Riwaya: Mtuhumiwa

Riwaya: Mtuhumiwa

Joined
Apr 2, 2020
Posts
80
Reaction score
167
Image may contain: one or more people and text
RIWAYA; MTUHUMIWA
MTUNZI; HUSSEIN TUWA
SEHEMU YA KWANZA.

Daily News, Julai 12 (Imetafsiriwa):

Jambazi hatari linalojishughulisha na biashara ya madawa ya kulevya huko Marekani ya Kusini limefanikiwa kwa mara nyingine tena kuwatoroka askari wa Kikosi Cha Kupambana na madawa ya kulevya cha Marekani (D.E.A) baada ya askari hao kuizingira kambi yake.

Habari za kuaminika zinaeleza kwamba jambazi hilo, Claudio Zapata, liliwatoroka askari hao baada ya mapambano makali ya kutupiana risasi kati ya kundi lake na wana usalama wa D.E.A. Katika mapambano hayo, askari kadhaa walijeruhiwa na wawili waliuawa. Wafuasi wengi wa jambazi hilo waliuawa na wachache waliokuwa wamejeruhiwa walitiwa mbaroni.
Kutokana na hali hiyo, msako mkali wa kimataifa umeanza dhidi ya jambazi hilo hatari ukiongozwa na askari wa D.E.A

wakishirikiana na wana usalama wa FBI ambapo habari zisizo za uhakika mpaka sasa, zinaeleza kuwa jambazi hilo hivi sasa limejificha ndani ya nchi za Afrika ya mashariki.

Balozi wa Marekani nchini Tanzania alikaririwa akisema kuwa panahitajika ushirikiano wa karibu sana baina ya Serikali ya nchi yake na nchi za Afrika ya Mashariki kwa ujumla kutokana na ukweli kwamba jambazi hilo linaweza kuwa ndani ya nchi yoyote miongoni mwa nchi za Afrika ya Mashariki . Chanzo chetu kingine cha habari kimedokeza kuwa tayari wana usalama wa FBI na D.E.A wameshaingia nchini Tanzania, kama jinsi walivyokwishaingia nchini Kenya, Uganda na hata kule Rwanda na Burundi katika harakati za kulisaka...

Disemba 15

Ndege kubwa ya Shirika la ndege la Uholanzi, KLM, ilitua kwa madaha kwenye uwanja wa ndege wa kimataifa wa Kilimanjaro (K I A) jijini Arusha. Ilikuwa ni saa nne za usiku, kiasi cha wiki mbili kabla ya sikukuu ya Noeli, na abiria wengi waliokuwa wakiteremka kutoka kwenye ndege ile walikuwa wamejawa bashasha zinazoambatana na maandalizi ya sikukuu ile mashuhuri.

Miongoni mwa abiria wale waliokuwa wakiteremka usiku ule alikuwamo Jaafar “Jeff” Bijhajha, mtu mmoja mrefu aliyejengeka kimichezo, hususan mchezo wa kikapu yaani basketball. Kwa mujibu wa hati zake za kusafiria, huyu jamaa alikuwa ni mwanafunzi wa shahada ya pili katika fani ya udaktari wa meno kutoka kwenye chuo kimoja cha kisichokuwa sana huko Uholanzi. Hati zake hizo pia zilibainisha kuwa mtu huyo alikuwa anaitwa Jaafar H. Bijhajha, mtanzania mzaliwa wa Machame huko Moshi, ingawa kabila lake lilikuwa ni Mfipa.

Iwapo angetokea mtu na kuamua kufuatilia ukweli wa maelezo haya, basi angegundua kuwa maelezo hayo yalikuwa ni kweli tupu kwa maana yalithibitishwa na vyeti vyote halali vinavyotambulika kitaifa.

Jamaa alikuwa amevaa suruali nzito aina ya Jinzi yenye rangi ya buluu na viatu vikubwa vya ngozi nyeusi vinavyofanana na vile vya wapanda milima huko Ulaya. Usoni alikuwa amevaa miwani ya kusomea iliyomletea ile taswira ya kitabibu haswa, na kichwani alikuwa amevaa kofia ya kepu au 'Kapelo' yenye lebo ya “Reebok”. Alikuwa amevaa shati zito la rangi ya buluu la mtindo wa drafti-drafti ambalo alikuwa amelichomekea vizuri sana ndani ya suruali yake. Begani alikuwa amening'iniza begi la wastani aina ya Ruksack.

Hakuwa na mzigo mwingine. Kutokana na kazi zake, mtu huyu mrefu alilazimika kutumia majina mbalimbali kwa nyakati tofauti kutegemea na kazi anayokabiliana nayo katika wakati husika, na kwa kazi hii iliyomleta hapa Tanzania safari hii (ambapo ukweli ndio nchi yake hasa aliyozaliwa), jina lake lilikuwa ni Jaafar Bijhajha, mwenyewe akipendelea zaidi kujitambulisha kama "Jeff Bijhajha".

Ingawa nia ya safari yake ilikuwa ni Dar es Salaam, mtu huyu mwenye ndevu zilizochongwa vizuri na kufanya umbo la herufi "O" kuuzunguka mdomo wake, alikata tiketi ya kuteremkia Kilimanjaro na ndivyo alivyofanya. Azma yake ilikuwa ni kusafiri kwa basi kutoka Kilimanjaro hadi Dar es Salaam siku iliyofuata.

Ukweli ni kwamba mtu huyu, ambaye kutokana na kazi yake ni nadra sana kutumia jina lake la halali alilopewa na wazazi wake kiasi cha miaka thelathini na minane hivi iliyopita, hakuwa mwanafunzi wala hakuwa akitokea Uholanzi masomoni.
Ingawa hati zake za kusafiria zilionyesha kuwa safari yake ilianzia Uholanzi, ukweli ni kwamba safari yake hii aliianzia Marekani, ambapo alisafiri kwa ndege ya kukodi akitumia jina tofauti na hati tofauti za kusafiria zilizobainisha kuwa alikuwa raia wa marekani mwenye asili ya kiafrika. Alisafiri mpaka Ukraine, ambako siku mbili baadaye, alipanda ndege nyingine hadi uswizi kwa zile zile hati zake za kimarekani. Huko akasafiri tena kwa treni akiwa kama Jeff Bijhajha, mwanafunzi kutoka Tanzania mpaka Uholanzi, ambako alifika mida ya saa mbili na nusu asubuhi, na saa nne na nusu asubuhi ile ile alipanda ile ndege ya KLM kuelekea Tanzania, mkoa wa Kilimanjaro.

Jeff Bijhajha alikuwa amekuja Tanzania kwa kazi maalum, na kama kawaida ya kazi zake zote, ambazo watu wanaomtuma huziita “Operesheni”, ilikuwa ni kazi ya hatari, mashaka na mikiki-mikiki isiyosemeka. Ilikuwa ni kazi ambayo uhakika wa kuikamilisha akiwa hai ni mdogo na matarajio ya kuimaliza akiwa kilema ni makubwa...

Kitabu Cha Kwanza:

JAKA
1
Ni usiku mnene. Kiza ni kizito. Mvua kubwa inanyesha.
Watu wamo vitandani mwao, wamelala. Wengine wakiichukulia mvua inyeshayo huko nje kama chachu ya kujumuika na wapenzi au wanandoa wenzao ndani ya nyumba au vyumba vyao. Wengine ndio hawana habari kabisa na yanayotokea, wala hawajui kama kuna mvua inanyesha huko nje. Wengine wanasikia kwa mbali tu kuwa mvua inanyesha huko nje, hawana haja ya kuacha usingizi wao.

Ni ndani ya jiji la Dar es Salaam.
Katika kiza hiki kinene na mvua hii kubwa, msichana mmoja yuko matatani. Amelowa mwili mzima kwa mvua na amechoka vibaya sana kutokana na mwendo sio tu mrefu bali pia wa mbio. Sauti imemkauka kwa kupiga kelele za kuomba msaada kwa watu, ambao kichwani mwake anajua kuwa wanamsikia, lakini cha ajabu ni kwamba hakuna hata mmoja anayetoka kwenda kumsaidia!

"Jamani nisaidieni mwenzenu nauawa jamani!" Anajitahidi kupiga tena kelele huku akiendelea kukimbia kwa taabu. Hata hivyo, kelele zake zile hazikusaidia lolote.

Na sasa sauti imemkauka, pumzi zimemjaa, na miguu imemlegea kwa kukimbia. Bila kujitambua anapiga mweleka mzito kwenye tope na maji ya mvua. Akiwa pale topeni anageuka kwa wahka kuangalia alipotokea.
Wabaya wake hawaonekani.

Sijui nao wamechoka na kuamua kumuachia?
Hapana.
Sauti zao zinasikika...vishindo vya miguu yao...wanakimbilia upande ule ule aliopo yeye.
Ni wanaume, hawa wabaya wake, na wana nguvu na nia mbaya sana dhidi yake. Wanapata wanne au watano hivi, mwanadada hakumbuki sawa sawa.

"Oi! Yulee...yule pale chini...! Tumempata mshenzi mkubwa...twende !" Mmoja wao anabwata.
"Aaah! Kaumia...! Katusumbua sana malaya huyu!" Mwingine anadakia kwa ghadhabu.
Msichana anainuka, lakini mwili wote unamuwia mzito.

Kimbia. Kimbia tu..! Utakufa ukiendelea kuzubaa hapo...! Watakuua hao!
Anaisikia sauti yake mwenyewe ikimshinikiza kichwani mwake.

Lakini nguvu za kukimbia zimekwisha. Hawezi tena kutetea maisha yake.
Wacha waje waniue tu sasa...hamna yeyote wa kunisaidia!
Bora ufe huku unajitetea kuliko kufa kibwege...jitahidi...kimbia!
Ile sauti yake inazidi kumsisitizia ndani ya kichwa chake.
Mbio!

Msichana anatimua tena mbio. Kwa taabu na kusuasua kwanza, halafu nguvu zinamrudia na anaongeza kasi. Miguno ya ghadhabu na vishindo vya mbio za wabaya wake vinazidi kurindima masikioni mwake kutokea nyuma yake.
Anaongeza kasi zaidi, huku akilia wazi wazi.

Kwa mbele yake anaona kona inayokata kuingia mtaa wa pili kutoka kwenye ule aliokuwako. Anaongeza kasi kuielekea ile kona. Kwa namna fulani anadhani akiifikia ile kona ataweza kuwapoteza wabaya wake. Lazima aifikie ile kona...lazima aifikie.

Nikiifikia tu ile kona tu nitawapoteza hawa jamaa...labda hawatanipata tena...!
Anajipa moyo.

Pumzi zimemwisha, kichwa kinagonga, miguu inagongana magotini...anataka kuanguka...kona bado iko mbali...
Lazima nifike kwenye kona...lazima niifikie...oh, Mungu wangu, lazima...
Anakata kona.

Anajikuta uso kwa uso na mtu mwingine!
Yowe linamtoka anapojipamia kwa kishindo kifuani kwa yule mtu. Nguvu zinamwishia kabisa! Miguu inamtepweta kutokea magotini na anaanguka chini kama gunia tupu lililoachiwa lisimame lenyewe.

Yule mtu anamdaka kabla hajafika chini. Naye amelowa chapachapa. Mgongoni amebeba begi dogo kama mtu anayesafiri.

Mkojo unampita mwanadada.
"Nisamehe kaka yangu...! Chukua chochote utakacho niachie uhai wangu tu tafadhali!" Analalamika na kuomboleza yule msichana hali akiwa ameshikiliwa mikononi mwa yule mtu ambaye amebaki akiwa amemshikilia huku amepigwa butwaa.
Jamaa hapati muda wa kumjibu lolote yule binti, kwani muda huo anawaona watu wengine wanne wakikunja ile kona na kusimama ghafla. Kisha hapo hapo wanajipanga kuwazunguka na kuwasogelea yeye na yule binti taratibu.

Jamaa anawatazama kwa kutoelewa kinachoendelea, bado akiwa amemshika yule msichana aliyekuwa akitetemeka kama bua la muanzi mikononi mwake. Bila ya kuwasemesha wale watu wanne wanawazingira yule jamaa na yule msichana, na jamaa anawatazama mmoja baada ya mwingine.

Mmoja, bonge la mtu, ana upara na madevu mengi mashavuni hadi kidevuni. Huyu amepiga suti ya kitambaa cha jinzi, yaani koti na suruali. Miguuni alikuwa amevaa viatu mithili ya vile vya jeshi na mkononi ameshika rungu refu na bila shaka, zito. Macho yake yanaonekana kung'aa kizani mithili ya yale ya paka anapokuwa kizani. Ni wazi kuwa huyu si mtu mwema. Alikuwa amesimama mbele yao, kiasi cha kama hatua tano hivi kutoka pale yule jamaa mwenye kibegi mgongoni alipokuwa amesimama na yule binti aliye matatani.

Kulia kwa yule jamaa mwenye kibegi mgongoni walisimama watu wengine wawili. Mmoja, kwa haraka tu, aliweza kumuona kuwa ni mdogo kuliko yule upara. Alikuwa amekata nywele zake zote za pembeni na kuachia kibwenzi tu, ambacho nacho hakikuchanwa. Juu alikuwa amevaa kizibao tu, na chini alikuwa amevaa suruali kama ya Upara ila miguuni alikuwa amevaa viatu vya raba.

Mkono wake wa kulia ulikuwa umening'iniza mnyororo mnene.
Yule mwingine alikuwa mikono mitupu, ila alikuwa na msuli mnene. Mikono yake mikubwa ilikuwa imetulia kiunoni pake, uzito wake ameuegemeza kwenye mguu wake wa kushoto ilhali mguu wake wa kulia akiwa ameutanguliza mbele kidogo kama mtu ambaye yuko tayari kushambulia. Alikuwa amevaa 'fulana mchinjo', au maarufu kama 'Singlet', nyeupe iliyomganda mwilini kutokana na kutota mvua. Suruali yake ilikuwa nyeusi au buluu, haikuwa rahisi kutofautisha.
"Oi! Kama unajali maisha yako bora umwachie 'uyo mwanamke!" Alisema kibabe mtu wa nne ambaye alikuwa kushoto kwa jamaa mwenye kibeki mgongoni. Huyu alikuwa ameshika kisu kikubwa kilichotoa mng'ao hafifu katika kiza kile cha usiku.

Lah!
Jamaa mwenye kibegi mgongoni akaanza kurudi nyuma taratibu huku akimweka mgongoni yule msichana, kwa namna ya kumweka mbali na wale watu wabaya. Huku akitetemeka na kubwabwaja vitu visivyoeleweka kwa urahisi, yule binti aling'ang'ania lile begi la 'mkombozi' wake kwa mgongoni, nae akirudi nyuma ili kuongeza umbali kati yao na watu wale.
"Jamani eeh...mie siwajui na nyie hamnijui. Ila ninachojua ni kuwa huyu msichana siwezi kuwaachia..." Jamaa alijibu kwa sauti ya kutetema.

"Unasemaje wewe !?" Kwa ukali Upara alimfokea, na hapo hapo akamvurumishia rungu lake kwa nguvu. Jamaa akabonyea na pigo likapita hewani na kufanya mvumo kama kwamba feni kubwa ilikuwa ikikata upepo, na hapo yowe kali lilisikika kutoka kwa yule muhuni aliyekuwa na kisu kwani lile rungu lilitua sawia kichwani kwake na kile kisu kikamtoka.
Wakati huo huo jamaa akarusha teke kali lililompata Upara kwenye sehemu zake za siri. Upara aliachia yowe kubwa kwa sauti yake mbaya huku akiinama akiwa amejishika sehemu zake za siri. Bila kupenda alipiga magoti matopeni, akigumia kwa maumivu.

Kwa pembe ya jicho lake jamaa aliona mmoja kati ya wale magangwe wawili waliokuwa kulia kwake akimjia mbio, nae akageuka ili amkabili huku akisikia sauti ya yule binti akipiga kelele kuomba msaada.

Jamaa alichelewa kama sekunde hivi katika kugeuka kwake, kwani alikutana na teke kali la uso kutoka kwa jamaa mwenye fulana mchinjo. Nyota zilimtawala usoni yule 'mkombozi' huku akipepesuka na kujigonga kwenye ukuta wa nyumba iliyokuwa pale karibu yao.

Pamoja na vishindo vyote walivyokuwa wanavitoa, bado hakuna hata mtu mmoja aliyetoka nyumbani kwake kuja kutoa msaada au kuchunguza kulikoni.

Mara hiyo yule mwenye mnyororo naye alituma pigo lake. Jamaa aliwahi kuyumba pembeni kidogo na sauti kali mithili ya mbinja ilipita sikioni mwake, mnyororo ukamkosa.

"AAAARRGHHH!" Aling'aka mwenye mnyororo kwa kuona pigo lake limepotea.
Wakati huo Upara akawa anajizoazoa kutoka pale kwenye tope alipokuwa amedondokea magoti. Jamaa akamuona na kumuwahi kwa teke lingine la nguvu sana lililotua katikait ya uso wake. Yowe jingine kubwa likamtoka Upara huku akienda tena chali matopeni, damu zikiruka kutoka puani kwake.

Jamaa hakumwona yule mtu mwenye misuli jinsi alivyomfikia, ila alishtukia akikandamizwa ngumi nzito sana ya tumbo iliyomlegeza miguu na kumtoa upepo wa ghafla kinywani, na kabla hajakaa sawa akabebeshwa ngumi nyingine nzito ya uso, ambayo ilimsukuma hadi ukutani huku akiachia kilio cha maumivu.

Jamaa alijikuta ameshikwa kwa nguvu kutokea nyuma na hakuweza kufurukuta hata kidogo kwani mikono yenye nguvu ilipenya makwapani mwake na kufanya kabali kali kwa nyuma ya shingo yake.

"Unajifanya bingwa sio?" Yule gangwe aliyekuwa na kisu hapo awali alimuuliza kwa hasira huku akijichua sehemu chini ya jicho lake la kulia kwa kiganja cha mkono wake.

Pale pale Upara alikurupuka kutoka pale chini alipokuwa akigaragara kwenye tope na kumshindilia konde zito la mbavu kwa hasira yule jamaa.

Jamaa aligumia kwa uchungu, na yule binti akaachia kilio sambamba na pigo lile kama kwamba amepigwa yeye.

HAYA MBATA ZISHAANZA, UNAJUA KITACHOENDELEA?
USIKOSE RIWAYA HII ITAKAYOKUPELEKA PUTA MANZO MWISHO, HAPO KESHO SAA TATU KAMILI ASUBUHI.
 
SEHEMU YA PILI.

Jamaa alijikuta ameshikwa kwa nguvu kutokea nyuma na hakuweza kufurukuta hata kidogo kwani mikono yenye nguvu ilipenya makwapani mwake na kufanya kabali kali kwa nyuma ya shingo yake.

"Unajifanya bingwa sio?" Yule gangwe aliyekuwa na kisu hapo awali alimuuliza kwa hasira huku akijichua sehemu chini ya jicho lake la kulia kwa kiganja cha mkono wake.

Pale pale Upara alikurupuka kutoka pale chini alipokuwa akigaragara kwenye tope na kumshindilia konde zito la mbavu kwa hasira yule jamaa.

Jamaa aligumia kwa uchungu, na yule binti akaachia kilio sambamba na pigo lile kama kwamba amepigwa yeye.
"Mshenzi sana 'uyu!" Kama kwamba lile pigo lilikuwa halitoshi Upara aliongezea na tusi.

Jamaa alijikunja kwa maumivu huku akihisi nguvu zote zikimhama kama jinsi upepo unavyotoka kwenye puto lililotobolewa. Lakini mikono iliyokuwa imemshikilia ilikuwa imeshiba, hivyo akabaki ananing'inia tu.
"Jamani basi tusameheni..." Yule binti aliomboleza, na kuendelea, "...chukueni herini...bangili...pete...na hata nguo mkitaka mtuvue...maisha yetu tu mtuachie ndugu zetu!"

