RIWAYA: Mifupa 206


HUYU MTU ANAYEFAHAMIKA KWA JINA LA STEPHEN MASIKA
amekuwa kama saratani mbaya inayohatarisha biashara yetu” Fred Bagunda
akaongea kwa utulivu huku mwili wake ukiwa umestarehe vizuri kwenye kiti
chake cha ofisini chenye foronya laini. Njama alikuwa mbele yake akimtazama kwa
makini.
“Umejuaje kuwa huyo mtu anaitwa Stephen Masika?” Njama akauliza kwa
mshango huku akiyatathmini kwa ukaribu maneno ya Fred Bagunda.
“Nilipigiwa simu na kuelezwa juu hali ya mambo ilivyo. Inavyoonekana sasa ni
kuwa huyu mtu anayefahamika kwa jina la Stephen Masika huwenda ndiye aliyehusika
na vifo vya Alba Gamo,Guzbert Kojo na P.J.Toddo. Nafikiri sasa unaweza kuvuta
picha kuwa huyu Stephen Masika ni mtu wa namna gani”
“Sasa unadhani jambo la busara litakuwa ni kuendelea kumuogopa na kumuacha
akiendelea kutamba mitaani?” Njama akauliza kwa utulivu.
“Nataka kwanza upate picha kuwa tunashughulika na mtu wa aina gani. Taarifa
nilizozipata ni kuwa kuna vijana watatu waliokabidhiwa kazi ya kumtafuta huyu
Tumbili” Fred Bagunda akafafanua.
“Unadhani huyu mtu ambaye sasa tunamfahamu kwa jina la Stephen Masika
anapata wapi nguvu za kupambana na huu mtandao?” Njama akauliza.
“Swali hilo ndiyo lililotufanya tukatoka kwenye kikao saa kumi usiku pasipo kupata
majibu ya kuridhisha. Hisia zetu zilikuwa zimejikita zaidi kwenye vyama pinzani
ambavyo hutafuta taarifa za udhaifu wa serikali kwa gharama zozote ili waweze
kuzitumia kama mtaji wa kisiasa kuombea kura kwa wananchi. Baadhi yetu walienda
mbele zaidi wakidai kuwa huwenda kuna watu fulani waliokuwa wakipanga kuipindua
serikali iliyoko madarakani”
“Kwanini mkafikiria hivyo?” Njama akauliza.
“Ni kutokana na tukio la kuuwawa kwa mkuu wa kurugenzi ya mawasiliano ya
rais Ikulu. P.J.Toddo ni mtu muhimu sana kiutawala na anayefahamu karibu kila kitu
kinachoendelea katika hii serikali”
“P.J.Toddo anaingiaje katika huu mkasa?” Njama akauliza.
“Hii kazi tunayoifanya ni kwa ajili ya maslahi ya baadhi ya wanasiasa na wanasiasa
hao ndiyo serikali yenyewe. Huwenda P.J.Toddo alikuwa akivujisha siri za mambo
yetu na hapo protokali ndiyo zikafuatwa”
“Kwa maana nyingine unataka kuniambia kuwa kifo cha P.J.Toddo kinatokana na
kuvujisha siri?” Njama akauliza.
“Huo ni mtazamo tu wa baadhi ya watu wakati tulipokuwa tukijadiliana”
“Mwisho wa mkutano wenu mkaazimia nini?”
“Ulinzi na umakini uongezwe na tahadhari zichukuliwe. Stephen Masika atafutwe
popote alipo na atakapopatikana azungumze yeye ni nani na anafanya kazi kwa
maslahi ya nani”
“Baada ya hapo?”
“Baada ya hapo protokari zitafuatwa”
“Vipi kuhusu mzigo wa yule mama?” Njama akauliza akihamisha mada.
“Nimeshafanya mawasiliano na White Sugar na hivi tunavyozungumza ameniambia
kuwa mzigo upo njiani” Fred Bagunda akaongea kwa hakika.
“Sasa yule mama amefikia wapi hapa jijini Dar es Salaam?”
“Yupo kwenye chumba kimoja cha Hotel Agent 11 hapa jijini Dar es Salaam
anaendelea kusubiri”
Maongezi baina ya Fred Bagunda na Njama yalikuwa yakiendelea katika chumba
kile cha ofisi za kampuni usafirishaji wa vifurishi vya kimataifa ya Intercontinental &
Overseas Parcels (I.O.P) iliyokuwa ikisemekana kumilikwa na wawekezaji wawili wa
ndani ya nchi.
___________
ILIKUWA IKIELEKEA KUTIMIA SAA MBILI ASUBUHI wakati
nilipoegesha gari langu kando ya kituo cha kujazia mafuta kinachotazamana na
barabara kuu ya Bagamoyo eneo la Mwenge jijini Dar es Salaam.
Usiku mzima uliopita nilikuwa nimelala usingizi wa mang’amung’amu huku akili
yangu akisumbuka kwa kila namna katika kutengeneza mtiririko mzuri wa matukio
yote ili yaweze kuleta maana. Lakini suala hilo lilikuwa limeshindikana kwani matukio
mawili au matatu niliyoyachukua na kuyaunganisha yalikataa kuunganika na hivyo
nikaendelea kuteseka kitandani.
Hata hivyo baada ya kuwaza sana hisia fulani zilikuwa zimeanza kujengeka
kichwani mwangu kuwa yule mndunguaji aliyenitoroka usiku wa jana alielekea
kufanana na yule msichana niliyemfuatilia kutoka kule Vampire Casino hadi mtaa wa
Nkuruham siku chache zilizopita.
Foleni za magari zikiwa zimeanza kushamiri katika baadhi ya barabara za jiji
la Dar es Salaam hivyo mara tu nilipofika kwenye kituo kile cha kujazia mafuta
nikashuka kwenye gari langu kisha nikavuka barabara nikielekea kwenye kituo cha
teksi kilichokuwa karibu na eneo lile.
Kumbukumbu nzuri juu ya lile gari lililotumika jana na mdunguaji ilikuwa bado
timilifu kichwani mwangu. Nililikumbuka vizuri gari lile aina ya Corolla limited yenye
kibandiko cha teksi juu yake na ufito wa njano ubavuni kuwa lilikuwa likisaka mkate
wake wa kila siku katika kituo cha teksi cha pale Mwenge kutokano na utambulisho
wake ubavuni.
Madereva wa teksi wa kituoni pale walinikaribisha kwa bahasha zote huku
wakiniweka kwenye kundi la mteja lakini waliposikiliza shida yangu baadhi yao
wakanipa mgongo na kuendelea na hamsini zao. Mzee mmoja mkongwe dereva
wa teksi mwenye busara akabaki akinikata jicho la kunisahili. Hali ile ikanipa ujasili
wa kutumbukiza mkono wangu mfukoni na kuchukua karatasi ndogo niliyokuwa
nimeiandika namba za ile teksi ya mdunguaji kisha nikampa yule mzee.
“Nimesahau mzingo wangu kwenye teksi yenye hizi namba” nilimwambia yule
mzee huku nikiupima uzito wa maneno yangu.
“Mzingo gani?” yule mzee akaniuliza huku akiitazama ile namba ya teksi kwenye
ile karatasi bila kuishika.
“Begi langu dogo jeusi lenye vitu vyangu muhimu vya kusafiria ikiwemo pasipoti”
“Wewe ni mgeni hapa jijini Dar es Salaam?” mzee yule akaniuliza na kupitia
matamshi yake nikafahamu kuwa alikuwa Mngoni wa Ruvuma.
“Mimi ni mkazi wa Songea mkoani Ruvuma” nikamwambia yule mzee huku
nikinuia kununua urafiki.
“Oh! kumbe wewe ni mkazi wa Songea hata mimi natokea Songea. Mke wangu na
watoto wanakaa eneo la Mfaranyaki. Mimi nimewatoroka kidogo na kuja hapa Dar es
Salaam kuangalia upepo wa maisha” mzee yule mwanalizombe akaongea kwa furaha
sana huku akijihisi kuwa amekutana na ndugu yake wa karibu.
“Sasa nyinyi wazee mkikimbia miji yenu na sisi vijana wenu tufanyeje?”
nikachombeza utani kidogo.
“Hapana! mimi sijakimbia nyumbani. Unajua hii nchi yetu ni huru na kuna amani
ya kutosha. Ukikaa sehemu moja na kuona mambo yako hayakuendei vizuri upo
huru kujaribu kwingine kwani hakuna mtu aliyekushika miguu,alimradi tu usisahau
nyumbani” mzee yule akaweka kituo na kunitazama kabla ya kuniuliza
“Songea unaishi sehemu gani?” mzee yule akaendelea kurefusha maongezi huku
akionekana kufurahi na kwa kweli sikutaka kupoteza muda hivyo nilichukua noti
moja ya shilingi elfu kumi kutoka mfukoni mwangu na kumshikisha mkononi.
“Tafadhali! naomba unisaidie” nilimwambia yule mzee na nilichokiona usoni
mwake ni furaha ya kushtukiza iliyochanganyika na mipango ya kifungua kinywa
kizito katika fikra zake.
“Namba hii ni ya teksi ya Momba hata hivyo sijamuona kwa hizi siku mbili tatu”
“Anaishi wapi?” nilimuuliza yule mzee.
“Nyumbani kwake siyo sehemu ya kupotea. Shukia kituo cha ITV halafu
mkono wako wa kushoto utaona barabara. Shuka na barabara hiyo na mwisho wake
utakutana na barabara nyingine inayokatisha kwa mbele. Sasa wewe ukifika hapo
ingia upande wa kulia halafu hesabu hadi nyumba ya nne upande wa kushoto kwako
utaona nyumba yenye uzio wa michongoma. Hapo ndiyo nyumbani kwa Momba.
Ukimkosa rudi hapa ndugu yangu nitakusaidia” mzee yule akanielekeza kwa furaha
huku akiushikashika mfuko wa shati lake alipoitumbukiza ile noti ya shilingi elfu kumi
niliyompa.
