Mtambo Wa Mauti

Mtambo Wa Mauti

Kiongozi ubarikiwe sana. Kwa kweli una stahili nafasi ya mbele kabisa peponi. Hapa nimekaa na kikombe cha tangawizi na karanga, hebu tupia episode kadhaa jioni iwe njema hii.
amina kiongozi, naweka nyingi nyingi ili umalize usiku wako vizuri
 
36.
Kambambaya hakumwelewa. “Ina maana umekosea na kufungua jokofu la maiti nyingine?” alimuuliza daktari huyo. “Hapana, Inspekta. Jokofu hilihili ndilo lililohifadhi maiti ya yule msichana. Na huyu ambaye yumo sasa ni mfanyakazi wetu wa chumba hiki ambaye alikuwa akihudumia mwili huo. Toka jana jioni Supa D hajaonekana. Ametafutwa kila mahali bila mafanikio. Nashangaa kumkuta humu, tena akiwa maiti.” Ndio kwanza ikampambazukia Kambambaya. “Yaani…” alitaka kumuuliza jambo, akasita. Badala yake aliuliza, “Kwa

hiyo maiti tunayoyatafuta yatakuwa wapi?” “Sijui.”

Kwa ushawishi wa Kambambaya daktari huyo alifungua majokofu yote. Kila maiti ilikuwemo, isipokuwa maiti moja tu, ya marehemu Mona Lisa.

Baada ya dakika nyingi za kuirudia tena na tena kazi hiyo na baada ya kupitia kumbukumbu za mapokezi mara mbilimbili, ilikuwa dhahiri Mona Lisa alikuwa ametoweka!



***

Mlipuko wa bomu uliotokea hotelini ulimpa Joram Kiango fursa nzuri sana. Hata kabla kishindo hicho hakijapoa yeye tayari alikuwa amechupa angani na kumfanya atue juu ya mgongo wa mtu aliyeiinamia injini ya gari kwa miguu yote miwili, huku wa pili akiwa amepokea kichwa kilichomfanya aangukie barabarani. Hakuinuka tena.

Mtu wa pili alikuwa mbishi zaidi. Alimtazama Joram kwa mshangao uliochukua sekunde moja tu, sekunde ya pili nafasi ya mshangao huo ilichukuliwa na hasira kali. Huku akivujwa na damu mdomoni alipangua pigo la pili la Joram kwa kukinga mkono huku akiachia teke farasi ambalo Joram Kiango hakulitegemea. Lilimpata barabara kifuani na kumfanya apepesuke. Teke la pili aliliona. Akalidaka kwa kuachia lake lililompata jamaa huyo katikati ya miguu yake, akaanguka akigugumia kwa maumivu.

Joram alimzoa na kumtupa ndani ya gari, kiti cha dereva. Alitaka kumchukua yule wa pili, lakini wakati huo watu walianza kufurika eneo hilo, huku magari yakiwa tayari yameweka msururu. Joram alifanya haraka kufunika boneti





na kisha kuingia kiti cha abiria, bastola mkononi. “Endesha gari,” alimwamuru mtu huyo ambaye bado alikuwa akiugulia, huku akimkuna utosi kwa mtutu wa bastola.

Si kwamba mtu huyo aliwasha na kuliondoa gari peke yake, aliliondoa kwa kasi ambayo Joram hakuitegemea, kuelekea ufukoni akiteremka na barabara ya Maktaba.

“Wewe!” Joram alimfokea, akimpiga kwa domo la bastola.

Ndio kwanza mtu huyo alikanyanga mafuta kwa nguvu zake zote. Akiwa na hakika kuwa mtu huyu alikusudia kuliendesha gari hilo hadi ndani ya Bahari ya Hindi, ambayo ilikuwa hatua chache tu mbele yao, Joram alimsukuma kwa nguvu kwa lengo la kumpokonya usukani. Hakuwahi. Lori lililosheheni masanduku ya bia, ambalo lilikuwa likiingia katika barabara hiyo, kutokea Barabara ya Sokoine, lilikutana nao uso kwa uso. Joram aliliona sekunde moja kabla alijawafikia. Aliwahi kufungua mlango na kuchupa nje ambako alibiringika mara kadhaa kabla ya kusimama na kuitazama ajali hiyo. Gari lile dogo, Toyota Mark II, sasa lilikuwa kama chapati mbele ya scania tani arobaini lililowagonga. Bado akiwa ameng’ang’ania usukani, mateka wake alikuwa sehemu ya chapati hiyo chochote ambacho Joram alikitegemea toka kwake asingekipata tena.

Huku akifuatwa na macho ya watu wenye mshangao kwa kunusurika kwake, Joram alipiga hatua mbili tatu kurudi New Africa, lengo likiwa kumpata yule mtu wa pili ili ajaribu kumdodosa na, hatimaye, kujua kitu gani kinaendelea. Haikuwezekana. Eneo zima lilikwisha zungukwa na polisi. Ving’ora vya magari ya polisi na zima moto pamoja na kelele za raia waliokuwa wakipambana na polisi eneo hilo vilipafanya pawe mahala palipojaa purukushani.

Akiwa hakujiandaa, huku mwanga ukizidi kuongezeka, Joram alijua kuwa ingekuwa hatari kwake kuendelea kukaa katika eneo hilo. Hivyo, alipenya taratibu hadi vichochoroni ambako alitembea taratibu, mkono mfukoni, sigara mdomoni, hadi nje kabisa ya eneo hilo.

Kichwa chake kikiwa kimejaa maswali, vitendawili na mafumbo tele ya kutatanisha, Joram alijua wazi kuwa alihitaji wasaa wa kutulia ili afikiri. Hata hivyo, hakuona kama
 
37.

alikuwa na wasaa huo. Roho yake ilikuwa ikitafutwa kwa udi na uvumba huku jitihada zake za kujificha zikiwa zimegeuka mzaha. Zaidi, kuna huyu Mona Lisa ambaye anakufa na kufufuka kama mchezo wa kuigiza. Hapana, hakuwa na nafasi kabisa ya kuketi mahala popote ili afikiri. Ili kuinusuru roho yake na ili aweze kuipa chakula roho hiyo iliyokuwa na njaa kali ya kukitegua kitendawili hicho kinachoendelea, Joram aliamini kuwa ilimpasa kulala huku akiwa amefumba jicho moja na kutembea huku jicho moja likiangalia mbele na la pili likiangalia nyuma; wakati huohuo akiituma akili yake kufikiri harakaharaka kama kompyuta.

Ni hilo alilolifanya. Wakati akipiga hatua moja baada ya nyingine alijiuliza kilichowawezesha polisi na yeyote yule anayejiita au kuitwa Mona Lisa kumfikia kwa urahisi na haraka kiasi hicho. Kwamba alikuwa amefuatwa toka pale hotelini hadi hospitali alikojificha kamwe hakuhafikiana nalo. Kwamba daktari yule alikuwa ‘amemuuza’ kwa kutoa siri ya maficho yake hilo hakuliafiki vilevile, kwani alikuwa na hakika kwa asilimia mia moja kwamba daktari yule alikuwa hamfahamu na alidanganyika zaidi kwa mavazi, sura na majina yake ya bandia.

Kitu gani basi kilifanya maficho yake yabainike mara moja? Alijiuliza akiutia mkono mfukoni na kuangalia vitu alivyokuwa navyo. Isipokuwa kwa simu yake ndogo ya mkononi na pesa chache alizochukua benki, mifuko yake ilikuwa mitupu. Mzunguko wa pesa ni jambo mojawapo ambalo hufichua maficho ya watu wengi. Mara nyingi polisi wazoefu, hasa wale wa INTERPOL, hufuata mkondo wa pesa hata kubaini wapi alikojichimbia mtuhumiwa, hasa anayetuhumiwa kuiba pesa nyingi. Joram alijua wazi kuwa hilo halikufanya maficho yake yagundulike haraka kiasi kile, kwani hakuwa ametumia fedha nyingi na hizo chache alizotumia mzunguko wake usingeweza kuwa wa haraka kiasi kile. Hivyo, wazo hilo alilitupa kando.

Simu! Akakumbuka. Akiwa pale kitandani aliitumia simu yake kutuma ujumbe wa maandishi. Pamoja na ukweli kuwa aliinunua simu hiyo kwa jina la bandia lakini kwa jinsi alivyokaa nayo muda mrefu siku zote alishuku kuwa polisi walikwishainasa namba hiyo na wanamfuatilia. Hakuwa na





shaka tena kuwa ujio wa haraka wa polisi katika eneo lile la Manzese ulitokana na ujumbe ule. Isingekuwa kazi kubwa kwao kwenda kwa kampuni inayoendesha simu hizo na kujua eneo ambalo simu hiyo ilitumiwa. Sitaitumia tena, aliwaza.

Joram aliamini kuwa alikuwa ametegua kitendawili kimoja. Hata hivyo, alijua fika kuwa kitendawili hicho kilikuwa kimoja tu kati ya vingi vilivyomtinga. Bado alihitaji kufahamu kwa nini polisi watumie nguvu nyingi kiasi kile. Zaidi ya wao, alijua kuwa zaidi ya polisi walikuwapo watu au kikundi cha watu ambao, kwa njia moja au nyingine, walikuwamo katika kasi ya kuisaka roho yake. Hakuona kuwa watu aliojaribu kuwateka pale New Africa ni polisi. Hali kadhalika, mwanamke anayejiita Mona Lisa na mwenye sauti ya Mona Lisa hakuonekana kuwa polisi. Aidha, hakuona vipi kifo cha msichana mmoja tu kiwe kisa cha purukushani kali na nzito kiasi hiki. Juu ya yote hayo hakuona uwezekano wowote wa simu ile kumwezesha binadamu yeyote kubaini jina la bandia aliloandikisha kwa daktari na kulitaja kwa ufasaha jina la hayati Mona Lisa, huku sauti ikiwa imefanana vilivyo na ile ya marehemu yule.

Vitendawili au mafumbo hayo vilifanya kitu fulani kiamke katika nafsi yake taratibu, kitu kisichoelezeka, kitu kilichokuwa katika usingizi wa pono. Naam, kitu ambacho kilianza kumpa hamu na shahuku kubwa ya kulikabili jambo hili badala ya kuwa mkimbizi anayekimbiza ubawa wake kama kunguru mwoga.

Wakati akiwaza hayo, alikuwa katika Mtaa wa Samora, ambao tayari ulianza kufurika watu wenye shughuli zao. Joram aliuendea mmoja wa migahawa michache mtaani hapo na kujipatia kahawa ya moto na sambusa mbili. Toka hapo akaingia duka moja la nguo ambamo aliagiza mavazi ambayo hakupata kuyavaa kwa muda mrefu; suruali nyeusi ya jeans na jaketi lake. Pia, alinunua kofia pana ambayo alipoivaa ilifunika sehemu kubwa ya sura yake. Vitu vyote hivyo alivivaa papo hapo dukani. Hivyo, alipotoka alikuwa mtu mpya, tofauti kabisa na yule mzee mchafumchafu aliyeingia dakika tano zilizopita.

Toka hapo Joram aliifuata tena Samora, safari hii akielekea magharibi. Kwenye makutano ya mtaa huo na Barabara ya





Morogoro lilipo jengo kubwa la watoza ushuru, TRA. Kando ya jengo hilo kuna moja kati ya maduka mapya ya silaha yalioanzishwa karibuni. Kwa kuachia ‘kitu kidogo’ aliweza kuushinda urasimu uliowekwa kwenye biashara hiyo na kuruhusiwa kununua bastola mpya, kopo moja la pilipili za kujihami na baada ya kuwaza sana; pingu.

Alijaza kijanja fomu zote zilizohitajika na kuahidi kumalizia hatua zilizobakia, za kuipeleka bastola hiyo polisi hadi kamati ya Silaha ya Mkoa itakapoketi, kamati ambayo Joram alifahamu kuwa kutokana na wingi wa vigogo waliomo na uzito wa shughuli zao, inaweza kukutana baada ya miezi sita! Akajiona kuwa kiasi amekamilika. Joram alianza safari yake nyingine. Safari hii alielekea Mnazi Mmoja, katika bustani ya Jiji, ambako aliingia. Kati ya vivutio vya bustani hiyo ipo sanamu ya mzee mmoja anayepiga ngoma, sanamu ambayo kwa namna fulani imejengewa katika kitu kama pango, ambalo enzi za neema liliongeza uzuri wa mandhari kwa kujazwa maji. Kwa sasa, likiwa kavu, shimo hilo lilimfaa sana Joram Kiango, kwani mmoja wa wasiri wake alikuwa akilitumia kumletea taarifa alizohitaji toka ndani ya Jeshi la

Polisi.

Ujumbe ule alioutuma, ambapo uliandikwa kwa maneno machache, ndani ya fumbo ambalo mtu yeyote asiyekusudiwa asingeweza kuuelewa; alivyomfahamu ‘rafiki’ yake huyo alijua, ungekuwa umefika.

Ndani ya bustani hiyo Joram Kiango aliketi kwa takribani dakika ishirini hivi, katikati ya kundi la vijana wa mjini watatu, ambao hawakuchelewa kum’bom’ sigara na kisha kumshirikisha katika maongezi yao. Walikuwa wakijadili uwezo wa wachezaji wa timu za Uingereza, Manchester United na Liverpool. Pamoja na ukweli kuwa Joram hakuwa mjuzi sana wa masuala ya soka, bado hakushindwa kutia neno hapa na pale, jambo lililofanya akubalike.

Laiti vijana hao wangejua jinsi macho ya Joram yalivyokuwa makini, yakitazama huko na huko kuona kama kulikuwa na mtu yeyote wa kumtilia shaka. Hakuwepo. Hali ilikuwa ya kawaida kabisa. Polisi mmoja pale, muuza kahawa mmoja pale, wamachinga wawili kule, kila mmoja akiwa na hamsini





zake. Hivyo, hakuna aliyeona pindi Joram alipo ‘teleza’ na kwenda chini ya sanamu ile ya mpiga ngoma na kuchokonoa chini ya kigoda alichokalia ambapo aliokota karatasi iliyokunjwakunjwa, yenye harufu ya shombo la samaki, ambayo alilitia mfukoni na kwenda sehemu yenye usalama zaidi, ambako aliifungua.

Ulikuwa ujumbe mfupi, ulioandikwa katika mafumbo vilevile. Joram aliutafasiri. Ulisema;

Unatafutwa kwa udi na uvumba. Vikosi vyote vya usalama vimewekwa katika hali ya hadhari.

Marehemu aliyefariki hotelini ametoweka Muhimbili. Maiti yake yanasakwa huku na huko.

Watu wanakufa hapa na pale. Polisi wanne, daktari mmoja, Manzese. Wahudumu watatu New Africa. Hali inatisha…

Habari, ambayo Joram aliiona katika taarifa hiyo ilikuwa ya kutoweka kwa mwili wa Mona Lisa Muhimbili! Kwa nini maiti yaibiwe? Nani ameyaiba? Kwa faida ya nani? Na kutoweka kwa maiti hayo kunahusiana vipi na mwanamke ambaye amekuwa akimtokea kila anakotorokea na kujiita Mona Lisa? Au ni kweli kuwa Mona Lisa aliyekufa amefufuka?

Joram hakuwa mtu wa kuamini katika miujiza. Hivyo, asingependa kuamini hilo pia. Hata hivyo, kwa kila hali habari hiyo ilikuwa juu ya furushi kubwa la utata, furushi ambalo alihisi likizidi kumwelemea. Furushi ambalo ilikuwa lazima alitue haraka, kwa bei yoyote ile.
 
38.


W 6 X

EJA Beka Mfumue alikuwa amelitumikia jeshi la polisi kwa takribani miaka ishirini sasa. Tangu alipomaliza masomo yake ya sekondari na kuchaguliwa kujiunga

na polisi hajapata si kuacha kazi pekee, bali kufikiria kuacha kazi. Ndiyo, mshahara ulikuwa hauridhishi kama ilivyo kwa watumishi wengine, hasa walio katika sekta binafsi. Ndiyo, kazi zilikuwa nyingi na shukrani haba. Lakini, pamoja na hayo yote, Mfumue aliipenda kazi yake, aliipenda sana kwani si kila kazi iwezayo kukupa hadhi na mamlaka mitaani kama ya polisi.

Hivyo, alipojikuta kasimama mbele ya Insepkta Haroub Kambambaya, akihisi macho yake makali yanapenya hadi ndani ya moyo wake, hakuwa na shaka kuwa mwisho wa uhai wake katika jeshi hilo ulikuwa umetimia.

“Unajua kuwa kama hutatoa ushirikiano tuna haki ya kukuhukumu kijeshi? Na hata tukikushitaki kiraia unajua kuwa tutakushitaki chini ya sheria mpya ya ugaidi? Kambambaya alikuwa akiendelea, nusu akizungumza katika hali ya kawaida, nusu akifoka.

“Najua,” Mfumue alijibu.