Jamaa alimgeukia yule binti, na hapo akaona kuwa na yeye pia alikuwa amedhibitiwa vilivyo na yule mtu aliyenyoa panki
"Ee jama ee...tufanye kweli tuishie jama...!" Mmoja wa wale watu wabaya alisema, na hapo Upara alianza kumvua pete za dhahabu yule binti kwa pupa, huku wale wenzake wakianza kulivua lile begi lililokuwa mgongoni kwa yule jamaa aliyeibuka ghafla kwenye uchochoro na kupamiana na yule binti aliyekuwa matatani. Lakini ghafla, kabla hawajafanikiwa kulitoa lile begi kutoka mabegani kwa yule jamaa, mwanga mkali uliwamulika wote pale.
"Mko chini ya ulinzi!" Sauti kali ya ki-askari ilisikika.
Si kizaa zaa hicho!

Wale waporaji wakawabwaga chini mateka wao na kuanza kutimua mbio. Lakini kule walipotaka kukimbilia nako mwanga mwingine mkali ukawamulika. Wakati huo huo yule jamaa aliyejitolea kumtetea yule msichana nae akatoka kasi sana kuelekea upande ambao kwake ulionekana kuwa ni salama. Lakini kabla naye hajafika popote alimulikwa na mwanga mkali usoni. Jamaa hakusimama. Alinyanyua mikono yake kuziba uso wake huku akiendelea kukimbia kuelekea kule kule mwanga ule ulipokuwa unatokea. Alichofanya ni kuikimbilia ngumi moja nzito ya uso, iliyompeleka chali kwenye tope.
Yule binti naye akatimua mbio kuelekea kwenye kona ya kutokea kwenye ule mtaa waliokuja nao, ambako ndiko mwanga wa mwanzo ulipotokea huku akipiga mayowe na kupayuka hovyo.

"Tusaidieni askari...tunauawa...watatuua! Heeeelllpp, for God’s Sake, jamaniii!"
"Tulia kama mlivyo! Tuna bunduki na tutavunja mguu mtu yeyote atakayejaribu kukimbia !" Sauti nyingine ya ki-askari ilifoka.

Wale majambazi wanne wakazingirwa mara moja na yule jamaa mwenye kibegi naye akaletwa na askari mwingine tayari akiwa ameshatiwa pingu. Askari wengine wawili walikuwa katika harakati za kuwatia pingu wale jamaa wanne, wakati askari mwingine alikuwa amemshikilia yule msichana kwa kumzungushia mkono wake mabegani kama ishara ya kumhakikishia usalama.

"Haya ndiyo tanayotu-distabu kira siku!" Mmoja wa wale askari alifoka kwa lafudhi ya ki-kurya huku akimtandika kofi kali la kisogo yule muhuni aliyenyoa panki.
Yule binti alishindwa kustahmili alipoona kuwa na yule jamaa aliyejitahidi kumsaidia naye ametiwa pingu kama wale wahuni.

"Afande huyu kaka sio mwenzao...tulikuwa wote katika balaa la hawa mabazazi...alikuwa akinisaidia huyo..."
"Waaacchaa! Mbona na renyewe ririkuwa rinajitahidi kuikimbia serikali, eenh?" Yule askari mwenye lafudhi ya ki-kurya alimkatisha yule binti kwa ukali.

"Kweli jamani...na yeye angeweza kuuawa na hawa jamaa..." Binti aliendelea kutetea.
"Hayo yote tutayajulia kituoni mama, sawa?" Aliingilia kati yule askari aliyemshika yule binti, ambaye ilionekama kuwa ndiye kiongozi wa doria ile.

Binti hakuwa na kauli zaidi.
Muda wote huo yule jamaa mwenye kibegi alikuwa kimya tu, uso wake akiwa ameuinamisha chini. Yule binti alimsogelea na kumshika bega kama ishara ya kumtoa hofu. Jamaa wala hakuonesha kama ameuhisi mkono wa yule binti begani kwake. Aliendelea kuinamisha uso wake huku akifuata ule msafara uliokuwa ukielekea kwenye Land Rover ya polisi iliyokuwa imepaki mwanzo wa ule mtaa.

Yeye na wale vibaka wanne pamoja na askari watatu waliingia nyuma ya ile gari iliyokuwa katika muundo wa “Pick-up”, ambako kulikuwa kumefunikwa kwa turubai. Yule askari aliyekuwa akiongoza ile doria akaingia sehemu ya mbele ya lile gari, yule binti akiwa katikati yake na dereva.

Safari ya kuelekea kituo cha polisi ikaanza.
Yule jamaa aliyejikuta matatani baada ya kujaribu kumsaidia yule binti aliyekuwa matatani aliendelea kuinamisha uso wake chini huku akiwa kimya.
Mvua iliendelea kunyesha kwa nguvu.
____________________
Walipelekwa kituo cha Polisi cha Oysterbay. Huko wale vibaka waliswekwa rumande bila ya kuulizwa lolote, na yule dada pampja na yule jamaa mwenye kibegi wakaingizwa kwenye ofisi nyingine ndani ya kituo kile na kuamriwa waketi kwenye benchi lililokuwa kwenye kona moja ya ofisi ile. Yule askari aliyekuwa akiongoza ile doria aliwaacha mle ndani pamoja na askari wenzake wawili, naye akatoka nje ya ofisi ile huku akivua koti lake la mvua.

Wale askari wawili waliobaki mle ofisini wakamtaka binti atoe maelezo ya kile kilichotokea kule mtaani, na ndipo binti alipoanza kutoa maelezo yake juu ya matata yaliyompata kutoka kwa wale watu wanne waliokuwa wakimfukuza katika usiku ule wa kiza kinene na mvua kubwa.

Alieleza kuwa yeye alikuwa ni msafiri aliyekuwa akitokea Dodoma kuja kumtembelea mjomba wake ambaye anaishi Mikocheni jijini Dar. Basi lao lilichelewa sana kufika Dar es Salaam kutokana na kuharibikiwa huko njiani kiasi kwamba hawakufika jijini hadi saa tano za usiku. Alichukua teksi kutoka pale stendi ya mkoa kuelekea huko Mikocheni.

"Sasa tulipofika pale Kinondoni Biafra nikaona dereva anasimamisha gari na kudai kuwa limeharibika. Kabla hata sijajua la kufanya, wale jamaa wanne wakavamia na wawili wakaingia kiti cha nyuma nilipokuwa nimekaa na wawili wakabaki nje, lakini mi’ niliwahi kuchomoka na kutoka nje. Wale wawili waliokuwa nje wakanikamata na kunipiga makofi, halafu wakanipora pochi langu na kulirushia mle mle ndani ya gari ambako bado begi langu la safari lilikuwamo. Ndani ya pochi kulikuwa na shilingi zangu elfu themanini, kadi zangu za benki na simu yangu ya mkononi...pamoja vitu vingne vidogo dogo na vijichenji-chenji...”

“Sasa huyu jamaa naye alikuwa wapi muda huo?” Mmoja wa wale askari alimuuliza, akimuoneshea yule jamaa mwenye kibegi.
“Ah, hapo huyu bado hajatokea! Sasa tukiwa pale nje ya gari wakaniamrisha nivue viatu na niwavulie vito vyangu vya dhahabu...nilijua kuwa hata nikiwapa kila kitu nilicho nacho, bado wangeniua tu...au wangenibaka. Ndipo nilipopata upenyo tu nikawachomoka na kuanza kukimbia huku nikiomba msaada bila mafanikio...Dah! Ama hakika Dar si mji wa kuishi. Yaani kelele zote nilizopiga hakuna hata mtu mmoja aliyesema aje kutoa msaada!"

"Sasa na huyu jamaa ulikutana naye vipi?" Yule askari alizidi kuhoji kuhusu yule jamaa mwenye kibegi.
Binti alimgeukia yule jamaa ambaye alikuwa amekaa kwenye benchi huku bado akiwa ameinamisha uso wake chini.
"Huyu kaka naye alikuwa na safari zake tu...tukapamiana pale kwenye kona...(hapo binti alitabasamu kidogo huku akimtazama yule jamaa aliyeendelea kuwa kimya huku akiwa amejiinamia) kwanza nilidhani ni mwenzao. Lakini hawa jamaa waliokuwa wakinikimbiza walipotukuta, wakaanza kututishia maisha sote. Hapo ndipo nikajua kuwa huyu kaka hakuwa upande wao...at least yeye alijitolea kunisaidia, na hapo ndipo ngumi zilipoanza kupigwa mpaka nyie mlipotokea." Binti alieleza kwa kirefu.

Baada ya hapo binti alitoa namba ya simu ya mjomba wake ambaye alimtaja kwa jina la Deogratius Salvatori, jina ambalo yule askari alionesha wazi kuwa si geni masikioni mwake.

Binti akaambiwa asubiri. Alishusha pumzi ndefu na kuketi pale kwenye benchi kando ya yule jamaa na kuanza kumtazama kwa makini zaidi.

Jamaa alikuwa na uso wa duara ambao ulikuwa na ndevu ndogo ndogo zilizochomoza kama jinsi zinavyokuwa kwa mtu ambaye amezoea kuzinyoa halafu akakaa siku kadhaa bila ya kufanya hivyo.

Kuna kitu kingine alichokiona kwa mtu yule ambacho hakuweza kukitambua mara moja...ilikuwa kama mvuto fulani hivi. Na jamaa alionekana kama...kama...msomi fulani hivi...yaani hakustahili kabisa kuwa pale...
Kuna kitu cha kushangaza kuhusu huyu mtu...
Alijiwazia.

Tangu wameingia kwenye mwanga wa mle kituoni yule jamaa hajamuangalia hata kidogo, jambo ambalo si la kawaida kumtokea pindi awapo karibu au akipita mbele ya wanaume. Na alipoulizwa jina lake na wale askari hakutaka kujibu. Askari walipotaka kupekua kibegi chake aliking'ang'ania mpaka walipokichukua kwa nguvu na kumchapa makofi.
Muda huo yule askari aliyekuwa kiongozi wa ile doria iliyowaokoa kutoka mikononi mwa wale wanyang’anyi alirudi mle ofisini akiwa amevua koti lake la mvua, hivyo cheo chake kilionekana kwenye mkono wa shati lake la polisi.
Alikuwa na cheo cha Sajenti.

Alimkazia macho yake madogo na makali yule jamaa, kisha taratibu akamsogelea na kusimama mbele yake. Taratibu yule jamaa akainua uso wake na kumtazama.

Kama angepigwa kofi, basi yule askari asingeruka kama alivyoruka kwa mshtuko baada ya kuiona sura ya yule jamaa.
"Wewe!" Aling'aka kwa sauti huku akimkodolea macho yule jamaa.

Jamaa aliendelea kumtazama tu bila ya kusema neno.
"Unafanya nini hapa wewe?" Alifoka kwa ghadhabu yule Sajenti.
Jamaa akazidi kumtazama tu bila ya kumjibu.

"Naongea na wewe ‘apo...ala! We' si unajua kuwa hutakiwi kuendelea kuwepo hapa mjini wewe...? Tena leo hii hii hukumu imepitishwa...ina maana umepinga hukumu ya mahakama wewe?" Aliendelea kubwata kwa hamaki yule Sajenti huku akiwa amemkazia macho yule jamaa, ambaye aliendelea kumkazia macho tu yule askari bila ya kujisumbua kujibu maswali yake.
Makubwa!
Binti akazidi kushangaa.
Mahakama?
Ina maana huyu mtu naye ni jambazi? Lakini mbona amenisaidia? Lakini...mbona haelekei kuwa anaweza kumdhuru mtu..?
"Naongea na wewe 'apo Jaka...nataka jibu!" Sajenti aliendelea kumsaili kwa hasira yule jamaa.
Jaka?

Ina maana huyu jamaa anaitwa Jaka...hadi polisi wanamjua!
Bila ya kukepua jamaa aliendelea kumuangalia yule askari bila ya kusema neno. Kwa hasira yule Sajenti alimrushia kofi la nguvu yule jamaa, na kwa wepesi usiotarajiwa mkono wa kushoto wa yule jamaa ulichomoka na kuudaka mkono wa yule askari kabla haujaufikia uso wake. Hapo hapo Sajenti akatuma kofi la mkono wa kushoto, nalo pia likadakwa na yule jamaa kwa mkono wake wa kulia huku akiwa amemkazia macho yake yule askari.

"Uuuww...Wwiii! Yaani rinaridaka mikono riserikari! Yaani rinarizuia riserikari risifanye kazi yake!" Alibwaka kwa mori yule askari mwenye lafudhi ya ki-kurya huku akimwendea kwa kasi yule jamaa aliyemkamata mikono yule Sajenti, na mara hiyo hiyo walitoka askari wengine wawili na kumvamia kwa nyuma yule jamaa.
Mateke, ngumi, virungu, mbata, ngwara!

Alimuradi mapigo kemkem yalimuangukia yule jamaa kama mvua.
"Basi...basi inatosha jamani, he!" Msichana aliropoka baada ya kuona kuwa wale askari walikuwa wanaendelea kumpa kipigo cha mbwa mwizi yule jamaa.

Jamaa akaanguka chini akiwa amejishika tumbo, huku amejikunja kwa uchungu, damu zikimtoka mdomoni.
"Wewe mama tulia 'apo! Usitufundishe kazi yetu ofisini kwetu saa hizi, umesikia we’? Tutakulaza ndani na wewe vilevile 'a'afu mjomba'ako aje kupiga kelele 'apa...au unabisha?" Mmoja wa wale askari alimjia juu yule msichana.
Binti naye akamjia juu.

"Kazi yenu? kazi yenu gani? Hii ndiyo kazi yenu hii? Kupiga watu hata wakiwa chini ya ulinzi, eeenh? Au hamjui maana ya human rights nyie? Na kama hamjui basi msidhani na sie hatuzijui bwana...tunazijua kiasi cha kutosha kutujulisha kuwa hii sio sahihi...hii sio sahihi kabbisa! Hii ni ukiukwaji mkubwa wa haki za binada..."
“Shut Up! ” Yule Sajenti alimkemea yule binti kwa ukali.

Binti akabaki amemkazia macho kwa hasira huku akihema kwa nguvu.
Jamaa alibaki akigaragara pale chini akiugulia kimya kimya.
Kama kwamba yule binti hakuingilia kati hata kidogo, yule Sajenti alimuinamia yule jamaa pale chini na kumbana taya zake kwa mkono wake wa kulia na kumgeuza uso wake ili watazamane.

"Tena una bahati sana wewe...maana ilikuwa unyongwe kabisa! Sasa bora usikie ushauri wangu...na sio watu wengi wanaopata bahati hiyo fala wewe...chukua virago vyako uondoke hapa mjini! Uondoke na usionekane tena! Umenisikia wewe?" Sajenti alimkoromea huku akiwa ameuma meno kwa hasira.
Eh! Kunyongwa tena? Huyu jamaa ni nani kwani?

Binti alizidisha idadi ya viulizo akilini mwake dhidi ya yule jamaa.
“Sasa we’ jitie kiburi halafu uone jinsi kitanzi kinavyounyofoa uhai wako mbovu kutoka mwilini mwako, bwege wewe!” Sajenti alimalizia kumkoromea yule jamaa, kisha akausukuma chini kwa nguvu uso wa yule jamaa na kumpigiza sakafuni kisogo chake. Maumivu makali yalimpata kichwani kwani jamaa alifumba macho kwa uchungu na akashika kichwa chake kwa mikono yake yote miwili, akigaragara huku akiinua juu magoti yake akiwa amelalia mgongo pale sakafuni.
 
SEHEMU YA TATU

Eh! Kunyongwa tena? Huyu jamaa ni nani kwani?
Binti alizidisha idadi ya viulizo akilini mwake dhidi ya yule jamaa.

“Sasa we’ jitie kiburi halafu uone jinsi kitanzi kinavyounyofoa uhai wako mbovu kutoka mwilini mwako, bwege wewe!” Sajenti alimalizia kumkoromea yule jamaa, kisha akausukuma chini kwa nguvu uso wa yule jamaa na kumpigiza sakafuni kisogo chake. Maumivu makali yalimpata kichwani kwani jamaa alifumba macho kwa uchungu na akashika kichwa chake kwa mikono yake yote miwili, akigaragara huku akiinua juu magoti yake akiwa amelalia mgongo pale sakafuni.
"Ai jamaani...Looh!" Alisikitika kwa simanzi yule msichana.
"Koplo!" Sajenti aliita kwa sauti.
"Afande!"

"Piga simu kwa huyo mjomba’ake aje amchukue huyu mgeni wake hapa...upesi!"
"Yes, Sir!"
Kisha yule Sajenti alimgeukia tena yule jamaa, ambaye sasa alikuwa amekaa chini huku ameegemea ukuta akikohoa huku akitikisa kichwa kwa uchungu na masikitiko. Alimwinamia pale chini na kumtomasa kwa nguvu kifuani kwa kidole chake cha shahada.

"Nakupa nafasi ya mwisho bwana mdogo. Sasa ni saa sita na nusu usiku. Nitakulaza hapa kituoni. Asubuhi nakupatia escort ya kuhakikisha kuwa unatoka nje ya mkoa huu...sasa ole wako urudi tena...utajuta kuzaliwa!"
Baada ya hapo jamaa alibebwa juu juu na kutupwa kwenye chumba cha mahabusu.

Yule binti alibaki akitazama hali ile kwa huzuni kubwa. Alitamani amwambie neno lolote la kumliwaza yule jamaa lakini hakulipata neno wala nafasi ya kufanya hivyo.

Muda wote wakati haya yanatokea, yule jamaa wala hakuwa na habari na yeye. Ni kama kwamba yule binti hakuwepo kabisa katika eneo lile.
2
Jaka ndilo jina la yule jamaa.
Jaka Brown Madega ndio jina lake kamili.
Jioni hii alikuwa amejiinamia nje ya nyumba moja ndogo iliyojengwa kwa tope na kuezekwa kwa bati kama jinsi nyumba nyingi nyingine katika eneo lile zilivyokuwa. Kwa mbali aliweza kusikia muziki wa zamani wa kikongo kutoka kwenye moja kati ya vilabu vingi vya pombe za kienyeji vilivyotawala eneo lile.

Nyumba aliyokuwa amekaa yeye ilikuwa ni ya vyumba viwili na sebule ndogo iliyotawaliwa na vigoda vya kigogo na majamvi. Jiko lilikuwa nyuma ya nyumba hiyo ambako pia ndipo kilipokuwa choo cha shimo, mlango wake ukiwa ni kipande cha gunia. Bafu lilikuwa kando ya choo. Kuta nne ambazo juu hazikuezekwa kitu chochote na uwazi ulioachwa kwenye moja ya kuta zile nne kuwa kama mlango ukiwa umefunikwa kwa kipande cha gunia kwa ajili ya ile faragha ya kibinaadamu pindi muogaji atakapohitaji faragha.

Mbele ya nyumba ile kulijengwa ukuta mdogo wa kozi zipatazo nne hivi kwa kutumia vipande vya matofali ya kuchoma. Ukuta huu ulitokea kwenye kona ya kulia ya nyumba ile na kwenda mbele kama hatua kumi na tano hivi za mtu mzima, kisha ukarudi kuelekea kushoto na kuacha uwazi mdogo usawa wa mlango wa mbele wa nyumba ile, halafu ukaendelea na kukutana na ukuta mwingine uliotokea kona ya kushoto ya nyumba ile.

Ni juu ya ukuta uliotokea kona ya kushoto ya nyumba hii ambapo huyu mtu aitwaye Jaka Brown Madega alikuwa amejiinamia, mgongo wake akiwa ameuegemeza kwenye ukuta wa sebule ya nyumba ile, miguu yake akiwa ameikunja kwa mbele, paji lake la uso akiwa ameliegemeza juu ya magoti yake hali akiwa amekumbatia miguu yake kwa kuzungusha mikono yake chini kidogo ya magoti yake. Alionekana kuwa ni mwenye mawazo mazito.

Ni siku nne sasa zimepita tangu alipopambana na ule mkasa uliotokea katika usiku wa mvua nzito ndani ya jiji la Dar es Salaam.

Baada ya kulala pale kituoni usiku ule, asubuhi na mapema kabla hata mkuu wa kituo kile hajaingia, yule Sajenti aliyekuwa akiongoza ile doria iliyomkumba usiku ule, ambaye Jaka alimjua kama Sajenti John Vata, alimtoa mahabusu na kumpakia ndani ya ile ile Land Rover iliyowabeba usiku uliopita na kuelekea naye mjini. Safari hii aliyekaa katikati ya Sajenti John Vata na dereva alikuwa ni Jaka. Nyuma ya ile Land Rover alikuwako Koplo mmoja mnene mwenye sura ya kibwege sana ambaye alikuwa na bunduki aina ya SMG aliyoipakata mapajani mwake.

