Riwaya: Kasri ya Mwinyi Fuad

Riwaya: Kasri ya Mwinyi Fuad

Abdallahking

JF-Expert Member
Joined
Mar 19, 2018
Posts
3,985
Reaction score
10,840
RIWAYA: KASRI YA MWINYI FUAD
MWANDISHI: ADAM SHAFI ADAM
IMELETWA KWENU NA
: BURE SERIES

SEHEMU YA 1

KIJAKAZI alizaliwa kutokana na ukoo wa kitumwa. Baba yake na mama yake walikuwa ni miongoni mwa watumwa watiifu sana wa Bwana Malik na kama wao, Kijakazi alinuia kuwa mtumishi wake mtiifu kabisa.

Wazee wa Kijakazi walifariki alipokuwa bado mdogo. Katika kukua kwake aliamini kuwa kule kuzaliwa kwake mtumishi ndiyo majaaliwa yake. Shabaha kubwa ya Kijakazi katika maisha yake ilikuwa ni kumfurahisha bwana wake, na kwa hiyo, alikuwa tayari kumfanyia kazi yoyote ile.

Mkewe Bwana Malik, kama alivyo yeye mwenyewe, alipenda sana kumtuma Kijakazi. Kazi za Kijakazi zilikuwa za nendarudi, mara afanye hili mara afanye lile, mara aende huko mara aende kule, mara achukue hiki mara achukue kile, kutwa kucha. Mara nyingi baada ya kuifanya kazi hurejeshwa kuifanya kazi hiyo hiyo mara ya pili. Kijakazi hakuwa na mapumziko hata kidogo ndani ya nyumba ya Bwana Malik.

Ghafla Bwana Malik humwita Kijakazi na kumpigia makelele. “Weel Nenda kamfunge mbuzi apate kula majani’.”

“Nishafunga mbuzi Bwana!”

“Wacha kujibu, wewe mbwal Fanya kama unavyoambiwa!”

Kabla ya kuitimiza ile amri aliyopewa mwanzo mara Bibi Maimuna, mke wa Bwana Malik, naye hutoa yake, “Kijakazi! Hebu kanitekee maji hapo kisimani nataka kuja kukoga, ma’na’ke n’najihisi n’nanuka jasho.”

“Maji nishateka, Bibi, lakini nitakwenda kuteka tena.”

“Unakwenda wapi tena? Unafikiri huko kisimani kuna maji ya kuchezea?”

Kijakazi husimama uwanjani kwa Bwana Malik, amepigwa na mshangao, hajui aende akafunge mbnzi au akateke maji, na Bwana Malik na Bibi Maimuna wakiendelea kumfokea na kumtolea maneno makali....

Hivi ndivyo yalivyokuwa maisha ya Kijakazi; kutwa yumo mbioni kutumwa na huku akisumbuliwa.

Haya yote hayakumkera Kijakazi hata kidogo, kwa sababu aliamini kuwa ndiyo majaaliwa yake. Aliamini kwamba wajibu wakc mkubwa katika maisha yake, ulikuwa kufanya anavyoweza kumfurahisha Bwana Malik na kila aliye wake. Hakupenda hata kidogo kumwona yc yote katika watu wa Bwana Malik amekasirika, na ilipokuwa hivyo, alijiona yeye ndiye chanzo na alijilaumu sana.

Jumba la Bwana Malik lilikuwa katikati ya shamba lake huko Koani, kubwa na la fahari, halina mfano wake jirani. Vyumba vyake vingi, waliovijua ni watumishi wa ndani na Bwana Malik na mkewe tu.

Kwenye ukumbi wa jumba la Bwana Malik kulikuwa na mapambo mengi ya fahari na starehe ya pekce. Kulikuwa na viti vya mpingo vya asili vilivyochongwa kwa nakshi. vyote vimetandikwa mito ya mahameli. Kuta zilikuwa zimepambwa kwa mapicha ya wafalme wa Kiarabu wa zamani, na chini ya mojawapo ya picha hizo limemng’inizwa jambia zuri la fedha. Sakafu ya ukumbi huo ilifunikwa na zulia kubwa kutoka Uajemi, na katika pembe moja liliwekwa kasba la msaji lililonakshiwa kwa misumari ya shaba.

Hapo ndipo Bibi Maimuna alipokuwa akipotezea wakati wake mwingi, akikaa na kujitandaza jua ya vile viti vizuri vilivyotandikwa mito ya mahameli, na kujipaka mafuta ya hal-ud na manukato mengine mazuri.

ADAM SHAFI ADAM = KASRI YA MWINYI FUAD.jpg
 
SEHEMU YA 2

Jumba hilo lilizungukwa na shamba zuri lililojaa mimea ya kila aina. Kutokana na rutuba ya ardhi ya sehemu hii na mvua za kutosha za kila mwaka, shamba la Bwana Malik lilikuwa daima zuri. Kama si maua ya mikarafuu na harufu yake nzuri basi yalikuwa matunda mbali mbali yakichumwa na watwana kwa bidii ili yasije haribikia shambani. Mabondeni, mpunga ulisitawi kwa wingi...na yote haya yalimletea Kijakazi furaha maalum, ijapokuwa yeye hakupata kitu cho chote katika mazao yanayopatikana shambani humo.

Mawazo mengi yatokanayo na shida zisizokwisha yaliunfisha uzuri wa sura ya Kijakazi, ukawa hauonekani. Uso wake ulikuwa umejaa mashaka; badala ya kutoa mwanga wa ari ya maisha, ulikunyaa na kuwa na mistari ya uchovu ambayo iliufanya uonekane wa mzee kuliko umri wake ulivyo. Mara moja moja, kwa nadra, hutokea jambo la kumfanya acheke na hapo uso humulika na kwa muda mdogo ule ukajaa bashasha za ujana, mashavu yake yenye vidimbwl vizuri yakajaa damu changa, vuguvugu. Lakini kawaida yake ni ile ya uchovu, ya mtu aliyechakaa, mwenye mikono iliyojaa visuguru na visigino vya miguu vilivyolika kwa kwenda. Si mvua, si jua; si usiku si mchana, kazi hazikumwisha Kijakazi.

Fuad alikuwa ni mtoto mkubwa mwenye umri wa kiasi cha miaka mitano na mtundu wa kutosha. Kutwa alikuwa anavunja vitu ndani ya nyumba na alipenda mchezo wa kuchupa huku na huku. Alikuwa anaweza kufanya jambo lo lote au kusema kitu cho chote mbele ya mtu ye yote na kwa yote haya hakuna aliyeweza kumkanya kwa kuchelea kutukanwa ama na Bwana Malik au na Bibi Maimuna. Alidekezwa kupita kiasi na kila alilolifanya yeye lilikuwa sawa kwa wazee wake. Kwa baadhi ya mambo aliyokuwa akiyafanya ilikuwa rahisi kwa mtu kuamini kwamba akili za Fuad hazikukaa sawa. Mtoto wa miaka mitano lakini hakukawia kujiliza akitaka kubebwa.

