45.
W 8 X
LE wimbo uliozoeleka, wa “Hali ngumu ya uchumi,’ ambao uliimbwa zaidi na viongozi wa serikali na chama tawala kuanzia miaka ya themanini uliambatana na vikolombwezo lukuki. Miongoni mwa vikolombwezo hivyo ni kutoweka kwa uhuru wa kujitawala kichumi na badala yake kina IMF na Benki ya Dunia kushika hatamu. Na walizishika kwelikweli. Walimimina amri baada ya amri, zote zikielekeza serikali kujitoa katika huduma nyingi za jamii. Elimu, ambayo awali ilitolewa bure, ikawa ya kulipia, na hivyo, kufanya watu wengi washindwe kuimudu, huduma za afya kadhalika zikawa hazishikiki, mashirika ya UMMA yakauawa moja baada ya jingine huku maelfu ya waliokuwa watumishi wake wakitupwa nje ya soko la ajira. Kitu kinachoitwa ruzuku toka serikalini
kikafanywa nuksi.
Viongozi wengi, wakitembelea magari ya gharama kubwa na kuishi katika majumba ya fahari, walipokea kwa furaha kila amri toka juu. Walifumbia macho ukweli kuwa huko zinakotoka amri si wakulima tu bali hata ng’ombe wao walikuwa wakilipwa ruzuku. Aidha, waliziba masikio ukweli kuwa kila raia asiye na kazi, tangu mtoto mchanga, alikuwa akilipwa posho hadi anapopata ajira, na kwamba mwananchi kupata ajira lilikuwa jukumu la serikali pia, si raia pekee.
Hivyo, katika hali hiyo hakuna aliyeona kama ni jambo la
ajabu pale wizara inayohusika na masuala ya ardhi, kama wizara nyinginezo, ilipojisahau kwa miaka kadhaa na kulifanya suala la mipango miji kama mojawapo ya anasa. Upimaji wa maeneo mapya ulisimama, uendelezaji wa miundombinu ukasahauliwa. Wakubwa walikuwa ‘busy’ kugombea ubunge, wakubwa kidogo wakihangaikia semina na warsha mbalimbali huku wale wenzangu na mie wakiikimbiza shilingi, ambayo ilionekana kama imeota matairi.
Lakini maisha yalikuwa yakiendelea. Watu waliendelea kufa, watu waliendelea kuzaliwa. Jiji la Dar es Salaam lilizidi kuwa dogo, hivyo likaendelea kupanuka. Wajanja wachache waliwasukuma wenyeji toka katika maeneo yao asilia ya Kigamboni, Tabata, Tegeta, Bunju na kwingineko na kujenga mahekalu yao. Wenzangu na mie walivamia vichochoro, mifereji ya maji machafu na mabonde yote yaliyolizunguka jiji la Dar es Salaam na kuweka vibanda vyao. Mradi wawe karibu na Dar es Salaam. Karibu na neema.
Ni katika hali hiyo, pale Bunju, eneo moja la ekari tano lilipopata mwenyewe. Likalimwa, likapandwa miti na matunda na kuzungushiwa seng’enge. Katikati ya shamba hilo jengo dogo, la ghorofa mbili, likaibuka. Hakuna aliyelishangaa wala kulitilia maanani kwani majengo hayo yalikuwa yakiibuka kama uyoga kila upande wa jiji bila mpangilio.
Hali kadhalika, hakuna aliyeshangaa jengo lilipokamilika na mzee mmoja wa Kimamkonde alipokabidhiwa kulilinda, mwezi, miezi, mwaka na, hatimaye, miaka bila ya wenyewe kuhamia. Hilo pia halikuwa la ajabu kwani majengo ya aina hiyo yalikuwa mengi katika miji mipya ya kandokando ya jiji la Dar es Salaam. Baadhi ya majengo ya aina hiyo yaliwahi kukaa zaidi ya miaka kumi kwani mwenye nyumba alikuwa nazo nyingine pengine tatu au nne, watoto na wajukuu zake wakiishi Ulaya au Marekani huku ndugu wengine wakiwa wamesahauliwa vijijini.
Lakini jengo hili lilikuwa na muujiza mmoja. Mlinzi wa Kimakonde hakupata kumfahamu mwajiri wake kwa sura wala jina. Si kwamba hakuwahi kumwona au kutajiwa jina lake, la hasha. Alimwona zaidi ya mara tatu. Lakini kila alipomwona mwajiri huyu alikuwa na sura au umbile tofauti.
