Riwaya: Msako wa Hayawani

SEHEMU YA TATU.

Gari la polisi na gari la wagonjwa yaliwasili nyuma ya Benk ya wakulima karibu wakati mmoja.
Kwenye gari la polisi waliteremka watu watatu. Wanaume wawili na mwanamke mmoja. Wanaume walikuwa Sajini Bob na Koplo Butu. Wote walikuwa katika sare zao za usalama barabarani.
Mwanamke alikuwa kachero Inspekta Bessy. Alikuwa katika milango ya miaka ishirini na saba,mrefu wa kuvutia. Alivaa sketi ya kijivu, shati jeupe na kikoti cha kijivu. Begani alibeba mkoba mweusi.
Kwenye gari la wagonjwa waliteremka watu watatu pia. Wawili walibeba machela na nesi mmoja ambaye baadaye alijitambulisha kwa jina Miriam.
Wote walikuwa katika sare zao nyeupe.
Nesi alipomuona tu majerui akaguta, "Mungu wangu! Ni Dk. Makete!"
"Unamfahamu? " Inspekta Bessy alimwuliza, akitoa kalamu na kijitabu kwenye mkoba wake.
"Ndiyo."Miriam alijibu kwa sauti ya mtetemo. "Ni Dk.Makete. Alikuwa Daktari wetu Mku, sasa amestaafu.
"Mtazame kama angali hai."
"Nesi akachutama na kuchunguza mapigo ya moyo.Akasema, Angali hai"!
"Mkimbizeni hospitali." Wakati Dk. Makete akiwekwa kweny machela,Bessy alimwuliza nesi, "Unalijua gari lake?"
"Ndiyo."
"Lipo hapa?"
Miriamu akageuza kichwa. Akaliona "Lile."
"Vizuri." Bessy akawatazama Bob na Butu. Akawaambia, "Anzeni kazi, mnajua nini cha kufanya."


**************************************


Kilometa kadhaa nje kidogo ya jiji, Benzi jeupe liliacha barabara kuu. Lilipinda kulia na kuingia eneo la Buffalo Hill. Barabara za eneo hilo zilikuwa nyembamba lakini nzuri, na nyumba zilikuwa mbalimbali. Karibu kila nyumba ilizungukwa na wigo wa aina moja au nyingine.
Katika mtaa wa kitosi Benzi lilipenye kwenye geti lenye namba ishinirini na moja.Likapita katikati ya bustani nzuri na kusimaa mbele ya jumba la kifahari la ghorofa moja. Mtu aliemgonga Dk. Makete akateremka na kulikagua gari upande wa mbele. Boneti na bampa lilikuwa limebonyea kidogo.
Kassim akajikuna utosi,macho yake yakionyesha alikuwa na mawazo mazito. Akatoa leso na kupangusa uso wake uliomeremeta kwenye mwangaza wa jua.
Wakati akirudisha leso mfukoni,alisikia hatua nyuma yake. Akageuka. Akamuona Isidori. Mtumishi mkuu wa jumba hilo,akitokea ndani. Akamuuliza, "Kuna habari yoyote?" Sauti yake ilikuwa ya kawaida kabisa -ya mtu mwenye uwezo mkubwa .
"Bwana Kembo alipiga simu." Alijibu mtumishi huyo. Alikuwa nadhifu kama mazingira ya hapo. Suruali nyeusi, shati jeupe na tai nyeusi. "Amesema umpigie."
"Sawa." Kassim akatoa kikebe cha dhahabu akakifungua na kutoa sigara nene ya kahawia,ya kutoka Havana -Cuba. Akaiweka mdomoni na kuiwasha kwa kiberiti cha gesi.
"Lipeleke hili gari gereji." Alisema baada ya sigara kukolea moto. "Waambie wanyoshe hapa.Kazi hiyo waifanye sasa hivi. Na waifanye vizuri, isijulikane kama limebonyea.Isipowezekana waweke boneti na bampa jipya.Wasijali gharama. Sawa?"
"Ndiyo Mzee."
"Na Isidori....."
"Ndiyo Mzee?"
"Koti hili linanibana. Alisema Kassim, akilivua koti lake la thamani.
"Hebu lijaribu."
Isidori alilipokea na kulivaa koti hilo akiwa na uso wa furaha na mshangao.Akasema, "Sawa kabisa." Ingawa lilimpyaya kidogo.
"Lako."
"Asante sana, Mzee."Akaanza kufungua vifungo .
"A-aah! Usilivue.Livae tu likuzoee.Ingawa halifanani na suruali yako lakini limekupendeza." Isidori akakifunga kifungo alichokifungua. Akaufungua mlango wa gari.
"Na Isidori...."
"Isidori akageuka. "Ndiyp mzee?
"Kuna jambo nataka ulifahamu."
"Ndiyo,Mzee.?
"Ennh....Kuna mtu nimemgonga mjini,nyuma ya Benki ya Wakulima.Ndiyo sababu ya boneti kubonyea." Isidoria akabaki kimya wakati sigara ikipelekwa mdomoni na kuondolewa.
"Ilikuwa bahati mbaya." Kassim akaendelea. "Lakini sikusimama. Unajua nini hutokea katika jiji hili....Yaani ukimgonga tu mtu na kusimama hata kama kosa ni lake,wahuni hukuvami na kukushambulia huku wakipora kila wawezacho kukitia mkononi.
"Naelewa, Mzee." Isidori alikubali huku akisisitiza kwa kichwa. "Kwa hiyo sikusimama." Kassim akaendelea.
"Kwa vile mwendo haukuwa mkubwa, sidhani kama mtu huyo ameumia sana. Na sidhani kama kuna mtu aliewahi kuchukua namba za gari. Hapakua na watu wengi."
Sigara ilibandikwa mdomoni ikabanduliwa.
" Lakini kama ikigundulika ....ikigundulika kama ni mimi ndie niliefanya ajali hiyo yatakua makubwa. Si tu faini na fidia itakua kubwa -hilo sijali bali heshima yangu katika jamii pia itaathirika."
Kassim aliivuta sigara akasema, "Iwapo itagundulika nataka useme ni wewe uliekuwa unaendesha. Hakuna usumbufu wowote utakaoupata. Ondoa shaka kabisa, wakili wangu Bw. Benson atasimamia mambo yote.Sana sana itakua faini na fidia ambayo nitalipa ndani ya nukta.Na nitakupa zawadi ya kukufaa katika maisha yote -kitu kama nyumba au gari. Chaguo lako"
Baada ya kuibandua sigara mdomoni,Kassim akauliza, "Sawa?" Kama mtu alielishwa limbwata,Isidori akajibu, " Sawa, Mzee."
 