Siku moja alikuwa amechukuliwa na mama yake baada ya kulia kwa muda mrefu, akaanza kujizengeresha huku na huku, mara amvute mama yake nywele mara amvute masikio. Bibi Maimuna alipojiona taaban kwa utundu wa mwanawe, alimtupilia mbali kwa ghadhabu bila kujali litakalompata, Kwa bahati nzuri Kijakazi alikuwa akifagia ukumbini na ghafla aliinuka na kuwahi kumdaka mtoto huyo ambaye kama si yeye, labda angeanguka na ku pasuka kichwa. Alimdaka, kama vile mtu anavyodaka kitu alichoruahiwa bila kutahadharishwa. Fuad wakati huu alikuwa akilia kwa kelele kabisa, kama aliyepagawa na wazimu. Mara tu baada ya Fuad kufika mikononi mwa Kijakazi alinyamaza.

Bibi Maimuna naye kwa haraka alimgeukia Kijakazi na kumpokonya mtoto kutoka mikononi mwake kwa nguvu na papara karibu ajigonge kwenye kiti kilichokuwa karibu nao. Mara baada ya kuchukuliwa na mama yake, Fuad alianza kupiga makelele tena na Bibi Maimuna akamtupilia mbali, tena, na kwa mara ya pili Kijakazi akamdaka. Mzunguko huu wa kupokezana mtoto ulichukua muda mpaka Bibi Maimuna alipokubali Fuad abaki mikononi mwa Kijakazi.
 
SEHEMU YA 3

“Atakuwa Bwana shamba bara bara,” alisema Bibi Maimuna.

Tokea siku hiyo Kijakazi al’acha kufanya kazi katika banda la ng’ombe na kuanza kufanya kazi jikoni. Hii haikuwa hivyo ili Kijakazi awe mlezi wa Fuad; hiyo ingekuwa fursa maalum ambayo ukoo wa Bwana Malik haukuwabi kumpa ye yote katika wafanyakazi wao. Nia ilikuwa kumfanya Kijakazi awe karibu na Bibi Maimuna na mtoto wake.

Fuad alikuwa akimpenda sana Kijakazi na alipenda kila wakati kucheza naye. Hapana aliyeelewa kwa nini yule mtoto mtundu alimpenda Kijakazi na kutulia wakiwa pamoja. Hata mwenyewe Kijakazi hakuweza kuelewa kwa nini alikuwa akipendwa na Fuad. Kijakazi anapomchukua Fuad wakati anapoanza kulia basi mara Fuad hunyamaza. Hii ndiyo sababu iliyofanya Kijakazi aondolewe kufanya kazi katika banda la ng’ombe na kupewa ile kazi yake mpya iliyokuwa haijambo kidogo - kazi ya kukaa jikoni.

Kusema kweli kazi zilikuwa zimeshamchosha Kijakazi ijapokuwa kila alilolifanya alilifanya kwa furaha. Furaha hiyo ilikuwa si furaha tupu bali ilikuwa ni furaha iliyochanganyika na machovu. Aliweka matumaini yake yote juu ya mtoto huyo ijapokuwa hakujua mpaka lini mtoto huyo atamnusuru ili aendelee na kuwapo jikoni kila siku na asirejee tena kule kwenye banda la ng’ombe.

Asubuhi moja Kijakazi alikuwa jikoni anachemsha maji ya kukoga Bibi Maimuna. Mara tu baada ya Fuad kuamka alikwenda huko jikoni ambako alijua kwamba atamkuta Kijakazi. Na Bibi Maimuna baada ya kuamka alikuwa anaranda huko na buko nyumbani mwake kwa maringo. Aliposikia sauti za furaha kutoka jikoni za Kijakazi na Fuad wakicheza, Bibi Maimuna alielekea huko na kufika mlangoni akamwona Kijakazi anambusu Fuad Kichwani. Bibi Maimuna alikasirika sana. Aliingia jikoni huku ameghadhibika, uso wake unatisha, akamsukuma Kijakazi upande kwa nguvu na kumpokonya yule mtoto. Masikini Kijakazi aliyaangukia masufuria yaliyokuwa nyuma yake na upesi upesi alijizoazoa na kurejea kumtazama Bibi Maimuna kwa hofu. Moyo ulikuwa ukimwenda mbio hajui litamfika jambo gani kwa alilolifanya ijapokuwa kosa lenyewe hakulijua.

“Unafanya nini we Kijakazi na mwanangu?” Bibi Maimuna alimkaripia Kijakazi.

“N-n-nisamche Bibi!” Kijakazi alijibu huku hofu imemjaa.

“Ngoja mpaka upate mtoto wako ndipo umbusu! Ala!” Bibi Maimuna alimwambia Kijakazi akitoka nje.

“Jee! Kuna nini tena huko? Mbona nasikia makelele?” Bwana Malik naye aliuliza kutoka chumbani alikokuwa amelala.

“Si huyu mbwa huyu, ati anambusu Fuad,” alijibu Bibi Maimuna.

“Mimi nilikwambia huyu hastahili kuwekwa huko jikoni, wewe ukasema tumwache huko huko. Leo kambusu Fuad, kesho utamkuta kakaa ukumbini juu ya kiti na Fuad kama yeye ndiye mwenye nyumba!” Bwana Malik alisema kwa makelele huku akitoka huko chumbani na kuja jikoni alikokuwa Kijakazi.
 
SEHEMU YA 4


Alipofika hapo jikoni alimkuta Kijakazi amejikunja, hofu imemjaa. Alimtazama kwa jicho kali na mara alimfyonya na kutoka nje ya nyumba.

Fuad alifanya kelele nyingi alipochukuliwa kutoka kwa Kijakazi lakini hata hivyo Kijakazi hakuruhusiwa tena kumchul a Fuad. Wacha kuruhusiwa kumchukua tu bali hata kukaa karibu naye ilikuwa marufuku tangu siku hiyo.

Mambo yalikwenda kinyume na alivyotaka Kijakazi. Tegemeo lake kwamba Fuad atamnusuru asirejee tena kule bandani kububurushana na kupigwa mateke na ng’ombe lilitoweka. Sasa ilimbidi arejee kule kule bandani kwa ng’ombe alikokuwa akifanya kazi zamani.

Bibi Maimuna alifanya kila jitihada ili Fuad amsahau Kijakazi na alifanikiwa, kwani baada ya muda mfupi Fuad hakuwa tena na hamu ya kubebwa na Kijakazi. Lakini kwa Kijakazi mambo yalikuwa kinyume; siku zilivyoendelea ndivyo mapenzi yake kwa Fuad yalivyozidi.

Fuad alikuwa mtoto mkubwa sasa. Mapenzi ya Kijakazi yalizidi vile vile na kila alipomwona mtoto huyo amesimama mbele ya uwanja wa nyumba ya Bwana Malik basi alifurahi kama ameliona jua wakati linapochomoza kutoka mawinguni. Mara nyingi Fuad alikuwa akija katikati ya uwanja huku akichupachupa kama mtoto wa mbuzi. Kila alipomwona Fuad, Kijakazi aliacha kila alichokuwa akifanya na alikaa kufikiri uzuri atakaokuwa nao kijana yule atakapokuwa mtu mzima.

Fuad alikuwa na mbwa wake na alipenda sana kucheza naye huku akimpa amri ya kufanya hiki na kile. Alikuwa akiranda na kufukuzana na mbwa huyo kwenye shamba la baba yake.

“Boby!” Fuad alimwita mbwa wake.