“Ahsante!” nikamwambia mzee yule na kumuaga nikirudi kule nilipoegesha gari
langu.
Muda mfupi baadaye nilikuwa nimefika kwenye kituo cha daladala cha ITV.
Maelezo ya yule mzee yalikuwa sahihi kwani nilipofika tu kwenye kituo kile upande
wa kushoto kwangu nikaiona barabara ya gari inayokatisha mitaani. Nikakunja
kona kuifuata barabara ile na baada ya muda mfupi nikawa nimeifikia ile barabara
inayokatisha kwa mbele. Hivyo nilipofika pale nikaingia upande wa kulia na kwenda
kuegesha gari langu nje ya nyumba ya nne iliyozungushiwa uzio wa michongoma
upande wa kushoto wa barabara ile.
Kama zilivyokuwa nyumba nyingi za jijini Dar es Salaam nyumba ya Momba
ilikuwa imekula chumvi nyingi kwa mwonekano. Mabati ya paa lake yalikuwa
yameshika kutu kila mahali na hata aina ya ujenzi wa nyumba ile ulikuwa ni wa mtindo
wa zamani wa Mgongo wa Tembo.
Nilishuka kwenye gari langu na kuelekea kwenye ile nyumba huku nikitarajia
kuiona ile teksi Corolla limited nyeupe ikiwa imeegeshwa pale nje. Sikuiona na hapo
hisia za wasiwasi kuwa huwenda Momba alikuwa ametoka zikanijia huku nikijiuliza
kuwa Momba alikuwa na uhusiano gani na yule mdunguaji hatari. Niliufikia mlango
wa mbele wa ile nyumba na kuanza kugonga hodi. Hakuna mtu aliyeniitikia na ule
mlango ukanitazama kama uliokufa.
Baada ya kugonga sana bila kujibiwa nikaamua kuzunguka na kuchungulia
kwenye dirisha moja la ile nyumba. Hata hivyo ilikuwa kazi bure kwani mle ndani
hapakuonesha dalili za uwepo wowote wa kiumbe hai.
Muda mfupi uliofuata nilikuwa ndani ya ile nyumba kwa msaada wa funguo zangu
malaya. Sebule ya nyumba ile ilikuwa na samani chakavu zisizokuwa na mpangilio
unaoeleweka na hali ile ikanitanabaisha kuwa huwenda Momba alikuwa akiishi maisha
ya ukapera.
Upande wa kushoto na sebule ile kwenye kona kulikuwa na chupa nyingi za
bia zilizotumika. Nilipotazama juu ya meza ndogo chakavu iliyokuwa pale sebuleni
nikaiona simu ndogo ya mkononi. Moyo wangu ukapiga kite kwa nguvu. Fikra zangu
zikanieleza kuwa simu ile haikuwa imesahaulika kwa namna ilivyokuwa imetelekezwa
pale juu ya meza.
”Kitu gani kinachoendelea?” nilijiuliza huku akili yangu ikishikwa na mduwao.
Wakati nikiendelea kuwaza mara ile simu pale juu ya meza ikaanza kuita. Nilisimama
nikiitazama ile simu kwa mshangao huku shughuli za mwili wangu zikiwa zimesimama
kwa sekunde kadhaa. Hisia zangu zikaniambia kuwa lile lilikuwa ni tukio la hila hata
hivyo sikuweza kufahamu kuwa ile ilikuwa ni hila ya namna gani.
Namba iliyokuwa ikiita kwenye simu ile ilikuwa ngeni na yenye tarakimu tano tu
na haikuelekea kufanana na namba za simu zitumikazo nchini Tanzania. Niliendelea
kuipuuza ile simu na kuiacha iendelee kuita huku nikiyatembeza macho yangu mle
ndani kuchunguza.
Kwa kuwa nilikuwa nguli wa shughuli za kijasusi ndani ya muda mfupi chini ya ule
mlango wa sebuleni kwenye kitasa nikaona kidude kidogo mfano wa kifungo cheusi
cha nguo kilichokuwa kimebandikwa. Niliukaribia vizuri ule mlango na kuinama
nikikichunguza kwa ukaribu kidude kile na hapo nikajikuta nikitabasamu.
Kile kidude kidogo mfano wa kifungo cheusi cha nguo kilikuwa ni kifaa kidogo
chenye nguvu kubwa ya kunasa mawimbi ya sauti na kuyasafirisha maelfu ya maili.
Kifaa kile kilikuwa kimepandikizwa pale mlangoni ili mtu yoyote akiingia mle ndani
kifaa kile cha mawasiliano kiweze kunasa mawimbi ya sauti na kuyapeleka kwa
mhusika aliyekiweka pale kifaa kile kwa hila.
”Blood fool!” nilijisemea na mara hii ile simu pale juu ya meza ilikata na kuanza
kuita tena. Safari hii nilisogea pale mezani nikaichukua ile simu na kubofya kitufe cha
kupokelea pasipo kuongea neno lolote.
“Rafiki yako yupo nyuma ya jengo la BML Contractors,Tabata relini” sauti tulivu ya
kiume ikaongea kutoka upande wa pili wa ile simu.
“Wewe mwoga ni nani?” nilimuuliza yule mtu kwa shauku huku nikiinakili vizuri
sauti yake kichwani. Hata hivyo yule mtu hakunijibu na badala yake ile simu ikakatwa.
Nikiwa bado nimeishikilia ile simu sikioni nikajikuta nimeshikwa na mduwao
huku fikra zangu zikienda mbali zaidi kutafuta majibu ya maswali chungu mzima
yaliyokuwa yakipita kichwani mwangu. Nilihisi kuwa kwa vyovyote mtu yule aliyepiga
ile simu alikuwa akitaka kucheza na akili yangu na kunitia woga usiokuwa na maana.
Lakini hadi kufikia pale nilikuwa nimechoshwa na michezo ya namna ile.
Nilimkumbuka yule mdunguaji na kumeza funda kubwa la mate. Ghadhabu
zilinipanda hivyo nikaichomoa bastola yangu kutoka mafichoni na kuitazama kwa
makini kisha nikairudisha mahala pake.
Ile simu ya mkononi nikaipigiza ukutani huku roho ya utulivu ikiwa imenitoweka
kabisa. Niliufikia ule mlango na kukinyofoa kile kifaa cha kunasia mawimbi ya sauti
kisha nikakitupa chini sakafuni na kukisaga kwa soli ngumu ya kiatu changu.
Mche wa sigara ukiwa unateketea taratibu kwenye pembe ya mdomo wangu
nilitoka nje ya nyumba ile na kuelekea sehemu nilipokuwa nimeegesha gari langu.
Muda mfupi uliyofuata nilikuwa njiani nikielekea eneo la Tabata relini.
_____
BAADA YA FOLENI KUBWA YA MAGARI kupungua kwenye barabara ya
Sam Nujoma na ile barabara ya Nelson Mandela hatimaye nikafika eneo la Tabata relini.
Sikuwa mwenyeji sana wa eneo lile hivyo ikabidi niulize kwa watu mahali lilipokuwa
jengo la BML Contractors.
Watanzania ni watu wakarimu sana. Maelekezo ya wapita njia yakiniridhisha kuwa
jengo lile lilikuwa umbali mfupi baada ya kuupita uzio wa ukuta wa ofisi za Mwananchi
Communication. Hivyo niliingia upande wa kulia nikiambaa na barabara ya vumbi
iliyokuwa ikipakana na ukuta wa ofisi za Mwananchi Communication huku macho yangu
mara kwa mara yakitazama vioo vya gari vya ubavuni katika kutaka kujiridhisha kuwa
hakukuwa na mtu yeyote aliyekuwa amenifungia mkia.
Nyuma ya lile jengo la Mwananchi Communication umbali mfupi kutoka pale kulikuwa
na gereji bubu na katika gereji ile kulikuwa na magari mengi yaliyoegeshwa. Magari
yale mengi yalikuwa ni malori makubwa ya kubebea mizigo ya kwenda mikoani na
nchi za jirani yenye matela makubwa.
Niliingia kwenye gereji ile na kuegesha gari langu. Kijana mmoja fundi wa gereji ile
aliyevaa mavazi ya kazi yenye madoa makubwa ya mafuta machafu ya gari akanikaribia
huku akionekana kuchangamkia fursa.
“Ongeza upepo wa kutosha kwenye magurudumu yote” nilimwambia yule kijana.
“Ondoa shaka!” kijana yule akaongea kwa furaha na wakati alipokuwa akitathmini
ujazo wa upepo kwenye yale magurudumu ya gari langu nikamtumbukizia swali.
“Jengo la BML Contractors liko wapi?”
“Endelea mbele na hii barabara uliyokujanayo na ukifika mbele kidogo utaona
mteremko na upande wa kushoto kuna godauni la wachina. Mwisho wa godauni hilo
kuna kichochoro upande wa kushoto. Fuata kichochoro hicho mwisho utatokezea
kwenye reli. Ukivuka hiyo reli mbele yako utaliona hilo jengo la BML Contractors”
“Ahsante! sana fanya kazi yako. Wacha mimi ninyooshe miguu kidogo nitarudi
muda siyo mrefu” nilimwambia yule kijana.
“Usihofu tajiri wangu” yule kijana akaitika huku akielekea kuchukua pampu ya
upepo.
Nililiacha gari langu kwenye gereji ile kisha nikashika uelekeo wa ile barabara ya
vumbi inayoelekea kule mbele kama alivyonielekeza yule kijana wa gereji. Niliendelea
kutembea na baada ya safari fupi nikaanza kushuka mteremko hafifu. Nilipokuwa
nikishuka mteremko ule upande wa kushoto nikaliona jengo refu la godauni ya
wachina. Mwisho wa goduani ile nikakiona kichochoro upande wa kushoto.
