RIWAYA: Mifupa 206

RIWAYA: Mifupa 206

Mtutu wa bunduki mojawapo
Mwandishi ndio kaisimamisha kuiandika kasema atatoka na kitabu moja kwa moja. Hizi ninazoleta humu pia mwanishi unakuta ameniinsruct niwe narusha page kadhaa. Yeye nia yake ni mnogewe kisha mumuunge mkono kwenye kazi yake kwa kununua vitabu. Mie najua kiu ya wenzangu kwani hata mie nasoma adithi humu na huwa arosto inanitesa kweli. Kwa hiyo naomba ujue na mie ni mmoja wenu. Nikipost kazi yote ya jamaa bila maelekezo yake nitakosa uhondo mwenzio. Faida nayoipata ni kusoma wa kwanza na kuwa na soft copy.
 
Mwandishi ndio kaisimamisha kuiandika kasema atatoka na kitabu moja kwa moja. Hizi ninazoleta humu pia mwanishi unakuta ameniinsruct niwe narusha page kadhaa. Yeye nia yake ni mnogewe kisha mumuunge mkono kwenye kazi yake kwa kununua vitabu. Mie najua kiu ya wenzangu kwani hata mie nasoma adithi humu na huwa arosto inanitesa kweli. Kwa hiyo naomba ujue na mie ni mmoja wenu. Nikipost kazi yote ya jamaa bila maelekezo yake nitakosa uhondo mwenzio. Faida nayoipata ni kusoma wa kwanza na kuwa na soft copy.
Na hii ya mifupa 206 ni hayohayo?
 
The banker tafadhali naomba umfikishie ujumbe mtunzi...mwambie asiogope kuuza kazi yake kwa njia ya softcopy kwani ndio njia rahisi ya kuwafikia wateja wengi bila kutumia gharama kubwa ya kuprint na gharama ya kusafirisha vitabu,Mwambie auze kwa season kama anavyofanya patrick ck,Mwisho wa siku ataingiza faida kubwa kwa gharama ndogo na hata bei itakuwa kubwa zaidi kuliko ya kitabu,Kuhusu kuogopa kazi kuvuja hata kwenye kitabu naweza kukinunua na nikawa napiga picha napost huku kwa wadau...mwambie watanzania tunaelemika na tunabadilika..tunaheshimu kazi za watu zinazowawezesha kuishi tofauti na zamani, zaidi ya yote yaan mimi ninunue nije niwape watu bure humu natafuta nini?umaarufu au?mwambie awasiliane na patrick CK tunanunua kazi zake sana na wala sijaziona humu JF...kazi ukiinunua inauma sana kumpa mwingine bure.
 
Ujumbe umefika na nakuhaidi nitaufikisha. Pia ukimpigia ukamjulisha kuhusu hili utakuwa umenisaidia sana. Japo ajue kuna mawazo tofauti kama haya. I guess it will work
 
Hatimaye nikaufikia ule mfuniko wa ile chemba kule juu. Nilipofika kule juu
nikasimama kidogo nikiupisha utulivu kichwani mwangu kisha nikaichukua ile bisbisi
kutoka kwenye mfuko wa koti langu na kuanza uharibifu huku mara kwa mara
nikiyatega vizuri masikio yangu kunasa sauti ya kitu chochote ambacho kingekuwepo
nje ya mfuniko wa chemba ile.
Sasa nilikuwa na hakika kuwa chemba ile ilikuwa eneo fulani katikati ya barabarani
kwani mara kwa mara niliweza kusikia muungurumo wa injini za magari yaliyokuwa
yakipita juu ya ile chemba. Gurudumu la gari moja liliukanyaga ule mfuniko wakati
nilipoanza kuusogeza pembeni na hivyo kuukandamiza haraka kiasi kwamba kama
nisingekuwa mwangalifu huwenda vidole vyangu vingekuwa vimefyekwa na ukingo
wa mfuniko ule wa chuma.
Nikasubiri kidogo kujipa utulivu na nilipoona kuwa hali ilikuwa shwari
nikausukuma tena pembeni ule mfuniko wa chemba na hapo nikapanda juu kidogo
kuchungulia tena kule nje.
Mvua kubwa ilikuwa ikiendelea kunyesha na kitendo cha kuufungua kidogo ule
mfuniko baadhi ya maji ya mvua ile yakapata upenyo wa kuingia mle ndani. Hata
hivyo sikujali badala yake nilitulia kidogo nikiitathmini hali ya mandhari ya kule nje.
Magari mawili au matatu yalipokaribia kuifikia ile chemba nilirudi ndani na kuufunika
ule mfuniko na magari yale yalipopita nikausogeza tena ule mfuniko na kuendelea na
tathmini yangu. Sasa nilikuwa na hakika kuwa ile chemba ilikuwa imejengwa katikati
ya barabara ingawa nilipojitahidi kuvuta picha nilishindwa haraka kufahamu kuwa
chemba ile ilikuwa ipo kwenye barabara ya mtaa upi wa jiji la Dar es Salaam japokuwa
nilikuwa na matumaini kuwa bado nilikuwa kwenye eneo la posta jijini Dar es Salaam.
Ni mara chache sana kwa barabara za mitaa ya jiji la Dar es Salaam kukaukiwa
kabisa na watembea kwa miguu lakini nilishangazwa sana na kitendo cha kutomuona
mtu yeyote akitembea katika barabara ile. Hata hivyo huwenda hali ile ilitokana na
mvua kubwa iliyokuwa ikiendelea kunyesha. Taa kutoka kwenye majengo marefu ya
ghorofa yaliyokuwa yametenganishwa na barabara ile ziliangaza barabarani hata hivyo
hazikufanikiwa kulitowesha giza lote eneo lile. Hatimaye nikausukuma ule mfuniko wa
ile chemba na nilipokuwa mbioni kuuweka kando ili nitoke mara kwa mbali nikaliona
gari moja likija usawa wa ile chemba hivyo haraka nikawahi kurudi tena mle ndani
na kujifungia. Lile gari lilipopita nikausukuma tena ule mfuniko na kuuweka kando
kisha bila kupoteza muda nikamalizia kuzipanda zile ngazi za ile chemba na kutoka
nje kisha nikaurudishia ule mfuniko wa ile chemba mahala pake huku nikiyatembeza
macho yangu kuyapeleleza mazingira yale huku nikichunguza kama kungekuwa na
mtu yoyote jirani na eneo lile akinitazama.
Hali ya mandhari yale ilikuwa tulivu hivyo haraka nikachepuka kando ya barabara
ile na kuanza kutembea kwa tahadhari. Matone mazito ya mvua kubwa iliyokuwa
ikiendelea kunyesha jijini Dar es Salaam yakanipa faraja huku mvua ile ikiendelea
kuniosha uvundo wa ile mifereji uliokuwa kwenye koti langu na kunifanya nijihisi
kama kiumbe aliyetoka kwenye safari ndefu ya kuzimu baada ya kushinda vita kubwa
ya wanyang’anyi wa roho yangu.
Nikaendelea kutembea huku mara kwa mara nikigeuka nyuma na kutazama kama
kungekuwa na mtu yoyote aliyekuwa akinifuatilia na kila nilipouona mwanga wa taa
za gari likija nyuma au mbele yangu nilichepuka na kujibanza kando ya barabara ile
hadi gari hilo lilipopita.
Ilinichukuwa muda mfupi tu kuvuta kumbukumbu sahihi kichwani mwangu
kuwa pale nilikuwa wapi kwani kupitia mandhari yale nikagundua kuwa ile ilikuwa
ni barabara ya Sokoine Drive hasa baada ya kuliona jengo la ofisi za Tanzania Buildings
Agency.
Bado sikuwa sehemu salama nilijiambia pale nilipokumbuka kuwa barabara ile ya
Sokoine Drive haikuwa mbali sana na lile eneo la Botanical Garden nilipokoswakoswa
kukamatwa na wale makachero. Hivyo nikakatisha kwenye uchochoro mmoja
ulionichukua moja kwa moja hadi nyuma ya lile jengo la Tanzania Buildings Agency.
Nyuma ya jengo lile kulikuwa na barabara ndogo ya lami ambayo sikuweza haraka
kuitambua vizuri hata hivyo niliingia kwenye barabara ile fupi nikishika uelekeo wa
upande wa kushoto huku upande wa kulia kwangu nikitazamana na majengo mengine
ya ghorofa yaliyokuwa yakitumika kama makazi ya watu na ofisi mbalimbali.
Nilipokuwa nikikaribia kufika mwisho wa barabara ile mara nikayaona magari
mawili aina ya Landcruiser kama yale niliyoyaona kule Botanical Garden muda mfupi
uliyopita yakikatisha mbele yangu. Niliwahi kujibanza nyuma ya pipa kubwa la taka na
kuyaacha magari yale yapite kisha nikajitokeza na kuendelea na safari yangu.
Nilipofika mwisho wa barabara ile nikaingia upande wa kulia nikitembea kwenye
barabara nyingine ya lami yenye giza zito zaidi lililotokana na vichaka vya matawi ya miti
iliyopandwa kando yake. Ilikuwa ni barabara ya Luthuli na kutoka pale sikuwa mbali
sana na eneo la Ikulu ya Magogoni. Sikuwa salama sana niliwaza ila angalau nilikuwa
mbali kidogo na lile eneo la Botanical Garden msako wangu ulipokuwa ukiendelea.
Vivuli vya matawi ya miti kando ya barabara ile ndiyo vikawa sehemu yangu ya
kujibanza kila nilipouona mwanga wa taa za gari kwenye barabara ile. Niliendelea
kutembea hadi pale nilipofika kwenye barabara ya Kivukoni. Kuingia kwenye barabara
ile kukanipelekea nisijisikie tena mpweke kwani kulikuwa na pilikapilika za watu ambao
haraka baadhi yao niliwatambua kuwa walikuwa wachuuzi wa samaki kwani soko la
samaki halikuwa mbali sana na eneo lile. Wengine walikuwa ni wasafiri waliokuwa
wakielekea kupanda Pantoni eneo la Feri.
Nilipoingia kwenye barabara ile ya Kivukoni nikashika uelekeo wa upande wa
kushoto kama ninayeelekea katikati ya jiji la Dar es Salaam halafu nilipofika mbele
kidogo nikashika uelekeo wa upande wa kulia. Kuingia kwenye uelekeo ule kukanifanya
niione ile sanamu ya Askari Monument mbele yangu na mashine za ATM za benki
ya NBC kushoto kwangu. Nilikumbuka kuwa sikuwa na pesa ya kutosha mfukoni
hivyo nikaingia kwenye zile ATM na kuchukua kiasi cha pesa ambacho kingenisaidia
kwenye harakati zangu. Nilipotoka kwenye zile mashine za ATM nikatembea hadi
katikati ya mtaa wa Azikiwe na Sokoine Drive nje ya New Africa Hotel ambapo nilikodi
teksi.
Dereva wa teksi alikuwa mzee wa makamo mfupi na mwenye maneno mengi.
Macho yake makubwa yaliyokosa utulivu yakanitanabaisha kuwa alikuwa mwerevu
sana wa dili za jijini Dar es Salaam na vichochoro vyake. Ingawa alikuwa mfupi sana
kiasi cha kutokuona kwa urahisi mbele yake lakini uzoefu ulimlinda wakati akiiacha
barabara moja na kuingia barabara nyingine kwa mbwembwe. Nilimtathmini vizuri
dereva yule na hapo nikahisi kuwa huwenda alikuwa Mpare wa Same au Mwanga
mkoani Kilimanjaro.
“Tunaelekea wapi bosi wangu?” hatimaye yule dereva akaniuliza na hapo
nikakumbuka kuwa sikuwa nimemueleza kule ninapokwenda. Hivyo nikaingiza
mkono mfukoni na kuchukua Business card niliyopewa siku ile kule Vampire Casino
na yule mwanamke mnaijeria aliyejitambulisha kwangu kwa jina la Iko–Ojo Obaje.
Nilipoichukua ile Business card nikawasha taa iliyokuwa chini ya paa la ile teksi na
kusoma maelezo yake kisha nikaizima ile taa. Dereva alikuwa amepunguza mwendo
kidogo kunisikiliza.
“Endesha gari hadi 79 Haile Selassie road eneo la Oysterbay”
“Unaenda Hotel Agent 11?” mzee yule akaniuliza huku akibadili uelekeo.
“Ndiyo” nikamwitikia huku nikigeuka kutazama nyuma.
“Oh! hoteli ya kifahari sana ile na ina mabinti warembo sijapata kuona” dereva
yule mzee akaongea na kwa kweli umri wake haukuendana na maongezi yale hata
hivyo sikumuacha mpweke.
“Umewahi kufika?” nikamuuliza
“Nimefika mara nyingi sana. Sisi madereva wa teksi hukodiwa sana na wateja wa
mahotelini na asikwambie mtu viongozi wengi wa kisiasa na baadhi ya matajiri wa
hapa jijini Dar es Salaam wanayatumia maficho yale kuchepuka na nyumba ndogo”
Nilicheka kidogo nikiyatafakari maneno ya dereva yule na kwa kweli alinipunguzia
sana upweke wa mawazo na kunisahaulisha kwa muda mkasa uliotokea nyuma
yangu. Hatimaye nikamtoa kwenye maongezi yale nikimpeleka kwenye masuala
ya siasa halafu mpira wa miguu na baadaye masuala ya mapenzi na kote alionesha
kuyamudu vyema maongezi huku akitia mbwembwe za hapa na pale. Nilipendezwa
sana na ucheshi wake na ilifika sehemu sote tukawa tumeishiwa hoja na hapo ukimya
ukachukua nafasi yake. Hali ile ikiwa inaendelea taratibu nilijiegemeza kwenye siti ya
gari huku nikipiga mwayo hafifu na kuanza kufanya tathmini ya kimyakimya ya kazi
yangu.
Hadi wakati ule nilikuwa nikiamini kuwa kama siyo serikali basi ni baadhi ya watu
katika serikali walikuwa wakifanya jitihada za juu na chini kuzizima harakati zangu na
kweli sikuweza kufahamu ni kitu gani hasa kilichokuwa kikiendelea. Nikakumbuka
mambo nilioyaona kule ndani ya ule mlango mweusi kwenye lile jengo la ghorofa
lililopo kule eneo la posta kisha nikaoanisha na yale maelezo ya Pastor Romanus.
Kufikia pale nilikuwa nimeanza kuvuta picha ya namna fulani kichwani mwangu
hata hivyo picha hiyo bado ilikuwa haijakamilika vizuri. Mawazo yangu yakahamia
kwa yule msichana kisura na mlimbwende wa aina yake yaani yule mdunguaji hatari
huku nikiwaza namna alivyoniokoa na kwa jinsi alivyokuwa akipambana na wale watu
hatari kwa namna ya kimyakimya na hapo nikajikuta nikivutiwa naye. Nilikumbuka
namna nilivyotazamana na mdunguaji yule hatari kwenye vile vyumba vya lifti kule
posta wakati tukishuka kwenye yale majengo ya ghorofa na hapo hisia juu yake
zikaanza kuziteka taratibu fikra zangu. Nikajiuliza tena mdunguaji yule hatari ni nani
na kwanini aliniokoa kutoka katika ile milipuko ya mabomu ya kutegwa kwenye gari
langu. Kisha nikaikumbuka ile milipuko ya mabomu huku nikiilinganisha na thamani
ya maisha yangu na hali ile ikanifanya nizidi kuhisi kuwa kulikuwa na siri kubwa
iliyokuwa imefichika katika mkasa huu.
Kwa mara ya kwanza nikaanza kuhisi kuwa nilikuwa nimejitumbukiza kwenye
mkasa hatari zaidi wenye siri nzito iliyofichika ndani yake. Siri ambayo gharama ya
kuitunza ililingana na thamani ya uhai wangu. Kitendo cha kuwaona wale makachero
wakiwa wamejiingiza katika mkasa huu siyo tu kwamba kitendo kile kilikuwa
kimenishtua bali pia kilikuwa kikielekea kuninyima usingizi kwani nilifahamu ugumu
ulipo katika kupambana na vyombo vya usalama vya serikali.
Nikiwa katika hali ile ya kutafakari nikaanza kufikiria namna ya kuutelekeza kando
mkasa huu na kutafuta maficho salama ambapo huko ningetulia hadi pale ambapo
ningekuwa na hakika kuwa harakati za makachero wale kunisaka mitaani zingekuwa
zimefifia hapo ndiyo ningejitokeza na kuendelea na harakati zangu. Lakini nilipozidi
kutafakari haraka sana nikaliweka kando wazo lile pale nilipokumbuka kuwa bado
nilikuwa sina taarifa za kutosha juu ya kile nilichokuwa nikikipeleleza. Hivyo sikuona
kama nilipaswa kurudi nyuma katika harakati zangu badala yake nikaona kuwa
nilitakiwa kuongeza juhudi katika kuutafuta ukweli wa mambo kwani huwenda ukweli
huo ungenipa kinga ya kifo dhidi ya wale makachero.
Nilimkumbuka tena yule mdunguaji hatari na hapo tabasamu jepesi likaniponyoka
bila hiana huku fikra zangu zikiendelea kutengeneza picha na kunifanya nijihisi
kama ninayemuona mdunguaji yule hatari akiwa mbele yangu akitabasamu na hivyo
kuyafanya meno yake meupe yenye mng’aro wa kipekee yaonekane sambamba na
vishimo vyake vidogo mashavuni vyenye kuweza kuziroga vibaya hisia zangu na hapo
nikabaki nikimuomba Mungu anikutanishe naye kwa mara nyingine.
“Tumefika bosi wangu” sauti ya yule dereva ikazirudisha tena fikra zangu mle
ndani ya teksi.