Yule mbwa alikuja mbio akionyesha mwenye furaha, Alimrukia Fuad mikononi huku akiutikisa mkia wake.

Fuad aliujaribu ubwana wake kwa mbwa huyo. Alikuwa haeshi kumpa amri hii na ile; mara amtume akalete hiki, mara kile, mara ampige makofi, mara mateke; almuradi alikuwa na chombo kizuri cha kujaribu ubwana wake na kujifunza kuamrisha. Mara nyingine yule mbwa huchoka kuhangaishwa na kukataa amri anazopewa na bwana wake.

“Boby, kalete bunduki yangu!” Fuad alimwamrisha yule mbwa siku moja baada ya kwisha kumtaabisha sana.

Yule mbwa hakwenda po pote, alibakia pale pale alipokuwa huku akibweka kwa kelele. Fuad alimpiga yule rnbwa kibao kikali sana hata akakimbia huku akibweka kwa makelele.
 
SEHEMU YA 5

Wakati wote huo Fuad alipokuwa akigombana na mbwa wake Kijakazi alikuwa amejibanza pembeni na furushi la majani ya ng’ombe aliyokuwa akiyapeleka ndani. Alipokuwa anaondoka hapo alipojibanza na kuyapeleka yale majani bandani aliiacha njia yake ya kawaida na kujipitisha karibu na Fuad ili walau apate kumwona mtoto aliyetenganishwa naye kwa siku nyingi. Fuad alimwona Kijakazi alipojipitisha hapo, bila ya kujali kitu cho chote alimpa amri Kijakazi, “Kijakazi, nenda kaniletee bunduki yangu!” Fuad aliamrisha kwa hamaki kama vile anapomhamakia mbwa wake. Hii ndiyo iliyokuwa amri yake ya kwanza kwa Kijakazi, mtumishi wao.

Bila ya kusema kitu cho chote Kijakazi aliukaza mwendo baada ya kuiweka ile chungu ya majani pembeni mwa njia, huku akifikiri vipi ataweza kuingia ndani ya nyumba ya Bwana Malik na kuichukua bunduki hiyo ya kuchezea aliyotumwa na Fuad.

Alipotia mguu wake tu ndani ya nyumba, Kijakazi alikutana na Bibi Maimuna ambaye alikuwa amekaa ukumbini, amevaa kanzu ndefu, viatu vya ndara, mtandio mwepesi uliopambwa kwa zari pembeni, ananukia kama jini. Kwa ajili ya mafuta mazuri aliyokuwa akinukia, aliweza kusikia mara moja harufu ya kupuo la ng’ombe alilokuwa akinuka Kijakazi. Alikunja uso wake na kumuonya asimkaribie akaja akaharibu manukato yake ambayo alichukua muda mrefu kujitia.

Kumwona tu Kijakazi anaingia ndani, Bibi Maimuna alianza kumtolea maneno, “Nini unataka hapa?”

“Bwana Fuad amenituma nije nimchukulie ile bunduki yake ya kuchezea!” Kijakazi alijibu buku mikono yake miwili ameikusanya pamoja chini ya kidevu chake.

Haya yalimfurahisha sana Bibi Maimuna aliyependa kumsikia mwanawe anaamrisha kibwana tokea udogoni mwake.

Tokea siku hiyo, Fuad alimpa Kijakazi amri kemkem na Kijakazi alizifuata zote kwa furaha. Siku zilivyoendelea sauti ya Fuad ilizidi kuwa ya kijeuri zaidi lakini Bibi Maimuna hakumkataza kwani alipenda mwanawe awe hivyo. Alitaka mwanawe awe Bwana mkali kama baba yake; bwana mtawala wa milki yake; bwana shamba wa siku za mbele. Alitaka mwanawe awe Bwana mkubwa ambaye ataweza kumwamuru mtu ye yote yule.

Siku moja Bwana Malik na mkewe walikuwa wakizungumza katika bustani nzuri iliyokuwa nyuma ya jumba lao. Ilikuwa wakati wa jioni wakipunga upepo katika bustani hiyo iliyokuwa na kila aina ya mti mzuri wa kuyafurahisha macho ya Bwana Malik: Miasumini, miwaridi, vilua, na miti mingine yenye harafu za kufurahisha. Inapofika magharibi, mrahati-el-leil uliokuwamo ndani ya bustani hiyo huibadilisha hewa ya pahala hapo na kuifanya inukie harufu nzuri ya maua yake meupe madogo madogo. Chini ya mti huo ndipo pahala ambapo Bwana Malik alipenda kukaa. Palikuwa na kibaraza kizuri cha saruji, na alipokuwa kibarazani hapo na mkewe, Bwana Malik hakutaka kukerwa na mtu ye yote - hata Fuad, mtoto wao mpenzi.
 
SEHEMU YA 6


Mishokishoki, mibalungi, mitufaa na miti mingine ya matunda ilikuwa imepandwa kwa kutupiwatupiwa katika kila sehemu ya bustani hiyo na miti hii iliyotawanya vivuli vyake vizuri ilizidisha faragha katika pahala hapo.

Palikuwa na pipa maalum la maji karibu na bustani hiyo lililounganishwa na mfereji uliokuwa ukimwagia maji kila asubuhi na jioni bustanini humo. Kazi ya kulijaza maji pipa hilo kila siku ilikuwa ni moja katika kazi kubwa alizokuwa nazo Kijakazi.

“Bwana, n’asikia yamekuja mafuta ya hal-ud kwa Ruwehi hivi juzi, tola shilingi mia tu,” Bibi Maimuna alimwambia mumewe walipokuwa wamekaa juu ya baraza ndani ya pepo waliyoitengeneza wenyewe katika shamba lile.

“Kesho basi nitamtuma mtu akakuchukulie. Tola ngapi unataka?”

“Tola tano zinatosha.”

“Basi kesho fungua kasha uchukue pesa unazozitaka na akija mke wa Bwana Zein na mumewe kutembea mpe akununulie.”

“Ala! Kwani kesho wanakuja?” Bibi Maimuna alijidai kustaajabu kama kwamba hakujua kuwa kila Ijumapili Bwana Zein na mkewe huja kwa gari lao jipya la aina ya May Flower kuwatembelea.

Kwa ghafla Bibi Maimuna aliyakatisha yale mazungumzo. Yeye hakuyaleta mazungumzo yale kwa kutaka ruhusa ya kutumia pesa. Alikuwa ameyaleta kwa kutaka kustawisha mazungumzo tu kwani inapojiri kutumia pesa. Bibi Maimuna alikuwa ni wa kufungua kasha na kuchukua azitakazo kwa kununua akitakacho. Ni yeye tu aliyeweza kuzitumia pesa za Bwana Malik namna hiyo.