SEHEMU YA NNE

Kassimu aliliangalia Benzi likitoka nje ya geti kisha akageuza kichwa na kumtazama mtunza bustani. Alikuwa kama hatua arobaini mbali naye,akimwagilia miwaridi. Akajiuliza kama ameweza kusikia kuyasikia mazungumzo yao. Alizungumza kwa sauti ndogo kwa ajili yake. Akaamua asingeweza kumsikia. Akageuka na kuingia ndani.

Vyumba vyote vya kulala vya jumba hilo vilikuwa ghorofani. Sehemu kubwa ya chini ilikuwa ukumbi mkubwa uliopambwa vilivyo. Sakafu yote ilifunikwa na zulia. Upande mmoja ulitawaliwa na meza iliyozungukwa na viti kumi na viwili. Upande mwingine ulikuwa na TV na rafu za vitabu,mapambo na vinywaji, hasa vikali na aina kadhaa za mvinyo aghali toka ng'ambo. Hapa na pale palikuwa na seti za sofa na vimeza vifupi. Ngazi za kwenda ghorofani zilikuwa mkabala na mlango wa mbele.

Kassim alikwenda moja kwa moja kwenye rafu ya vinyaji. Akatoa chupa ya kinywaji kikali na kjitilia robo glasi. Akaimeza kwa mkupuo.
Kisha akaenda kwenye simu iliyokuwa pembeni. Baada ya kubonyeza namba atakazo na kujibiwa, akasema "Nipatie Bwana Kembo." Punde sauti upande wa pili akasema, " Kembo hapa." Kassim akatamka neno moja tu, "Vipi?"
"Ohh, Bwana Kessy! Nahitaji kukuona. Tuna tatizo."
"Na mimi pia nina tatizo."
"Tatizo gani?" Kembo aliuliza kwa mashakamashaka.
"Tuna watu karibu sehemu zote mhimu."

"Vizuri. Kuna mtu alifikwa na ajali ya gari nyuma ya Benki ya Wakulima muda mfupi uliopita. Nataka kujua ni nani mtu huyo na hali yake ikoje. Unaweza kufanya hivyo?"

"Hakuna lisilowezekana, Bwana Kessy. Hakuna lisilowezekana."
"Fanya hivyo halafu njoo unione,"


***********************


Bessy hakua mgeni na Dk. Beka, Daktari Mkuu wa hospitali kuu ya serikali. Tangu avishwe uinspekta mwaka mmoja na nusu nyuma, alikwisha kutana nae mara kadhaa,kuhusiana na kesi mbalimbali.
Kwa hiyo alipofika hapo hospitalini alikwenda moja kwa moja ofisini kwake. Akabisha na alipoambiwa aingie, akaufungua mlango na kuingia.
"Ohh, ni wewe Inspekta." Alisema Dk. Beka kwa suti yake tulivu na ya chini. Leo Bessy aliona,ilikuwa ya chini zaidi - ya huzuni.

