Marilyn Monroe
Member
- Apr 2, 2020
- 80
- 167
MTUNZI; HUSSEIN TUWA
SEHEMU YA KWANZA.
Daily News, Julai 12 (Imetafsiriwa):
Jambazi hatari linalojishughulisha na biashara ya madawa ya kulevya huko Marekani ya Kusini limefanikiwa kwa mara nyingine tena kuwatoroka askari wa Kikosi Cha Kupambana na madawa ya kulevya cha Marekani (D.E.A) baada ya askari hao kuizingira kambi yake.
Habari za kuaminika zinaeleza kwamba jambazi hilo, Claudio Zapata, liliwatoroka askari hao baada ya mapambano makali ya kutupiana risasi kati ya kundi lake na wana usalama wa D.E.A. Katika mapambano hayo, askari kadhaa walijeruhiwa na wawili waliuawa. Wafuasi wengi wa jambazi hilo waliuawa na wachache waliokuwa wamejeruhiwa walitiwa mbaroni.
Kutokana na hali hiyo, msako mkali wa kimataifa umeanza dhidi ya jambazi hilo hatari ukiongozwa na askari wa D.E.A
wakishirikiana na wana usalama wa FBI ambapo habari zisizo za uhakika mpaka sasa, zinaeleza kuwa jambazi hilo hivi sasa limejificha ndani ya nchi za Afrika ya mashariki.
Balozi wa Marekani nchini Tanzania alikaririwa akisema kuwa panahitajika ushirikiano wa karibu sana baina ya Serikali ya nchi yake na nchi za Afrika ya Mashariki kwa ujumla kutokana na ukweli kwamba jambazi hilo linaweza kuwa ndani ya nchi yoyote miongoni mwa nchi za Afrika ya Mashariki . Chanzo chetu kingine cha habari kimedokeza kuwa tayari wana usalama wa FBI na D.E.A wameshaingia nchini Tanzania, kama jinsi walivyokwishaingia nchini Kenya, Uganda na hata kule Rwanda na Burundi katika harakati za kulisaka...
Disemba 15
Ndege kubwa ya Shirika la ndege la Uholanzi, KLM, ilitua kwa madaha kwenye uwanja wa ndege wa kimataifa wa Kilimanjaro (K I A) jijini Arusha. Ilikuwa ni saa nne za usiku, kiasi cha wiki mbili kabla ya sikukuu ya Noeli, na abiria wengi waliokuwa wakiteremka kutoka kwenye ndege ile walikuwa wamejawa bashasha zinazoambatana na maandalizi ya sikukuu ile mashuhuri.
Miongoni mwa abiria wale waliokuwa wakiteremka usiku ule alikuwamo Jaafar “Jeff” Bijhajha, mtu mmoja mrefu aliyejengeka kimichezo, hususan mchezo wa kikapu yaani basketball. Kwa mujibu wa hati zake za kusafiria, huyu jamaa alikuwa ni mwanafunzi wa shahada ya pili katika fani ya udaktari wa meno kutoka kwenye chuo kimoja cha kisichokuwa sana huko Uholanzi. Hati zake hizo pia zilibainisha kuwa mtu huyo alikuwa anaitwa Jaafar H. Bijhajha, mtanzania mzaliwa wa Machame huko Moshi, ingawa kabila lake lilikuwa ni Mfipa.
Iwapo angetokea mtu na kuamua kufuatilia ukweli wa maelezo haya, basi angegundua kuwa maelezo hayo yalikuwa ni kweli tupu kwa maana yalithibitishwa na vyeti vyote halali vinavyotambulika kitaifa.
Jamaa alikuwa amevaa suruali nzito aina ya Jinzi yenye rangi ya buluu na viatu vikubwa vya ngozi nyeusi vinavyofanana na vile vya wapanda milima huko Ulaya. Usoni alikuwa amevaa miwani ya kusomea iliyomletea ile taswira ya kitabibu haswa, na kichwani alikuwa amevaa kofia ya kepu au 'Kapelo' yenye lebo ya “Reebok”. Alikuwa amevaa shati zito la rangi ya buluu la mtindo wa drafti-drafti ambalo alikuwa amelichomekea vizuri sana ndani ya suruali yake. Begani alikuwa amening'iniza begi la wastani aina ya Ruksack.
Hakuwa na mzigo mwingine. Kutokana na kazi zake, mtu huyu mrefu alilazimika kutumia majina mbalimbali kwa nyakati tofauti kutegemea na kazi anayokabiliana nayo katika wakati husika, na kwa kazi hii iliyomleta hapa Tanzania safari hii (ambapo ukweli ndio nchi yake hasa aliyozaliwa), jina lake lilikuwa ni Jaafar Bijhajha, mwenyewe akipendelea zaidi kujitambulisha kama "Jeff Bijhajha".