“Oh! mara hii tu” nikaongea kwa uchovu kama niliyeishiwa na hoja ya kuzungumza
na hapo dereva yule akanitazama kupitia kioo cha ndani cha gari huku akitabasamu.
“Ushasau kuwa usiku huu hakuna foleni barabarani?” mzee yule dereva akaongea
kwa msisitizo kana kwamba ile hoja aliitoa baada ya kuhisi kuwa nilikuwa nikitaka
kupingana naye kwa kuionea uchungu pesa yangu mfukoni.
Teksi ilisimama kwenye barabara ya 79 Haile Selassie eneo la Oysterbay mbele ya
Hotel Agent 11 na hapo nikaingiza mkono mfukoni na kuchukua wallet yangu ndogo
ya ngozi ya Bitis arietans-Puff adder kisha nikaifungua na kutoa noti moja ya shilingi elfu
kumi na kumpa dereva. Dereva akaipokea noti ile kwa bashasha zote na kuitia kwenye
mfuko wa mbele wa shati lake huku akitabasamu.
“Shukrani kijana” dereva yule akanishukuru huku akiupapasapapasa ule mfuko
wa shati lake.
“Ondoa shaka” nikamwambia yule mzee kwa utulivu.
“Nikufuate saa ngapi bosi wangu?” yule dereva akaniuliza huku akinitazama
kupitia kile kioo cha ndani ya gari kilichokuwa chini ya paa.
“Safari yangu inaishia hapa mzee kama nitakuhitaji zaidi nitakufata pale kituoni
kwako”
“Chukua basi namba yangu ya simu kwani huwezijua utanihitaji muda gani” yule
dereva akaning’ang’aniza na sikutaka kuendeleza upinzani hivyo nikachukua simu
yangu na kuzuga kuzinakili namba za simu yake wakati alipokuwa akinitajia katika
namna ya kutaka kumridhisha.
“Hebu nipigie niinakili namba yako” yule dereva akanisisitiza
“Simu yangu haina muda wa maongezi” nikamwambia yule dereva huku
nikifungua mlango wa teksi na kushuka. Dereva yule akageuka na kunikodolea macho
na alipoona simpatilizi akawasha gari na kugeuza akirudi kule alipotoka na hali ile
kwangu ikawa afadhali.
Mvua ilikuwa imepungua hivyo mara baada ya kushuka kwenye ile teksi
nikasimama kidogo nikiitazama Hotel Agent 11 kwa udadisi. Ilikuwa hoteli ya kisasa na
yenye hadhi kiasi kwamba mtu yeyote mwenye kipato cha wasiwasi asingejisumbua
kuulizia huduma ya malazi.
Kulikuwa na magari machache yaliyoegeshwa nje ya hoteli ile na yote yaliashiria
kuwa wamiliki wake walikuwa ni watu wa vipato vya kueleweka. Hatimaye nikaingiza
mikono kwenye mifuko ya koti langu kisha nikavuka barabara nikikatisha kwenye geti
la hoteli ile kuingia ndani. Nilipozifikia ngazi za mbele za ile hoteli nikazipanda taratibu
huku nikigeuka nyuma kutazama kama kungekuwa na mtu yoyote akinifuatilia. Hali
bado ilikuwa shwari na huwenda walinzi wa getini kwenye hoteli ile hawakutaka
kunihoji kwa kunidhania kuwa huwenda nilikuwa miongoni mwa wateja wa hoteli ile.
Kipande cha zulia maridadi cha rangi nyekundu kikanichukua kutoka eneo la
mlangoni la hoteli ile hadi sehemu ya mapokezi na wakati nikitembea nikayazungusha
macho yangu taratibu kuzikagua sura za watu waliokuwa wameketi kwenye makochi
ya sofa ya kifahari yaliyokuwa kwenye ukumbi ule. Baadhi ya watu mle ukumbini
walikuwa wakiendelea kupata vinywaji huku wengine wakionekana kuendelea na
maongezi ya hapa na pale hata hivyo Iko–Ojo Obaje hakuwepo miongoni mwao.
Mandhari ya ukumbi wa chini wa hoteli ile yalifaa kuitwa ya kistaarabu
yanayoendana na watu wakwasi wanaofahamu namna ya kutumia pesa. Madirisha
makubwa ya ukumbi ule yalikuwa yamefunikwa kwa mapazia marefu na mapana
yanayopendeza na ukutani kulikuwa kumetundikwa picha nzuri kubwa na tofauti
za kuchora zinazovutia kuzitazama bila kuchoka. Sakafuni kulitandikwa zulia zuri
linalopendeza na sehemu fulani mle ndani ukutani kulikuwa na seti mbili za runinga
zilizotundikwa kwenye pande mbili za ukutani na wakati nikitembea kwa mbali
nilisika sauti ya muziki laini uliokuwa ukirushwa kwenye spika zilizokuwa sehemu
fulani katika ukumbi ule.
“Karibu sana” kijana moja wa mapokezi akanikaribisha na nilipomchunguza
nikagundua kuwa alikuwa mwembamba wa wastani lakini mwenye sura ya ucheshi na
alikuwa amevaa sare za kazi. Suruali ya rangi ya nyeusi,shati jeupe na tai ndogo nyeusi
shingoni mwake.
“Ahsante!” nilimwitikia yule kijana huku nikigeuka na kuyatembeza tena macho
yangu kuwatazama wale watu waliokuwa mle ndani ya ukumbi. Sikumuona mtu yeyote
ninayemfahamu hivyo nikageuka tena na kumtazama yule kijana huku nikiingiza
mkono wangu mfukoni kuichukua ile kadi ndogo aliyonipa Iko-Ojo Obaje halafu
nikaitelezesha kwenye meza ya kaunta ile ya mapokezi. Yule kijana hakuichukua
ile kadi badala yake akaipitishia macho kuitazama kisha akayahamishia macho yake
kwangu.
“Nimemkuta?” nilimuuliza yule kijana mhudumu wa mapokezi.
“Wewe ni nani?”
“Mimi ni mgeni wake tafadhali naomba umpigie simu chumbani kwake
umwambie kuwa Stephen Masika amefika kumuona” nilimwambia yule kijana na
hapo akanitazama kwa mashaka kidogo kisha akanyanyua simu iliyokuwa pale mezani
pambeni yake halafu akauweka mkonga wa simu sikioni huku akibonyeza tarakimu
fulani. Ile simu ilipoanza kuita yule mhudumu akageuka na kunitazama kwa udadisi
muda mfupi uliyofuata nikamsikia akiongea kwa lugha safi ya kiingereza kisicho cha
kuungaunga na hapo nikajua kuwa alikuwa akimtaarifu Iko-Ojo Obaje kuwa mimi
nimefika. Yule kijana alipokata ile simu na kuirudishia mahala pake akageuka tena na
kunitazama.
“Chumba namba 22 ghorofa ya pili” yule kijana akaniambia kwa kisirani kama
ambaye hajapokea tip hata mmoja kutoka kwa mteja tangu kulipopambazuka.
“Ahsante!” nikamwambia yule kijana huku nikiichukua ile kadi yangu pale juu
ya meza na kuitia mfukoni kisha nikazunguka ile kaunta kuelekea sehemu ya nyuma
yake kulipokuwa na chumba cha lifti. Niliifikia ile lifti na kutokomea ndani kisha
nikabonyeza kitufe cha ghorofa pili na hapo ile lifti ikaanza kupanda juu ya lile jengo
la hoteli.
Muda mfupi uliofuata kile chumba cha lifti kikatia nanga ghorofa ya pili na hapo
mlango ukafunguka. Nilipotoka nje nikajikuta nimetokezea kwenye korido pana kiasi
inayotazamana na milango mingi ya vyumba. Mandhari ya eneo lile yalikuwa tulivu
na yenye harufu nzuri na usafi wa hali ya juu. Nilianza kutembea huku nikiyatembeza
macho yangu kutazama milango iliyokuwa ikitazamana na korido ile.
Chumba namba 22 kilikuwa baada ya kuipita milango miwili upande wa kulia.
Nilipoufikia mlango wa chumba kile nikasimama na kujikarabati kidogo mwonekano
wangu kisha nikabonyeza kitufe cha kengele kilichokuwa kando ya mlango ule. Mwito
wa kengele yangu haukusubiriwa sana kwani mlango ule ulifunguliwa mapema na
hapo macho yangu yakatulia juu ya taswira ya mlimbwende chakaramu.
Iko-Ojo Obaje alikuwa amevaa pensi nyanya fupi ya rangi nyekundu iliyoiacha
wazi sehemu kubwa ya minofu ya mapaja yake laini. Fulana yake nyepesi ya rangi
nyeupe ilikuwa na mshono wa umbo la V shingoni na hivyo kuipelekea nusu ya
shehena ya matiti yake makubwa ya wastani kubaki wazi pasipo uzio wowote wa
sidiria. Fulana ile pia ilikuwa fupi kiasi cha kuipelekea nusu ya sehemu yake ya tumbo
kubaki wazi na hivyo tumbo lake ng’avu na laini kuonekana. Miguuni alikuwa amevaa
viatu vya kuchomeka vyenye manyoya laini ya rangi ya majani makavu ya miti. Nywele
zake za rasta alikuwa amezikusanya na kuzifunga kwa nyuma kama mkia wa farasi.
Kutoka pale aliposimama niliweza kuinusa harufu nzuri ya manukato yake ya gharama
aina ya Caron’s Poivre.
Macho yake legevu yenye uchovu kiasi yalinitazama kwa huba huku tabasamu
laini likiuponyoka uso wake wenye pua ndefu kiasi na midomo laini yenye kingo pana
zilizokolea vizuri rangi nyekundu ya lipstick. Tathmini yangu ya haraka ikinieleza kuwa
Iko-Ojo Obaje alifaa kushiriki kwenye kinyang’anyiro cha mashindano ya kumtafuta
mwanawake mzuri wa asili barani Afrika,na hapo roho yangu ikapoteza utulivu kabisa.
“Karibu ndani” hatimaye Iko-Ojo Obaje akanikaribisha kwa sauti nyepesi yenye
kuulevya mtima wangu kwa lugha ya kiingereza chake fasaha.
“Ahsante sana!” nikaongea kwa utulivu huku nikiliruhusu tabasamu langu
kuchanua usoni halafu nikamkonyeza kidogo kwa furaha kisha nikaingia na kufunga
ule mlango nyuma yangu na wakati Iko-Ojo Obaje akitembea kuelekea kwenye kochi
moja kati ya makochi mawili ya sofa yaliyokuwa mle ndani hisia zangu zikamezwa
vibaya na mtikisiko wa makalio yake laini yaliyojificha ndani ya kitambaa chepesi
cha ile pensi nyanya yake bila nguo ya ndani. Kwa uzoefu mzuri niliyokuwanao kwa
wanawake wa sampuli ile kwa haraka niliweza kufahamu kuwa Iko-Ojo Obaje alikuwa
ni mwanamke wa namna gani na alikuwa akihitaji nini kwangu.
Mapenzi!...nikajiambia moyoni huku nikianza kulivua koti langu na kulitupa
sakafuni wakati huo tabasamu jepesi likiwa limejivinjari usoni mwangu. Nilipoanza
kufungua vifungo vya shati langu Iko-Ojo Obaje alikuwa tayari ameshanifikia pale
nilipokuwa na hapo akauzungusha mkono wake mmoja nyuma ya shingo yangu
taratibu huku mkono wake mwingine ukianza kufungua mkanda wa suruali yangu
ya jeans kiunoni. Nikiwa bado nimesimama pale katikati ya chumba niliweza kuzisikia
pumzi nyepesi za Iko-Ojo Obaje mbele yangu kwa namna mapigo ya moyo wake
yalivyopoteza utulivu. Nikamtazama Iko-Ojo Obaje na hapo akashindwa kabisa
kunitazama usoni badala yake akafumba macho yake legevu na kuuzamisha taratibu
ulimi wake kinywani mwangu.
Sasa tulikuwa kwenye zero distance na sikuweza kabisa kuvumilia uchokozi wa
namna ile hivyo nikaipandisha juu fulana yake na hapo mikono yangu ikaanza kufanya
ziara taratibu kwenye chuchu zake nyeusi zilizotuna katikati ya matiti yake yenye
ukubwa wa wastani kifuani mwake.
Suruali yangu alipoanguka chini nikaitupia pembeni kwa teke langu huku mkono
wangu mwingine ukiwa umekikamata vyema kiuno chake na kuanza kukipapasa
taratibu. Mkono laini wa Iko-Ojo Obaje ulipofika katikati ya mapaja yangu uvumilivu
ukanishinda huku nikihema ovyo.
 
KOPLO TSEGA ALIENDESHA GARI LAKE taratibu kuelekea mtaa wa
Undali eneo la Upanga jijini Dar es Salaam huku mara kwa mara akivitazama
vioo vya ubavu wa gari kuchunguza kama kungekuwa na mtu yoyote
aliyekuwa akimfuatilia nyuma yake. Akagundua kuwa hakuna mtu yoyote aliyekuwa
akimfuatilia hivyo hali bado ilikuwa shwari na jambo lile likamfurahisha sana.
Mvua bado ilikuwa ikinyesha na hivyo kupelekea barabara nyingi za mitaa ya jiji
la Dar es Salaam kuwa na hali ya upweke. Saa ya ndani ya gari kwenye dashibodi
ilionesha kuwa ilikuwa ikielekea kutimia saa nane na robo usiku wakati Koplo Tsega
alipoitazama na kisha kuyatumbukiza mawazo yake kwenye tafakari nzito ya mikasa
yote iliyotokea tangu alipowasili jijini Dar es Salaam. Akaanza kukumbuka namna
siku ya kwanza alivyoanza kufuatiliwa na yule mtu asiyemfahamu wakati alipokuwa
akitoka kule Vampire Casino. Kisha akakumbuka namna vichwa vya magazeti
mbalimbali vilivyokuwa vimejikita katika kukinadi kifo cha Momba. Tukio lile lilikuwa
limemuuma sana moyoni hasa alipowaza kuwa yeye ndiye aliyekuwa sababu kubwa
ya kifo kile. Koplo Tsega akaendelea kukumbuka namna ambayo yule mtu wa ajabu
alivyomfukuza siku ile katika lile jengo la ghorofa la Rupture & Capture kabla ya kumzidi
ujanja na kumuacha solemba muda mfupi baada ya kumdungua vibaya P.J.Toddo nje
ya baraza la Vampire Casino.
Fikra zake zikatia nanga kwenye tukio lile na kuanza kuunda hoja juu ya mtu yule
ambaye kwa hakika sura yake ilikuwa ngeni kabisa machoni pake. Mwanzoni Koplo
Tsega alikuwa amemhusisha mtu yule moja kwa moja na kifo cha Momba kwani ni
yeye ndiye aliyekuwa amemuona siku ile alipokuwa kule juu ya jengo la biashara la
Rupture & Capture na baadaye kutoroka na teksi ya Momba na hivyo akawa ameapa
kumsaka mtu yule na kumwangamiza kama sehemu ya kulipa kisasi chake kwa
kumuua Momba.
Lakini sasa adhma hiyo alikuwa ameiweka kando mara baada ya mchana wa siku
iliyopita kumuona mwanaume yuleyule aliyekuwa akimfuatilia siku ile wakati alipokuwa
akitoka Vampire Casino na siku chache baadaye mwanaume huyo akimfukuza kwenye
lile jengo la biashara la Rupture & Capture,kumuona na yeye akifukuzwa na watu
aliyokuwa akiwawinda kwa hali na mali jijini Dar es Salaam. Kisha akakumbuka
namna alivyomuokoa yule mtu na mateka wake chini ya lile jengo la ghoroga eneo la
posta kutoka kwenye gari lake lililokuwa limetegwa milipuko na wale watu hatari. Mtu
yule ni nani na kwanini alikuwa akitaka kuangamizwa?. Akajiuliza bila kupata majibu.
Koplo Tiglsi Tsega akwenyeea kukumbuka namna risasi yake moja makini
ilivyoivunja na kuitawanya vibaya shingo ya mtu aliyeitwa Balimenya ambaye alikuwa
mkuu wa itifaki ya tume ya kuratibu na kudhibiti dawa za kulevya nchini. Namna
Koplo Tsega alivyofahamu juu ya wapi alipokuwepo Balimenya wakati ule ilikuwa kazi
rahisi sana. Kwani kupitia nyaraka muhimu na simu ya mkononi aliyoipata nyumbani
kwa Pierre Kwizera akaweza kupata namba ya simu ya Balimenya. Koplo Tsega
akakumbuka namna alivyompigia simu Balimenya akimsihi waonane huku akijidai
kuwa na taarifa nyeti za kusaidia kumnasa muuaji waliyekuwa wakimtafuta Balimenya
na makachero wenzake. Balimenya hakuwa amepata muda wa kuitathmini vizuri sauti
ya mpigaji wa simu ile na badala yake akamtaka Koplo Tsega kuwa amfuate kwenye
lile jengo la ghorofa lililokuwepo eneo la posta kulipotokea ile milipuko.
Koplo Tsega hakupoteza mfupi kwani muda mfupi baadaye alikuwa kwenye
chumba cha jengo moja la ghorofa lililokuwa likipakanana na lile jengo la ghorofa
alilokuwepo Belimenya na makachero wenzake kama alivyomuelekeza kwenye
maongezi ya simu. Kupitia chumba kile kilichokuwa kikitazamana na korido ya lile
jengo la ghorofa alilokuwapo Balimenya na makachero wenzake,Koplo Tsega akaitega
bunduki yake ya kudungulia 338 Lapua Magnum na kumsubiri Balimenya ajitokeze
vizuri kwenye korido ya lile jengo la ghorofa la jirani.
