Riwaya: Msako wa Hayawani

shukran mkuu huu ndo ulevi wetu wengine so jitaidi kutupatia vipande japo viwili kwa cku ki1 asbh na kingine jioni ni ombi pliz!
 
SEHEMU YA NANE.

Mbele ya jumba namba 21 Mtaa wa kitosi,eneo la Buffalo Hill, palikuwa na bustani nzuri ya maua iliyokuwa ikitunzwa na kijana wa makamo aliejulikana kwa jina la Kikoti, kwa sababu kikoti shake kikuukuu kilikuwa hakimtoki mwilini, iwe siku ya joto au baridi, mvua au jua.


Nyuma ya jumba hilo palikuwa na bwawa kubwa la kuogelea. Kando yake, hapa na pale, palikuwa na miamvuli mikubwa ya rangi mchanganyiko.
Chini ya mwamvuli mmojawapo waliketi Kassim na Kembo kwenye viti vya kukunja vya kitambaa cha turubai. Kati yao palikuwa na kimeza kifupi chenye chano chenye chupa ya pombe kali, glasi mbili,kibakuli cha vidonge vya barafu na kibakuli cha bisi.


Kassim alikuwa amevaa kaptura nyeupe kama ya kuchezea tenesi, na shati jepesi ambalo halikufungwa vifungo. Alikuwa akivuta sigara yake ya kahawia ya kutoka Havana.
"Mtu wako ni daktari mstaafu Raymond Makete." Alisema Kembo akijichanganyia kinywaji, baada ya Isidori aliyewaandalia, kuondoka.
"Raymond Makete?" Kassim aliuliza akiwaza. Kembo alikubali kwa kichwa, akimeza funda. Alikuwa hajatimiza hata miaka arobaini, lakini alikuwa na mvi. Zilimfanya aonekane mkubwa zaidi kuliko alivyokuwa.


Akasema, "Alikuwa daktari mkuu. Alistaafu miaka mnne au mitano iliyopita." Kassim akatingisha kichwa. "Simfaham.Sijui alinijuaje! Ikoje hali yake?"
"Mbaya, mahututi. Amefanyiwa operesheni ngumu iliyochukua masaa. Ametolewa thieta muda mfupi tu uliopita. Yuko jengo D, ghorofa ya pili,chumba namba kumi na tatu - cha mwisho mkono wa kulia."
"Kwa ujumla ikoje hali yake?"
"Sijui. Mpaka anafikishwa hospitalini alikuwa hajitambui. Sijui huko thieta. Lakini jinsi hali yake inavyosemekana ilivyo, haiyumkini kusema lolote la maana."


Kembo aligida funda akauliza, "unasema alikutambua - una maana gani?"
"Nilikuwa natoka benki. Tukagongana mlangoni. Akanitazama kwa macho makali na kuniuliza kama ndie Kassim. Alinishitua sana."
Kembo alisogea kwenye ncha ya kiti akamkazia macho mwenyeji wake na kumwuliza, "Bwana Kessy, wewe ndie uliemgonga?"


"Nilitaharuki!" Kassim alimaka. "Jinsi alivyonitazama ,nina hakika kuna kosa nililomtendea siku za nyuma. Sijui ni kosa gani, lakini inaelekea ni kubwa, lisiloweza kusameheka pamoja na miaka kupita. Kosa ambalo lingeweza kuniangamiza kama angeripoti."
Kembo alivuta pumzi akajiwashia sigara.


Kassim akaendelea, "Kwanza sikukusudia kumgonga. Nilisubiri mbele ya benki ili akitoka nimtazame vizuri, pengine ningemkumbuka na kukumbuka nilichomtendea. Hakukawia kutoka. Hilo liliniongezea hofu. Ilikuwa wazi hakufanya chochote humo ndani, kama vile aliairisha shughuli zake kwa sababu yangu."
Baada ya kuibandika sigara mdomoni na kuibandua, Kassim akaendelea, "Nikaamua kumfuata nione anaelekea wapi. Akaelekea nyuma ya benki. nikajua anaelekea polisi. Nikafikia upeo wa kutaharuki. Nilipoona sehemu yenyewe haina watu nikaona la kufanya ni moja tu - kummaliza hapohapo. Kwa vile bastola sikuwa nayo...."


"Hukummaliza sawasawa." Alisema Kembo. Akauliza, "Unauhakika hakuna mtu alieiona ajali hiyo? Hakuna aliechukua namba za gari?"
"Sijui. Eneo lote la karibu lilikuwa tupu kabisa. Isitoshe, niliwahi kukata kona na kutoweka. Kitendo chote kilitendeka katika nukta chache tu."