Ingawa nia ya safari yake ilikuwa ni Dar es Salaam, mtu huyu mwenye ndevu zilizochongwa vizuri na kufanya umbo la herufi "O" kuuzunguka mdomo wake, alikata tiketi ya kuteremkia Kilimanjaro na ndivyo alivyofanya. Azma yake ilikuwa ni kusafiri kwa basi kutoka Kilimanjaro hadi Dar es Salaam siku iliyofuata.
Ukweli ni kwamba mtu huyu, ambaye kutokana na kazi yake ni nadra sana kutumia jina lake la halali alilopewa na wazazi wake kiasi cha miaka thelathini na minane hivi iliyopita, hakuwa mwanafunzi wala hakuwa akitokea Uholanzi masomoni.
Ingawa hati zake za kusafiria zilionyesha kuwa safari yake ilianzia Uholanzi, ukweli ni kwamba safari yake hii aliianzia Marekani, ambapo alisafiri kwa ndege ya kukodi akitumia jina tofauti na hati tofauti za kusafiria zilizobainisha kuwa alikuwa raia wa marekani mwenye asili ya kiafrika. Alisafiri mpaka Ukraine, ambako siku mbili baadaye, alipanda ndege nyingine hadi uswizi kwa zile zile hati zake za kimarekani. Huko akasafiri tena kwa treni akiwa kama Jeff Bijhajha, mwanafunzi kutoka Tanzania mpaka Uholanzi, ambako alifika mida ya saa mbili na nusu asubuhi, na saa nne na nusu asubuhi ile ile alipanda ile ndege ya KLM kuelekea Tanzania, mkoa wa Kilimanjaro.
Jeff Bijhajha alikuwa amekuja Tanzania kwa kazi maalum, na kama kawaida ya kazi zake zote, ambazo watu wanaomtuma huziita “Operesheni”, ilikuwa ni kazi ya hatari, mashaka na mikiki-mikiki isiyosemeka. Ilikuwa ni kazi ambayo uhakika wa kuikamilisha akiwa hai ni mdogo na matarajio ya kuimaliza akiwa kilema ni makubwa...
Kitabu Cha Kwanza:
JAKA
1
Ni usiku mnene. Kiza ni kizito. Mvua kubwa inanyesha.
Watu wamo vitandani mwao, wamelala. Wengine wakiichukulia mvua inyeshayo huko nje kama chachu ya kujumuika na wapenzi au wanandoa wenzao ndani ya nyumba au vyumba vyao. Wengine ndio hawana habari kabisa na yanayotokea, wala hawajui kama kuna mvua inanyesha huko nje. Wengine wanasikia kwa mbali tu kuwa mvua inanyesha huko nje, hawana haja ya kuacha usingizi wao.
Ni ndani ya jiji la Dar es Salaam.
Katika kiza hiki kinene na mvua hii kubwa, msichana mmoja yuko matatani. Amelowa mwili mzima kwa mvua na amechoka vibaya sana kutokana na mwendo sio tu mrefu bali pia wa mbio. Sauti imemkauka kwa kupiga kelele za kuomba msaada kwa watu, ambao kichwani mwake anajua kuwa wanamsikia, lakini cha ajabu ni kwamba hakuna hata mmoja anayetoka kwenda kumsaidia!
"Jamani nisaidieni mwenzenu nauawa jamani!" Anajitahidi kupiga tena kelele huku akiendelea kukimbia kwa taabu. Hata hivyo, kelele zake zile hazikusaidia lolote.
Na sasa sauti imemkauka, pumzi zimemjaa, na miguu imemlegea kwa kukimbia. Bila kujitambua anapiga mweleka mzito kwenye tope na maji ya mvua. Akiwa pale topeni anageuka kwa wahka kuangalia alipotokea.
Wabaya wake hawaonekani.
Sijui nao wamechoka na kuamua kumuachia?
Hapana.
Sauti zao zinasikika...vishindo vya miguu yao...wanakimbilia upande ule ule aliopo yeye.
Ni wanaume, hawa wabaya wake, na wana nguvu na nia mbaya sana dhidi yake. Wanapata wanne au watano hivi, mwanadada hakumbuki sawa sawa.
"Oi! Yulee...yule pale chini...! Tumempata mshenzi mkubwa...twende !" Mmoja wao anabwata.
"Aaah! Kaumia...! Katusumbua sana malaya huyu!" Mwingine anadakia kwa ghadhabu.
Msichana anainuka, lakini mwili wote unamuwia mzito.
Kimbia. Kimbia tu..! Utakufa ukiendelea kuzubaa hapo...! Watakuua hao!
Anaisikia sauti yake mwenyewe ikimshinikiza kichwani mwake.