Akiwa bado amejibanza kwenye kile chumba Koplo Tsega akajikuta akivutiwa
na watu fulani waliofika chini ya lile jengo la ghorofa alilokuwepo Balimenya na
makachero wenzake. Watu wale mara tu waliposhuka kutoka kwenye gari jeupe
aina ya Landcruiser lile gari likaondoka haraka eneo lile na hapo akawaona wale watu
walioshuka kwenye lile gari lililoondoka muda mfupi uliyopita wakiharakisha kuelekea
kwenye maegesho ya magari ya jengo lile sehemu kulipokuwa na gari dogo aina ya
Peugeot 504 huku mmoja wao akiwa amebeba mfuko mweusi uliyotuna.
Koplo Tsega akaendelea kuwatazama wale watu chini ya lile jengo la ghorofa
kupitia darubini ya bunduki yake na wale watu walipolifikia lile gari wakafungua mlango
wa dereva na kuingia ndani. Kwa kutaka kupata taswira nzuri juu ya kilichokuwa
kikiendelea kwenye lile gari waliloingia wale watu na mfuko wao mweusi,Koplo Tsega
akairekebisha vizuri darubini ya bunduki yake akiielekezea ndani ya lile gari kupitia
kioo cha ubavuni. Alichokiona ndani ya lile gari Peugeot 504 kikamshtua sana.
Wale watu walikuwa wakitega mabomu mawili makubwa kwenye lile gari na tukio
lile likawa limemshangaza sana Koplo Tsega hata hivyo alijipa uvumilivu. Muda mfupi
baadaye mara akawaona wale watu wakitoka kwenye lile gari bila ya ule mfuko mweusi
huku wakiharakisha kuelekea kwenye lile jengo la ghorofa alipokuwepo Balimenya na
makachero wenzake.
Tukio lile likawa limempelekea Koplo Tsega aisogeze tena darubini ya bunduki
yake kutazama kwenye ile korido ya lile jengo la ghorofa alipokuwa akitazama hapo
awali. Haukupita muda mrefu mara akauona mlango mweusi uliokuwa kwenye
korido ya lile jengo ukifunguliwa. Kufunguliwa kwa mlango ule kukapelekea watu
wawili watoke nje. Koplo Tsega alipowachunguza vizuri watu wale mara akamuona
Balimenya akitoka kwenye ule mlango mweusi na kuanza kutimua mbio akielekea
upande wa kushoto wa ile korido walipokuwa makachero wenzake. Koplo Tsega
hakutaka kufanya makosa hivyo shingo ya Balimenya alipoenea vizuri kwenye msalaba
wa shabaha ya darubini yake akawahi kuvuta kilimi cha bunduki yake. Balimenya
hakupata nafasi ya kufurukuta kwani risasi moja tu iliyofunga safari ikaivunja na
kuikata vibaya shingo yake kiasi kwamba wale makachero wenzake waliokuwa kwenye
ile korido wakaanza kutimua mbio wakishuka ngazi kwa taharuki.
Koplo Tsega akiwa anaendelea kuendesha gari lake akakumbuka muda mfupi
baada ya tukio lile namna alivyomuona mwanaume mwengine akiwa anatoka kwenye
ule mlango mweusi kwenye ile korido huku mtu huyo akiwa amemdhibiti mwanaume
mwingine mwenye mwili mkubwa kwa kabari makini ya mkono wake wa kushoto na
mkono wa kulia ukiwa umeielekezea bastola yake kwenye kichwa cha yule mateka.
Akiwa kwenye maficho yale Koplo Tsega akaendelea kuwatazama vizuri wanaume
wale wawili kupitia darubini kali ya bunduki yake. Muda mfupi baadaye akajikuta
akishikwa na mduwao wa aina yake baada ya kumuona na kumkumbuka vizuri yule
mtu aliyemdhibiti vizuri mateka wake kwa kabari matata na bastola mkononi kuwa
alikuwa ndiye yule mtu aliyemfukuza kwenye lile jengo la Rupture & Capture siku
chache zilizopita.
Koplo Tsega akaendelea kukumbuka namna ambayo mtu yule na mteka wake
walivyoingia kwenye chumba cha lifti ya lile jengo la ghorofa alilomdungua Balimenya
kabla ya mtu huyo na mateka wake kuanza kushuka kwa lifti chini ya ya lile jengo.
Akaendelea kukumbuka namna alivyoshtuka wakati alipomuona yule mtu na mateka
wake wakielekea kwenye lile gari Peugeot 504 lililokuwa chini ya lile jengo huku likiwa
limetegwa mabomu mawili na wale watu hatari ambao sasa alikuwa na hakika kuwa
walikuwa na ushirika mkubwa na Balimenya.
Koplo Tsega akiwa anaikumbuka ile taswira ya ile milipuko miwili mikubwa
iliyotegwa kwenye lile gari Peugeot 504 akajikuta akiishiwa nguvu pale alipokumbuka
kitu kilichotokea muda mfupi baadaye mara baada ya kumpa ishara fulani yule mtekaji
na mateka wake kuwa wasilikaribie lile gari wakati yeye bado akiwa kwenye kile
chumba cha lifti kwenye lile jengo la ghorofa la jirani na eneo lile.
Akiwa anaendelea na safari yake Koplo Tsega akajikuta akizama kwenye
tafakuri nzito juu ya yule mwanaume mtekaji ambaye siku chache zilizopita alikuwa
amefanikiwa kumkimbia kwenye lile jengo la Rupture & Capture. Kupitia mlolongo
wa matukio Koplo Tsega akawa na hakika kuwa mtu yule mtekaji hakuwa na ushirika
wowote na Balimenya na wale makachero wenzake. Hivyo kwa tafsiri nyingine ni
kuwa mtu yule mtekaji kwa namna moja au nyingine hakuwa na sababu ya kumuua
Momba na hivyo kisasi hakikufaa kuelekezwa kwake. Swali likabaki kuwa mtu yule
mtekaji ni nani na aliingiaje katika mkasa huu?. Na kama mtekaji yule hakuwa shirika
moja na Balimenya kwanini siku ile alitaka kumkamata yeye kwenye lile jengo la Rupture
& Capture muda mfupi baada ya kumdungua P.J.Toddo?. Koplo Tsega akaendelea
kujiuliza bila kupata majibu.
Hata hivyo Koplo Tsega akajikuta katikati ya mgogoro wa nafsi yake pale
alipoyakumbuka maelezo ya kutoka kwa wahudumu wa Hotel 92 Dar es Salaam
pamoja na picha zilizonaswa na kamera za usalama za hoteli ile zilizokuwa ukumbini
zikimuonesha mwanaume yule mtekaji akitoka muda mfupi baada ya ile maiti ya Sikawa
kugundulika kule chumbani kwake. Huyu mtekaji ni nani hasa katika mkasa huu?.
Koplo Tsega akaendelea kujiuliza bila kupata majibu kisha akaapa kuwa angefanya
jitihada zote katika kuufahamu ukweli wa kile kilichokuwa kikiendelea huku akiwaza
kuwa huwenda Sikawa asingeuwawa endapo angekuwa ameyafuata maelekezo yake
ya kutokufika kule chumbani kwake hadi pale ambapo angemhitaji. Kwani ilikuwa
baada ya Sikawa kufika kule chumbani siku ile na kumkosa Koplo Tsega alikuwa
amefungua mlango wa kile chumba kwa funguo aliyoichukua eneo la mapokezi na
kuingia mle chumbani akimsubiri Koplo Tsega.
Saa nane na nusu usiku ilipotimia Koplo Tsega akaegesha gari lake barabara ya
pili kutoka kule yalipokuwa maskani ya Balimenya mtaa wa Undali eneo la Upanga.
Kisha akashuka na kuanza kutembea kwa miguu akielekea kwenye maskani hayo.
Taarifa alizokuwa amezipata kupitia nyaraka za Pierre Kwizera zilikuwa zimemsaidia
kufahamu kwa wepesi zaidi jina la mtaa na nyumba aliyokuwa akiishi Balimenya.
Wakati huu wa usiku wa manane ulikuwa umepelekea sehemu kubwa ya eneo
la Upanga kugubikwa na ukimya wa aina yake. Kelele pekee zilizokuwa zikisikika
zilikuwa ni zile za mbwa waliokuwa wakibweka ndani ya mageti makubwa ya majumba
ya kifahari yaliyokuwa eneo lile.
Koplo Tsega akaendelea kutembea kwa makini huku mara kwa mara akigeuka
nyuma na kutazama kama kungekuwa na mtu yeyote aliyekuwa akimfuatilia. Hali
bado ilikuwa tulivu hivyo alipofika kwenye jengo la ofisi ndogo za shirika la posta
akashika uelekeo wa upande wa kushoto akiingia kwenye mtaa wenye nyumba
aliyokuwa akiishi Balimenya. Ukimya wa mtaa ule ukampelekea azisikie vizuri hatua
zake zilivyokuwa zikisafiri kwa utulivu barabarani. Bastola yake ikiwa tayari mkononi
Koplo Tsega akaapa kumtia adabu mtu yeyote ambaye angeonekana kuleta kizuizi
mbele yake.
Mara tu Koplo Tsega alipomaliza kulipita lile jengo lenye ofisi ndogo za posta
mbele kidogo akalipita jengo la ofisi za TTCL kisha akaingia upande wa kushoto
kwenye kichochoro kidogo kilichokuwa baina ya uzio wa bustani ndogo ya wazi na
jengo la ghorofa la shirila la nyumba la taifa. Wakati alipokuwa akimaliza kukatisha
kwenye kichochoro kile mara akasita na kusimama baada ya kuhisi kuwa kulikuwa na
mtu kama siyo watu waliokuwa sehemu fulani kwenye bustani ile wamejibanza.
Hisia zake zikimtanabaisha hivyo Koplo Tsega akasimama kwa utulivu huku
akiyatembeza macho yake kwa makini kulikagua vizuri eneo lile la bustani. Hata
hivyo hakumuona mtu yeyote isipokuwa mvua na hisia za upepo mwepesi uliyokuwa
ukiendelea kuvuma na kuyumbisha matawi ya miti iliyokuwa eneo lile. Hatimaye
akazipuuza hisia zake na kuendelea mbele na safari yake.
Koplo Tsega akaendelea kutembea na alipokuwa mbioni kufika mwisho wa
kichochoro kile hisia kama zile za awali zakamjia tena lakini mara hii kwa namna
tofauti kidogo kwani nyuma yake akahisi ni kama vile kulikuwa na mtu fulani aliyekuwa
akimfuatilia. Hisia hizo zikampelekea achepuke na kujibanza kwenye mti mmoja
uliokuwa jirani na eneo lile huku akiwa ameikamata vema bastola yake mkononi.
Kutoka pale nyuma ya mti ule alipojibanza,Koplo Tsega akageuka taratibu na
kutazama kule nyuma alipotoka safari hii akiwa makini zaidi kuyatembeza macho
yake katika vipenyo vyote vya eneo lile. Bado hakuweza kumuona mtu yeyote na hali
ilikuwa tulivu kama ilivyokuwa mwanzo. Hata hivyo Koplo Tsega hakutaka kuridhika
mapema kuwa hali ilikuwa shwari hivyo akaendelea kujibanza nyuma ya ule mti kwa
muda mrefu zaidi huku akitarajia kumuona mtu yeyote akijitokeza.
Lakini hali ilikuwa tofauti kwani hakukuwa na mtu yeyote aliyejitokeza na hali
ile ikampelekea ajione kuwa ni mwenye wasiwasi mwingi na woga usiyokuwa na
sababu za msingi. Hatimaye akaamua ayaache maficho yale na kuingia tena kwenye
kile kichochoro na wakati akitembea kuendelea na safari yake hakutaka tena kugeuka
nyuma ingawa alikuwa amejidhatiti kwa kila hali kukabiliana na hatari yoyote ambayo
ingejitokeza.
Alipofika mwisho wa uchochoro ule Koplo Tsega akaingia upande wa kulia
akitembea katikati ya uwazi mpana kidogo uliotenganisha jengo moja la ghorofa la
shirika la nyumba la taifa na uzio wa eneo la mahakama. Baada ya kutembea safari
fupi kwenye uwazi ule Koplo Tsega akawa amefika sehemu kulipokuwa na ngazi
za kuelekea juu ya lile jengo la ghorofa la shirika la nyumba la taifa kwa upande wa
kushoto. Koplo Tsega alipozifikia ngazi zile kabla ya kuanza kuzipanda akageuka tena
na kutazama nyuma. Hakumuona mtu yeyote hivyo akaanza kuzipanda zile ngazi kwa
utulivu huku akiwa ameikamata vyema bastola yake mkononi.
Usiku bado ulikuwa tulivu na wenye ukimya wa aina yake na kwa mbali sauti pekee
iliyosikika ilikuwa ni sauti ya manyunyu ya mavua iliyokuwa ikiendelea kunyesha.
Katika ghorofa ya tatu ya jengo lile la ghorofa nyumba namba 38 ndipo yalipokuwa
maskani ya Balimenya. Koplo Tsega akajikuta akikumbuka wakati alipokuwa
akiendelea kuzipanda zile ngazi taratibu huku mara kwa mara akisimama na kusikiliza
kama kungekuwa na sauti yoyote ya hatua za mtu aliyekuwa akimfuatilia nyuma yake.
Hakusikia sauti yoyote hivyo bado hali ilikuwa tulivu.
Akaendelea kuzipanda zile ngazi na alipofika kwenye korido ya ghorofa ya pili
Koplo Tsega akasimama tena huku akiyatathmini vizuri mandhari ya eneo lile. Katika
sehemu ile hapakuwa na makazi ya watu isipokuwa ofisi za shirika fulani la mtu binafsi
kutokana na vyeo vilivyokuwa vimeandikwa kwenye baadhi ya milango iliyokuwa
kwenye korido ile na nembo za shirika hilo. Mwanga wa taa iliyokuwa kwenye korido
ile ulikuwa hafifu na hapakuwa na dalili za uwepo wa mtu yeyote eneo lile. Hivyo
hatimaye akaendelea na safari yake akipanda ngazi kuelekea ghorofa inayofuata.
Koplo Tsega alipofika ghorofa ya tatu akagundua kuwa hali ilikuwa tofauti
kidogo na zile ghorofa za chini. Kulikuwa na milango nane ya vyumba vilivyokuwa
vikitazamana na korido ile na mandhari yake yalidhihirisha kuwa eneo lile lilikuwa
likikaliwa na watu. Mlango wa nyumba namba 38 ulikuwa mwisho upande wa
kushoto wa korido ile. Koplo Tsega mara tu alipoingia kwenye korido ile akatembea
kwa utulivu huku akiyatembeza macho yake upande huu na ule. Kitendo cha kuuona
mlango wenye namba 38 upande wa kushoto kikampelekea asimame kwa utulivu nje
ya mlango ule huku akiyatega kwa makini masikio yake ili kunasa hali ya utulivu wa
eneo lile. Hali bado ilikuwa tulivu hivyo akausogelea karibu ule mlango huku akiyatega
tena masikio yake kwenye tundu la kitasa cha ule mlango. Utulivu wa ndani ya ile
nyumba ikawa ni dalili tosha kuwa mle ndani hapakuwa na mtu yoyote.
Akiwa bado ameikamata vema bastola yake mkononi Koplo Tsega akasimama na
kuyatembeza tena macho yake kwenye ile korido. Ukimya wa eneo lile ukamtanabaisha
kuwa bado alikuwa peke yake.
Hivyo hatimaye akakishika kitasa cha ule mlango wenye namba 38 juu yake na
kuusukuma taratibu. Ule mlango ulikuwa umefungwa na imara kama jiwe na hapakuwa
na njia mbadala ya kuufungua mlango ule bila ya funguo kama lengo lingekuwa ni
kutowashuta wakazi wa eneo lile. Hivyo Koplo Tiglis akaingiza mkono mfukoni na
kuchukua mkungu wa funguo malaya ambapo alianza kujaribu kuufungua ule mlango
kwa funguo moja baada ya nyingine. Alipoifikia funguo ya nne majibu yakapatikana.
Kabari ya kitasa cha mlango ule ikafyatuka na hapo akakizungusha kile kitasa taratibu
huku akiusukuma ule mlango kwa ndani. Ule mlango ukafunguka taratibu huku
mdomo wa bastola yake akiutanguliza mbele.
Mara baada ya kuingia mle ndani Koplo Tsega akaurudishia ule mlango nyuma
yake na kuwasha taa ambayo swichi yake ilikuwa nyuma ya ule mlango. Baada ya
kuyatembeza macho yake akiyatathmini kwa haraka mandhari ya mle ndani nafsi
yake ikamtanabaisha kuwa sehemu ile ilikuwa sebule ya Belimenya. Kulikuwa na
makochi makubwa manne ya sofa ya vitambaa vyeusi yanayopendeza huku yakiwa
yamepangwa katika mtindo wa kuizunguka meza fupi na nyeusi ya kioo iliyokuwa
katikati ya sebule ile.
Sehemu fulani upande wa kushoto ukutani kulikuwa na runinga kubwa na
chini yake kulikuwa na meza fupi yenye king’amuzi cha Dstv na deki moja ya DVD
iliyounganishwa na spika mbili zilizosimamishwa kando yake. Sakafuni kulikuwa
na zulia zuri la manyoya lenye rangi ya ngozi ya pundamilia na hivyo kuyapelekea
mandhari yale yapendeze sana.
Kwenye kona ya sebule ile upande wa kulia kulikuwa na jokofu kubwa la rangi ya
kijivu lenye milango miwili ya juu na chini. Pembeni ya jokofu lile kulikuwa na stuli
ndefu na juu ya stuli ile kulikuwa na feni dogo. Wakati Koplo Tsega akipiga hatua zake
kuyatathmini vizuri mandhari yale mbele yake akaliona kabati dogo lililokuwa umbali
wa hatua chache kutoka pale ulipokuwa ule mlango wa kuingilia.