Kembo akatikisa kichwa. Akasema, "Mzee Mustafa atakaposikia hatafurahi. Tulipo tuna matatizo ya kutosha. Kuna watu wenye silaha - bunduki, bastola, nondo na mapanga waliofanya ghasia leo asubuhi katikati ya jiji. Kadhaa wamekamatwa, baadhi yamejeruhiwa, wawili wamekufa hapo hapo. Idadi ya wafu, bila shaka itaongezeka. Serikali na viongozi wa vyama vingine vya upinzani wanadai watu hao ni wetu."

Baada ya kuipeleka glasi mdomoni na kumeza, Kembo akaendelea, "Jambo hili la Dk. Makete si dogo. Linaweza kuharibu kila kitu. Watu kadhaa wanajua kuwa Mzee Mustafa ni rafiki yako, na unamsaidia katika kampeni yake. Baadhi yao ni maadui zetu. Lakini hakuna anaeijua historia yako ya kweli. Kila mtu anaamini kuwa Kassim Hashiri ameshakufa siku nyingi. Ikijulikana kuwa ndio wewe ..." Kembo akatikisa tena kichwa. "Hapana! Mzee Mustafa hatafurahi hata chembe."


"Mustafa ananihitaji mimi zaidi kuliko ninavyomhitaji yeye."Kwa hivi sasa ndiyo. Lakini atakapokuwa Rais ..."
"Hataweza kuwa Rais bila msaada wangu!"
"Bwana Kessy, usidhani uko peke yako unaemsaidia Mzee Mustafa ashinde katika uchaguzi ujao hata kama utajitoa ..."
"Ah! Sasa tunazungumza kama wapumbavu."
Alisema Kassim. "Ile ajali ilitokea saa nne asubuhi. Sasa ni saa tisa. Masaa matano yamekwishapita. Polisi wangezipata namba za gari yangu wangeshakuwa hapa zamani. Ingewachukua muda mfupi tu kujua anaemiliki na anapoishi."


"Dk.Makete angali hai." Kembo alimkumbushia.
"Dakika yoyote anaweza kuzinduka na ..."
"Ulisema una watu wako hospitalini?"
"Kwa hiyo?"
"Lazima nikuchoree picha?"
"Bwana Kessy, kutaka kuelezwa jina la mgonjwa na hali yake ilivyo ni jambo moja. Kutaka mgonjwa huyo amalizwe ni jambo jingine kabisa."


"Watu wako wameshafanya vitimbi vikubwa zaidi kuliko kumchinja lagalagamauti. Isitoshe, kila siku wewe hudai hakuna lisilowezekana."
"Hili litakugharimu pesa. Kitita cha kutakata."
"Usijali gharama. Niko tayari kutoa kiasi chochote kile. Milioni mbili, tatu..hata tano...hata kumi ikibidi! Mtu yule akipona na kunitaja maisha yangu yatakuwa hatarini. Kwa kosa la kujaribu kuua tu naweza kufungwa maisha, achilia mbali hayo makosa mengine."


Kembo akakubali kwa kichwa, macho yake yakimeta kwa matumaini. Akasema kwa sauti tulivu, ya kirafiki, iliyojaa huruma na upendo. "Niachie mimi."
 
SEHEMU YA TISA.

Dk. Beka aliufungua mlango wa chumba cha mapumziko namba Namba 4 wakaingia wodini. Kilikuwa chumba kidogo chenye kitanda na kiti kimoja. Kwenye kiti aliketi Bessy, kalamu mkononi, kijitabu chake gotini. Kitandani alilala Mama Denny, Bi mkubwa wa makamo. Alikwishaamuka lakini macho yake yangali na machovu.


Kufunguliwa kwa mlango kulimfanya ayapeleke macho yake upande huo. Akamwona mwanae. Akasema, "Denny!"
"Mama!" Dennis akavuta hatua mbili ndefu na kukifikia kitanda. Akaketi nchani na kuufumbata mkono wa mamake. Akamuuliza
"Unajisikiaje sasa mama?"
"Sijambo."Sauti yake haikuwa madhubuti kama aliyoizoea Dennis. Alivikanda vidole vyake,alimwambia. "Punguza wasiwasi. Baba atapona tu."
"Oh! Denny! Nilishituka mno!"
"Hata mimi nilishtuka niliposikia. Baradhuli aliyeniarifu alisema hali ni mbaya sana."
Bi mkubwa akashusha pumzi. Dennis akaendelea. "Madamu ametoka thieta salama, atapona tu. Mjomba amemkagua sasa hivi. Amesema anaendelea vizuri, hana hali ya kutisha."


Kikapita kimya cha nukta mbili tatu. Dk.Beka akakivunja kwa kusema, "Denny, huyu ndiye Kachero Inspekta Bessy."
Dennis akageuzwa kichwa. Ajikuta anatazamana na msichana wa rika lake. Tena wa kuvutia. Na kwa mara ya kwanza tangu aingie humo humo ndani akaisikia harufu ya marashi anayoyapenda - ya Gucc. Akashangaa kimoyomoyo kwa nini vitu hivyo viwili, uzuri wa binti huyo na manukato yake, hakuvigundua mapema!