"S'jui kwa ni' n'sikurudishe tena mahakani na kukufungulia shitaka la kukiuka amri ya mahakama wewe!" Alisema Sajenti Vata huku akimtupia Jaka jicho la pembeni.

Jaka hakumjibu kitu. Alibaki kimya tu, akitazama mbele wakati safari ikiendelea.
"Utakwenda mpaka Dodoma na utaripoti kwa Kamanda wa Polisi wa mkoa, yaani RPC, ukiwa na barua yako kutoka mahakamani, sawa?"
Kimya.

Bila kujali kwamba Jaka hakujibu kitu, Vata aliendelea, "Koplo Aporinari atakwenda na wewe mpaka Dodoma na kukukabidhi kwa RPC, kisha yeye atakuja kuripoti huku...hiyo ndio maana ya escort, tumeelewana?"
Kimya.

"Na utatakiwa uripoti kwa RPC kila siku asubuhi na jioni kwa siku zako zote unazotakiwa kuwa huko, najua hilo ulishaelezwa zamani tu, labda utake kuleta tena huo upumbavu wako!"
Hakutarajia jibu lolote kutoka kwa Jaka, ambaye aliendelea kutazama mbele tu bila kujibu lolote. Bila kujali yule Sajenti aligeuka kule nyuma alipokuwa yule Koplo na kupitia kwenye kidirisha kidogo kilichokuwa baina ya upande wa dereva na ule wa nyuma ya gari ile aliita, "Aporinari! "

"Afande!" Aliitikia yule Koplo kule nyuma.
"Amri uliyopewa inasemaje iwapo huyu mfungwa atajaribu kutoroka?"
"Kupiga risasi ya mguu kwanza, halafu kuuliza maswali baadaye afande!" Alibwaka yule Koplo kutokea kule nyuma, isipokuwa tu ile 'risasi' aliitamka kama “rithathi”, na 'maswali' ilisikika kama “mathwali”.
"Nzuri! Endelea Koplo!"

"Yes Sir!"
Ilisikika kama “Yeth-Tthaa.”
Jaka alibaki kimya tu na safari ikaendelea.
Jaka na yule Koplo wakapakiwa kwenye basi la Shabiby lililoondoka saa moja kamili asubuhi ile kuelekea Dodoma. Kwa vile hawakutoa nauli, iliamriwa Jaka asimame na yule askari akapatiwa kiti karibu sana na aliposimamishwa Jaka, SMG yake mkononi. Macho yaliwatoka pima abiria waliokuwa ndani ya basi lile kwani halikuwa jambo la kawaida kuona askari akisafiri na silaha wazi mkononi kwenye basi la abiria.

Kabla basi halijaondoka ndipo Jaka alipofungua kinywa chake. Alimshika mkono Sajenti Vata kwa nguvu na kumwambia, "Sajenti...tafadhali sana naomba ukamwambie mama yangu kuwa niko salama...tafadhali sana Sajenti!"
"Oke, Oke...nitamwambia. Lakini na wewe usifanye tena upuuzi kama huu huko. Miaka mitano sio mingi sana, Okay?"
"Oke...Sir!" Alijibu Jaka akiwa amemkazia macho ya ghadhabu yule Sajenti huku akimtemea lile neno “sir” kwa kejeli na ghadhabu.
_________________

Miaka mitano!
Alikuwa akiwaza Jaka.
Miaka mitano akae mbali na mji aliozaliwa na kukulia! Mji ambao alitegemea kuanzia maisha mara baada ya kumaliza masomo yake! Sasa ndoto zake zote hizo zilikuwa zimekatika...hakuna tena mategemeo ya kurudi na kuishi kama alivyozoea na alivyotarajia.
Roho ilimuuma sana.

Kwa nini dunia inamfanyia hivi? Si bora angekufa tu?
Lakini haiwezekani...siwezi kufa na kumuacha mama yangu mpenzi peke yake.
Alijirekebisha mawazoni akiwa amejikunja pale juu ya ule ukuta mfupi wa matofali ya kuchoma, muziki wa kizamani wa kikongo ukiendelea kusikika kwa mbali kutokea pale alipokuwa.

Lakini hata sasa, Jaka aliendelea kuwaza, mimi ni sawa na mfu tu...
“Ah! Mimi sina makosa. Sijafanya hilo kosa ambalo Mheshimiwa Jaji, pamoja na madigrii yake yote, na busara zake zote, ameona kuwa nimelifanya kiasi cha kustahili adha hii. Cha ajabu ni kwamba watu wazima na shahada za vyuo vikuu mbalimbali wameshindwa kuelewa kuwa mimi sikufanya kosa lile na kwamba nimesingiziwa tu...!” Sasa alijisemea peke yake kwa sauti.

Laiti ningekuwa na pesa za kutosha ningetafuta wakili mwingine wa binafsi nikakata rufaa..
“Sajenti Vata anasema eti ingefaa ninyongwe kabisa! Bora wangeninyonga basi kuliko kunipa hii adhabu ya kifungo cha nje kama wenyewe walivyoiita (alisonya kwa sauti). Eti nisionekane katika mkoa wa Dar es Salaam kwa muda wa miaka mitano! Na katika miaka mitano hiyo nisipatikane na kosa jingine lolote, vinginevyo adhabu itakuwa kali zaidi na eti huenda ikawa hata kifungo cha maisha! (akasonya).” Alijiogelesha kwa sauti.

Hata mama yangu siruhusiwi kuonana naye isipopkuwa kwa barua tu...kibaya zaidi ni kwamba barua zangu zote lazima zipitie kwa RPC wa hapa Dodoma...naye ana wajibu wa kuzifungua, kuzisoma, na akiona zina mashaka naweza nisizipate kabisa! Maisha gani haya....
Alizidi kuwaza kwa simanzi.

Na kama kweli hao wanasheria waliokabidhiwa hili jukumu la kuhakikisha kuwa haki inatendeka katika jamii walijihakikishia kuwa kweli mimi nimefanya hivyo nilivyotuhumiwa kuwa nimefanya, kwa nini basi wasinipe hizo adhabu wanazosema kuwa ningestahili? Kwa nini wasininyonge moja kwa moja au wasinihukumu hicho kifungo cha maisha? Wanaishia kunipa eti kifungo cha nje ya jiji la Dar kwa miaka mitano! (akawatukania mama zao, akasonya).
Akapiga kimya kingine mawazoni.

“Mnhu! Hapa kuna namna tu...si bure. Laiti wangeamua kunisikiliza na kuyafanyia uchunguzi mambo niliyokuwa nikijaribu kuwaeleza!” Alijisemesha kwa sauti. Yaani kama kuna mtu ambaye angekuwa anamfuatilia wakati ule, hakika angeamini kuwa jamaa alikuwa kwenye hatua za mwanzo za kuingiwa wazimu.

Sasa alikunja uso kwa kuvuta lindi jipya la mawazo, akiinua uso wake juu na kuegemeza kisogo chake ukutani, akinyoosha mguu mmoja pale juu ya ukuta, hali mwingine akibaki kuwa ameukunja kama hapo mwanzo.
Lakini...nahisi kuna kitu fulani ambacho kingeweza kunitoa kwenye janga hili bwana...! Kuna ushahidi fulani hivi...sijui nini...Akh! Tatizo ni kwamba toka misukosuko hii ilipoanza sijapata muda wa kukaa nikafikiri lolote kwa kituo...ilikuwa ni vurumai moja baada ya nyingine. Lakini kwa kweli kuna kitu fulani...kipo tu!

Kwa mbali akilini mwake Jaka alianza kuwa na mashaka iwapo akili yake itaweza kufanya kazi tena kama zamani.
"He! Anko! Mbona umejiinamia hivyo!"

Jaka alishtuka kutoka kwenye mawazo pale juu ya ukuta wa nyumba aliyofikia. Akageuza uso wake kumtazama mtu aliyemsemesha na mara ile ile akatabasamu na macho yake yakatoa nuru yake ya uhai.

"Ah! Anko Mnyaga umerudi..." Jaka alisema huku akitabasamu kwa huzuni kama kwamba hakutaka mtu yeyote amsumbue kutoka kwenye mawazo yake, halafu kama kumfanya yule mtu aliyemwita Anko Mnyaga asiendelee kumuuliza maswali zaidi akaongezea, "Sijajiinamia Anko...eem..nilikuwa napunga upepo tu hapa, kumbe nikaanza kupitiwa na usingizi." Hapo hapo akajua kuwa uongo wake haukufanikiwa.

Yule mtu aliyeitwa Mnyaga alimuangalia kwa sekunde kadhaa, kisha bila ya kusema neno akaondoka kuelekea ndani ya nyumba ile. Mkononi, kama kawaida yake, alikuwa amebeba kapu lake la kuendea "kibaruani" kama mwenyewe alivyozoea kusema.

Jaka alimtazama yule mzee mwenye umri upatao miaka arobaini na minane hivi na ambaye bado alionekana imara na mwenye nguvu, akipotelea ndani ya nyumba ile ya matope.
Alimpenda sana yule mzee...tangu utotoni mwake.
______________________

Jaka hakuwa na ndugu yeyote jijini Dodoma wala mkoa mwingine wowote nchini Tanzania. Ndugu yake hapa duniani alikuwa ni mama yake mzazi tu, ambaye wakati ule alikuwa jijini Dar es Salaam ambako ndiko Jaka alipozaliwa na kukulia.
Baba yake Jaka alifariki zamani sana wakati yeye akiwa bado tumboni mwa mama yake. Mama yake alimwambia kuwa baba yake alikuwa mwanajeshi na alifariki akiwa vitani. Aliwahi kuziona picha za marehemu baba yake akiwa katika mavazi yake ya kijeshi, na akakiri kuwa hakika alifanana sana na baba yake.

Ni wakati huo miaka kadhaa iliyopita wakati Jaka akiwa bado mdogo sana, ndipo mzee Mnyaga, wakati huo akiwa kijana tu, alipoletwa nyumbani kwao huko Lugalo kama msaidizi wa nyumbani. Na kutokea wakati huo Mnyaga akawa mlezi wa Jaka. Mama yake Jaka akienda kazini, mtoto Jaka alibaki nyumbani na Mnyaga. Hata alipoanza shule ya watoto wadogo Mnyaga ndiye aliyekuwa akimpeleka na kumfuata shuleni kila siku ili kumpa mama Jaka muda mzuri wa kuwahi kazini na kufanya mambo mengine ya kikazi bila mtoto Jaka kuwa kipingamizi.

Hali hii ilimfanya mtoto Jaka kumzoea zaidi Mnyaga kuliko hata mama yake, hali ambayo iliendelea mpaka Jaka alipotimiza umri wa miaka saba na kupelekwa kuanza darasa la kwanza katika shule ya Mnazi Mmoja jijini Dar es Salaam, ambako pia ilibidi awe anapelekwa na kufuatwa na Mnyaga. Wakati huu Jaka alikuwa tayari ameshaanza kumwita Mnyaga “Anko Mnyaga”.

Mnyaga aliishi na Jaka pamoja na mama yake kwa utii na uelewano mzuri mno, kwa muda mrefu sana. Hata alipoamua kuacha kazi na kurudi kwao Dodoma, Jaka alikuwa na umri wa miaka ishirini kamili. Lakini huo haukuwa mwisho wa umoja wao. Muda wote ambao Mnyaga alikuwa mbali nao, waliendelea kuwasiliana kwa njia mbali mbali za mawasiliano.

Mara kadhaa baada ya mama Jaka kustaafu kazi serikalini na kuanza kujishughulisha na biashara, alikuwa akisafiri kuelekea mikoa ya Mwanza na Shinyanga katika biashara zake kwa basi au treni, Mnyaga alijitahidi sana kufika Stesheni ya treni au kituo cha mabasi pale Dodoma ili kumsalimia na kumpa zawadi ndogo ndogo.
Kwa hiyo walikuwa kama ndugu.

Kutokana na hali hii basi, wakati Jaka alipolazimika kuuhama mji wa Dar es Salaam, mama yake kwa uchungu mwingi alimwambia aende Dodoma na akafikie kwa Anko wake Mnyaga ambaye alikuwa anafanya biashara ya kuuza matunda katika soko kuu la Dodoma. Baada ya kufika Dodoma Jaka hakupata taabu kumpata Mnyaga kwani tayari mawasiliano ya simu yalishafanyika tangu awali. Mnyaga alisikitishwa kwa Jaka kufika pale Dodoma katika mazingira yale. Baada ya Jaka kumueleza yaliyomsibu, akioanisha na maelezo aliyokwishapewa na mama Jaka hapo awali kwa njia ya simu, Mnyaga alisikitika maradufu na machozi yakamtoka kwa uchungu. Ndipo alipomkaribisha Jaka hapo kibandani kwake, katika eneo la Makole pale Dodoma mjini.

ITAENDELEA
 
SEHEMU YA NNE

Kutokana na hali hii basi, wakati Jaka alipolazimika kuuhama mji wa Dar es Salaam, mama yake kwa uchungu mwingi alimwambia aende Dodoma na akafikie kwa Anko wake Mnyaga ambaye alikuwa anafanya biashara ya kuuza matunda katika soko kuu la Dodoma. Baada ya kufika Dodoma Jaka hakupata taabu kumpata Mnyaga kwani tayari mawasiliano ya simu yalishafanyika tangu awali. Mnyaga alisikitishwa kwa Jaka kufika pale Dodoma katika mazingira yale. Baada ya Jaka kumueleza yaliyomsibu, akioanisha na maelezo aliyokwishapewa na mama Jaka hapo awali kwa njia ya simu, Mnyaga alisikitika maradufu na machozi yakamtoka kwa uchungu. Ndipo alipomkaribisha Jaka hapo kibandani kwake, katika eneo la Makole pale Dodoma mjini.
Alimuomba asijisikie mnyonge bali ajisikie kuwa yuko nyumbani na asiwe na wasiwasi kabisa kumfahamisha pindi atakapokuwa na tatizo lolote pale Dodoma kwani yeye sasa ni sawa na mzazi wake.
Jaka alimshukuru sana yule mzee na leo ndio siku ya nne tangu akaribishwe pale nyumbani kwa Mnyaga.
"Jaka...mbona hukula kile chakula nilichokuwekea pale mezani mwanangu?" Mnyaga alitoka ndani na kumuuliza. Safari hii Jaka alikuwa amesimama akiangalia barabarani huku mikono yake akiwa ameizamisha ndani ya mifuko ya suruali yake, na mabega yake akiwa ameyainua juu kwa kujikunyata kutokana na baridi kali la pale Dodoma.:
"Sijisikii kula kabisa leo Anko." Jaka alimjibu bila kugeuka, jibu ambalo lilikuwa ni kweli tupu.
"Na lini unategemea kujisikia kula?" Mnyaga alimuuliza huku akimkazia macho kwa ukali. Tangu amefika Jaka amekuwa akikataa kula kwa sababu mbali mbali naye amekuwa akimlazimisha na kumbembeleza ili ale.
"Labda nitakula jioni..."
"Jioni si ndio hii...kuna jioni gani tena?"
"Nilikuwa namaanisha baadae kidogo, Anko."
"Sikiliza Jaka...kula kwako ni muhimu sana hivi sasa. Wewe una mawazo mengi ambayo yanakula sana mwili wako...usipokula chakula utazidi kuihatarisha afya yako na mwisho wake utakufa..."
"Potelea mbali hata nikifa! Kwani kuna tofauti gani tena sasa?" Jaka alidakia kwa sautti ya ukali. Mnyaga hakubabaika. Alimjibu kwa upole huku akimtazama usoni kwa macho makali.
"Sidhani kama mama yako amekuagiza uje huku ili ufe, Jaka."
"Wewe Anko kwako ni rahisi kusema hivyo kwa sababu hayajakukuta yaliyonikuta mimi..."
"Mimi yamenikuta kama jinsi ambavyo mama yako anavyoona yamemkuta...matatizo yako Jaka, ni yetu sote! Cha kufanya ni kusaidiana kuyakabili matatizo haya na sio kuongezeana mengine juu yake!"
Jaka hakuweza tena kuendelea kumjibu yule mzee, kwani alimheshimu sana.
"Samahani Anko...nilikuwa sijui nasema nini..."
"Naelewa Jaka. Huu ni wakati mgumu sana kwako...ila inabidi ukabiliane na hali hii kiume. Unakumbuka nilikwambia nini wakati ule bado uko mdogo? Siku uliporudi shuleni unalia njia nzima baada ya kupigwa na mwenzako?"
Jaka alimtazama yule mzee kwa muda bila ya kusema neno, kisha uso wake ukachanua kwa tabasamu pana.
"Hah! Yaani Anko bado unakumbuka mambo hayo?" Alimuuliza, halafu akacheka sana kwa sauti na Mnyaga nae akacheka huku akimshika mkono na kumuongoza ndani.
"Twende tukale bwana." Alimwambia, na bila kupinga Jaka akaelekea ndani huku akiwa ameshikana mikono na Mnyaga. Kichwani mwake alikuwa akiyafikiria yale maneno aliyokumbushwa na Mnyaga. Zamani sana Mnyaga alimwambia maneno yale, lakini leo aliona ni kama jana tu wakati Mnyaga alipokuwa akimwambia maneno hayo...
Mwanaume kamwe hakabiliani na adui yake kwa machozi, bali hukabiliana naye kwa ngumi na hupigana mpaka mikono yake itumbukie mwilini mwa adui yake...na hapo mwanaume huanza kutumia miguu...
Jaka alikumbuka kuwa siku iliyofuata baada ya kuambiwa maneno yale na Mnyaga, alimtafuta yule mtoto aliyempiga na kumtaka wapigane. Mwisho pambano yule mtoto aliondoka analia akiwa na nundu kubwa kichwani huku akiacha meno mawili kwenye uwanja wa pambano. Jaka alirudi nyumbani akiwa mshindi.