Bibi Maimuna aliondoka pale juu ya kibaraza alipokuwa amekaa na kuanza kuzungukazunguka ndani ya bustani ile, kwenye ile miti yenye maua mazuri, akachuma asumini kidogo, tena ua moja zuri la waridi, balafu kilua kimoja kikubwa na kukipachika katika nywele zake ndefu za mawimbi alizopenda kuziacha matimtim na kuzipasua njia katikati... akasogea kwenye miti ya matunda. Kila alipochuma tufaa au tunda lo lote lile zuri kutoka katika miti ilc ambayo ilipandwa makusudi iwc mifupi ili matunda yake yaweze kuchumika kwa urahisi. basi humgeukia. mumewe na kumwita kwa furaha na kumrushia tunda hilo. Hapo tena Bwana Malik ambaye hupenda kukaa tu pale juu ya kibaraza kilc huku ametundika miguu, humbidi ajilazimishe kuruka pale alipokaa kulidaka tunda alilorusbiwa na mkewe. Bibi Maimuna aliona raha kumtaabisha mumewe namna ile na kucheka mpaka pumzi zikampaa wakati Bwana Malik anapokosea kulidaka tunda analorushiwa akataka kuanguka.
 
SEHEMU YA 7

Starehe yote hiyo waliyokuwa nayo Bwana Malik na mkewe ilivunjwa kwa kelele za Fuad aliyekuwa akija mbio akipiga kelele, “mama! mama!” huku Boby yuko nyuma yake anamfukuza, akimbwekea kwa hasira tayari kumtia meno!

“Siku zote n’akwambial Usimpige mbwa huyu, atakutafuna siku moja!” Bibi Maimuna alimwambia Fuad huku pumzi zake ziko juu juu kwa namna alivyostuka kwa kumsikia mwanawe akipiga kelele. Bwana Malik ndiyo alikwisha kabisa. Tokea hapo alikuwa na maradhi ya moyo na aliposikia kelele zile za Fuad, alinyong’onyea pale juu ya baraza alipokuwa amekaa. Aliposimama kutaka kuingia ndani hakuweza peke yake na ilibidi asaidiwe kwa kushikwa mkono na Bibi Maimuna.

Hapo hapo starehe ya bustanini ilimalizika. Bwana Malik alipelekwa ndani na baada ya kulazwa kitandani. tu mambo yalizidi. Moyo ulimwenda mbio, pumzi jau juu, akitoa shahada mbili mbili, “Lailaha illa LIah! Lailaha iila Liah !”

Bibi Maimuna alibabaika, akawa anakizunguka chumba kizima, mikono yake yote miwili amejitwisha kichwani huku akipiga kelele, “Masikim mume wangu! Masikini mume wangu!”

Alimwona mumewe yumo katika sakarat-el-maut, Dawa zote za kienyeji zilizokuwamo chumbani mle akazileta Ba kumpa. Mara alimpaka marashi, mara alimfukiza mafusho... lakini Bwana Malik alibakia kukoroma tu, hana kauli tena sasa. Yote yale, Fuad alikuwa akiyaangalia tu, hayaelewi, amebaki kumfuata mama yake kila anapokwenda.

Kuiona hali ya mumewe imezidi kuwa mbaya Bibi Maimuna alitoka saa zile za magharibi kwenda kutafuta mganga. Kabla ya kwenda alimwita Kijakazi ili akae na Bwana Malik na yeye alikwenda moja kwa moja mpaka kwa Maftah, mganga mashuhuri mtaani pale.

Alipofika kwake alimkuta Sheikh Maftah amekwenda msikitini akamsubiri mpaka akarudi. Baada ya kuingia ndani tu, Bibi Maimuna alimwambia huku machozi ‘yanamtoka, “Niwahi Sheikh!”

“Kumezidi nini teoa?” Sheikh Maftah alistuka.
 
SEHEMU YA 8

“Mume wangu kashikwa ghafla!”

Hawakukaa. Walitoka hapo hapo mpaka kwa Bwana Malik wakamkuta mahututi, anakoroma tu.

“Lahaula!” Sheikh Maftah alistuka alipomwona. Alivuta kiti kilichokuwamo chumbani mle na kukaa upande wa kichwani wa Bwana Malik huku akimsomeasomea.

“Yamemwanza wapi haya?”

“Tulivyokuwa bustanini!”

“Saa kama hizi si saa za kutembea chini ya miti! Amekumbwa na shetani mbaya huyu!” Alimkamata kichwa na kuendelea kumsomea, na ghafla aliuliza “Ipo zaafarani hapa?”

“Ipo!“

Bibi Maimuna aliingia chumba cha pili na kuanza kupekua mikebe yote mpaka akaigundua zaafarani ilipo. “Hii,” Bibi Maimuna alimpa sheikh, kwikwi na kilio vimemshika.

“Ipo sahani ndogo?”

“Ipo!”

Mara sahani ililetwa ria Sheikh Maftah akamtengenezea kombe Bwana Malik na kumnywesha. Alitia kombe lililobakia ndani ya chupa na kumwambia Bibi Maimuna, “Baada ya muda utamnywesha kidogo, na kidogo utampaka usoni.”

“Asante,” Bibi Maimuna alishukuru, huku uso umemvimba kwa kulia.

“La-haula! La-haula” Sheikh Maftah alisema akitoka.

Bibi Maimuna alifanya kama alivyoambiwa. Alimnywesha Bwana Malik kombe lile na jingine akampaka usoni... lakini hakupata nafuu. Ilipofika alfajiri alikata roho.

Usiku kucha Bibi Maimuna alikuwa pembeni mwa Bwana Malik na baada ya kukata roho alipiga kelele na kulia huku akiomboleza.

Usiku ule hapana aliyethubutu kulala katika wapagazi wa shambani pale. Walikuwamo katika harakati tu.

Asubuhi ilipoingia, habari za kifo cha Bwana Malik zilifika mjini na ilipofika kiasi cha saa nne, mabwana shamba na matajiri mbali mbali kutoka mjini walianza kumiminika nyumbani kwa marehemu kwa matayarisho ya mazishi.

Bwana Malik alizikwa baada ya sala ya alasiri na hayo yalikHwa mazishi ya kutolewa mfano. Ilisomwa hitima ya siku tatu na katika siku hizo tatu, hapana aliyepika cha jioni katika majirani kwani paliandaliwa vipochopocho vya kila aina na kutolewa sadaka kwa wakulima masikini wa mtaani pale.
 
SEHEMU YA 9

Ole wake Kijakazi! Kwa msiba mkubwa alipkuwa nao kwa kufiwa na Bwana wakc, alikuwa mnyonge kuwashinda wote na kila wakati akijiinamia. Kila akipata nafasi nyakati za magharibi alikwenda kaburini kwa marehemu na hapo huomboleza mpaka macho yakamvimba. Kifo cha Bwana Malik kilikuwa ni msiba mkubwa kwa Kijakazi.

Baada ya tanga kukunjwa tu jamaa zake Bwana Malilc walikusanyika na siku hiyo kasha lake lilifunguliwa kutaka kujulikana kilichomo ndani. Vitu vilivyokuwemo ndani ya kasha hilo vilisasambuliwa kimoja kimoja na kwa jumla vilivyokuwemo ndani ya kasha hilo vyote vilikuwa vya fahari tu. Vitara» vya dhahabu na majambia ya fedha. Jozi mbili za matarawanda ya fedha na vikuku kadha vya dhahabu. Baada ya kuangalia kila kitu sehemu za siri za kasha hilo zilianza kufunguliwa na zaidi ya fedha nyingi zilizokuwemo ndani ya sehemu hiyo mlikuwa na wasia wa Bwana Malik aliousia kwamba mali yake yote ibakie chini ya wakala wa Bwana Zein mpaka Fuad atakapofikia umri wa kukabidhiwa hazina aliyoirithi kwa baba yake.