Mbele ya sebule ile upande wa kulia kulikuwa na mlango wa kuelekea chumbani
na mlango ule ulikuwa umefunguliwa nusu na kuachwa wazi. Koplo Tsega alipoufikia
mlango ule akasogeza pazia pambeni na kupitia mwanga hafifu uliopenya aliweza
kuona mle ndani.
Kilikuwa chumba kikubwa chenye kitanda kipana cha futi sita kwa sita. Kitanda
hicho kilikuwa kimefunikwa vizuri kwa shuka safi zenye rangi ya hudhurungi na mito
miwili ya kuegemea. Pembeni ya kitanda kile kulikuwa na meza fupi yenye redio na taa
ndogo ya Lampshade pembeni yake.
Kwa upande wa mbele kitanda kile kilitazamana na kabati kubwa la nguo ambalo
milango yake ilikuwa imefungwa. Kulikuwa na nguo chache za kiume zilizokuwa
zimetundikwa kwenye kining’inizo maalum cha nguo kilichokuwa ukutani. Koplo
Tsega akapiga hatua zake taratibu na kusimama kando ya kitanda kile akiyatembeza
macho yake mle ndani huku akikumbuka vizuri kuwa Balimenya alikuwa hajaoa wala
kuishi na mwanamke.
Mlango mwingine uliokuwa kwenye kona ya chumba kile kwa upande wa kushoto
ulikuwa ni wakuelekea kwenye chumba cha maliwato. Koplo Tsega alipoufikia mlango
ule na kuusukuma na hapo macho yake yakajikuta yakitazamana na sinki kubwa la
kuogea pamoja na choo cha kukaa cha marumaru kilichopakana na bomba dogo la
maji.
Koplo Tsega alipogeuka nyuma akawa akitazamana na kitanda cha mle ndani
huku akiikumbuka sehemu ya ukumbi mdogo wa kulia chakula iliyokuwa ikipakana
na sebule na jiko ambako bado alikuwa hajazikagua sehemu hizo.
Akiwa ameanza kuridhishwa na hali ya usalama wa mle ndani Koplo Tsega
akaanza kufanya upekuzi kwenye kile chumba. Chini ya godoro hakukuwa na kitu
chochote cha maana zaidi ya faili moja lenye nyaraka muhimu za ofisi ya Balimenya.
Koplo Tsega akakiacha kitanda kile na kuziendea droo mbili za ile meza fupi ya mle
chumbani ambazo nazo hazikuwa na kitu chochote cha maana.
Hatimaye jitihada zake akazihamishia kwenye lile kabati la nguo lililokuwa
likitazamana na kitanda cha mle ndani. Alipoanza upekuzi katika droo ya kwanza
akakuta bastola ndogo aina ya 25 Revolver,magazini mbili za bastola hiyo zilizojaa risasi
na kitambulisho cha kazi cha Belimenya. Ndani ya droo ya pili kulikuwa na mafaili
kadhaa yenye taarifa zinazoihusu ofisi ya Belimenya. Droo ya mwisho ya meza ile
ilikuwa imefungwa. Koplo Tsega akatia utundu wake na ndani ya muda mfupi akawa
amefanikiwa kuifyatua kabari ya droo ile na kuifungua. Mle ndani hakukuwa na kitu
kingine zaidi ya bahasha moja tu ya kaki hivyo Koplo Tsega akaichukua bahasha ile na
kuanza kuichunguza. Ilikuwa bahasha nyepesi yenye kitu mfano wa karatasi nyepesi
ndani yake na juu ya bahasha ile hakukuwa na maelezo yoyote.
Koplo Tsega akaichukua bahasha ile na kuanza kuitathmini kana kwamba ndiyo
kitu pekee alichokuwa akikihitaji. Lakini wakati akiwa anaendelea na tathmini ile hisia
zake zikamtanabaisha kuwa hatua chache nyuma yake kulikuwa na mtu aliyekuwa
akimtazama. Kuitowesha hofu iliyoanza kuzitawala hisia zake akapiga moyo konde
huku akiupisha utulivu kichwani mwake. Hakupata utulivu kwani mikono yake
ilikuwa imeanza kutetemeka huku jasho jepesi likimtoka. Hata hivyo akajihimili na
kuikamata vyema bastola yake mkononi huku akipanga kugeuka ghafla na kufanya
shambulizi la uhakika kwa mtu yoyote ambaye angekuwa nyuma yake akimvizia kwa
hila. Hata hivyo alikuwa amechelewa.
“Tupa bastola yako chini mrembo” sauti ya kiume kutoka nyuma yake ilimuonya.
“Wewe ni nani?” Koplo Tsega akauliza huku sauti yake ikionekana kupwaya.
“Wewe ni nani na umefuata nini humu ndani?” ile sauti nyuma yake ikaongea
kwa tahadhari huku ikilipuuza swali lake na Koplo Tsega alipotaka kugeuka nyuma
akajikuta akikabiliana na maumivu makali ya ngumi mbili kavu mbavuni mwake.
“Utii ni bora kuliko shuruti” yule mtu akasisitiza
Koplo Tsega akaendelea kugugumia maumivu makali yaliyokuwa yakisambaa
mwilini mwake na wakati akifanya hivyo mtu mwingine akaongezeka mle ndani
ambaye alimfikia na kuanza kumpekua kila mahali. Upekuzi ule ulipoisha ile bahasha
ya kaki na bastola yake mkononi vikawa vimechukuliwa na yule mtu.
“Geuka nyuma na mikono juu!” ile sauti nyuma yake ikamtahadharisha na Koplo
Tsega alipogeuka nyuma akajikuta akikabiliana na njemba mbili matata zikimtazama
kwa hasira. Miili ya wanaume wale ilikuwa imeshiba mazoezi ya uhakika. Mmoja
alikuwa mfupi na mwingine alikuwa mrefu ingawa tofauti ya vimo vyao haikuwa
kubwa sana. Wote walikuwa wamevaa suti nadhifu nyeusi na bastola zao mikononi.
Koplo Tsega akabaki akitazamana na wale watu kwa sekunde kadhaa bila mtu
yeyote kutia neno kisha yule mtu mrefu akamfanyia ishara fulani yule mtu mfupi na
hapo yule mtu mfupi akaondoka. Muda mfupi baadaye yule mtu mfupi akarejea na
kiti kimoja alichokichukua kutoka kwenye meza ya chakula ya mle ndani na kukiweka
kando ya kitanda kilichokuwa mle chumbani.
“Karibu uketi mrembo kwani tumeona kuwa hakuna haja tena ya kutumia nguvu
kubwa kama utakuwa tayari kutupa ushirikiano” yule mtu mfupi akaongea kwa utulivu
ingawaje sura yenye chuki bado haikutoweka usoni mwake. Koplo Tsega akajikuta
akijishauri kuwa akae kwenye kile kiti au asikae na wakati akiendelea kujishauri
akashangaa akichotwa mtama wa nguvu na yule mtu mfupi hali iliyompelekea matako
yake yatue kwa kishindo juu ya kiti kile na hapo akapiga yowe la maumivu. Koplo
Tsega alipotaka kufurukuta akatandikwa ngumi nyingine tatu mgongoni huku shingo
yake ikienea vizuri kwenye kabari matata ya yule mtu mfupi.
Kufumba na kufumbua akajikuta amefungwa kamba iliyokazwa kisawasawa
kama mnyama anayetayarishwa kuchinjwa. Mambo yote yakafanyika kimyakimya na
zoezi lile lilipokamilika zile njemba mbili zikashika pembe mbili za kile kiti na kuanza
kukiburuta kile kiti kuelekea kwenye kile chumba cha maliwato kilichokuwa kwenye
kona ya kile chumba.
“Mnanipeleka wapi nyinyi majangili?” Koplo Tsega akauliza huku ameshikwa na
hofu.
“Tunataka kukusaidia mrembo”
“Pumbavu! nani aliyewaambia kuwa nahitaji msaada wenu?” Koplo Tsega akauliza
kwa kufoka
“Hujatuomba ila tumegundua kuwa unahitaji msaada na kwa vile ndiyo kazi yetu
basi hapajaharibika neno” yule mtu mrefu akaongea kwa utulivu lakini bila kujali huku
kwa pamoja wakiendelea kumburuta Koplo Tsega kwenye kile kiti kuelekea kwenye
kile chumba cha maliwato.
Mle ndani ya kile chumba cha maliwato kulikuwa na beseni kubwa la kuogea
pembeni ya koki ya maji. Wale watu wakaendelea kumburuta Koplo Tsega hadi kando
ya lile beseni la kuogea huku akiwa bado amefungwa kwenye kile kiti. Walipofika
yule mtu mfupi akamchapa Koplo Tsega makofi kadhaa na kumsogeza kando ya lile
beseni kisha taratibu akaanza kufungulia maji kwenye lile beseni na hapo mahojiano
yakaanza.
“Wewe ni nani?” yule mtu mrefu akasogea karibu na kuanza kumhoji Koplo
Tsega kwa utulivu huku akiinama chini vizuri ili waweze kutazamana.
“Mbona siwaelewi?” Koplo Tsega akawauliza wale watu kwa hila hata hivyo
akajikuta akiambulia makofi mawili mengine ya usoni.
“Jibu swali kama ulivyoulizwa na usitupotezee muda wetu” yule mtu mfupi
akafoka huku akiisukasuka ovyo shingo ya Koplo Tsega na kumtazama kwa hasira.
“Naitwa Sama” hatimaye Koplo Tsega akaongea kinyonge akidanganya tukio
lililowapelekea wale watu watazamane kidogo kabla ya kuendelea na mahojiano.
“Umefuata nini humu ndani?” yule mtu mrefu akamuuliza Koplo Tsega kwa
utulivu.
“Mimi ni mchumba wa Balimenya” Koplo Tsega akajitetea kwa hila huku
akiyatembeza macho yake taratibu kuwatazama wale watu na alipomaliza akahitimisha
kuwa wale watu walikuwa wageni kabisa machoni mwake ingawa hakuwa na shaka
yoyote kuwa walikuwa ni maafisa usalama.
“Unadhani tunaweza kuuamini huo uongo wako dhaifu?” yule mtu mrefu akauliza
kwa utulivu.
“Mtafuteni mwenyewe mumuulize kama hamniamini” Koplo Tsega akajitetea
kwa hila huku akifahamu fika kuwa hadi kufikia pale Balimenya alikuwa mfu kwa
risasi zake makini zilizohitimisha uhai wake kwenye lile jengo la ghorofa kule maeneo
ya posta katikati ya majengo marefu ya ghorofa.
“Tangu lini msichana mrembo kama wewe ukaenda kwa mchumba wako na
bastola mkononi?” yule mtu mrefu akamuuliza Koplo Tsega kwa utulivu huku
akiigeuzageuza ile bastola ya Koplo Tsega na kuitazama mikononi mwake.
“Bastola hiyo siyo yangu” Koplo Tsega akajitetea.
“Kama siyo yako ni ya nani?” yule mtu mfupi akasogea karibu na kuuliza kwa
shauku.
“Ni ya Balimenya” Koplo Tsega akajitetea kwa hila hata hivyo uongo wake
haukufua dafu.
“Usidhani kuwa sisi ni watoto wadogo kama wewe. Tunatambua silaha zote
zinazomilikiwa na maafisa usalama wetu na hii bastola haipo miongoni mwazo” yule
mtu mfupi akafafanua
“Nyinyi ni maafisa usalama?” Koplo Tsega akauliza huku akijitia mshangao
hata hivyo hakujibiwa kitu badala yake yule mtu mfupi akautoa mfuko mweusi
wa kitambaa kutoka mfukoni mwake na kumvalisha Koplo Tsega kichwani kisha
mahojiano yakaendelea
“Tuambie vizuri wewe ni nani na umefuata nini humu ndani vinginevyo utakiona
cha mtema kuni” yule mtu mrefu akauliza kwa utulivu kama mtu ambaye hakuwa
ameyasikia yale maelezo yote yaliyotangulia.
“Nimekwisha waambia kuwa mimi naitwa Sama,mchumba wa Balimenya. Mbona
hamtaki kunielewa?” Koplo Tsega akaendelea kujitetea kwa hila hata hivyo hakuna
aliyemsemesha tena badala yake akainamishwa kwenye kile kiti alichoketi na kichwa
chake kuzamishwa kwenye yale maji ya beseni kubwa la kuogea ambalo yale maji
yaliyokuwa yakimiminika kwenye ile koki tayari yalikuwa mbioni kujaa.
Likiwa ni tukio la ghafla ambalo Koplo Tsega hakuwa amelitarajia hivyo akajikuta
akifurukuta bila mafanikio kwani wale watu waliendelea kumkandamiza kwenye yale
maji ya lile beseni kwa nguvu zao zote hadi pale walipoanza kuona kuwa alikuwa
akielekea kuishiwa nguvu ndipo wakamuachia huku akihema ovyo. Walipomuweka
sawa yule mtu mfupi akauondoa ule mfuko mweusi kichwani kwa Koplo Tsega na
kumkaba shingo kwa kiganja chake huku akimsogelea kumuuliza.
“Tuambie wewe ni nani?” Koplo Tsega hakujibu chochote badala yake akaendelea
kukohoa ovyo kwani alikuwa amepaliwa vibaya na yale maji huku macho yamemtoka
pima.
“Hatuwezi kukuua msichana mrembo kama wewe. Hata hivyo kama hautotupa
ushirikiano wa kutosha hatuna budi kufanya hivyo”
“Tuambie wewe ni nani na umefuata nini humu ndani” yule mtu mfupi akauliza
kwa msisitizo.
“Nimekwisha waeleza mbona hamtaki kunielewa?” Koplo Tsega akaendelea
kujitetea hata hivyo wale watu wakampuuza na badala yake akashtukia akivalishwa
tena ule mfuko mweusi wa nguo na kichwa chake kukandamizwa tena kwenye yale
maji ya lile beseni la kuogea huku mara hii zoezi lile likifanyika kwa muda mrefu zaidi.
Koplo Tsega akijitahidi kujitetea bila mafanikio.
Wale watu wakaendelea kumkandamiza Koplo Tsega kwenye yale maji ya beseni
la kuogea mle ndani hadi pale walipoona tena kuwa alikuwa ameanza kuishiwa nguvu
ndipo wakamuacha. Yule mtu mfupi akautoa tena ule mfuko mweusi kichwani mwa
Koplo Tsega tukio lililompelekea Koplo Tsega atapike maji mengi kwa mkupuo na
kuanza kukohoa ovyo huku macho yamemtoka.
“Msichana mrembo kama wewe haipendezi kabisa kuwa muongo. Tuambie wewe
ni nani na umefuata nini humu ndani?” yule mtu mfupi akamsogelea tena Koplo Tsega
na kumuuliza huku amemkwida shingoni hata hivyo Koplo Tsega hakuzungumza
neno badala yake aliendelea kukohoa kama aliyepaliwa huku akihema ovyo. Kitendo
cha Koplo Tsega kukaa kimya kikampelekea yule mtu mrefu amsogelee na kumchapa
kofi zito usoni kabla ya kumwambia
“Ni afadhali utuambie ukweli vinginevyo tutakuua humu ndani na kwenda
kuitelekeza maiti yako sehemu kusikojulikana”
“Sina jingine ninalolijua zaidi ya huo ukweli niliyowaambai” Koplo Tsega akaongea
kwa utulivu huku akiendelea kuhema ovyo na macho yamemtoka kwa hofu.
“Hii ndiyo nafasi pekee uliyonayo mrembo vinginevyo usidhani kuwa tutakuwa
na muda mwingine wa kukulazimisha utueleza ukweli” yule mtu mfupi akamsogelea
tena Koplo Tsega na kuishika shingo yake kwa kiganja imara cha mkono wake huku
akimvutia karibu yake na kumtazamana wakati mtutu wa bastola yake mkononi
ukiikunakuna shingo ya Koplo Tsega. Kisha taratibu yule mtu mfupi akaihamishia
bastola yake kwenye matiti ya Koplo Tsega huku akiyatekenya taratibu kwa mtutu wa
bastola yake huku tabasamu la kifedhuli likiumbika usoni mwake.
Tukio lile likampelekea Koplo Tsega ashikwe na hasira na kisha kumtemea
mate usoni yule mtu mfupi. Yule mtu mfupi kuona vile akashikwa na hasira hivyo
akasimama na kujifuta yale mate usoni kwa kiganja chake kisha akaanza kumchapa
makofi ya nguvu na ya mfululizo Koplo Tsega huku akiporomosha matusi ya kila
namna. Kipigo kile kilipozidi mwenzake akaingilia kati na kumzuia. Koplo Tsega
akapiga mayowe kwa nguvu ya kuomba msaada kabla ya kuanza kuhema ovyo huku
damu nyingi ikimtoka mdomoni na puani.
Haukupita muda mrefu mara yule mtu mrefu akasogea karibu na kuanza
kumburuta Koplo Tsega kwenye kile kiti hadi katikati ya kile chumba cha maliwato
kisha akachota yale maji kwenye lile beseni la kuogea kwa ndoo na kuanza kummwagia
Koplo Tsega pale kwenye kile kiti katika namna ya kumuweka sawa kisha akamsogelea
tena na kuendeleza mahojiano. Hali ya Koplo Tsega ikaanza kuwa mbaya na nguvu
mwilini zikaanza kumwishia taratibu. Kipigo cha nguvu kutoka kwa wale watu kikawa
kimeupelekea mdomo wake kuchanika sehemu ya chini na maumivu makali ya
mwamba wa pua yake.