Ulipita muda ndipo Dennis akajitambua kuwa alikuwa anakodoleana macho na msichana huyo. Bila ya kujijua ikamtoka "Oh!" kwa sauti ndogo.
Bessy akanyoosha mkono. Dennis akaupokea. Akashangaa kuona haukuwa legelege kama alivyotazamia. Ulikuwa mkakamavu karibu sawa na mkono wa kiume.
Akasema, "Inasikitisha kukutana nawe mahali kama hapa. Ilifaa tukutane mahali pachangamfu zaidi."
"Kama vile kwenye karamu, au dansini?" Sauti yake haikuwa na stihizai hata chembe.Ilimfurahisha Dennis na kumpunguzia majonzi.


"Dr.Beka akauliza. "Umeambua lolote la kukusaidia kutoka kwa mama Denny, Inspekta?"
"Ameamuka punde tu." Alijibu Bessy. "Alichowai kunieleza ni kwamba Mzee Makete aliondoka asubuhi nyumbani kwenda benki kuchukua pesa."


"Hilo nilikuwa nikilifahamu. Katika vitu nyake vya mfukoni mlikuwa na kitabu cha hundi. Kinachoshangaza ni kwamba hakuandika hundi yoyote leo, na hali aligongwa wakati anatokea benki,na sio akienda benki."
"Ajali yenyewe ilitokeaje?" Dennis aliuliza.

"Nasikitika kusema hadi hivi sasa tunachokijua kwa hakika ni kidogo mno. Tunaamini baba yako amegogwa na Benzi jeupe nyuma ya Bnki ya Wakulima. Aliemgoga hakusimama, na hakuna aliewai kuchukua namba za gari. Tunashuku alimgonga kusudi.
Mdomo wazi kwa mshangao, Dennis akauliza. "Unamaana alitaka kumwua?"
"Nasikitika yaelekea hivyo." Alijibu Bessy.


Baada ya kushusha pumzi akaendelea, "Kwa hiyo inaelekea kuna mtu mwenye uhasama na baba yako. Uhasama mkubwa."
"Huo ni mzaha!" Dennis alimaka, akikiri kimoyomoyo alishindwa kutumia neno 'upuuzi' kwa sababu ya staha.
Bessy akainua mabega. Baada ya kupumua kwa nguvu, Dennis akauliza. "Ndiyo kusema huyo mwendawazimu amepuruchuka?"
"Ni mapema mno..."
Dennis akamkatiza. "Hamna fununu yoyote?" Akamtazama Dk. Beka . "Baba hakuwahi kusema lolote?"


Ni Bessy aliemjibu. "Katika maneno aliyoyatamka ni mawili tu yaliyosikika vizuri. 'kasi hashi.' Je yana maana yo...."
"Kassim Hashir!"
Wote wakageuza vichwa kumtazama mama Denny.


Kwa sauti yake dhaifu, akarudia,"Kassim Hashir!" Kisha akaongeza kwa uchungu "Oh,Mungu, hapana! Oh, Mungu wangu!"


*********************************


Kikoti alikuwa mdaku. Wakati akiusokota mpira wa maji, alipolipua, mawazo yake yalikuwa mbali. Hakuwa na furaha.Yeye alikuwa mtu asiyependwa kupitwa na jambo. Lakini leo, aliamini, palikuwa na jambo linalotaka kumpita. Na huo ni mwiko wa mdaku.


Mapema alichanganywa na vitendo vya mwajiri wake - kumwona akilikagua gari lake kwa uso mzito na kijasho usoni, kama vile lilikuwa na dosari kubwa; kumwona akimwonyesha Isidori sehemu ya mbele ya gari; kumwona akimpa koti lake jipya na la thamani.


Lakini juu ya yote, ilikuwa kumwona akimsimulia Isidori kisa kirefu. Haikuwa tabia yake. Tabia yake kwa watumishi wake ilikuwa ni kutoa amri. Neno moja au mawili tu. Basi kwisha. Siyo kutoa maelezo ya dakika kadhaa.
Hapana. Palikuwa na jambo linalotaka kumpita.
Kuhusu lile koti, moyo ulimwuma. Kwa nini asipewe yeye maskini wa Mungu? Isidori alishawahi kupewa nguo mara kadhaa. Si mpya na za zamani kama lile koti, lakini nguo ni nguo. Isitoshe, alikuwa akishonewa nguo za kazi.Juu ya hayo, ilikuwa dhahiri mshahara wake ulikuwa mkubwa kuliko wake. Mshahara na marupurupu. Na nafasi ya vitu vya... vya 'kuokota' katika jumba hilo.