Bila kupoteza muda nikaingia kwenye kichochoro kile kilichofanywa baina ya
kuta mbili ndefu. Mwisho wa kichochoro kile kirefu chenye giza hafifu nikaiona reli
ikikatisha mbele yangu. Maelekezo ya yule kijana yalikuwa sahihi hivyo nikakatisha
kwenye reli ile na nilipokuwa nikikatisha kwenye ile reli mbele yangu nikaliona jengo
kubwa la BML Contractors.
Kuliona jengo lile kukanipelekea niipapase vyema bastola yangu mafichoni.
Niliifuata ile reli huku hatua zangu zikipungua na nilipofika mbele nikachepuka upande
wa kushoto na hapo nikawa nimetokezea nyuma ya lile jengo la BML Contractors.
Kama yalivyokuwa maeneo mengi ya kampuni za ujenzi jengo lile la BML
Contractors lilikuwa limezungushiwa uzio wa mabati yaliyoandikwa jina la kampuni
ile ya ujenzi. Uzio ule hafifu kwenye baadhi ya vipenyo vyake viliniwezesha kuona
ndani. Baadhi ya wafanyakazi wa kampuni ile walikuwa wakiendelea na shughuli zao.
Malori makubwa ya kokoto yalikuwa yameegeshwa huku winchi ndefu na mashine za
kuchanganyia zege zikiwa zinaendelea na kazi. Hali ile ikanitanabaisha kuwa nilikuwa
kwenye eneo sahihi.
Sasa fikra zangu zikaanza kufanya kazi huku nikiyatembeza macho yangu
kupeleleza eneo lile. Lilikuwa ni eneo lenye magari mabovu na mabaki ya mashine
mbovu za ujenzi. Nikasimama nikiendelea kulipeleleza eneo lile huku macho
yangu yakitarajia kumuona yule mtu niliyezungumza naye kwenye simu. Lakini hilo
halikutokea badala yake moshi wa takataka chache ulikuwa ukifukiza eneo lile.
Kabla ya kuendelea mbele zaidi nililichunguza jengo la ghorofa lililokuwa
limepakana na eneo lile. Lilikuwa jengo fupi chakavu la ghorofa sita na hapo wazo
fulani likachipuka akilini. Jengo lile lingeweza kumhifadhi mtu yeyote ambaye kwa
wakatu huu huwenda angeitumia nafasi ile kuzichunguza nyendo zangu. Hisia
zile zikaniongezea umakini zaidi na hapo nikaanza kuzitupa hatua zangu taratibu
nikilikagua eneo lile.
Nilizipita mashine mbovu za ujenzi zilizotelekezwa eneo lile nikiruka baadhi ya
vifusi vya mabaki ya ujenzi huku nikiyatembeza macho yangu huku na kule. Sikutaka
kuishika bastola yangu mkononi kwani kwa kufanya vile ningeweza kumjengea hoja
mtu yoyote ambaye angekuwa eneo lile akinitazama. Niliyapita magari mabovu mawili
yaliyokuwa eneo lile na wakati nikilikaribia gari jingine bovu nikasikia kelele hafifu za
mnyama akichakura nyuma ya gari lile bovu. Nikapiga moyo konde na kulisogelea lile
gari kwa nyuma.
Nilichokiona nyuma ya gari lile kikapelekea kwa sekunde kadhaa shughuli za mwili
wangu zisimame. Mwili wa mwanaume mmoja ulikuwa umekaa chini huku mgongo
wake ukiwa umeegemea lile gari bovu kwa nyuma. Ingawa sura ya yule mtu ilikuwa na
majeraha mengi usoni na damu nyingi iliyoganda katika majeraha yake lakini niliweza
kuukadiria umri wake kuwa ulikuwa ni kati ya miaka thelathini na nane na arobaini
na mbili.
Mwanaume yule mwenye afya njema alikuwa amenyongwa kwani nilipomchunguza
vizuri nikagundua kuwa mikono na miguu yake ilikuwa imefungwa na kukazwa kwa
waya mwembamba lakini imara kiasi cha kuzipelekea sehemu zile kwenye mwili
wake zivimbe na kuwamba. Mdomo na macho yake vilikuwa wazi na inzi wakubwa
walikuwa wakitabaruku.
Nikaokota jiwe na kuwafurusha mbwa koko wawili waliokuwa wakiitafuna miguu
yake iliyokuwa wazi. Yule mtu kifuani alikuwa wazi huku chini akiwa amevaa suruali
nyeusi.
Alikuwa mwanaume mwenye afya na nilipoichunguza shingo yake iliyovimba
nikauona waya mwembamba kama ule uliokuwa umefungwa kwenye miguu na
mikono yake ukiwa umeizingira shingo yake. Hali ile ikanifanya nihitimishe kuwa mtu
yule alikuwa amenyongwa hadi kufa.
Ingawa nilikuwa simfahamu yule mtu lakini hisia zangu zikanitanabaisha kuwa
macho yangu yalikuwa yakimtazama Momba. Hasira zikanipanda hata hivyo sikuwa
na namna ya kufanya huku roho ikiniuma sana.
Pembeni ya mwili ule niliiona simu ya mkononi kama ile niliyoiona juu ya meza
kule sebuleni kwa Momba na sasa simu ile ilikuwa imeanza kuita tena. Niliitazama
simu ile kwa hasira nikishawishika kutaka kuichukua lakini roho yangu ilinikataza
huku hisia zangu zikiniambia kuwa nigeuke nyuma na kutazama kule juu ya lile jengo
la ghorofa lililokuwa jirani na eneo lile.
Nilikuwa sahihi kwani ilianza risasi moja iliyoniparaza bega langu la kushoto huku
nikiitumia bahati ile kujitupa chini kisha nikajiviringisha na kujibanza kwenye kona ya
lile gari bovu nikiwa nimeshikwa na taharuki ya aina yake.
Mvua ya risasi ikaanza kurindima upande ule huku risasi hizo zikitoba bodi la lile
gari bovu nililokuwa nimejibanza. Nikajitahidi kuzikwepa risasi zile kwa kuhama hapa
na pale nikienda upande wenye afadhali.
Kutoka pale nilipokuwa hadi lilipokuwa gari bovu jingine hapakuwa na umbali
mrefu hata hivyo nilijionya kuwa endapo ningeendelea kujibanza eneo lile hatimaye
zile risasi zingenifikia. Zile risasi ziliendelea kurindima na wakati huo niliendelea
kujibanza huku nikitafuta upenyo mzuri wa kumchunguza adui yangu.
Mara nikawa nimepata uwazi mdogo ulioniwezesha kuona kule juu ya lile jengo
la ghorofa. Wanaume watatu walikuwa wemejibanza kwenye ukingo wa ghorofa
lile wakiendelea kufyatua risasi pale nilipokuwa. Angalau nikaridhika kuwa yule
mdunguaji hakuwa miongoni mwao. Nikaendelea kuwatazama wale watu huku akili
yangu ikisumbuka katika kutafuta namna ya kujinasua.
Umbali uliokuwa baina yangu na wale watu ulikuwa mrefu hivyo sikupata nafasi
nzuri ya kuziona sura zao. Kwa kweli sikupenda kuendelea kuwepo eneo lile kwani
zile risasi zingeweza kuwavuta watu na dhana ya kuwa mimi nilikuwa jambazi
ingeweza kuibuliwa hasa baada ya kukutwa pale na ule mwili wa Momba. Baada ya
hapo nilifahamu kuwa raia wasingekubali kuniachia hivyo sikutaka kusubiri.
Haraka nikajilaza pale chini kisha nikaanza kutambaa nikilitoroka eneo lile
kuelekea kwenye kifusi cha mabaki ya ujenzi kilichokuwa jirani na eneo lile. Kwa
kuwa nilikuwa nikitambaa kwa kuufuata ule usawa wa lile gari bovu wale watu juu ya
lile jengo la ghorofa walikuwa hawajaniona hivyo wakawa wakiendelea kufyatua risasi
zao ovyo bila malengo.
Nilikifikia kile kifusi na kujibanza nyuma yake huku nikipata nafasi nzuri ya
kulichunguza tena eneo lile. Kutoka pale kwenye kile kifusi na lilipokuwa gari jingine
bovu kulikuwa na umbali mfupi hivyo nikapiga tena mahesabu ya kulifikia lile gari.
Nikakusanya nguvu kisha kwa kasi ya ajabu nikakimbia na kwenda kujibanza nyuma
ya lile gari bovu.
Nikiwa nyuma ya lile gari bovu nikahisi kuwa angalau nilikuwa sehemu salama
kidogo kwani kutoka kwenye lile gari bovu nililojibanza eneo lililofuatia lilikuwa na
vichaka hafifu cha miti midogo na baada ya kulivuka eneo lile ningekuja kutokezea
kwenye ile reli.
Mahesabu yangu yalipokamilika nikaliacha lile gari bovu na kuanza kukimbia
nikitokomea kwenye kile kichaka na nilipokuja kuibuka upande wa pili nikawa
nimetokezea kwenye ile reli.
Baadhi ya wapita njia kwenye ile reli walinishangaa wakati nikijitokeza kutoka
kwenye kile kichaka hata hivyo sikuwatilia maanani badala yake nikawa natembea
kuelekea mbele nikiifuata ile reli. Wakati nikiendelea kutembea kwa mbali niliendelea
kuisikia ile milio ya risasi kule nyuma yangu. Mara nikajikuta nimechanganya miguu
na kuanza kukimbia nikielekea kwenye lile jengo la ghorofa walipokuwa wale watu
wakinifyatulia risasi.
Niliendelea kukimbia na ndani ya muda mfupi tu nikawa nimelifika lile jengo la
ghorofa na nilipolichunguza vizuri nikagundua kuwa jengo lile lilikuwa halitumiki
kutokana na taratibu ujenzi wake kuwa zimekiukwa. Sasa nilikuwa na hakika kuwa
tukio lile lote lilikuwa limepangwa.