Hata mavazi yake pia hayakumsaidia sana. Kila safari alikuja na vazi tofauti na awali; mara joho la ki-Naijeria, mara suti ya Kiingereza, mara jeans za wachunga ng’ombe wa Texas; na kadhalika.
Mara zote hizo alitajiwa jina. Lakini lilikuwa gumu, la lugha iliyofanana sana na Kihabeshi au Kifaransa. Mmakonde hakulishika na asingeweza kulishika. Laiti angejua kuwa hakukusudiwa kulishika..
Kazi yake haikuwa ngumu, kutunza mazingira ya nyumba kwa kufyeka majani yanapozidi, kumwagilia maua na kutunza nyumba. Mshahara ulikuwa mnono. Wakati walinzi wengine waliambulia shilingi 15,000 kila mwezi, yeye alipokea 50,000 huku akiletewa chakula kingi ambacho kilimshinda.
Mzee wa Kimakonde alinenepa, akanawiri. Mashavu yake yaliyoanza kuingia ndani kwa lishe duni na upungufu wa meno mdomoni yalianza kujaa tena, sura yake ikirudia ujana. Tahamaki miaka yake sitini na minane ya umri ilishuka na kuwa arobaini na minane machoni mwa watu wengine, hali iliyomwezesha ajikute akiishi na msichana wa Kidigo, mwenye umri wa miaka ishirini, kama mama watoto wake.
Mafanikio na uhuru huo wa muda mrefu ulimfanya aanze kujisahau kuwa yeye ni mlinzi tu wa nyumba hiyo, badala yake akajiona kama mwenye nyumba. Hata aliwaambia hivyo rafiki zake wasiomjua vizuri, kwamba mwanawe anayeishi Japan ndiye aliyemjengea nyumba hiyo. Alianza hata kuota ndoto zinazoashiria mawazo hayo. Ndoto ambazo zilimwonyesha kuwa siku za karibuni mwanawe huyo angemletea gari la kutembelea na kumfungulia mradi wa bwawa la kuogelea.
Njozi zake hizo za usiku na mchana zilikoma ghafla, usiku wa saa tatu kasoro, pale kengele za geti zilipolia. Alipokwenda kufungua mwajiri wake aliingia na gari taratibu katika banda la kuhifadhia magari. Alikuwa katika mavazi ya ajabu zaidi machoni mwa Mmakonde. Na alifuatana na mwanamke! Mwanamke mzuri! Lakini kilichomvutia zaidi Mmakonde si mwanamke bali kile alichokiona katika mavazi ya tajiri wake wakati akishuka toka ndani ya gari.
Damu!
Nguo zake zilikuwa zimeloa damu!
Mmakonde huyo alipata mshituko mkubwa zaidi pale alipomwona tajiri wake akimvuta mgeni wake huyo ambaye alifungwa pingu za mikononi. Yeye pia alikuwa na michubuko usoni na mikononi.
“Funguo, tafadhali,” aliomba huku akijaribu kumtoa wasiwasi mlinzi huyo kwa kumzawadia tabasamu jepesi.
“Funguo zipi?”
“Za geti. Sitaki mtu yeyote aingie wala kutoka humu ndani leo. Sawa?”
“Sawa… bo… bosi,” alijibu akitoa funguo hizo na kumkabidhi.
***
Kama ilivyo katika mambo yake mengine, Joram Kiango aliijenga nyumba hii kwa siri kubwa. Akiwa amejenga katika shamba alilonunua kwa mzee wa Kizaramo aliyeamua kurudi Bagamoyo, Joram hakuhitaji kutumia jina lake halisi. Na hata maombi yake ya hatimiliki ya eneo hilo pale Wizara ya Ardhi yalikuwa katika moja ya majina yake ya akiba. Mafundi aliowatumia aliwatoa nje ya nchi na hakuonana nao mara kwa mara isipokuwa tu pale ilipobidi. Wao pia walimjua kwa majina tofauti na walikuwa wakibadilishwa kila hatua, kiasi kwamba hakukuwa na fundi yeyote mwenye ramani halisi ya jengo hilo.
Kazi nyingine, nyeti zaidi, Joram Kiango alizifanya kwa mkono wake mwenyewe, usiku na mchana, akitumia vitendea kazi ambavyo ama alinunua ama alikodisha kwa hila vilevile. Alifunga umeme kwa njia na namna zake, aliunganisha maji na mashine za kupozea hewa kwa mitindo yake na kuweka milango na madirisha kwa namna ya kukidhi mahitaji yake. Alikuwa na vyumba vya siri na milango ya siri ambayo mtu yeyote asingebaini bila matakwa yake.