Lakini, Kikoti aliiuliza nafsi yake, kama koti lie angepewa yeye angelifanyia nini? Asingeweza kulivaa. Yeye alikuwa mfupi na mwembamba. Na wala asingeweza kulipeleka kwa mshoni alipunguze. Ni dhahiri angeliuza.
Je, hilo ndilo lililomfanya Mzee asimpe yeye?


Alitaka kumpa mtu wa kuweza kulivaa na kumwona amelivaa muda wote? Kwa nini Isidori baada ya kulijaribu,alipotaka kulivua alikatazwa? Kikoti alikiona wazi wazi kitendo hicho. Hata kauli ya mzee aliisika - "A-a! Usilivue. Livae tu likuzoee....limekupendeza."

Kikoti hakudhani hivyo. Hakudhani lilimpendeza Isidori. Aliona limempwaya na halikuchukuana na weusi wake wa mpingo. Au ni maya? Kisa cha sungura na zabibu? Na lile gari je? Lilikuwa na dosari gani
Na ile risala je? Mbona ilikuwa ndefu vile? Na Mzee alizungumza kwa sauti ya chini, mara moja moja akimtupia jicho yeye, kama vile hakutaka amsikie, kama vile ilikuwa siri kubwa.


Hata hivyo alidaka maneno mawili matatu, kama vile 'ajali, heshima yangu, faini na fidia...'
Hapana. Lilikuwepo jambo linalotaka kumpita. Jambo kubwa. Asipokuwa makini, alijiambia, litampita kweli. Na huo ni mwiko kwa mdaku.
 
Heee! Kumbe idawa una Riwaya unayotuletea humu? Leo ndio nimeiona.
Ngoja nisubscribe nitaisoma ikiisha.
 
Last edited by a moderator:
SEHEMU YA KUMI.


"Ni nani mtu huyo?" Bessy aliuliza kwa sauti kali. Lakini mama Denny alikwishageukia ukutani na kuanza kulia kimya kimya.
Bessy akainuka na kumfanyia Dennis ishara ya kichwa kutaka watoke nje. Wakati wakitoka nje. Dk. Beka alijongea kitandani kumfariji mke wa rafiki yake.


Mara tu baada ya kutoka na kufunga mlango, Bessy akauliza kwa matuamaini makubwa. "Ni nani huyo Kassim Hashir?"
"Sijawai hata kumsikia katika maisha yangu." Dennis alijibu uso ukiwa umemnywea. Bessy akakunja uso.
"Itakuwaje usimfahamu na hali wazazi wako wote wawili wanamfahamu?"
"Unategemea kuwa nawafahamu watu wote wanaofahamiana na wazazi wangu? Mimi ni mwanajeshi, wakati mwingi huwa sipo nyumbani."
"Inalekea babako na mamako wanamfahamu vizuri mtu huyo. Nadhani mama yako anaufahamu uhasama uliopo kati ya babako na mtu huyo. Lakini katika hali aliyonayo hawezi kutueleza lolote. Ni vyema tumwache atulie."


Dennis akakubali kwa kichwa.
Baada ya kuwaza kidogo, Bessy akasema. "Twende zetu Makao Makuu ukachukue gari la babako. Na tukapekue mafaili. Pengine huko Kassim Hashir si mgeni nasi."

"Itabidi nifike Makao Makuu yetu kwanza nikarudishe gari lao na kuomba likizo ya dharura. Ikiwa nimeweza kuchokoa vikaragosi vya vichakani hakitanishinda cha mjini."


*********************
Siku hiyo Kikoti 'aliokota' nusu chupa ya wiski iliyosahauliwa chini ya meza,kando ya bwawa la kuogelea. Aliiona chupa hiyo kwa macho yake makali mara tu alipotokeza nyuma ya jengo hilo, akitokea kwenye stoo ya kuhifadhia zana za kazi yake.


Alipoina na kuikota na kuifutika kotini, mwenyewe alidhani hakuna mtu aliemwona. Lakini Kassim Hashir alikuwa dirishani, ghorofani, akimtazama. Hakujali. Si kwa vile alikuwa na mambo makubwa zaidi akilini, bali nusu chupa ya wiski ilikuwa si chochote kwake. Aliona kama vile mtumishi wake amefanya jambo zuri kuondoa takataka. Kwa upande mwingine, kitendo hicho kilimwongezea fahari, furaha,na utamu wa ukwasi - kuona kuna watu dhalili wanaodiriki kuiba hata chupa karibu tupu.


Nje ya geti, Kikoti alielekea kwenye kituo cha basi akiwa ameridhika kabisa na vuno la siku hiyo. Alijua nini cha kufanya. Atakwenda moja kwa moja kwa Shangazi suzy anakokunywa mapuya kila siku. Hapo asingekosa mtu wa kuelewana naye kwa namna moja ama nyingine.