Bibi Maimuna alikaa eda ya miezi minne na siku kumi. Wake wa mabwana shamba kutoka sebemu mbali mbali walikuja kumazi oa kumliwaza.

Baada ya kutoka eda, Bibi Maimuna alikuwa hana uzima tena. Alikuwa maradhi hayamwishi na baada ya mwaka mmoja na yeyo alifariki. Alizikwa pembeni ya kaburi la marehemu mumewe.

Bwana Zein alimlea Fuad kama namna alivyoagizwa na rafiki yake marohemu Bwana Malik. Hakupitisha dhulma wala ghalat kwani kwa mali tu, yeye mwenyewe alikuwa nayo ya kumtosha na kumkinaisha.

Kwa muda wa miaka kumi Fuad aliishi chini ya maongozi ya Bwana Zein aliemfundisha mbinu zote za kulinda utajiri na utukufu wake na katika kipindi hicho alifanya majaribio mazuri ya kutuma watwana na mafukara walio chini ya amri yake. Alipotimia miaka ishirini na tano Fuad alikabidhiwa mali yake yote na hapo akaanza kuchimba kufuru.

Fuad sasa alikuwa ndiye mwenye dhamana ya shamba na kila kilichokuwamo ndani ya shamba hilo pamoja na kila kilichokuwa mali ya baba yake. Alilitengeneza shamba bilo vizuri na kuongeza ardhi zaidi. Alijenga banda zuri la matofali na kuongeza ghorofa moja katika ghala yake ya kuwekea bidhaa.

Kwa Kijakazi, mwendo wa kufanya kazi kwa Fuad, ulikuwa ni ule ule. Alifanya kazi kama wakati wa uhai wa marehemu Bwana Malik. Alikuwwa akiacha kazi moja anashika nyingine; akifanya kazi mfano wa mashine. Akili yake yote ilikuwa iko katika kufikiri kazi alizokuwa akitarajiwa kuzifanya na alichukua hadhari kubwa ili asiharibu kitu cho chote katika kazi yake. Alifanya kazi kama punda na hapana binaadamu aliyeweza kufanya kazi mfano wa mwanamke huyo.
 
SEHEMU YA 10

Jioni moja alipokuwa analitembelea shamba lake. Fuad alipitia huko kwenye mabanda ya ng’ombe. Kwa machofu makubwa aliyokuwa nayo, Kijakazi alikuwa ameegemea nguzo moja ndani ya banda hilo huku ng’ombe wakila majani. Bila ya yeye mwenyewe kukusudia, usingizi ulimchukua na Fuad alipofika alimkuta amelala, ng’ombe wamekwisha kula majani wanangojea kupewa maji.

Fuad alimnyemelea Kijakazi kidogo kidogo na ilhali yumo usingizini, kampiga teke la ubavu.

“Ah! Nisamehe, Bwana!” alisema Kijakazi, huku anahia maumivu na huku akiona amefanya kosa kubwa asilowahi kulifanya.

“Wewe unafikiri uko wapi hapa! Mimi tokea saa ile nafikiri wewe unafanya kazi kumbe umekuja kujilicha huku na kulala!” Fuad kahamaki kweli kweli.

“Nisamehe, Bwana! Sitofanya tena!” Kijakazi alisema kwa sauti ya hofu huku akichukua madoo matupu yaliyokuwa bandani humo na kukimbilia kisimani kwenda kuteka maji.

“Mpumbavu mkubwa! Kizee hiki hakina akili hata chembe. Hakiwezi kazi; basi kimekaa hapa bure tu!” Fuad aliendelea kupiga makelele ijapokuwa alikuwa peke yake.

Kijakazi alikimbilia kisimani na mara alirejea na madoo yaliyojaa maji, akawanywesba ng’ombe. Walipomaliza, alirudi kuteka maji tena, mara mbili, mara tatu. mpaka akawamaliza ng’ombe wote.

Baada ya bayo Kijakazi aliegemea lile lile guzo alilokuwa ameegemea mwanzo na kuwaza yaliyotokea.

“Lo! Leo nimemkera sana Bwana!” Alijinong’onea. “Sijui atafikiri nini!”

Usiku kucha Kijakazi hakulala kwa mawazo aliyokuwa nayo. Maskini Kijakazi alifanya kila aliloweza ili kumfurahisha na kumtii Bwana wake. Lakini kwa jambo dogo tu amemkasirisha.

“Nitajitahidi yasitokee tena kama yaliyotokea leo,” Kijakazi alijituliza.

Siku ya pili Kijakazi aliamka alfajiri. Jogoo la kwanza yeye alikwisha nyanyuka. Hakusimama pahala popote mpaka kwenye banda la ng’ombe na kuanza kuwakama maziwa. Baada ya kumaliza kazi hiyo alitoka nje ya banda.

Kumekwisha kucha. Fuad amekwisha amka. Alikuwa anatembea nje ya nyumba yake ili kupata hewa ya asubuhi na mara alikutana na Kijakazi aliyekuwa akikimbia kuyapeleka maziwa aliyokwisha yakama kwa Fuad.

Kijakazi roho ilimpiga na alisimama kidogo kama aliyepigwa na mshangao.

“Ushakama maziwa?” Fuad alimwuliza Kijakazi kwa sauti ya ukali.

“Nishakama Bwana!” Kijakazi alijibu.
 
SEHEMU YA 11

“Haya; nikirudi nikukute ushawapa ng’ombe wote majani!” Fuad alimwambia Kijakazi huku akiendelea na safari yake ya kulizunguka shamba lake wakati wa asubuhi.

Fuad alikwenda kitambo kidogo na mara alimgeukia tena Kijakazi na kumwita, “Ohaa!”

Kijakazi alifahamu kuwa hakuna mwingine anayeitwa isipokuwa yeye na aligeuka kwa gbafla, nusura ndoo moja ya maziwa imdondoke.

“Halafu usisahau kwenda kuwafunga mbuzi!” Fuad alisema. Alikwenda mbele kidogo na mara alitoa amri nyingine, “Na yale mabanda ya kuku yote uyasafishe leo.”

Baada ya kusikiliza amri zote alizopewa, Kijakazi aliyachukua madoo ya maziwa aliyokuwa ameyabeba na kuyaweka hapo kwenye baraza la nyumba ya Fuad yakingojea kuja kuchukuliwa na wachukuzi kupelekwa mjini baada ya kwisha kupimwa na Fuad mwenyewe.

Kidogo hofu ilimpunguka Kijakazi alipoona Fuad hakumkumbusha yaliyotokea jana. Kucha alikuwa akifikiri Fuad atamwambia nini leo. na alivyokuwa hakumwambia kitu alihisi kama mtu aliyetaa mzigo mkubwa uliokuwa umemtopea.

Kijakazi hakuelewa jambo lo lote katika mambo yaliyokuwa yaldpita ulimweaguni na yale yaliyokuwa yakitokea karibu naye alijifanya kama hayaoni.