3
Wiki mbili zilikuwa zimeshapita tangu awasili pale Dodoma, na amekuwa akienda kuripoti kituo cha polisi kila asubuhi na kila jioni bila kukosa, ikiwa ni sehemu ya masharti ya kifungo chake kile cha miaka mitano nje ya jiji la Dar. Siku zote anapokwenda kuripoti humkuta askari mmoja mwenye nguo za kiraia katika chumba maalum alichoelekezwa kuwa ndio awe anaenda kuripoti.
Jioni hii alipoenda kuripoti amemkuta askari mwingine kabisa. Huyu alikuwa amevaa mavazi ya kiaskari, na si ya kiraia, ambayo kwa kweli yalikuwa yamemkaa vyema. Mabegani mwake alikuwa ana nyota mbili na hivyo Jaka alihisi kuwa alikuwa ni Luteni, ingawa hakuwa na uhakika. Kwa muda alibaki akimtazama yule askari bila ya kusema lolote.
Sura ya huyu bwana haikumvutia Jaka hata kidogo, kwani alionekana kuwa ni mtu mpenda shari na mkorofi.
Hakukosea katika dhana yake hiyo.
"Wewe ndio Jaka?" Aliuliza yule bwana huku akimtazama kwa dharau. Jaka hakufanya haraka kumjibu. Alikuwa akiendelea kumzama kwa makini.
Sura yake pana haikuwa nzuri. Macho yake makubwa yalikuwa mekundu na yaliyotokeza nje kama ya mtu aliyekabwa, na Jaka alijikuta akijiuliza iwapo macho yale yaliweza kufumba pindi mtu yule alalapo, kwani ngozi zilizo juu ya macho yale zilionekana ndogo kuliko macho ambayo zilitakiwa ziyafunike.
Pua yake pana na fupi ilimtambaa karibu uso wote na chini ya pua ile kulikuwa kuna ndevu zilizolala juu ya mdomo wake wa juu na kufanya mustachi mnene.
Midomo yake ilikuwa minene na mipana, na kutoka kwenye kona ya kushoto ya mdomo wake huo kulitambaa kovu moja baya lililokwenda hadi chini kidogo ya taya lake la kushoto. Wazo jingine lililomjia Jaka ni kwamba hapo nyuma kuna mtu alijaribu kumpanua mdomo wake huo kwa kisu kikubwa na kikali sana.
Moyoni alimpongeza mtu huyo.
Kidevu cha yule bwana kilikuwa kimejaa mapele yaliyotokana na kunyoa ndevu zilizotaka kukitawala kidevu kile, mapele ambayo yalitapakaa chini ya kidevu hicho hadi sehemu ya mbele ya shingo lake nene.
"Naongea na wewe 'apo...! We' ndio Jaka?" Alifoka kwa ghadhabu yule askari baada ya kuona kuwa Jaka hakumjibu haraka kama jinsi yeye alivyotaka. Jaka aligundua kuwa pindi afokapo, pua ya yule askari hutanuka na kuwa pana zaidi, hivyo kufanya nywele ndogo za ndani ya pua ile kutokeza nje.
"Yes Sir...mimi ndio Jaka...nimekuja kuripoti." Hatimaye alimjibu.
Yule bwana alimtazama kwa makini, kisha akaitazama picha ndogo saizi ya pasipoti iliyokuwa kwenye faili lililokuwa mbele yake pale mezani, faili ambalo lilikuwa limeandikwa jina la Jaka juu yake na chini ya jina lile kulikuwa na neno moja tu lililoandikwa kwa wino mwekundu, “Murder”, yaani "Mauaji".
Mwili ulimsisimka Jaka kwa kuliona neno lile likinasibishwa na jina lake pale kwenye lile faili namna ile.
"Mimi naitwa Inspekta Osman Mgunya, na nimekuja Dodoma maalum kutoka Dar es Salaam kwa ajili yako wewe!" Jamaa alimkoromea kwa sauti nene ya kukwaruza. Jaka akapigwa butwaa. Alibaki akimtazama tu, asijue la kusema.
“Kwa hiyo ukae ukijua kuwa nitakuwa nikifuatilia nyendo zako kwa makini sana hapa Dodoma.” Jamaa lilimwambia na kutulia kidogo, kisha likaendelea, “…na nikikupata na kosa tu...” Likapitisha kidole chake cha shahada kutoka upande mmoja wa shingo lake pana hadi mwingine, likikifananisha kidole chake na kisu, huku akitoa sauti ya “Krrrr!” kumaanisha kuwa atamchinja.
Jaka hakuelewa alimaanisha nini kwa kitendo kile.
Alimtazama machoni yule bwana kabla ya kumuuliza kwa upole.
"Kwa nini?"
Osman Mgunya alibaki kimya kwa kama dakika moja hivi huku naye akimtazama Jaka machoni, kama kwamba aliyekuwa akijishauri iwapo amjibu au amchape makofi. Katika dakika moja hiyo Jaka naye hakupepesa wala kukwepesha macho yake kutoka kwa yule askari mwenye sura ya kuchukiza. Hakuna kilichosikikandani mle ndani zaidi ya sauti za pumzi zao tu wakihema, mithili ya majogoo yaliyopigana na kugundua kuwa yote yalikuwa nguvu sawa.
Hatimaye Mgunya aliamua kujibu swali lile. Huku bado macho yao yakiwa yamefungana, alimwambia kwa sauti ya kunong'ona ili kusisitizia uzito wa maneno yake.
"Kwa sababu imegundulika kuwa umepewa adhabu ndogo kuliko kosa ulilofanya Jaka. Na kazi yangu ni kuhakikisha kuwa unafanya kosa jingine moja tu, basi! Umeelewa?" Kisha bila kusubiri jibu kutoka kwa Jaka, alimsukumia Jaka kwa nguvu kile kitabu cha kusaini kuwa alikuwa ameripoti pale kituoni jioni ile.
"Saini hapo na upotee upesi machoni mwangu, muuaji mkubwa wewee!" Alimkoromea kwa hasira.
Taratibu Jaka alichukua kalamu iliyokuwapo pale mezani, akasaini sehemu aliyotakiwa kusaini, kisha akailaza juu ya lile daftari ile kalamu. Baada ya hapo aliinua macho yake na kumtazama tena yule askari mbaya, na bila ya kusema neno lolote aligeuka na kutoka nje ya chumba na hatimaye, jengo lile.
___________________

Imegundulika kuwa adhabu uliyopewa ni ndogo kuliko kosa ulilofanya...
Maneno hayo yalijirudia tena na tena kichwani kwa Jaka usiku ule akiwa amelala chali kitandani kwake. Kwa usiku ule hakuwa na mategemeo ya kupata usingizi, kwani alikuwa amezongwa na mawazo mengi sana na yote hayakuwa mazuri hata kidogo.
Yaani... kweli Mungu anaweza kuangalia tu jinsi waja wake tunavyofanyiana unyonge hapa duniani bila ya kuingilia kati hata kidogo...? Na kisha baada ya yote haya bado tena watu tunakufa na kurudi kwake ili tukahukumiwe kutokana na matendo yetu hapa duniani...! Sasa sisi tunaoanza kupata hukumu hapa hapa duniani tukienda huko tutakuwaje...?
Jaka aliendelea kuwaza kwa unyonge huku bila ya yeye mwenyewe kujua, machozi yakimtoka.
Kwa mbali, ndani kabisa ya akili yake alipitiwa na ile hisia kuwa kuna kitu ambacho kingeweza kumtoa katika janga lile la kusingiziwa...
Lakini ni kitu gani...?
Hakujua ni muda gani ulipita akiwa amejilaza chali pale kitandani akiumiza akili kutafuta njia ya kujikwamua kutoka katika janga lile, bila mafanikio. Alipoanza kusinzia, majogoo yalikuwa yakiwika huko nje.

_____________________

Anakimbia. Pumzi zimemjaa. Amechoka kupita kiasi. Lakini hawezi kusimama.
Lazima akimbie...na anaendelea kukimbia, tena kwa kasi. Hajui anamkimbia nani au anakimbilia wapi, analojua ni kwamba ni lazima akimbie. Anatazama mbele...Kiza. Haoni kitu. Ni kiza totoro! Radi inapiga na mwanga mkali wa radi ile unamuonesha njia kidogo naye anaifuata mbio.
Mvua kubwa inamnyeshea. Moto. Maji ya mvua ile ni ya moto! Yanamuunguza kichwani, mgongoni, mikononi na mwili mzima. Anapiga kelele kwa maumivu ya kuunguzwa na yale maji ya moto huku anakimbia. Radi imetoweka na kiza kimetawala tena, anatumbua macho ili aone vizuri, na maji ya moto ya mvua ile yanamuingia machoni. Ananapiga ukelele mkubwa...haoni mbele.
Ghafla mwanga unajitokeza kwa mbali sana mbele yake. Anaukimbilia. Anaona anaufikia haraka sana ule mwanga...hapana ule mwanga nao unamsogelea. Anasimama ghafla. Ule mwanga ni taa ya Chemli. Msichana mzuri ameishika chemli ile kwa mkono wake wa kulia na kwa mkono wake wa kushoto ameshika mwavuli ambao amejifunika kujikinga na mvua ile ya ajabu. Msichana wa ajabu...
Nuru imemzunguka msichana yule mwenye uzuri wa kuvutia.
Malaika...?
Amevaa gauni refu jeupe na jepesi sana ambalo linaonesha mwili wake wote...hakuwa amevaa nguo yoyote nyingine chini ya gauni lile jepesi. Anatumbua macho kumshangaa yule msichana wa ajabu.
Anayatazama matiti yake yaliyochomoza mbele kiasi cha kutishia kuitoboa nguo ile laini. Kiuno chake chembamba kilitenganisha vizuri sehemu iliyokuwa imebeba matiti yale na sehemu ya chini ya mwili wake wenye kushawishi. Mapaja yake yalikuwa yamejaa vizuri na miguu yake ilikuwa ni yenye kuvutia hasa kwa vile alivyokuwa hakuvaa viatu. Wazo jipya linagonga akilini mwake.
Ni jini...?
Woga mkubwa unamshika. Anataka kugeuka na kukimbia kurudi kule alipokuwa anatokea, lakini macho ya yule binti yanamkataza...anayatazama tena macho yale...
Yule msichana anainama na kuiweka chini ile taa, kisha anainuka huku akiwa amemnyooshea mkono wake wa kulia kwa ishara kuwa amsogelee. Bila ya kujitambua anamsogelea yule msichana wa ajabu. Anapomfikia, yule binti anampa ule mwavuli naye anaanza kunyeshewa na ile mvua ile ya moto. Anauchukua ule mwamvuli na kumsogelea zaidi yule msichana. Wanajifunika pamoja kwa mwamvuli ule, msichana anaichukua ile taa na kwa pamoja wanaanza kuondoka kuelekea kule kule alipokuwa anapakimbia hapo mwanzo.
Mara yule msichana anasimama na kuanza kumuangalia usoni kwa huzuni huku akitiririkwa machozi. Anashangaa. Haelewi, na punde yule msichana wa ajabu anaangua kilio kikubwa na cha uchungu mno!
Anataka ambembeleze lakini hawezi...ananyoosha mkono wake ili amshike lakini mkono wake unamuwia mzito sana.
Woga unamzidi maradufu!
Na mara hiyo anasikia sauti kali ikimwita kwa jina lake kutoka kule walipokuwa wakielekea. Anainua uso wake kutazama ni nani anayemwita. Anamuona Osman Mgunya akiwafuata pale walipokuwa kwa mwendo wa haraka huku amekunja uso kwa ghadhabu zisizo kifani, mkono wake wa kulia ukiwa umeshika upanga mrefu ambao mara ile alipoinua uso wake kumuangalia yule mtu tu ule upanga ukatoa radi kubwa...upanga wa radi !
Osman Mgunya alikuwa akimwendea mbio huku akimwita jina lake mfululizo... Jaka!....Jaka!....Jaka!.....Jaka !
 
SEHEMU YA TANO

Na mara hiyo anasikia sauti kali ikimwita kwa jina lake kutoka kule walipokuwa wakielekea. Anainua uso wake kutazama ni nani anayemwita. Anamuona Osman Mgunya akiwafuata pale walipokuwa kwa mwendo wa haraka huku amekunja uso kwa ghadhabu zisizo kifani, mkono wake wa kulia ukiwa umeshika upanga mrefu ambao mara ile alipoinua uso wake kumuangalia yule mtu tu ule upanga ukatoa radi kubwa...upanga wa radi !
Osman Mgunya alikuwa akimwendea mbio huku akimwita jina lake mfululizo... Jaka!....Jaka!....Jaka!.....Jaka !
" ... Jaka ! Jaka...! Jaka...amka, utachelewa kuripoti kituoni....saa mbili kasoro sasa!"
Jaka alishtuka kutoka kwenye usingizi na ndoto ile ya ajabu.
Kijasho chembamba kilikuwa kikimtoka. Alifumbua macho kisha upesi akayafumba pale mwanga wa jua ulipompiga moja kwa moja usoni. Alijikinga uso wake kwa kiganja chake kutokana na mwanga wa jua lile na kuyafumbua tena macho yake taratibu.
Mnyaga alikuwa amemwinamia hali mkono wake wa kulia ukiwa begani kwake, akimtikisa.
"Anko leo umelala sana...nimeanza kukuamsha kitambo!" Mnyaga alimwambia.
" Unnnhh...aaankhh...nilikuwa naota....saa ngapi sasa?" Jaka alibwabwaja huku mwayo ukimtoka.
"Saa mbili kasoro kumi sasa!" Mnyaga alimwambia, naye akakurupuka na kuketi kitandani.
Jambo la kwanza lililomjia akilini mwake baada ya usingizi kumtoka ni kwamba sura ya yule binti aliyemuota kwenye ile ndoto haikuwa ngeni akilini mwake. Alikuwa na hakika kabisa kuwa ilikuwa ni sura ya mtu anayemjua...alishapata kuiona sura ile kabla ya ndoto ile...
Tatizo ni kwamba hakuweza kukumbuka ni wapi au lini. Alijiuliza sana ni nini maana ya ndoto ile katika wiki yote ile bila mafanikio. Jambo pekee alilokuwa na uhakika nalo ni kwamba yule askari aliyejiita Osman Mgunya hakuwa na nia nzuri kabisa naye. Hilo halikuwa na shaka hata kidogo akilini mwake.
______________________

Miezi minne baadaye alikuwa ameisahau kabisa ile ndoto, naye akawa ameshazoea hali ya pale Dodoma. Mara kwa mara alikuwa akienda sokoni pamoja na mzee Mnyaga na kumsaidia katika biashara zake za matunda. Katika moja ya siku hizo alipatwa na msukosuko ambao ulikuwa ni mpango wa Osman Mgunya katika kuhakikisha kuwa Jaka anafanya kosa litakalompa fursa ya kumchukulia hatua kisheria.
Siku hiyo alikuwa akiuza zabibu pale sokoni na mara wakaja jamaa wanne walioonesha nia ya kutaka kununua zabibu. Jaka alijaribu kuwakaribisha kwa uchangamfu na kuanza kuwatajia bei za mafungu mbalimbali ya matunda yale aliyoyapanga vizuri pale mezani.
Cha ajabu ni kwamba baada ya kukaribishwa, mmoja kati ya wale jamaa alichukua chana moja ya zabibu na kuikamua yote pale juu ya meza huku wale wenzake wakicheka kwa dharau na kebehi. Mara moja Jaka akabaini kuwa wale jamaa walikuwa wametumwa. Akaamua kunyamaza kimya.
"Vipi, mbona unagwaya wewe...huna ubavu nini?" Aliuliza kwa kejeli mmoja kati ya wale jamaa.
Kabla Jaka hajajibu, jamaa mwingine akamchapa kofi kali la uso. Kwa ghadhabu Jaka alitaka kumrukia yule jamaa lakini akawahi kujizuia. Mwingine akachukua chana mbili za zabibu na kuzitupa chini. Jaka akatoka nyuma ya meza yake na kwenda kuziokota. Vile anainama tu alipigwa ngwara kali sana kwa nyuma na kuanguka chali pale chini, na wale jamaa wakaendelea kumcheka kwa fujo.
Watu waliokuwa pale sokoni wakaanza kujaa huku wengine wakitaka kujua kulikoni.
Mara hiyo akatokea mzee Mnyaga, ambaye kwa hasira aliwafokea wale jamaa. Mmoja wa wale jamaa alitaka kumletea jeuri na Mzee Mnyaga akamtwanga konde zito lililompeleka moja kwa moja mpaka chini. Basi huo ukawa ndio mwanzo. Wafanya biashara wengine pale sokoni nao wakawavamia wale jamaa na kuwapa mkong'oto wa haja!
Na ni hapo ndipo Land Rover ya polisi ilipowasili kwa vishindo eneo lile huku askari wakiruka chini kwa jazba kuja kutuliza ghasia ile. Osman Mgunya alikuwa ndio kiongozi wa kundi lile la askari. Jaka alimtupia jicho kwa chati huku akendelea kupanga zabibu zake taratibu pale mezani na kumuona jinsi uso ulivyomshuka baada ya kuwaona wahalifu na kubaini kuwa Jaka hakuwa miongoni mwao. Aligeuka huku na kule akijaribu kumtafuta Jaka. Alipomuona, Jaka alikuwa ametulia kimya nyuma ya meza yake ya zabibu akimtazama. Osman alimtulizia jicho la chuki mno, kisha akaingia kwenye gari lile kwa ghadhabu na kubamiza mlango.
Wale jamaa wanne ndio waliotiwa mbaroni baada ya watu wote pale sokoni kuwataja kuwa ndio chanzo cha vurugu ile. Jaka alijua kuwa wataenda kuachiliwa mbele ya safari na bila shaka kupewa na posho yao kwani alikuwa na hakika kabisa kuwa wale jamaa walikuwa wametumwa na Osman Mgunya.
Jioni ile alipoenda kuripoti pale kituoni alimkuta Osman Mgunya akiwa amefura vibaya sana kwa ghadhabu, jambo lililomhakikishia kuwa mawazo yake kuhusiana na tukio lile yalikuwa sahihi. Osman alimsukumia daftari na kalamu ili aweke saini yake kwa jioni ile. Bila ya kusema neno alichukua ile kalamu na kusaini sehemu aliyotakiwa kisha akamsogezea Mgunya daftari lile ili naye asaini.
Mgunya akaweka kiganja chake kinene mithili ya chana ya ndizi juu ya kiganja cha mkono wa Jaka na kukigandamiza kwa nguvu pale juu ya daftari. Kwa mshangao Jaka alimuinulia uso wake uliojaa viulizo kutaka kujua kulikoni, na hapo akakutana na kofi kali sana la uso kwa mara ya pili katika siku ile.
Khah!
Kabla hajatanabahi kutokana kofi lile Osman alikuwa ameshamdaka shingo kwa kono lake la kushoto na kumbana koo.
Ebwana we!
Macho yalimuwiva Jaka kwa kofi lile na akiona vinyota vikielea mbele ya macho yake huku akiuhisi uso ukimtutumka. Aliinua mikono yake yote miwili na kuushika ule mkono uliomkaba koo akijaribu kuutoa bila mafanikio.
Mgunya alimvuta mbele kwa nguvu mpaka sura zao zikawa zimetenganishwa na sentimeta chache mno baina yao. Hali ile ilisababisha Jaka avutwe kutoka upande mwingine wa meza ile na kupandishwa kiwiliwili chake juu ya meza ile hali miguu yake ikining'inia upande wa pili wa meza ile.
Osman alimkazia macho yake mekundu yaliyotokeza nje kama ya mtu aliyekabwa.
"Unajua wewe unajifanya mjanja sana...lakini ambacho hukijui ni kwamba muda wako unazidi kufikia ukingoni kwani hatimaye nitakupatia tu, fisi we! " Alimkoromea kwa sauti ya kunong'ona iliyojaa ghadhabu na vitisho.
Jaka alikunja uso kwa maumivu huku akifinya macho na pua yake kutokana na pumzi za Osman zilizonuka sigara.
Baada ya maneno hayo Osman alimuwekea usoni kiganja cha mkono wake wa kulia kumsukuma nyuma kwa nguvu huku wakati huo huo akimuachia ile shingo yake kwa mkono wake wa kushoto. Jaka alirushwa nyuma huku yowe likimtoka, akipepesuka kinyuma nyuma na hatimaye kujibwaga chali hatua chache kutoka kwenye mlango wa chumba kile.
Alijiinua kwa hasira kutoka pale chini akiwa na wazo la kumparamia Osman pale mezani kwake na kumpa ngumi nyingi tu, liwalo na liwe. Lakini kabla hajafanya hivyo aligundua kuwa alikuwa ameangukia miguuni kwa mtu ambaye alikuwa anaingia katika chumba kile.
Aliinua uso wake na kukutana na mtu wa makamo, aliyepata kiasi cha miaka kama hamsini na tatu au na nne hivi. Alikuwa mfupi na mnene, ingawa unene wake haukuwa ule wa kibwanyenye ila wa mtu mwenye nguvu. Mavazi yake ya ki-askari hayakuonesha alikuwa na cheo gani kutokana na koti refu jeusi alilolining'iniza mabegani mwake juu ya mavazi yale.
Uso wake wa duara haukuwa ukimtazama Jaka bali ulielekezwa moja kwa moja kule alipokuwa Osman Mgunya hali macho yake madogo yakionesha hasira kubwa.
"What's this...What's going on here, Osman?" Yule bwana alimfokea Osman kwa kiingereza, akimaanisha kuwa anataka aeleweshwe kilichokuwa kinaendelea pale ofisini wakati ule.
Wakati huu Jaka alikuwa ameshasimama pembeni akiwatazama Osman Mgunya na yule mtu kwa zamu, akiwa amemakinika na namna yule jamaa alivyomsemesha Osman kwa mamlaka namna ile. Osman alivyobabaika vibaya sana.
Alijikurupusha kutoka nyuma ya meza yake na kupiga saluti hali akiwa amekauka kama ubao, macho yake mekundu yakiwa yamemtoka pima.
"Hivi ndivyo ulivyofundishwa namna ya kuwatendea raia hata kama ni wahalifu?" Badala ya kuijibu ile saluti, yule bwana aliendelea kumuuliza Osman.
"Eeh...Yaani...Hapana afande...! Haitatokea tena afande!" Osman alijibu kwa kubabaika.
"Hii sio namna ya kuwatendea watu, Osman...na nataka leo ndio iwe mwisho. Sitaki kabisa mkoa wangu upate kashfa magazetini kwa unyanyasaji wa raia wowote, wawe wahalifu au vinginevyo, tumeelewana?" Aliendelea kuasa yule mtu ambaye mara moja Jaka alibaini kuwa ndiye mkuu wa polisi wa mkoa.
"Ndi…ndio afande!"
Yule bwana akamgeukia Jaka na kumtazama kwa muda kama mtu anayejaribu kukumbuka alipata kumuona wapi, kisha kama mtu aliyekumbuka akamuuliza, “Unaitwa Jaka Madega, sio?” Na kabla Jaka hajajibu lolote akaendelea, “…nadhani kwa mujibu wa maelezo ya faili lako wewe ni msomi, na hivyo unazijua fika haki zako za kisheria au sio? Sasa nataka hili jambo lililotokea leo ulisahau na nina imani kuwa bwana Osman hapa…” Akamgeukia Osman Mgunya na kumkazia macho, “…atahakikisha kuwa halitokei tena.”
Jaka alibaki akiwa ameduwaa tu. Hakujua iwapo yule mtu alikuwa akimaanisha yale aliyokuwa akiyasema au alikuwa akimkebehi tu. Kwa mambo aliyoyapata kutoka kwa wana-usalama hapo nyuma, hakuwa na imani na askari yeyote hapa nchini. Yule bwana alimtazama Jaka kwa makini zaidi.
“Au kila siku unapokuja kuripoti huwa unapigwa bwana mdogo? Ni mara ya ngapi sasa tukio kama hili linakutokea hapa kituon?” Hatimaye aliongezea kumsaili.
Jaka alimgeukia Osman na kumtazama usoni. Mgunya aligwaya wazi wazi, midomo ikimcheza na nyusi zikimtetema.
“Hapana mzee...jambo kama hili halijawahi kunitokea hata siku moja hapa kituoni.” Jaka alijibu huku akiendelea kumtazama Mgunya usoni kwa macho makavu. Osman alimeza fundo kubwa la mate huku pua zikimtanuka na kumsinyaa haraka haraka. Hakuamini masikio yake.
Jaka alimgeukia yule mzee na kumshukuru.
“Nashukuru sana kwa wema wako mzee...”
“No! Sio swala la wema hilo bwana mdogo. Huu ni wajibu wangu...na ni wajibu wa askari yeyote mzuri...kulinda na kuhudumia umma.” Yule bwana alimwambia.
“Nashukuru sana...”
Yule bwana akamnyooshea mkono wake wa kulia huku akijitambulisha.
“Naitwa Januari Mwakaja, ndio RPC wa hapa Dodoma.”
“Na...nafurahi sana kukufahamu mzee.” Jaka alijibu huku akiupokea kwa heshima mkono wa yule mzee. Januari Mwakaja alitabasamu.
“Twende. Nitakupa lifti mpaka njia ya Makole...naamini unaishi Makole, au sio?” Ilikuwa ni zamu ya Jaka ya kutoyaamini masikio yake kwa siku ile. Yule mkuu wa polisi wa mkoa alionekana kujua kila kitu kuhusu yeye, na hili lilimkosesha amani kidogo Jaka.
“Eeenh...ndio mzee...lakini...nitatembea tu!” Alibwabwaja, na Januari Mwakaja akamcheka kidogo.
“Wacha uoga dogo...twende nikupe lifti. Angalau uone kuwa askari ni watu wema pia.” Alimwambia.
Jaka hakuwa na namna.
Wakiwa garini kuelekea Makole, Mzee Mwakaja alimuuliza Jaka alikuwa akifanya nini pale Dodoma wakati anapokuwa anasubiri muda wa kuripoti kituoni. Jaka alimwelwza kuwa huwa anamsaidia mjomba wake kuuza matunda sokoni.
Mzee Mwakaja aliendelea kuendesha gari lake aina ya Toyota Prado akiwa kimya kwa muda mrefu.
“Unajua si kila mfungwa ni mkosa, na hata huko magerezani wafungwa huwa wanafanya kazi mbalimbali ili kuwaandaa na maisha ya uraiani mara baada ya kumaliza adhabu zao...ili wasije kuwa wazururaji tu baada ya kutoka vifungoni...” Hatimaye yule mzee aliongea.
Jaka aliendelea kumsikiliza bila ya kusema neno, akijaribu kuchambua maana ya maneno yale.
Si kila mfungwa ni mkosa...
Ina maana anajua kuwa sikufanya kosa nililoadhibiwa kwalo ?
“Si...sijakuelewa unamaanisha nini mzee...”
“Ni kwamba na wewe una haki ya kujitayarisha kukabiliana na maisha yako ya baadaye baada ya kumaliza muda wako hapa Dodoma." Januari Mwakaja alimwambia.
Jaka alitikisa kichwa tu kuashiria kuwa alikuwa amemuelewa. Alihisi kuwa mzee Januari Mwakaja alikuwa ni mtu ambaye angeweza kumuamini. Alijiuliza ingekuwaje iwapo angesema ukweli juu ya mambo aliyokuwa akifanyiwa na Osman Mgunya pale kituoni....labda Osman angerudishwa Dar es Salaam....
Hapo Jaka alikumbuka wakati alipokuwa JKT akilitumikia Jeshi La Kujenga Taifa kwa mujibu wa sheria. Jambo moja alilojifunza huko lilikuwa ni kwamba hata kama mtu ukiwa unajuana au unaelewana sana na mkuu wa kikosi au CO, yaani Commanding Officer, haitakusaidia kitu iwapo utakosa kuelewana na Koplo tu, ambaye ni afisa wa cheo cha chini lakini ndiye unayekuwa naye muda wote. Hivyo Koplo anaweza kukutafutia adhabu kadhaa wa kadhaa na kukufanyia visa kemkem na kuyafanya maisha yako kuwa ni ya mashaka makubwa sana, pamoja na kujuana kwako na CO .
Na ni katika misingi hiyo hiyo ndivyo alivyoiona ile hali iliyojitokeza kati yake, Osman Mgunya na Januari Mwakaja.
___________________