*******************************
Alasiri hiyo, ulifanyika mkutano mfupi katika ofisi ya Daktari Mkuu. Kama kawaida, mwenyekiti alikuwa Dr.Beka mwenyewe. Wengine walikuwa madaktari bingwa wanne waliomshughulikia Dk. Makete thieta.


Baada ya wote kuketi, Dk.Beka akasema, "Sawa. Nipeni mawazo yenu."
"Ana matumaini makubwa." Alisema bingwa wa kwanza. "Tumejitaidi kadri ya uwezo wetu. Sidhani kama kuna mtu angeweza kufanya zaidi ya tulichokifanya. Naweza kusema tumefanya kazi nzuri."


Dk,Beka kakubali kwa kichwa. Akamtazama bingwa mwingine.
"Jambo zuri ni kwamba alifikishwa hospitali haraka." Alisema bingwa huyo. "Hakuwai kuvuja damu ndani kwa undani. Na vitu viwili mhimu, moyo na ubongo, havikuathiriwa."
"Na alikuwa na bahati nzuri," Alisema bingwa wa tatu. "Sisi sote tulikuepo na hatukuwa na shughuli mhimu."
"Likini itamchukua muda kupona sawasawa."
Alisema bingwa wa mwisho. "Na hata hivyo hatakuwa kama alivyokuwa zamani. Ninashuku itabidi atembelee kiti cha magurudumu maisha yake yote yaliyosalia."


"Cha mhimu ni uhai," Alisema Dk.Beka. "Ninachoombea, apone." "Tuna imani atapona. Tumefanya kazi nzuri sana."
*********************
Masjala ya Makao Makuu ya Polisi ilikuwa kubwa. Ilijaa rafu na makabati ya mafaili. Pia mlikuwa na meza mbili tatu, lakini Bessy na Dennis walipoingia, meza moja tu - ile kubwa kuliko zote ndiyo ilikuwa na mtu. Alikuwa amevaa kiraia.
Alisema, "Karibu Inspekta." "Asante Robby."
Bessy akajibu, akivuta kiti. Akaketi na kumwashiria Dennis aketi kando yake.


"Mbona umeadimika, Bessy?" Robby aliuliza.
"Siku nyingi sijawa na kesi mhimu. Leo nimeamua kujipa moja. Wengine walikataa. Walidhani ni ajali ya kawaida."
"Sasa nikusaidie nini?"
"Tuna habari zo zote kuhusu mtu aitwaye Kassim Hashir?"


Robby akabonyeza vibatani, akaliandika jina 'Hashir' kwenye kompyuta iliyokuwa mezani pake. Mashine ile ikaanza kuchakarika,ilipotulia Robby akasema, akisoma kwenye kioo. "Tuna Hashir mmoja tu. Kassim Ismail Hashir. Namba ya faili yake ni 997/69...."


"Sitini na tisa!?" Bessy aliuliza kwa mshangao. "Una maana faili hilo lilifunguliwa miaka ishirini na nne iliyopita?"
"Ndiyo na likafungwa mwaka 1974"
"Baada ya miaka mitano? Ilichukua muda huo kuikamilisha kesi yake?"
"Hapana. Kesi yake haikuwai kukamilika. Kassim hakuwai kukamatwa. Afariki."


Bessy akamtazama Dennis,macho yake yakimsaili. Alipokosa jibu akayarudisha kwa Robby. Akamwuuliza, "Kesi yake ilihusiana na nini?"
"Kwa hilo, maka tulipekue faili lake."
"Unaweza kutupatia,tafadhali?"
"Bila ya tabu." Robby akainuka na kuelekea kwenye rafu za mwisho. "Inaweza kuwa mzee amekosea - si Kassim aliemgonga?"
"Sijui." Alijibu Dennis."Lakini kadri niwezavyo kukumbuka, sijawai kumwona akikosea."
"Kumbuka hakuwa katika hali ya kawaida."


Kabla ya Dennis hajajibu, Robby alirejea mezani akiwa na faili ambalo halikuonyesha dalili yoyote ya kuwa na umri wa miaka ishirini na nne. Bessy akalipokea na kulifungua. Lilikuwa na ukurasa mmoja tu na picha ya kijana wa kati ya mika ishirini na mitano na thelathini mwenye uso wa duara na macho makubwa. Baada ya Bessy na Dennis kuitazama kwa muda, wakausoma ukurasa huo.


Kifupi,ulieleza kwamba Kassim Hashir alituhumiwa kutorosha kiasi kikubwa cha fedha za kigeni, dhahabu, almasi, na madini mengine ya themani, na vipusa, pembe za tembo na ngozi za chui. Vyote hivyo alivitorosha wakati wa utawala wa fasishti Ibrahim Mbwelwa. Kassim aliyeyuka muda mfupi kabla ya Mbelwa kuangushwa.Ilihisiwa alikimbilia Ulaya alikolimbikizia utajiri mkubwa. Alifia Kenya, mwaka 1974 katika ajali ya gari.Chini ya maelezo hayo palikuwa na saini.