Ilipokamilika ilikuwa nyumba ya pekee, ingawa wapita njia waliichukulia kama mojawapo ya nyumba za kawaida. Kumwajiri mzee yule wa Kimakonde ili ailinde, badala ya kuitumia moja ya kampuni lukuki za ulinzi zilizopo jijini, kwa Joram ilikuwa sehemu ya kuendeleza usiri wa jengo lake hilo. Mzee hakuwa mdadisi, wala hakuwa makini. Mara nyingi
sana Joram amekuja nyumbani hapo na kufanya shughuli zake huku mzee akiwa hana habari. Mara mbili aliwahi kulala usiku mzima na kuondoka zake alfajiri huku mlinzi wake akikoroma.
Hivyo, kadhia hili zito, ambalo liliambatana na vifo na maafa ya kila dakika, lilimfanya Joram Kiango alazimike kuja hapa. Hakuona wapi pengine panafaa kumweka kitako msichana huyo wa ajabu anayejiita Mona Lisa na aliyefanana naye reale kwa ya pili, msichana ambaye hashikiki, hatabiriki.
Haikuwa kazi rahisi kumfikisha hapo. Mara mbili walinusurika kifo kufuatia vurumai ambayo aliianzisha ghafla mara walipokaribia Barabara ya Bagamoyo. kwa bahati, joram alikuwa tayari. Ule utulivu na ukimya wa muda mrefu aliokuwa nao toka Uwanja wa Ndege haukumpumbaza Joram. Alikuwa makini, jicho lake la wizi likiwa halijamwacha hata kwa dakika moja. Hivyo, pale Joram alipomwona akifumbua macho kwa hila na kisha kuyafumba, huku mkono wake mmoja ukipelekwa taratibu katika mfuko wake wenye bastola, Joram alimsubiri. Mara tu alipoipata bastola hiyo Joram alimpokonya, kitendo ambacho kilifuatiwa na pigo kali la kareti toka kwa msichana huyo. Pigo hilo lilimpata Joram Kiango barabara shingoni, likalifanya gari liyumbe, nusura kupinduka. Kwa bahati, Joram aliwahi kulizima gari huku akizuia pigo la pili na kuachia lake lililompata shingoni na kumlegeza msichana huyo. Joram aliitumia fursa hiyo kumkamata na kumtia pingu za mikono. Alishangaa kuona Mona Lisa huyo akiruhusu kufungwa pingu kwa utulivu kabisa, kinyume na matarajio yake.
“Uko tayari kuzungumza?” Joram alimhoji msichana huyo.
Hakujibu. Badala yake alifumba macho yake na kukilaza kichwa chake kwenye kiti.
Jaribio la pili alilifanya wakati gari likikaribia kuvuka daraja linaloitenga Tegeta na Bunju. Kwa kuitumia mikono yake yenye pingu, aliuvamia usukani na kuupinda akilielekeza gari kutumbukia mtoni. Joram alitumia nguvu za ziada kulirejesha barabarani. Lakini haikuwa kabla ya gari hilo kugonga ukuta wa daraja na kubonyea vibaya upande wa kushoto. Kwa bahati, magari yalikuwa yamepungua sana njiani. Vinginevyo,
hadithi ingekuwa nyingine.
‘Mona Lisa’ alitulia tena. Hakufanya vurugu ya aina yoyote tangu gari lilipoondoka eneo hilo, likaiacha Barabara ya Bagamoyo na kufuata njia ndogo iliyowafikisha yalipo makazi ya Joram Kiango. Wala hakuwa mbishi wakati geti lilipofunguliwa naye kuongozwa hadi ndani ya jumba.
“Tunahitaji kuzungumza,” Joram alimwambia mara walipofika ndani. “Bila shaka mazungumzo yetu hayatakuwa mafupi. Hivyo,” aliongeza, “Nadhani unahitaji kuoga. Umechakaa sana.” Alimwelekeza kwenye kimojawapo cha vyumba vya wageni na kumfungulia akimwambia, “Humo kuna bafu, sabuni na dawa za meno. Nadhani utapata hata nguo za kubadili. Tumia muda wako, usiku bado mbichi huu.” Joram alitoa funguo za pingu na kumfungua mikono.