Lakini nguvu za kukimbia zimekwisha. Hawezi tena kutetea maisha yake.
Wacha waje waniue tu sasa...hamna yeyote wa kunisaidia!
Bora ufe huku unajitetea kuliko kufa kibwege...jitahidi...kimbia!
Ile sauti yake inazidi kumsisitizia ndani ya kichwa chake.
Mbio!
Msichana anatimua tena mbio. Kwa taabu na kusuasua kwanza, halafu nguvu zinamrudia na anaongeza kasi. Miguno ya ghadhabu na vishindo vya mbio za wabaya wake vinazidi kurindima masikioni mwake kutokea nyuma yake.
Anaongeza kasi zaidi, huku akilia wazi wazi.
Kwa mbele yake anaona kona inayokata kuingia mtaa wa pili kutoka kwenye ule aliokuwako. Anaongeza kasi kuielekea ile kona. Kwa namna fulani anadhani akiifikia ile kona ataweza kuwapoteza wabaya wake. Lazima aifikie ile kona...lazima aifikie.
Nikiifikia tu ile kona tu nitawapoteza hawa jamaa...labda hawatanipata tena...!
Anajipa moyo.
Pumzi zimemwisha, kichwa kinagonga, miguu inagongana magotini...anataka kuanguka...kona bado iko mbali...
Lazima nifike kwenye kona...lazima niifikie...oh, Mungu wangu, lazima...
Anakata kona.
Anajikuta uso kwa uso na mtu mwingine!
Yowe linamtoka anapojipamia kwa kishindo kifuani kwa yule mtu. Nguvu zinamwishia kabisa! Miguu inamtepweta kutokea magotini na anaanguka chini kama gunia tupu lililoachiwa lisimame lenyewe.
Yule mtu anamdaka kabla hajafika chini. Naye amelowa chapachapa. Mgongoni amebeba begi dogo kama mtu anayesafiri.
Mkojo unampita mwanadada.
"Nisamehe kaka yangu...! Chukua chochote utakacho niachie uhai wangu tu tafadhali!" Analalamika na kuomboleza yule msichana hali akiwa ameshikiliwa mikononi mwa yule mtu ambaye amebaki akiwa amemshikilia huku amepigwa butwaa.
Jamaa hapati muda wa kumjibu lolote yule binti, kwani muda huo anawaona watu wengine wanne wakikunja ile kona na kusimama ghafla. Kisha hapo hapo wanajipanga kuwazunguka na kuwasogelea yeye na yule binti taratibu.
Jamaa anawatazama kwa kutoelewa kinachoendelea, bado akiwa amemshika yule msichana aliyekuwa akitetemeka kama bua la muanzi mikononi mwake. Bila ya kuwasemesha wale watu wanne wanawazingira yule jamaa na yule msichana, na jamaa anawatazama mmoja baada ya mwingine.
Mmoja, bonge la mtu, ana upara na madevu mengi mashavuni hadi kidevuni. Huyu amepiga suti ya kitambaa cha jinzi, yaani koti na suruali. Miguuni alikuwa amevaa viatu mithili ya vile vya jeshi na mkononi ameshika rungu refu na bila shaka, zito. Macho yake yanaonekana kung'aa kizani mithili ya yale ya paka anapokuwa kizani. Ni wazi kuwa huyu si mtu mwema. Alikuwa amesimama mbele yao, kiasi cha kama hatua tano hivi kutoka pale yule jamaa mwenye kibegi mgongoni alipokuwa amesimama na yule binti aliye matatani.
Kulia kwa yule jamaa mwenye kibegi mgongoni walisimama watu wengine wawili. Mmoja, kwa haraka tu, aliweza kumuona kuwa ni mdogo kuliko yule upara. Alikuwa amekata nywele zake zote za pembeni na kuachia kibwenzi tu, ambacho nacho hakikuchanwa. Juu alikuwa amevaa kizibao tu, na chini alikuwa amevaa suruali kama ya Upara ila miguuni alikuwa amevaa viatu vya raba.
Mkono wake wa kulia ulikuwa umening'iniza mnyororo mnene.
Yule mwingine alikuwa mikono mitupu, ila alikuwa na msuli mnene. Mikono yake mikubwa ilikuwa imetulia kiunoni pake, uzito wake ameuegemeza kwenye mguu wake wa kushoto ilhali mguu wake wa kulia akiwa ameutanguliza mbele kidogo kama mtu ambaye yuko tayari kushambulia. Alikuwa amevaa 'fulana mchinjo', au maarufu kama 'Singlet', nyeupe iliyomganda mwilini kutokana na kutota mvua. Suruali yake ilikuwa nyeusi au buluu, haikuwa rahisi kutofautisha.