“Kama unajua sasa utatuambia ukweli. Yuko wapi Joram Kiango?” alihoji, macho yake bado yamekazwa barabara kumtazama Mfumue.





Katika hali ya kawaida Beka asingestahili kusimamishwa mbele ya mtu huyu ambaye zaidi ya kuitwa Inspekta cheo chake halisi hakikufahamika, mtu ambaye mara kwa mara anaitwa Inspekta tu, ingawa vikao vyake vingi humuweka pamoja na majeruhi wakuu wa majeshi yote, mtu ambaye mara nyingi huwa mwenyekiti wa vikao hivyo. Hivyo, meja Beka alijua kuwa ili kuuvuka mtihani huu mkubwa wa uhai wake alihitaji kuituliza vizuri akili yake. Jikaze, alijinong’oneza. Kukubali kiasi fulani cha ukweli siku zote huwa ni dawa katika hali kama hii.

“Natumaini sauti yangu inasikika vizuri Meja,” Kambambaya alirudia. “Yuko wapi Joram Kiango?”

“Sijui,” Mfumue alijibu. Lilikuwa jibu la kweli.

“Toka alipokupigia simu ile hamjapata kuwasiliana tena?” “Bado,” jibu jingine la kweli.

Kambambaya alimkazia macho kabla hajauliza, “Una hakika?”

“Ndiyo.”

“Ujumbe aliokutumia uliandikwa katika hali ya fumbo.

Alitaka nini?” Kambambaya alihoji ghafla.

Mtego, Beka aliwaza. “Alitaka msaada,” akamjibu. “Msaada gani?”

“Habari.” “Habari gani?”

“Alitaka kujua kama kuna habari au tukio lolote la kusisimua, lililotokea karibuni, ambalo linafuatiliwa na polisi,” nusu lilikuwa ukweli nusu uongo.

Kambambaya pia alihisi hivyo. Alimkazia Beka macho kwa muda kabla ya kuuliza taratibu, “ Kama tukio lipi?”

“Kama mauaji, wizi wa fedha nyingi, ugaidi na mambo kama hayo. Joram ni mshabiki mkubwa wa mambo hayo…”

“Ulimjibu nini?” Kambambaya aliuliza ghafla.

Mtego. Meja Mfumue aliwaza. Akaamua kutoa uongo wake wa kwanza, “Bado sijamjibu.”

“Kwa nini?”

“Sijapata nafasi,” uongo mwingine. “Vilevile,” aliongeza. “Sijawa na jambo lolote ambalo linaweza kumsisimua.”

Sasa Kambambaya alikuwa na hakika kuwa Meja Beka





alikuwa hasemi ukweli. “Meja,” akaita kwa sauti yenye hasira kidogo. “Unajua kuwa unajiweka mahala pabaya? Unafahamu hilo?”

Beka naye alianza kuchoshwa na vitisho hivyo, akamwambia, “Inspekta, na wewe unajua kuwa toka umeniita hapa na kuanza kunisaili kama mhalifu hujaniambia kosa langu?”

“Hujui kosa lako?” Kambambaya alishangaa. “Hujui kama umekiuka kiapo chako cha kutotoa nje siri za jeshi? Huoni kama huo ni uhaini? Hujui kama kumsaidia mhalifu ni uhalifu? Alihoji, kwa mbali akitwetwa.

“Sijatoa siri yoyote Inspekta,” Meja Mfumue alisisitiza. “Na kuwasiliana na Joram Kiango ninayemfahamu mimi sidhani kama ni uhaini wa aina yoyote. Hakuna asiyejua mchango na harakati zake zilivyoinusuru nchi hii na Afrika nzima mara kwa mara. Kama ni mhalifu basi leo ndio nafahamu, toka kwako.”

Kambambaya hakuutegemea ujasiri huo toka kwa Meja Beka Mfumue. Kwa ujumla, alitumia njia ya vitisho kwa matarajo ya kupata chochote ambacho kingemsaidia kumpata Joram Kiango. Alikuwa na kila sababu ya kuamini kuwa kumpata Joram ilikuwa sawa na kuupata ufunguo ambao ungemfungulia mlango wa siri ya mikasa na maafa haya makubwa ambayo yanazidi kutokea.

Awali, ilianza kama mauaji ya kawaida, ambayo kwa kila hali inafanya Joram Kiango awe mtuhumiwa wa kwanza. Katika kumtafuta Joram Kiango yakaibuka mauaji makubwa zaidi; polisi wanne, daktari mmoja Manzese. Mgonjwa wa bandia aliyesababisha yote hayo si mwingine zaidi ya Joram Kiango.

Kana kwamba hayo hayatoshi, alfajiri hiyohiyo iliambatana na habari za kutisha zaidi. Tukio la mapambano makali ya silaha na mlipuko wa bomu la mkono katika hoteli ya New Africa, lililopelekea vifo vya watu watatu, watumishi wawili wa hoteli na mtu mmoja anayedaiwa kujibamiza mwenyewe kwenye gari kubwa kwa kila hali lilikuwa chachu nyingine ya kumpata upesi zaidi Joram Kiango.

Tukio hilo lilimfikia kwa taarifa ya maandishi. Ilikuwa baada

ya kutoka hospitali ya Muhimbili, ambako alishuhudia maajabu
 
39.

ya kutoweka kwa mwili wa marehemu ambaye anaelekea kuwa chanzo cha zahama hii alikuta jalada likimsubiri juu ya meza yake. Lilikuwa bado halijakamilika. Hivyo, lilieleza kwa ufupi tu, kama taarifa, juu ya yaliyotokea hotelini hapo, kwamba alfajiri hiyo. Mzee mmoja mchovumchovu alitokea mapokezi na kutaka chumba. Wakiwa na hakika kuwa hangekuwa na uwezo wa kulipia bei ya vyumba vyao walimwambia kuwa kuna vyumba. Kwa mshangao mzee huyo alitoa pesa na kukabidhiwa chumba chake, kwamba muda mfupi baada ya makabidhiano alitokea mgeni mwingine, mwanamke, ambaye alitaka kumwona mzee huyo. Walizungumza kidogo kwenye simu kabla mama huyo hajapanda lifti kumfuata mzee huyo ghorofani.

Mtoa habari huyo, ambaye ni mmoja wa wapokeaji wageni aliyekuwa zamu, anasema toka hapo hakumbuki kilichondelea kwani ulifuatia mlipuko mkubwa wa bomu ambao ulimfanya yeye na kila kitu ukumbini hapo wapae angani na baadaye kutua chini wakiwa nyang’anyang’a, yeye akiwa amevunjika miguu yote miwili na kuungua sehemu kubwa ya kichwa na kisogo. Alitoa taarifa hiyo akiwa Muhimbili, kitengo cha MOI, ambako anapatiwa matibabu.

Jambo lililofanya Kambambaya ahisi kuwa mzee yule, pale New Africa hakuwa mwingine zaidi ya Joram na taarifa alizoziandikisha:

Jina: Kondo Mtokambali! Kabila: Mtanzania!

Anakotoka: Dar es Salaam. Anakokwenda: Dar es Salaam

Majibu hayo na uwiano wa muda toka lile tukio la Manzese hadi lile la katikati ya mji, pamoja na mlolongo wa matukio, yaliyofuata ndivyo vilivyomfanya Kambambaya asiwe na chembe yoyote ya mashaka kuwa Joram Kiango yumo katikati ya dimba hilo.

Hivyo, wafumbuzi wa mafumbo walimthibitishia kuwa ile simu ya maandishi ilitoka kwa Joram Kiango pamoja na kumpatia jina la mmoja wa maafisa wa polisi, ambaye alipelekewa ujumbe ule, Kambambaya hakuona kama ilimpasa kuvuta subira. Alimtaka Joram Kiango. Na alimtaka





haraka sana, kabla ya maafa zaidi kutokea. Ndipo akataka aitiwe Meja Beka Mfumue na kumketisha mbele yake huku akimsukumia vitisho kwa matarijio ya kupata ukweli mara moja.

Hivyo, Mfumue alipobadilika na kuipoteza ile hali ya ushirikiano aliyoionyesha mwanzo wa mahojiano hayo, Kambambaya alianza kuuona ugumu wa kazi iliyokuwa mbele yake. Ni kweli kuwa katika hatua hii alikuwa hana namna ya kumtuhumu Meja Mfumue kwa lolote. Kwa mujibu wa Katiba ya Jhamuri ya Muungano wa Tanzania Meja Mfumue, kama mtu huru, ana haki na uhuru wa kukutana na mtu yeyote huru, kuzungumza naye na kushirikiana naye, mradi hawavunji sheria. Joram bado alikuwa mtu huru. Tuhuma juu yake, pamoja na yote yanayoendelea kutokea, bado zilikuwa ni hisia tu, hadi pale itakapothibitika vinginevyo.

“Sikiliza Meja,” Kambambaya alitamka ghafla, akimkazia Mfumue macho. “Kwa sasa unaweza kusema chochote unachojisikia kusema. Lakini unafahamu vizuri sana kuwa kuna mambo ya kutisha ambayo yametokea katika saa ishirini na nne zilizopita, mauaji ya watu wasio na hatia, milipuko ya mabomu; na mengineyo. Nadhani unafahamu pia, kwa njia moja au nyingine, kuwa Joram Kiango anahusika au kuhusishwa na hali hii. Hivyo, lazima apatikane, haraka iwezekanavyo. Wewe kama afisa wa jeshi, kama mtu uliyekula kiapo cha kuilinda na kuitetea nchi hii, una wajibu wa kusaidia kufanikisha jitihada hizi. Uongo?”

“Kweli, mzee.”

“Na utatusaidia haraka zaidi kwa kutuwezesha kumpata, au walao kuwasiliana na Joram Kiango. Uongo?”

“Kweli.”

“Kwa hiyo,” Kambambaya aliongeza. “Kama kweli hujaujibu ujumbe wake wa maandishi nenda kaujibu. Mpe maelekezo ya kukutana naye mahala. Utajua namna ya kumweleza. Lakini hakikisha unaniarifu, mimi binafsi, maendeleo ya jitihada hizo. Kuanzia leo, mimi na wewe tutakutana kila siku jioni, ili unipe taarifa za jukumu hilo. Sawa?”

Halikuwa ombi. Ilikuwa amri. Mfumue hakuwa na kauli zaidi ya “Sawa, Inspekta.”





Ulikuwa mtego mwingine kwa Meja Beka. Kitu ambacho hakujua, kitu ambacho wengi hawajui, ni kwamba ziko njia nyingi za kunasa ujumbe wa maandishi toka simu yoyote ya mkononi kwenda nyingine. Moja wapo ya njia hizo ni kile ambacho watu wengi hawajui, kuwa ujumbe unapotumwa toka simu fulani hubakia ndani ya simu hiyo hata kama umeufuta. Zamani kidogo ujumbe huo ulikuwa unakaa katika kadi. Siku hizi, baada ya maendeleo zaidi katika teknolojia, ujumbe huo hukaa katika hifadhi ya kumbukumbu. Simu za kisasa zaidi huweza kuhifadhi maelfu ya ujumbe wa maandishi. Hivyo, mtu akiinasa simu yako anaweza kusoma simu zako mbalimbali za maandishi bila mwenyewe kujua.

Lakini kuna njia nyingine, ya uhakika zaidi. Unapotuma ujumbe wa maandishi, ujumbe huo hupitia katika kituo chako cha mawasiliano, hapa nyumbani vituo maarufu vikiwa ama Vodacom, Airtel, Zantel au Tigo. Hawa, pamoja na kuupeleka ujumbe wako kama ulivyoagiza, nakala ya ujumbe huo hubakia katika hifadhi yao kwa muda mrefu. Kumbukumbu ya simu iliyopigwa huweza kuhifadhiwa kwa kati ya miezi sita hadi miaka mitano kabla ya kuteketezwa. Hivyo, mtu yeyote mwenye nyenzo na utaalamu angeweza kuchimba katika msitu huo wa ‘meseji’ na kupata kile anachokitafuta.

Kambambaya alilijua hilo. Na tayari watu walikuwa kazini kuchimba chochote ambacho kilikuwa kimepita baina ya simu ya Joram Kiango na Meja Beka, au mtu mwingine yeyote, katika siku hizo mbili tatu.

Hivyo, kama Meja Beka alidhani angemlaghai Kambambaya, Kambambaya aliamini kuwa angekuwa akijidanganya mwenyewe.



***

Toka bustani ya Mnazi Mmoja Joram aliifuata Barabara ya Lumumba na baadaye kuingia ya Uhuru, akielekea Kariakoo. Alihitaji nafasi ya kutulia ili awaze na kuwazua hadi atakapokifikia kiini cha fumbo au kitendawili hiki, utulivu ambao, kwa hali ilivyokuwa aliamini kuwa hakuna mahala pengine ambapo angeupata zaidi ya katikati ya msongamano wa watu. Utulivu wa aina yoyote mwingine, kama ule





alioutafuta wodini Manzese na hoteli ya New Africa tayari ulikuwa umepelekea kutokea kwa maafa makubwa. Mitaa ya Kariakoo, hasa ile ya Msimbazi na Kongo, kwa vyovyote vile, ilikuwa sehemu muhafaka kwa sasa. Pamoja na maafa yote hayo bado Joram hakuamini kuwa yeyote huyo anayemfuatilia angeweza kuuteketeza mtaa mzima uliofurika watu kwa ajili ya roho moja, Joram Kiango.

Akiwa katika mavazi yaliyomfanya afanane sana na mamia ya vijana wa mitaa hiyo, kofia pana ikiwa imefunika uso wake, Joram alitembea mtaa huu hadi ule bila wasiwasi wowote. Alikuwa mmojawao, mmoja wa Wamachinga, mmoja wa wabangaizaji wa jiji la Dar es Salaam ambao kwao vumbi, jasho na msongamano ni sehemu tu ya maisha yao katika jitihada za kutafuta riziki ya siku hiyo.

Lakini kama mtu angebahatika kuingia katika kichwa chake angeshuhudia jinsi ubongo wake ulivyokuwa kazini, ukiwaza kwa nguvu zake zote, wazo kubwa zaidi likiwa ni kujaribu kutafuta kiini cha maficho yake yote kugundulika mara moja kana kwamba alikuwa akijianika hadharani huku akipiga mbiu kumwashiria adui yake wapi aliko.

Ndiyo, alibaini madhara ya simu na kuitupilia mbali. Hata hivyo, bado aliamini kuwa haraka iliyotumika kumfikia kule Manzese haikotokana na matumizi ya taaluma hiyo dhidi ya simu za mkononi. Kwa vyovyote, ingechukua muda, ikiwa pamoja na kulikagua eneo la mraba lisilopungua ekari tano kabla ya kubaini mahala alipo. Hali kadhalika, taaluma hiyo ilifanikiwa pale tu mwenye simu hiyo anapoitumia. Joram hakuwa amepiga wala kupigiwa simu pale New Africa. Waliwezaje kufika haraka kiasi kile?

Huku akitembea aliendelea kujikagua kuona kama alikuwa na chombo chochote kingine kinachoweza kutumiwa kusafirisha mawasiliano. Aliitoa kalamu yake na kuitazama. Ilikuwa aina ya packer, ya kawaida kabisa, tena iliyonunuliwa toka kwa mmachinga. Aliitazama saa yake, Omax, ambayo amekuwa nayo miaka sita sasa. Hajawahi kumwazima mtu, wala haijawahi kwenda kwa fundi ambako ingewekewa kwa siri vyombo vya mawasiliano.

Ni wakati akiitazama saa yake hiyo, alipoiona ile pete
 
40.

kubwa ya Mona Lisa, ikiwa imetulia katika kidole chake. Joram alikumbuka vizuri kilichopelekea pete hiyo iwe hapo kidoleni pake.

“Unaogopa!” “Naogopa nini?” “Mchumba wako.”

“… Mchumba! Mchumba gani? Mie bado niko single. Sina mume wala mchumba.”

“Umeanza kuwa mwongo… pete hiyo hapo inakusuta. Kama sio ya uchumba ni ya ndoa…”

Maongezi baina yake na Mona Lisa, yakiwa mzaha tu, lakini uliopelekea Mona Lisa kuivua na kumwachia Joram Kiango pete hiyo.

Ingawa maongezi hayo yalifanyika siku mbili tatu tu zilizopita, Joram aliyahisi kama yaliyofanyika miaka nenda rudi, kwa jinsi matukio mengi na ya kutatanisha yalivyolifuatia tukio hilo. Joram aliitazama kwa makini zaidi pete hiyo, pete ya Mona Lisa; msichana aliyemfia mikononi mwake huku yeye akiwa usingizini kama mzoga, msichana ambaye mauti yake yamejaa utata mkubwa. Alikufa… yeye mwenyewe aliushuhudia mwili wake pale kitandani… mara mwili huo unadaiwa kutoweka toka katika chumba cha maiti… mara sauti ya Mona Lisa huyohuyo ikimfikia Joram na kumtaka wakutane… sauti ambayo mara zote ilifuatiwa na umwagaji mkubwa wa damu, bila shaka za watu wasio na hatia.