Akasema, "Ni kuhusu Dk. Makete." Naye pia alitumia sauti ndogo. Dk.Beka akaitikia kwa kichwa. akaivua miwani yake na kuyafikicha macho yake machovu.
"Ikoje hali yake?" Bessy aliuliza,akiketi na kukitoa kijitabu chake.
"Nasikitika kusema si nzuri. Bado yuko thieta anashughulikiwa na wataalamu wa hali ya juu."
"Uko uwezekano wake wa kuishi?"
"Kitu kama hamsini kwa hamsini,"
Bessy alikwishaizoea kauli hiyo. Dk. Beka hakupenda kumkatisha mtu tamaa,hata kama alijua kuwa mgonjwa huyo asingetoka thieta akiwa hai.
Akauliza, "Aliwai kurudiwa na fahamu?"
"Alizinduka thieta kwa nukta chache tu kabla ya ganzi kumkolea sawasawa."
"Aliwai kusema lolote lile katika nukta hizo chache?" Bessy aliuliza kwa matumaini kalamu ikisubiri mdomoni.

"Alisema maneno machache. Lakini hakusikika vizuri. Alikuwa kama anaeota - anaeweweseka. Sauti yake ilikuwa ya chini sana, na maneno hayakuwa ya kuleta maana. Nilichoweza kukidaka ni maneno mawili tu - kama tutayaita maneno - 'kassi hashi.' Aliyarudia maneno hayo mara mbili tatu."

Baada ya kuyaandika maneno hayo,Bessy akasema kwa sauti ya mkazo , "Dk. Beka, lazima nizungumze na Dk. Maketemapema iwezekanavyo - kabla....kabla mambo hayajawa mabaya zaidi. Dk. Makete aligongwa kusudi. Na kwa bahati mbaya hakuna aliewai kuzisoma namba za gari."
"Una maana haikuwa ajali ya kawaida?" Dk. Beka aliuliza kwa mshangao wa kutoamini.
"Hapana! Lilikuwa jaribio la kuua!" Sauti ya Bessy ilikuwa imepanda. Akavuta pumzi na kuendelea kwa sauti ya kawaida. "Nadhani Dk. Makete anamfahamu mtu aliemgonga. Na sababu yake. Huwezi kumgonga mtu kusudi bila sababu."

" Una uhakika haikuwa ajali? Madereva wengi wanapomgonga mtu...."
"Najua. Hukimbia. Hukimbilia polisi kujisalimisha. Lakini huyu hakufanya hivyo. Zaidi ya masaa mawili sasa yameshapita. Nina hakika hata jisalimisha. Isitoshe, uchochoro aliogongewa Dk. Makete hautumiwi na magari, na kama kuna gari litapita, basi si kwa kasi ya kuweza kusababisha ajali.


Dk. Beka akatikisa kichwa kwa majonzi.
Inspekta Bessy akaendelea, "Isitoshe tuna ushahidi. Ingawa kichochoro kile - kichochoro cha Benki ya Wakulima - hakina pilika za watu. Tumebahatika kupata watu wawili walioshuhudia tukio hilo. Wote wanaelekea kuwa watu wa kuaminika. Wote wapo tayari kuapa kuwa Dk.Makete aligongwa kusudi."

Dk. Beka alifumbua mdomo ili aseme neno lakini akabadili mawazo na kuufumba

Bessy akaendelea, "Mashahidi hao wanatoa sababu mbili. Kwanza. Dk Makete hakuwa katikati ya njia. Alikuwa pembeni. Alifuatwa. Pili, gari lililomgonga lilimnyemelea. Liliongezwa mwendo ghafla lilipomkaribia. Mmoja kati ya mashahidi hao aliwai hata kuguta. Hakumbuki alisema kitu gani. Bila ya shaka kitu kama 'Hey...! au 'Wewee...!' Hajui kama alikuwa anamkemea yule dereva au anamtahadharisha Dk. Makete. Anasema alikuwa katika mshituko wa kuruka akili. Ndiyo maana hakuweza kuzisoma namba za gari."


Dk.Beka akatikisa tena kichwa. Akasema, "Nashindwa kuamini."
"Amini usiamini, hivyo ndivyo mambo yalivyo. Dk. Makete amegongwa kusudi."

"Hukunielewa. Nina maana....." Beka alitafuta maneno ya kumalizia sentesi yake lakini hakuyapata. Akasema, "Namfahamu Dk. Makete vizuri sana. Nimefanya nae kazi kwa zaidi ya miaka ishirini. Miaka kumi nikiwa msaidizi wake mkuu. Ni rafiki yangu mkubwa. Tumekuwa kama ndugu. Siri yake ni yangu. Mkewe ananiita shemeji, na mwanae ananiita mjomba. Hata siku moja sijaona wala kusikia Raymond akikorofishana na mtu. Nakuhakikishia yeye si mtu wa kuweza kuwa na adui hata mmoja hapa duniani."