"Oi! Kama unajali maisha yako bora umwachie 'uyo mwanamke!" Alisema kibabe mtu wa nne ambaye alikuwa kushoto kwa jamaa mwenye kibeki mgongoni. Huyu alikuwa ameshika kisu kikubwa kilichotoa mng'ao hafifu katika kiza kile cha usiku.
Lah!
Jamaa mwenye kibegi mgongoni akaanza kurudi nyuma taratibu huku akimweka mgongoni yule msichana, kwa namna ya kumweka mbali na wale watu wabaya. Huku akitetemeka na kubwabwaja vitu visivyoeleweka kwa urahisi, yule binti aling'ang'ania lile begi la 'mkombozi' wake kwa mgongoni, nae akirudi nyuma ili kuongeza umbali kati yao na watu wale.
"Jamani eeh...mie siwajui na nyie hamnijui. Ila ninachojua ni kuwa huyu msichana siwezi kuwaachia..." Jamaa alijibu kwa sauti ya kutetema.
"Unasemaje wewe !?" Kwa ukali Upara alimfokea, na hapo hapo akamvurumishia rungu lake kwa nguvu. Jamaa akabonyea na pigo likapita hewani na kufanya mvumo kama kwamba feni kubwa ilikuwa ikikata upepo, na hapo yowe kali lilisikika kutoka kwa yule muhuni aliyekuwa na kisu kwani lile rungu lilitua sawia kichwani kwake na kile kisu kikamtoka.
Wakati huo huo jamaa akarusha teke kali lililompata Upara kwenye sehemu zake za siri. Upara aliachia yowe kubwa kwa sauti yake mbaya huku akiinama akiwa amejishika sehemu zake za siri. Bila kupenda alipiga magoti matopeni, akigumia kwa maumivu.
Kwa pembe ya jicho lake jamaa aliona mmoja kati ya wale magangwe wawili waliokuwa kulia kwake akimjia mbio, nae akageuka ili amkabili huku akisikia sauti ya yule binti akipiga kelele kuomba msaada.
Jamaa alichelewa kama sekunde hivi katika kugeuka kwake, kwani alikutana na teke kali la uso kutoka kwa jamaa mwenye fulana mchinjo. Nyota zilimtawala usoni yule 'mkombozi' huku akipepesuka na kujigonga kwenye ukuta wa nyumba iliyokuwa pale karibu yao.
Pamoja na vishindo vyote walivyokuwa wanavitoa, bado hakuna hata mtu mmoja aliyetoka nyumbani kwake kuja kutoa msaada au kuchunguza kulikoni.
Mara hiyo yule mwenye mnyororo naye alituma pigo lake. Jamaa aliwahi kuyumba pembeni kidogo na sauti kali mithili ya mbinja ilipita sikioni mwake, mnyororo ukamkosa.
"AAAARRGHHH!" Aling'aka mwenye mnyororo kwa kuona pigo lake limepotea.
Wakati huo Upara akawa anajizoazoa kutoka pale kwenye tope alipokuwa amedondokea magoti. Jamaa akamuona na kumuwahi kwa teke lingine la nguvu sana lililotua katikait ya uso wake. Yowe jingine kubwa likamtoka Upara huku akienda tena chali matopeni, damu zikiruka kutoka puani kwake.
Jamaa hakumwona yule mtu mwenye misuli jinsi alivyomfikia, ila alishtukia akikandamizwa ngumi nzito sana ya tumbo iliyomlegeza miguu na kumtoa upepo wa ghafla kinywani, na kabla hajakaa sawa akabebeshwa ngumi nyingine nzito ya uso, ambayo ilimsukuma hadi ukutani huku akiachia kilio cha maumivu.
Jamaa alijikuta ameshikwa kwa nguvu kutokea nyuma na hakuweza kufurukuta hata kidogo kwani mikono yenye nguvu ilipenya makwapani mwake na kufanya kabali kali kwa nyuma ya shingo yake.
"Unajifanya bingwa sio?" Yule gangwe aliyekuwa na kisu hapo awali alimuuliza kwa hasira huku akijichua sehemu chini ya jicho lake la kulia kwa kiganja cha mkono wake.
Pale pale Upara alikurupuka kutoka pale chini alipokuwa akigaragara kwenye tope na kumshindilia konde zito la mbavu kwa hasira yule jamaa.
Jamaa aligumia kwa uchungu, na yule binti akaachia kilio sambamba na pigo lile kama kwamba amepigwa yeye.
HAYA MBATA ZISHAANZA, UNAJUA KITACHOENDELEA?
USIKOSE RIWAYA HII ITAKAYOKUPELEKA PUTA MANZO MWISHO, HAPO KESHO SAA TATU KAMILI ASUBUHI.