“Kama hutaki kutueleza ukweli tutakuua”
“Mnanionea bure mimi sifahamu chochote” Koplo Tsega akajitetea hata hivyo
hakuna mtu aliyemsikiliza badala yake akajikuta akianza kukabiliana na kipigo cha
nguvu kutoka kwa wale watu. Kipigo chenye mchanganyiko wa ngumi,makofi na
mateke ya kila mahali. Hali ya Koplo Tsega ikazidi kuwa mbaya akawasihi wale watu
wamuache bila mafanikio. Hatimaye nguvu zikaanza kumuishia. Ile sauti ya mayowe
ya kuwasihi wale watu wamuache nayo ikaanza kufifia taratibu. Mwishowe uwezo wa
macho yake kuona nao ukaanza kupungua na mbele yake akawa akiliona wingu jepesi
la giza. Mdomo wake ukawa mzito kuongea. Mwishowe macho yamemtoka
“Msichana mrembo kama wewe haipendezi kabisa kuwa muongo. Tuambie wewe
ni nani na umefuata nini humu ndani?” yule mtu mfupi akamsogelea tena Koplo Tsega
na kumuuliza huku amemkwida shingoni hata hivyo Koplo Tsega hakuzungumza
neno badala yake aliendelea kukohoa kama aliyepaliwa huku akihema ovyo. Kitendo
cha Koplo Tsega kukaa kimya kikampelekea yule mtu mrefu amsogelee na kumchapa
kofi zito usoni kabla ya kumwambia
“Ni afadhali utuambie ukweli vinginevyo tutakuua humu ndani na kwenda
kuitelekeza maiti yako sehemu kusikojulikana”
“Sina jingine ninalolijua zaidi ya huo ukweli niliyowaambai” Koplo Tsega akaongea
kwa utulivu huku akiendelea kuhema ovyo na macho yamemtoka kwa hofu.
“Hii ndiyo nafasi pekee uliyonayo mrembo vinginevyo usidhani kuwa tutakuwa
na muda mwingine wa kukulazimisha utueleza ukweli” yule mtu mfupi akamsogelea
tena Koplo Tsega na kuishika shingo yake kwa kiganja imara cha mkono wake huku
akimvutia karibu yake na kumtazamana wakati mtutu wa bastola yake mkononi
ukiikunakuna shingo ya Koplo Tsega. Kisha taratibu yule mtu mfupi akaihamishia
bastola yake kwenye matiti ya Koplo Tsega huku akiyatekenya taratibu kwa mtutu wa
bastola yake huku tabasamu la kifedhuli likiumbika usoni mwake.
Tukio lile likampelekea Koplo Tsega ashikwe na hasira na kisha kumtemea
mate usoni yule mtu mfupi. Yule mtu mfupi kuona vile akashikwa na hasira hivyo
akasimama na kujifuta yale mate usoni kwa kiganja chake kisha akaanza kumchapa
makofi ya nguvu na ya mfululizo Koplo Tsega huku akiporomosha matusi ya kila
namna. Kipigo kile kilipozidi mwenzake akaingilia kati na kumzuia. Koplo Tsega
akapiga mayowe kwa nguvu ya kuomba msaada kabla ya kuanza kuhema ovyo huku
damu nyingi ikimtoka mdomoni na puani.
Haukupita muda mrefu mara yule mtu mrefu akasogea karibu na kuanza
kumburuta Koplo Tsega kwenye kile kiti hadi katikati ya kile chumba cha maliwato
kisha akachota yale maji kwenye lile beseni la kuogea kwa ndoo na kuanza kummwagia
Koplo Tsega pale kwenye kile kiti katika namna ya kumuweka sawa kisha akamsogelea
tena na kuendeleza mahojiano. Hali ya Koplo Tsega ikaanza kuwa mbaya na nguvu
mwilini zikaanza kumwishia taratibu. Kipigo cha nguvu kutoka kwa wale watu kikawa
kimeupelekea mdomo wake kuchanika sehemu ya chini na maumivu makali ya
mwamba wa pua yake.
“Kama hutaki kutueleza ukweli tutakuua”
“Mnanionea bure mimi sifahamu chochote” Koplo Tsega akajitetea hata hivyo
hakuna mtu aliyemsikiliza badala yake akajikuta akianza kukabiliana na kipigo cha
nguvu kutoka kwa wale watu. Kipigo chenye mchanganyiko wa ngumi,makofi na
mateke ya kila mahali. Hali ya Koplo Tsega ikazidi kuwa mbaya akawasihi wale watu
wamuache bila mafanikio. Hatimaye nguvu zikaanza kumuishia. Ile sauti ya mayowe
ya kuwasihi wale watu wamuache nayo ikaanza kufifia taratibu. Mwishowe uwezo wa
macho yake kuona nao ukaanza kupungua na mbele yake akawa akiliona wingu jepesi
la giza. Mdomo wake ukawa mzito kuongea. Mwishowe macho yakafunga taratibu taratibu na baada ya muda fahamu zikamtoka asijue kinachoendelea.
 
FAHAMU ZILIMRUDIA Koplo Tsega sambamba na maumivu makali mwilini
yaliyompelekea ahisi kutaka kutapika. Taratibu akataka kujisogeza kutoka pale
alipokuwa ameketi hata hivyo hakufanikiwa kwani haraka akakumbuka kuwa alikuwa
amefungwa kwenye kiti na wale wanaume wawili waliomteka na kuanza kumhoji mle
ndani. Koplo Tsega akayafumbua macho yake taratibu na kuanza kuyatembeza mle
ndani na taswira iliyoumbika machoni mwake ikamtanabaisha kuwa bado alikuwa
kwenye ile nyumba ya Balimenya lakini mara hii akiwa kwenye kile chumba kikubwa
na siyo kule kwenye maliwato alipokuwa akiteswa na wale wanaume wawili.
Koplo Tsega akaendelea kuyatembeza macho yake taratibu mle ndani ya kile
chumba katika namna ya kukipeleleza na kwa kufanya vile jambo moja likamshangaza.
Wale wanaume wawili waliokuwa wakimtesa mle ndani hawakuwepo
“Wameenda wapi?”Koplo Tsega akajiuliza pasipo kupata majibu. Alipoendelea
kuchunguza mbele yake kitandani akaona pakiti ya sigara na kiberiti cha gesi. Taa ya
mle ndani ilikuwa imewashwa na juu ya meza ndogo ya mbao iliyokuwa kando ya
kitanda juu yake kulikuwa na glasi mbili na mzinga mkubwa wa kilevi kando. Utulivu
bado ulikuwa mkubwa mle ndani.
“Wale watu watakuwa wameenda wapi?”Koplo Tsega akaendelea kujiuliza pasipo
kupata majibu hata hivyo kitendo cha kuziona zile glasi na ule mzinga wa pombe
kali juu ya ile meza ndogo pembeni ya kile kitanda mle chumbani kikawa kimeibua
hoja mpya kichwani mwake kuwa huwenda wale watu walikuwa wakitumia kile kilevi
wakati walipokuwa wakimsubiri azinduke baada ya kupoteza fahamu. Ile ingekuwa
nafasi nzuri ya kutoroka mle ndani kabla ya wale watu hawajarudi Koplo Tsega
akajikuta akiwaza.
Koplo Tsega alipotulia na kuyatega vizuri masikio yake mle ndani hakusikia kitu
chochote hivyo taratibu akaanza kuzifungua zile kamba alizofungwa kwenye kile kiti.
Haikuwa kazi rahisi kwani zile kamba zilikuwa imara na zilizofungwa kwa ufundi wa
hali ya juu kiasi cha kutoruhusu mwanya wowote wa kufurukuta. Hata hivyo Koplo
Tsega akiwa ameanza kuhisi kuwa ile ndiyo ingekuwa nafasi yake pekee ya kutoroka
mle ndani hakutaka kulaza damu badala yake akaendelea haraka kuzifungua zile
kamba alizofungwa kwenye kile kiti.
Ilikuwa ni wakati Koplo Tsega alipokuwa akimalizia kujifungua zile kamba kwenye
kile kiti ule mlango ulipofunguliwa na kisha wale wanaume wawili watekaji kuingia
mle ndani kwa mwendo hafifu wa kilevilevi huku bastola zao zikiwa mikononi. Koplo
Tsega hakuwa na namna ya kufanya zaidi ya kutulia kwenye kile kiti na kujidai kuwa
bado alikuwa amepoteza fahamu.
Wale watu walipoingia mle ndani yule mtu mrefu akasimama pale mlangoni huku
yule mtu mfupi akielekea pale kwenye kile alipofungwa Koplo Tsega.
“Mchunguze kama amerudiwa na fahamu?” yule mtu mrefu akaongea akimpa
maelekezo yule mtu mfupi. yule mtu mfupi akaendelea kujongea taratibu hadi pale
kwenye kile kiti alipofungwa Koplo Tsega na kisha kuanza kumchunguza kwa makini
lakini kwa kuwa Koplo Tsega alikuwa bado hajaziondoa zile kamba mwilini yule mtu
mfupi hakuweza kushtukia kitu chochote.
“Bado hajarudiwa na fahamu huyu!” yule mtu mfupi akaongea kwa kujiamini
baada ya kufanya uchunguzi wa kilevilevi.
“Una hakika?” mwenzake akamuuliza
“Kama huniamini basi uje umtazame wewe mwenyewe” yule mtu mfupi akaongea
kwa jazba kidogo baada ya kuona kuwa yule mwenzake bado ana mashaka na lile jibu
lake.
“Unadhani atarudiwa na fahamu mapema?” baada ya kitambo kifupi cha ukimya
kupita yule mtu mrefu pale mlangoni akauliza.
“Daktari anaweza kuwa na jibu la hakika zaidi hata hivyo naamini kuwa atarudiwa
na fahamu muda siyo mrefu kama tutaendela kusubiri”
“Mkuu atafurahi sana pale tutakapomkabidhi huyu mrembo mikononi mwake”
yule mtu mrefu akaongea huku akitabasamu.
“Hilo siyo jambo la kuharakisha Masam japo huyu dada anaonekana ni mtu hatari
kuliko tulivyomdhania hapo awali. Si umeona mwenyewe mifukoni tumemkuta na
kitabu kidogo chenye orodha ya majina ya watu wetu wa usalama waliouwawa. Mimi
naamini kuwa huyu ndiye muuaji mwenyewe tuliyekuwa tukimtafuta na siyo yule mtu
aliyetutoroka kule posta chini ya ghorofa. Huyu dada amevamia humu ndani akiwa
na bastola mkononi hii inamaanisha kuwa alikuwa amejipanga kukabiliana na hatari
yoyote ikiwezekana hata kutoa uhai wa mtu. Huyu dada ni mtu hatari sana tusifanye
naye mzaha hata kidogo” yule mtu mfupi akaongea kwa msisitizo huku akimtazama
Koplo Tsega pale kwenye kiti.
“Kama tutambana vizuri tunaweza kupata pesa yote kupitia zile hundi tulizozikuta
mkukoni mwake”
“Tutafanya kila litakalowezekana katika kuhakikisha kuwa pesa ya kwenye hizi
hundi inaishia mikononi mwetu vinginevyo tukizipeleka kwa wakubwa tutajikuta
tukiwafaidisha wao na familia zao wakati kazi kubwa tunaifanya sisi” yule mtu mfupi
akasisitiza.
“Kuna jambo fulani linaloendelea kufuatia haya mauaji ya wanausalama wenzetu
hata hivyo naamini kuwa huyu dada atakuwa akifahamu vizuri kila kitu. Hivyo atake
asitake mara tu atakapozinduka ni lazima tumbane vizuri atueleze nini kinachoendelea”
yule mtu mrefu akaongea kwa utulivu pale mlangoni.
“Turudi zetu kule sabuleni” yule mtu mfupi akapendekeza akimshawishi
mwenzake.
“Hapana! hatuwezi kuendelea kulewa,huyu dada siyo wa kumfanyia mzaha”
“Ondoa shaka Masam hatuwezi kukaa humu ndani na kumsubiri azinduke kwa
muda wake wakati Balimenya ametuachia vinywaji vingi kwenye jokofu lake” yule
mtu mfupi akajaribu kujenga hoja huku akiangua tabasamu la kilevi kisha akamuacha
Koplo Tsega pale kwenye kiti na kuelekea kwenye mlango wa kile chumba. Alipofika
akampigapiga yule mwenzake begani katika namna ya utani kisha akafungua ule
mlango na kutoka akielekea sebuleni. Yule mtu mrefu akaendelea kusimama pale
mlangoni akimtazama Koplo Tsega kwa utulivu kama anayefikiria jambo. Hata
hivyo baada kitambo kifupi cha ukimya kupita naye ni kama aliyehisi upweke kwa
kukosa mtu wa kuzungumza naye mle ndani. Hivyo na yeye akafungua ule mlango
wa chumba na kutoka akielekea kule sebuleni na baada ya muda mfupi kile chumba
kikawa kimerudiwa na ile hali yake ya ukimya wa awali.
Koplo Tsega akiwa na hakika kuwa wale watu wameshatoka mle chumbani na
kuelekea kwenye sebule ya ile nyumba akayafumbua tena macho yake na kuanza
kuyatembeza taratibu mle ndani. Hakumuona mtu yeyote na mandhari ya mle ndani
bado yalikuwa tulivu hivyo akaendelea kujifungua zile kamba pale kwenye kile kiti na
baada ya muda mfupi akawa amemaliza zoezi lile. Mara baada ya kumaliza kujifungua
zile kamba Koplo Tsega akasimama kichovuchovu huku maumivu makali ya kile
kipigo alichokipata yakianza tena kusambaa mwilini mwake. Koplo Tsega alipojikagua
mifukoni akajua kuwa kile kitabu chake chenye orodha ya majina ya watu aliokuwa
akiwatafuta na ile bahasha yenye hundi nyingi aliyoichukua chumba kwa Meja Khalid
Makame vyote vilikuwa vimechukuliwa na wale watu waliomteka mle ndani. Hivyo
bila kupoteza muda akaichukuwa ile chupa ya mzinga wa pombe kutoka juu ya ile
meza fupi iliyokuwa kando ya kitanda cha mle ndani na kuelekea kwenye ule mlango
wa kile chumba wa kuelekea sebuleni.
Kupitia tundu dogo la funguo kwenye kitasa cha ule mlango wa kile chumba
Koplo Tsega alipochungulia aliweza kuwaona wale wanaume wawili waliomteka.
Wote walikuwa wakitazama runinga iliyokuwa pale sebuleni huku taratibu wakiendelea
kujipatia kinywaji kwenye makochi ya sofa ya pale sebuleni na bastola zao zikiwa
mikononi. Koplo Tsega hakuwa na mashaka yoyote kuwa watu wale hawakuwa
wameshtukia chochote wakati yeye alipokuwa akijifungua zile kamba kwenye kile
kiti mle chumbani. Wakati akiendelea kuwachungulia wale watu kwenye lile tundu
la funguo kwenye kitasa Koplo Tsega akajikuta akiikumbuka bastola yake namna
ambavyo ingeweza kuwa msaada mkubwa katika kukabiliana na watu wale bila ya
kutumia nguvu. Hata hivyo alitambua kuwa suala lile lisingewezekana kwani ile bastola
yake ilikuwa imechukuliwa na wale watu.
Koplo Tsega akaendelea kuchungulia kwenye lile tundu la kitasa katika namna
ya kujithibitishia kuwa wale watekaji walikuwa wamezama kwenye hamsini zao na
aliporidhika na hali ile akauacha ule mlango na kuelekea kwenye kile chumba cha
bafu akipeleleza mazingira ya mle ndani. Hali ya mle ndani ilikuwa shwari hata hivyo
hakupata silaha yoyote ya kumsaidia hivyo akarudi tena kule chumbani na kuendelea
na upekuzi. Wakati akiifungua ile droo kwenye kabati akagundua kuwa hata ile bastola
iliyokuwa mle ndani nayo ilikuwa imechukuliwa na wale watu.
Ilikuwa ni wakati Koplo Tsega alipokuwa akiendelea na upekuzi mle ndani mara
ghafla akasikia sauti ya hatua za mtu akiukaribia ule mlango wa kile chumba. Haraka
Koplo Tsega akaichukua ile chupa ya mzinga wa pombe na kwenda kujibanza nyuma
ya ule mlango. Haukupita muda mrefu mara kitasa cha ule mlango wa kile chumba
kikazungushwa na ule mlango kusukumwa.
Mtu aliyeingia mle ndani alikuwa ni yule mtu mfupi huku akiwa ameitanguliza
bastola yake mbele kizembezembe. Ulikuwa ni muda mzuri kwa Koplo Tsega kufanya
shambulizi hivyo kwa kasi ya ajabu akatupa pigo moja makini la ile chupa nyuma ya
kichwa cha yule mtu mfupi. Tukio lile likasababisha sauti kali ya mpasuko wa ile chupa
na kabla yule mtu mfupi hajaanguka chini pigo jingine la teke la mkononi lililotupwa
na Koplo Tsega likaipokonya mkononi ile bastola ya yule mtu mfupi na kuitupa
hewani. Yule mtu akaanguka chini kama mzigo huku ile bastola ikitua mkononi mwa
Koplo Tsega. Yule mtu alipojitahidi kusimama haikuwezekana kwani risasi mbili za
mgongoni zikamrudisha chini na kumlaza kifudifundi huku akiwa hajitambui.