Siku iliyofuata hakupata vishindo vyovyote kutoka kwa Osman Mgunya ambaye alimkuta akiwa amepoa sana. Baada ya kusaini kwenye kitabu aligeuka na kuanza kuondoka, lakini Osman alimwita na kutoa bahasha kutoka kwenye droo ya meza yake.
Akaitupia pale juu ya meza.
“Barua yako hiyo.”Alimwambia na kuangalia pembeni.
Jaka aliichukua ile bahasha na mara moja akajua ilikuwa imetoka wapi kwani hati iliyoandika jina lake juu ya bahasha ile kwa anuani ya RPC Dodoma aliijua fika, na kwa nukta ile alipouona mwandiko ule, moyo wake ulifanya kitu kama sarakasi hivi.
Ulikuwa ni mwandiko wa mama yake!
Kwa furaha Jaka alitamani kumshukuru Osman kwa kumpa mkono, lakini hakufanya hivyo. Badala yake aliitazama ile bahasha taratibu na kugundua kuwa ilikuwa imefunguliwa hivyo akajua kuwa Osman alikuwa ameshaisoma. Aliangalia muhuri wa Posta wa siku barua ile ilipofika pale Dodoma, na kugundua kuwa barua ile ilikuwa imefika zaidi ya wiki mbili nyuma.
Alimtazama Osman kwa hasira ya wazi.
“Sasa si bora ungenisimulia tu yaliyoandikwa kwenye barua hii, unaonaje?” Alimwambia kwa hasira, kisha bila kusubiri jibu aligeuka na kuondoka.
Osman alibaki akiwa amefura kwa hasira.

ITAENDELEA
 
SEHEMU YA SITA

Kwa furaha Jaka alitamani kumshukuru Osman kwa kumpa mkono, lakini hakufanya hivyo. Badala yake aliitazama ile bahasha taratibu na kugundua kuwa ilikuwa imefunguliwa hivyo akajua kuwa Osman alikuwa ameshaisoma. Aliangalia muhuri wa Posta wa siku barua ile ilipofika pale Dodoma, na kugundua kuwa barua ile ilikuwa imefika zaidi ya wiki mbili nyuma.
Alimtazama Osman kwa hasira ya wazi.
“Sasa si bora ungenisimulia tu yaliyoandikwa kwenye barua hii, unaonaje?” Alimwambia kwa hasira, kisha bila kusubiri jibu aligeuka na kuondoka.
Osman alibaki akiwa amefura kwa hasira.

4
Akiwa amebakiza miezi miwili akamilishe mwaka mmoja mjini Dodoma, Jaka alirejewa tena na ile ndoto ya yule msichana wa ajabu. Kwa muda wote uliopita alisahau kabisa kuhusu ndoto ile. Jambo lililomshangaza ni kwamba ndoto ile ilimrudia vilevile kama ilivyomjia mara ya kwanza.
Hili lilimpa taabu sana kulielewa.
Nini maana ya ndoto hii?
Ni utabiri wa aina fulani au...?
Vyovyote iwavyo hii si ndoto ya kawaida...si ya kawaida kabisa! Sasa kwa nini inanijia namna hii?
Alikuwa akiwaza mambo hayo huku akitembea jioni ya siku iliyoamkia usiku alioota ile ndoto kwa mara ya pili. Ilikuwa inapata saa moja kasoro robo hivi za jioni.
Alikumbuka maneno ya mzee Mnyaga mara alipomueleza habari za ndoto ile baada ya kumrudia tena asubuhi ya siku ile. Mnyaga alibaki mdomo wazi, na kwa muda mrefu alibaki kimya kabla ya kumwambia kuwa alikuwa na uhakika kuwa ndoto ile ilikuwa inambashiria mambo fulani ambayo yangemtokea baadaye au yaliyomtokea hapo awali. “...ila kwa hakika hiyo ndoto inakubashiria mafanikio fulani...” Mnyaga alimalizia huku akionyesha kuwa na mawazo mengi.
“Mafanikio? Kwa vipi anko?” Alimuuliza huku akionyesha kutoamini kabisa maneno yale.
Mnyaga aliguna kidogo kabla ya kumjibu.
“Kwanza kuna mwanga katika ndoto yako, ambayo ni ishara ya ufumbuzi fulani...halafu kuna mwamvuli...mwamvuli unaashiria kinga au ushindi wa aina fulani...” Mnyaga alisita kidogo, kisha akaendelea “...sijui lakini...ila nadhani vitu vyote hivyo vinaashiria mafanikio...ushindi dhidi ya matatizo, ambayo humo ndotoni yamekuja kama mvua ya maji moto na yule khabithi Osman Mgunya laana za manani zimuangukie milele!”
Jaka alimcheka sana kwa majibu yale, akimtania Mnyaga kuwa ni vyema angeanzisha biashara ya kutabiri ndoto.
Lakini sasa kila alivyozidi kulifikiria swala lile ndivyo lilivyozidi kumtia wasiwasi kwani lilionesha uhusiano fulani na jambo jingine ambalo kwa muda mrefu limekuwa likimkosesha raha. Kwa namna fulani amekuwa akipatwa na hisia kwamba kuna kitu au jambo fulani hivi, ambacho kingeweza kumtoa katika janga lile alilotumbukizwa...
Ni kitu gani basi?
Hakuweza kukiweka sawa akilini mwake kitu hicho, ingawa uwepo wake ulizitawala sana hisia zake. Ni kitu ambacho kilikuwepo muda wote tangu mwanzo.
Sasa na hii ndoto tena...
Mungu wangu ! Ni nini kinanitokea mimi?
Kwa nini mimi... ?
___________________

Maisha ya binadamu huweza kubadilika kwa namna ya ajabu kabisa na kwa namna ambayo hata binadamu mwenyewe hawezi kufanya lolote katika aidha kuyazuia yasibadilike au kuyafanya yabadilike na kuingia kwenye hali hiyo yanayobadilikia.
Ni sawa na jinsi alivyoeleza mwanafalsafa mmoja wa Ujerumani aliyeishi karne kadhaa zilizopita aliyeitwa Hegel. Yeye alisema kuwa binadamu hawezi kubadilisha au kuongoza matukio katika historia, bali mwanadamu huishi maisha yake kutekeleza yale ambayo matukio ya historia yametayarisha yamtokee mwanadamu katika maisha yake mafupi hapa duniani.Hivyo kadiri matukio yanavyobadilika na binadamu nae hulazimika kubadilika.
Sio watu wengi waliokubaliana na Hegel wakati ule alipokuwa akiandika falsafa zake hizo katika karne ya kumi na nane. Na pia sio wote wanaokubaliana nae leo hii katika karne hii tuliyonayo sasa.
Lakini bila shaka katika wale wachache watakaoweza kukubaliana na falsafa hii ya marehemu Geog Wilhelm Friedrich Hegel katika karne yetu hii, Jaka atakuwa ni mmoja kati yao hasa ukizingatia jinsi maisha yake yeye yalivyobadilika kwa namna ya ajabu kabisa kwanza bila ya yeye mwenyewe kutaka na pili bila ya yeye kuwa na lolote aliloweza kufanya kuzuia mabadiliko hayo na hatimaye akajikuta Dodoma.
Na bila ya yeye kutaka au kujua, ilifika siku akiwa pale Dodoma ambapo mlolongo mzima wa maisha yake ulibadilika kwa namna ya ajabu kabisa na bado asiwe na la kufanya zaidi ya kupigwa na butwaa tu. Ni siku ambayo hakujua kama ingefika na hata ilipofika hakutegemea kwamba ndio ingekuwa mwanzo wa kufungua ukurasa mpya kabisa katika hadithi ya maisha yake...kama jinsi alivyosema bwana Hegel.
Tofauti pekee ni kwamba ni wazi kuwa Jaka na watu wengi wa karne hii wangesema kuwa kila jambo hupangwa na Mungu...
________________________

Jaka alikuwa ameegemea nguzo ya jengo la Benki Ya Taifa Ya Biashara (NBC) tawi la Mtendeni pale Dodoma mjini akiangalia vijana wenzake wakipita kwa mbwembwe na furaha kuelekea ndani ya ukumbi wa disko wa NK ambao jengo lake lilikuwa linatazamana na lile jengo la Benki.
Ilikuwa ni siku ya jumatano na muda ulikuwa ni kama saa tatu na robo hivi za usiku. Vijana wengi waliokuwa wakielekea ndani ya ukumbi ule, wake kwa waume, walikuwa wamejipendezesha kwa mavazi ya kileo ambayo mengi yao yalivaliwa kufuatia mitindo ya uvaaji ya wanamuziki maarufu duniani.
Kile alichokuwa akikiona pale nje ya ule ukumbu wa disko usiku ule kilimkumbusha wakati akiwa Dar es Salaam ambapo naye alikuwa ni mhudhuriaji mzuri wa maeneo kama yale, pamoja na matamasha mbalimbali ya muziki. Pia hali ile ilimkumbuka mtu ambaye mara nyingi alikuwa akiambatana naye katika matukio kama yale. Mtu ambaye yeye aliamini kuwa walikuwa wanapendana sana...mpaka ilipofikia siku ile aliposhuhudia maisha na ndoto zake zote zikisambaratika mbele ya macho yake...na ndipo alipogundua kuwa kama ni penzi, basi lilikuwa la upande mmoja tu...
Kila alipomfikiria yule binti ambaye yeye aliamini kuwa baina yao kulikuwa kuna upendo wa hali ya juu, roho ilimuuma sana. Hakutaka kuendelea kumfikiria, hivyo alihamishia mawazo yake kule walipokuwa wale vijana wenzake na jinsi walivyokuwa wakisherehekea ujana wao.
Akiwa anaendelea kutazama matukio ya kufurahisha pale nje ya ule ukumbi maarufu wa disko, gari aina ya Nissan X-Trail lilifika eneo lile na kuegeshwa hatua chache kutoka pale alipokuwa amesimama. Yeye aliamua kuondoka eneo lile akiwa na wazo moja tu la kwenda kulala. Kwake siku ilikuwa imeisha salama. Aliangaza kulia na kushoto na kuamua kuchukua njia iliyokuwa kulia kwake ambayo ingempeleka mpaka chuo cha biashara cha CBE, huko angekata kushoto na kuingia Makole.
Alikuwa anageuka kulia ili aanze hiyo safari yake.
Na hapo ndipo alipomuona.
Moyo ukamlipuka na hapo hapo ukaanza kumuenda mbio. Na hata pale alipokuwa amesimama akimkodolea macho yule mtu aliyeteremka kutoka kwenye ile X-Trail, bado ilimuwia vigumu kuamini macho yake. Pamoja na mtu yule aliyemduwaza Jaka pale nje ya ule ukumbi wa disko, waliteremka vijana wengine watatu, wawili wakiwa wasichana. Haikuwa na shaka kuwa nao walikuwa wamekwenda kujiburudisha kwa disko usiku ule pale NK.
Alibaki akiwa amekodoa macho kuwatazama.
Yule mtu aliyemfanya moyo ulimpuke alikuwa amesimama nje ya lile gari hali akiwa ameegemeza mkono wake juu ya paa la gari lao wakati mkono wake mwingine ameuzungusha kiunoni kwa mmoja kati ya wale wasichana wawili wazuri sana waliofika nao eneo lile. Uso wake alikuwa ameuelekeza kwenye lango kuu la kuingilia kule ukumbini, na kutokea pale alipokuwa, Jaka alikuwa akiuona upande wa kushoto wa sura ya yule mtu.
Hivi ni yeye kweli au nimemfanaisha? Atakuwa amekuja kutafuta nini huku?
“Duh! Inaelekea mambo yameshaanza hapa, you know what I'm sayin' ?” Yule jamaa alisema kwa sauti ya mbwembwe za kimarekani kuwaambia wenzake huku akiendelea kutazama kule kwenye jengo lenye ule ukumbi wa disko.
Ah! Ile sauti...Ni ile ile!
Na yale maneno....you know what I'm sayin' ....
Hapo Jaka ndipo haswa alipopata uhakika juu ya mtu yule.
Ni yeye bloody swine!
Hasira zilianza kumpanda kwa kasi ya ajabu.
Alimfahamu fika yule jamaa...kwani ndiye hasa chanzo cha matatizo yote yaliyomkumba.
Sasa wamekuja kukutana tena huku Dodoma!
Bila kufikiri zaidi alijikuta ameshamsogelea yule jamaa na alimwita kwa jina huku akinyoosha mkono wake ili amshike bega.
“Aisee, Tony...”
Hapo ndipo alipoishia, kwani yule jamaa alipouona mkono wa Jaka ukimjia kwa pembe ya jicho lake, alishtuka na kugeuka ghafla huku akifikiria kuwa Jaka alikuwa ni mwizi aliyetaka kumpora cheni yake ya dhahabu aliyokuwa ameivaa shingoni. Masikini Jaka hakufikiria kuwa kwa muonekano aliokuwa nao wakati ule, hata vijana wenzake walimuona mzee, kwani uso ulimjaa ndevu, nywele zake hazikuwa zimenyolewa kwa muda mrefu kiasi cha kunasibishwa na uchafu, na zaidi ya hapo, mavazi yake yalikuwa tofauti kabisa na hadhi ya eneo lile.
Hivyo mtu yeyote angeambiwa kuwa Jaka alikuwa mwizi, asingekataa.
Basi yule jamaa ambaye Jaka alimtambua kwa jina la Tony na ambaye ki-umri hawakutofautiana sana, alimgeukia Jaka kwa ghadhabu na mara ile ile yule kijana mwingine aliyekuwa safari moja na yule mtu ambaye Jaka aliamini kuwa ndiye chanzo cha matatizo yote yaliyomkuta, alipiga yowe la mwizi kwa woga.
Na katika sekunde ile ambayo yule mtu alimgeukia Jaka kwa ghadhabu, macho yao yalikutana. Mara moja Jaka akaona kuwa na yule mtu alikuwa amemtambua, kwani alipigwa na butwaa na kubaki akimtazama kwa kutoamini.
Walibaki wakitazamana.
Kama jinsi walivyowahi kutazamana hapo nyuma.
Lakini kabla ya yeyote kati yao hajasema lolote, vurumai ilianza.
Ule ukelele wa "mwizi" uliwavuta vijana wengine waliokuwa pale nje ya ule ukumbi ule ambao walifika kwa kasi pale kwenye ile X-Trail huku wakipiga mayowe ya jazba. Jaka akagundua kuwa tayari maisha yake yalikuwa hatarini. Haraka alimgeukia yule jamaa aliyepiga kelele ya "mwizi" ili amfahamishe kuwa yeye sio mwizi.
Ile anageuka tu alikutana na kofi kali sana la uso. Mmoja kati ya wale wasichana waliokuja na yule mtu aliyejulikana na Jaka kama Tonu akapiga kelele wawoga. Jaka alijishika uso wake na kuinama kwa uchungu. Mara alishtukia miguu yake ikichotwa ngwara kali naye akaenda chini kwa kishindo huku yowe likimtoka, akisikia matusi kemkem yakivurumishwa dhidi yake. Alijitahidi kuinuka kutoka pale chuni huku akijinadi kuwa si mwizi, na hapo alianza kupokea mvua ya mapigo kutoka kila upande. Mateke, fimbo, ngumi, mawe...
Alipiga kelele za kujitetea huku akijitahidi kuinuka kutoka pale chini bila mafanikio. Ilikuwa ni vipigo vya mfululizo. Damu ilimtoka puani, mdomoni na sehemu nyingine za mwili kutokana na mapigo yale.
Matusi yaliendelea kumuangukia sambamba na mapigo yale, naye akahisi alikuwa anaanza kurukwa na akili. Kwa mbali aliweza kusikia sauti za akina dada wakilia na wengine wakimuombea msamaha bila mafanikio.
Aliamini kuwa mwisho wake hapa duniani ulikuwa umewadia.
Sura ya mama yake ilimjia akilini huku akihisi macho yake yakiingia kiza...
"Jamani mmeua!"
"Bado 'uyo...! 'uoni bado anahema 'uyo?"
"'Uyo dawa yake kuchomwa moto tu...!"
"Kwani pale benki si kuna askari? Apelekwe tu kituoni akafie huko huko!"
"Aaah...yule askari kasema tumwache aende zake tu...unajua ye' 'awezi kuacha lindo lake aje 'uku kuangalia vibaka, benki ikiibiwa kazi hana..."
Jaka aliyasikia maongezi hayo kwa mbali huku akiwa amelala akitweta pale chini. Alikuwa akisikia maumivu makali mwili mzima na macho yake yalikuwa yanaingia kiza na kuacha mara kwa mara. Alijiona akibebwa kimabavu kutoka pale chini na kupelekwa sehemu ambayo hakuijua.
“Sio mwiz...sio mwizi miye jam...mani...!” Alijitahidi kujieleza huku akijaribu kujigeuza kumtafuta yule mtu aliyemwita kwa jina la Tony. Alimuona kwa mbali akiwa amesimama kando ya gari lake akiwa bado amepitisha mkono wake kiunoni kwa yule msichana mzuri sana aliyekuwa naye, akiangalia wakati yeye akibebwa kuondolewa katika eneo lile.
Jaka alimnyooshea mkono kwa namna ya kumuita, au kumuomba msaada, au kumtaka aseme kitu kuthibitisha kuwa yeye hakuwa mwizi, lakini yule jamaa alibaki akimtazama tu vile vile.
“Aaah, niachieni ndugu zangu...sio mwizi mim...”
“Kelele!” Alikemewa na hapo hapo akachapwa bakora kali mgongoni, na yowe la uchungu likamtoka.
Baada ya mwendo mfupi alibwagwa chini na kutandikwa bakora nyingine ya mgongo. Alijaribu kujiinua lakini akapigwa teke kali la mbavu, naye akarudi chini kwa kishindo.
"Lete petroli!" Alisikia sauti ikiagiza kwa jazba.
Oh, Mungu wangu...!
Mara alihisi akimwagiwa petroli mwili mzima.
Hah! Nachomwa moto hivi hivi sasa!
Alijikurupusha na kusimama kutoka pale chini, lakini akapigwa ngwara iliyorudisha tena ardhini kwa kishindo huku akisikia lile kundi la watu likiendelea kumpigia mayowe ya jazba. Akajua kuwa sasa mwisho wake ulikuwa umedhihiri. Hakuwa tayari kulikubali hilo. Kwa nguvu zake zilizosalia alijitahidi kujiinua kutoka pale chini ili aukwepe umauti ule uliokuwa ukimkabili. Hapo ikawa kama ndio amechokoza nyuki, kwani aliangushiwa mapigo makali kutoka kila upande. Alipigwa rungu la nguvu kichwani na akahisi fahamu zikimpotea taratibu.