Kila wafanyakazi walipochukua hatua za kudai haki zao waliitwa maaskari wa kikoloni ambao walitumia silaha zao za virungu, mabomu ya kuumiza macho na bunduki kuwatawanya. Baadhi ya viongozi wao na wafanyakazi wengine jasiri walitiwa vifungoni ambako waUteswa na kufanyiwa ukatili wa kila aina. Umaskini ulikuwa umejaa nchini na unyonge umewazonga wananchi. Hata hivyo, au kutokana na dhiki hizo, wafanyakazi hawakwisha kufanya migomo, maandamano na mikutano ya hadhara na ya siri ya kupinga mabepari na makabaila na kudai uhuru kutoka kwa wakoloni.

Yote haya yakija na kuondoka lakini kwa Kijakazi wakati haukugeuka wala haukubadilika. Kwake yeye maisha yalikuwa ni kufanya kazi tu ili kumfurahisha Bwana Fuad.

Wakati wa mchana ilikuwa hapana anayezungumza naye ili kumweleza yaliyokuwa yakitokea katika nchi. Sauti za wale alioweza kukutana nao pindi alipopata nafasi wakamwelezea yaliyotokea, alizisikia kwa mbali. Yeye alifurahi kuona yote yaliyotokea hayakumhusu. Kila mara alikuwa akishukuru Mungu kwa kumpa uwezo wa kufanya kazi zake vizuri.

Wapagazi kadha wa kadba walikuja na kuondoka. wakubwa na wadogo, wanaume na wanawake, lakini Kijakazi alibakia pale pale. Wengine walikuja na hata kabla Kijakazi hakuyajua majina yao waliacha kazi. Yote haya yalikuwa kwa sababu ya ujeuri, usafihi na utovu wa adabu wa Fuad. Alikuwa bamjali mkubwa wala mdogo; kila aliyekuwa akifanya kazi kwake au kwa jumla kila mkulima kwake yeye alikuwa ni mtwana tu.
 
SEHEMU YA 12

Fuad alikuwa na wapagazi wengi katika shamba lake na si wote waliokuwa watiifu kama alivyokuwa Kijakazi. Kwa mfano, tabia ya Mariam ilikuwa kinyume na ile ya Kijakazi.

Mariam alikuwa ni msichana mzuri wa kuvutia, alikuwa mzuri wa tambo na sura. Alikuwa na macho mazuri yaliyo duara na yenye kumeremeta mfano wa nyota zikiwa mawinguni.

Si kama Mariam alikuwa mkaidi hapo kazini. Alikuwa anajitahidi kufanya kazi zake kama anavyoweza lakini alikuwa hakubali kutumwa kama punda. Pindi alipojihisi amechoka kwa wingi wa kazi, alikuwa kidogo kidogo akijitafutia upenu na kujipumzisha.

Kwa ajili ya uzuri aliokuwa nao Mariam, Fuad alishindwa kujizuia hata kidogo na mara kwa mara alikuwa akimnyemelea nyemelea kama paka aliyeshikwa na ugonjwa wa mapenzi.

Siku moja Mariam alikuwa yumo ndani ya banda la ng’ombe anawapa majani. Fuad alimwona alipokuwa akiingia ndani ya banda hilo akamfuata humo.

“Mariam, hebu njoo nikwambie kitu mara moja,” Fuad alisema taratibu.

Mariam alishangaa sana kumsikia Fuad akizungumza naye kwa sauti kama ile yenye heshima na upole kinyume cha kawaida yake. Aliitika mwito ule akaeoda.

Mara Fuad alianza, “Unajua Mariam, yako maneno kila siku nilitaka kukwambia lakini sijakupatia nafasi.”

“Maneno gani Bwana?”

“Maneno gani?” Fuad aliuliza, “Sogea hapa basi nikwambie”

“Sema tu Bwana, mimi nitasikia hapa hapa nilipo.”

Pale pale upole ulimwisha Fuad na ubwana ukamjia.

“Ebo! Mimi tokea wakati ule nakwita hapa, wewe una...” Hakuwahi kumaliza kusema aliyotaka kusema mara alimvamia Mariam na kuanza kumbusu mashavuni.

“Sitaki! Sitaki! Unanikamata kwa nguvu!” Mariam alipiga kelele.

Baada ya kujikurupua sana Mariam aliweza kutoka mikononi mwa Fuad akaukimbilia mlango wa banda ambao Fuad aliufunga makusudi alipoingia ndani humo. Kwa bahati Mariam aliweza kuufungua.

Sauti ya hamaki ya Fuad ilisikika mpaka upande wa pili wa uwanja wa nyumba yake akipiga kelele.

“Nguruwe mchafu we!”

Nje ya banda la ng’ombe walikuwapo wafanyakazi. wengine waliokuwa wakifanya kazi za kupalilia na za kilimo. Fuad hakupenda Ble jambo atilolifanya lijulikane. Alipofika nje ya banda alijidai kuyababaisha maneno.

“Basi kazi kucheza kazini tu! Siku ya pili nikikukuta unafanya mchezo katika kazi nitakuvunja kichwa chako! Nitakufukuza shambani kwangu kama nilivyokwisha kuwafukuza watwana wengine kama wewe!”

Wale wafanyakazi wengine walinyamaza kimya kila mmoja akiwa na wasiwasi mwingine yupi katika wao atakayetukanwa.
 
SEHEMU YA 13

“Na nyie mnasikiliza nini? Fanyeni kazi zenu!” Fuad aliwapigia kelele wale wafanyakazi.

Fuad alifutuka kwa hamaki na akaufuata ule ujia mwembamba uliooteshwa maua pande zote mbili ulioongozea kwake kutoka pale lilipokuwa banda la ng’ombe. Alikwenda moja kwa moja mpaka kwake na alipofika huko aliingia chumbani mwakc.

Mariam, alibaki pale nje ya banda la ng’ombe kwa muda mrefu amejikunja, roho ipamwenda mbio.

“Je! umefanya nini tena?” Mfanyakazi mmoja alimjongelea Mariam na kumwuliza pole pole. Alizungumza naye huku akiendelea na kazi yake bila kumtazama ili asije Fuad akatokea akawakuta wanazungumza likawa balaa jingine.

“Anataka kunipiga!” Mariam alijibu, mkono wake mmoja umeizuia kanzu yake chafu iliyopasuka katika vita vyake na Fuad.

Ijapokuwa jambo alilofanyiwa Mariam na Fuad ni jambo baya, hakutaka kuwajulisha wale wafanyakazi wenzake nini hasa lililotokea.

“Anataka kukupigia nim?” yule mfanyakazi alimwuliza tena Mariam, uso wake ukiwa bado unaangalia pale pale alipokuwa akijidai kupalilia.

Mariam hakumjibu tena; alinyamaza Idmya. Kwa jinsi ghadhabu zilivyomzidi, machozi yalianza kummiminika. Jambo hili lilimtia haya na pale pale aliondoka na kurejea kazini ndani ya banda la ng’ombe akifuta machozi

Fuad aliingia chumbani mwake na kujilaza chali juu ya kitanda. Alivuta pakiti ya sigareti iliyokuwa pembeni ya kitanda, akachomoa sigara moja na kuiwasha. Alimwaza Mariam huku akiuangalia moto ukiila sigara yake. Moyo wake pia ulikuwa ukiungua kwa kumtaka Mariam. Bali ari yake ya kibwana ilikuwa ikiteketea: Vipi, vipi, kijakazi kama kile kimkatae bwana wake...? Kilithubutuje kusema “sitaki!”, kupiga kelele. kumtia aibu...ah!

