ya 'Utaratibu wa kudai fidia ya bima kwa abiria aliyepata ajali (claim procedure).
Kwa nijuavyo mimi, katika hali ambapo ndugu yako hana bima binafsi lakini ajali ilitokea katika chombo cha usafiri chenye bima, bado ana haki ya kudai fidia. Hii ni kwa sababu kampuni za usafiri zinapaswa kuwa na bima ya abiria ambayo inalinda abiria dhidi ya majeraha au madhara yanayotokana na ajali wakati wa safari. Hapa ni hatua unazoweza kufata ili kulipwa Fidia.
Wasiliana na kampuni ya usafiri ili kupata taarifa kuhusu bima yao na utaratibu wa kudai fidia.
Kusanya nyaraka zote muhimu kama vile ripoti ya polisi, cheti cha matibabu, na mchanganuo wa gharama za matibabu.
Andika barua ya kudai fidia na uambatanishe nyaraka hizo.
Wasilisha barua na nyaraka kwa kampuni ya bima inayohusika na bima ya chombo cha usafiri.
Ikiwa kampuni ya bima itakataa kulipa fidia au kuna mzozo wowote, wasilisha malalamiko kwa Ombudsman wa bima.
Ombudsman wa bima nchini Tanzania ni
Msuluhishi wa Migogoro ya Bima (TIO), ambaye ameanzishwa chini ya
Kifungu cha 122 cha Sheria ya Bima Tanzania ya mwaka 2009. TIO ina jukumu la kusuluhisha migogoro inayotokea kati ya watumiaji wa bima na watoa huduma za bima nchini Tanzania.
Kwa mujibu wa
Kifungu cha 124
kinachohusu
Mamlaka na Majukumu ya Ombudsman
kinaeleza yafuatayo:
Ombudsman ana mamlaka ya kutoa tuzo kwa mlalamikaji kwa ajili ya hasara na madhara ya moja kwa moja ambayo mlalamikaji amepata, hadi kiasi cha juu cha shilingi milioni kumi na tano.
Baada ya kupokea malalamiko, Ombudsman atachunguza malalamiko hayo au kusababisha yachunguzwe.
Kwa madhumuni ya kufanya uchunguzi, Ombudsman atakuwa na mamlaka sawa na yale ya Kamishna chini ya kifungu husika.
Taratibu za kupokea, kusikiliza, na kuamua malalamiko na huduma ya Ombudsman zitaelezwa katika kanuni.
Hii inamaanisha kwamba Ombudsman ana uwezo wa kisheria wa kushughulikia malalamiko na kutoa maamuzi ambayo yanaweza kujumuisha fidia ya moja kwa moja kwa mlalamikaji. Aidha, Ombudsman ana mamlaka sawa na Kamishna kwa ajili ya kufanya uchunguzi wa malalamiko yaliyowasilishwa. Taratibu za jinsi malalamiko yatakavyopokelewa, kusikilizwa, na kuamuliwa unaweza kuzipata
hapa
Ni muhimu kuhakikisha kwamba ndugu yako anafuata utaratibu huu kwa usahihi na kwa wakati ili kuepuka ucheleweshaji wowote katika mchakato wa kudai fidia. Ombudsman wa bima ataweza kusaidia katika kuhakikisha kwamba haki za ndugu yako zinalindwa na fidia inalipwa kulingana na sheria na kanuni zilizopo.