HAYA JAKA NDIYO YASHAMKUTA YAKUMKUTA! NINI KITAENDELEA?! USIKOSE KUSOMA KESHO SAA TATU ASUBUHI.
 
SEHEMU YA SABA.

Mara alihisi akimwagiwa petroli mwili mzima.
Hah! Nachomwa moto hivi hivi sasa!
Alijikurupusha na kusimama kutoka pale chini, lakini akapigwa ngwara iliyorudisha tena ardhini kwa kishindo huku akisikia lile kundi la watu likiendelea kumpigia mayowe ya jazba. Akajua kuwa sasa mwisho wake ulikuwa umedhihiri. Hakuwa tayari kulikubali hilo. Kwa nguvu zake zilizosalia alijitahidi kujiinua kutoka pale chini ili aukwepe umauti ule uliokuwa ukimkabili. Hapo ikawa kama ndio amechokoza nyuki, kwani aliangushiwa mapigo makali kutoka kila upande. Alipigwa rungu la nguvu kichwani na akahisi fahamu zikimpotea taratibu.
“Lete kibiriti upesi tumuwashilie mbali kimburu huyu!” Sauti yenye jazba iliamuru.
Na mara hiyo lilitokea gari na kumulika lile eneo kwa taa zake kali. Jaka alihisi kuwa aliweza kuusikia mvumo wa gari hilo ila fahamu zilikuwa zinamhama kwa kasi. Taa za gari lile ziliwamulika wale watu waliokuwa tayari wameshawasha mwenge kwa makaratasi na kipande cha mti ili wamchome moto "kibaka" yule. Walipoona kuwa wamemulikwa na taa za lile gari, wale watu walitimua mbio na kumuacha Jaka pale chini akipigania fahamu zake zisimtoke.
Ukungu mzito ulitanda mbele ya macho yake. Alijitahidi kutambaa kwa tumbo kuliendea lile gari lakini hakujua iwapo alikuwa anafanikiwa au alikuwa akiendelea kujigaragaza tu pale pale alipokuwa. Aliona mlango wa lile gari ukifunguka karibu sana pale alipokuwa na akashindwa kuelewa kuwa hiyo ilitokana na juhudi zake za kulisotea lile gari au ni kutokana na lile gari kumsogelea yeye pale alipokuwa akigaragara.
“Msss...aaadah!”
Aliona miguu ya mtu ikikimbia kuelekea pale alipokuwa amelala...hakuweza kuelewa iwapo ilikuwa ni miguu ya mwanamke au mwanaume, lakini hakujali. Kiza kilikuwa kinazidi kuyafunika macho yake naye alikuwa akijitahidi kutazama kule ile miguu ilipokuwa inatokea...au alipohisi kuwa inatokea, lakini ilikuwa ni kazi ngumu mno.
Kitu cha mwisho alichoweza kukisikia, au kwa lugha fasaha, alichoweza kukinusa, kilikuwa ni harufu nzuri ya uturi, na baada ya hapo alijihisi akitumbukia kwenye shimo refu lenye kiza kinene....
Alipoteza fahamu.
____________________

Clara Wilfred Mashauri Zaza alikuwa ni mwanadada aliyeumbwa, akaumbika. Si kama hakukuwa na wasichana wengine ambao wangeweza kupewa sifa kama hiyo. La hasha. Bali Clara alikuwa ni miongoni wa wale waliokuwa matawi ya juu kabisa katika kundi hilo.
Alikuwa mrefu. Urefu ambao ni athari ya kizazi chake ambacho hakikuwa cha kitanzania halisi bali chenye mchanganyiko wa damu ya kitanzania na ya kizungu. Ni mchanganyiko wa mbali kidogo na Clara mwenyewe hakupenda kabisa kujinasibisha na mchanganyiko huo. Badala yake alipenda kutambulika kama mtanzania halisi, na hivyo ndivyo alivyojitahidi kuyaweka maisha yake.
Mama yake Clara ndiye hasa aliyekuwa na mchanganyiko huu wa mzungu-mtanzania.
Joanna Salvatori alikuwa ni mwanamke ambaye baba yake alikuwa mzungu wa damu kabisa kutoka Italia aliyeitwa Rocco Salvatori. Rocco aliamua kuoa binti mzuri wa kizaramo na kuhamia kabisa Tanzania.Wakati huo Tanzania ilikuwa bado iko katika makucha ya wakoloni na mzee Rocco Salvatori alikuwa akimiliki shamba kubwa la mkonge kule Tanga. Jinsi alivyokutana na binti huyo wa kizaramo haijulikani, lakini alimpenda na kumjali sana mke wake huyo.
Hawa ndio waliomzaa mtoto Joanna ambaye ndiye akaondokea kuwa mama yake Clara.
Joanna alijaaliwa vitu vitatu; urefu, ambao aliurithi kutoka kwa baba yake mzee Rocco Salvatori, weupe ambao uliuzidi hata ule wa baba yake, na busara ya hali ya juu.
Wazazi wake hao walifariki katika ajali mbaya ya ndege wakati wakirejea Tanzania kutoka Uingereza ambako mzee Rocco Salvatori alikwenda kwa matibabu ya ini, na Joanna akajikuta ameachiwa utajiri mkubwa sana, utajiri ambao uliambatana na jukumu la kumlea mdogo wake wa kiume aliyeitwa Deogratius.
Pamoja na huzuni kubwa iliyowakumba yeye na mdogo wake kutokana na vifo vya wazazi wao, msichana Joanna hakutetereka hata kidogo. Hekaheka za kuanzishwa kwa siasa za vyama vingi zilipokuwa zinazidi kupamba moto nchini Tanzania, Joanna alimuuuzia tajiri mmoja wa kiarabu shamba la marehemu baba yao ambalo lilikuwa ni sehemu ya urithi wao kwa pesa nyingi mno kisha akamchukua mdogo wake na pamoja wakaenda Uingereza ambako ndiko alipokuwa akipatia elimu yake kabla ya kuondokewa na wazazi wao.
Joanna alitunisha akaunti aliyofunguliwa na baba yake kule Uingereza alipokuwa akisoma katika benki maarufu ya Barclays kwa kuweka fedha nyingi alizopata baada ya kuuza shamba lao la urithi. Baada ya hapo yeye na mdogo wake wakaondoka Uingereza kuelekea Parlermo, mji mkuu wa kisiwa cha Sicily, kilichopo Italia ya kaskazini, kwa jamaa za baba yao.
Baada ya uchaguzi wa kwanza wa vyama vingi kuisha na hali kuonekana kuwa shwari Joanna alirejea Tanzania na kuanza biashara ya madini kutoka Tanzania kwenda nchi mbali mbali za ulaya na uajemi. Ni katika kipindi hiki ndipo alipokutana na kijana wa kisukuma aliyeitwa Wilfred Mashauri Zaza ambaye pia alikuwa akijishughulisha na biashara hiyo. Wilfred Mashauri Zaza alikuwa akitoa madini kama dhahabu, rubi na almasi kutoka sehemu za Magu, Nyarugusu na nyinginezo na kuziuza kwa wahindi na wafanya biashara wakubwa ambao waliziuza nje ya nchi.
Baada ya kukutana na Joanna, Wilfred alianza kuwasilisha madini yote aliyokuwa akikusanya huko vijijini kwenye machimbo na kuikabidhi kwa Joanna ambaye aliyasafirisha nje ya nchi. Biashara hiyo ilikuwa na kuwapatia faida kubwa wote wawili.
Mwaka huo huo Joanna na Wilfred waliacha biashara ile ya madini ambayo ilikuwa imeshaingiliwa na wafanyabiashara wengi zaidi na kuifanya biashara hiyo kuwa ya mazingira ya hatari. Ni katika mwaka huo huo ndipo walipofunga ndoa na kufungua kampuni nyingine iliyojishughulisha na usafirishaji wa bidhaa mbali mbali ndani na nje ya nchi .
Wakiwa na utajiri wa kutosha na hamu ya kutulia katika maisha ya raha kama mke na mume, Joanna na Wilfred walipagawa kwa furaha pale Joanna alipopata ujauzito mwaka mmoja baada ya ndoa yao. Ujauzito ule nusura umpotezee uhai Joanna kwani ulimpa taabu sana. Kutokana na matatizo ya ujauzito ule Joanna alijifungua mtoto wa kiume kwa taabu mno, mtoto ambaye alijaaliwa kuishi kwa siku nne tu kabla ya kufariki dunia.
Hilo lilikuwa ni pigo kubwa sana kwao.
Tangu hapo afya ya Joanna haikuwa nzuri tena. Kutokana na ukubwa wa tatizo la afya yake ya uzazi, madaktari bingwa kadhaa waliwashauri kuwa ni bora Joanna afunge kizazi kabisa kwa usalama wa maisha yake, kwani kulikuwa kuna uwezekano mkubwa sana wa kupoteza maisha iwapo angejaribu kuzaa tena.
Wilfred alikubaliana moja kwa moja na wazo la daktari. Hakuwa tayari kumpoteza mke wake kipenzi, hata kwa gharama ya kukosa mtoto maishani.
Joanna hakukubaliana asilani na wazo hilo.
Ndoto yake kubwa maishani ilikuwa ni kuchuma mali ya kutosha kisha apate watoto wa kutumia na kuiendeleza mali ile. Kwa sababu mali tayari walikuwa nayo, lililobaki ilikuwa ni kupata watoto, na hili ndilo Joanna alilolitaka kuliko kitu kingine chochote hapa duniani kwa wakati ule.
Ingawa hiyo pia ilikuwa ndiyo ndoto ya Wilfred, hakuweza kabisa kuvulia wazo la kumpoteza mke wake mpenzi, hivyo alijaribu bila ya mafanikio kumshawishi Joanna kutekeleza ushauri wa daktari.
Joanna hakubadili msimamo wake juu ya hilo.
Miaka mitatu baadaye Joanna alifanikiwa kwa taabu sana kujifungua mtoto wa kike waliyemwita Clara. Kinyume na moja ya hofu zao, mtoto Clara alikuwa na afya nzuri na kila dalili za kuishi zaidi. Ila hofu yao ya pili hawakuweza kuitoa. Afya ya Joanna ilikuwa mbaya sana baada ya kujifungua mtoto yule.
Joanna Salvatori alifariki dunia miezi miwili baadaye, akimuachia Wilfred mtoto Clara akiwa na miezi miwili tu tangu aje duniani.
Kifo cha Joanna kilikuwa ni pigo kubwa sana kwa Wilfred, kwani Joanna alikuwa ndiyo familia yake pekee. Wakati alitarajia kukuza familia hiyo kwa kuzaliwa kwa Clara, matarajio hayo yalifutwa kabisa na kifo cha mkewe mpenzi. Na ni hapo ndipo kwa uchungu mwingi alipoamua kuwa familia yake iliyobaki itakuwa ni shemeji yake Deogratius ambaye walielewana sana, na mwanae Clara.
Hakutaka tena kuoa maishani mwake.
Mwaka mmoja baadaye Wilfred alibadili jina la kampuni yao kutoka The Continental Freighters na kuwa Zaza Cargo Movers na kuhamishia makao makuu ya kampuni hiyo Dodoma ambapo alinunua nyumba nzuri katika eneo la uzunguni.
Yeye alihamia Dodoma na mwanae Clara na shemeji yake Deogratius Rocco Salvatori alibaki jijini Dar es Salaam ambako alikuwa meneja wa tawi la kampuni yao ya Zaza Cargo Movers.
Wilfred Mashauri Zaza alibaki kuwa Mkurugenzi Mtendaji wa kampuni hiyo.
____________________

Mtoto pekee na kipenzi cha mzee Wilfred Mashauri Zaza alikuwa ni msichana mpole na mara nyingi alionekana mpweke, kitu ambacho kwa namna ambayo haikuwa rahisi kuielezea, kilimfanya azidi kuonekana mrembo. Sura yake nyembamba ilikuwa na macho madogo yenye kope ndefu na za kupendeza. Pua yake ndogo na nyembamba ilikuwa ndefu zaidi ya pua za wabantu wengi, ila mdomo wake mdogo ulikuwa umejaa kibantu hasa na hivyo kumfanya awe na sura ya kuvutia mno.
Kidevu chake kilikuwa kimechongwa mithili ya ncha ya yai. Kichwa kilichobeba urembo wake ule kilikuwa kimebebwa na shingo ndefu na nyembamba, shingo ambayo ilikiunganisha kichwa kile na kiwiliwili ambacho kilimfanya awe na umbo la namba nane.
Ingawa Clara hakuwa mnene, mwili wake ulikuwa umejaa vyema. Matiti yake ya wastani yaliyoweza kuwapendeza mwanaume wengi yalitulia vyema kifuani kwake na tumbo lake la ubapa lilitambaa vizuri na kuishia kwenye kiuno chake chembamba kilichotenganisha sehemu ya juu na ile ya chini ya mwili wa kiumbe huyu mrembo.
Mapaja yake yaliyojaa vizuri na yalifanya miinuko ya kuvutia katika kila upande wa nje wa miguu yake, kama kwamba alikuwa ameshindilia bastola kubwa kila upande wa mapaja yale.
Wengi wangeweza kusema kuwa Clara alikuwa mweupe kwa rangi, weupe uliofanywa utokeze zaidi kutokana na nywele zake ndefu, laini na nyeusi mno.
Basi huyo ndiye Clara Zaza.
Elimu yake yote, tangu chekechea hadi Chuo Kikuu aliipatia Nairobi nchini Kenya, ambapo alisomea katika shule za kimataifa katika madarasa ya chekechea, msingi na sekondari kabla ya kujiunga na Chuo Kikuu cha Nairobi.
Baada ya kufaulu vizuri shahada yake ya Uongozi na Uhusiano wa kimataifa katika Chuo Kikuu cha Nairobi, aliamua kurudi Tanzania kumsaidia baba yake kuongoza Kampuni yao.
Akiwa na umri wa miaka ishirini na sita, Clara ndiye alikuwa meneja mkuu mdogo kuliko wote, wa kampuni maarufu ya usafirishaji katika afrika ya mashariki yenye makao yake makuu mjini Dodoma, nchini Tanzania. Kampuni ya Zaza Cargo Movers.
____________________

Clara alikuwa akitabasamu peke yake huku aliendesha gari lake kubwa na ghali aina ya Jeep Cherokee.
Alikuwa akirejea nyumbani kwake eneo la uhindini akitokea kwenye tafrija ya kuwaaga wafanyakazi wa Zaza Cargo Movers waliokuwa wanastaafu kutokana na umri mkubwa. Tafrija hiyo ilikuwa imefanyikia katika ukumbi wa maarufu wa Dodoma Hotel naye kama meneja mkuu wa Zaza Cargo Movers aliwajibika kuhudhuria hafla hiyo.
Hata hivyo hilo silo lililomfaya awe akitabasamu peke yake garini usiku ule. Ni mawazo yaliyokuwa yakipita kichwani mwake ndiyo yaliyomfanya ajikute akitabasamu namna ile.
“Well...that's my daddy!” Hatimaye alisema kwa sauti na kuangua kicheko kikubwa, akikumbukia vituko vya baba yake.
Kila anapofikiria jinsi baba yake alivyokuwa akijitahidi kumlea kama yai hadi wakati ule ambao yeye ameshafikia umri wa kujiamulia mambo mengi mwenyewe hujikuta aidha akitabasamu peke yake au akicheka kabisa.
Alicheka tena kwa sauti ya chini na kutikisa kichwa huku akiendelea na safari yake.
Baada ya kukabidhi zawadi na hundi za fedha kwa wastaafu wa kampuni yao usiku ule, yeye aliaga na kuwaomba wafanyakazi na wageni waalikwa waliohudhuria hafla ile waendelee na sherehe waliyoandaliwa kisha yeye na baba yake wakatoka kurejea nyumbani.
“Una hakika hutaki kulala nyumbani kwetu leo, dear?” Mzee Zaza alimuuliza bintiye huku wakishuka ngazi za pale hotelini taratibu kuyaelekea magari yao.
“ery sure...baba, si nimekwambia kuwa leo n’talala nyumbani kwangu?" Clara alimjibu baba yake huku akitasamu.
"Sawa...lakini pale pia ni nyumbani kwako dear, unaweza kuja wakati wowote."
"Na pia naweza nisije wakati wowote vile vile, au sio dad?" Clara aliendelea kumkorofisha baba yake.
"Clara dear, unajua jinsi gani najisikia nikifikiria..."
"Yeah, yeah, najua...mtoto wa kike, peke yangu kwenye nyumba, sijaolewa, blah,blah,blah...Baba! Si nimekwambia tangu mwanzo tu kuwa leo nitalala nyumbani kwangu?"
"Sawa...lakini na mimi pia si nimekwambia kuwa nyumbani kwangu kwa hakika ni nyumbani kwako, Clara...?"
"I know dad, lakini na wewe lazima ukubali kuwa sasa mimi ni msichana mkubwa na I can take care of myself! Besides, sehemu kubwa ya maisha yangu nimekuwa nikiishi peke yangu tu, yaani boarding school tena nje ya nchi, you shouldn't worry about me that much dad..." Clara alimbishia baba yake, akimsisitizia kwa kizungu kuwa kwa umri aliofikia anaweza kujitunza.
“Yeah…labda hiyo ndiyo sababu sasa nataka niwe karibu na wewe dear, nifidie kwa muda wote huo uliolazimika kukaa peke yako nje ya nchi ukiwa masomoni...?” Mzee Zaza alimwambia bintiye kwa kimombo.