Nilichokuwa nimepanga sasa ilikuwa ni kuingia ndani ya lile jengo la ghorofa na
kupanda kule juu walipokuwa wamejibanza wale watu ili nikawafanyie shambulizi
la kushtukiza. Lakini nilipokuwa katika harakati za kufanya vile mara nikajikuta
nikishtushwa na muungurumo wa gari lililokuwa likija kwa kasi kwenye lile jengo.
Tukio lile likanipelekea haraka niirudishe mafichoni bastola yangu niliyokuwa
nimeishika mkononi nikilikaribia lile jengo. Muungurumo ule wa gari ulizidi kusikika
ukija upande ule wa ghorofa na tukio lile likanipelekea nijibanze kwenye ukuta wa
jengo lile.
Nikiwa naendelea kuchungulia kule mbele mara nikaliona gari la polisi aina ya
Landcruiser likichomoza kwa kasi na kushika breki kali mbele ya lile jengo la ghorofa.
Askari wanne wenye bunduki mikononi mwao wakawahi kuruka chini katika mtindo
wa aina yake hata kabla ya gari lile halijasimama vizuri.
Haikunichukua muda mrefu kufahamu kuwa mara ile tena nilikuwa nimezidiwa
ujanja kwani uwezekano wa kutekeleza adhama yangu usingewezekana tena baada ya
wale polisi kufika eneo lile. Niliendelea kuwatazama wale polisi ambao sasa nilihisi
kuwa huwenda walikuwa wamepigiwa simu na msamaria mwema baada ya kusikika
kwa ile milio ya zile risasi zilizokuwa zikifyatuliwa na wale watu waliokuwa kule juu ya
lile jengo ghorofa.
Kitendo cha kumuona polisi mmoja akija kwenye ule ukuta niliojibanza
kikanipelekea niyaache taratibu maficho yale na kupotelea vichakani nikilikimbia
eneo lile huku jinamizi la kuzidiwa ujanja kwa mara nyingine likiendelea kuniandama.
Nilipenda nibaki eneo lile ile niweze kuona mwisho wa tukio lile lakini fikra zangu
zikanionya kuwa ile haikuwa sehemu salama tena kwangu.
Nilirudi kwenye ile gereji huku nikiwa nimekata tamaa sana na mwenendo
wa harakati zangu kwani tangu nianze kazi yangu sikuwahi kukutana na vizingiti
vya sampuli ile vinavyonifanya nikose hata sehemu ya kuanzia yenye chanzo cha
kuaminika.
Wakati nikimpa yule kijana malipo yake aliduwaa akishangazwa na kuchafuka
kwangu kuliko sababishwa na zile rabsha za kule nilipotoka. Hata hivyo sikushtushwa
na hali ile badala yake nilimuacha yule kijana akiendelea kunishangaa huku nikifungua
mlango wa gari langu na kuingia ndani. Muda mfupi uliyofuata nikageuza gari langu
na kushika uelekeo wa barabara ya Mandela.
 
MVUA KUBWA ILIYOKUWA IMEANZA KUNYESHA tena ilikuwa
imefanikiwa kuwafukuza watu katika barabara za mitaa ya jiji la Dar es
Salaam na hivyo kupelekea idadi ya magari barabarani iongezeke maradufu
kiasi cha kusababisha kero kubwa ya foleni.
Taarifa kupitia vituo mbalimbali vya redio zilikuwa zimejikita zaidi katika maafa
ya mvua ile kama;mafuriko katika baadhi ya maeneo,uharibifu wa miundombinu ya
barabara,mali na vifo vya watu. Wananchi waliojenga mabondeni waliendelea kuitupia
lawama serikali huku wajibu wao wa kuhama mabondeni wakiufumbia macho.
Labda serikali ilikuwa na sehemu yake ya kulaumiwa kwa uwepo wa miundombinu
mibovu ya maji taka na barabara kama siyo kuufumbia macho ujenzi wa makazi holela
ya watu katika baadhi ya maeneo. Kila mmoja alistahili lawama kwa upande wake.
Taarifa juu ya athari za mvua ile ziliendelea kumfikia Koplo Tsega kupitia redio ya
gari. Alikuwa ameegesha gari lake mkabala na ofisi za wizara ya ulinzi na mambo ya
ndani nyuma kidogo ya makutano ya barabara za mtaa wa Ghana na ule mtaa wa Ohio
eneo la posta jijini Dar es Salaam.
Mvua kubwa iliyokuwa ikinyesha ilikuwa imepelekea maji mengi kutuama
barabarani. Maji ambayo kwa hakika hayakustahili kutuama endapo miundombinu
mizuri ya majitaka ingekuwepo kuyatapisha maji yale kwenye bahari ya Hindi ilikuwa
umbali mfupi kutoka pale.
Kitendo cha Koplo Tsega kuegesha gari lake Corolla limited nyeupe yenye kibandiko
cha teksi juu yake na ufito wa njano ubavuni sambamba na mvua kubwa iliyokuwa
ikiendelea kunyesha kilikuwa kimepelekea usumbufu mkubwa wa mara kwa mara
kugongewa vioo madirishani na watu waliokuwa wakihitaji huduma ya usafiri. Kazi
yake ikawa ni kuwajibu watu wale kuwa kuna mtu aliyekuwa akimsubiri.
Kero hiyo ilipozidi Koplo Tsega hakujishughulisha kuwajibu watu hao badala yake
akapandisha na kufunga vioo vya gari. Hivyo mtu yeyote aliyegonga alimpuuza huku
macho yake yakiendelea kutazama kwenye mlango wa mbele wa kutokea kwenye lile
jengo la wizara ya ulinzi na mambo ya ndani.
Tangu ilipotimia saa tisa alasiri Koplo Tsega alikuwa ameegesha gari lake eneo lile
huku macho yake yakiendelea kutazama mbele ya ule mlango wa lile jengo. Tangu
saa tisa alasiri na sasa ilikuwa imetimia saa tatu usiku akiendelea kusubiri ndani ya gari
lile lakini bado alikuwa hajakata tamaa. Alikuwa akimsubiri mtu mmoja aliyefahamika
kwa jina la Pierre Kwizera.
Kama Koplo Tsega asingekuwa ameliona gari la Pierre Kwizera Landcruiser V8
likiwa limeegeshwa kwenye eneo la maegesho la ofisi zile basi huwenda angekuwa
tayari amekata tamaa na kuondoka zake. Lakini kwa sasa uwepo wa gari lile ulikuwa
umemfanya aendelee kuwa mvumilivu akisubiri. Mara kwa mara akajikuta akitazama
kwenye mlango ule kila alipomuona mtu fulani akitoka kwenye lile jengo. Pierre
Kwizera bado hakuonekana.
Usiku huu wa saa tatmwinginea magari yalikuwa yamepungua sana kwenye
maegesho ya ofisi zile. Masaa ya kazi yalikuwa yamefika ukomo kwa siku ile hivyo
kila mfanyakazi aliyetoka kwenye lile jengo alielekea sehemu alipoegesha gari lake na
kuondoka. Pierre Kwizera hakuwa miongoni mwao.
Katika magari machache yaliyokuwa yameegeshwa kwenye eneo la maegesho
ya magari la ofisi zile gari la Pierre Kwizera lilikuwepo. Hivyo uwepo wa gari lile
ukampelekea Koplo Tsega aamini kuwa kulikuwa na wafanyakazi wengine wachache
waliokuwa wamesalia ndani ya lile jengo huku Pierre Kwizera akiwa miongoni mwao.
Koplo Tsega akaendelea kujipa moyo wa uvumilivu na wenye subira.
Haikuwa mpaka ilipofika saa nne usiku pale mwanaume mrefu na mwenye mwili
mpana alipojitokeza kwenye mlango ule wa kutokea nje ya ofisi za wizara ya ulinzi
na mambo ya ndani huku akiwa amevaa suti nadhifu nyeusi na begi dogo la ngozi
mkononi.
Macho ya Koplo Tsega yakarejewa na uhai wakati yalipomtazama mtu yule
akitoka kwenye ule mlango. Mara yule mtu alipotoka akasimama kidogo kwenye
baraza ya jengo lile huku akiitazama saa yake ya mkononi. Kisha akaanza kutembea
akishuka ngazi kueleka kwenye sehemu ya maegesho ya magari ya jengo lile huku
akiwa ameufyatua mwamvuli kujikinga na mvua iliyokuwa ikiendelea kunyesha.
Koplo Tsega alipomchunguza vizuri yule mtu haraka akagundua kuwa alikuwa ni
Pierre Kwizera na hapo tabasamu jepesi likajipenyeza usoni mwake. Pierre Kwizera
alitembea kwa kujiamini akielekea sehemu alipokuwa ameegesha gari lake.
Koplo Tsega hakutaka kuendelea kusubiri hivyo akashusha kioo cha mlango
wa gari hadi pale alipopata upenyo mzuri wa kuupitisha mdomo wa sniper rifle-338
Lapua Magnum. Kisha haraka akairekebisha lensi ya darubini ya bunduki yake huku
akiwa amelifinya jicho lake moja. Taswira ya kichwa cha Pierre Kwizera ilipoenea
vizuri kwenye msalaba wa shabaha wa darubini yake akavuta pumzi nyingi na kuibana
kifuani.
Koplo Tsega alipokuwa akijiandaa kuvuta kilimi cha bunduki ili ahitimishe safari
ya Pierre Kwizera akajikuta akisita kufanya hivyo baada ya mtu fulani kuanza kugonga
kioo cha dirishani cha gari lake. Tukio lile likamshtua na kumpelekea amlaani sana
mtu yule. Hivyo akaiondoa haraka bunduki yake na kuificha nyuma ya kiti chake cha
dereva.