"Na mimi nakuhakikishia kuwa anao. Angalau mmoja. Na ni wajibu wangu kumtia mbaroni. Nina imani Dk. Makete anamfahamu mtu huyo. Kwa hiyo lazima nizungumze nae kabla hali yake haijawa mbaya zaidi."

Dk. Beka aliinua uso akauliza, "Unamaana iwapo hata .... hatarudiwa na kauli, mtu huyo hataweza kupatikana?"
Badala ya kujibu swali hilo Inspekta Bessy alisema kwa sauti kavu, "Dk. Beka tafadhali usinifiche niambie ukweli. Dk. Makete atatoka thieta akiwa hai au maiti?"

"Mimi siyo mtabiri! Wala siyo Mungu!" Ingawa maneno hayo yalitamukwa kwa sauti ndogo lakini ilikuwa sauti ya ukali. Iliyojaa uchungu na ghadhabu. Dk. Beka akapumua na kusema kwa sauti yake ya kawaida, "Bessy, hatuwezi kufanya miujiza, kufanya lisilowezekana. Hatuwezi kufufua maiti. Hakuna anaeweza kufanya hivyo zaidi ya Yesu."
"Ndiyo kusema Dk. Makete hana tumaini?"
"Sijasema hivyo. Raymond hajawa maiti. Hivi tunavyozungumza anashughulikiwana mabingwa. Wanaweza wakafaulu kuyaponya maisha yake, wanaweza wasifaulu. Ikishindikana, hakuna yeyote wa kuweza kufanya lolote."

Bessy alikunja uso na kusema. " Kuna sindano ya kuua ganzi na kumzindua mtu na kumfanya aweze kijibu swali moja au mawili kabla ya kukata roho.Kama Dk. Makete hana tumaini lazima sindano hiyo itumiwe ili atutajie mtu alie mgonga."
"Dk.Beka akamtazama Bessy kwa mshangao. Akamwuliza, "Umeisikia wapi hiyo sindano?"
"Katika kitabu."
"usiamini kila unachosoma kwenye vitabu vya hadithi."
"Hakikuwa kitabu cha hadithi."
Kimya kizito kikazagaa humo ndani kwa nukta kadhaa. Hatimaye Bessy akauliza "Sindano hiyo ipo au haipo?"


"Ndiyo - ipo."Dk. Beka alijibu kwa karaha. "Lakini haitumiwi ovyo. Kwa sababu humumaliza kabisa mgonjwa. Hata kama alikuwa asife atakufa."
"Kwa mtu asie na matumaini ....?"
"Ni nani wa kuamua kuwa hana matumaini? Si mimi. Ninavyoamini mimi, mtu anaepumua ni mzima, Hata kama tumaini la kupona ni moja katika milioni. Oh, tunapoteza bure wakati kuizungumzia sindano hiyo. Kwanza hatuwezi kuitumia bila amri toka juu. Ni nani wa kwenda ikulu? Wewe?
Na hata kama nitalazimishwa kuitumia sitaitumia. Nitajiuzulu. Kwa sababu moja tu. Siwezi kukubali kuua - kumwua mtu yeyote yule, achilia mbali mtu huyo kuwa rafiki yangu mkubwa."


Bessy alishusha pumzi ndefu akasema. "Nimekuelewa, Dk. Samahani."
Dk. Beka akapumua pia. Akasema, "Kuhusu swali langu?"



itaendelea.
 
tunashukuru mkuu..huyo jamaa aliyekutoa sege dansa tunamshukuru sana , tulikosa uhondo muda mrefu
 

Huyo hayawan kashapatikana au? Ndio umeshaghaili kumsaka maana Ni muda haujatupa muendelezo wake
 
SEHEMU YA TANO.

Enspekta Bessy aliinua mabega kidogo akasema. "Tunafanya - na tutaendelea kufanya kila tuwezalo ili tumpate mtu huyo. Kwa bahati mbaya kama nilivyokwambia, hakuna aliewahi kuzisoma namba za gari lililomgonga Dk. Makete. Mara tu lilipomgonga lilipinda na kutoweka. Tunachokifahamu ni kuwa gari hilo ni jeupe - pengine Benzi. Na aliekuwa akiendesha alivaa koti au jaketi la kunguru. Ni msaada mdogo sana."
Dk. Beka akatikisa kichwa.

"Tegemeo langu kubwa lipo katika kumhoji Dk.Makete." Bessy aliendelea.
"Nadhani sasa unauona umhimu wa kuzungumza naye mapema iwezekanavyo."
"Tutaangalia atakapo zinduka. Lakini usitegemee kuwa itakuwa leo au kesho. Upasuaji anaofanyiwa ni mkubwa na mgumu. Ameamua vibaya. Ni bahati kuwa hai hadi hivi sasa. Kinachomsaidia ni kuwa alikuwa na afya nzuri sana."
"Jambo moja jingine." Alisema Bessy akiifunga kalamu. "Atakapotoka thieta lazima apewe chumba cha peke yake."
"Hilo sio la kusema, Raymond atahudumiwa kama Rais."