ITAENDELEA
 
SEHEMU YA NANE

"Yeah, yeah, najua...mtoto wa kike, peke yangu kwenye nyumba, sijaolewa, blah,blah,blah...Baba! Si nimekwambia tangu mwanzo tu kuwa leo nitalala nyumbani kwangu?"
"Sawa...lakini na mimi pia si nimekwambia kuwa nyumbani kwangu kwa hakika ni nyumbani kwako, Clara...?"
"I know dad, lakini na wewe lazima ukubali kuwa sasa mimi ni msichana mkubwa na I can take care of myself! Besides, sehemu kubwa ya maisha yangu nimekuwa nikiishi peke yangu tu, yaani boarding school tena nje ya nchi, you shouldn't worry about me that much dad..." Clara alimbishia baba yake, akimsisitizia kwa kizungu kuwa kwa umri aliofikia anaweza kujitunza.
“Yeah…labda hiyo ndiyo sababu sasa nataka niwe karibu na wewe dear, nifidie kwa muda wote huo uliolazimika kukaa peke yako nje ya nchi ukiwa masomoni...?” Mzee Zaza alimwambia bintiye kwa kimombo.
“Aah, hiyo imeshapita tena baba…na unajua mie nashukuru sana kwa hilo? Kuweza kuishi peke yangu ugenini.... kujifunza kufanya maamuzi mengi mwenyewe. Hiyo ni zawadi kubwa kwangu baba. Just you be happy for me dad, okay?” Clara alimjibu babiye, akiongezea kwa kimombo kuwa awe na furaha kwa ajili yake.
“Okay, okay...ni sawa dear, nimekuelewa....nitajitahidi kuelewa, okay?” Mzee Zaza alisalimu amri kwa shingo upande.
“Okay...Goodnight dad." Clara alikatisha mazungumzo yale huku akimbusu shavuni baba yake.
“Goodnight baby... sleep tight."
Clara aliendelea kutabasamu peke yake huku akikumbukia mjadala ule baina yake na baba yake, akiwa ndani ya ile Jeep Cherokee yake yenye rangi nyekundu.
“Mnhu! Yaani baba mpaka leo bado ananiona mimi mtoto mdogo tu!” Alijisemea peke yake huku akiizungusha Jeep Cherokee yake kiufundi kwenye mzunguko wa Jamatini pale Dodoma mjini. Alifuata barabara inayoelekea Dar es Salaam na kukata kushoto kuingia kwenye mtaa mfupi uliopo baina ya ofisi ya Mamlaka ya Ustawishaji Makao Makuu (CDA) na hoteli maarufu ya Nooreen. Mtaa ule mfupi ulimpeleka mpaka kwenye njia panda ya msikiti maarufu wa Nunge pale mjini. Hapo aliingia kulia ili atokee kwenye barabara inayoelekea Uhindini ikitokea maeneo ya ukumbi wa disko wa NK ambapo angekata kushoto na kuelekea zake Uhindini.
Na hapo mawazo yake yote yalikatika ghafla mara alipoona kundi la watu likiwa katikati ya barabara mbele yake, wengine wakiwa wameshika mienge na silaha mbali mbali. Roho ilimlipuka na wazo lililomjia kichwani mwake wakati ule ni kwamba wale walikuwa ni majambazi waliojaa barabarani makusudi ili asimame wapate kumpora gari na mali nyinginbe zozote atakazokuwa nazo mle garini.
Woga mkubwa ukamshika, akikumbukia tukio jingine baya la kuvamiwa na vibaka lililowahi kumtokea maishani mwake.
Alianza kujilaumu kwa nini hakukubali kulala nyumbani kwa baba yake usiku ule huku akipata wazo la kugeuza gari kwa kasi na kutokomea kwa njia nyingine. Lakini kabla hajatekeleza wazo lake hilo alishangaa kuona wale watu wakitimua mbio, wakimuacha mtu mwingine akigaragara pale barabarani.
Mara moja alielewa kilichokuwa kimetokea. Bila shaka yule mtu alikuwa amepigwa na kaporwa pesa zake zote na majambazi wale.
Sijui wamemuua...?
Bila kujishauri zaidi alisogeza gari lake hadi karibu na pale alipokuwa yule mtu na akaona kuwa yule mtu alijaribu kujiinua kutoka pale chini lakini alishindwa. Akiwa amepata imani kuwa yule mtu alikuwa hai, Clara alizidi kumsogelea kuona kama angeweza kumsaidia kwa angalau kumpeleka hospitali. Alisimamisha gari karibu na yule mtu na kuchungulia huku na huko kutokea mle garini. Kote kulikuwa kimya, hakukuwa na dalili ya wale watu waliokuwa wakimpiga yule mtu. Aliteremka haraka na kukimbilia pale chini alipolala yule mtu.
Alipiga goti moja kando yake na kumtazama kwa makini zaidi. Alimuwekea mkono kifuani na kusikiliza mapigo ya moyo, na hapo harufu kali ya petroli ikazishambulia pua zake na akagundua kuwa nguo za yule mtu zilikuwa zimemwagiwa petroli.
Walitaka kumchoma moto! Ndio maana walikuwa wameshika ule mwenge, wauaji wakubwa!
Mwili ulimsisimka kwani alielewa kuwa asingetokea eneo lile wakati alipotokea, basi yule mtu angechomwa moto!
“Loh! watu wanawezaje kuwa wakatili kiasi hiki jamani!” Aliwaza kwa mshangao ulichanagnyika na huzuni.
Hapo wazo jingine likamjia. Ni wezi tu ndio waliokuwa wakichomwa moto siku hizi hapa nchini.
“Au huyu mtu ni mwizi?"
Aliamua kumuangalia kwa makini zaidi kama aliyetaka kujihakikishia kuwa yule mtu hakuwa mwizi. Alimgeuza uso wake uliokuwa umelalia upande mmoja na kumtazama usoni.
Khah!
Moyo ilimlipuka vibaya sana alipoiona sura ya yule mtu. Mara moja alijua kuwa aliwahi kuiona sura ile sehemu fulani, wakati fulani. Lakini kwa nini moyo ulimlipuka kiasi kile? Kwa pale alipokuwa amepiga goti alikuwa ameupa mgongo mwanga wa taa za gari lake na hivyo sura ya yule mtu ilikuwa imezibwa na kivuli chake. Alisogea pembeni na mwanga wa taa za gari lake ukammulika moja kwa moja usoni yule jamaa.
Naam. Sasa alimkumbuka yule mtu, na hakuwa na shaka kabisa juu ya hilo.
Alikuwa ni yule mtu wa ajabu aliyemsaidia na kuokoa maisha yake siku nyingi zilizopita katika jiji la Dar es Salaam.
E bwana we!
Ingawa sasa alionekana mwembamba zaidi, Clara aliweza kumkumbuka bila shaka hata kidogo. Asingeweza kuisahau kabisa sura ya yule mtu hata angemuona wapi na katika mazingira gani. Tangu siku ile alipomuacha pale kituo cha polisi akigaragazwa na wale askari, akili yake haikuweza kuacha kumfikiria yule mtu.
Mara kwa mara amekuwa akirejewa na mawazo kuhusu yule mtu, akijaribu kujiuliza ni masahibu gani yaliyomkuta yule kijana bila ya kufanikiwa kupata jibu maridhawa. Naye hakutegemea kabisa kuonana naye tena maishani.
Na sasa bila ya kutegemea kabisa anamuona tena yule jamaa, tena katika mazingira yale yale ya ajabu kama jinsi alivyokutana naye kwa mara ya kwanza kiasi cha mwaka moja uliopita kule jijini Dar!
Akili ilikuwa ikimzunguka kwa kasi sana. Ilibidi apitishe uamuzi haraka kabla wale watu hawajarudi kuja kummalizia kabisa kijana yule wa ajabu.
Wazo alilokuwa anajitahidi kushindana nalo ni la kumuacha pale pale alipo nae ashike hamsini zake akamwombee tu kwa mungu labda atamjaalia kuokoka kutokana na madhila makubwa ya kidunia yaliyoelekea kumuandama kijana yule.
Akili yake ilimwambia kuwa kwa vyovyote yule kijana naye alikuwa ana mambo yake ambayo si mema. Yule Sajenti wa polisi siku ile mwaka mmoja uliopita alisema kuwa kwa kosa alilofanya adhabu ya kunyongwa tu ndiyo ingemfaa. Clara hakuwa mjinga, hivyo alijua kuwa kuna makosa machache sana hapa nchini yanayostahili adhabu ya kunyongwa, na kubwa miongoni mwa hayo ni kosa la mauaji...
Sasa niondoke au...?
Moyo wake ulimuwia uzito sana kumuacha yule jamaa namna ile pale barabarani.
Kwani mimi amenifanyia ubaya gani?
Hakuna alichonifanyia ila ni wema tu...tena kwa kujihatarishia maisha yake katika kujaribu kuniokoa mimi kutoka mikononi mwa wauaji ambao bila shaka wangeweza hata kunibaka!
Na kama na yeye pia alikuwa ni muuaji, angeshindwa nini kuwaacha tu wale watu wanifanye watakavyo naye akashika hamsini zake?
Tena kwa sababu ya kunisaidia mimi, mtu ambaye hanijui nami simjui, ndio akashikwa na wale polisi ambao bila shaka alikuwa ameshawatoroka...nao wakampa kipigo kizito na sijui amekutwa na mambo mangapi mengine hadi leo hii nakuja kumkuta hapa katika hali kama hii...!
Hata!
Haiwezekani, lazima nimsaidie. Kama yeye alikubali kunisaidia mimi bila kujali iwapo angeweza kupoteza maisha yake katika kufanya hivyo, basi na mimi leo ndio nafasi yangu ya kumlipa kwa wema alionifanyia....
Bila kuchelewa zaidi, Clara alijitahidi kumzoazoa yule jamaa kutoka pale chini na kumburura kuelekea kwenye gari lake. Alipofika usawa wa mlango wa nyuma wa gari lile alimlaza chini na haraka akawahi kufungua mlango ule. Kwa taabu aliweza kulaza kichwa na sehemu ya juu ya kiwiliwili cha mtu yule, ambaye muda wote huo alikuwa amepoteza fahamu, kwenye kiti cha nyuma cha gari lile na kuacha sehemu ya chini ya kiwiliwili chake ikining'inia nje.
Huku akitweta na moyo ukimwenda mbio alikimbia kuzungukia upande wa pili wa gari lile na kufungua mlango wa nyuma wa upande ule na kuingia kwenye kiti cha nyuma cha gari lile. Akiwa kwenye kiti kisafi cha gari lake aliyoipenda sana, alipitisha mikono yake chini ya makwapa ya yule mtu na kuuvutia ndani ya gari mwili wote wa yule mtu na kumlaza chali pale kitini.
Aliteremka mbio-mbio na kuufunga ule mlango na moyo wake ukapiga sarakasi aliposikia sauti za watu zikielekea pale alipokuwa. Aligeuka kule zile sauti zilipokuwa zinatokea, na akaona kundi la watu likitokea upande wa ukumbi wa disko wa NK likielekea pale aliposimama huku wakiwa wameshika kitu kama mwenge. Miguu ikamwisha nguvu na akatamani atimue mbio aache gari na yule mtu pale pale, lakini alijipa moyo kuwa bado wale watu walikuwa mbali naye. Alikimbia haraka na kuzunguka upande wa pili wa gari na kuubamiza kwa nguvu mlango wa pili wa nyuma wa gari lake na kujitupa nyuma ya usukani na kutazama mbele.
Wale watu walianza kutimua mbio kuelekea kule kule alipokuwa huku wakimpigia kelele!
Duh!
Huku akitetemeka aliingiza gia na kukanyaga mafuta kwa nguvu zake zote. Gari lilivuma kwa nguvu lakini halikusogea hata kidogo!
Heeeh!
Clara alichanganyikiwa. Kwa nini gari halitaki kwenda tena? Aliinua macho na kuwatazama wale watu waliokuwa wakimwendea kwa kasi huku wakipiga mayowe yaliyoashiria kuua watu tu. Sasa aliwaona kwa ukaribu kuwa walikuwa wameshika marungu, fimbo, mapanga na wengine wakaanza kumrushia mawe.
Alikanyaga tena mafuta na kwa mara nyingine gari likavuma bila kwenda popote.
Jiwe kubwa likatua juu ya boneti la gari lake na yowe kubwa likamtoka, taharuki ikimtawala.
"Let's go goddammit! Move! " Alifoka kwa kuchanganyikiwa huku akijaribu tena kukanyaga mafuta ili gari liondoke, na gari likazidi kuvuma tu bila kusogea hata kidogo. Wale watu walizidi kuwakaribia huku wakizidi kupiga mayowe na jiwe jingine likajikita juu ya paa la gari lake.
Clara aliona nguvu zikimwishia hivi hivi. Jasho lilikuwa likimtiririka usoni na makwapani huku moyo wake ukitishia kuchomoka kutoka kifuani kwake kwa jinsi ulivyokuwa ukirukaruka kwa kasi isiyo ya kawaida.
"Sasa ni nini tena...jamaniii !" Alilalama huku akikanyaga tena mafuta. Gari bado liliendelea kuvuma likiwa palepale!
Alianza kulia kwa sauti kama mtoto. Aliinama na kutazama chini ya usukani kuhakikisha iwapo ufunguo ulikuwapo lakini alijua kuwa hilo si tatizo kwani taa za gari zilikuwa zinawaka na hivyo gari lilikuwa linafanya kazi vizuri. Sasa ni nini? Alipeleka mkono kwenye gia, na hapo moyo wake ukanywea alipogundua kosa lake.
Ah, bloody fool me!
Katika kiherehere cha kutimua mabio kutoka eneo lile, alikuwa ameweke gis kwenye “neutral” badala ya kwenye “drive”!
"Pumaaaaaaaaavvvv!" Alipiga kelele huku akihamishia gia kwenye sehemu ya “drive” na akikanyaga
breki na kuiachia huku akihamishia mguu kwa nguvu kwenye ile pedeli ya mafuta. Wale watu walikuwa kiasi cha hatua zipatazo kumi kutoka pale alipokuwa. Jeep Cherokee iliruka mbele kwa kasi kama jiwe lililoachiwa kutoka kwenye manati iliyovutwa kisawa sawa. Iliwaelekea kwa kasi mbaya wale watu waliokuwa na nia ya kuua. Jamaa walitawanyika na kuruka pembeni, kila mtu kwa uelekeo wake wakihofia kugongwa huku wakipiga mayowe ya woga na ghadhabu.
Clara alisikia mayowe na kelele zao alipowapita kwa kasi, wakimtukana na kumlaani kwa hasira. Yeye hakujali, aliongeza kasi huku machozi na kamasi vikimvuja bila mpangilio na moyo ukimdunda kwa mguvu. Alikata kona kwa kasi na kutimua vumbi zito, gari ikaserereka huku tairi zikitoa mlio wa malalamiko kabla ya kutulia barabarani sawia.
Kwa mara nyingine jiwe likatua juu ya paa la gari lake, naye akakanyaga mafuta zaidi. Jeep Cherokee iliunguruma kwa nguvu na wale watu waliokuwa wamepandwa jazba ya kuua waliambulia kukodolea taa nyekundu za gari lile zikitokomea katikati ya vumbi na kiza cha usiku ule.
_____________________

Jaka alifumbua macho taratibu na hapo hapo akayafumba baada ya kukutana na mwanga mkali wa taa. Kichwa kilikuwa kikimgonga kwa mbali na alihisi maumivu kwenye ubavu wake wa kulia. Aliendelea kulala kimya huku akiwa amefumba macho akijaribu kukumbuka kilichokuwa kimemtokea hata akawa amelala pale.
Kwamba pale hapakuwa nyumbani kwa mjomba wake Mnyaga lilikuwa wazi kabisa akilini mwake, kwani kitanda chake cha Makole hakikuwa na godoro laini namna ile. Aidha, kwa mzee Mnyaga hakukuwa na taa ya umeme hata moja kama ilivyo pale alipojikuta akiwa amelala muda ule.
Aliweza kukumbuka kuzongwa na watu wengi...na kumuona tena yule jamaa aliyeitwa Tony...
Ndiye haswa.
Tony...mzee wa You know what I am sayin'?
Tony...mshenzi wa tabia!
Alihisi maumivu mengine kwenye ugoko wake wa kushoto, na taratibu aliukunja mguu wake na kuupapasa ugoko wake, na kugundua kuwa ulikuwa umefanya uvimbe kidogo.
Kipigo.
Alikumbuka kuwa alipigwa sana. Hakuweza kukumbuka ni nani hasa aliyempiga...ila alikumbuka kuchezea kipigo kikali, na kumwagiwa petroli yenye harufu kali...
Hakukumbuka kitu kingine zaidi kuhusiana na tukio lililosababisha yeye kuwa pale wakati ule...
Hapana. Alikumbuka kuona taa za gari zikielekea kumgonga wakati yeye akiwa anagaragara barabarani, kisha akakumbuka kufikiwa na harufu nyingine, sio ya petroli, bali ya uturi mzuri wa kupendeza... kisha kote kukawa kiza.

NINI KINAENDELEA HAPA?!
 