“Mwachilie. sasa nitamwita huku ndani na akifika atashika adabu yake: Nitamwita mmoja katika wale mbwa wenzake aje anisaidie kumkamata”
 
SEHEMU YA 14

Fuad alikuwa mwingi wa mwili lakini kwa ajili ya kukaa bure maisha yake yote, unene aliokuwa nao ulikuwa ni wa maji matupu. Hakumweza Mariam kwa vibiru na ilimbidi ampate mtumishi wake mwingine kumsaidia. Alitoka chumbani kwake akaenda kule kule kwenye banda la ng’ombe. Alipofika, alifungua mlango wa banda kwa ghafla na kwa nguvu. Mariam aligeuka kwa haraka akamwona Fuad amejaa pale mlangoni, uso umemwiva kwa hamaki.

“Njoo huku!” Fuad alimwamuru.

Aliondoka pale mlangoni na kumwelekea mmoja katika wale wafanyakazi waliokuwapo pale.

“Na wee, njoo huku!”

Alifikiri wote watamfuata lakini Mariam alipofika nje ya banda alifuata njia nyingine na kukimbia. Aliingia kichakani na mara moja akatoweka.

Baada ya hatua chache, alipogeuka kuwaangalia aliowaita, Fuad alimwona yule mfanyakazi mwingme tu aliyemwita.

“Yuko wapi yule?”

“Amepitia huku Bwana,” mmoja katika wale wafanyakazi alijibu.

“Amekimbia siyo! Kamtafuteni mumlete hapa na akifika hapa basi kichwa chake halali yangu!” Fuad aliwatuma wale wafanyakazi.

Wote kwa pamoja waliyatupa majembe waliyokuwa wakifanyia kazi na kuingia maguguni kumtafuta Mariam. lakini hata baada. ya muda mrefu hawakumwona.

Ijapokuwa kwa tabia za kibwana-shamba ni aibu kwa bwana shamba kumtaka mwanamke mkulima, lakini Fuad hakuweza kujizuia kuwapenda. Mara kwa mara Fuad alisikia hadithi kutoka kwa vijana wenzake, watoto wa mabwana shamba, kuhusu namna gani watoto wa kike wa kishamba walivyo mahodari katika kuwastarehesha Bwana zao. Kwa sababu hii, Fuad alifanya kila njia aweze kupata mtoto mwingine wa kiamboni pale ili kuhakikisha ukweli wa hadithi hizo alizozisikia.
 
SEHEMU YA 15

Ilipofika magharibi, baada ya kwisha kusali. Fuad aliteremkia viamboni na kujidai kuzungumza na wale wakulima anaowajua na ambao hujipendekeza kwake. Dhamiri ya ziara hiyo ilikuwa siyo kuwatembelea wale watu hasa bali kutafuta vigori. Alitembelea nyumba moja moja na alipofika nyumbni kwa mzee Sharwani akakaa humo kwa muda mrefu akipiga soga.

Mzee Sharwani alikuwa na kibanda kidogo. Ukiingia ndani tu baada ya kufunguliwa mlango waona utajiri wa nyumba yote mbele yako - kitanda cha mayowe kilichotandikwa mkeka mkuukuu, vibao vidogo vidogo vya msonobari, na katika pembe’moja ya ukuta chungu ya makozi ya kupikia.

Mzee huyu hakujua nia halisi ya matembezi ya Fuad na hata kama angejua angeona ni fahari kubwa kwake kwa kuwa na binti anayemfaa bwana shamba mkubwa yule. Baada ya kukaribishwa kwa hamu na mzee Sharwani, Fuad aliingia ndani kwa hadhari akichelea asizitie nguo zake uchafu. Alivaa kanzu nzuri ya darzi na kikoi cha Jabir, kofia ya mjazo ya mkono na viatu vya makubadhi.

Mzee Sharwani alitoa mkeka mpya alikuwa nao, akasogeza upandc ghasia ndogo ndogo zilizokuwapo hapo na kuutandika.

“Tafadhali Bwana!” Mzee Sharwani alimkaribisha Fuad kukaa juu ya ule mkeka.

Yeye mwenyewe alikaa juu ya kibao cha msonobari na hapo soga likaanza.

Mzee Sharwani alikuwa mtu mzuna sana na aliukumbuka vizuri ujana wa Bwana Malik, baba yake Fuad, na hata aliikumbuka sherehe kubwa iliyofanywa hapo Koani alipozaliwa Fuad, Mazungumzo yote jioni hiyo yalikuwa juu ya nyumba ya Bwana Malik.

“Oh, Bwana Malik! Alikuwa mtu mardadi sana. Juu ya kanzu yake alikuwa hathubutu kutua inzi! Bwana Malik alikuwa mtu mwema sana, hapa kisiwani kote hapana mfanowe,”

Hizi ndizo zilizokuwa hadithi za mzee Sharwani. Bwana Malik hivi, Bwana Malik vile; Bi Maimuna hivi, Bi Maimuna vile. Aliwapa sifa ambazo nyingi hawakuwa nazo almuradi yeye akitaka kumfurahisha Fuad.

Lakini hayo siyo yaliyompeleka Fuad hapo. Habari na sifa za Bwana Malik, Fuad alizielewa, na zile asizozijua siyo aambiwe saa hii. Kilichompeleka kwa Mzee Sharwani ni mjakuu wake kigori. kwa jina, Mkongwe.

“Siku hizi naona Mkongwe amekua mkubwa?” Fuad alisema akiingilia kati mazungumzo ya Mzee Sharwani juu ya sifa za baba yake na mama yake.

“He! He! Mwali mzima tena sasa,” Mzee Sharwani alijibu huku akijichekesha kicheko cha kuona haya.
 
Niliisomaga yote nakumbuka.Inahusu mapambano ya ukombozi wa wazanzibari weusi kutoka kwa utawala wa kisultani.
 
SEHEMU YA 16



Hamkuwa na raha yo yote ndani ya kibanda cha Sharwani na kwa Fuad kibandani humo ilikuwa kama motoni ukilinganisha na raha na starehe zilizokuwako kwake. Kulikuwa na joto kali mle ndani na kibatari kilichokuwa kikitoa moshi kilimfanya Fuad atokwe na machozi Alifungua kifungo cha shingoni cha kanzu yake na kujipepea kwa mkone wake. Kijasho chembamba kilikuwa kildmtoka.

“Anafanya nini siku hizi?”

Mzee Sharwani kinywa wazi, hana jino hata moja kwa kuzeeka, alijibu huku aldjichekesha, “Analima na kunisaidia kazi zangu nyingine. Huo mkeka uliokalia kausuka na kuushona yeyc. Mjukuu wangu ni mtoto hodari kabisa.”

Joto lilizidi mle ndani na Fuad akashindwa kulistahimili akayakata mazungumzo.

“Mimi ninaondoka nakimbilia kwenda kusali el-isha.” Fuad alisema.

“Hewalla Bwana! Karibu!” Mzee Sharwani alimuaga Fuad kwa kujipinda kuonyesha heshima.

