Huu ndio msumari kwa Lowassa
Ibara ya 52 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya Mwaka 1977 inatamka wazi kuwa Waziri Mkuu ndiye mwenye madaraka ya juu ya udhibiti, usimamiaji, utekelezaji wa siku hadi siku wa kazi na shughuli za Serikali ya Jamhuri ya Muungano na ndiye Kiongozi wa shughuli za Serikali Bungeni. Kamati Teule haikufurahishwa hata kidogo na taarifa hizo zinazomgusa moja kwa moja Mhe. Waziri Mkuu katika kuipendelea Richmond Development Company LLC. Hata hivyo Kamati Teule imetimiza wajibu wake kwa uwazi na ukweli kama ilivyoagizwa na Bunge letu Tukufu. Kwa kuzingatia umuhimu wa nafasi aliyonayo Mhe. Waziri Mkuu katika uendeshaji wa shughuli za Serikali na uongozi wa nchi kwa ujumla, ni wajibu wake yeye mwenyewe kupima uzito wa matokeo ya uchunguzi huu na wajibu wake kikatiba ndani na nje ya Bunge. Vile vile ni wajibu wa Bunge ambalo linathibitisha uteuzi wake kwa mujibu wa Ibara ya 51 inayothibitisha uteuzi wake. Kuangalia ikiwa matokeo ya uchunguzi huu hayajaathiri hadhi na uzito wake ndani ya Bunge.