Mwanaume mmoja aliyekuwa akigonga upande wa pili kwenye kioo cha gari lile
alikuwa akiulizia usafiri wa teksi kuelekea eneo la Magomeni Mikumi. Koplo Tsega
akashusha kioo cha gari akimtazama mwanaume yule na bila kuzungumza neno
akapandisha kioo kile cha gari na kukomelea kabari ya mlango.
Wakati Koplo Tsega akiyapeleka tena macho yake kumtazama Pierre Kwizera
kwenye yale maegesho ya magari hakumuona na badala yake akaliona lile gari la Pierre
Kwizera likaacha maegesho ya magari ya eneo lile na kuingia barabarani.
Koplo Tsega hakuwa na namna ya kufanya kwani alikuwa na kila hakika kuwa
jaribio lake la kwanza lilikuwa limeshindikana hivyo akajipa subira kidogo huku
akiliacha gari lile Landcruiser V8 liache maegesho yale na kuingia barabarani. Muda
mfupi uliyofuata Koplo Tsega akawasha gari lake na kuingia barabarani akilifungia
mkia lile gari kwa nyuma.
Uelekeo wa ile Landcruiser V8 ukamtanabaisha Koplo Tsega kuwa Pierre Kwizera
alikuwa akielekea nyumbani kwake eneo la Upanga. Foleni ya magari ilikuwa imepungua
kwenye barabara nyingi za jiji la Dar es Salaam hivyo lile gari Landcruiser V8 lilikuwa
likikata upepo barabarani pasipo pingamizi lolote. Koplo Tsega akajitahidi kwa kila
hali akihakikisha gari lile halimpotei.
Koplo Tsega akaendelea kulifuatilia gari lile kwa nyuma wakati lilipokuwa likiingia
barabara ya mtaa mmoja na kutokezea kwenye barabara ya mtaa mwingine huku
safari ikiendelea.
Mvua kubwa ilikuwa ikiendelea kunyesha sambamba na giza zito lililokuwa
limetanda angani hata hivyo macho ya Koplo Tsega hayakuacha kulitazama lile gari
la Pierre Kwizera mbele yake wakati lilipokuwa likiacha barabara ya mtaa mmoja na
kuingia barabara ya mtaa mwingine. Baada ya safari ndefu hatimaye wakafika eneo la
Upanga.
Baada ya kuzipita nyumba kadhaa za ghorofa za shirika la nyumba la taifa mara lile
gari Landcruiser V8 likabadili uelekeo na kuingia wa upande wa kulia lilikatisha katika
barabara pana ya lami. Barabara ile ilikuwa ikikatisha katikati ya majumba makubwa ya
kifahari yenye kuta ndefu zenye sistimu maalum ya umeme wa kuzuia wezi. Ndani ya
uzio wa nyumba zile sauti ya mbwa wakali wakibweka zilikuwa zikisika.
Mara kwa mara Koplo Tsega alilazimika kupunguza mwendo baada ya kuliona
gari lile Landcruiser V8 likipunguza mwendo katika nyakati tofauti. Hatimaye lile gari
likakata kona na kuelekea upande wa kushoto likikatisha katika mtaa tulivu wenye
barabara pana ya lami inayotazamana na mageti makubwa ya majumba ya kifahari.
Lile gari Landcruiser V8 hatimaye likaenda kusimamia mbele ya geti la nyumba ya
tano ya mtaa ule. Huwenda mwanga wa taa za gari lile ulikuwa umemshutua mlinzi
wa ile nyumba hata kabla honi ya gari haijapigwa. Kwani haukupita muda mrefu
lile geti likafunguliwa na mlinzi na lile gari taratibu likaingia mle ndani. Koplo Tsega
akapunguza mwendo wa gari lake huku akilitazama lile gari Landcruiser V8 wakati
likiingia kwenye ile nyumba. Wakati akipita mbele ya lile geti mlinzi wa ile nyumba
ndiyo alikuwa anamalizia kufunga lile geti hivyo Koplo Tsega akafanikiwa kuona
kwa sehemu tu ya mandhari ya mle ndani. Mara lile geti lilipofungwa Koplo Tsega
akakanyaga mafuta na kuendelea na safari na kwenda kuegesha gari lake mwisho wa
barabara ile sehemu yenye kona ya kuingia barabara ya mtaa unaofuata.
Mlinzi akakisogeza kifuniko kidogo cha getini na kuchungulia nje kupitia tundu
dogo huku akishangazwa kidogo na utaratibu uliotumika na mgeni yule wa kugonga
geti badala ya kubofya kitufe cha kengele kilichokuwa pembeni ya geti lile ukutani.
Kitendo cha kumuona msichana mrembo akiwa amesimama nje ya geti lile
kikamtoa wasiwasi hivyo akaufunga ule mfuniko wa lile tundu kisha akasogea pembeni
na kufyatua komeo la mlango mdogo wa geti lile kumruhusu mgeni yule kuingia.
Mara tu mlango ule mdogo wa geti ulipofunguliwa Koplo Tsega akaitumia nafasi ile
kujikaribisha mle ndani. Mlinzi wa nyumba ile hakupata muda wa kufanya mahojiano
na Koplo Tsega kwani kufumba na kufumbua akapigwa mapigo matatu Smart ya
chapuchapu ya Karate. Mapigo mawili kifuani na pigo moja funga kazi la shingoni na
hapo shughuli za mwili za mlinzi yule zikasimama huku uzito ukimuelemea. Mlinzi
yule akafumba macho yake taratibu na kuanguka chini mzima mzima hata hivyo
Koplo Tsega akawahi kumdaka kabla hajafika chini kisha akamburuta hadi nyumba
ya kibanda chake cha kazi kilichokuwa kando ya lile geti.
Sauti za mbwa waliokuwa wakibweka zilisikika mle ndani hata hivyo Koplo Tsega
alipochunguza vizuri akagundua kuwa mbwa wale walikuwa ndani ya banda lililokuwa
nyuma ya kile kibanda cha mlinzi.
Jumba kubwa la kifahari lilikuwa limepandwa katikati ya uzio ule huku likiwa
limezungukwa na bustani ya maua mazuri na miti ya kuvutia. Lile gari Landcruiser V8
halikuonekana nje ya lile jumba lakini uwepo wa banda la kuegeshea gari lililokuwa
kando ya lile jumba ukaashiria kuwa lile gari lilikuwa limeingizwa ndani ya lile banda
muda mfupi uliyopita.
Taa ya sebuleni kwenye lile jumba ilikuwa ikiwaka ingawa mapazia mazito
yaliyokuwa madirishani hayakuruhusu mtu yoyote kuona kwa urahisi mle ndani.
Koplo Tsega akapanda ngazi za barazani na kuusogelea mlango wa mbele wa lile
jumba huku akizitupa hatua zake kwa utulivu. Hali ilikuwa shwari na dalili zikaonesha
kuwa ndani ya ile sebule hakukuwa na mtu yoyote hivyo Koplo Tsega akakishika
kitasa cha mlango ule wa mbele na kuusukuma ndani taratibu. Ule mlango ulikuwa
wazi hivyo hapakuwa na upinzani wowote.
Koplo Tsega alipoingia ndani akajikuta akitazamana na sebule kubwa yenye
samani za kisasa kama seti mbili za makochi makubwa ya sofa juu ya zulia la manyoya
laini la rangi ya kijivu. Katikati ya sebule ile kulikuwa na meza fupi lakini pana ya mti
wa mpingo. Upande wa kushoto kulikuwa na rafu kubwa ukutani iliyopangwa aina
tofauti za vitabu. Ukutani kulitundikwa picha nzuri za kuchorwa zinazovutia. Upande
wa mbele wa ile sebule kulikuwa na runinga pana juu ya meza fupi ya kioo iliyopakana
na kabati dogo lenye droo nne.
Pierre Kwizera hakuwepo pale sebuleni wala lile begi lake alilotokanalo ofisini na
badala yake jumba yote lilikuwa kimya hali ile ikiashiria kuwa Pierre Kwizera alikuwa
akiishi peke yake mle ndani.
Akiwa amejiridhisha kuwa Pierre Kwizera hakuwepo pale sebuleni Koplo Tsega
akaurudishia mlango wa pale sebuleni nyuma yake kisha akaichomoa bastola yake
kutoka mafichoni na kuikamata vyema mkononi. Ukimya wa mle ndani ukampelekea
ayasikilizie mapigo hafifu ya moyo wake yalivyokuwa yakihangaika ovyo kifuani
mwake.
Sehemu fulani ndani ya nyumba ile mlango ukasikika ukifunguliwa na kisha
kufungwa halafu baada ya hapo zikasikika hatua tulivu za mtu akitembea kuja pale
sebuleni. Mtu yule alikuwa ni Pierre Kwizera na wakati huu alikuwa amebadili mavazi
yake. Pierre Kwizera alikuwa amevaa suruali ya pajama na fulana ya mchinjo na
miguuni alikuwa amevaa viatu laini vya manyoya.
Pierre Kwizera akaendelea kutembea kwa kujiamini na alipofika pale sebuleni
akaelekea mlangoni ambapo aliufunga mlango ule kwa funguo. Alipomaliza akaelekea
kwenye madirisha ya pale sebuleni na kusogeza vizuri mapazia katika namna ya
kufunika sehemu zote zilizokuwa wazi. Hatimaye akaelekea kwenye makochi
yaliyokuwa pale sebuleni na kuwasha runinga huku akiketi kwenye kochi moja kati ya
makochi mengi yaliyokuwa eneo lile. Pierre Kwizera akiwa ameketi kwenye kochi lile
ghafla akahisi kuwa chuma cha baridi kilikuwa kikikigusa kisogo chake kwa nyuma.
Hali ile ikampelekea Pierre Kwizera ageuke kwa ghafla na kutazama nyuma yake.
Koplo Tsega ambaye alikuwa amejibanza nyuma ya ile rafu ya vitabu pale sebuleni
alikuwa amejitokeza tayari kumkabili Pierre Kwizera pale kwenye kochi. Pierre
Kwizera akageuka kwa ghafla kutazama nyuma yake na mshtuko alioupata baada ya
kumuona Koplo Tsega ukampelekea aduwae kwa muda na kuganda kama sanamu.