Fuad alijenga msikiti mdogo, mzuri, karibu na nyumba yake na ndani ya msikiti huo walisali wale waliokuwa na madhehebu ya kiibadhi tu kama yeye mwenyewe.

Aliingia mskitini kusali lakini hata hivyo hakuacha kumwaza na kumtamani Mkongwe. Alipotoka aliazimia kwenda kwa Mzee Sharwani kila siku hadi apate kumwajiri Mkongwe.

Fuad hakuacha kumfikiri Mkongwe. Ijapokuwa mara kwa mara alikwenda mjini na kukutana na wasichana wazuri, bado sura ya Mkongwe ilimjia akilini mwake kama ndoto, akashindwa kuitoa. Alikerwa sana na hali hii ya kumtamani msichana ambaye katika jamii ya matabaka kama yale ya Unguja siku zile hakuwa na thamani yo yote kwake. Mara nyingi alijiuliza, “Nifanye nini nimtoe Mkoogwe kichwani mwangu? Nimwite nyumbani kwangu nimchukue kwa nguvu au nimpe zawadi za nguo na pesa kidogo akubali yeye mwenyewe kufanya ninavyotaka? Nimwachie mbali mtumwa huyu anayenuka jasho, niache kujihangaisha bure?”

Lakini wapi, alivyozidi kujiuliza maswali haya ndivyo alivyozidi kumtamani. Mwishoni aliamua kumfuata baba yake, Mzee Sharwani. amwombe amruhusu Mkongwe kwenda kufanya kazi sbambani kwake. Alidhani kuwa akiisha kuanza kazi njia itapatikana ya kumshawishi kufanya na hayo mengine.

Matembezi ya Fuad kwa Mzee Sharwani yaliongezeka. Hazikupita siku tatu bila yake kwenda na mazungumzo yake sasa yakiishia katika kuuliza kwa nini Mkongwe haendi kwake kufanya kazi, Mzee Sharwani akimjibu kuwa Mkongwe mwenyewe hataki kumwacha Mzee wake na kwenda kufanya kazi kwa Bwana Fuad. Kila siku Fuad humwuliza swali hilo na kila siku Mzee Sharwani hujibu vile vile.

Fuad alipoona hafiki mbali kwa kuuliza kwa njia bii ya upole alianza kutumia vitisho lakini akivificha katika lugha ya mafumbo! “Mzee Sharwani. naona hutaki Mkongwe aje kufanya kazi shambani kwangu; maana yake nini? Mimi natafuta kijana kama yeye kunifanyia kazi lakini naona wewe unamwekea vipingamizi.”

“Hapana, Bwana Fuad,” Mzee Sharwani alianza kujitetea. “Mimi simkatazi Mkongwe kuja kufanya kazi kwako; kwa nini nimkataze? Yeye mwenyewc pengine hataki, na kama anataka sitamkataza.”

“Basi mwambie aje kesho kule shambani aanze kazi.”

“Haya Bwana Fuad, nitamwambia na kama anaweza atakuja. Haya kwakberi bwana Fuad, karibu tena Sahib wangu.”
 
SEHEMU YA 17



Baada ya mazungumzo mengi ya ulaghai na vitisho, Fuad aliweza kumfanya mzee Sharwani kumruhusu Mkongwe kwenda kufanya kazi kwake na huko kwa Fuad kazi kubwa aliyokuwa nayo Mkongwe ilikuwa ni kushirikiana na Kijakazi katika kazi zisizokwisha za shambani mle.

Siku moja Mkongwe alikuwa kisimani anateka maji, akiitumbukiza ndoo kisimani na kuivuta na halafu kuitumbukiza tena kisimani baada ya kumimina maji ndani ya mtungi wake. Hakujua kabisa kama kuna mtu aliyekuwa akimtazama.

Fuad alijificha kichakani akimtazama. na kuuhusudu uzuri wake. Na kweli Mkongwe alikuwa mzuri wa maumbile. Mashavu yake yalikuwa ya duara na nywele zake nyeusi zilizosukwa zilipendeza sana. Alikuwa amejifunga kipande cha kaniki kifuani na kanga moja amejitupia kichwani, na nguo hizo zikivaliwa na wanawake wa Kisiwani huonyesha vizuri vifua vyao vilivyojaa kwa maziwa ya ujana wao na sehemu nyingine za mwili.

Fuad alimtazama Mkongwe kwa muda mrefu na baadaye alitoka pale kichakani alipokuwa amejificha na kuelekea kule kisimani alipokuwa. Mkongwe aliivuta ile kanga aliyokuwa amejitupia kichwani na kujistiri sehemu ya kifuani baada ya kumwona Fuad.

“Nini habari?” Fuad alimwuliza huku uso wake ameukunja kwa kutaka kumtia hofu.

“Nzuri Bwana!” Mkongwe alijibu.

Fuad alimwangalia tokea juu mpaka chini na mara alikwenda zake bila ya kumwambia kitu cho chote.

Kazi aliyokuwa nayo Mkongwe hapo shambani kwa Fuad ilikuwa na kushirikiana na Kijakazi katika kazi zake. Kwa hakika, hakuajiriwa Jli amsaidie Kijakazi na kumpunguzia mzigo wa kazi nyingi alizokuwa nazo, bali kuwa pamoja naye ili kazi ifanyike kwa wingi zaidi.

Kazi za Kijakazi zilikuwa kama kawaida, moja baada ya moja, bila mapumziko. Mkongwe alijitahidi kushirikiana na Kijakazi lakini mwisho aliona atakonga kabla ya siku zake kwa kazi zilivyokuwa nyingi. Kazi yenyewe haikuwa na mshahara maalum. Mfanyakazi alipewa kipande kidogo cha ardhi kulima ambacho bwana shamba angeweza kumnyang’anya wakati wowote, na hapakuwa na pahala popote pa kwenda kulalamika.

Siku moja saa saba mchana katika jua kali, Kijakazi na Mkongwe walikuwa wakimg’oa majani ya ng’ombe. Kijakazi hakuwa na wakati wa kuzungumza na mfanyakazi mwenzake kwa jinsi alivyokuwa akifanya kazi. Mkongwe aliinuka kwa ghafula baada ya kuinama muda mrefu akichuma majani akamtazama kwa makini Kijakazi. Alipobaini kuwa anatazamwa na Mkongwe, yeye pia aliinuka na kupumua.

“Kijakazi mbona unafanya kazi namna hii? Hivi utajiua kwa kazi. Halafu unapata faida gani hasa kujivunja kwa kazi namna hiyo?” Mkongwe aliuliza.

Kijakazi alishtushwa na maneno ya Mkongwe kwani hakupata hata siku moja kuambiwa maneno kama yale na mtu ye yotc. Hakupenda hasa kuambiwa maneno kama yale kwani furaha yake kubwa ilikuwa ni kusifiwa kuwa ni mfanyakazi hodari na mwenye juhudi.

“Mimi, shoga yangu, nitamaliza maisha yangu hapa hapa. Hapa ndipo nilipoanzia na hapa ndipo nitakapomalizikia.”

Mkongwe alimtazama Kijakazi kwa huruma. Akimtazama umri wake. afya yake na namna alivyofanya kazi, alimwona kama mtu mwenye wazimu aliyedhamiria kujiua makusudi.
 
Back
Top Bottom