Kelele za mikikimikiki ya mle chumbani zikawa zimemshtua yule mtu mrefu kule
sebuleni hivyo haraka akasimama na kuikamata vyema bastola yake akinyata kwa
tahadhari kuusogelea ule mlango wa kile chumba. Koplo Tsega kuona vile akawahi
kujibanza nyuma ya ule mlango wa kile chumba huku akimvizia yule mtu na bastola
yake mkononi. Yule mtu akaendelea kunyata hadi pale mlangoni halafu kama aliyehisi
jambo lisilo la kawaida akasimama kwa utulivu huku akiyatega masikio yake kwa
makini kusikiliza mle ndani ya kile chumba. Hakusikia kitu chochote hata hivyo zile
kelele hafifu za zile risasi mbili kutoka kwenye bastola iliyofungwa kiwambo maalum
cha kuzuia sauti ya Koplo Tsega na zile kelele za mpasuko wa chupa mle ndani zikawa
zimemjengea tahadhari ya aina yake. Yule mtu mrefu akaendelea kusimama pale
mlangoni huku akijipa utulivu na alipoona hakuna kitu chochote kinachosikika mle
ndani akainama taratibu na kuchungulia kwenye like tundu la funguo kwenye kitasa.
Hakuona kitu chochote hivyo akasimama na kuanza kumuita mwenzake kwa sauti ya
chini yenye hofu.
“Remmy,kuna nini?” hakuna mtu aliyemjibu na hali ile ikazidi kumtia mashaka
yule mtu. Kitambo kifupi cha ukimya kikafuatia kabla ya yule mtu kuanza kumuita
tena yule mwenzake na alipoona kuwa hajibiwi akakishika kitasa cha ule mlango na
kuufungua ule mlango taratibu. Ule mlango ulipofunguka nusu yule mtu akachungulia
mle ndani hata hivyo hakuweza kumuona yule mwenzake kwani Koplo Tsega tayari
alikuwa amewahi kumburuta yule mtu na kumficha nyuma ya ule mlango. Yule mtu
mrefu akaendelea kusimama pale mlangoni huku akichunguliachungulia mle ndani
hata hivyo hakuona vizuri hivyo taratibu akaanza kunyata akiingia mle ndani na
bastola yake ikiwa tayari kufanya kazi mkononi.
Koplo Tsega akiwa tayari amejiandaa kukabiliana na yule mtu akakusanya nguvu
za kutosha na kutupa pigo makini la kareti akinuia kuiputa chini bastola ya yule mtu
mkononi. Mara hii lengo lake halikufanikiwa kwani yule mtu alikuwa makini na
mwerevu hivyo akawahi kuukwepesha kidogo mkono wake na kulipelekea pigo la
Koplo Tsega likate upepo bila mafanikio huku yule mtu akiwahi kujitupa mle ndani
sakafuni katika mtindo wa kujiviringisha kama gurudumu. Koplo Tsega alipofyatua
risasi kumlenga yule mtu,yule mtu tayari akawa ameshapotelea kwenye uvungu wa
kitanda cha mle ndani hivyo zile risasi nazo zikachana anga bila majibu.
Kimya kifupi kikafuatia mle ndani huku kila mmoja akijitahidi kumvizia mwenzake.
Yule mtu akajitokeza tena upande wa pili wa kile kitanda na kufyatua risasi hata
hivyo Koplo Tsega aliwahi kujitupa kando huku zile risasi zikimpunyua mgongoni.
Sasa kukawa na kutupiana risasi mle ndani huku kila mmoja akimvizia mwenzake
na kujificha. Majibishano ya risasi yakaendelea kurindima mle ndani na yule mtu
alipoona kuwa ameishiwa risasi akawahi kujitupa na kumkumba Koplo Tsega pale
aliposimama. Tukio lile likawapelekea wote kwa pamoja wapige mwereka na kuanguka
chini kwa kishindo. Hata hivyo yule mtu alipotaka kuwahi kusimama akajikuta tayari
kichwa chake kimeshaenea kwenye kabari matata ya miguu ya Koplo Tsega kabla ya
kukabiliana na mapigo mawili ya ngumi za uso zilizouvunja vibaya mwamba wa pua
yake. Yule mtu akapiga yowe la maumivu makali na kwa kuwa alikwishaiona hatari
ya kudhibitiwa na Koplo Tsega akakusanya nguvu na kuinuka huku akiwa amembeba
Koplo Tsega mzegamzega akipanga kwenda kumpigiza ukutani. Hata hivyo Koplo
Tsega alikuwa mjanja kuishtukia hila ile hivyo haraka akawahi kufungua ile kabari ya
miguu shingoni kwa yule mtu kisha walipofika ukutani akawahi kuikita mbele miguu
yake na kujitupa kwa nyuma huku akimchapa yule mtu kwa kiwiko cha mgongo na
yeye akirukia upande wa pili.
Yule mtu akajipigiza ukutani huku maumivu makali yakisambaa mwilini mwake
hata hivyo aliwahi kugeuka na kurudi kule nyuma kumkabili Koplo Tsega. Yule mtu
alipomfikia Koplo Tsega akatupa mapigo mawili ya ngumi usoni mwake hata hivyo
Koplo Tsega akawahi kuyapangua mapigo yale kisha akageuka na kutupa pigo moja
makini la teke la kifua lililomtupa chini yule mtu bila pingamizi lolote. Yule mtu kuona
vile akashikwa na hasira hivyo haraka akalivua koti lake la suti na kulitupa kando. Safari
hii Koplo Tsega hakufua dafu kwani wakati akifika pale chini kumkabili yule mtu
akajikuta akirudishwa kule alipotoka kwa pigo makini la teke la tumbo lililompelekea
apige yowe kali la maumivu na kabla hajatulia yule mtu tayari akawa amemfikia na
kuanza kumtupia mvua ya ngumi kila mahali. Koplo Tsega akajikuta akikabiliana na
wakati mgumu wa kuzikwepa na kuzipangua zile ngumi kwa haraka ili zisimfikie na
kuzidi kumtia udhaifu. Hata hivyo yule mtu hakumpa nafasi ya kujitetea kwani akawa
akizidisha mashambulizi zaidi na ya nguvu.
Koplo Tsega kuona vile akawahi kuinama na kumkwepa yule mtu huku akijirusha
juu ya kile kitanda na kujiviringisha akiangukia upande wa pili. Yule mtu kuona vile
akamfuata Koplo Tsega kule alipoangukia akipita juu ya kile kitanda hata hivyo
alikwishachelewa kwani wakati akifika katikati ya kile kitanda Koplo Tsega akawahi
kukibinua kile kitanda na kumrusha yule mtu kule alipotoka na hapo chaga za kile
kitanda zikavunjika. Yule mtu kuona vile akakisogeza kile kitanda pembeni na
kuchukua mbao moja ya chaga kisha akaruka karibu na kumkabili Koplo Tsega pale
alipokuwa. Alipomfikia akaanza kutupa mapigo mengi kwa kutumia ile mbao ya
chaga ya kitanda. Koplo Tsega akawa akihama kwenda upande huu na ule kuyakwepa
mapigo yale. Hata hivyo yule mtu alikuwa mjuzi wa hila hivyo akawa akimtishia Koplo
Tsega upande mmoja na kumtandika kwa ile mbao upande mwingine. Pigo moja
likampata Koplo Tsega begani na kumsababishia maumivu makali. Mapigo mengine
yaliyofuata akawa akiyapangua ingawa yalimuumiza vibaya mikononi. Pigo la mwisho
likampata vizuri mgongoni kiasi cha kuipelekea ile mbao kupasuka vipandevipande.
Koplo Tsega akapiga yowe kali la maumivu huku akipepesuka na kurudi nyuma.
Yule mtu kuona vile akazidi kumfuata Koplo Tsega haraka kumkabili hata hivyo
hakufanikiwa badala yake akajikuta akichapwa mateke mawili ya kifua yaliyomrudisha
nyuma na kumtupa kwenye kabati la mle ndani na kuvipelekea vioo vya kabari lile
kuvunjika na kuanguka chini.
Yule mtu kuona vile akazidi kushikwa na hasira hivyo akawahi kusimama na
kuanza kutimua mbio akipanga kumvaa Koplo Tsega na kuanguka naye chini. Koplo
Tsega akiwa tayari ameishtukia hila ile akamkwepa kidogo yule mtu na kumsindikiza
kwa teke lingine zito la mgongoni lililompigiza tena yule mtu ukutani. Yule mtu akiwa
tayari ameanza kuhisi dalili za kuzidiwa maarifa kwa hasira akachana shati lake na
kulitupa sakafuni huku akibakiwa na tai shingoni na singlet nyeupe kifuani kisha
haraka akasogea karibu kumkabili Koplo Tsega. Mapigo mawili ya kareti aliyotupa
moja likasababisha maumivu makali kwenye titi la kushoto la Koplo Tsega huku
jingine likitia udhaifu mkubwa kwenye shingo yake na kumpelekea apepesuke
akirudi kinyumenyume. Pigo la tatu lilipomfikia usoni akawahi kulikwepa na kisha
kuchomoka na kichwa kimoja makini kilichokongoloa meno manne ya mbele ya yule
mtu na kuusambaratisha vibaya mwamba wa pua yake na kupelekea kamasi nyepesi za
damu zianze kuchomoza taratibu kwenye matundu ya pua yake. Maumivu yale makali
yakampelekea yule mtu apige yowe kali la maumivu huku akiyumbayumba ovyo kama
bondia aliyetupiwa sumbwi zito.
Koplo Tsega kuona vile akajitupa hewani na kuzunguka kwa uhodari akitupa
mapigo mawili makini ya mateke yaliyokilevya vibaya kichwa cha yule mtu na kumtupa
tena kwenye lile kabati la mle chumbani. Lilikuwa ni pigo la funga kazi kwani yule
mtu alikipigiza vibaya kichwa chake kwenye kona ya lile kabati kabla ya kuanguka
chini na wakati akifanya vile Koplo Tsega akawa tayari amekwishajitupa sakafuni na
kuizoa ile bastola yake iliyomponyoka pale awali. Kufumba na kufumbua tayari akawa
ameishajiviringisha na kumfikia yule mtu pale alipoangukia kisha haraka akamkwida
yule mtu kwa tai yake shingoni. Hata hivyo alijikuta katikati ya mshangao kwani
tofauti na alivyotarajia mara hii Koplo Tsega alipata upinzani hafifu kwani kichwa cha
yule mtu kilikuwa kimepasuka kwa nyuma na damu ilikuwa imeanza kuvuja kutoka
kwenye lile jeraha.
“Mna shida gani na mimi?” Koplo Tsega akamuuliza yule mtu kwa hasira
huku akimkwida shingoni kwa ile tai yake. Yule mtu akajitahidi kuzungumza neno
hata hivyo halikusikika badala yake akasikika akitoa sauti hafifu ya mkoromo na
kujinyonganyonga miguu na mikono yake huku damu nyingi ikimtoka puani na
mdomoni.
“Nyinyi ni nani na mnashida gani na mimi?” Koplo Tsega akaendelea
kumuuliza yule mtu huku akizidi kumkwida shingoni kwa tai yake. Hata hivyo
yule mtu hakuzungumza kitu kwani hali yake ilikuwa imezidi kuwa mbaya sana na
hapakuonekana tumaini lolote la uzima nafsini mwake.
Koplo Tsega hakuona sababu ya kuendelea kupoteza muda hivyo akainama na
kuanza kumpekua vizuri yule mtu. Upekuzi ule ulifanyika kwa haraka na alipomaliza
akawa amepata kitambulisho cha kazi cha yule mtu kilichomtambulisha kama afisa
wa usalama,simu ya mkononi na ile bahasha yenye hundi nyingi aliyoichukua kule
nyumbani kwa Meja Khalid Makame. Vyote vikiwa kwenye mfuko wa ndani wa
koti la suti la yule mtu. Koplo Tsega Akaichukua ile bahasha na kuitia mfukoni kisha
akasimama na kumsindikiza yule mtu kwa risasi mbili za kifua zilizompelekea yule
mtu atikisike kidogo na kutulia huku roho yake ikiwa mbali na mwili.
Ndani ya muda mfupi uliofuata Koplo Tsega akawa pia amemaliza kumfanyia
upekuzi yule mtu mwingine mfupi ambaye ndiye aliyekuwa wa kwanza kumuua
mle ndani. Kwenye mfuko mrefu wa koti lake la suti akakuta magazine moja ya
bastola iliyojaa risasi,kitambulisho kimoja cha kazi kikimtambulisha yule mtu kama
afisa usalama kama yule mwenzake pamoja na ile bahasha iliyokuwa kwenye droo
ya kabati la mle chumbani ambayo wale watu walikuwa wameichukua kwake wakati
walipokuwa wakimteka mle ndani. Ile bahasha ya kaki akaitia mfukoni na kuanza
kuzunguka mle ndani akiitafuta ile bastola yake sehemu ilipokuwa imeangukia wakati
ule yale mapambano yalipokuwa yakiendelea mle ndani.
Kwa namna moja au nyingine Koplo Tsega aliamini kuwa wale watu aliopambana
nao mle ndani wangekuwa wakisubiriwa kutoa ripoti juu ya nini kilichokuwa
kikiendelea juu ya kazi waliyotumwa. Hivyo ukimya wao wa muda mrefu ungeweza
kusababisha mashaka kwa huyo mtu wao aliyekuwa akisubiri kupewa ripoti kutoka
kwao na hali hiyo ingeweza kumpelekea mtu huyo kufika pale mapema iwezekanavyo.
Koplo Tsega hakutaka kukutwa tena mle ndani hivyo kila alichokifanya alikifanya kwa
haraka. Muda mfupi uliofuata akawa amemaliza kufanya upekuzi makini katika ile
nyumba ya Balimenya pasipo kupata kitu chochote kingine muhimu katika uchunguzi
wake.Hatimaye hakuona sababu ya kuendelea kupoteza muda wake zaidi mle ndani
hivyo haraka akatoka kwenye ile nyumba ya Balimenya na muda mfupi uliyofuata
alikuwa akitembea taratibu na kwa tahadhari akielekea kwenye ile barabara ya mtaa
alipoegesha gari lake. Dakika chache baadaye Koplo Tsega alikuwa mbali na ile
nyumba ya Balimenya akikatisha kwenye mitaa ya jiji la Dar es Salaam huku mawazo
mengi yakipita kichwani mwake. Usiku bado ulikuwa mwingi.
 
TAARIFA ZA KUUWAWA KWA MAAFISA wengine wawili wa usalama
zilikuwa zimempelekea mkurugenzi mkuu wa usalama wa taifa M.D Kunzugala
kuiona kahawa aliyokuwa akiinywa imebadilika ghafla na kuwa chungu kama supu
ya mwarobaini ndani ya ofisi yake hii iliyopo juu ya jengo moja la ghorofa. Taratibu
akakishusha kikombe chake cha kahawa na kukiweka juu ya meza yake ya ofisini
huku mkono wake wa kushoto ukiwa bado umeshikilia kiwambo cha simu ya
mezani sambamba na sikio lake. Sauti ya upande wa pili wa ile simu haraka ilikuwa
imempelekea amfahamu mzungumzaji. Sulle Kiganja,kachero na mwanausalama
mwandamizi alikuwa akizungumza upande wa pili wa ile simu.
“Umejuaje?” M.D Kunzugala akauliza kwa taharuki akiendeleza maongezi yale.
“Nipo eneo la tukio Chifu” Sulle Kiganja akatanabaisha.
“Unamaanisha kuwa sasa hivi upo nyumbani kwa Balimenya?” M.D Kunzugala
akauliza kwa hakika
“Ndiyo Chifu,tumeikuta miili miwili ya maafisa wetu”
“Damn shit!,nani aliyefanya upuuzi huo?” M.D Kunzugala akauliza kwa jazba
huku akifahamu fika kuwa asingeweza kupata jibu la moja kwa moja hali iliyompelekea
aanze kulikumbuka tena jina la Chaz Siga,komandoo mstaafu wa jeshi la wananchi
wa Tanzania aliyesemekana ndiye aliyemteka mmoja wa wanausalama wake katika
lile jengo moja refu la ghorofa lililopo maeneo ya posta jijini Dar es Salaam. Hasira
zikamshika akakizoa kile kikombe cha kahawa juu ya meza na kukibamiza ukutani
kikipasuka vipande vipande na kutengeneza doa hafifu la kahawa nyeusi.
“Chifu?...” sauti ya Sulle Kiganja upande wa pili wa ile simu ikaita baada ya kitambo
kifupi cha ukimya kuzidi kuendelea.
“Una hakika gani kuwa hiyo miili ni ya watu wetu?” M.D Kunzugala akauliza
huku akijitahidi kuimeza hasira kali kifuani mwake kwa kitendo cha idara yake ya
usalama kuzidi kuchafuliwa na mauaji ya kiholela.
“Masam na Remmy ni maafisa wetu,nawatambua vizuri na ni watu wangu wa
karibu ambao wamekuwa wakifanya kazi na mimi kwa muda mrefu” Sulle Kiganja
akafafanua huku akikohoa kuiweka sauti yake sawa.
“Walikuwa wakifanya nini nyumbani kwa Balimenya?” M.D Kunzugala akauliza
kwa udadisi.
“Niliwatuma kuichunguza nyumba ya Balimenya na kuweka mtego wa kumnasa
mtu yeyote ambaye angeonekana kuinyemelea nyumba hiyo. Nadhani muuaji
aliwazidi nguvu” Sulle Kiganja akaongea kwa utulivu huku sauti yake ikipwaya baada
ya kuhisi alikuwa na sehemu ya kulaumiwa katika mauaji yale. Kitambo kifupi cha
ukimya kikapita huku kila mmoja akionekana kuzama kwenye fikra fulani kisha sauti
ya M.D Kunzugala ikarudiwa tena na uhai baada ya kikohozi hafifu kusikika.
“Bado sijaridhika na utendaji wako Sulle,nadhani haupo makini. Ulishindwa
kumkamata muuaji wakati ukiwa na watu wa kutosha na makini kule posta kwenye
jengo la ghorofa na sasa unanipigia simu kunifahamisha juu ya vifo vya maafisa wangu
waliouwawa na mtu huyohuyo uliyemruhusu kutoroka”
“Samahani sana Chifu nataka kukuhakikishia hilo halitatokea tena kwani tunafanya
kila jitihada za kuhakikisha kuwa mtu aliyehusika na mauaji haya anakamatwa na sheria
kuchukuwa nafasi yake” Sulle Kiganja akajitetea huku akianza kuingiwa na hofu juu ya
hatari ya kupoteza kazi yake. Hata hivyo M.D Kunzugala akayapuuza maelezo yake na
kumtumbukizia swali jingine.