Joram alichunguza kwa makini zaidi pete hiyo. Aliyaamuru macho yake kupuuza mng’aro wa madini yaliyotumika kuitengeneza, badala yake akayakaza kutazama ndani kabisa ya ua hilo lililokuwa likimeremeta. Akahisi kuona kitu cha ziada, kitu kidogo sana, kilichokaa katikati ya ua hilo, ambacho kilikuwa hakimeremeti pamoja na pete nzima. Joram alishuku jambo. Akaipeleka pete hiyo sikioni na kusikiliza kwa makini. Kama alivyohisi, kwa mbali sana alisikia mlio wa tik-tak-tik- tak toka katika pete hiyo.

Joram akatabasamu. Hakuwa na shaka tena kuwa amebaini kisa cha kufanya maficho yake yawe yakibainika ghafla kila mara. Chombo hicho kidogo, kilichofichwa ndani ya pete hiyo, bila shaka kilikuwa aina fulani ya mtambo wenye nguvu





za kieletroniki, ambazo zilimwezesha mtu fulani, mahala fulani, kujua pete hiyo ilipo na, hivyo, kuweza kumpata kila alipojichimbia.

Hata hivyo, kwa Joram Kiango ugunduzi huo bado haukuwa ufumbuzi. Kwa ujumla alihisi kama ulikuwa nyongeza tu ya utata mzima. Hakuwa na shaka kuwa pete hiyo ilibeba chochote cha mawasiliano, kilichokuwa kikiyafichua maficho yake. Lakini kilichomtatiza ni jinsi alivyopata pete hiyo. Kwa kila hali, Mona Lisa alikuwa amempa kimapenzi tu, bila ajenda yoyote ya siri. Na hakuitoa mahala pengine zaidi ya kidoleni, alipokuwa ameivaa. Wala hakuifanyia utaalamu wowote kabla ya kumkabidhi. Kama hivyo ndivyo, Joram aliwaza, ni wazi kuwa Mona Lisa mwenyewe alikuwa akiitumia bila kufahamu matumizi yake. Kwa maneno mengine, ni kwamba mtu ambaye amekuwa akimfuatilia yeye, bila shaka amekuwa akimfuatilia Mona Lisa pia. Na kama huo pia ndio ukweli ni wazi kuwa mtu huyo ama ndiye aliyemuua ama anahusika sana na kifo chake, aliwaza.

Mawazo hayo yaliibua maswali mengi zaidi, ni nani huyu mtu? Alitaka nini kwa Mona Lisa? Mswada wa “Ubongo wa Mwalimu Nyerere?” na kama ni ule kwa nini alimuua Mona Lisa badala ya kuuchukua tu na kuondoka? Na kwa nini alimwacha yeye akiwa hai badala ya kumuua pamoja na Mona Lisa? Hlafu, kama aliamua kumwachia kwa nini sasa anamwinda huko na huko? Na huyu msichana anayejiita Mona Lisa, mwenye sauti kama ya Mona Lisa, ambaye amekuwa akizuka kama kizuka kila anapojificha, ni nani na anahusika vipi na yote hayo?

Msitu wa maswali ulikuwa mpana sana. Joram alihisi kuwa angeweza kutembea kwa miaka katika msitu huo na asipate jibu, kama angeendelea kuwa mtu wa kuwindwa badala ya kuwa mwindaji, mtu wa kutafutwa badala ya kutafuta. Akafanya uamuzi. Toka dakika hiyo atakuwa mwinda badala ya mwindwaji.

Akaiinua pete ya Mona Lisa na kuibusu. Pete, aliinong’oneza, ni wewe utakayenipeleka mbele ya adui kama ulivyomwezesha adui kufika mbele yangu. Utake usitake.

Baada ya sala hiyo aliirejesha kidoleni huku akiendelea





kupigana vikumbo na wapita njia wenzake waliofurika mitaani.



***

Kwa Papaa Mulumba mchana wa siku hiyo ulijaa maajabu ambayo hakupata kuyaona tena maishani mwake. Kwanza kabisa, alikuwa mkavu kabisa mfukoni. Alifika kazini hapo kibahatibahati baada ya kutumia utoto wa mjini uliomlainisha kondakta wa daladala apokee shilingi mia mbili tu, badala ya mia nne ambayo ni nauli halali. Kutwa nzima hiyo alijaribu kuchora kila aina ya mchoro ili apate walao elfu moja ya kianzio bila mafanikio. Ghafla sasa hivi alikuwa na shilingi elfu hamsini zilizomjia “hivihivi tu,’ bila jasho.

Si hilo tu. Kazi yake ngumu pia ilikuwa imechukuliwa na mtu, yeye akiwa na uhuru wa kwenda zake, ama kuitumia fedha yake ya bure ama nyumbani kwake hadi kesho. Mgeni huyo wa ajabu aliyeinunua kazi yake kwa elfu hamsini tayari alikuwa amevaa viatu vyake vya mpira, joho lake refu la plastiki na kofia yake ya kapero na sasa yuko kazini akisafisha vyoo na masinki kwa utaratibu wa kawaida kabisa. Mtu yeyote ambaye angeingia maliwatoni humo, kama asingemsemesha angetoka huku akiwa na hakika kuwa mtumishi huyo hakuwa mwingine zaidi ya Papaa Mulumba.

Papaa Mulumba ni mtoto wa mjini. Ingawa alitoka kwao Mahenge miaka tisa tu iliyopita, mara baada ya kumaliza shule ya msingi, tayari mitaa ya Ilala, Magomeni na Kinondoni ilimpokea na kumkubali kama mmoja wa vijana wa mjini. Kila alipopata pesa zake alizipanga katika mafungu muhimu matatu; kuvaa, kula na kunywa.

Alikuwa hodari wa kuchagua mashati na suruali za mitumba kwa makini kiasi kwamba kila alipozivaa, alionekana kuvaa nguo mpya za kutoka ughaibuni. Unywaji wake pia aliufanya kwa uangalifu. Kwake ilikuwa mwiko kunywa katika baa za vichochoroni. Alipendelea baa kubwakubwa, zenye majina, huku akijichanganya na watu wakubwawakubwa, wenye pesa na vyeo; jambo lililompatia marafiki wa maana. Mmoja wa marafiki hao ndiye aliyempatia kazi Uwanja wa Ndege wa Dar es Salaam.

Papaa Mulumba wala halikuwa jina lake halisi. Alizaliwa





na kubatizwa kwa jina la Paskali, baba yake akiitwa mzee Kirumba. Vaa yake ya kufungia suruali tumboni, mwili uking’ara kwa pafyumu na vipodozi, huku akiwa hakosekani katika kumbi za muziki bandia za Maquis inapotumbuiza, ni miongoni mwa sababu zilizofanya jina la Paskali life na ‘Papaa’ kuzaliwa.

Sababu nyingine iliyompa jina hilo ni lugha. Kuupenda kwake u-Kongo kulimfanya abadili lafudhi ya Kiswahili chake kiasi kwamba watu wengi wasiomfahamu walimfikiria kuwa ni Mkongo, tena mwanamuziki. Lafudhi hiyo iliambatana na ‘lugha’ yake katika kuwatoa rafiki zake ‘kitu kidogo’ kila anapojikuta hana pesa mfukoni, jambo lililolifanya jina la Papaa lishamiri zaidi.

Papaa alikuwa mtumishi wa Mamlaka ya Viwanda vya Ndege. Aliajiriwa katika uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Dar es Salaam. Mwenyewe alipenda sana kuutambulisha kwa Kiingereza, “Niko Dar International Airport,” akiamini kuwa kuutaja kwa Kiswahili kuliupunguzia hadhi na, hivyo kumpunguzia yeye mwenyewe hadhi. Kila alipohojiwa yuko idara gani hapo uwanjani alijibu harakaharaka “Huduma ya Jamii,” akikwepa kuitaja kazi yake halisi ya utunzaji wa vyoo, kazi ambayo alikuwa ameipokea shingo upande, baada ya elimu yake kuonekana kuwa isingempatia nafasi nyingine. Lakini baadaye alikuja baini kuwa haikuwa kazi mbaya kama ilivyofikiriwa. Kwanza, sare zake za kazi, ikiwa pamoja na joho refu, kofia ya kapero na glovu zilifanya hata mtu anayemfahamu kwa karibu anapomkuta kazini ashindwe kumtambua. Pia, kazi hiyo ilikuwa na pesa kuliko alivyotegemea. Watu wengi wenye magendo yao, hasa dawa za kulevya, walikuja chooni kuficha bidhaa zao. Kila mara walimwachia ‘kitu kidogo’ kama bakshishi. Baadhi alidiriki kuwatolea au kuwaingizia bidhaa zao hizo na, hivyo, kumwachia ‘kitu’ ambacho hakikuwa ‘kidogo’ hali iliyomwezesha kumudu vikao vya high table na rafiki zake baadaye.

Jana tu aliondoka kazini hapo na elfu ishirini. Alitegemea angetumia elfu tano tu, lakini walipokwenda Diamond Jubilee ambako Kanda Bongo Man alikuwa akitumbuiza na bia mbili tatu baadaye ndipo akajikuta akiamka na mia mbili mfukoni.





Hivyo, ujio wa huyu ‘brother’ wa kutaka aachiwe kazi hiyo ngumu, kutwa nzima ya leo, na shilingi elfu hamsini juu, ilikuwa kama nyota ya jaha.

“Natumaini huna ajenda ya siri, ambayo itaniharibia kazi,” Papaa alionya.

Kicheko. “Sina ajenda yoyote. Kuna kitabu naandika. Sehemu mojawapo ya kitabu hicho inamhusu mtu aliyekuwa akifanya kazi kama hii. Hivyo, ili nitoe picha halisi ya kazi yenyewe lazima nifanye angalao kidogo, badala ya kuandika hisia tu. Ukitaka unaweza kukaa hapo kuniangalia. Ingawa mimi nakushauri uende zako popote unapotaka.”

“Nitatoka kidogo. Nitakuwa nikirudi kukutazama kila baada ya muda fulani. Saa za kazi zikiisha nitakuja kuchukua vifaa vyangu na kuvifungia.”

“Bila wasiwasi,” mgeni huyo wa ajabu alijibu.

Mgeni ambaye hakuwa mwingine zaidi ya Joram Kiango. Ndani ya mavazi ya kazi ya Papaa, Joram Kiango alikuwa amejikamilisha. Pamoja na silaha na vifaa alivyonunua pia alikuwa ameipitia kamera ndogo ya video wakati akija Uwanja wa Ndege. Alikuwa akimsubiri Papaa aondoke ili ategeshe vifaa hivyo, pamoja na kuiweka ile pete mahala muafaka. Alikuwa na hakika kuwa usingepita muda mrefu kabla ya ugeni mwingine, mzito zaidi, kuingia katika eneo hilo.

Alikuwa tayari, akisubiri.
 
41.


W 7 X

AKATI mikono ya Joram ikiwa shughulini kusafisha vyoo vya pale uwanjani, mikono ya Inspekta Haroub Kambambaya nayo ilikuwa kazini ikichambua mamia

ya taarifa ambazo ziliendelea kumiminika mezani pake, taarifa ambazo ziliambatana na namba za simu zilizowahi kupigwa kwenye simu ya Joram Kiango; nakala za simu za maandishi; majina ya baadhi ya watu wenye simu hizo; na kadhalika. Kambambaya aliichambua kila taarifa kwa makini kabisa, akitafuta neno lolote au jina lolote lile ambalo lingefanikisha kupata ama fununu ya kila kinachoendelea, ama kauli ambayo ingemwezesha kubaini alipo Joram.

Haikuwa kazi rahisi. Joram hakuwa mtumiaji mzuri wa simu. Na hizo chache alizowahi kupiga hazikuwa na lolote lile ambalo ambalo lingefanikisha kupata ama fununu ya kila kinachoendelea, ama kauli ambayo ingemwezesha kubaini alipo Joram.

“Atapiga tu. Naamini hataitumia tena simu yake wala simu yoyote ya mkononi. Lakini endeleni kufuatilia simu zote za watu aliopata kuwasiliana nao. Simu ya Meja Mfumue itazamwe kwa makini zaidi. Naamini atahitaji kuwasiliana naye kwa namna moja au nyingine,” Kambambaya aliwaagiza wasaidizi wake.

Wasaidizi wake walishangazwa sana na mabadiliko ya





ghafla katika wajihi wa bosi wao. Katika muda wa saa arobaini tu zilizopita mzee alikuwa amekonda, uso umesinyaa na mvi kuongezeka kichwani mwake maradufu. Alionekana kama mtu ambaye kipindi hicho hakupata kula wala kulala vizuri. Kwa ujumla, alionekana kama mtu aliyeko katika mateso makubwa, kimwili na kiakili, kiasi cha kulisahau tumbo lake na kuipuuza afya yake.

Haikuwa uongo. Ubongo wa Kambambaya ulikuwa katika changamoto nzito kuliko zote zilizowahi kumkuta kazini. Vifo vya watu, askari kwa raia wasio na hatia vilimchanganya sana. Matarajio ya maafa mengine, wakati wowote, mahala popote, huku wanausalama wakiwa hawana uwezo wa kuyathibiti, yalimchanganya zaidi, nusura kumtia kichaa.

Kutoweka kwa Joram Kiango, kutoweka kwa mwili wa msichana anayeshukiwa kuwa aliuawa na Joram toka chumba cha maiti, mlolongo wa mauaji ambayo, kwa namna zote, yanahusiana na matukio haya yaliendelea kuwa kiini cha akili yake kuhangaika kupita kiasi.

Idara yake na jeshi zima la polisi walikwishafanya kila ambacho walistahili kukifanya, kwa nia ya kuimaliza kadhia hii mapema; bila mafanikio. Kila polisi alipewa picha ya Joram Kiango na kuamriwa kutoa taarifa mara atakapoonekana. Zaidi ya watu mia tayari walinaswa kwa kufananishwa naye. Vituo vyote vya mabasi, viwanja vyote vya ndege, stesheni za treni na, hasa, vichochoro vya miguu vinavyotoka nje ya Dar es Salaam viliwekewa ulinzi mkali kwa dhamira hiyo. Bado si Joram wala mtu yeyote anayeelekea kuhusika na maafa haya aliyekamatwa.

Hali kadhalika, maiti aliyetoweka Muhimbili naye alitafutwa kwa namna zote bila mafanikio. Vibali vyote vya mazishi vilipigwa marufuku kwa muda, kila mwili unaosafirishwa ukikaguliwa na kupekuliwa kwa makini kabla ya kuruhusiwa kuondoka. Ule mwili mzuri, wa aliyekuwa Mona Lisa, haukupatikana. Ilikuwa kama ametoweka kama zile hadithi za Alfu Lela u Lela.

Pengine nuru pekee ambayo Kambambaya alianza kuiona katika mkasa huu ni ile ya kufahamika kwa jina la marehemu huyo aliyetoweka. Moja ya taarifa za karibuni ilikuwa ile





ya kuitambua picha ya marehemu Mona Lisa kama mmoja wa wapangaji wao ambaye alikuwa hajaonekana hotelini hapo kwa siku mbili bila taarifa yoyote. Vitabu vya wageni vilimtambulisha kama mkazi wa Arusha aliyetokea Zanzibar na kuja Dar es Salaam ambapo tayari alikaa kwa wiki moja. Nafasi ya kabila ilimtaja kama Mmanyema.

Siku zote, mwanausalama anapopata jina huwa ni hatua moja mbele. Lakini haikuwa hivyo katika hili. Hali hiyo ilitokana na pale picha hiyohiyo ilipopelekwa kwa yule mtumishi wa hoteli ya New Africa aliyelazwa MOI alipomtambua kama mgeni aliyefika hotelini hapo alfajiri na kuomba kuonana na mgeni mwingine aliyejiandikisha kama Kondo Mtokambali, mgeni ambaye mara tu alipoanza kukiendea chumba cha Mtokambali mlipuko mkubwa wa bomu ulitokea ukifuatiwa na yale mauaji ya kutisha.

Madai hayo yaliongeza utata katika fikra za Kambambaya na wapelelezi wenzake. Haikumyukinika mtu aliyeuawa, tena kwa risasi, maiti yake ikapotea kimiujiza toka chumba cha maiti, adaiwe kuwa alionekana alfajiri akidai kuonana na mtu anayetuhumiwa kwa mauaji yake. Kambambaya aliamua kumchukulia majeruhi yule wa New Africa kama mtu ambaye ama kwa ajili ya hofu ama kutokana na akili yake kuathiriwa na mlipuko wa bomu, hakuwa na hakika na madai yake.

