Muda wa kumuonesha trafiki leseni ni mpaka siku tatu kama umesimamishwa na huna

Muda wa kumuonesha trafiki leseni ni mpaka siku tatu kama umesimamishwa na huna

Bashir Yakub

Member
Joined
May 27, 2013
Posts
96
Reaction score
1,745
=========
ILANI: Makala hii hailengi wale wasio na leseni kabisa. Aidha, unashauriwa kupiga picha leseni yako ili angalau uwe na kumbukumbu ya namba ya leseni
=========​

Kusimamishwa na trafiki barabarani, na ukawa huna leseni mfukoni kwa muda huo sio kosa. Mwambie huyo trafiki kuwa hilo sio kosa. Sheria inatutaka kutembea na leseni tunapoendesha vyombo vya moto, lakini pia haisemi kuwa utakapokuwa hauna pale unapoombwa na trafiki basi ni kosa.

Tunaongelea Sheria ya Usalama Barabarani, Sura ya 168. Wapo watu wameandikiwa faini kisa wameombwa leseni wakasema hawana, au wakasema wamezisahau majumbani. Hawa waliotozwa faini katika mazingira kama haya wameonewa. Na wanastahili kurudishiwa fedha walizotoa haraka.

Ni kweli kifungu cha 77 cha Sheria ya Usalama Barabarani kinamtaka kila mwendesha chombo cha moto kutembea na leseni barabarani. Ni kweli askari anayo mamlaka kumsimamisha mwendesha chombo cha moto. Na ni kweli pia kuwa askari anayo mamlaka ya kumtaka mwendesha chombo cha moto aoneshe leseni yake. Lakini sio kweli hata kidogo kuwa mwendesha chombo cha moto asipoonesha leseni kwa wakati huo basi tayari ametenda kosa. Sio kweli.

Kifungu cha 77(1) cha Sheria ya Usalama Barabarani kinasema kuwa mtu hatatiwa hatiani, kwa maana ya kulipa faini au kuandikiwa kosa au kuadhibiwa na chombo chochote ikiwamo mahakama, kwasababu tu hakubeba, au hakutoa/kuonesha leseni pale alipotakiwa kufanya hivyo, isipokuwa ana siku tatu za kutoa au kuonesha leseni hiyo tokea siku hiyo aliposimamishwa.

Tafsiri iko wazi kuwa unaposimamishwa, ukaombwa kuonesha leseni, ukawa huna kwa mda huo, unazo siku tatu mbele za kutakiwa kuleta na kuonesha. Anachotakiwa kufanya askari sio kukuandikia kosa, laa hasha, bali ni kukutaka umuoneshe leseni hiyo ndani ya siku tatu tokea siku hiyo. Ukishindwa kufanya hivyo ndani ya siku hizo hapo ndipo linaweza kuwa kosa.

Watu wasionewe. Wapo askari wengine pia hawajui hizi sheria. Hawa sisi madereva tuwaelimishe. Unaweza kudhani askari anakuonea kumbe naye hajui. Kwahiyo kazi unayo wewe kuhakikisha unamweleza huyo askari kuhusu kifungu hiki na namna kinavyotaka. Wewe ndiye mtetezi wa kwanza wa haki yako kabla ya kutetewa na mtu mwingine.

Na kama itatokea ukaandikiwa adhabu kwa lazima kwa kitu kama hiki, basi unayo haki ya kukataa kulipa na kuomba kufikishwa mahakamani ili sheria ikatafsiriwe. Mwambie “Sitalipa nataka sheria ikatafsiriwe mahakamani”.

Kukataa kulipa sio kosa au ukorofi na hivyo huna haja ya kukhofu. Kukataa kulipa ni haki katika haki ulizonazo ukihisi umeonewa. Na kama umeshalipa au ulilipa huko nyuma katika mazingira ya jambo kama hili na unao ushahidi basi unayo haki ya kudai hela uliyolipa. Unaweza kuidai huko ulikotozwa au mahakamani.

Sheria imetoa ahueni hii ikizingatia mazingira ya ubinadamu. Huwezi kila unapoamka asubuhi ukakumbuka leseni. Huwezi kila unapokuwa na safari ukakumbuka leseni. Safari nyingine ni za ghafla na za kushtua, mfano kuitiwa msiba, ugonjwa, matatizo kazini, bila kusahau msongo/stress za ada na kodi. Atapata wapi muda wa kukumbuka leseni mtu huyu?

Mwingine amebadilisha nguo na hivyo leseni kubaki kwenye nguo iliyovuliwa, mwingine amebadilisha gari na hivyo leseni kubaki kwenye gari jingine. Na mazingira mengine kama hayo. Zote hizi ni dharula za kibinadamu zilizowafanya watunga sheria kuweka muda wa siku tatu kwa ajili ya kutoa au kuonesha leseni.

Basi wote tubadilike, madereva na askari wasimamia usalama barabarani. Dereva asiwe mkorofi, kadhalika askari asimwonee dereva
 
Hizo sheria ni za kitabuni. Hapa Bongo polisi he is alyways right.

Halafu mahakama zetu ni analogue hazina muda wa kusikiliza kesi kwa haraka. Huna leseni ni faini. Iwe ni robo saa, siku nzima au mwaka.

Hapa nchini polisi ndio wanatafsiri sheria, ukienda mahakamani utatoa rushwa uliyokwepa kuitoa barabarani.

Tunashukuru kwa kutuonyesha sheria inasemaje, ila ujue kuna sheria na uhalisia.
 
Back
Top Bottom