"Ninazungumzia usalama wake."Besy alisema kwa sauti kavu huku akiendelea.
"Atakuwa na askari chumbani mwake masaa ishirini na nne. Aliejaribu kumwua, naamini ni mtu alietaharuki. Katika hali ya kawaida huwezi kufanya kitendo kama kile, kujaribu kuua kwa gari hadharani. Ni bahati yake namba za gari hazikupatikana, ama sivyo tayari angeshakua pabaya."
"Unawasiwasi anaweza kujaribu tena - hapa hospitalini?"
Bessy alikubali kwa kichwa, "Akisikia Dk. Makete angali hai atazidi kutaharuki. Acaha huo uhasama wao wa mwanzo.Makete akipona na kumtaja, atakamatwa na kufunguliwa shitaka la kujaribu kuua. Hilo si shitaka la mchezo.Lazima atakuwa anafahamu hivyo.

Dk.beka hakusema neno.
Bessy akaendelea, "Kwa hiyo lazima alindwe usiku na mchana. Na uhakikishe watu wanaoingia chumbani mwake kumhudumia - madkatari, wauguzi,wafagiaji na kadhalika ni watu waaminifu wa hali ya juu. Mmojawapo ni yule nesi aliekuwa kwenye gari la wagonjwa." Bessy alikifungua kijitabu chake akalitafuta jina la nes huyona kusema ,"Miriam"
"Hakuna wa kumdhuru hapa hospitalini."
Alisema Dk.Beka .
"Anapendwa na kila mmoja. Wengi wao walitokwa machozi kwenye karamu ya kumuuaga."
"Kama miaka minne hivi iliyopita. Minne na nusu."
"Na tangu wakati huo hakuna watumishi wowote walioajiriwa?"
"Oh,wapo. Kila mwaka tunapokea wawili watatu wapya. Hata hivyo sidhani kama kuna wa kumdhuru."
"Huwezi kujua. Kuna kitu kiitwacho pesa. Watu wanafanya mambo ya ajabu sababu ya pesa."
"Vizuri, nitakuwa macho." Alisema Dk. Beka. Akauliza, Kwa nini umempendekeza nes Miriamu?"
"Alipoona aliegongwa ni Dk. Makete alifadhaika mno.

Alijijasirisha kiume asitokwe machozi hadharani. Lakini alipoingia garini wakati akinipa jina lake, machozi yalikuwa yanamlengalenga."
Dk. Beka akakubali kwa kichwa . "Miriam alimhusudu Dk. Makete. Na Raymond alimpenda Miriam kama mwanae."
"Huyo ndio wa kumhudumia Dk. Makete."
"Lakini Miriam hakuwa mtu wa pekee kumhusudu Dk. Makete. Wengi walimhusudu. Karibu watumishi wote. Huwezi kufanya kazi na mtu kama Raymond bila ya kumhusudu. Alipokuwa kiongozi wa hosptitali hii hakuna shida hata ya mtu mmoja aliyoipuuza, iwe shida kubwa au ndogo. Mara kadhaa alitoa pesa mfukoni mwake kuwasaidia waliokwama.
"Katika miaka kumi ya uongozi wake," Dk. Beka aliendelea, "Hakuna mgogoro wowote mkubwa uliotokea isipokuwa mmoja tu. Wa wizi wa mhasibu wetu wa zamani. Hata hivyo Raymond alimpa nafasi ya kurudisha pesa alizoiba, ili mambo yaishe na yasifike kokote. Lakini Bosco - huyo mhasibu ambaye sikufichi alikuwa hapendwi na kila mtu alijiona majanja sana. Aliamini kuwa mahakamani angeshinda. Hakushinda. Alifungwa miaka saba. Na bado Raynmond alimsikitikia kama vile hakustahili adhabu ile,na hali alidokoa mali ya umma. Kusema kweli Bessy, mimi sina moyo huo.
"Yaelekea wewe na huyo Bsco mlikuwa mlikuwa mbalimbali."
"Si mimi tu. Bosco alikuwa na tabia mbaya. Licha ya kuwa na dharau na kiburi, alikuwa na tabia yakuchelewesha kusudi malipo ya watu mpaka apewe chochote. Na wakati mwingine alichukua Benki pesa za mishahara ya wafanyakazi na kuzizungusha kwanza kwenye biashara zake kisha baade ndio huja kulipa. Tulimwonya lakini wapi. Kama mimi ningekuwa ndio Raymond ningekwishamtimua mapema sana, hata huo wizi usingetokea."
Bessy akashusha pumzi. Baada ya kurudisha kalamu na kitabu mkobani.
Akasema, "Ninavitaji vitu vilivyokuwa katika mifuko ya Dk. Makete. Ni kutapatapa tu, lakini imewai kutokea kitu kimoja kutoa mwanga. Na gari lake lazima likaondolewe pale lilipo. Nitazihita pia funguo."
"Nitakupatia."
"Na familia yake je,imekwishaarifiwa?"
"Ndiyo. Hilo lilikuwa jambo la kwanza. Mkewe amekwisha fika. Ilibidi na yeye adungwe sindano ya kumtuliza. Tumempa kitanda apumzike. Mwanae ni mwanajeshi. Yuko Ndala nimekwisha yaarifu Makao Makuu ya Jeshi. Watamfahamisha."
******************************
Mafunzo ya ukomandoo hutolewa hatua kwa hatua, sehemu mbalimbali . Karibu kambi zote za mafunzo ya msingi huwa msituni, kwa nchi zenye misitu. Kwa baadhi ya nchi zisizo na misitu huwa hata mapangoni.
Katika kambi hizo wanajeshi hujifunza mambo mbalimbali, kama vile ukakamavu,ujasiri, uvumilivu, kutumia silaha mbalimbali, kupigana, kujificha na kufichua,kukimbia na kukimbia masafa marefu usiku na mchana kwa kutumia ramani, dira, jua, mwezi hata nyota. Na wakati wote hujifunza kuua bila kusita wala kuona kinyaa au kuchafukwa matumb. Kuua kwa kutumia chochote kile.