Alichokihisi baada ya pale ni kuwa sehemu fulani mwilini mwake jasho jepesi
lilikuwa likianza kutoka. Mapigo ya moyo wake yakasimama kwa sekunde kadhaa
kabla ya kuanza kwenda mbio kama mtu aliyekuwa akifukuzwa na mnyama mkali.
Macho ya mshangao yakamtoka huku koo lake likikauka taratibu na kwa mbali nyuma
ya masikio yake mishipa yake ya damu ilianza kutuna na kusukuma damu kwa kasi hali
iliyompelekea jasho jepesi lianze kushuka kwenye paji lake.
Pierre Kwizera hisia zake zikamueleza kuwa alichokuwa akikiona mbele yake
ulikuwa ni mzimu wa Koplo Tsega na hapo akili yake ikaanza kufanya kazi haraka.
Bastola yake ilikuwa kwenye droo ya tatu ya kabati dogo lililokuwa pembeni ya
runinga pale sebuleni. Kufumba na kufumbua Pierre Kwizera akafanya hila kwa
kulisukuma lile kochi kwa nyuma na hapo bastola ya Koplo Tsega ikamponyoka huku
yeye akijitupa upande ule uliokuwa na lile kabati dogo pale sebuleni kisha akavuta
droo ya tatu na kuichukua bastola yake
Makadirio ya Pierre Kwizera yalikuwa sawia kwani ndani ya muda mfupi akawa
amefanikiwa kulifungua lile kabati na kuichuka ile bastola yake. Lakini Koplo Tsega
hakumpa nafasi Pierre Kwizera ya kutimiza adhma yake kwani bastola ile aliipangusa
na kuitupilia mbali kwa teke lake. Hata hivyo Pierre Kwizera hakuwa mtu rahisi kwani
pigo la pili la teke la Koplo Tsega lilipokuja akawahi kuinama chini akilikwepa kisha
akamchota Koplo Tsega kwa mtama wa aina yake uliomrusha hewani na alipokuwa
mbioni kutua chini akamuwahi na kumtandika pigo la teke la tumbo lililomtupa
ukutani. Kisha Pierre Kwizera akajibetua na kusimama huku amepandwa na ghadhabu.
Koplo Tsega akaugulia maumivu makali ya kipigo kile huku akijilaumu kwa kufanya
makadirio ya chini dhidi ya adui yake. Pierre Kwizera hakumpa nafasi Koplo Tsega
hivyo kabla Koplo Tsega hajasimama pale chini akatupa pigo jingine la teke usawa wa
kichwa chake. Mara hii Koplo Tsega alikuwa mwepesi kujihami akijiviringisha haraka
mara mbili pale sakafuni kulikwepa pigo lile huku damu nyepesi ikimtoka puani.
Pigo jingine la teke la Pierre Kwizera lilipokuja Koplo Tsega akaliona na kulidaka
kwa nguvu zake zote kisha akauzungusha ule mguu na hapo Pierre Kwizera akarushwa
hewani. Lakini Pierre Kwizera hakwenda mbali kwani Koplo Tsega aliwahi kuivuta
fulana yake mchinjo kwa nyuma na kumshindilia mgumi mbili kavu za mgongoni
zilizompelekea abweke kama mbwa huku maumivu makali yakisambaa mwilini
mwake. Pierre Kwizera akayumbayumba akitafuta mhimili hata hivyo alichelewa
kwani teke jingine la Koplo Tsega likamtandika shingoni na kumtupia ukutani.
Pigo jingine la ngumi ya uso lilipomfikia Pierre Kwizera ambaye alishaanza kuona
dalili za kuzidiwa maarifa akawahi kulipangua kisha kwa nguvu zake zote akamsukuma
Koplo Tsega kwenye ile rafu ya vitabu iliyokuwa pale sebuleni. Ile rafu ikaanguka chini
huku vioo vyake vikipasuka na vile vitabu vikitawanyika ovyo pale chini sakafuni.
Koplo Tsega akapiga yowe la hofu kwani vile vioo vilikuwa vimemchana
mikononi. Pierre Kwizera aliwahi kumfikia Koplo Tsega pale chini akamvuta na
kumkaba kabari matata shingoni. Koplo Tsega akajaribu kufurukuta bila mafanikio
kwani Pierre Kwizera alikuwa mtu mwenye nguvu sana. Hata hivyo Koplo Tsega
hakukata tamaa badala yake aliendelea kurusha miguu yake huku na kule akitafuta
namna ya kujinasua. Pierre Kwizera akiwa amelitambua hilo hakumpa nafasi Koplo
Tsega ya kujinasua badala yake akaendelea kuikaza ile kabari na kumbeba juu juu.
“Si unajidai mzimu basi tulia nikuoneshe,ngedere mkubwa we!” Pierre Kwizera
akafoka huku akiendelea kumkaba Koplo Tsega shingoni kiasi cha kumnyima nafasi
nzuri ya kuhema. Koplo Tsega akaanza kupoteza matumaini huku akihema kwa taabu.
Huku akiwa ametoa macho Koplo Tsega akaanza kuhisi wingu jepesi la giza
likitanda mbele yake hata hivyo hakukata tamaa badala yake akaendelea kurusha
miguu yake huku na kule katika namna ya kutaka kujinasua.
Shughuli ilikuwa pevu hata hivyo mikikimikiki ile ikawapelekea taratibu wasogee
karibu na ukuta wa pale sebuleni. Walipoufikia ule ukuta Koplo Tsega akaitumia fursa
ile kuikita miguu yake ukutani kisha akakusanya nguvu za kutosha na kuusukuma
ule ukuta kwa miguu yake. Tukio lile likawarusha wote na kuwabwaga pale sakafuni
kwa kishindo. Pierre Kwizera akapiga yowe kali na hapo akaifungua ile kabari bila
kupenda. Alipotaka kusimama Koplo Tsega akamuwahi kwa kumtandika kiwiko
cha nguvu kilichoupasua mwamba wa pua yake na kumpelekea apige yowe kali la
maumivu kama aliyekalia msumari. Pigo la pili la ngumi lilipomfikia akawahi kuliona
hivyo akalikwepa kwa kujirusha pembeni hivyo pigo la Koplo Tsega likakata hewa
bila majibu.
Pierre Kwizera akiwa bado anaugulia maumivu ya pua huku kamasi za damu
zikimtoka akakusanya nguvu na kusimama hata hivyo akashangaa kujikuta akirudi
tena pale chini bila kupenda.
Koplo Tsega alikuwa ameishtukia haraka dhamira ya Pierre Kwizera hivyo akawa
amemuwahi kwa kumchota mtama wa chini uliompaisha hewani mzobemzobe.
Pierre Kwizera alipokuwa akitua chini akatua juu ya ile meza fupi ya mbao ya mpingo
iliyokuwa pale sebuleni huku mkono wake ukivunjika na hapo akapiga yowe kali la
maumivu.
Koplo Tsega hakumpa Pierre Kwizera nafsi ya kutafakari pale chini kwani
akamuwahi haraka kwa pigo moja madhubuti la judo kichwani. Pierre Kwizera
akatulia kimya akining’inia juu ya meza ile kama mbuzi kwenye kiti cha baiskeli huku
fahamu zikiwa mbali naye.
_____
FAHAMU ZILIPOMRUDIA Pierre Kwizera akajikuta amefungwa kwenye
kiti kikamilifu huku kamba iliyotumika kumfunga ikiwa ni pazia mojawapo la pale
sebuleni. Jicho lake moja lilikuwa limevimba na kuvilia damu. Sehemu ya juu upande
wa kushoto usoni alikuwa amechanika na damu ilikuwa ikiendelea kutoka kwenye
jeraha. Mdomo wake ulikuwa umechanika na jino lake moja lilikuwa limevunjika. Ile
fulana yake mchinjo ilikuwa imeraruka vibaya na kuning’inia kama mikia ya Pweza.
Maumivu ya ule mkono wake uliovunjika yakampelekea ayafumbe macho yake
taratibu huku akizipa uhai fikra zake. Koplo Tsega alikuwa ameketi kwenye kiti mbele
yake akimtazama.
“Unajisikiaje?” Koplo Tsega akamuuliza Pierre Kwizera kwa utulivu huku
akimtazama
“Wewe ni nani?” Pierre Kwizera akauliza kivivuvivu huku bado akiona
maruweruwe.
“Koplo Tsega mdunguaji na askari komandoo wa jeshi la wananchi Tanzania.
Usiniambie kuwa mara hii umenisahau” Koplo Tsega akacheka kwa kicheko hafifu
lakini kilichohifadhi chuki ndani yake.
“Koplo Tsega au mzimu wa Koplo Tsega?” Pierre Kwizera akauliza kwa taabu
huku akipambana na maumivu makali mwilini mwake.
“Koplo Tsega na siyo mzimu wa Koplo Tsega” maelezo ya Koplo Tsega
yakampelekea Pierre Kwizera afungue macho yake vizuri na kumtazama Koplo Tsega
mbele yake. Taswira ya Koplo Tsega ilipojengeka vizuri machoni mwake akashikwa
na mshangao.
“Koplo!...ni wewe?” Pierre Kwizera akauliza kwa mshangao.
“Ndiyo mimi hebu nitazame vizuri” Koplo Tsega akaongea huku akitabasamu
na hapo macho ya Pierre Kwizera yakaweka kituo yakimtazama Koplo Tsega mbele
yake.
“Sasa yule aliyezikwa ni nani?” Pierre Kwizera akauliza kwa mshangao.
“Rafiki yangu”
“Mbona sikuelewi?”
“Ni hadithi ndefu na hicho siyo kilichonileta hapa” maelezo ya Koplo Tsega
yakampelekea Pierre Kwizera azidi kushikwa na mshangao. Kitambo kifupi cha
ukimya kikapita kisha Pierre Kwizera akavunja tena ukimya.