“Nani aliyekufahamisha juu ya vifo vya hao maafisa usalama nyumbani kwa
Balimenya?”
“Nilikuwa nikiwasiliana nao kwa simu tukifahamishana juu ya kile kilichokuwa
kikiendelea lakini baadaye muda mrefu ulipita pasipo kusikia chochote kutoka kwao
ndiyo ikanibidi niongozane na maafisa wengine kufuatilia nini kinachoendelea” Sulle
Kiganja akafafanua.
“Nini kinachoendelea sasa hivi?” M.D Kunzugala akauliza huku sauti yake
ikionekana kukosa utulivu.
“Nimewasambaza watu wangu kila kona ya eneo hili kwani inaonekana kuwa
mauaji haya yamefanyika muda mfupi uliyopita. Hivyo ni imani yangu kuwa hadi
kufikia wakati huu muuaji atakuwa bado hajafika mbali sana na eneo hili. Kama bahati
itakuwa kwetu huwenda huyu muuaji tukamtia mikononi mapema iwezekanavyo”
“Sikiliza Sulle…,mimi sipendi mambo ya kubahatisha. Wapange vizuri watu wako
na uhakikishe kuwa huyo muuaji anakamatwa mapema sana iwezekanavyo. Kama
wewe unavyoona mambo magumu kwako na mimi pia ni hivyohivyo. Ungekuwepo
hapa ofisini kwangu na kushuhudia simu zinazomiminika kutoka kwa wakubwa wangu
sidhani kama ungethubutu kuzungumzia masuala ya bahati katika kushughulika na
hili jambo. Nimekwambia fanya linalowezekana kuhakikisha haya mauaji hayaendelei
na mhusika anakamatwa. Nimeitwa Ikulu ninakikao cha dharura na Rais juu ya haya
mauaji yanayoendelea. Ni matumaini yangu kuwa tutakapowasiliana tena utakuwa
na taarifa zinazoeleweka na siyo hizi blah! blah! zako unazonizugia na nazo kunipa
matumaini” M.D Kunzugala akamaliza kuongea kwa jazba na kukata simu kwa hasira.
 
MIFUPA 206 KEVIN e. MPONDA

MSITU WA GOVENDER KIVU YA KASKAZINI
Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo

UKIMYA WA KUTISHA ulikuwa umetawala eneo lote la msitu wa Govender
katika jimbo hili la Kivu ya Kaskazini nchini D.R Congo. Mvua kubwa
iliyonyesha kwa muda wa masaa matatu ilikuwa imeninyea chapachapa huku
nikiwa nimelalia tumbo langu juu ya tawi nene la mti mrefu na mkubwa aina ya Liana￾Entada gigas.
Mvua hiyo sasa ilikuwa imeacha athari kubwa za mafuriko ya kutisha na kelele
kali za vyura zilizokuwa zikihanikiza kila mahali pamoja na zile kelele nyingi za ndege
wa mwituni kama Mchochea mvua, Kitwitwi, Yombiyombi, Furukombe, Kanga,
Kware, Nderi, Tetere, Kirukanjia, Kulastara, Hondohondo, Kinega, Kuzumburu,
Gogota, Mnana, Mwewe, Vumatiti, Mwari, Kwarara na wengine wengi mara kwa
mara wakizikung’uta mbawa zao na kuzipa tena uhai sauti zao baada ya kusalimika na
athari za mvua hii kubwa ya aina yake.
Upepo mkali uliyokuwa ukivuma katika msitu huu uliliyumbisha tawi nililolilalia
huku na kule ukilisukasuka ovyo hata hivyo sikuliachia wala kukata tamaa kwani
kanuni za kijeshi zilinifunza uvumilivu hususani nikiwa kama mdunguaji makini
ninayehitaji matokeo mazuri ya kazi yangu.
Muda wa masaa tisa ulikuwa tayari umetokomea tangu nilipoukwea mti huu
mkubwa na mrefu msituni wenye maficho mazuri ya majani mengi makubwa
na matawi imara ya kuubeba uzito wangu bila wasiwasi wowote huku nikiendelea
kusubiri mtu au watu fulani nisiyokuwa na miadi nao wajichanganye kwenye targets
zangu ili niwachakaze vibaya kwa risasi.
Jicho langu la kazi kamwe halikuhama kwenye Eyepiece Lens ama sehemu ya kuona
ya durubini pandikizi yenye nguvu kali iliyokuwa juu ya bunduki yangu maalum ya
kudungulia adui.
Kwa kuwa nilikuwa naipenda sana kazi yangu hii hivyo nilikuwa nimechukua
vifaa vyangu vyote muhimu vya kazi kama bunduki yangu maalum ya kudungulia
adui ama Sniper Rifle aina ya 338 Lapua Magnum yenye uwezo wa kudungua bila bugdha
yoyote windo lililopo ndani ya umbali wa mita 1400 ama sawa na urefu wa viwanja
kumi na nne vya mpira wa miguu na iliyojazwa risasi za kutosha. Redio ya upepo ya
mkononi kwa ajili ya mawasiliano. Kisu chenye dira ama Compass/GPS. Kibuyu cha
maji ya kunywa ama Water Bladder. Filimbi ndogo. Dawa ya kujipaka mwilini kwa
ajili ya kujikinga na wadudu wabaya wenye sumu wa porini ijulikanayo kama Insects
Repellent. Min Thermometer. Mchanganyiko wa chakula chepesi lakini chenye kushibisha
kwa muda mrefu. Vifaa muhimu vya huduma ya kwanza. Vifaa vya kuzuia sauti kali
na wadudu wasiingie masikioni. Kurunzi ndogo mfano wa kalamu yenye mwanga
mkali iitwayo Penlight. Mlipuko mdogo wenye moshi mwingi ambao nikiutupa
hulipuka na kutoa wingu kubwa la moshi ili kumzuia adui asinione wakati nikitoroka
uitwao Chemical Mace. Rangi za kujipaka ili kujikinga nisionekane kwa urahisi na adui
iitwayo Camouflage Paste. Strobe Light ama mlipuko mwingine mdogo ambao nikiulipua
hewani hutoa mwanga mkali wa rangi tofauti pale inapotokea kuwa nimepoteana na
wenzangu ili waweze kufahamu nilipo au pale ninapohisi kuwa mbele yangu kuna
adui ili niweze kuyaona maficho yake na kummaliza. Pia kitabu kidogo na kalamu kwa
ajili ya kuandika mambo muhimu ya kazi yangu pamoja na Laser Ranger Finder ama
kifaa kidogo kinachotumika kutambulisha umbali wa adui.
Kwa muda wa siku tatu sasa nilikuwa sijatongoa lepe la usingizi wa kueleweka.
Mapigano yenye upinzani mkali yaliyodumu kwa muda wa siku tatu kati ya vikosi vya
jeshi la MONUSCO-Organization Stabilization Mission in Democratic Republic of the Congo
chini ya mwamvuli wa Umoja wa Mataifa UNFIB- The United Nations Force Intervention
Brigade na lile la waasi wa M23 yalikuwa yameniacha hoi taabani kwa uchovu. Hata
hivyo tulikuwa tumefanikiwa kuiteka miji mitatu muhimu kutoka mikononi mwa
waasi wa M23. Miji hiyo ikiwa ni mji wa Kitchanga, mji wa Nyiabiondo na mji wa
Kibati.
Kwa kiasi fulani uchovu niliokuwanao ulikuwa umemezwa na furaha ya mafanikio
binafsi niliyoyapata katika kazi yangu. Kwa muda wa wiki mbili tangu vikosi vyetu
vya MONUSCO vilipoanza operesheni zake za kupambana na waasi nilikuwa
nimefanikiwa kuwadungua wapiganaji 18 wa jeshi la waasi la M23 huku wachache
wakifanikiwa kunipa mgongo na kupotelea msituni. Hivyo bado kazi yangu ilikuwa
inaridhisha.
Nikiwa nimelala juu ya tawi la mti huu mrefu mawazo mengi yalikuwa yakipita
kichwani mwangu. Mawazo ambayo mara kwa mara yalikatishwa na sauti za sokwe
waitwao Bonobo na nyani aina ya Black Colobus, Golden Lion Tamarind, Black Titi, Proboscis,
Black-Crested Mangabey, Black-Crested Macaque-Macaca Nigra na Baboon waliokuwa
wakipiga kelele bila sababu ya kueleweka akilini mwangu.
Kuna wakati akili yangu ilipumbazwa kwa muda na kelele za maporomoko ya
maji yaliyokuwa jirani na eneo lile yakitokea sehemu za juu za misitu hii ya Ikweta.
Maporomoko hayo hatari yakisomba magogo,wanyama wa porini na takataka nyingine
za msituni lakini bado jicho langu halikuhama kwenye lenzi ya bunduki yangu.
Kwa muda wa takribani masaa matatu yaliyopita nilikuwa nimepitiwa na nyoka
hatari wenye sumu kali waliopo katika msitu huu kama Rhombic Night Adder, Rhinocero’s
Horned Viper, Albino Burmese Python, Green Mamba na African Bush Viper ambao walipita
mikononi mwangu, shingoni, kichwani, mgongoni na hatimaye kuendelea na safari
zao huku wakiniacha nimeganda kwenye tawi kama sanamu. Hali iliyopelekea mapigo
ya moyo wangu yasimame kwa sekunde kadhaa katika vipindi tofuati.
Kwa kweli msitu ulikuwa unatisha sana ingawa zile sauti za milipuko na kelele za
risasi zilikuwa zimekoma muda mfupi uliyopita baada ya adui kushindwa nguvu na
kukimbia.
Nilikuwa nimefanikiwa kuwadungua wapiganaji wawili wa M23 waliokuwa nyuma
ya gogo umbali wa mita takribani mia sita na ushei wakinitazama. Kazi ilikuwa rahisi
tu kwani risasi moja niliyoiruhusu ilipita katikati ya kioo cha darubini ya mmoja wa
adui wale kisha jichoni na kuufumua vibaya ubongo wake nikimlaza chali. Mwenzake
alinisumbua kidogo akijibanza nyuma ya mti mkubwa uliyokuwa pembeni ya eneo
lile. Sikutaka kuwa na haraka hivyo nilisubiri kwa muda mrefu nikitaka kumwaminisha
adui yule aliyesalia kuwa mambo yalikuwa sawia.
Baada ya kitambo kirefu cha kusubiri yule adui akafanya makosa ambayo
yalimgharimu. Akiamini kuwa mambo yalikuwa sawa sawia akachungulia katikati
ya tundu la mti lililotengenezwa na ndege wa porini aina ya Woodpecker. Jicho langu
makini likiwa kwenye Eyepiece Lens, mkono wangu wa kushoto ulikikamata kilimi cha
bunduki na ule wa kulia ukashika sehemu ya kurekebishia pembe nzuri ya shabaha
kwenye darubini ya juu ya bunduki ama Elevetion Adjastment Knob. Taswira ya adui yule
ilipoenea vizuri kwenye Objective Lens nikabana pumzi ya kutosha kisha nikavuta kilimi
cha Sniper Rifle na hapo kufumba na kufumbua matunda ya kazi yangu yakaonekana.
Risasi moja tu niliyoiruhusu ilipenya kwenye lile tundu la mti yule bwege alipokuwa
akichungulia kisha ikapita jichoni na kulifumua vibaya fuvu lake na hapo nikapapasa
katika mfuko wa gwanda langu la kijeshi na kuchukua pipi ya kijiti kisha nikaimenya
na kuitia mdomoni. Mambo yote yalikuwa kimyakimya kwani bunduki yangu ilikuwa
na kiwambo maalum cha kuzuia sauti ama Sound Suppressor.
Kwa upande huu wa msitu tulikuwa wadunguaji watatu makini kwenye mpango
wa Quick Reaction Force of Task, Group Alpha ya Brigade. Kati ya wadunguaji hao
watatu,wadunguaji wawili tulikuwa ni askari wa kutoka Tanzania Army Special Force.
Yaani mimi Koplo Tsega codename Lady butterfly na Sajenti Chacha Marwa codename
Chameleon. Mdunguaji mwingine akiwa ni wa kutoka jeshi la D.R Congo mwenye cheo
cha Private akifahamika kwa jina la Gina Yhombi-Opango Makiadi codename Lovebird.
Umbali wa kutoka hapa nilipo hadi alipokuwa mdunguaji mwingine ulikuwa si
chini ya mita mia tano na mara kwa mara tuliweza kuwasiliana kupitia redio zetu
za upepo katika kujulishana hali ya usalama ilivyokuwa ikiendelea. Kwa kweli
nilikuwa nimevutiwa sana na Private Gina Yhombi-Opango Makiadi kwa namna
alivyokuwa mpiganaji hodari ingawa alikuwa na umri mdogo zaidi yangu. Binti huyo
wa kikongomani alikuwa amepata shabaha zote wakati wa kufanya mazoezi hali
iliyonishangaza sana kwa uwezo wake mkubwa wa kulenga shabaha.
Nikiwa bado nimelala juu ya tawi hili mawazo mengi yalikuwa yakipita kichwani
mwangu huku nikikumbuka matukio yote yaliyotokea tangu nilipokuwa jijini Dar es
Salaam kabla ya majina yetu yaani mimi na Sajenti Chacha Marwa kupendekezwa
katika mpango wa amani wa hapa Kivu kaskazini nchini D.R Congo.
Sote tulikuwa kwenye tume maalum inayoshughulika na udhibiti na upambanaji
wa biashara haramu ya dawa za kulevya nchini Tanzania. Kwa muda wa miezi
sita tangu tulipojumuishwa kwenye tume hiyo ya kudumu tulikuwa si tu kwamba
tumeiletea mafanikio makubwa tume hiyo lakini pia tulikuwa tumetoa muelekeo
mzuri wa kuwatambua na kuwafikia wachuuzi wakubwa wa biashara hiyo haramu.
Hata hivyo kwa kuwa sisi hatukutaka mambo ya kisiasa katika kukabiliana na wale
washukiwa wa biashara hiyo hivyo mara kwa mara tulikuwa tukikutana na upinzani katika ufanyaji wa kazi yetu kama si kulaumiwa kuwa tulikuwa hatuzingatii misingi ya sheria za nchi na haki za binadamu katika kushughulika na janga hilo lililokuwa mbioni kuimeza kabisa nguvu kazi ya taifa.
Kwa kuzingatia ukubwa wa janga lenyewe tume yetu ilikuwa imeundwa na watu
wa kutoka idara tofauti kutegemeana na umuhimu wa uwepo wa watu hao. Askari wa
kutoka jeshi la wananchi wa Tanzania tulikuwa watatu;yaani mimi Koplo Tsega kutoka
kikosi 92 cha makomandoo Sangasanga mkoani Morogoro. Meja Khalid Makame
kutoka kambi ya kijeshi 521 ya Chukwani kisiwani Zanzibar na Sajenti Chacha Marwa
kutoka kikosi 36 cha kambi ya jeshi Msangani mkoani Pwani. Wengine walikuwa ni
wajumbe wa kutoka shirika la kimataifa la haki za binadamu-Human Rights Watch.
Mwanasheria wa serikali. Wajumbe kutoka idara ya usalama wa taifa. Wanasiasa
kutoka maeneo tofuati ya kiutendaji pamoja na askari polisi waandamizi akiwemo
kamishna mkuu wa jeshi la polisi na wawakilishi wa vijana.
Kitu kilichokuwa kimenishangaza sana ni kuwa wakati kazi yetu ikiwa mbioni
kutoa suluhisho la kudumu katika kukabiliana na biashara hiyo haramu ya dawa za
kulevya nchini Tanzania ndiyo tukapewa barua za kuingizwa kwenye mpango wa
amani ya kudumu hapa nchini D.R. Congo. Tena wanajeshi wote watatu tuliyokuwa
kwenye tume hiyo tukienguliwa bila sababu za kueleweka.
Kwa kuwa kazi yetu katika tume hiyo ilikuwa bado haijafikia ukomo na tulikuwa
tukielekea katika hatua nzuri zaidi ya kuwaweka bayana wafanyabiashara hao.
Tulijaribu kwa kila hali kupingana na hoja ya kujumuishwa kwetu kwenye mpango
wa amani ya kudumu ya hapa D.R Congo lakini hatimaye tuligonga mwamba
kwani viongozi wetu wa juu walitumia mamlaka yao kupingana na hoja zetu. Hivyo
hatukuweza kukaidi zaidi ya kutii amri zao kitendo ambacho kilinitia hasira sana. Hata
hivyo, sikuwa na namna kwani mojawapo ya misingi inayoliletea sifa kubwa jeshi letu
ni utii na nidhamu. Na sasa nilikuwa hapa eneo la Bunagana msituni juu ya mti mrefu
nikitekeleza wajibu wangu kwa taifa.
Niligeuka kuitazama saa yangu ya mkononi na hapo nikagundua kuwa ilikuwa
tayari imekwishatimia saa nane usiku na dakika chache mbele yake. Manyunyu hafifu
ya mvua yalikuwa yameanza kuanguka tena kutoka angani na kwa kweli sikupenda
mvua iendelee kunyesha katika msitu huu ingawa kunyesha kwa mvua kubwa lilikuwa
ni jambo la kawaida sana katika nchi za Ikweta kama nchi hii ya D.R Congo yenye
kilometa za mraba 2,345,410 hali ya hewa ya joto na baridi yenye wastani wa jotoridi
nyuzi 25 digrii sentigredi na wastani wa mvua kiasi cha sentimeta 130 hadi 200 kwa
mwaka ardhini.