Kambi ya Mafunzo ya Msingi ya Ukomandoo (KMMU) ambako Luteni Dennis Makete alikuwa Mkufunzi mmoja wapo, ilikuwa katikati ya msitu wa Ndala,zaidi ya kilomita mia na hamsini kutoka jiji la mji mkuu.
Ilikuwa kambi ya siku nyingi lakini haikua na jengo la kudumu hata moja.Palikuwa na mahema tu.


Itaendelea.
 
SEHEMU YA SITA.


Sajini Bob alikazana kujipepea kwa gazeti. Yeye na Koplo Butu walikuwa wameketi ndani ya gari lao la polisi waliloliegesha pembeni, karibu na makutano ya barabaraya Wazawa.
Palikuwa mahali pa pirikapirika za magari. Taa za barabarani, ambazo zilikuwa za kisasa, za kuning'inia juu,zilikazana kuamuru maderevakusimama na kuondoka. Bob na Butu walikuwa wakisubiri mtu avunje sheria wamtoe upepo au wamchukulie hatua, mno hilo la kwanza.


Bob ambaye alikuwa mnene, na hasa sehemu ya tumbo alikuwa akitokwa jasho, pamoja na kujipepea kwa nguvu na kuuacha wazi mlango wa upande wake. Butu, aliekuwa mwembamba, alikuwa mkavu kabisa. Alikuwa anavuta sigara na kuuangalia kwa jicho moja moshi aliokuwa akiupulizia pembeni. La pili likiyavinjari magari yaliyosongamana barabarani, akiomba kimoyomoyo mojawapo livunje sheria.


"Unaweza kuvuta katika fukuto kama hili?" Bob alimwuliza. Yeye hakuwa mvutaji. Alikuwa mtu wa lawalawa. Hata dakika hiyo alikuwa akimung'unya moja. Alitaka kumuuliza, Na wewe unaweza kufutuka mtumbo katika usawa mgumu kama huu.? Lakini akajikuta akisema , "Ni mazoea, Bob mazoea." Akaongeza, "Wanasema mazoea ni kitu kibaya sana. Nadhani ni kweli. Kusema kweli, mimi hukushangaa wewe kuweza kumung'unya pipi wakati wote.Mdomo haochoki?"


Bob akaguna. Akaitazama saa yake na kusema, "Nadhani tunapoteza bure wakati wetu hapa." Kisha akatega masikio.


Wote wakausikia mvumo wa injini inayolalamika kwa kulazimishwa. Wakageuza kichwa. Wakaliona gari lenyewe. Lilikuwa Jeep la kijeshi likitokea upande wa Ndala na kuelekea mjini. Taa zote za gari hilo zilikuwa zikiwaka, honi ikihanikiza, likichenga magari mengine kama mchezaji wa mpira aliepania kufunga goli.


Bob akatikisa kichwa. Akasema kwa karaha, "Hawa wanajeshi wakati mwingine hujisahau kabisa. Huyu lazima tumfunze adabu. Ndio wanaosababisha ajali za kipumbavu kama ile iliyotokea nyuma ya benki leo asubuhi."


"Ile haikuwa ajali ya kawaida, Bob." Butu alimkumbusha. "Ilikuwa kusudi."
"Hata huyu akigonga itakua kusudi." Ingawa taa za barabarani zilimuamuru derva wa Jeep asimame lakini hakusimama. Huku matairi yakiuma lami na kulalama, akapinda kushoto na kuendelea na safari yake kwenye barabara ya Wazawa."