“Sasa una shida gani na mimi hadi univamie usiku huu?” swali la Pierre Kwizera
likampelekea Koplo Tsega atabasamu tena kisha akaingiza mkono mfukoni kuichukua
ile bahasha yenye zile hundi. Koplo Tsega alipoifungua bahasha ile akapekuwa hadi
pale alipoifikia hundi yenye jina la Pierre Kwizera na kuichomoa.
“Nani anayewapa hizi fedha?” Koplo Tsega akavunja ukimya akimuuliza Pierre
Kwizera huku akimuonesha ile hundi yenye jina lake. Pierre Kwizera akaitazama ile
hundi kwa makini na hapo mshangao ukazidi kumshika.
“Nani aliyekupa hundi yangu?” Pierre Kwizera akauliza kwa hamaki.
“Bado hujanijibu swali langu komredi!” Koplo Tsega akaongea kwa msisitizo.
Pierre Kwizera akashikwa na kugugumizi huku akiendelea kuitazama ile hundi kwa
mshangao.
“Sifahamu chochote!” hatimaye akaongea kwa utulivu baada ya kukohoa kidogo.
“Ulikuwa ukitarajia hundi ya namna hii kukufikia?” Koplo Tsega akauliza huku
akiipigapiga ile hundi kwa kidole chake na wakati huo akimtazama Pierre Kwizera
mbele yake. Pierre Kwizera akaitazama tena ile hundi kwa utulivu huku akioneka
kama aliyekuwa njia panda katika kutoa jibu dhidi ya lile swali.
“Ndiyo!..ha..hapana!”
“Mbona hueleweki?”
“Jibu ni ndiyo” hatimaye Pierre Kwizera akaongea kwa kujiamini.
“Okay! tia sahihi yako hapa” Koplo Tsega akamwambia Pierre Kwizera huku
akimpa ile hundi na kalamu ya wino. Pierre Kwizera akaipokea ile hundi kwa taabu
kwani sehemu za mikono yake zilikuwa zimefungwa huku akiwa ameshikwa na
mshangao. Akamtazama Koplo Tsega kwa mashaka kisha akatia sahihi kwenye ile
hundi. Alipomaliza Koplo Tsega akaichukua ile hundi na kuitia kwenye bahasha
kisha ile bahasha akaitika mfukoni huku akimuacha Pierre Kwizera katika mshangao
usioelezeka. Hata hivyo hakuzungumza neno.
“Unaweza kuniambia ulikuwa ukitarajia kupokea hundi hii kutoka kwa nani?”
Koplo Tsega akauliza kwa utulivu baada ya kuiweka ila bahasha mfukoni. Pierre
Kwizera akamtazama Koplo Tsega kwa makini kama ambaye anajutia jibu lake
lililotangulia. Kisha kwa sauti ya uchovu akajitahidi kuzungumza
“Sifahamu chochote kuhusu hiyo hundi!”
“Nilitarajia jibu la namna hiyo kwako hata hivyo natambua kuwa unanidanganya.
Wewe na wenzako mmepewa pesa kwa ajili ya kuniua mimi na Sajenti Chacha Marwa.
Nafahamu kuwa yupo mtu anayewapa hizi fedha na ni afadhali ukamtaja kwani jaribio
lenu limeshindikana” Koplo Tsega akaongea huku uso wake ukiwa mbali na mzaha.
“Mbona sielewi unachosema?” Pierre Kwizera akaongea kwa utulivu huku
mshangao ukishindwa kujificha machoni mwake.
“Utaendelea kujidanganya kuwa huelewi hadi lini komredi wakati ukweli
unaufahamu vizuri?” Koplo Tsega akamuuliza Pierre Kwizera kwa utulivu.
“Koplo mbona unanichanganya kwa habari ambazo sizielewi?” Pierre Kwizera
akauliza huku akionesha kukata tamaa.
“Mtu wenu mliyemtuma hakuwa makini sana” Koplo Tsega akaendelea kuongea
kwa utulivu.
“Mtu gani unayemzungumzia?” Pierre Kwizera akauliza kwa shauku
“Meja Khalid Makame!”
“Nani aliyekwambia?” Pierre Kwizera akauliza kwa mshangao hali iliyompelekea
Koplo Tsega atabasamu kidogo.
“Hakuna mtu aliyeniambia komredi nimejionea mwenyewe kwa macho yangu.
Mtu wenu Meja Khalid Makame hakuwa makini katika kukamilisha mpango wenu na
mimi sikufanya makosa kumchakaza vibaya kwa risasi”
“Mungu wangu! kwa hiyo wewe ndiye uliyemuua Meja Khalid Makame?” Pierre
Kwizera akauliza kwa mshangao.
“Ndiyo! tena nimemuua kwa risasi zangu mwenyewe” Koplo Tsega akajigamba
kwa ghadhabu. Pierre Kwizera akamtazama Koplo Tsega kama ambaye hakumsikia
vizuri lakini ukweli ni kuwa alikuwa amemsikia vizuri Koplo Tsega na jasho jepesi
lilikuwa likianza kumtoka mwilini.
“Oh! my God umefanya nini Koplo?. Kwanini umuue Meja Khalid Makame?”
Pierre Kwizera akauliza kwa hamaki.
“Acha kuigiza komredi. Unadhani mazingira ya kifo cha Meja Khalid Makame
yametawaliwa na hisia?. Sijamuua kwa bahati mbaya na wala sijuti kwa nilichokifanya
kwani ningezembea kidogo angenimaliza na mipango yenu ingeenda sawa. Huwenda
muda huu mngekuwa mkifanya tafrija ya kujipongeza kwenye hoteli moja kubwa ya
kifahari hapa jijini Dar es Salaam” Koplo Tsega akaongea huku akiangua kicheko
hafifu cha dhihaka kisha akaendelea
“Sasa tafrija yenu imeanza kugeuka msiba mzito sana kwani nitawawinda mmoja
baada ya mwingine ili mfidie hasara ya maisha ya watu mliyowaua bila hatia. Kweli
hamna haya na ufedhuli wenu yaani kumbe shughuli zote zile tulizokuwa tukizifanya
kwenye hii tume ni kiini macho tu!. Kama hamkutuhitaji kwanini mlituita?” Koplo
Tsega akacheka tena kwa dhihaka kabla ya kuendelea
“Sasa kaeni chonjo kwani yule msiyemtaka amekuja” Koplo Tsega akaendelea
kuongea huku akicheka kwa dhihaka na hasira.
“Kuwa makini Koplo kwani sasa naanza kuhisi kuwa mapigano ya msituni
yamekuchanganya akili yako vibaya” Pierre Kwizera akaongea kwa hasira huku
akijitahidi kujinanusua kwenye kile kifungo bila mafanikio. Koplo Tsega akaendelea
kucheka na kicheko chake kilipofika ukomo akamkata jicho la hasira Pierre Kwizera
mbele yake.
“Kama isingekuwa bahati mbaya basi muda huu ungekuwa unatafutiwa sanduku
zuri la mzishi yako huku wataalam wakikuandalia wasifu mzuri wenye mbwembe na
heshima nyingi kwa wale wasiokujua”
“Una maanisha nini?” Pierre Kwizera akuliza kwa hasira.
“Risasi zangu mbili makini zingekuwa zimekufumania vizuri na kukifumua vibaya
kichwa chako wakati ulipokuwa ukitoka nje ya lile jengo la ofisi za wizara ya ulinzi na
mambo ya ndani muda mfupi uliyopita” Koplo Tsega akaongea huku akitabasamu.
Pierre Kwizera akashikwa na mshangao wa aina yake huku akilikumbuka gari dogo
jeupe aina ya Corolla limited aliloliona mara mbili na zaidi nyuma yake na kulipuuza
wakati alipokuwa akitoka ofisini kwenye lile jengo la wizara ya ulinzi na mambo ya
ndani.
“Koplo!...so you wanted to kill me?” Pierre Kwizera akauliza kwa mshangao.
“Definitely!...” Koplo Tsega akaongea kwa utulivu huku uso wake ukishindwa
kuonesha tashwishwi yote.
“Why…?” Pierre Kwizera akauliza hata hivyo Koplo Tsega akalipuuza swali lile na
badala yake akatumbukiza swali lake.
“Nani anayewapa hizi fedha?”
“Sifahamu chochote Koplo” Pierre Kwizera akajitetea
“Huwezi kufa na siri hiyo moyoni komredi kwani haupo peke yako. Ukifa wewe
wenzako wataniambia tu!” Koplo Tsega akaongea kwa utulivu
“Hufahamu unachokizungumza Koplo!” Pierre Kwizera akaongea kwa kulalama
huku akionekana kuzama kwenye tafakuri.
“Nafahamu kuwa kuna maslahi makubwa mliyoyapata au mliyoahidiwa kuyapata
mara baada ya vifo vyetu. Hizi hundi nimezikuta nyumbani kwa Meja Khalid Makame
mtu mliyemtuma D.R Congo kuja kutimiza mpango wenu mchafu. Bahati mbaya
sana mpango wenu umeharibika hivyo hamuwezi kupiga hatua nyingine mbele zaidi
bila ya kuniua mimi. Lakini mimi nimekufa na kila mtu ana amini hivyo na hali hiyo
ndiyo inayonipa nafasi nzuri ya kupambana na nyinyi huku nikiwa sipo katika fikra
zenu kabisa just because i am dead,burried and forgotten” Koplo Tsega akaongea huku
akiangua kicheko hafifu cha hasira na dhihaka.
“Nakushauri urudi nyumbani ukapumzike kwanza kwani akili yako inaonekana
imeathirika vibaya na milio ya mabomu na risasi msituni” Pierre Kwizera akaongea
kwa dharau huku tabasamu hafifu likipita usoni mwake. Koplo Tsega akamtazama
Pierre Kwizera kwa hasira bila kusema neno lolote badala yake akasimama na kuelekea
kwenye kochi lililokuwa jirani na eneo lile.