Taa nyekundu ndogo iliyowaka haraka kwenye redio yangu ya upepo ikayahamisha
mawazo yangu na hapo nikageuka na kuitupia macho huku nikiitazama kwa mshtuko
kama niliyeshikishwa bomu. Taa ile ilikuwa na maana kuwa kulikuwa na simu
iliyokuwa ikiingia jambo ambalo lilikuwa la kawaida kabisa kutokea lakini sijui ni
kwanini nilishtuka sana.
Haraka nikaizungusha durubini yangu juu ya bunduki ku-scan taswira yoyote iliyokuwa eneo lile na hapo nikaona kuwa hali ilikuwa shwari hivyo nikabonyeza kitufe kwenye redio yangu ya upepo kuruhusu ile simu kuingia. Kwa kufanya hivyo
ile taa nyekundu ikapotea na kuwaka taa ya kijani halafu kukasikika sauti ya mvumo
wa upepo. Koo langu likakauka ghafla pale nilipokumbuka kuwa simu ya namna ile
ilikuwa ikitoka kwa mmoja wa wadunguaji wenzangu katika msitu huu. Ile sauti ya
mvumo wa upepo ilipokoma nikasikia sauti ya upande wa pili wa simu ambayo haraka
niliweza kuitambua kuwa ilikuwa ni sauti ya Sajenti Chacha Marwa codename Chameleon.
“Lady butterfly are you there? ...unanisikia?” sauti ya upande wa pili iliongea hata
hivyo niliitambua haraka kuwa sauti ile ilikuwa ikipwaya kwa hofu na iliyotawaliwa na
kitetemeshi…’Jambo la hatari?’ Nilijiuliza.
“Lady butterfly unanipata?” Ile sauti ikajirudia safari hii kwa nguvu kidogo.
“Ndiyo nakupata Chameleon, any trouble?” Nilimuuliza kwa wasiwasi.
“Yes! I got shot, very severely.”
“What!...umepigwa risasi?” Nilimuuliza kwa taharuki
“Ndiyo! Risasi mbili Lady Butterfly. Risasi moja imenipata begani na nyingine
imenitoboa sehemu ya kushoto kifuani sentimita chache mbali na moyo,” Chameleon
alizungumza kwa sauti hafifu ya kukoroma.
“Oh! My God uko wapi sasa?” Nilimuuliza.
“Nyuma ya jiwe umbali mfupi kutoka pale nilipokuwa,” Chameleon aliendelea
kuongea kwa shida huku sauti yake ikionekana kuzidi kupoteza mhimili.
“Okay! Hold on Sajenti am coming right now.”
“Don’t ever try to come here Lady Butterfly kwani inavyoonekana ni kuwa anajua tulipo
hivyo itakuwa kazi rahisi kwake.”
“Nani?” Nilimuuliza Chameleon kwa mshangao.
“Adui mdunguaji,” Chameleon aliendelea kuniweka bayana lakini sauti yake ilikuwa
ikizidi kuyoyoma.
“Nakuja!” Nilitaka kuzidi kumdadisi Chameleon lakini nilighairi wazo langu kwa
haraka kwani ningekuwa nikipoteza muda wangu na huwenda asingenijibu kutokana
na udhaifu wake.
Nilihisi kuwa bado kulikuwa na nafasi ya kuyaokoa maisha yake endapo ningeweza
kucheza na muda wangu vizuri ingawa maelezo yake yalikuwa na kiasi kikubwa cha
ukweli wa kunionya.
“Chameleon…! Chameleon unanisikia?” Niliita tena lakini mara hii sikujibiwa na
badala yake kwa mbali nilisikia sauti ya mikoromo yake hafifu.
“Chameleon unanisikia?” niliita tena lakini sauti ile upande wa pili ilipoteza uhai
na hapo huzuni ikaniingia moyoni. Machozi yaliyoanza kutafuta makazi machoni
mwangu nikayazuia kwa kufumba macho na kumeza funda kubwa la mate ili
kuitowesha hasira kifuani mwangu.
Bila kupoteza muda zaidi nikaikata ile simu kisha nikabonyeza tena vitufe kadhaa
vya simu yangu halafu nikaishikilia vizuri simu yangu. Baada ya kitambo kifupi cha
kusubiri ili simu yangu ipate signals nzuri za mawasiliano hatimaye ile simu ikaanza kuita tena upande wa pili huku nikitarajia kuisikia sauti ya mdunguaji mwingine Private Gina Yhombi-Opango Makiadi codename Lovebird. Hata hivyo hilo halikutokea kwani ile simu iliendelea kuita mara kadhaa pasipo kupokelewa. Kwa kweli nilijihisi
kuchanganyikiwa. Nikaikata ile simu na kuipigia tena huku nikiwa na kihoro cha aina
yake lakini bado ile simu haikupokelewa na tukio lile likazidi kuwa ishara mbaya zaidi
kwangu.
“Lovebird are you there?...zungumza Lovebird unanisikia?” niliendelea kuita lakini ni
kama niliyekuwa nikijiuliza mimi mwenyewe. Ile simu haikupokelewa wala sauti ya
Lovebird kusikika. Moyo wangu ukapiga kite kwa nguvu kisha koo likanikauka na hapo
baridi nyepesi ikaanza kusafiri taratibu nyuma ya mgongo wangu. Sikuwa na namna ya
kuendelea kusubiri zaidi hivyo nikaizima simu yangu ya upepo na kuichimbia kwenye
mfuko wa gwanda langu huku nikiwa nimeanza kuingiwa na hofu ingawa sikutaka
kupoteza umakini.
Muda mfupi uliyofuata nikaifyatua bi-pod stand ya bunduki yangu Sniper Rifle 338
Lapua Magnum na kuikunja vyema kisha nikaanza kujivuta taratibu nikiteleza kwenye
tawi lile la mti kwa ulaini kama Boomslang nyoka hatari kwa vipenyo. Kwa namna
nilivyojipamba kwa majani mwili mzima jicho lolote la kiumbe hai eneo lile lisingesita
kunifananisha na kichaka.
Kidole cha mkono wangu wa kushoto kikiwa kimekamata vyema kilimi cha Sniper
Rifle nikaifyatua kamba iliyokuwa kiunoni mwangu na kuifunga kwenye tawi imara
la mti kisha kwa msaada wa kamba hiyo nikaanza kushuka kwenye mti ule taratibu
huku mara kwa mara nikiweka vituo kutazama hali ya usalama wa eneo lile. Wakati
nilipokuwa nikikaribia kufika chini ya ule mti mara hisia mbaya zikanijia kuwa sehemu
fulani mbali kidogo kwenye msitu ule macho ya mtu fulani yalikuwa yakinitazama na
hali ile ikazidi kunipa wasiwasi. Hivyo nilipomaliza kushuka chini ya ule mti haraka
nikaivuta ile kamba na kuanza kuikunja na wakati nikifanya hivyo kiasi cha umbali wa
kama mita miamoja na ushei mbele yangu nikakiona kichaka kidogo kikichezacheza
baada ya mwanga mkali wa radi kumulika eneo lile.
Hofu ikazidi kunishika hivyo nilipomaliza kuikunja vizuri ile kamba nikajibanza
nyuma ya ule mti niliyoushuka muda mrefu uliyopita na bila shaka bahati ilikuwa
kwangu kwani ni muda uleule risasi iliniparaza begani na kuvunja tawi la mti uliyokuwa
jirani na eneo lile. Nikajua kuwa maficho yangu tayari yalikuwa yamefichuliwa. Adui
yule alikuwa mdunguaji mahiri sana aliyeweza kucheza vizuri na akili yangu. Ile risasi
moja aliyoifyatua alikaa kimya tena akitaka kuniaminisha kuwa nilikuwa nikiota juu ya
tukio lile au huwenda yale yalikuwa mawazo yangu.
Nilimuelewa vizuri na kwa kutaka kulithibitisha hilo nikautikisa kidogo mti mfupi
usawa wa kimo changu uliyokuwa jirani yangu kwa buti langu gumu mguuni. Mti ule
mfupi ulipotikisika risasi moja akakata vitawi vidogo vya mti ule na kuvipeperusha
hewani na hapo nikajua kuwa adui yule alikuwa mtu makini sana na kazi yake. Kisha
baada ya pale hali ya ukimya ikafuatia tena.
Wakati nikiwa nimejibanza nyuma ya ule mti sikutaka kujiridhisha kuwa pale nilikuwa sehemu salama. Mvua ilikuwa imeanza kunyesha tena sambamba na upepo mkali uliyoanza kuyumbisha matawi ya miti na vichaka vya eneo lile. Ilikuwa ahueni kwangu kwani adui yule mkorofi kwa vyovyote angepoteza umakini kwa kuyumba
kwa vichaka vile. Hivyo kwa kuichangamkia vizuri fursa ile nikajitupa chini na kuanza tutambaa kwa tumbo nikienda mbele kutoka usawa wa ule mti. Muda mfupi baadaye nikawa nimefanikiwa kujichomeka kwenye kichaka cha jirani na eneo lile. Niligeuka tena kutazama kule kwenye kile kichaka na sikuona chochote ingawa hali ile haikuweza kunithibitishia kuwa adui yule alikuwa amenisamehe.
Kichaka kile hakikuwa maficho mazuri ingawa kilinihifadhi kwa muda kidogo
kabla ya kutambaa tena na kuhamia kwenye kichaka kingine kilichoshiba miti zaidi
kilichokuwa eneo lile pembeni. Nikiwa katika kichaka kile niliitumia tena darubini ya
bunduki yangu kulichunguza eneo lile hata hivyo kwa kuwa ule mti niliyojibanza hapo
awali ulikuwa umenizuia kuona kule nyuma ilinibidi nihamie kwenye kichuguu kidogo
kilichokuwa mbele kidogo ya eneo lile.
Nikiwa nyuma ya kichuguu kile niliifyatua bi-pod stand ya Sniper Rifle na kuitega
vyema kisha kupitia darubini yake yenye nguvu nikaanza kufanya scaning makini eneo
lile. Sikuweza kuona kitu chochote eneo lile na hali ile ilinishangaza sana. Kile kichaka
ambacho hapo awali kilikuwa kikitikisika sasa kilikuwa kimetulia pia sikuweza kuona
kiumbe chochote eneo lile hivyo mwishowe nikakata tamaa kabisa huku nikiunyanyua
mkono kuitazama saa yangu ya mkononi na wakati nikifanya hivyo mwanga wa radi
uliyomulika eneo lile ukanisaidia kuona kule mbele.
Mtu fulani alikuwa amechepuka kutoka nyuma ya mti mmoja uliyokuwa eneo
lile na kwenda kujibanza nyuma ya mti mwingine kiasi cha umbali wa mita mia moja
na ushei mbele yangu na hapo nikatabasamu na kujifuta maji ya mvua yaliyokuwa
yakichuruzika uso wangu. Nikajilaza tena vizuri nyuma ya kichuguu kile kisha
nikalisogeza jicho langu kwenye Eyepiece Lens ya darubini ya Sniper Rifle na safari hii
nilichokiona kikanipelekea nizidi kutabasamu.
Yule mtu sasa alikuwa amejibanza nyuma ya ule mti na kwa kuwa ule mti ulikuwa
mwembamba kidogo ilikuwa ni sawa na mtu aliyejifunika shuka fupi kwani mabega
yake yalikuwa yakionekana. Yule mtu alikuwa amejikinga nyuma ya ule mti huku
akiitumia nafasi ile kujaza risasi kwenye bunduki yake na hilo lilikuwa kosa kubwa
kwani nilimjaza vizuri akaenea kwenye Objective Lens ya darubini yangu na hapo
nikavuta pumzi nyingi na kuibana. Risasi moja niliyoiruhusu ikaniletea majibu ya
hakika kwani risasi hiyo ilipenya kwenye bega lake la kulia kisha ikapekenya mfupa
wake na kuendelea mbele na safari. Yule mtu akapiga yowe kali huku bunduki yake
ikimponyoka mkononi na kuangukia chini na hapo akayumbayumba na kupoteza
mhimili. Hilo likawa kosa jingine kwani kwa kufanya vile kichwa chake kikaenea
vizuri kwenye lenzi ya darubini yangu. Tukio lile likanifanya nipige mruzi mwepesi
wa furaha. Risasi nyingine niliyoiruhusu kufunga safari ikakifumua vibaya kichwa cha
yule adui na kuutawanya vibaya ubongo wange huku yule adui akitupwa hewani. Jicho
langu bado halikuhama kwenye Eyepiece Lens ya darubini yangu hivyo yule mtu wakati akitua chini nikamkandamiza kwa risasi nyingine ya kifua iliyomlaza chali kimya. Kazi ikawa imekwisha hivyo nikaitoa pipi yangu ya kijiti kutoka mfukoni kisha nikaimenya na kuitia mdomoni.
Niliendelea kujibanza nyuma ya kile kichuguu huku jicho langu likiendelea kufanya kazi kwenye ile darubini kulichunguza eneo lile hadi pale niliporidhika kuwa hali ya usalama wa eneo lile ilikuwa shwari ndiyo nikachukua mashine yangu ya kazi na kusimama. Niliitazama tena saa yangu ya mkononi na kushtuka kuwa muda ulikuwa
umeenda tangu nilipoongea na Chameleon.
Niliichukuwa tena simu yangu ya upepo na kumpigia Chameleon lakini simu haikupokelewa. Nikampigia tena simu Lovebird lakini bado hali ilikuwa vilevile kwani ile simu yake haikupokelewa. Sikupenda kuendelea kupoteza muda zaidi hivyo muda mfupi uliyofuata nilikuwa nikiupangua msitu ule kwa mbio zisizo za kawaida.
Kwa kuwa nilikuwa nikiyafahamu vizuri maficho ya wenzangu hivyo sikupata shida katika kuwafikia. Nilimkuta Sajenti Chacha Marwa Code-name Chameleon akiwa ameegemea jiwe kubwa kando ya maficho yake na hapo nikajua kuwa baada ya
Chameleon kushambuliwa na adui alikuwa ametoroka kwa shida na kujificha nyuma
ya jiwe lile. Mdomo na macho yake vyote vilikuwa wazi ingawa nilipomsogelea na kumshika alikuwa wa baridi huku kifo tayari kikiwa kimemchukua. Damu nyingi kutoka kwenye majeraha yake ya risasi kifuani na begani ilikuwa imezitotesha vibaya gwanda zake. Kitu cha ajabu na kilichonishangaza ni kuwa Chameleon hakuwa na ile redio yake ya upepo wala ile silaha yake ya kudungulia adui na hali ile ilinitia mashaka
sana. Nilisimama kidogo nikimtazama Chameleon kwa huzuni kama mtu ambaye
nisingeweza kuonana naye tena hapa duniani. Sikuwa na jinsi hivyo nikamsogelea
pale alipoketi na kumfumba mdomo na macho yake huku nikizikumbuka enzi za
urafiki wetu tangu tulipoanza kufahamiana kwenye tume ya udhibiti na upambanaji
wa biashara haramu ya dawa za kulevya jijini Dar es Salaam. Hivyo nikaichukua kamera yangu ndogo na kumpiga picha chache kama sehemu ya kumbukumbu zangu za mwisho kwake.
Muda mfupi baadaye nilikuwa tena porini nikikimbia kuelekea kwenye maficho
ya mdunguaji mwingine Private Gina Yhombi-Opango Makiadi codename Lovebird.
Kwa kweli nilichokiona baada ya kufika kilizidi kupeleka simanzi moyoni mwangu.
Nilimkuta Lovebird akiwa ananing’inia mtini kama nyama ya ng’ombe kwenye mtungo buchani. Ni kama alikuwa kwenye jitihada za kushuka kutoka juu ya mti ule yalipokuwa maficho yake lakini hakuwa amefanikiwa kutimiza adhama yake. Risasi za adui zilimfumania wakati akiwa anakaribia kufika chini ya ule mti na hivyo kumuacha akining’inia kwenye kamba ile huku umauti ukiwa tayari umemfika. Mbaya zaidi ni
kuwa Lovebird hakuwa na kichwa na badala yake kilibakia kichuguu cha shingo yake
tu ambacho kwa wakati huu kilikuwa kikiendelea kuvuja damu taratibu. Risasi kali za
adui zilikuwa zimekifumua kichwa chake na kuutawanya ovyo ubongo wake.Roho iliniuma sana kwa kumpoteza rafiki yule mwenyeji wetu hata hivyo sikuwa na jinsi. Machozi yalinitoka wakati nikichukua picha zake kwa kamera yangu ndogo yadigital. Nilipoendelea kumchunguza vizuri Lovebird nikagundua kuwa kama ilivyokuwa
kwa Chameleon naye pia silaha yake na vitu vyake muhimu vilikuwa vimechukuliwa
bila shaka na adui. Kilichonisikitisha zaidi ni kuwa hata ile kamera yake kubwa ya
ki-uandishi wa habari vitani aina ya Toymaster ilikuwa imekwenda. Mbali na kuwa
mwanajeshi na mdunguaji mahiri Private Gina Yhombi-Opango Makiadi codename
Lovebird pia alikuwa mwandishi wa habari aliyeajiriwa na shirika la habari la The Reuters
kwa mkataba akichukua picha matukio ya vitani. Hivyo ile kamera ya kuchukulia
picha za matukio alikuwa amepewa na shirika hilo.
ITAENDELEA
"Nikapapasa mfuko wangu wa Gwanda nikatoa pipi ya kijiti nikamenya nikala"[emoji1] [emoji1] [emoji1] [emoji1] [emoji1] [emoji1] [emoji1] [emoji1] [emoji1]
 
Back
Top Bottom