Bessy akauliza, "Hii siyo sahii ya Mzee Maliki?"
"Ndiyo, ni yake." Robby alijibu. Lakini wakati huo hakua Kamishna Msaidizi."
Bessy akaitazama saa yake. Akaunyakua mkono wa simu na kusema. "Nipatie Mzee Maliki, kama angalipo ofisini mwake."
"Tangu lini akaondoka kabla ya taa kuwashwa?"
Aliuliza opareta. Kisha akasema, "Zungumza nae."

"Mzee? Ni Bessy hapa.Nataka kukuona."
"Kuhusu?" Ilikuwa sauti nzito, tulivu."
"Kassim Hashir."
"Kassim Hashir? Sidhani kama namfahamu."
"Si ajabu. Ni miaka mingi imekwishapita. Ulimfungulia faili mwaka 1969. Nitakuja nalo faili hilo."
"Sawa."
Faili mkononi, Bessy akainuka na kumwambia Dennis, "Twende kileleni."
 
mkuu ukimalizia sehemu ya 11 utakuwa umenisaidia sana jioni hii ya baridi kali.NAWASILISHA MAOMBI
 

mkuu ukimalizia sehemu ya 11 utakuwa umenisaidia sana jioni hii ya baridi kali.NAWASILISHA MAOMBI

Na mm nakazia ombi LA sniper
 
Mkuu endelea.hii mambo ni nzuri sana.
 
SEHEMU YA KUMI NA MOJA.

Kwa Shangazi Suzy palikuwa na mambo. Mojawapo lilikuwa ni lile la watu kutengwa kufuatana na daraja. Wateja wa daraja la kwanza - 'maofisa' waliwekwa chumbani, ambamo mlikuwa na kitanda maridadi, seti ya sofa, viti na meza. Labda waliwekwa humo kwa vile hawakuwa wengi. Na walikuwa wasafi. Na hawakupendelea sana mapuya. Zaidi walikunywa bia na konyagi.


Wateja wa daraja la pili - 'waungwana,' waliwekwa ukumbini kwenye mabenchi. Hakuna alieweza kukisia sababu ya wao kuwekwa hapo. Wengi wao walikuwa wa umri mkubwa. Mno walikunywa mapuya. Waliagiza konyagi kwa nadra. Bia - mwaka mara moja. Sikukuu hadi sikukuu.


Wateja wa daraja la tatu na la mwisho - vichwa vya panzi - waliwekwa uani, ambako walikalia chochote kile, kuanzia matofali hadi chini aridhini.
Sababu za wao kuwekwa huko zilikuwa wazi. Kwanza walikuwa wengi, na wengi wao walioga na kufua kauka nikuvae, Jumapili hadi jumapili. Pili walikuwa hususani watu wa mapuya. Tatu, walikuwa wadoezi na wagandaji - yaani nusu lita ilimfanya mtu agande hapo tangu asubuhi mpaka usiku wa manane. Na nne walilipata jina lao 'vichwa vya panzi' - kwa sababu walikuwa hawakawii kulewa . Na hapo huwa wenye kelele, wagomvi, waimbaji na wachezaji.


Lakini ajabu ni kwamba hakuna hata mmoja, hata siku moja, alielalamikia ubaguzi huo. Kila mmoja alipajua mahali pake na aliridhika napo.


Lakini kwa Kikoti alikuwa tofauti kidogo. Yeye alijipandisha ngazi moja moja. Alianzia kwa 'vichwa vya panzi' alipokuwa hana kazi maalum, ndiyo kwanza aingie jijini.
Akahamia kwa 'waungwana' alipopata kibarua katika kampuni moja ya ujenzi. Akahamia kwa 'maofisa' alipota kazi ya kuhudumu huko Buffalo Hill.


Hata huvyo, kwa kuwa hakuwa mgeni mahali popote, na alikuwa 'memba' kila siku,ilikuwa juu yake mwenyewe kuchagua pa kuketi - aghalabu kutokana na mfuko wake au mwaliko.
Siku hiyo, mfuko wa karatasi mkononi, alipitiliza moja kwa moja hadi chumbani akawakuta 'maofisa' wawili wa kudumu, Bob na Butu, wamekwisha fika,walikuwa wakinywa konyagi.Bob, kwa sababu ya kitambi chake, katika nguo za kawaida alionekana kama meneja wa benki.


Bila ya kusema neno, Kikoti aliitoa chupa ya wiski na kuikita mezani. Bob akaitazama kwa makini. Akainua uso na kuuliza. "Umeipata wapi wiski hii, Kikoti? Ni ya thamani sana!"
"Kanipa tajiri yangu." Kikoti aliongopa, macho makavu. "Huyo ndie tajiri wa kumtumikia. Nikichoka kufokeana na madereva wakorofi, nitakwambia unipeleke na mimi nikaombe kazi."