Aliporudi alikuwa ameshika kompyuta mpakato aliyoichukua kwenye begi la
ofisini la Pierre Kwizera kule chumbani kwake muda ule Pierre Kwizera alipokuwa
amepoteza fahamu baada yay ale mapambano makali.
Baada ya kuketi Koplo Tsega akaifungua ile kompyuta mpakato na alipoiwasha
akamtazama Pierre Kwizera kwa uyakinifu kabla ya kuvunja ukimya.
“Nahitaji password yako” Koplo Tsega akaongea kwa utulivu huku akimsogezea
karibu Pierre Kwizera ile kompyuta. Pierre Kwizera akaitazama kompyuta yake kwa
makini hata hivyo hakuingiza password yake kama alivyoambiwa na badala yake akainua
macho yake akimtazama Koplo Tsega huku akitabasamu.
“Unadhani mimi ni mjinga kiasi hicho?” Pierre Kwizera akaongea huku akiendelea
kutabasamu. Koplo Tsega akamtazama Pierre Kwizera kwa kitambo huku akiyapima
maneno yake na hapo akagundua kuwa Pierre Kwizera alikuwa akimaanisha kile
alichokuwa akikisema. Hasira zikampanda Koplo Tsega huku akianza kupoteza moyo
wa uvumilivu.
“Nimewaua Meja Khalid Makame,Guzbert Kojo na P.J.Toddo hivyo kama
utaendelea kushikilia msimamo wako sioni sababu ya kukuvumilia komrade” Koplo
Tsega akaongea huku akimtazama Pierre Kwizera mbele yake. Pierre Kwizera
akashikwa na taharuki baada ya kuyasikia maelezo yale.
“My God! kumbe ni wewe…?”
“Don’t west my time comrade,I need your password please…!” Koplo Tsega akasisitiza
“Kwa hiyo umekuja kuniua na mimi?. Utaua watu wangapi Koplo?. Kwanini
ufanye makosa yasiyo na ulazima?. Serikali hii ina mtandao mkubwa itakufikia popote
utakapojificha. Utakamatwa na kufunguliwa mashtaka ya mauaji ya kukusudia na
mwisho wako ni kunyongwa tu”
”Unanitisha?. Unadhani utafanikiwa kunitisha?. Mimi siyo mwoga kama nyinyi.
hebu niambie komredi feki ni pesa kiasi gani mliyolipwa kuuondoa uhai wetu?.
Kwa miaka mingi mmekuwa mkifanya kiini macho kama Paka mwenye njaa kali
anayesalisha kundi kubwa la Panya huku akiwa amevaa rozari ya dagaa.
Nguvu kazi kubwa ya taifa hili imeharibika kwa ajili yenu. Pesa nyingi ya wazalendo
walipakodi wa taifa hili mnazitafuna na kujineemesha na familia zenu. Watoto wenu
wanasoma kwenye shule na vyuo vikubwa vikubwa nje ya nchi ili baadaye waje
kushika madaraka hata kama ni bongo lala. Wakati watoto wa masikini wanataabika
mitaani na ndiyo mnazidi kuwamaliza kwa biashara zenu chafu.
Kila kunapokucha tume zisizo na vichwa wala mikia zinaundwa kutatua
matatizo yasiyo ya lazima na matokeo yake ni utafunwaji wa mabilioni ye fedha kwa
wapumbavu wachache wanaojiita wajanja waliobarikiwa. Hii nchi mnataka kuipeleka
wapi nyinyi wapumbavu?” Koplo Tsega akaweka kituo akimtazama Pierre Kwizera
huku amepandwa na hasira.
“Huelewi unachokizungumza Koplo. Mimi nakuona kama unayepiga kampeni za
kisiasa” Pierre Kwizera akaongea huku usoni akiumba tabasamu la dharau.
“Mlidhani kuwa mambo yangekuwa rahisi komredi lakini mlikosea sana kwani
nimerudi nikiwa na nguvu za kutosha za kuwashughulikia mmoja baada ya mwingine.
Tafadhali! ingiza password yako kwenye hii kompyuta kwani muda wa nasaha
umekwisha” Koplo Tsega akaongea huku uso wake umejawa na chuki.
“Kwanini uning’ang’anize kuweka password kwenye kompyuta yangu?”
“Nahitaji faili langu” Koplo Tsega akaongea huku uso wake umetulia kama jiwe.
“Faili lipi?” Pierre Kwizera akauliza huku akimtazama Koplo Tsega kwa makini.
“Faili lenye taarifa zangu zote nilizozifanyia kazi wakati nikiwa kwenye hii tume”
Koplo Tsega akaongea kwa utulivu huku uvumilivu ukipungua. Pierre Kwizera
akamtazama kabla ya kuangua kicheko cha dhihaka.
“Hii ni serikali Koplo siyo Project ya mtu binafsi au Ngo’s. Unapoteuliwa kwenye
tume yoyote huwa kuna taratibu zake za kufuata na unapotolewa huwa ni vilevile. Hii
siyo miradi kama Mkukuta au Mkulabita. Unapoondolewa kwenye tume taarifa zako
huwa ni confidencial hivyo huna haki ya kuzidai tena.
Wewe,Sajenti Chacha Marwa na Meja Khalid Makame mlishaondolewa kwenye
hii tume hivyo huwezi kurudi kienyeji na istoshe kazi zenu walishateuliwa watu
wengine kuzifanya” Pierre Kwizera wakati akimaliza kuongea akajikuta akiambulia
kichapo cha nguvu kutoka kwa Koplo Tsega kilichomsababishia maumivu makali
mwilini.
“Ingiza password yako komredi ukaidi hautokusaidia kitu” Koplo Tsega akaongea
kwa hasira.
“Go on you bastad kwani najua kuwa huwezi kuniua” Pierre Kwizera akaongea huku
tabasamu lake likiwa limechanganyika na maumivu makali. Koplo Tsega kuona vile
akabadili mtindo wa mateso akimtimba Pierre Kwizera miguuni kwa kisigino cha
viatu vyake. Pierre Kwizera akaendelea kulalama pasipo kuweka password kwenye ile
kompyuta yake.
“Utaniua lakini hautafanikiwa kufika mbali Koplo”
“Subiri uone” Koplo Tsega akaongea huku akiikamata vyema bastola yake kisha
akaielekeza bastola ile kwenye paja la Pierre Kwizera na kuisukuma risasi moja. Pierre
Kwizera akapiga yowe kali huku akiwa haamini macho yake. Maumivu aliyoyapata
kutokana na lile jeraha la ile risasi yakamchanganya kabisa. Jasho likaanza kumtoka
huku akihema ovyo wakati alipoitazama damu yake kwenye lile jeraha.
“Nilikwambia kuwa ukaidi hautakusaidia kitu komredi. Tafadhali! ingiza password
yako kwenye hii kompyuta” Koplo Tsega akaongea kwa ghadhabu huku akiilekeza
bastola yake tena kwenye paja jingine la Pierre Kwizera. Pierre Kwizera kuona vile
akahamaki na kushikwa na hofu huku mdomo ukimchezacheza na mikono yake
ikitetemeka ovyo. Mara hii akaupeleka mkono wake taratibu na kuanza kubofya vitufe
vya keyboard ya kompyuta yake akiingiza password. Muda mfupi uliyofuata ile kompyuta
ikafunguka.
“Good boy!” Koplo Tsega akaongea huku akitabasamu kisha tabasamu lake
lilipofifia na kukoma sura yake ikavaa uso wa kazi na hapo akaikamata vizuri bastola
yake mkononi. Tukio lile likampelekea Pierre Kwizera aingiwe na hofu.
“Ukifika mwambie P.J.Toddo kuwa mimi ndiye niliyemuua”
“Nikifika wapi?’’ Pierre Kwizera akauliza kwa shauku lakini hakujibiwa na badala
yake risasi mbili za bastola ya Fort 12 iliyofungwa kiwambo maalum cha kuzuia
sauti zikapenya kwenye pafu lake la kulia na kutengeneza matundu mawili madogo
yanayovuja damu. Pierre Kwizera akapiga yowe kidogo na kutulia huku umauti ukiwa
tayari umemchukua.
Koplo Tsega akamtazama Pierre Kwizera kwa utulivu huku akitabasamu kisha
akachukua kitabu chake kidogo na kalamu kutoka mfukoni. Kupitia kitabu kile
akafunua kurasa hadi pale alipolifikia jina la Pierre Kwizera ambapo aliweka kituo na
kuweka alama ya X kisha akakirudisha kile kitabu mfukoni. Koplo Tsega hatimaye
akachukua pipi ya kijiti kutoka mfukoni kisha akaimenya taratibu na kuitia mdomoni.
Muda mfupi baadaye msako aliomaliza kuupitisha ndani ya nyumba ya Pierre
Kwizera ukawa umempatia vitu fulani muhimu alivyovihitaji. Koplo Tsega hakuwa
na muda wa kupoteza hivyo akafungua mlango wa ile nyumba na kutoka nje.
Mvua kubwa iliyokuwa ikiendelea kunyesha haikumzuia kuendelea na safari yake
wakati alipoitoroka nyumba ile na kupotelea mitaani.
 
Mkuu Banker naona umerudi kwa speed ya supersonic. Big up !
 
Kaka mbona nipo? Nilikuwa naiamsha kwanza riwaya ya tai kwenye mzoga. Umeshaisoma hiyo riwaya?
Hii ndio ulituacha km vipi tupia zaidi tusonge kufidia Gap. Tai kwenye mzoga nilishawahi kuisoma mkuu !
 
Koplo sio muuaji professional kila ukiua unaacha link ya ganda LA pipi ili uje ukamatwe kirahisi.
 
Cookies are required to use this site. You must accept them to continue using the site. Learn more…