“Usijisumbue kufikiria kutoroka,” alimwambia. “Ni rahisi sana kuingia katika nyumba hii, sio kutoka,” alisema akivuta mlango wa chumba na kuufunga kwa rimoti.
Yeye pia alihitaji kuoga. Alikuwa mchovu na mwenye njaa. Hali kadhalika, hakuwa amechafuka tu, bali kuchakaa. Mchanganyiko wa damu, jasho na vumbi mwilini mwake ulimfanya ajisikie kunuka. Alitamani sana aingie katika beseni lake la kuogea, ajilaze katika maji ya baridi na kukaa humo kwa saa moja au zaidi.
Lakini hakuwa na muda huo. Alikuwa na mengi ya kufanya. Awali ya yote, alihitaji kukaa mbele ya kompyuta yake. Alihitaji majibu ya maswali aliyoyasambaza kwa rafiki zake kupitia mtandao wa E-mail. Hivyo, alikiendea chumba chake cha kujisomea na kuiwasha kompyuta yake ndogo, lap top aina ya Mackintosh toka katika kiwanda cha yule kijana tajiri kuliko watu wote duniani, Bill Gate. Pia, akafungua mtandao wake wa huduma ya bure, hotmail, na kuita moja ya anuani zake zenye majina bandia.
Alikuwa hata hajatulia vizuri wakati mlio wa risasi za SMG
uliposikika ghafla toka mbele ya geti lake.
***
Othman Mchopanga alikuwa amemfuata Joram Kiango hadi nyumbani kwake kwa urahisi kuliko alivyotegemea. Kuna
wakati aliwatangulia na kuruhusu magari kadhaa kati yao, mara moja walimpita kasi na kuendelea na safari yao. Kwa mbali alizishuhudia zile purukushani za yule msichana na Joram Kiango pale darajani. Angeweza kuwaua kwa urahisi sana na kulilipua gari lao kwa tenki la gari lao lakini alisita kufanya hivyo. Alitaka kazi yake iwe nzuri, ya kujivunia, si kubahatisha.
Faida moja ya kuishi katika dunia ya kile marafiki zake wanachokiita ‘dunia ya mafichoni’ ni kujua mambo mengi ya watu wengine hali yako hayajulikani, mfano mzuri ukiwa safari hii ya kumfuatilia Joram Kiango. Hakuwa na papara ya kufanya lolote kwa kuwa alijua wanaelekea wapi. Alipata fununu muda mrefu kuwa jengo lile lilikuwa la Joram Kiango. Hakupata kufikiria kuwa fununu hizo zingekuwa na manufaa yoyote kwake hadi leo, wakati akiwafuata kwa kazi moja tu.
Wakati huohuo alikuwa na hakika kabisa kuwa hakuna mtu yeyote aliyejua kuwa mbili kati ya zile boti ziendazo kasi kati ya Dar es Salaam na Zanzibar ni zake. Hali kadhalika, kama wapo waliofahamu ni wachache sana, kuwa hoteli nne za kitalii jijini Dar es Salaam, Arusha na Zanzibar ni zake. Walichofahamu majirani zake kule Makongo Juu ni kuwa yeye alikuwa mfanyabiashara wa jumla wa vipodozi toka Dubai na Falme za Kiarabu. Aidha, walimtambua kama mtu mpole, mkarimu na muumini mzuri wa dini ambaye alikosa sala kwa nadra sana.
Mtu ambaye hakumtambua zaidi ya watu wote ni mkewe. Binti Kalenga, mtoto wa Kifipa aliyezaliwa na kukulia Dar es Salaam aliolewa angali kinda, mara baada ya kushindwa kuendelea na elimu ya sekondari. Baba yake, mzee Kalenga, akiwa amezibwa macho kwa kitita cha fedha za kishika uchumba, mama yake akiwa amelogwa kwa zawadi za mavazi na hereni za dhahabu kutoka Dubai, binti yao angepata lipi la kusema? Yeye pia, mara baada ya kuingia katika ‘hekalu’ la mume wake na kukabidhiwa umalkia wa kila kitu katika nyumba hiyo moyo wake haukuwa na nafasi ya kumchunguza mume wake. Na pale alipopewa usimamizi kamili wa bidhaa zote toka nje, huku mara mojamoja wakisafiri pamoja kwenda nje, alijikuta akiondokea si kumwamini tu bali kumwabudu