Uchunguzi mkali uliofanyika katika chumba cha marehemu pia haukumsaidia sana. Zaidi ya nguo zake chache, vitabu vya riwaya na vipodozi hakikupatikana kitu chochote ambacho kingewezesha kufahamika haraka kwa habari za marehemu huyo.

Hivyo, wakati polisi wa Arusha wakipewa jukumu la kutafuta habari za marehemu mwenye jina hilo, Kambambaya aliendelea kuyatia matumaini yake yote katika haja ya kupatikana kwa Joram Kiango, haraka iwezekananvyo. Aliamini kuwa hiyo ingekuwa njia ya mkato zaidi ya kufikia ufumbuzi wa kadhia hii.



***

Mageuzi ya uchumi, kwa lugha nyingine mfumo wa ubepari, ambao ulipokelewa na kuhalalishwa nchini Tanzania kwa jina
 
42.

la kutatanisha, utandawazi, yaliambatana na kuchangamka vilivyo kwa Uwanja wa Ndege wa Dar es Salaam. Idadi ya ndege za kuingia na kuondoka, iliongezeka kila siku, jambo ambalo lilipelekea kuwapo kwa pilikapilika nyingi za watu, magari na mizigo uwanjani hapo. Hazikupita dakika mbili bila ya ama gari lingine kufika, ama kuondoka; likiwa na abiria. Aidha, kama ilivyokuwa katika vyumba vya kusubiria safari, eneo la nje pia lilikuwa na watu wengi, baadhi yao wakisindikiza, baadhi wakiwapokea wageni wao, baadhi wakiendesha biashara zao mbalimbali.

Ni katika hali hiyo teksi moja ilipomshusha abiria mmoja mkimya, aliyekuwa na kijimfuko kidogo tu mkononi. Abiria huyo alilikodi gari hilo toka mtaa wa Uhuru, Kariakoo. Kwa kiasi fulani, alionekana abiria wa ajabuajabu kwa dereva wa teksi iliyomleta. Alikuwa mkimya sana, kinyume kabisa na abiria wengi wa jijini Dar es Salaam. Mara baada ya kutamka maneno “Airport… mwendo wa haraka, tafadhali.” Hakutia neno jingine. Jitihada za dereva huyo kumshirikisha maongezi hazikuzaa matunda.

Dereva wa teksi hiyo aliamua kumchukulia abiria wake kuwa ni wa ajabu tangu pale abiria huyo alipolifuata gari lake na kuomba kupelekwa Uwanja wa Ndege. Alikuwa ameshuka toka katika teksi nyingine yenye namba za Ilala, jambo ambalo lilimfanya dereva huyo ahisi kuwa ama ni mkorofi katika malipo au hajui anakokwenda. Hivyo, hakuwa na hakika ya malipo yake alimtajia bei ya juu zaidi. Abiria huyo alikubali kwa kichwa huku akifungua pochi yake na kutoa pochi nyingine ndogo iliyokuwa ndani yake, akaifungua hiyo pia na kutoa pesa alizomlipa dereva.

Jambo jingine lililomshangaza dereva huyu kwa abiria wake ni mavazi. Pamoja na abiria huyo kufunika sehemu kubwa ya sura yake kwa miwani mipana ya jua, huku nusu ya kichwa chake ikiwa imemezwa na kofia pana ya jua vilevile, bado dereva alipata hisia kuwa mavazi hayo yalimficha kiumbe mmoja mzuri sana. Kilichomshangaza ni pale alipogundua kuwa kiumbe huyo alikuwa amevaa suruali ya jeans ambayo ilionyesha kuchakaa kidogo na jaketi lililofanana na suruali hiyo, ambalo nalo lilikuwa na dalili ya ama kuchafuka au





kutumiwa kwa muda mrefu zaidi.

“Unasafiri au unatarajia mgeni?” dereva alijaribu tena

maongezi. “Mgeni.”

“Anatokea wapi?” Kimya.

“Wewe mwenyewe unaishi hapa jijini au nje?” Kimya.

Dereva akaamua kuufyata mkia hadi alipowasili uwanjani na kumfungulia mlango. Alishuka taratibu, akauendea ukuta wenye ratiba za safari na kuusoma kwa dakika mbili tatu. Baadaye, alichanganyika na watu wengine ambao ama walikuwa wakisubiri wageni ama wakisubiri safari.



***

Joram Kiango alimwona mgeni huyo kitambo. Alimwona pale alipoketi na wageni wengine, akiwa na gazeti la Daily News mkononi. Ni gazeti hilo ambalo lilimsaidia Joram Kiango kumshuku haraka. Alikuwa halisomi kwa makini, kwa ujumla, alikuwa alisomi kabisa bali alilitumia kama ngao ya kuuficha uso wake, wakati macho yake yakitazama huku na huko kwa makini sana.

Kabla ya kulinunua gazeti hilo mwanamama huyo alikwenda maliwatoni mara mbili na kutoka akiwa na dalili za mshangao mkubwa machoni mwake. Msala aliouingia mara zote hizo ni ule ambao Joram aliutumia kuificha ile pete, nyuma ya sinki la maji. Mgeni wake alikwenda moja kwa moja na alikaa huko kwa dakika mbili nzima. Kisha alitoka na kutazama huku na huko kwa takribani dakika tano nzima kabla hajakwenda tena. Alipotoka ndipo aliponunua gazeti na kuketi kwa utulivu, lakini macho yake yakiwa kazini.

Joram hakuwa na shaka kuwa huyu alikuwa ndiye mgeni wake. Ingawa alikuwa hajapata wasaa wa kumkaribia, lakini umbile lake na mwendo wake vilitosha kumfanya apoteze mpangilio mzima wa ratiba yake ya awali. Hii ilitokana na ukweli kuwa umbile lile na mwendo ule haukuwa wa binadamu mwingine yeyote yule zaidi ya Mona Lisa! Mona Lisa ambaye ni marehemu! Mona Lisa ambaye pamoja na kuwa marehemu amekuwa akimfuatafuata kila anakokwenda!

Joram angeweza kumwendea msichana huyo, palepale alipokuwa, na kumuuliza yakoje mambo haya. Angeweza kumlazimisha ili aupate ukweli wa kitendawili hiki kinachomsumbua. Hata hivyo, alisita kufanya hivyo mara moja kwa sababu nyingi; kubwa ikiwa kwamba sehemu hiyo haikuwa mwafaka kwa majadiliano mazito kama hayo.

Pia, haukuwa wakati mwafaka kwani Mona Lisa hakuwa mgeni pekee wa kutatanisha uwanjani hapo. Muda mfupi kabla Mona Lisa hajafika macho mazoefu ya Joram yaliwaona wageni wengine wa kutiliwa mashaka. Walikuwa wanaume wawili. Waliketi mahala wakinywa soda na kusoma magazeti. Walikuwa kazini, macho yao yakikitazama kila kitu na kila mtu kwa makini. Mara kwa mara mikono yao iliingizwa katika mifuko yao ya koti, ambayo kwa uzoefu wa Joram Kiango, ilihifadhi silaha.

Joram aliwatazama watu hawa kwa muda mrefu. Aliwashuku zaidi pale mwanamke huyo mwenye umbile la Mona Lisa alipofika, ambapo mmoja wao alitoa simu yake ya mkononi na kuzungumza kwa muda mfupi. Baada ya hapo wote walionekana makini zaidi.

Si hao tu. Polisi na wanausalama uwanjani hapo walikuwa wengi kuliko kawaida. Joram angeweza kumnusa polisi yeyote hata akiwa mita mia moja toka alipo, awe na magwada asiwe nayo. Kwa hesabu za harakaharaka Joram aliona kama idadi ya askari wasio na magwanda, wanaopita huko na huko wakiwa maradufu. Wote walionekana kama waliokuwa na majukumu yasiyo ya kawaida, majukumu ya ziada, ambayo yalifanya wasiwe na ile hali ya utulivu na kujiamini kama ilivyo kawaida yao.

Subira Joram, Subira! Ni subira pekee itakayokuwezesha

kufikia mradi wako, Joram alijinong’oneza kimoyomoyo.

Aliitazama saa yake. Ilikuwa inakaribia saa moja na robo za usiku, robo saa zaidi ya muda ambao Papaa Mulumba aliahidi kuja kukusanya vifaa vyake, jambo ambalo lilimtia hofu Joram Kiango, kuwa ujio wake huo ungeweza kutibua mpangilio aliokuwa nao na, hivyo, kutibua mwelekeo wa mambo. Kwa bahati, Papaa alichelewa.





Joram akaendelea kusubiri, mikono yake ikiendelea kusugua vyoo na sakafu za choo baada ya choo, macho yake yakiendelea kufuatilia kila tukio katika maeneo yote yaliyofikiwa na upeo wa macho hayo. Na kila alipopata mwanya aliitumia mikono yake ndani ya mavazi yake kuhakikisha kuwa silaha na vifaa vyake vyote viko salama na angeweza kuvifikia muda wowote wakati utakapojiri.

Mambo yalitokea ghafla na haraka kuliko Joram alivyotegemea. Alikuwa ameinama kuokota kishungi cha sigara iliyotupwa na msafiri mmoja aliyeonekana mlevi. Wakati akiinuka alimwona mmoja wa wale wanaume wawili akimlenga bastola yule mwanamama mwenye sura na umbile la Mona Lisa. Kulikuwa na sekunde chache tu kati ya uhai na kifo cha mwanamama huyo, ambaye alikuwa amegeuka upande mwingine. Joram hakufikiria mara mbili. Aliichomoa bastola yake na kumlenga mtu huyo kwenye bega la mkono wake wa kulia. Akavuta kifyatulia.

Mlipuko wa bastola hiyo, kilio cha ghafla cha mtu aliyejeruhiwa na kuanguka kwa bastola aliyokuwa ameishikilia mkononi, vilizua purukushani ya ghafla chumbani humo. Umati wa watu ulilipuka na kuanza kukimbia huku na huko, wengi wakiwa hawajui kitu gani kimetokea.

Mtu wa pili alipoona mwenzake kaanguka, damu nyingi zikimvuja toka begani naye aliitoa bastola yake na kumlenga mwanamama yule. Alikuwa amechelewa. Risasi mbili zilimwingia mwilini, moja ikiwa imetoka katika bastola ya Joram, ya pili ikiwa imetoka katika bastola ya mwanamama huyo na ilimwingia barabara kifuani. Alikata roho hata kabla hajaifikia sakafu ambayo aliiangukia kifudifudi.

Matuko hayo ambayo yalitokea ndani ya sekunde ishirini tu yalizidi kuwasha moto wa hofu na purukushani uwanjani hapo. Wako walioendelea kukimbia huko na huko, wako waliojilaza chini ya viti na wako pia walioduwaa wima wakiwa hawajui lipi la kufanya.

Ni wanausalama waliokuwa katika eneo hilo ambao walimtia hofu Joram. Wote walichupa chini na kuzielekeza bunduki zao kwa mwanamama huyo huku mmoja wao akitoa amri ya kumtaka adondoshe silaha yake chini. Mmoja kati





ya wanausalama hao alikuwa amemwona Joram na kumpiga risasi bila ya kulenga vizuri. Risasi hiyo ilimchubua paja la mguu wake wa kushoto. Risasi ya pili Joram aliikwepa kwa kujirusha chini na kujikinga kwa pipa la taka. Wakati huohuo mkono wake ulikuwa ukiishughulikia ile chupa yake yenye moshi wa pilipili aliyoinunua duka la silaha. Aliifungua na kuirusha katikati ya chumba hicho. Ilipotua ilipasuka kwa mlio mkubwa wa kitu kama bomu, lililofuatiwa na ukungu mkubwa wa moshi unaowasha kupita kiasi. Kila mtu alifumba macho yake akilia kwa maumivu makali.

Kila mtu, isipokuwa Joram Kiango ambaye, alikuwa amejiandaa. Yeye aliutumia mwanya huo kuchupa hadi alipokuwa yule mwanamama na kumshika mkono huku akimwelekeza mlangoni. “Twe’nzetu,” alimhimiza. “Joram Kiango?” mwanamama huyo aliuliza.

“Ndiye, twende!” Joram alimwamuru akimvuta kutoka nje. Akiwa ameshikwa kwa mkono wenye nguvu kama koleo, akiwa haoni, huku machozi yakimtoka kwa maumivu ya macho, mwanamama huyo alikubali kuongozwa kikondoo

toka ndani ya chumba hicho.

Hakuna asiyejua hofu ya bomu. Toka ugaidi ulipopamba moto duniani, toka Marekani na ubabe wake uliposhindwa kufanya lolote wakati yale majengo yake marefu zaidi kati ya machache ya aina hiyo duniani yakilipuliwa kwa ndege za abiria zilizogeuzwa mabomu; toka nchi ya Irak ilipogeuka uwanja wa majaribio ya kila aina ya bomu; hofu ya bomu iliingia katika moyo wa kila binadamu anayeishi katika karne hii.

Kwa Watanzia hofu ya mabomu iliongezeka maradufu Agosti 7, mwaka 1998, pale wakazi wa Dar es Salaam waliposhuhudia bomu moja tu likiulipua Ubalozi wa Marekani pale Oysterbay, Barabara ya Bagamoyo, bomu ambalo lililipuka sambamba na lile la Nairobi, ambalo nalo liliulipua Ubalozi wa Marekani nchini humo na kuteketeza mamia ya watu wasio na hatia, hofu ambayo ilizidishwa nguvu na vyombo vya habari, vikiongezwa nguvu na vile vya Marekani yenyewe, ili iweze kuhalalisha malengo yake ya kisiasa na kiuchumi duniani.

Ni hofu hii ambayo ilimkumba kila mtu aliyekuwa uwanjani
 
43.


hapo jioni hii. Joram na mateka wake walipotoka nje ya jengo walikuta hali iliyokuwa nje haikuwa tofauti na ya ndani. Watu walikuwa wakilia ovyo, kila mmoja akikimbilia huku na kule bila mpangilio; wote wakiamini kuwa wakati wowote uwanja huo ungelipuka kwa bomu kubwa zaidi.

Hali hiyo ilikuwa mwafaka kabisa kwa Joram Kiango, ambaye alimvuta mwanamama huyo hadi katika eneo la kuegesha magari. Madereva wengi walikuwa wameyasahau magari yao na kukimbia bila hata kufunga milango. Dereva mmoja yeye hata ufunguo wa kuwashia gari aliuacha ukining’inia sehemu yake. Joram alimsukumiza mateka wake katika gari hilo, kisha akaingia upande wa dereva na kuliwasha moto kuelekea mjini.

Gari hili lilikuwa aina ya Mark II Grand. Mwendo wake ulikuwa wa uhakika na petrol ilikuwa nusu tenki. Ingeweza kumfikisha Joram na abiria wake popote alipotaka. Hivyo, aliliendesha kwa mwendo wa kasi, akipita gari baada ya gari, huku akiangalia kwa makini kwenye kioo cha ndani kama hafuatwi. Nyuma yake barabara ilionekana nyeupe. Ukiacha magari mengi ya kupishana nayo Joram hakuona gari lolote nyuma yake, ambalo lingeweza kumtia mashaka.

Pamoja na kutazama magari, Joram Kiango alikuwa makini vilevile kumtazama abiria wake. Toka alipomwona akichupa angani na kutua sakafuni bila kishindo chochote kama paka shume kuufuatia ule mlipuko wa bastola, na alivyomwona akiitoa bastola yake kwa wepesi wa ajabu na kummiminia risasi yule mtu aliyetaka kumwua pale uwanjani, Joram alijua huyu si mwanamke wa kawaida. Macho yake hayakuonyesha dalili yoyote ya hofu wala mshituko hata pale mlipuko wa lile bomu la bandia ulipotokea. Ni pale tu chumba kilipojaa moshi wenye pilipili ndipo, kama watu wengine, alishindwa kujizuia na kupata upofu wa muda, huku machozi yakimtiririka, machozi ambayo yalianza kunyauka, lakini mwenyewe akaendelea kuyafumba macho yake na kutulia pale kwenye kiti katika hali ya ukimya na upole; tofauti kabisa na yule chui jike aliyecharuka dakika mbili tatu zilizopita pale uwanjani, chui ambaye hadi sasa aliishikilia bastola yake, japo kwa kuificha katika mfuko wake wa mkononi. Joram hakuwa na





shaka kuwa wakati wowote mwanamama huyo angeweza kucharuka tena na kuanzisha purukushani. Wakati wowote angeweza kuua, na safari hii marehemu mtarajiwa asingekuwa mwingine zaidi ya Joram Kiango, wazo ambalo lilimfanya aongeze umakini wa kumchunguza.