"Shangazi yupo wapi utupe glasi?" Kikoti akauliza. "Atakuwa wapi kama sio kwa vichwa vya panzi?" Butu alimwuliza.

**********************


"Karibuni." Mzee Maliki aliwakaribisha. Alikuwa mtu wa makamo alietazamia kustaafu muda wowote. Sare yake ya Ukamishna Msaidizi ilimpendeza sana. Ofisi yake ilikuwa pana na nadhifu.
"Ketini." Wakaketi. "Ni nani mwenzako Bessy?"


"Luteni Dennis Makete. Baba yake, Dk.Raymond Makete, aligongwa na gari leo asubuhi nyuma ya Benki ya Wakulima. Aliemgonga hakusimama na hakuna mtu aliwahi kuzisoma namba za gari. Tunaamini mtu huyo ni Kassim Hashir na alimgonga Mzee Makete kusudi."
"Simkumbuki..."


"Ulimfungulia faili hili mwaka 1969 na kulifunga mwaka 1974, ukiamini amekufa."
Mzee Maliki akalipokea lile faili na kulifungua. Baada ya kuupitisha macho ukurasa uliokuwemo, akasema, "Ndiyo, nakumbuka sana. Nilipokea telegram kutoka Polisi ya Kenya ikieleza Kassim Hashir alifikwa na ajali mbaya ya gari na kufariki papo hapo. Sijui kwa nini telegram hiyo haimo humu! Ukweli ni kwamba kesi yake ilikuwa dhaifu sana. Kila mtu aliidharau, pamoja na kuhusiana na mamilioni ya pesa za kigeni. Kwa nini mnadhani yuko hai na ndiye aliemgonga Dk.Makete?"


"Mzee Makete alizinduka kwa nukta chache alipokuwa thieta na kulitaja jina lake."
"Hawezi kuwa amekosea?"
"Hatujui. Lakini kwa vile hatuna fununu yoyote nyingine..."
"Ikoje hali ya babako, Denny?"
"Niliarifiwa amejeruhiwa vibaya. Lakini Dk.Beka anaamini hayuko katika hali ya kutisha." Alijibu Denny. "Huwezi kufanya chochote kile kuhusu mtu huyo?"


" Hatujui chochote kile zaidi ya kulijua jina lake na kuiona picha iliyomo humo, ambayo sidhani kama itatusaidia sana,ni ya zamani mno - tuko gizani kabisa."


"Mmmh, labda nianze toka mwanzo." Alisema Mzee Maliki, akiwaza. "Kama unavyofahamu, nchi hii ilipata uhuru mwaka 1960. Bwana Nelson Benjamin Nseloa akawa Rais wa kwanza. Watu wote walifurahi jinsi alivyopigani uhuru, wote tulimpenda Nselo.


"Lakini kadri miaka ilivyozidi kupita bila ya yeye kutimiza kile ambacho wananchi wengi walitamazamia angetenda, mapenzi yakaanza kupungua. Wananchi wengi walitazamia kuwa baada ya uhuru, Nselo angewafukuza wageni wote - wazungu na waasia na mali zao kugawiwa kwa wazawa. Yeye hakufanya hivyo. Kinyume chake, aliwatetea na kuwalinda. Kwa vile tangu mwanzo walikuwa ndio wafanyabiashara wakubwa na wenye kumiliki mashamba makubwa na mazuri, wakazidi kutajirika. Wananchi wakaishiwa furaha."


Mzee Maliki alitoa mtemba akaanza kuujaza tumbaku kabla hajauwasha na kuukoleza.
"Mkuu wa majeshi wakati huo, Meja Jenerali Ibrahim Mbelwa,akaamua kuutumia mwanya huo. Akaipindua serikali ya Nelson Benjamin Nselo,ambaye alikuwa ng'ambo, na kutwaa madaraka."


Baada ya kuuwasha mtemba kwa kutumia njiti tatu,akaendelea, "Hiyo bila shaka, ni historia mnayoifahamu vizuri. Inasikitishwa vile watu wanavyofurahishwa na kitendo cha Mbelwa, hasa alipowafukuza wageni na kugawa mali zao kwa wananchi. Lakini haukupita muda mrefu kabla ya hulka ya kweli ya Mbelwa kudhihirika. Kwa vile hakuwa na elimu, aliwachukia wasomi, kwa vile alikuwa Mwislam ,aliwachukia wakristo. Kwa vile alikuwa Mshongwe, aliwachukia watu wa makabila mengine,hasa kabila la Nelson Nselo. Si tu aliuteketeza uchumi wa nchi, bali aliteketeza watu karibu milioni. Kwa vile wakati huo tulikuwa miloni chache tu, idadi hiyo ilikuwa kubwa ya kutisha. Watu wakaanza kujuta."


