Zanzibar kuwa nchi
na Hassan Shaaban, Zanzibar
SERIKALI ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ) inafanya marekebisho ya katiba ya mwaka 1984, ambayo yanaipa Zanzibar hadhi kamili kama nchi ndani ya Jamhuri ya Muungano.
Marekebisho hayo ya katiba yanatarajiwa kuwasilishwa katika kikao cha Baraza la Wawakilishi kinachoanza leo Zanzibar, ambapo pia yataruhusu kuundwa kwa serikali ya umoja wa kitaifa baada ya uchaguzi wa Oktoba mwaka huu.
Kwa mujibu wa rasimu ya marekebisho ya katiba hiyo, sura ya kwanza ibara ya kwanza iliyokuwa ikisomeka, Zanzibar ni sehemu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imefutwa chini ya marekebisho hayo.
Rasimu hiyo ambayo itawasilishwa na Mwanasheria Mkuu, Idd Pandu Hassan, inapendekeza kifungu hicho sasa kisomeke ‘Zanzibar ni nchi ambayo eneo la mipaka yake ni eneo lote la visiwa vya Unguja na Pemba pamoja na visiwa vidogo vilivyoizunguuka na bahari yake, ambayo kabla ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar iliitwa Jamhuri ya watu wa Zanzibar'.
Aidha, marekebisho hayo ya katiba yamegusa kifungu cha pili na kueleza kuwa Zanzibar ni miongoni mwa nchi mbili zinazounda Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Marekebisho hayo pia yamegusa mamlaka ya rais katika kuigawa Zanzibar katika mikoa, wilaya na maeneo mengineyo kwa kufuata utaratibu uliowekwa na sheria iliyotungwa na Baraza la Wawakilishi.
Kabla ya marekebisho hayo kifungu cha pili cha Katiba ya Zanzibar kilikuwa kikisomeka ‘kwa ajili ya utekelezaji bora wa shughuli za serikali, Rais wa Jamhuri ya Muungano akishauriana na rais anaweza kuigawa Zanzibar katika mikoa, wilaya na maeneo mengineyo kwa kufuata utaratibu uliowekwa'.
Marekebisho hayo pia yamempa uwezo Rais wa Zanzibar kuteua wakuu wa mikoa bila ya kushauriana na Rais wa Jamhuri ya Muungano, kama ilivyokuwa kabla ya marekebisho hayo.
Marekebisho hayo ya 10 ya Katiba ya Zanzibar iwapo yatapitishwa na wajumbe wa Baraza la Wawakilishi yatamaliza msuguano uliokuwa umejitokeza kuhusu nafasi ya Zanzibar katika Jamhuri ya Muungano, baada ya Waziri Mkuu Mizengo Pinda, kudai kuwa "Zanzibar si nchi".
Hata hivyo, baadaye Rais Jakaya Kikwete akitoa ufafanuzi wa suala hilo alisema Zanzibar ni nchi ndani ya Jamhuri ya Muungano, lakini "Zanzibar si nchi nje ya Jamhuri ya Muungano kama ilivyo kwa Tanganyika. "
Aidha, marekebisho hayo ya katiba yanampa uwezo Rais wa Zanzibar kuteua makamu wawili wa rais, akiwamo makamu wa kwanza ambaye atateuliwa baada ya rais kushauriana na chama kilichoshika nafasi ya pili katika kura za rais kwenye Uchaguzi Mkuu.
Rais pia atamteua makamu wa pili wa rais ambaye atakuwa ndiye mtendaji mkuu wa shughuli za serikali ndani ya Baraza la Wawakilishi
Wakati wajumbe wa Baraza la Mawaziri watateuliwa kwa uwiano wa viti vya wajumbe ndani ya Baraza la Wawakilishi.
Pia mswada huo unafuta wadhifa wa Katibu Mkuu Baraza la Mapinduzi na kuweka Katibu Mkuu Kiongozi, ambapo pia kutakuwa na makatibu wakuu wa ofisi ya makamu wa kwanza wa rais na katibu mkuu ofisi ya makamu wa pili wa rais.
Source: Tanzania Daima