Kitu kimoja kilimsumbua Joram katika sura na umbile lake. Toka alipoanza kumchunguza pale uwanjani mpaka sasa akiwa naye ubavu kwa ubavu, mwanamama huyu hakuwa mwingine zaidi ya Mona Lisa. Urefu wake wa kadiri, umbile lililokatika kati kike kabisa, ngozi laini ya maji kunde; Mona Lisa mtupu! Lakini kile alichokiona pale uwanjani, alivyomwona anavyocharuka kama kifaru aliyejeruhiwa mara alipohisi kutishiwa uhai wake, alivyolenga shabaha na kumuua yule mtu kwa wepesi na utulivu wa ajabu, Joram aliapa kimoyomoyo; Hapana huyu si Mona Lisa. Kwanza Mona Lisa alikuwa amekufa pale kitandani, mbele ya macho yake. Kisha, Mona Lisa yule hakuwa mtu wa kuweza kumuua hata mende huku akiwa ametulia kama tembo aliyekanyaga sisimizi.

Mwanamke huyu ni nani? Ni swali ambalo alikusudia mwanamke mwenyewe alijibu mara wakati utakapojiri, ampe jibu hilo na pengine majibu ya mlolongo mzima wa kitendawili hicho. Alikuwa na kila hakika kuwa mwanamke huyo alikuwa ama kufuli ama funguo wa mengi yaliyofichika katika kadhia hii. Ni hilo lililomshawishi akubali kuhatarisha maisha yake kwa kumteka nyara, na kumwingiza katika gari hili, ili aweze kupata mahala ambapo angehakikisha anapata majibu yote, kwa bei yoyote.

Walipofika katika makutano ya Barabara za Nyerere na Mandela taa za barabarani ziliwazuia. Ilibidi wasubiri. Ni mwanga toka gari la nyuma yao uliomfanya Joram ashituke kwa jinsi alivyolowa damu. Lile jereha la risasi, ambalo awali aliliona dogo, lilikuwa linavuja damu nyingi kiasi cha kumfanya ajikute amekalia kiti kilichojaa damu, huku yale mavazi ya Papaa Mulumba ambayo alikuwa hajayavua yalowe chapachapa.

Hilo lilimsumbua Joram kiasi. Hakuona kama alikuwa na

nafasi ya kutosha ya kujisafisha. Kadhalika, gari alilokuwa





akiliendesha lilikuwa la kupora. Alitarajia kulibadili mara baada ya kuingia mjini, hatua ambayo pia ililenga kumpoteza mtu yeyote ambaye anaweza kuwa anawafuata au trafiki ambao punde watapewa taarifa ya wizi wa gari na namba zake. Akiwa ametota kwa damu, akiwa na abiria asiyetabirika wala kuaminika, hata kwa sekunde; Joram hakuona kama ulikuwepo uwezekano wa kushuka ndani ya gari hilo na kukodi jingine. Akaamua kuendelea nalo.

Kitu kingine ambacho kilimsumbua Joram ni utulivu wa mwanamama huyo. Alivyotulia pale juu ya kiti, macho kayafumba kana kwamba yuko usingizini, kana kwamba ni mwanamke wa kawaida anayesafiri na mumewe; ni jambo lililomtisha Joram. Liliashiria ukongwe na uzoefu wake. Kwa jinsi alivyoifahamu ile sumu ya pilipili, baada ya dakika tano huwa imekatika machoni, kwa mwanamke ngangari kama huyu, dakika mbili au tatu zilimtosha awe amefumbua macho na kuanza kutazama uwezekano wa kuendelea na ratiba yake.

Kwa Joram utulivu wake uliashiria jambo moja tu, uzoefu, hakuna jambo jingine. Joram aliamini kuwa ndani ya ukimya na utulivu huo mwanamama huyo alikuwa kazini akiandaa mikakati mipya, mikakati ambayo kwa vyovyote haikumkusudia tena lolote.

Joram hakuona kama alikuwa na la kufanya katika hatua hiyo. Akaendelea kusubiri. Subira yavuta heri! Alijikumbusha. Taa ziliporuhusu aliliondoa gari kwa kuiacha Barabara ya Nyerere na kuifuata ile ya Mandela. Ilimchukua hadi inapokutana na ile ya Morogoro. Taa zilikuwa zikiwaka kijani. Hivyo, alivuka na kuifuata ile ya Chuo Kikuu, Mlimani. Aliifuata hadi mwenge, ambako aliicha na kuingia ile ya Ali

Hassan Mwinyi.

Alijua anakoelekea.



***

Ndiyo, purukushani za pale Uwanja wa Ndege zilimshitua takribani kila mtu. Mameneja waliziacha ofisi zao na kukimbilia vyooni, maafisa wa kawaida wakikurupuka kukimbilia huku na kule huku watu wengine, abiria kwa





wasio abiria, wakihaha ovyoovyo. Mamia waliumia vibaya kwa kugongana au kuanguka. Watu watatu walipoteza maisha kwa kukanyagwakanyagwa na watoto kadhaa walipotezana na wazazi wao.

Hata hivyo, hali hii ilimsisimua sana mtu mmoja. Huyu alifuatilia kila tukio na kila kitendo kwa makini, tabasamu jembamba likiwa limechanua usoni mwake. Mtu huyu alikuwa na majina mengi. Zamani kidogo aliwahi kumtania mmoja wa waajiri wake aliyekuwa amemtumia zaidi ya mara mbili kwa kumwambia, “Utapendelea kuniita nani?” pale mwajiri huyo alipomuuliza ana majina mangapi baada ya kumtajia majina mapya kila walipoonana.

Safari hii bwana huyu alijiita Othman Mchopanga, jina ambalo lilikuwa kwenye kitambulisho chake bandia kinachomtabulisha kama mkurugenzi wa fedha katika kampuni moja inayojihusisha na uagizaji wa vipuri vya magari na mitambo mbalimbali.

Mchopanga alifika uwanjani hapo muda mfupi kabla ya kuanza kwa purukushani. Alisimama nje ya uwanja, sigara mdomoni, mikono mfukoni, macho yake yakiwa kazini yakimtazama kila mtu anayeingia na anayetoka. Alimwona yule mwanamke aliyeshuka harakaharaka kwenye gari na kuingia ndani ya chumba cha kusubiria.

Pia, aliwaona wale watu wawili waliokuwa wakimfuatilia mama huyo, sura zao zikionyesha wazi kuwa walihitaji roho yake. Aidha, alimwona pia yule mtunzaji wa vyoo na kubaini mara moja kuwa hakuwa mfagizi wa kawaida.

Baada ya kumtazama sana Mchopanga alibaini kuwa mfagizi huyo alikuwa nani, jambo lililofanya tabasamu lake lizidi kuchanua.

Lakini kitu kilichomvutia zaidi ni yule msichana mwenye miwani na kofia pana ya jua. Alimjua fika msichana yule. Alimjua toka sauti, ukucha hadi unywele wake wa mwisho. Alikuwa amemfuatilia kwa wiki nzima, usiku na mchana, kabla hajapewa ile amri ya mwisho, ya kumuua. Na alimuua kwa mkono wake mwenyewe, pale kitandani na kumwacha bwana wake akikoroma kama nguruwe lililochoka, kazi ambayo aliifanikisha kwa urahisi baada ya kupenyeza mvuke





wa dawa za kulevya chumbani humo na, hivyo, kuwafanya walale fofofo, nusu maiti, kwa muda mrefu.

Mchopanga hakuwa mtu wa kuua wanawake. Wala hakuwa mtu wa kuua binadamu waliolala usingizi. Kwa kawaida, alipenda kumuua mtu huku marehemu mtarajiwa akikiona kifo kinavyomchukua. Alipenda kuyaona macho ya anayeuliwa yakitoka pima; kumtazama muuaji wake pindi risasi inapopenya kifua na kuuchoma moyo.

Hivyo, ingawa kazi ya kumuua mwanamke yule, ilikuwa nyepesi kuliko kazi zote alizowahi kufanya, ikiwa na malipo murua kuliko yote aliyowahi kupokea, bado aliona nzito sana; si kwa ajili ya kumuua mwanamke tu, tena akiwa usingizini. La hasha! Ugumu wake ulitokana na mwanamke anayeuawa. Alikuwa msichana mzuri, mzuri, mzuri. Mchopanga hakupata kukutana na mwanamke aliyekamilika kama huyu, sura ya kusisimua, umbile la kupendeza na mwendo wa kuvutia. Zile siku saba za kumfuatilia, kwake ilikuwa adhabu kubwa. Alitamani kuzungumza naye, aisikie sauti yake. Kusikia tu! Alitamani agusane naye ili aionje ladha ya ngozi yake. Kuionja tu! Uwezo alikuwa nao. Moja ya kumi ya pesa alizolipwa kwa kazi ndogo ya kumwondoa duniani zingetosha kumfanya msichana huyo apate wazimu.

Hata hivyo, Mchopanga alijitahidi kumshinda nguvu shetani wake. Maadili ya kazi yake hayakumruhusu kufanya mzaha wa aina yoyote. Vilevile, hakuona kama mwajiri wake alikuwa mtu wa kuvumilia upuuzi wa aina yoyote. Lakini, kubwa zaidi ni msichana mwenyewe. Muda wote wa kumfuatilia alimwona kama mtu asiye wa kawaida. Wakati wote alikuwa makini, macho yake yakiwa na kila dalili ya hadhari kama anayejua kuwa anafuatiliwa, hali iliyomfanya ajione kama kitendo chake cha kumfuatilia kilikuwa sawa na kucheza na chui jike aliyejeruhiwa. Hakujua kwa nini alilipata wazo hilo. Badala yake aliendelea kumfuatilia na kutoa taarifa ya nyendo zake zote kwa mwajiri wake hadi pale alipopewa amri ya kumuua usiku ule.

Amri hiyo aliitekeleza kikamilifu, lakini, saa ishirini na nne baadaye akaarifiwa kuwa alikosea na kumuua mtu asiyehusika. Na kwamba mtu aliyemwacha hai, pale kitandani,
 
44.

alikuwa Joram Kiango, mtu ambaye alitakiwa kufa mara elfu moja na zaidi badala ya yule msichana.

Taarifa hiyo ilimchanganya Othman kuliko jambo lolote jingine. Katika maisha yake ya ajira hakuwahi kukosea wala kuua kwa bahati mbaya. Alikuwa makini na alilifuatilia windo lake kwa makini kabla ya kuitekeleza kazi yake. Alikuwa na hakika asilimia mia moja kuwa aliyemuua ndiye aliyekusudiwa, uhakika ambao ulianza kuingia mashaka pale alipomwona mtu yuleyule, akiwa katika mwendo na tabia ileile, japo katika mavazi tofauti pale uwanjani. Mashaka yake yaliongezeka zaidi pale alipomwona mwanamama huyo, akibadilika ghafla na kuwa kama paka shume aliyetishiwa maisha yake. Othman Mchopanga alimhusudu alipomwona akichupa angani na kutua chini kwa utulivu kama unyoya. Alimhusudu zaidi kwa wepesi wake na shabaha sahihi wakati alipoitoa bastola yake huku angali angani na kumuua mmoja wa maadui zake bila kuonyesha jitihada yoyote katika kulenga shabaha.

Othman Mchopanga alisisimkwa na damu zaidi alipomwona yule mfagizi akipata uhai ghafla na kuyaweka mambo chini ya himaya yake. Alimwona alivyo mwepesi wa mwili na akili. Aliona vidole vyake vilivyokuwa ‘sharp’ katika kuchezea bastola na hila aliyoitumia katika kulilipua lile bomu lisilo na madhara, lililokusudiwa kuongeza mparanganyiko wa mambo uwanjani hapo ili apate mwanya wa kutoroka. Alimwona alivyomnyakua yule msichana kama kuku na kinda lake na kumwongoza nje. Alimwona pia alivyopokonya gari na kulitia moto. Hata alifanikiwa kunukuu namba ya gari lile. Othman Mchopanga hakuhitaji ushahidi zaidi ya kuhakikishiwa kuwa mtu huyo hakuwa mwingine zaidi ya Joram Kiango.

Awali, jukumu lililomleta Mchopanga uwanjani hapa lilikuwa dogo tu, kuhakikisha yule msichana ameuawa na kisha awaue wale wauaji wake ili kufuta uwezekano wowote wa kuvuja kwa kiini cha mauaji hayo. Na kama wauaji hao wangeshindwa tena kumuua msichana yule mdogo yeye aliagizwa kutekeleza mara moja.

Angeweza kuitekeleza kazi hiyo kwa urahisi kabisa. Ule moshi wa pilipili uliowapa watu upofu wa muda yeye haukumfikia. Hali kadhalika, milipuko ya lile bomu la kuparanganyisha





watu yeye haikufanikiwa kumtisha kwani alikwishaizoea. Hata hivyo, alisita kufanya hivyo kwa sababu mbili za msingi. Moja, ni mabadiliko ya mambo yaliyotokea. Kuwepo kwa Joram Kiango katika eneo hilo la kujiingiza kwake kikamilifu katikati ya dimba la mambo hayo kulimfanya asite kufyatua bastola yake ambayo ilikuwa imemlenga vizuri sana kisogoni, wakati akimvuta yule msichana kuelekea kwenye gari.

Lakini sababu nyingine, ambayo Othman Mchopanga aliiona ya msingi zaidi ilitokana na malipo. Fedha alizolipwa, japo zilikuwa nyingi, bado hazikumhusisha Joram Kiango. Uzito wa jina lake na ukali wa kiu ya damu yake kwa mwajiri wake vilifanya aamini kuwa pato lake lingepanda maradufu kama angezungumza kabla sio baada ya kuitekeleza kazi hiyo. Hivyo, wakati Joram Kiango na msichana wake wakiondoka uwanjani hapo yeye pia aliliendea gari lake, aina ya pajero, na kulitia moto. Aliwafuata kwa mwendo wa wastani akiruhusu magari matatu au manne kuwatenganisha. Wakati huohuo simu yake ya mkononi ilikuwa hai ikitoa taarifa ya mwenendo

wa mambo uwanjani hapo.

“Joram tena!” Sauti upande wa pili ilifoka. “Na bado hukumwua!”

“Ningeweza kumwua. Hata sasa bado naweza kumwua vizuri tu, yeye na yule msichana wake anayeonekana anataka kufa mara mbili. Lakini unajua hatujazungumza mzee?”

“Kuzungumza nini tena?” “Dau.”

“Dau?”

“La kichwa cha Joram Kiango.”

“Akh! Hilo tu! Ungemuua, halafu tukazungumza.”

“Unajua huwa sifanyi kazi kwa mkopo mzee? Joram anaweza kufa wakati wowote, usiku huuhuu. Lakini si kabla ya kupokea dau langu.”

Sauti upande wa pili ilionyesha hasira kidogo iliposema, “Huu ni usiku sana. Kesho saa mbili utalipata dau lako. Lakini Joram na huyo malaya wake lazima wafe usiku wa leo. Jua likichomoza kesho, wangali hai, kazi itakuwa imekushinda.”

Mchopanga aliitafakari kauli hiyo kwa muda. Aliujua ugumu wa kumwachia Joram Kiango usiku huo ili apate malipo yake





kwanza, halafu aanze kumtafuta baadaye. Ingekuwa sawa na kurudia kosa. Yule msichana vilevile, roho yake ilitakiwa kwa udi na uvumba. Mamilioni ya fedha yalikuwa tayari yametapanywa kwa watu mbalimbali kwa dhamira hiyo bila mafanikio. Kumpoteza ingekuwa kosa jingine.

“Haya, nimekubali,” alisema baadaye. “Umekubali?”

“Kuwaua usiku huu, kesho nione pesa zangu zikiwa tayari katika akaunti yangu. Kama utashindwa kufanya hivyo, elewa kuwa kichwa chako kitakuwa asusa yangu kesho hiyohiyo.”

Mchopanga alisikia kitu kama kicheko cha kebehi toka upande wa pili, kicheko kilichofuatiwa na neno “Vizuri,” na kIsha, “Bila wasiwasi wowote.”

Maneno hayo yalimfariji. Akautia mkono wake mfukoni na kuipapasa bastola yake Smith & Wesson 459, iliyokuwa imejaa risasi. Mfuko wa pili ulikuwa na visu viwili vya aina mbalimbali; kamba ya nailoni maalumu kwa kunyongea, kijaluba chenye unga wa cocaine na vikorokoro vingine. Chini ya kiti cha gari hilo alihifadhi bunduki kubwa, AK-47, lensi yake na kasha la risasi. Pembeni ya bunduki hiyo palikuwa na nyundo, lundo la funguo bandia na chupa mbalimbali za ainaaina za sumu.

Niko barabarani, Othmani aliwaza, akilifuata gari la Joram kwa makini zaidi.

Gari lao lilipovuka kuifuata barabara ya Mwenge, yeye alipinda kuifuata ya Chuo Kikuu cha Mlimani. Alijua angewakuta wapi.

Kwa ujumla alijua wanakoelekea.
 
45.

