BINAFSI sitamsamehe Neymar. Katika umri wa miaka 25, nyakati unazotamani kuona akielekea juu kabisa ya kilele cha ubora duniani, anachagua kuondoka Barcelona na kwenda PSG.
Kwa mchezaji wa aina yake mwenye uwezo kama wake, unatokaje kirahisi katika ligi bora duniani na kuchagua kucheza Ligue 1, ligi namba 5 kwa ubora barani Ulaya?
Tatizo ni nini? Pesa au ni kweli amechoshwa kuwa nyuma ya kivuli cha Lionel Messi? Labda sababu ya kwanza, vijana wa Amerika Kusini mioyo yao haijapishana sana na Waafrika.
Dhiki kali walizokumbana nazo utotoni zilishaichoma mioyo yao na kuiacha ikiwa na hasira kali ya kimaisha. Ilipo pesa, walipo wao.
Hapa kwenye kukimbia kivuli cha Leo Messi, ndiko kunakonipa shaka kidogo. Hapa Neymar anatudanganya, tena uongo mbaya wenye kukera.
Sikatai, kivuli cha Messi kimemficha sana. Ubora wake hauzungumzwi tena. Neymar yule tuliyemsikia akiwa Santos, si huyu wa sasa tuliyenaye hapa Nou Camp.
Chochote atakachofanya kimeshafanya na Messi tayari. Barca wana mfalme mmoja tu, La Pulga pekee. Kwa alipofika Neymar alitakiwa kuondoka Barca.
Lakini kama kweli sababu ni kusaka ufalme wa soka duniani, Neymar alitakiwa kujiuliza mara mbili, ni wapi anaweza kwenda na kutengeneza ufalme wa dunia?
Unakimbiaje kivuli cha Messi kwa kwenda PSG? Dunia ya sasa inaanza vipi kutoa mfalme wa soka katika ligi dhaifu kama ile ya Ligue 1?
Mtazame Zlatan Ibrahimov. Ni mfalme wa PSG. Ni mfalme wa Paris, ni gwiji wa Ligue 1, lakini yuko mbali na hadhi ya wafalme wa dunia. Neymar analijua hili?
Kwa miaka 10 sasa Ligue 1 imeendelea kuwa ligi kubwa ya kawaida duniani. Haisisimui kabisa. Wachezaji bora hudumu kwa msimu kadhaa kisha huamua kusaka malisho sehemu nyingine.
Eden Hazard amepata heshima aliyonayo baada ya kucheza Premier League. N’golo Kante pia. Hivyo hivyo kwa Riyad Mahrez na Didier Drogba.
Mtazame tena Kylian Mbappe? Pamoja na ubora wake, dunia imekuwa na mashaka naye bado. Wengi hawaamini kama ni mkali kama takwimu zinavyosema. Kwanini? Ni takwimu za Ligue 1.
Watu hawaiamini sana ligi ile, ni ngumu sana kuona akiibuka mfalme wa dunia maeneo yale. Neymar asiendelee kutudanganya. Kivuli cha Messi hakiwezi kufutwa kwa nyota anayevaa jezi ya PSG. Ni uongo huu.
Kama kweli Cristiano Ronaldo alimshauri kufikiria mara mbili kabla hajatoka Barcelona, basi CR7 ni mkubwa sana kifikra katika dunia ya soka ya sasa. Tusishangae anavyozidi kufanikiwa.
Ni klabu mbili tu ambazo Neymar angeweza kwenda na kuupata ufalme anaoutaka. Real Madrid na Manchester United. Lakini tayari Madrid wanaye Ronaldo, chaguo sahihi kwake lilikuwa Old Trafford.
Neymar angeweza kusimama na kugombea ufalme wa dunia akiwa na jezi ya Manchester. Pale ndipo mahala anakoweza kushindana na kina Leo Messi na Ronaldo, si PSG.
Ukweli mchungu unaofichwa na Neymar na baba yake ni huu, kinachowakimbiza Barcelona ni pesa tu. Hizi stori za Ufalme ni uongo tu.
Neymar hana shida na mataji tena, hana shida na tuzo ya Ballon d’Or. Shida yake ni pesa tu. Na kwa PSG amekutana na wendawazimu wa biashara, watampatia.
Tayari kuna ofa ya mshahara wa pauni 500,000 kwa wiki. Atapimwa afya katika hospitali ya kifahari kule Qatar, kisha atatambulishwa pale uliposimama mnara wa Paris maarufu kama mnasa wa Eiffel. Maisha yanataka nini tena zaidi?
PSG wanamhitaji Neymar kibiashara. Hawana shida ya miguu yake, wana shida na sura yake. Neymar ndiye mtu pekee duniani atakayeweza kukaa kwenye matangazo ya ndege zao na wakafanya biashara kubwa.
Sent using
Jamii Forums mobile app