Mtemba ulikuwa umezimika. Akauwasha tena kabla ya kuendelea. "Kwa sababu moja au nyingine, maelfu ya wananchi wakaihama nchi na kuomba hifadhi katika nchi jirani. Nelson Nselo akaweza kuwaunganisha na kuwapa mafunzo ya kijeshi. Wakati ulipowadia wakaingia nchini. Wakashinda kirahisi askari wa Ibrahim, ambao hawakuwa na moyo hata na moyo wa kupigana. Yeye mwenyewe aliuliwa wakati akijaribu kutoroka nchi. Risasi zangu zilikuwa miongoni mwa risasi zilizomtoa roho."


Kikapita kimya cha muda, Dennis akajikuta anamtazama Mzee Maliki kwa matazamo mpya. Mzee huyo akaendelea, "Sasa kuhusu Kassim Hashir. Yeye na Ibrahim walikuwa marafiki, licha ya kutokuwa rika moja. Akampa Kassim pasipoti ya kibalozi na kumtumia kutorosha mali. Katika kipindi cha utawala wa miaka mnne ya utawala wake, Kassim alitorosha mamilioni kwa mamilioni. Alikwenda Ulaya karibu kila wiki kupeleka pesa za kigeni na chochote kile ambacho kilikuwa mali. Kazi hiyo inasemekana aliimudu vizuri. Pia inasemekana alikuwa na kichwa cha biashara. Hakuyaacha mamiloni hayo yalale benki, aliyazalisha katika vitega uchumi mbalimbali.


"Alipoona mambo yanaanza kuharibika hapa nyumbani, akayeyuka. Kwanza alikimbilia Ulaya, baadaye akawa hatulii mahali pamoja. Akawa mfanyabiashara wa kimataifa. Bila ya shaka aliposikia Ibrahim amekufa aliinua mikono mbinguni. Hakuwa na mtu wa kumghasi na wala kugawana nae tena. Na kama ni kweli angali hai atakuwa tajiri mkubwa sana - tajiri wa kuweza kushindana na serikali yoyote ya nchi ya Kiafrika."


Bessy akashusha pumzi. "Sioni kitendo chake cha kurosha mali kinaweza kuhusiana na Dk.Makete."
"Hata mimi sioni." Alikubali Mzee Maliki. Dennis akauliza, "Kwa nini ulisema kesi yake ilikuwa dhaifu - hamkujali sana?"


"Mara tu baada ya Ibrahim kung'olewa, niliteuliwa kuongoza skwadi ya kuwasaka, kuwakamata na kuwapeleka mahakamani wote waliotenda makosa wakati wa utawala wa fasishisti huyo. Walikuwa wengi, zaidi ya elfu. Wengine walikuwa wamefanya makosa madogo tu, lakini wengi walikuwa wametenda unyama kweli kweli. Kwa wengine palikuwa na ushaidi, na kwa wengine hapakuwa na ushaidi wa kutosha. Ilikuwa kazi kubwa kupata majina yao na makosa yao kuwafungulia mafaili, kuwasaka, kuwakamata, kutafuta ushaidi na hatimae kuwapeleka mahakamani. Kadhaa tuliwanasa na walihukumiwa kunyongwa au kufungwa. Lakini wengi pia ilibidi waachiwe na makama kwa uhaba wa ushaidi."


" Wote tuliona Kassim angekuwa mmojawapo wa kuachiwa. Kwanza, kwa vile alikuwa na pesa, angeweka mawakili kabambe. Pili, hatukuwa na ushahidi madhubuti kumtia hatiani. Mashahidi tuliowapata ni maafisa wa forodha na uhamiaji, ambao walikiri kuwa hawakuwa wakimpekua Kassim aendapo ng'ambo kwa sababu ya pasi yake ya kibalozi, ingawa walishuku mizigo yake. Huo sio ushahidi kitu mahakamani. Walishindwa hata kusema kwa hakika ni vitu gani alivitorosha.


"Ushahidi mwingine ulikuwa wa minong'ono tu, wa watu waliokuwa wakimtafutia bidhaa,ambao hatimae akawadhulumu. Unadhani wangekubali kusimama mahakamani na kutoa ushaidi? Wao na wao walikuwa wanavunja sheria. Hata kama wangekubali ili kumkomoa Kassim,wakili yoyote yule angewachakaza vibaya sana."


"Bessy akauliza, "Kwa hiyo hakuna juhudi zozote zilizofanywa za kutaka akamatwe huko Ulaya na kumrudisha nyumbani?"
 

Idawa kweny ubora wake, shusha nyingine kaka
 
Vipi mkuu unao msako wa Mr x niya edd ganzel pia
Mkuu huo Msako wa Mr x mara ya mwisho nimeusoma kwenye jarida la Bongo, sidhani kama umewai kutolewa kitabu.
 
Cookies are required to use this site. You must accept them to continue using the site. Learn more…