W 8 X

LE wimbo uliozoeleka, wa “Hali ngumu ya uchumi,’ ambao uliimbwa zaidi na viongozi wa serikali na chama tawala kuanzia miaka ya themanini uliambatana na vikolombwezo lukuki. Miongoni mwa vikolombwezo hivyo ni kutoweka kwa uhuru wa kujitawala kichumi na badala yake kina IMF na Benki ya Dunia kushika hatamu. Na walizishika kwelikweli. Walimimina amri baada ya amri, zote zikielekeza serikali kujitoa katika huduma nyingi za jamii. Elimu, ambayo awali ilitolewa bure, ikawa ya kulipia, na hivyo, kufanya watu wengi washindwe kuimudu, huduma za afya kadhalika zikawa hazishikiki, mashirika ya UMMA yakauawa moja baada ya jingine huku maelfu ya waliokuwa watumishi wake wakitupwa nje ya soko la ajira. Kitu kinachoitwa ruzuku toka serikalini

kikafanywa nuksi.

Viongozi wengi, wakitembelea magari ya gharama kubwa na kuishi katika majumba ya fahari, walipokea kwa furaha kila amri toka juu. Walifumbia macho ukweli kuwa huko zinakotoka amri si wakulima tu bali hata ng’ombe wao walikuwa wakilipwa ruzuku. Aidha, waliziba masikio ukweli kuwa kila raia asiye na kazi, tangu mtoto mchanga, alikuwa akilipwa posho hadi anapopata ajira, na kwamba mwananchi kupata ajira lilikuwa jukumu la serikali pia, si raia pekee.

Hivyo, katika hali hiyo hakuna aliyeona kama ni jambo la





ajabu pale wizara inayohusika na masuala ya ardhi, kama wizara nyinginezo, ilipojisahau kwa miaka kadhaa na kulifanya suala la mipango miji kama mojawapo ya anasa. Upimaji wa maeneo mapya ulisimama, uendelezaji wa miundombinu ukasahauliwa. Wakubwa walikuwa ‘busy’ kugombea ubunge, wakubwa kidogo wakihangaikia semina na warsha mbalimbali huku wale wenzangu na mie wakiikimbiza shilingi, ambayo ilionekana kama imeota matairi.

Lakini maisha yalikuwa yakiendelea. Watu waliendelea kufa, watu waliendelea kuzaliwa. Jiji la Dar es Salaam lilizidi kuwa dogo, hivyo likaendelea kupanuka. Wajanja wachache waliwasukuma wenyeji toka katika maeneo yao asilia ya Kigamboni, Tabata, Tegeta, Bunju na kwingineko na kujenga mahekalu yao. Wenzangu na mie walivamia vichochoro, mifereji ya maji machafu na mabonde yote yaliyolizunguka jiji la Dar es Salaam na kuweka vibanda vyao. Mradi wawe karibu na Dar es Salaam. Karibu na neema.

Ni katika hali hiyo, pale Bunju, eneo moja la ekari tano lilipopata mwenyewe. Likalimwa, likapandwa miti na matunda na kuzungushiwa seng’enge. Katikati ya shamba hilo jengo dogo, la ghorofa mbili, likaibuka. Hakuna aliyelishangaa wala kulitilia maanani kwani majengo hayo yalikuwa yakiibuka kama uyoga kila upande wa jiji bila mpangilio.

Hali kadhalika, hakuna aliyeshangaa jengo lilipokamilika na mzee mmoja wa Kimamkonde alipokabidhiwa kulilinda, mwezi, miezi, mwaka na, hatimaye, miaka bila ya wenyewe kuhamia. Hilo pia halikuwa la ajabu kwani majengo ya aina hiyo yalikuwa mengi katika miji mipya ya kandokando ya jiji la Dar es Salaam. Baadhi ya majengo ya aina hiyo yaliwahi kukaa zaidi ya miaka kumi kwani mwenye nyumba alikuwa nazo nyingine pengine tatu au nne, watoto na wajukuu zake wakiishi Ulaya au Marekani huku ndugu wengine wakiwa wamesahauliwa vijijini.

Lakini jengo hili lilikuwa na muujiza mmoja. Mlinzi wa Kimakonde hakupata kumfahamu mwajiri wake kwa sura wala jina. Si kwamba hakuwahi kumwona au kutajiwa jina lake, la hasha. Alimwona zaidi ya mara tatu. Lakini kila alipomwona mwajiri huyu alikuwa na sura au umbile tofauti.





Hata mavazi yake pia hayakumsaidia sana. Kila safari alikuja na vazi tofauti na awali; mara joho la ki-Naijeria, mara suti ya Kiingereza, mara jeans za wachunga ng’ombe wa Texas; na kadhalika.

Mara zote hizo alitajiwa jina. Lakini lilikuwa gumu, la lugha iliyofanana sana na Kihabeshi au Kifaransa. Mmakonde hakulishika na asingeweza kulishika. Laiti angejua kuwa hakukusudiwa kulishika..

Kazi yake haikuwa ngumu, kutunza mazingira ya nyumba kwa kufyeka majani yanapozidi, kumwagilia maua na kutunza nyumba. Mshahara ulikuwa mnono. Wakati walinzi wengine waliambulia shilingi 15,000 kila mwezi, yeye alipokea 50,000 huku akiletewa chakula kingi ambacho kilimshinda.

Mzee wa Kimakonde alinenepa, akanawiri. Mashavu yake yaliyoanza kuingia ndani kwa lishe duni na upungufu wa meno mdomoni yalianza kujaa tena, sura yake ikirudia ujana. Tahamaki miaka yake sitini na minane ya umri ilishuka na kuwa arobaini na minane machoni mwa watu wengine, hali iliyomwezesha ajikute akiishi na msichana wa Kidigo, mwenye umri wa miaka ishirini, kama mama watoto wake.

Mafanikio na uhuru huo wa muda mrefu ulimfanya aanze kujisahau kuwa yeye ni mlinzi tu wa nyumba hiyo, badala yake akajiona kama mwenye nyumba. Hata aliwaambia hivyo rafiki zake wasiomjua vizuri, kwamba mwanawe anayeishi Japan ndiye aliyemjengea nyumba hiyo. Alianza hata kuota ndoto zinazoashiria mawazo hayo. Ndoto ambazo zilimwonyesha kuwa siku za karibuni mwanawe huyo angemletea gari la kutembelea na kumfungulia mradi wa bwawa la kuogelea.

Njozi zake hizo za usiku na mchana zilikoma ghafla, usiku wa saa tatu kasoro, pale kengele za geti zilipolia. Alipokwenda kufungua mwajiri wake aliingia na gari taratibu katika banda la kuhifadhia magari. Alikuwa katika mavazi ya ajabu zaidi machoni mwa Mmakonde. Na alifuatana na mwanamke! Mwanamke mzuri! Lakini kilichomvutia zaidi Mmakonde si mwanamke bali kile alichokiona katika mavazi ya tajiri wake wakati akishuka toka ndani ya gari.

Damu!

Nguo zake zilikuwa zimeloa damu!





Mmakonde huyo alipata mshituko mkubwa zaidi pale alipomwona tajiri wake akimvuta mgeni wake huyo ambaye alifungwa pingu za mikononi. Yeye pia alikuwa na michubuko usoni na mikononi.

“Funguo, tafadhali,” aliomba huku akijaribu kumtoa wasiwasi mlinzi huyo kwa kumzawadia tabasamu jepesi.

“Funguo zipi?”

“Za geti. Sitaki mtu yeyote aingie wala kutoka humu ndani leo. Sawa?”

“Sawa… bo… bosi,” alijibu akitoa funguo hizo na kumkabidhi.



***

Kama ilivyo katika mambo yake mengine, Joram Kiango aliijenga nyumba hii kwa siri kubwa. Akiwa amejenga katika shamba alilonunua kwa mzee wa Kizaramo aliyeamua kurudi Bagamoyo, Joram hakuhitaji kutumia jina lake halisi. Na hata maombi yake ya hatimiliki ya eneo hilo pale Wizara ya Ardhi yalikuwa katika moja ya majina yake ya akiba. Mafundi aliowatumia aliwatoa nje ya nchi na hakuonana nao mara kwa mara isipokuwa tu pale ilipobidi. Wao pia walimjua kwa majina tofauti na walikuwa wakibadilishwa kila hatua, kiasi kwamba hakukuwa na fundi yeyote mwenye ramani halisi ya jengo hilo.

Kazi nyingine, nyeti zaidi, Joram Kiango alizifanya kwa mkono wake mwenyewe, usiku na mchana, akitumia vitendea kazi ambavyo ama alinunua ama alikodisha kwa hila vilevile. Alifunga umeme kwa njia na namna zake, aliunganisha maji na mashine za kupozea hewa kwa mitindo yake na kuweka milango na madirisha kwa namna ya kukidhi mahitaji yake. Alikuwa na vyumba vya siri na milango ya siri ambayo mtu yeyote asingebaini bila matakwa yake.

Ilipokamilika ilikuwa nyumba ya pekee, ingawa wapita njia waliichukulia kama mojawapo ya nyumba za kawaida. Kumwajiri mzee yule wa Kimakonde ili ailinde, badala ya kuitumia moja ya kampuni lukuki za ulinzi zilizopo jijini, kwa Joram ilikuwa sehemu ya kuendeleza usiri wa jengo lake hilo. Mzee hakuwa mdadisi, wala hakuwa makini. Mara nyingi





sana Joram amekuja nyumbani hapo na kufanya shughuli zake huku mzee akiwa hana habari. Mara mbili aliwahi kulala usiku mzima na kuondoka zake alfajiri huku mlinzi wake akikoroma.

Hivyo, kadhia hili zito, ambalo liliambatana na vifo na maafa ya kila dakika, lilimfanya Joram Kiango alazimike kuja hapa. Hakuona wapi pengine panafaa kumweka kitako msichana huyo wa ajabu anayejiita Mona Lisa na aliyefanana naye reale kwa ya pili, msichana ambaye hashikiki, hatabiriki.

Haikuwa kazi rahisi kumfikisha hapo. Mara mbili walinusurika kifo kufuatia vurumai ambayo aliianzisha ghafla mara walipokaribia Barabara ya Bagamoyo. kwa bahati, joram alikuwa tayari. Ule utulivu na ukimya wa muda mrefu aliokuwa nao toka Uwanja wa Ndege haukumpumbaza Joram. Alikuwa makini, jicho lake la wizi likiwa halijamwacha hata kwa dakika moja. Hivyo, pale Joram alipomwona akifumbua macho kwa hila na kisha kuyafumba, huku mkono wake mmoja ukipelekwa taratibu katika mfuko wake wenye bastola, Joram alimsubiri. Mara tu alipoipata bastola hiyo Joram alimpokonya, kitendo ambacho kilifuatiwa na pigo kali la kareti toka kwa msichana huyo. Pigo hilo lilimpata Joram Kiango barabara shingoni, likalifanya gari liyumbe, nusura kupinduka. Kwa bahati, Joram aliwahi kulizima gari huku akizuia pigo la pili na kuachia lake lililompata shingoni na kumlegeza msichana huyo. Joram aliitumia fursa hiyo kumkamata na kumtia pingu za mikono. Alishangaa kuona Mona Lisa huyo akiruhusu kufungwa pingu kwa utulivu kabisa, kinyume na matarajio yake.

“Uko tayari kuzungumza?” Joram alimhoji msichana huyo.

Hakujibu. Badala yake alifumba macho yake na kukilaza kichwa chake kwenye kiti.

Jaribio la pili alilifanya wakati gari likikaribia kuvuka daraja linaloitenga Tegeta na Bunju. Kwa kuitumia mikono yake yenye pingu, aliuvamia usukani na kuupinda akilielekeza gari kutumbukia mtoni. Joram alitumia nguvu za ziada kulirejesha barabarani. Lakini haikuwa kabla ya gari hilo kugonga ukuta wa daraja na kubonyea vibaya upande wa kushoto. Kwa bahati, magari yalikuwa yamepungua sana njiani. Vinginevyo,





hadithi ingekuwa nyingine.

‘Mona Lisa’ alitulia tena. Hakufanya vurugu ya aina yoyote tangu gari lilipoondoka eneo hilo, likaiacha Barabara ya Bagamoyo na kufuata njia ndogo iliyowafikisha yalipo makazi ya Joram Kiango. Wala hakuwa mbishi wakati geti lilipofunguliwa naye kuongozwa hadi ndani ya jumba.

“Tunahitaji kuzungumza,” Joram alimwambia mara walipofika ndani. “Bila shaka mazungumzo yetu hayatakuwa mafupi. Hivyo,” aliongeza, “Nadhani unahitaji kuoga. Umechakaa sana.” Alimwelekeza kwenye kimojawapo cha vyumba vya wageni na kumfungulia akimwambia, “Humo kuna bafu, sabuni na dawa za meno. Nadhani utapata hata nguo za kubadili. Tumia muda wako, usiku bado mbichi huu.” Joram alitoa funguo za pingu na kumfungua mikono.

“Usijisumbue kufikiria kutoroka,” alimwambia. “Ni rahisi sana kuingia katika nyumba hii, sio kutoka,” alisema akivuta mlango wa chumba na kuufunga kwa rimoti.

Yeye pia alihitaji kuoga. Alikuwa mchovu na mwenye njaa. Hali kadhalika, hakuwa amechafuka tu, bali kuchakaa. Mchanganyiko wa damu, jasho na vumbi mwilini mwake ulimfanya ajisikie kunuka. Alitamani sana aingie katika beseni lake la kuogea, ajilaze katika maji ya baridi na kukaa humo kwa saa moja au zaidi.

Lakini hakuwa na muda huo. Alikuwa na mengi ya kufanya. Awali ya yote, alihitaji kukaa mbele ya kompyuta yake. Alihitaji majibu ya maswali aliyoyasambaza kwa rafiki zake kupitia mtandao wa E-mail. Hivyo, alikiendea chumba chake cha kujisomea na kuiwasha kompyuta yake ndogo, lap top aina ya Mackintosh toka katika kiwanda cha yule kijana tajiri kuliko watu wote duniani, Bill Gate. Pia, akafungua mtandao wake wa huduma ya bure, hotmail, na kuita moja ya anuani zake zenye majina bandia.

Alikuwa hata hajatulia vizuri wakati mlio wa risasi za SMG

uliposikika ghafla toka mbele ya geti lake.



***

Othman Mchopanga alikuwa amemfuata Joram Kiango hadi nyumbani kwake kwa urahisi kuliko alivyotegemea. Kuna





wakati aliwatangulia na kuruhusu magari kadhaa kati yao, mara moja walimpita kasi na kuendelea na safari yao. Kwa mbali alizishuhudia zile purukushani za yule msichana na Joram Kiango pale darajani. Angeweza kuwaua kwa urahisi sana na kulilipua gari lao kwa tenki la gari lao lakini alisita kufanya hivyo. Alitaka kazi yake iwe nzuri, ya kujivunia, si kubahatisha.

Faida moja ya kuishi katika dunia ya kile marafiki zake wanachokiita ‘dunia ya mafichoni’ ni kujua mambo mengi ya watu wengine hali yako hayajulikani, mfano mzuri ukiwa safari hii ya kumfuatilia Joram Kiango. Hakuwa na papara ya kufanya lolote kwa kuwa alijua wanaelekea wapi. Alipata fununu muda mrefu kuwa jengo lile lilikuwa la Joram Kiango. Hakupata kufikiria kuwa fununu hizo zingekuwa na manufaa yoyote kwake hadi leo, wakati akiwafuata kwa kazi moja tu.

Wakati huohuo alikuwa na hakika kabisa kuwa hakuna mtu yeyote aliyejua kuwa mbili kati ya zile boti ziendazo kasi kati ya Dar es Salaam na Zanzibar ni zake. Hali kadhalika, kama wapo waliofahamu ni wachache sana, kuwa hoteli nne za kitalii jijini Dar es Salaam, Arusha na Zanzibar ni zake. Walichofahamu majirani zake kule Makongo Juu ni kuwa yeye alikuwa mfanyabiashara wa jumla wa vipodozi toka Dubai na Falme za Kiarabu. Aidha, walimtambua kama mtu mpole, mkarimu na muumini mzuri wa dini ambaye alikosa sala kwa nadra sana.

Mtu ambaye hakumtambua zaidi ya watu wote ni mkewe. Binti Kalenga, mtoto wa Kifipa aliyezaliwa na kukulia Dar es Salaam aliolewa angali kinda, mara baada ya kushindwa kuendelea na elimu ya sekondari. Baba yake, mzee Kalenga, akiwa amezibwa macho kwa kitita cha fedha za kishika uchumba, mama yake akiwa amelogwa kwa zawadi za mavazi na hereni za dhahabu kutoka Dubai, binti yao angepata lipi la kusema? Yeye pia, mara baada ya kuingia katika ‘hekalu’ la mume wake na kukabidhiwa umalkia wa kila kitu katika nyumba hiyo moyo wake haukuwa na nafasi ya kumchunguza mume wake. Na pale alipopewa usimamizi kamili wa bidhaa zote toka nje, huku mara mojamoja wakisafiri pamoja kwenda nje, alijikuta akiondokea si kumwamini tu bali kumwabudu
 
46.

mume wake. Hakuhoji chochote pale mume alipotoweka ghafla kwa siku na hata wiki kadhaa na kurejea akiwa na hadithi za ‘safari ya ghafla.’ Hakushangaa pindi mumewe anapoondoka mikono mitupu na kurejea na fuko lililofurika noti.