Bob akaufunga mlango wa gari kwa nguvu kupita kiasi na kuamuru, "Mwandame!" Butu akasita. Akasema, "Bob unadhani hakutuona?'


"Una maana gani?"
"Katuona!"
"Kwa hiyo?"
"Ametudharau!"
"Nimesema mwandame!" Bob alifoka kwa sauti yake ya kisajini. "Tutaona mwisho wa dharau yake!"
Butu alitia moto gari. Huku king'ora kikibweka na kimwelumwelu kikimetemeta,wakaliandama Jeep.Lakini hakuweza kulikamata.


Hatimaye likapinda kushoto na kutulizwa kwenye uwanja wa kuegesha magari wa Hospitali Kuu ya Serikali. Mwanajeshi aliekuwa akiliendesha akateremka na kuelekea lango kuu.
"Kamkamate!" Bob alimwamuru Butu,baada ya mwenzake kulisimamisha gari kando ya Jeep lililotapakaa vumbi.
Butu akasita. Akasema, "Bob yule ni Luteni," "Kwa hiyo?" Huoni kama ni bora uende wewe?" "Hapana! Nenda wewe. Akileta ukorofi nitakuja kukusaidia."
Kwa shingo upande, Butu akateremka na kumfuata mwanajeshi yule, ambaye alikuwa akilikaribia lango. Akamwita, "Luteni!"
Mwanajeshi akasimama na kugeuka taratibu. Akauliza, "Kitu gani?" "Kuhusu uendeshaji wako .... Butu akauhisi mdomo wake ukiwa mzito.


Akajikuta anaangalia macho ambayo hajapata kuyaona maishani mwake .Yalikuwa kama ya Nyoka alieghadhabika. Kama yanatoa cheche . Kama yanayosema , "Ropoka neno moja tu la kipuuzi na utaingizwa humu ndani kwa machela."
Ghafla, Butu akaanza kutokwa jasho jembamba .Mwanajeshi aligeuka na kuingia hospitalini.Kwa hatua nzito za kupwaya Butu akaanza kurudi kwenye gari lao. Akilini akishindwa kuamini kijana kama yule kuweza kuwa na macho kama yale, pamoja na kuwa mwanajeshi.


"Vipi?" Bob alimwuliza. Butu alijikuna kichwa na kusema, "Alikuwa na sababu ya kuendesha vile."
"Sababu?" Bob akauliza. "Sababu gani?"
"Eee. Ya usalama." Usalama? Usalama gani?"
"Usalama wa Taifa," Alijibu Butu huku akiingia garini. "Bob akauliza, "Usalama wa Taifa?"
"Bob, acha kuwa kama kasuku." Alisema Butu akilitia gari moto. "Kijana yule si wa kawaida. Achana naye. Twende zetu."


Itaendelea
 

Hahahaha! Hapo wamekutana wrote waoga Bob na butu
 
SEHEMU YA SABA.


Dennis alitembea kwa hatua ndefu, sakafu ikivuma kila alipokutana na soli ya kiatu chake cha kijeshi.
Alikwenda moja kwa moja kwenye ofisi ya Daktari Mkuu, ambayo zamani ilikuwa ofisi ya babake. Alipotaka kubisha mlango ulifunguliwa na Dr. Beka akachomoza, akiwa anataka kutoka.
"Ooh, Denny!"
"Mjomba! Imekuwaje?"
"Mzee amegogwa na gari. Ametolewa thieta sasa hivi. Twende tukamwone."


Wakaanza kutembea kulekea kwenye majengo ya kulala wagonjwa. "Hali yake ikoje?" Dennis aliuliza.
"Ni mapema mno kusema lolote la uhakika. Jambo mhimu ni kwamba angali hai."
"Mama je?"
"Alishituka mno. Ikabidi adungwe sindano ya kumtuliza. Amepewa kitanda apumzike."
"Ajali hiyo imetokeaje?"
"Bora akueleze Inspekta Bessy, anaeifanyia uchunguzi. Yupo hapa hapa hospitalini, anamsubiri mama yako aamke."


Waliingia jengo D, wakapanda ngazi hadi ghorofa ya pili. Kila upande kulikuwa na vyumba. Wakasimama mbele ya mlango Namba 13. Dk.Beka akaufungua, wakaingia.
Kilikuwa chumba cha ukubwa wa wastani,chenye kitanda kimoja, viti viwili, sofa moja dogo, kimeza na kabati. Madirisha yote yalikuwa wazi, pazia zimekunjwa. Juu pangaboi lilizunguka kwa kasi ya wastani.


Kwenye kiti kimojawapo aliketi kijana ambaye alionekana wazi kuwa ni askari, ingawa alivaa kiraia. Kitandani alilala Mzee Raymond Makete, macho amefumba,akiongozewa damu iliyokuwa inaning'inia kando ya kitanda.
Dk. Beka akainama na kumchunguza mapigo ya moyo. "Ni dhaifu," Alisema, "Lakini si hali ya kutisha. Ni jambo la kawaida kwa mtu aliefanyiwa operesheni ngumu kama yake. Twende tukamuone mama yako."