Ni siku moja tu ambapo alipata kumshuku mumewe. Alikuwa amempigia simu kuwa angesafiri ghafla kwenda Nairobi. Lakini usiku wa manane alirejea akiwa na jeraha baya la risasi katika ubavu wake wa kushoto. Hadithi yake ilikuwa fupi tu, “Nimevamiwa na majambazi.” Lakini binti Kalenga alipomshauri atoe taarifa polisi alikataa katakata kwa kisingizio kuwa hakuwa na muda wa ‘kuwasaidia polisi.’ Hata alipomshauri kwenda hospitali vilevile aligoma kwa maelezo kuwa angelazimika kupata fomu za PF3 ambazo zingewafanya polisi wamlazimishe ‘kuwasaidia.’

Mkewe alilazimika kuchukua nafasi ya udaktari na unesi. Kwa maelekezo ya mumewe, alimtibu jeraha hilo usiku na mchana kwa wiki mbili bila kumhusisha wala kumweleza mtu yeyote juu ya ‘ugonjwa’ wa mumewe. Jeraha lilipopona mumewe alimpa zawadi ya kutembelea Ufaransa na Ubelgiji, akiwa na ruhusa ya kunua chochote ambacho angekitamani. Aliishia kununua magauni sita ya mmeremeto, kwani kila alichohitaji alikuwa nacho.

Maisha yalikuwa matamu kama ndoto ya kuvutia si kwa Binti Kalenga tu, bali pamoja na Othman mwenyewe. Hakukoma kushangaa kwa jinsi hali yake ya uchumi ilivyokuwa ikipanda kwa kasi siku baada ya siku toka baada ya ile ‘kazi’ yake ya kwanza, kazi ambayo ilisambaza sifa zake na kumpa hadhi kubwa katika dunia yao ya giza.

Ilikuwa ndio kwanza anarejea nchini toka katika gereza moja nchini Pakistan, ambako alifungwa maisha kwa kukamatwa na dawa za kulevya alizobeba kwa matarajio ya kulipwa chochote iwapo angefanikiwa kufika nazo jijjini Dar es Salaam. Kwa bahati, alitumikia kifungo hicho miaka miwili tu na kufanikiwa kutoroka wakati ulipozuka mgomo gerezani humo, uliofuatiwa na mapambano makali baina ya polisi na wafungwa. Alikuwa miongoni mwa wafungwa wanane waliobahatika kutoroka. Akapata hati za bandia na kuvuka mipaka ya nchi hadi nchi hadi alipofika Dar es Salaam. Akiwa





amejifunza mengi gerezani humo, akiwa ametaabika sana kwa njaa na karaha nyinginezo wakati wa ukimbizi wake, Mchopanga aliapa kuwa asingekubali tena kurudi katika umasikini.

Hasira zake dhidi ya umasikini zilianzia kwa mtu aliyemtuma kuchukua mzigo ule Pakistan na kisha kumtelekeza mara alipokamatwa. Alikuwa mtu mzito kisiasa na kibiashara. Alikataa katakata kumfidia Mchopanga kwa masaibu yaliyompata kwa maelezo kuwa uzembe wake ulimsababishia hasara kubwa. Kwa ujumla, alimfukuza kama mbwa na kumpiga marufuku kukanyaga nyumbani kwake. Hata pale Mchopanga alipomtishia kuwa angelipa kisasi tajiri huyo alicheka na kumpuuza.

Lakini wiki moja baadaye alipookotwa chini ya uvungu wa kitanda chake, kichwa chake kikiwa kimetenganishwa na kiwiliwili chake kwa kisu, huku sefu lake la fedha lilikutwa tupu; ndipo sifa za Mchopanga ziliposambaa kama upepo. Haukupita mwezi kabla hajaombwa kumtoa roho polisi mmoja aliyelishikilia jalada la kesi ambayo ingewaumbua wakubwa fulani. Huyu kifo kilimkuta wakati akila chakula cha usiku na familia yake. Mtutu wenye bastola iliyowekwa kiwambo cha kuzuia sauti ulimchungulia dirishani na kumfumua moyo. Wakati familia hiyo ikitokwa na mshangao na kupiga mayowe. Mchopanga tayari alikuwa mtaa wa pili wa eneo hilo.

Matukio hayo yalifanya atumiwe na watu mbalimbali, wanasiasa wenye visasi na wenzao, wafanyabiashara waliodhulumiana, washitakiwa waliokusudia kufutilia mbali ushahidi; na kadhalika. Na kati ya waliomtumia, kila ambaye alijaribu kukiuka makubaliano roho yake ilikuwa halali yake. Wakati wote huo, machoni mwa jamii isiyojua chochote kinachoendelea nyuma ya mapazia, Othman Mchopanga aliendelea kuwa mfanyabiashara halali, aliyelipa kodi zote na kustahi heshima zote. Tabasamu zake za mara kwa mara, uchangamfu wake kwa kila mtu na misaada kwa wahitaji mbalimbali hakukumpa mtu yeyote fursa ya kufikiria tu

kuwa angeweza kuwa mtu wa aina yake.

Hivyo, ilipokuja kazi mpya, ya kuua kasichana tu, tena kakiwa kamelala kitandani, kwa mamilioni ya fedha; aliona





kama aliyekaribishwa katika mchezo wa kitoto. Hakukutana na tajiri wake huyo ana kwa ana. Lakini mjumbe wake alipokuja na kila kitu alichokihitaji; picha ya marehemu mtarajiwa, ratiba ya mwenendo wake, namba ya chumba atakacholala na, zaidi ya yote, fuko la mamilioni ya malipo yake, aliitekeleza kama mchezo vilevile, ingawa alikuwa amemfuatilia wiki nzima kwa taabu sana.

Hivyo, kuambiwa kuwa alikosea na kupewa mtu mpya ambaye yeye alikuwa na hakika kuwa ndiye yuleyule ambaye alimuua tokea majuzi; pamoja na mtu anayeitwa Joram Kiango kuongezwa kwenye orodha hiyo, ndipo Mchopanga alipojikuta akianza kuvutiwa na ‘mchezo’ huo.

Hivyo, aliruhusu dakika ishirini zipite kabla hajaanza kunyata kuuendea upande wa pili wa uwanja wa jengo hilo, ambako alitegemea kukata seng’enge ili apenye ndani. Giza likiwa limetanda huku na huko, nyumba za jirani zikiwa ekari moja au zaidi pembeni, huku kichaka cha miti na nyasi kikiwa kimeshamiri upande huo; Othman Mchopanga hakuwa na shaka yoyote ya kuvurugikiwa na ratiba yake hiyo.

Mshangao wa kwanza aliupata pale alipoifikia sehemu nzuri na kugusa seng’enge ili aanze kuzikata. Alijikuta akitupwa angani na kisha kuanguka chini kama gunia. Umeme! Aliwaza. Nyaya zilikuwa zimetegeshwa umeme. Alijikusanya, akajifuta vumbi na kisha kutoa vifaa vyake ili aone kama alikuwa na kitu chochote ambacho kingemwezesha kukata nyaya hizo bila kugusa umeme.

Ni wakati akifanya hivyo alipopatwa na mshangao wa pili. Alijikuta akimulikwa ghafla na kurunzi yenye mwanga mkali, mwanga ambao ulifuatiwa na sauti kali iliyotokea ghafla kichakani humo ikisema; Polisi! Weka mikono yako juu!”

Hakuyaamini masikio yake. Polisi! Wametokea wapi na wanafanya nini hapo?

Weka mikono yako juu! Amri ya pili! Aliamrishwa tena. Mchopanga hakuwa mtu wa kutii amri, hasa za polisi.

Badala ya kuweka mikono yake juu aliipeleka mfukoni mwake na kutoa bastola. Pamoja na ukweli kuwa alikuwa kipofu kwa nuru kali iliyokuwa ikimmulika machoni, pamoja na kuwa hakupata muda wa kulenga; lakini bado aliachia





risasi mbili za harakaharaka kufuata kurunzi hiyo. Alisikia kilio cha mtu, kikifuatiwa na kurunzi kudondoka. Ni hayo tu aliyoweza kuyaona kwani sekunde hiyohiyo alinyeshewa na mvua kubwa zaidi ya risasi ishirini ambazo zilimfanya akate roho hata kabla hajaanguka.



***

Utajisikia vipi pale utakapojikuta ukipigiwa simu na Rais wa Jhamuri ya Muungano wa Tanzania, ambaye pia ni Amiri Jeshi Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi na Usalama? Zaidi utajisikia vipi wakati Rais akikumiminia maswali mazito, tena ya harakaharaka, ambayo wewe huna majibu yake.

Hayo ndiyo yaliyomkuta Inspekta Haroub Kambambaya jioni hiyo. Alikuwa bado kaduwaa ofisini mwake, juu ya kiti chake, mikono yake yote miwili ikiwa inakilea kichwa chake ambacho alikiona kizito zaidi kufuatia taarifa mpya toka Uwanja wa Kimataifa wa Dar es Salaam. Vifo vya watu watano, wawili kwa risasi, watatu kwa kukanyagana, huku wengine kwa makumi wakikimbizwa mahospitalini, taabani kwa kukanyagwa ama kujipigiza kwenye kuta na ajali za magari, vilimfanya achanganyikiwe.

Kilichomchanganya zaidi Kambambaya ni taarifa ya kuonekana uwanjani hapo kwa yule mwanamke wa miujiza, ambaye kila anapotokea maisha ya watu wengi huteketea, mwanamke ambaye kama kawaida yake alitoweka tena wakati watu wengi, wakiwemo wanausalama, wakiuguza maumivu makali ya ile sumu ya macho.

Uamuzi wa Kambambaya kuweka ulinzi mkali katika vyanzo vyote vya kutokea jijini Dar es Salaam ulitokana na matarajio ya kumpata Joram Kiango, ambaye aliamini angekuwa ufunguo wa kadhia hii ya kutatanisha. Badala yake aliyetokea tena ni yule mwanamke, ambaye ameondokea kuwa kama mjumbe wa kifo.

Kutoweka kwa maiti yake pale Muhimbili na kudaiwa kwake kuwa anazuka hapa na pale, kuzuka kunakoambatana na vifo hakukumwingia akilini Kambambaya. Kama angekuwa anaamini miujiza na ushirikina angeweza kuapa kuwa mwanamke huyu ni mzimu wa yule aliyetoweka chumba cha





maiti kule Muhimbili. Kambambaya hakuwa na imani hiyo. Hivyo, akajikuta akiishia kukilea kichwa chake, kilichojaa maswali mengi majibu sifuri.

Na wakati akiendelea kuwaza na kuwazua ndipo ikaingia kengele ya simu yake maalumu, ambayo haikuorodheshwa mahala popote. Alipoipokea, sauti nzito ambayo daima haina mzaha, ilinguruma kutaka aeleze kinachoendelea. “Nchi imekumbwa na hofu kubwa. Vifo na maafa kila dakika. Unadhani ni kitu gani kinachotokea?” Ile sauti iliuliza.

Kambambaya alikuwa hana jibu sahihi. Aliropoka hili na lile ambalo bila shaka Rais alilipuuza na badala yake akaongeza swali jingine, “Kitu gani ambacho mnafanya, ambacho mnadhani kitakomesha maafa haya mara moja?”

“Tunafanya kila tunaloweza mzee,” Kambambaya alijikongoja. “Tunachukua kila hadhari. Nadhani tutafanikiwa tu.

“Nasikia mnamtafuta Joram Kiango. Mmeshampata?” “Bado mzee, lakini…”

“Lakini!” Rais alikatiza tena. “Siku zote niliamini Joram Kiango ni kijana wetu. Na amefanya mengi ambayo yameliletea taifa letu sifa na hadhi kubwa duniani. Leo yakoje tena mambo hayo?”

“Ndiyo maana tunamtafuta mzee. Ili atusaidie. Tunaamini tukimpata tutapata mwanga mapema zaidi,” Kambambaya alijitetea.

“Ningependa hali hii isiendelee tena katika saa ishirini na nne zijazo,” Rais alisema. “Nadhani umenielewa, Inspekta.”

“Ndiyo, mzee.”

Simu ikakatwa upande wa pili.

Kambambaya aliona simu kama imezidisha tani elfu moja zaidi juu ya kiroba kizito kilichomwelemea kichwani.

Hivyo, ilikuwa kama faraja kubwa kwake nusu saa baadaye alipopokea taarifa ya Joram Kiango kuonekana akiingia katika nyumba moja huko Bunju, huku akimburuza mwanamke mmoja.

“Nakuja,” alitamka mara moja, akiinuka na kuuendea mlango, aliikumbuka bastola yake iliyokuwa katika kijaluba cha meza. Akaikagua na kuona kuwa ilijaa risasi. Akaitia
 
47.

mfukoni na kulikimbilia gari lake.

“Bunju! Kwa mwendo wa kupaa,” alimwamuru dereva wake ambaye alikwishalitia gari moto.

Kuwa mkubwa wa Idara kuna raha na karaha zake. Karaha ni pale mambo yanapokwenda mrama kama sasa, lawama zote hutupwa juu ya mabega yako. Lakini ziko nyakati za neema, nyakati ambazo utafurahia madaraka yako si kwa ajili ya mshahara mnono, nyumba nzuri na marupurupu mengine peke yake. Zaidi ni kwa kuwa katika nafasi ya kujua na kuhifadhi mambo mengi kuliko wasaidizi wako, kujua mkubwa yupi ana siri ipi, yupi anaumwa na anaumwa ugonjwa upi, yupi anaiba na fedha zake amezificha wapi, yupi amemkabidhi yupi kulinda miradi yake haramu; na kadhalika.

Kuzijua siri nyingi za Joram Kiango kwa Kambambaya ilikuwa miongoni mwa neema hizo za ukubwa. Hakuna msaidizi wake hata mmoja aliyejua kuwa amejenga. Hata pale alipowaagiza askari wanne kuilinda nyumba hiyo, usiku na mchana, hakuwaambia ni nyumba ya nani. Hivyo alipopata simu ikimwarifu juu ya Joram Kiango kuonekana huko Bunju akiingia kwenye ‘nyumba moja’, alifurahi kuona moja ya mitego yake ikifyatuka.

Dereva wa Kambambaya alikuwa ‘kichaa’ barabarani. Alikwishapewa amri ya ‘mwendo’ wa ‘kupaa,’ alipaa kikwelikweli. Alitafuna lami, akiyapita magari upande huu na ule kana kwamba yuko katika mashindano. Alivuka Lugalo, akitafuna Mbezi Beach na kuimeza Tegeta katika muda wa dakika nane tu. Lami inayovutia toka Tegeta hadi Bunju ililifanya gari liteleze kwa dakika nne tu hadi walipoufikia uchochoro unaoelekea kwenye nyumba waliyohitaji.

Kwa maelezo ya Kambambaya waliliacha gari mita kadhaa nje ya eneo la nyumba hiyo na kutembea kwa miguu. Milio ya risasi iliwafikia wakiwa mita tano tu toka kwenye eneo la tukio. Huku akiitoa bastola yake mfukoni, Kambambaya alikimbia kuliendea eneo hilo.

Alikuwa tayari amechelewa. Askari wake watatu, silaha zao mkononi waliduwaa wakiitazama miili ya watu wawili waliolala chini wakiwa maiti. Maiti mmoja alikuwa msaidizi wake, afande Chaku Chikaya. Maiti wa pili alikuwa raia.





Kambambaya aliyatazama harakaharaka na kushusha pumzi alipoona kuwa marehemu hakuwa Joram Kiango.

“Kitu gani kimetokea?” aliuliza.

Askari mmoja alieleza jinsi walivyomwona marehemu huyo akifanya jitihada za kujipenyeza ndani. Na kwamba alipopewa amri ya kusimama ili ajitambulishe alitoa bastola yake na kumuua mwenzao aliyekuwa akimmulika kwa kurunzi, kitendo ambacho kilifanya walazimike kummiminia risasi ili kuokoa maisha yao.

Kambambaya aliamuru gari la wagonjwa liitwe mara moja na kuwachukua marehemu. Aliamuru pia mpigapicha apige picha za yule raia kwa makini zaidi pamoja na kuchukua alama za vidole vyake ili uchunguzi kamili juu yake uweze kufanyika.

“Natumaini Joram Kiango bado yumo ndani.” “Yumo afande.”

“Na mateka wake.” “Bila shaka.”

“Mnadhani kuna watu wengine zaidi yao ndani ya nyumba hii?”

“Ndiyo, afande. Yumo mlinzi wake, mzee mmoja mlevimlevi na mkewe.”