Alipofika mlangoni, Dk.Beka akakumbuka jambo. Akageuka na kumwambia kijana alieketi kitini. "Huyu ndiye Luteni Dennis Makete." Kijana huyo alikubali kwa kichwa na kusema. "Ndiyo mzee."


***********************


"Butu, ulisema yule kijana sio wa kawaida. Ulikuwa na maana gani?" Bob alimuuliza mwenzake. Walikuwa wanakula chakula cha mchana katika kantini ya Kituo Kikuu cha Polisi.
Tonge mdomoni, Butu alitikisa kichwa. Akatafuna na kumeza. Akasema, "Kusema kweli, Bob, sijui." Akawaza kwa nukta mbili tatu, huku akifinyanga tonge jipya. Yeye hakuwa akitumia kijiko kama mwenzake. Hatimaye akasema. "Huoni kuwa si jambo la kawaida kijana kama yule kuwa Luteni?"
"Kwa nini?"

"Ni mdogo mno. Sana sana atakuwa na miaka ishirini na tatu au na nne tu. Mimi nakaribia kutimiza miaka thelathini, wewe umekwishavuka. Lakini tazama - wewe ungali Sajini na mimi Koplo."
"Hilo si ajabu. Mbona hushangai yule msichana, Bessy kuwa Inspekta, na hali ni mdogo kuliko sisi? Tena mwanamke. Si kwa sababu unafahamu amesoma kuliko sisi. Ana shahada ya Sheria. Pengine yule Luteni pia amesoma kuliko sisi. Au pengine katenda kitendo cha kishujaa. Wanajeshi wana nafasi nyingi za kupandia vyeo, sio kama sisi wachunga magari."


"Tonge mdomoni, Butu akasema kama anaewaza kwa sauti. "Lakini macho yake....."
"Macho yake? Bob aliuliza, akiwa ameachwa mbali. "Macho yake yana nini?"
"Si ya kawaida - kwa kijana mdogo kama yule." Alijibu Butu, uso ameukusanya, akiwaza kwa dhati. "Yanatisha. Ni ya mtu asieogopa chochote, anaeweza kufanya lolote. Sitashangaa kusikia amekwishaua. Yaani kikazi. Jinsi gari lake lilivyochafuka, bila shaka ametoka Ndala."
"Ndala?"
"Usianiambie kuwa hujui nini kinachoendelea katika msitu wa Ndala."
"Oh, kuna kambi ya wanajeshi."


"Si wanajeshi wa kawaida. Ni makomandoo. Makomandoo si watu wa kuchezea hata kidogo. Kozi wanayochukua ni ngumu mno. Huwezi kuichukua bila kutafuta uchizi kidogo. Kwao kuua na kuuawawa ni jambo la kawaida kabisa."
Bob alibaki kimya.


Butu akaujaza mdomo. Akasema huku akitafuna, "Unakumbuka mwaka jana - Kikosi 32x kilipoasi na baadhi yao wakakimbilia msituni? Walitumwa makomandoo wachache tu kwenda kuwashughulikia waliokataa kujisalimisha. Hawakuwa zaidi ya makomandoo ishirini, lakini waliwateka waasi zaidi ya miatatu na kuwaua zaidi ya mia."
"Na wao?" Bob aliuliza huku akitafuna.
"Hakuna hata mmoja aliyejeruhiwa! Inawezekana mmoja wapo alikuwa yule Luteni."

Uso wa Bob ukanywea. Akabaki akiuchezea wali wake kwa kijiko. Hatimaye akasema, "Na kuhusu usalama wa Taifa? Ulikuwa na maana gani?"
Butu akaanguka kicheko kirefu. Kiliwafanya wote waliokuwa humo ndani wageuke kumtazama. Alikuwa kama aliepagawa. Alipoweza kujizuia akamwuliza, "Bob, uliamini?"
Uso ukiwa bado umemnywea, Bob akatikisa kichwa.


"Kijana yule," Butu alinong'ona, "Hakusema lolote zaidi ya kuniuliza, "kitu gani?" basi."
Taratibu uso wa Bob ukaanza kuchanua . Akatabasamu. Ghafla na yeye akakiangua kicheko chake cha mwaka. Butu akamtazama kwa mshangao. Akashindwa kujizuia. Akajiunga naye.
Askari aliekuwa meza ya pili akawatazama kwa mshangao. Nae pia akashindwa kijizuia akajiunga nao. Akamwambukiza askari wa kike alieketi naye. Kufumba na kufumbua, ukumbi mzima ukalokezwa. Kila mmoja aliekuwemo humo akawa anacheka kama aliepagawa.


Itaendelea...
 
Cookies are required to use this site. You must accept them to continue using the site. Learn more…