Kambambaya alifikiri kwa muda kabla ya kutoa amri nyingine, “Tuko wangapi hapa? Sita.” Aliuliza na kujijibu. Halafu akatoa amri, “Nataka kila pembe ya ua huu iwe na mtu mmoja. Kila mmoja awe makini kuhakikisha hatoroki. Mimi na askari wawili tuliobaki tutaingia kupitia geti la mbele. Sawa?”

“Sawa, afande.”

“Sawa. Sasa kuna kitu kimoja. Bado tunamtaka sana Joram Kiango, akiwa hai. Zaidi, tumechoshwa na vifo vya hapa na pale. Hivyo, kila mmoja wenu awe makini katika kutumia silaha. Zitumike pale tu inapobidi, si vinginevyo.”

Askari waliitikia kukubali. Kisha kila mmoja akachukua sehemu yake. Kambambaya aliuendea mlango wa geti la mbele kwa nia ya kuusukuma.

“Mzee, ametegesha umeme” mmoja wa askari aliokuwa nao alimwonya.





“Ametegesha umeme!” Kambambaya alirudia maneno hayo kwa mshangao. “Sidhani kama itamsaidia sana.”

Alirudi kwenye gari lake na kumwamuru dereva wake ampe kipaza sauti. Alipopewa alirudi getini na kukielekeza ndani ya nyumba hiyo. “Joram Kiango,” alinguruma. “Tunajua uko ndani. Tunajua unao watu wengine watatu. Wote inueni mikono yenu juu na mtoke mara moja. Hii ni amri halali ya jeshi la polisi.”

Kambambaya alisubiri dakika moja kisha aliirudia tena amri hiyo kwa sauti kubwa kuliko awali.

“… amri ya pili,” alimaliza.

Baada ya kusubiri dakika moja nyingine alirudia ujumbe uleule kwa mara ya tatu na kumalizia akisema “… amri ya tatu na ya mwisho.”

Bado hakujibiwa. Hivyo, akaongeza “Sasa tutatumia nguvu, kwa mujibu wa sheria halali za nchi.”

Kwa kutumia redio yake ya mkononi Kambambaya aliagiza askari ishirini zaidi waletwe eneo hilo. Aidha, aliagiza eneo hilo likatwe umeme mara moja ili waweze kukata nyaya hizo kwa urahisi.
 
48.

W 9 X



MBIU ya Inspekta Kambambaya ilimfikia Joram Kiango vizuri kabisa chumbani humo. Mbiu hiyo ilifuatia mlio wa risasi toka nyuma ya jengo lake. Hata hivyo, hii ikiwa nyumba yake, aliyoijenga kwa mkono wake, Joram alijikuta akimhurumia Inspekta huyo. ‘Atasubiri sana.’ Aliwaza. Macho yake yalikuwa bado yamezama kwenye tovuti ya hotmail vidole vyake vikigonga hapa na pale kwenye bodi ya maandishi.

Angeweza kushangazwa na wepesi wa polisi hao kufika nyumbani kwake hapo dakika chache tu baada ya kufika kwake. Angeweza kushangaa zaidi kwa kuzingatia kile alichoamini kwamba polisi walikuwa wakimfikia haraka kwa kufuatilia nyendo za mwanamama huyu anayejiita Mona Lisa, ambaye yeye binafsi alifanikiwa kuyabaini maficho yake yote kwa kuongozwa na ile pete aliyokuwa akiivaa, pete ambayo aliitelekeza katika choo kimojawapo cha Uwanja wa Ndege wa Dar es Salaam. Msichana huyo sasa akiwa mateka wake, naye akiwa na kila hakika kuwa hakufuatwa na mtu yeyote, achilia mbali polisi, toka uwanjani hadi hapa, angeweza kushangazwa na wepesi huo wa polisi.

Hali kadhalika, Joram angeweza kushangazwa au kujiuliza risasi zilizotembezwa huko nje zilikuwa baina ya nani na nani. Kwa bahati mbaya, Joram hakuwa na muda huo kwa sasa. Kitu alichokuwa akikisoma katika kompyuta hiyo





kilimshangaza na kumvutia zaidi. Ulikuwa ujumbe mfupi, toka kwa mmoja wa rafiki zake aliowasambazia ili wampe kile walichokifahamu juu ya mtu anayeitwa Mona Lisa, nchini Tanzania na duniani.

Wengi walikuwa hawajamjibu lolote. Wawili watatu walimkumbusha juu ya yule Mona Lisa aliyepata umaarufu duniani baada ya kuchorwa kule Italia takribani miaka mia sita iliyopita. Lakini kati yao mmoja ndiye aliyemsisimua zaidi.

Mona Lisa: Jina la utani alilopewa toka utotoni Jina halisi: Margareth Johnson

Kuzaliwa: Agosti 28,1958

Kufa: Agosti 28, 2000 Sababu ya kifo: Ajali ya gari.

Kazi yake: alikuwa askari, Jeshi la Polisi Kituo: Moshi mjini, Kituo cha kati.

“Joram Kiango…” sauti ya Inspekta ilinguruma tena na kumfikia Joram. “Tunajua uko ndani… inueni mikono yenu juu na mtoke mara moja… Amri ya tatu.”

Joram alipuuza. Alifungua maandishi juu na kufungua kiambatanisho kilichotumwa na taarifa hiyo. Kilikuwa na picha mbili. Moja ilikuwa picha ya mazishi, polisi wakitoa heshima zao za mwisho kwenye jeneza lenye maandishi; SJN MARGARETH JOHNSON. Picha ya pili ilikuwa ya ‘merehemu,’ enzi za uhai wake. Alikuwa amesimama, katika mavazi yake ya kijeshi, huku akitabasamu.

“… Amri ya nne na ya mwisho… sasa tutatumia nguvu…” Kambambaya alikuwa akiendelea kufoka katika kipaza sauti.

Joram hakumsikia. Au hasa hakumsikiliza. Alikuwa amekodoa macho kuitazama picha hiyo.

Haikuwa ya mtu mwingine zaidi ya Mona Lisa.

Mara ikamjia kumbukumbu ya usiku ule wa chanzo cha balaa. Yale maneno ya Mona Lisa yakamrudia akilini aliposema, “Ni kweli hujui… Hujui kama unabaka. Na unambaka afisa wa ngazi za juu wa Jeshi la Polisi…”

Mona Lisa ambaye ni mateka wake katika chumba kimojawapo katika nyumba hiyohiyo! Mona Lisa ambaye majuzi tu alikufa hali wamekumbatiana pale hotelini! Mona Lisa ambaye maiti yake yalitoweka toka chumba cha maiti





Muhimbili! Mona Lisa ambaye amekuwa akimtokea tena na tena, huku kutokea kwake kukiambatana na maafa makubwa! Mona Lisa…

Chochote ambacho Joram alijaribu kukiwaza kilitoweka pale umeme ulipokatika ghafla na kiza totoro kukimeza chumba hicho na jengo zima.



***

Inspekta Kambambaya hakuyaamini macho yake pale umeme uliokatizwa katika eneo lote hilo ulipowaka ghafla katika jengo zima la Joram Kiango. Ilichukua dakika moja tu kiza kutanda katika nyumba hiyo, dakika ya pili nuru ya uhakika, kama ileile ya awali, ilitamalaki.

Laiti angejua kuwa kitendo cha kukatika kwa umeme unaomilikiwa na Tanesco katika jengo la Joram ni kufyatua mtambo mwingine wa umeme, uliounganishwa kwenye envetor ambayo ilipokea umeme utokanao na mwanga wa jua, kupitia katika betri kubwa ya gari na kusambazwa katika njia zote za umeme kama kawaida, kamwe asingejisumbua kuamuru katizo la umeme.

Kambambaya aliduwaa kwa dakika moja mbili, akitafakari afanye lipi jingine. Alikuwa na taarifa ya kuunganishwa kwa umeme kwenye nyaya zilizoizunguka nyumba hiyo. Na alikuwa na hakika kuwa isingewachukua vijana wake dakika kumi kutumia vifaa vyao kukata nyaya hizo na kuingia ndani. Lakini hakujisikia kufanya hivyo. Hakuona kama ingekuwa hekima kuwapeleka vijana wake, ‘mchana kweupe,’ mbele ya mtu kama Joram Kiango na hasa akiwa pamoja na mwanamke yule ambaye amekuwa kama anayefuatana na kifo popote alipo.

Wakati akiwaza hayo mara alisikia sauti ya kike ikiangua kilio toka ndani ya nyumba hiyo, sauti ambayo ilifuatiwa na kishindo kwa kupigwa mlango mara kwa mara.

“Nifungulieni nitoke… sitaki kufia humu,” mwanamke huyo

alisikika akisema katikati ya kilio chake.



***

Aliyekuwa akilia ni yule msichana wa Kidigo, Natasha, mke





wa mzee wa Kimakonde.

Hofu ilianza kumwingia msichana huyo toka pale alipoona mumewe akifungua mlango na kuwaruhusu yule mwanamume na mwanamke wake kuingia huku wakivutana. Watu hao walimtia hofu, mwanamume akiwa kaloa damu, bastola mkononi, huku akimkokota mwanamke yule mzuri, ambaye pia alichakaa. Huku akitetemeka, Natasha aliwachungulia hadi walipoingia kwenye vyumba vyake.

Mume wake alimwongezea hofu pale yeye pia alipoonyesha kila dalili ya kuduwaa, akiwa hana uhakika kama huyu ndiye mwajiri wake au la, na kama ndiye kwa nini awe na damu, bastola mkononi, huku akimburuza mtu muda huo.

Hofu yao iliongezeka maradufu pale risasi zilipoanza kurindima huko nje, risasi ambazo muda mfupi baadaye zilifuatiwa na tangazo la polisi likiwataka kutoka nje.

Natasha alikurupuka kukimbilia nje. Kwa mikono yake inayotetemeka alijaribu kufungua mlango huo ili atoke. Hakufanikiwa. Ilimchukua muda kubaini kuwa kitasa cha kawaida cha mlango huo hakikuwa kimefungwa, bali kitasa kingine, ambacho kilifunguliwa kwa nguvu za electroniki ndicho kilichochukua nafasi.

Halafu, umeme ukakatika.

Halafu, ukarudi tena ghafla.

Ndipo alipoangua kilio akiamini kuwa maisha yake yamefika ukingoni. Akaulaumu umasikini wa wazazi wake uliomfanya ashindwe kuendelea na shule na, hivyo, kuja mjini kwa matarajio ya kupata kazi, kazi ambayo iliishia kuwa ya kuuza pombe za kienyeji katika vilabu. Akailaani ‘bahati’ yake iliyofanya jioni ile, baada ya kununuliwa kuku na viazi, akubali kuondoka na mzee huyu mwenye umri zaidi ya baba yake mzazi. Akaishutumu zaidi tamaa yake pale alipoletwa katika jumba hili na kukuta lilivyojaa tele vitu vya anasa na vyakula ainaaina, jambo lililopelekea ajikute akisahau kurejea katika geto lake kule Mabwepande na kujikuta mke katika jengo hili, ambalo sasa lilielekea kuwa kaburi lake.

Kichwani mwake alikuwa na hadithi tele za watu wasio na hatia waliokufa mikononi mwa polisi. Moja ya hadithi hizo ikiwa ya shoga yake ambaye walipata kuishi nyumba moja,





akatoweka, hadi siku tatu baadaye picha yake ilipotolewa katika vyombo vya habari kama mmoja wa majambazi sugu yaliyouawa katika mapambano na polisi.

Hayo ndiyo yaliyofanya azidiwe na hofu. Alipomtazama ‘mume’ wake alimwona yeye pia haelewi la kufanya. Hivyo, akaendelea kulia huku akiupiga mlango kwa nguvu zake zote.



***

‘Mona Lisa’ katika chumba kingine, pia alikuwa akiutazama mlango katika hali ya kukata tama. Kama angekuwa na machozi katika macho yake angeweza kuangua kilio cha kwikwi. Kwa bahati mbaya, hakuwa nayo. Yalikauka kitambo kutokana na purukushani ngumu na dhoruba tele katika maisha yake.

Kama binadamu wengine, hakuumbwa kwa chuma wala mfupa. Alitumia damu mwilini na ubongo kichwani mwake. Kama binadamu wengine, mwili wake ulijua kuchoka na ubongo wake ulihitaji mapumziko.

Kwa takribani siku tatu sasa si mwili wala akili yake iliyopata fursa ya mapumziko hayo. Muda wote alikuwa mashakani, akikimbiza mtu huku yeye pia akikimbizwa, akijua kuwa anamkimbiza mtu hatari; akijua vilevile kuwa anakimbizwa na watu hatari. Kila dakika ilimkuta macho kimwili na kiakili, kuisaka roho ya mtu huku akiilinda roho yake mwenyewe.

Aliitaka roho ya Joram Kiango. Aliitaka kwa bei yoyote ile. Na angeweza kumuua kitambo kirefu. Safari yao toka Uwanja wa Ndege hadi hapa ilikuwa fursa nzuri sana kwake kuitimiza azma yake. Hata hivyo, jambo moja tu lilimfanya ashindwe kufanya hivyo; mashaka. Alitaka uhakika, kupitia katika sauti na macho ya Joram Kiango mwenyewe kama kweli ndiye aliyemuua au la. Toka alipopata taarifa kuwa nani aliyemuua, haikumwingia akilini kuwa angeweza kuwa Joram.

Joram, ambaye waliburudika naye usiku kucha! Joram, ambaye alikuwa mwanamume wake wa kwanza kumtia kichaa cha mapenzi hata kwa mara ya kwanza vilevile akafikiria kuolewa! Joram, aliyekuwa mcheshi na mchangamfu sirini na hadharani! Joram, ambaye nuru katika macho yake ilikuwa ikimshawishi kutapika uwozo wote uliofurika katika moyo wake





na kumlazimisha kumfuata popote ambapo angemwelekeza!

Haikumwingia akilini.

Na ni mashaka hayo yaliyomfanya Joram Kiango awe hai hadi sasa.

Ama hilo, ama uchovu wa mwili na akili, ama yote kwa pamoja, kwani alipokabidhiwa chumba na kuliona beseni la maji likimeremeta kwa usafi juu ya marumaru iliyofurika kila pembe ya ukuta na sakafu, chumba cha pili kitanda kipana kikimwalika kwa shuka safi zilizotandikwa vizuri; zile tani elfu moja na moja za uchovu alizoziacha kando zikamrejea. Kuoga alitamani, kulala alitamani. Zaidi ya yote njaa, ambayo kwa muda wote huo hakupata kuisikia, ilianza kumkereketa.

Ni wakati akiwa bado ameduwaa katikati ya chumba hicho, hajui aanze lipi, aishie lipi, aliposikia mlio wa risasi toka nje.

Mara hii! Aliwaza akiuendea mlango na kubaini kuwa ulikuwa umefungwa. Alijaribu moja ya funguo zake bandia. Hakufanikiwa. Akakumbuka kumwona Joram Kiango akitia mfukoni mwake rimoti ndogo mara baada ya kumfungulia. Hakujisumbua kupigana na mlango huo kama yule msichana wa Kidigo. Badala yake aliyatuma macho yake huku na huko kuangalia uwezekano wa kuweza kutoroka chumbani humo. Hakuiona namna zaidi ya kupitia mlangoni. Dirisha lilikuwa na nondo na vioo. Na hata bila hivyo kupitia dirishani kichwa chake kingekuwa halali ya risasi za hao wanaosubiri nje.

Onyo la kwanza lilitolewa wakati bado ametulia mbele ya

mlango huo akifikiri kwa nguvu zake zote.

“Joram Kiango… Tunajua uko ndani…” maneno ya Kambambaya yalimfikia vizuri chumbani humo. Joram Kiango! Sio Mona Lisa! Alijiuliza, hali iliyopelekea aamini kuwa polisi pia bado walikuwa gizani. Kwa kila hali aliamini kuwa si polisi tu, bali umati mzima ambao ulikuwa ukiiwinda roho yake kwa udi na uvumba ungenufaika mara elfu moja na moja kwa kumpata yeye badala ya Joram Kiango.

Halafu, umeme ukakatika.

Ghafla, ukawaka tena.

Hakuwa mwoga wa kifo, hasa kwa kuzingatia ukweli kuwa kifo ni ada ya kila binadamu. Lakini hakuwa tayari kufa kabla ya kupata majibu ya mashaka yake. Hakuwa tayari kabla ya





kutekeleza jukumu lake la pili, ambalo lilihusiana na kutimiza wajibu wake kwa taifa lake, dunia yake na muumba wake.

Ni baada ya hapo tu ndipo angekuwa radhi kuwaachia roho yake. Si kabla!
 
Story matata sana. Umetisha sana kaka. Usitusahau weekend kutupia madini mengine. Again, thanks brother. Hiki kitabu sikuwa kisoma.
 
Back
Top Bottom