SEHEMU YA TISA

Alikumbuka kuwa alipigwa sana. Hakuweza kukumbuka ni nani hasa aliyempiga...ila alikumbuka kuchezea kipigo kikali, na kumwagiwa petroli yenye harufu kali...
Hakukumbuka kitu kingine zaidi kuhusiana na tukio lililosababisha yeye kuwa pale wakati ule...
Hapana. Alikumbuka kuona taa za gari zikielekea kumgonga wakati yeye akiwa anagaragara barabarani, kisha akakumbuka kufikiwa na harufu nyingine, sio ya petroli, bali ya uturi mzuri wa kupendeza... kisha kote kukawa kiza.
Taratibu alifimbua macho na kuanza kukichunguza kile chumba alichokuwamo.
Kilikuwa na ukubwa wa wastani chenye dari nyeupe ya zege. Kwenye dari la chumba kile taa ndefu ya muanzi ilikuwa inawaka. Kuta za chumba kile zilikuwa zimepakwa rangi ya buluu bahari na ufito mwembamba wa rangi nyekundu kwa chini. Kitanda alichokuwa amelalia kilikuwa kimewekwa kwenye kona ya chumba kile, kikiwa chini ya dirisha moja kushoto kwake, wakati dirisha jingine likiwa kwenye ukuta uliokuwa upande ambao kichwa chake kilikuwa kimeelekea. Madirisha yote yalikuwa yamefunikwa kwa mapazia mazito ambayo yalisababisha mle ndani kuwe na kiza kilichoufanya mwanga wa ile taa iliyokuwa inawaka mle ndani uonekane kuwa ni mkali sana.
Ukuta uliokuwa mbele yake ulikuwa umepambwa kwa picha za wasanii mbali mbali wa filamu na muziki wa ndani na nje ya nchi. Mbele ya ule ukuta uliotapakaa picha za wasanii wale maarufu kulikuwa kuna meza ya kuandikia na kiti, ambapo juu ya meza ile Jaka aliona kompyuta mpakato na vitabu kadhaa.
Jaka akaguna, na wasiwasi ukampanda.
Muda wote ule alikuwa akihisi kwamba alikuwa kwenye wodi ya hospitali fulani, lakini zile picha pale ukutani na ile meza iliyokuwa na komyuta juu yake vilimhabarisha kuwa pale hapakuwa hospitali bali ni nyumbani kwa mtu.
Ni nani?
Ni mtu mwema au mwovu?
Ana nia gani na yeye hata akamuweka kwenye chumba kile kizuri na kisafi namna ile?
Ni wapi?
Akapeleka macho yake kwenye ukuta uliokuwa kulia kwake ambako ndiko kulikuwa kuna mlango wa kuingilia na kutokea ndani ya chumba kile na kuachia mguno wa fadhaa huku moyo ukimlipuka, kwani saa kubwa ilikuwa imetundikwa juu ya mlango ule ilikuwa inamwambia kuwa muda ulikuwa ni saa tano na robo!
Alitakiwa akaripoti kituo cha polisi!
Mungu wangu, leo Mgunya ataua!
Alikurupuka kutaka kutoka pale kitandani lakini alipambana na maumivu makali kifuani na kwenye mbavu. Alitoa mguno wa maumivu na kujilaza tena chali pale kitandani huku akigeuzia kichwa chake kwenye ukuta uliokuwa pembeni ya mlango wa chumba kile.
Na ndipo alipomuona.
Alikuwa amekaa kwenye kochi lililokuwa kando ya mlango ule hali miguu yake akiwa ameikunja na kuipandisha kwenye kochi lile na kuilaza kulia kwake na hivyo kufanya kiwiwliwili chake cha juu kulalia kushoto huku uzito wake ukiuegemea mkono wake wa kushoto ambao ulifanya "mbinu".
Alipomuona tu Jaka alijua kuwa alishawahi kumuona yule msichana mara kadhaa hapo kabla na alijua alimuona wapi.
Alikuwa ni yule msichana wa kwenye ile ndoto iliyokuwa ikimrudia mara kwa mara!
Mshituko alioupata safari hii ulikuwa mkubwa mno. Bila kujali maumivu yake alijiinua tena kutoka pale kitandani na kuketi huku akiwa amemtumbulia macho pima yule msichana. Midomo ilimcheza, pua zilimtanuka. Alijaribu kumeza mate akashindwa kwani ghafla koo likamkauka kwa namna ya ajabu kabisa, huku moyo nao ukimwenda mbio haijawahi kutokea.
Mawazo mengi sana yalipita kichwani mwake ndani ya zile sekunde chache ambazo yeye aliziona kama masaa. Alikuwa anaota...? Au alikuwa anaanza kupatwa wazimu?
Au yule mwanamke ni jini?
Yaani ameanza kumjia ndotoni na sasa ameamua kumchukua kabisa na kumleta nyumbani kwake?
Ina maana hapa ndio ujinini au...?
Hapana. Haiwezekani.
Kama haiwezekani hapa ni wapi basi?
Alijua kuwa ile haikuwa ndoto, lakini yule mwanamke....!?
Muda wote huo yule binti alikuwa akimwangalia tu huku akitabasamu.
"Naona umeamka hatimaye...karibu tena duniani kaka..." Hatimaye yule binti aliongea huku akiendelea kutabasamu na kuteremsha miguu yake sakafuni kutoka kwenye kochi.
Sauti!
Ile sauti!
Jaka aliikumbuka ile sauti...!
Alishawahi kuisikia...wapi?
Sasa aliamini kuwa yule msichana alikuwa jini. Alikumbuka kusikia simulizi kwamba miguu ya majini wa aina ile huwa sawa na kwato za punda au farasi. Haraka aliitupia macho miguu ya yule binti.
Ilikuwa ya kibinadamu.
Sasa ni kitu gani?
"Usiwe na wasiwasi wala usiogope..." Yule binti alimwambia kwa upole huku akimsogelea pale kitandani. Jaka aliendelea kumkodolea macho akiwa mdomo wazi.
Naikumbuka hii sauti ...na hii sura...kwa nini?
"Wewe!" Jaka alimaka ghafla, na yule binti akisimama kwa mshituko.
Naam, Jaka alimkumbuka yule binti. Sasa mambo yote yalikuwa yakimjia vizuri akilini mwake.
Yule ndiye haswa binti wa kwenye ile ndoto ya ajabu.
Lakini pia aligundua kitu kingine. Kwa nini siku zote alikuwa akipatwa na hisia kuwa yule binti wa kwenye ile ndoto, aliyekuwa akimuota akimjia na taa na mwamvuli katika usiku wa kiza kizito na mvua kubwa ambayo maji yake ni ya moto, alikuwa amewahi kumuona sehemu fulani kabla ya ndoto ile ingawa hakuweza kukumbuka ni wapi.
Sasa alipata jibu.
Akiwa pale kitandani akimkodolea macho yule binti, akili yake ilirudi nyuma siku nyingi zilizopita, katika mji mwingine kabisa.
Alikumbuka kupamiana na yule msichana kwenye kichochoro kimoja ndani ya usiku mmoja wenye kiza kizito na mvua kubwa. Alikumbuka jinsi yule binti alivyokuwa akimuomba msamaha asimdhuru usiku ule, kabla hawajavamiwa na vibaka wanne na pamoja kujikuta katika wakati mgumu sana...
Ndiye huyu binti aliyejaribu kumsaidia usiku ule wa kiza kizito ndani ya jiji la Dar, na matokeo yake nusura na yeye auawe. Ni huyu msichana ambaye kama asingejitolea kumsaidia usiku ule, hata yeye asingekamatwa tena na polisi na kujikuta akihamishiwa Dodoma chini ya ulinzi mkali na kulazimika kuishi maisha ya kikimbizi ndani ya nchi yake mwenyewe.
Na ndiye huyu huyu aliyekuwa akimuona kwenye ile ndoto ya ajabu.
Sasa tena ni huyu huyu msichana leo hii, kiasi cha kilomita zisizopungua mia nne kutoka kwenye mji aliokutana nae kwa mara ya kwanza, tena katika mazingira ambayo hakuyategemea kabisa, anakutana nae tena kwa namna ile ile ambayo yeye hakuweza kutegemea...na bila shaka ni huyu binti ndiye aliyemuokoa kutoka kwenye kile kipigo kikali cha usiku uliopita...
"Wewe...wewe, una...fanya nini hapa...yaani mbona mimi niko hapa....aa..aaa...namaanisha...nimefikaje... hapa...yaani hapa ni wapi...?" Jaka alibaki akibwabwaja huku akizidi kumkodolea macho yule binti kutoka ndotoni.
"Tulia tu kaka’angu, tulia. Hapa uko salama. Unahitaji kupumzika." Yule binti alimwambia kwa upole huku akimuwekea viganja vya mikono yake laini kifuani na kumlaza tena kitandani. Ndipo Jaka alipogundua kuwa alikuwa amefunikwa shuka zito ambalo alipojiinua liliteremka na kuacha kifua chake kikiwa wazi, lile shuka lilimfunika sehemu ya kiuno kuteremka chini.
"Shati langu liko wapi?" Alimuuliza yule binti kwa wasiwasi huku akifumbata mikono yake kifuani.
"Nguo zako zote zilikuwa hazitamaniki kabisa na wala hazifai tena kuvaliwa..." Yule binti aliendelea kumjibu kwa upole huku akitabasamu.
Nguo zako zote?
Haraka Jaka alipeleka mkono wake chini ya ile shuka na kujipapasa ili kuhakikisha iwapo alielewa sawasawa. Naam, alikuwa ameelewa sawasawa, kwani suruali na nguo yake ya ndani vyote havikuwapo! Alikuwa uchi wa mnyama chini ya lile shula!
Aka!
Alimuinulia uso wa mshangao yule msichana.
“Umenifanya nini kingine wewe, eenh?” Alimuuliza kwa ukali.
Binti hakuonesha kubabaika wala kuwa na wasiwasi juu ya ukali wake.
"Sijakufanya chochote kingine zaidi ya kukuosha mwili mzima...”
“Mwili mzima...?”
“Of Course! Mtu ulikuwa umetapakaa damu, vumbi na umemwagiwa petroli mwili wote... nisingeweza kukulaza hivyo hivyo bila kukusafisha, au we’ unaonaje?" Alimjibu, na kabla Jaka hajaongea lolote aliendelea, "Umepoteza fahamu kwa saa takriban kumi na matatu hivi tangu nilipokukuta umetupwa pale barabarani. Nilidhani hutaamka tena...lakini daktari niliyemleta alisema kuwa ungeamka tu. Ila itabidi upumzike sana..."
Akili ya Jaka ilikuwa inafanya kazi kwa kuruka ruka na hakuweza kuzingatia maneno yote aliyokuwa akiambiwa na yule binti. Alimkumbuka Osman Mgunya.
"Sasa mimi inanibidi niondoke...ni lazima niende....nipe nguo zangu sasa hivi!" Alimaka huku akizidi kujitahidi kuinuka kutoka pale kitandani.
"Uende wapi? We' unahitaji kupumzika sana na unahitaji ule vizuri...huwezi kwenda popote katika hali hiyo. Unaweza kuanguka njiani!" Binti alimpinga vikali.
Jaka alitamani amfokee, amueleze kuwa binti kama yeye hawezi kuelewa kwa nini ni lazima Jaka aende kuripoti kituo cha polisi, na tena asizoee tena kumuuliza kuhusu anataka kwenda wapi.
Lakini alijizuia.
Alijua kuwa yule binti ndiye akiyeokoa maisha yake kutokana na kifo kibaya usiku uliopita.
"Anti sikiliza...kwanza samahani sana kwa kukutolea ukali. Halafu naomba nikushukuru sana kwa msaada wako..."
"Bila samahani kaka. Mimi naelewa kuwa imekuwa vigumu sana kwako kuelewa mambo yote haya...hasa kwa jinsi ambavyo tumekuwa tukikutana kiajabu-ajabu, na kwa nini mimi niamue kukuchukua na kukuleta hapa wakati hatujuani kiasi hicho....nadhani sasa umenikumbuka? Mimi nilikukumbuka jana nilipokukuta ukiwa umetupwa barabarani ndio maana niliamua kukuchukua na kukuleta hapa..." Binti alidakia kabla Jaka hajamaliza kutoa maelezo yake, na kuendelea huku akitabasamu, "...bila ya wewe kujitolea nafsi yako kunisaidia mimi siku nyingi zilizopita kule Dar, bila shaka mimi nisingekuwa hai leo hii."
Jaka alimtazama yule binti na moyo wake ulijaa shukurani. Hakuona kuwa alilolifanya yeye kwa yule binti siku nyingi zilizopita kuwa lilikuwa na umuhimu wowote kulinganisha na yale aliyofanyiwa na binti yule usiku uliopita.
"Asante sana dada...lakini nasikitika kwamba mimi ni lazima niondoke...natakiwa niwe sehemu fulani...ni muhimu sana. Sasa...naweza kupata nguo zangu tafadhali?" Alimwambia kwa upole ili kumfanya yule binti aelewe.
"Ni matatizo yako na polisi, sio?" Binti alimuuliza huku akimkazia macho kwa makini.
Jaka alimtazama machoni kwa muda, kisha akaafiki kwa kichwa.
"Basi nitakupeleka." Binti alimwambia huku akiinuka kujiandaa na safari.
Jaka alilipinga vikali swala hilo lakini yule binti alitoka nje ya chumba kile bila kujali, kama kwamba alikuwa hamsikii. Aliporudi alikuwa ameshavaa viatu vya raba na suruali ya jeans iliyomkaa vyema na fulana kubwa nyeupe iliyokuwa na nembo ya bendera ya Tanzania kifuani. Alipendeza sana. Alimuwekea nguo kando yake pale kitandani.
"Vaa nguo hizi halafu nikupeleke huko unapotaka kwenda, okay?" Alimwambia.
"Sio Okay, kwa sababu sidhani kama ni vyema kwa mtu kama wewe kujihusisha na mimi...We' hujui nimefanya nini mpaka nikapatwa na yale uliyoyaona na kuyasikia pale kituo cha polisi kule Dar...na hujui ni kwa nini nipo Dodoma hivi sasa..." Jaka alimpinga.
"Fanya upesi usije ukachelewa zaidi huko unapotakiwa kwenda." Binti alimhimiza kama kwamba hakuwa amemuwekea pingamizi.
"Sawa, lakini naenda peke yangu...kwani hata nikianguka njiani wewe utaweza kunibeba?" Jaka alimjia juu. Badala ya kumjibu, yule msichana alianza kutoka nje ya chumba na alipofika mlangoni alimgeukia.
"Kwani hujajiuliza jana niliwezaje kukufikisha hapa? Vaa upesi twende mwanamume...mi' nakusubiri hapa nje." Kisha akatoka na kufunga mlango.
"Shit!" Jaka alilaani huku akiinuka na kuanza kuvaa zile nguo. Hazikuwa nguo zake. Zilikuwa ni nguo nyingine kabisa.
Sijui hizi ni nguo za mumewe?
Alijiuliza huku akivaa chupi ambayo aligundua kuwa ilikuwa ni mpya kabisa, kwani bado ilikuwa ndani ya mfuko wake wa nailoni. Alivaa suruali ya jeans ambayo ilimkaa vizuri ila ilikuwa fupi kidogo. Akamalizia na fulana nyeusi ambayo ingeweza kuwa ya msichana na ilimbana kidogo. Aliona viatu vya raba pale chini ya kitanda, akavijaribu. Vilimkaa, lakini kiasi vilimbana.
Alitoka nje ya chumba kile akijua wazi kuwa alikuwa hakupiga mswaki.
Hakujali.

5

Maisha ya Jaka yalibadilika kwa kiasi kikubwa sana baada ya kukutana tena na yule binti wa ajabu aliyekutana naye kwa mara kwanza jijini Dar katika usiku wa kiza kinene na mvua kubwa. Bila ya kuamini ukweli wa mambo yale, alijishuhudia akibadilika kutoka kuwa mtu hohehahe asiye na mbele wala nyuma, na kuwa mtu mwenye mwelekeo mzuri wa maisha na matumaini ya maisha mazuri zaidi kwa siku za mbeleni. Ilikuwa ni ajabu na vigumu kwake kuamini, lakini ndivyo ilivyokuwa.
Miezi mitatu baada ya kukutana tena na Clara katika yale mazingira ya ajabu pale Dodoma, Jaka alikuwa amekwisha kutana tena na binti yule mara kadhaa na walikuwa wameongea mambo mengi ya kimaisha. Ingawa Jaka hakutaka kumwelezea ukweli juu ya matatizo yake, Clara alionesha kujali zaidi kuwa naye kuliko kujua matatizo yake, na hilo lilimpa Jaka wepesi katika kuendelea kuonana na kuongea na yule binti.
Matunda ya makutano yao hayo ya mara kwa mara yalikuwa ni Clara kufanikiwa kumshawishi baba yake kumpatia Jaka ajira kwenye kampuni yao ya ZazaCargo Movers kama msaidizi wa afisa ugavi wa kampuni ile. Alipatiwa mshahara mzuri na hivyo katika muda wa miezi miwili tangu apatiwe ajira ile, Jaka aliweza kurudia muonekano ule ule aliokuwa nao kabla ya kukutana na masahibu yaliyomkutanisha na yule binti kwa mara ya kwanza kule jijini Dar.

HAYA MAMBO YANAZIDI KUKOLEA. USIKOSE KUSOMA RIWAYA PENDWA HII, KESHO SAA TATU ASUBUHI.
 
SEHEMU YA KUMI

Matunda ya makutano yao hayo ya mara kwa mara yalikuwa ni Clara kufanikiwa kumshawishi baba yake kumpatia Jaka ajira kwenye kampuni yao ya ZazaCargo Movers kama msaidizi wa afisa ugavi wa kampuni ile. Alipatiwa mshahara mzuri na hivyo katika muda wa miezi miwili tangu apatiwe ajira ile, Jaka aliweza kurudia muonekano ule ule aliokuwa nao kabla ya kukutana na masahibu yaliyomkutanisha na yule binti kwa mara ya kwanza kule jijini Dar.
Lakini Clara hakuishia hapo. Baada ya Jaka kumtambulisha kwa mzee Mnyaga, Clara alimpatia yule mzee ajira katika ile kampuni yao kama utingo kwenye magari yao yaliyokuwa yakisafiri kuelekea nchi mbali mbali barani Afrika. Hivyo na maisha ya mzee Mnyaga pia yalibadilika na kuwa bora zaidi, kwani mshahara aliokuwa akilipwa na posho za safari za nje ya nchi vilikuwa ni vikubwa kuliko alivyowahi kutarajia. Nyumba yake ilibadilika na kuwa nzuri na imara zaidi, ingawa mwenyewe alikuwa safarini muda mwingi.
Ingawa Jaka alikuwa na uwezo wa kupanga chumba na kuishi mwenyewe, au hata kuishi nyumbani kwa Mnyaga, Clara alimuomba sana aendelee kukaa naye ndani ya nyumba yake, jambo ambalo lilipingwa vikali na Jaka pamoja na mzee Wilfred Mashauri Zaza, baba yake Clara, lakini lilitetewa kwa nguvu na Clara mwenyewe pamoja na mzee Mnyaga. Hatimaye Clara alifanikiwa na Jaka akaendelea kuishi mle nyumbani kwake kwenye chumba kile kile alichokuwa amelazwa baada ya kuokolewa na Clara kutoka kwenye kipigo kikali.
Jaka alipewa ruhusa ya kutumia magari ya kampuni kwa kazi za kiofisi na hata kwa safari zake binafsi. Hali hii ilimfanya ajisikie vizuri sana, kwamba ingawa hakuwa nyumbani kwao kama ambavyo angetaka, angalau alikuwa akiishi kama binadamu wengine. Hata hivyo, bado hakusahau sababu za kuwepo kwake pale Dodoma na bado alikuwa akihesabu siku zilizobaki kabla hajarudi tena kwenye maisha yake ya hapo awali, ingawa sasa alianza kupata mashaka kama alitaka tena kurudi huko.
Lakini asubuhi ya siku hii, ikiwa ni miezi mitatu tangu akutane tena na Clara pale Dodoma, Jaka hakuwa akijisikia vizuri hata kidogo. Alikuwa akiendesha gari la Zaza Cargo Movers aina ya Suzuki Vitara kuelekea kazini akitokea kuripoti kituo cha polisi kama kawaida huku kichwani akiwa amezongwa na mawazo mazito. Mawazo yaliyomzonga yalitokana na ukweli kwamba jambo alilokuwa akilihofia siku zote tangu akubali kuhamia nyumbani kwa Clara, sasa kilikuwa linajitokeza.
Clara alikuwa akimtaka kimapenzi.
Hilo aliligundua mapema mno na hilo ndilo jambo alichokuwa akilihofia siku zote. Yeye hakuwa tayari kabisa kujihusisha kimapenzi sio tu na Clara, bali na msichana yeyote maishani mwake. Alishajihusisha na mapenzi hapo nyuma, tena mapenzi mazito kabisa, lakini yaliyompata...!
Alikata kona na katika mtaa mfupi ambao ndio ofisi za Zaza Cargo Movers zilikuwepo. Baada ya kufunguliwa geti kubwa na kuingia ndani ya uzio mpana wa eneo la ofisi zile, aliegesha gari na kuelekea moja kwa moja kwenye jengo kubwa ambamo ofisi yake ilikuwamo. Kabla hajalifikia lango kuu la kuingilia ndani ya jengo lile, yule mlinzi aliyemfungulia geti alimwita huku akimkimbilia. Jaka alisimama na kumsubiri.
"Samahani sana mista Brown..." Alisema huku akitweta yule mlinzi, kwa lafudhi ya kigogo.
"Bila samahani Chonya, unasemaje?" Jaka alimjibu. Pale ofisini watu wote walimjua kwa jina la Brown Madega.
"Hapana mzee...ila kuna jambo tu nilitaka nikueleze. Juzi usiku nilikuwa zamu hapa. Kiasi cha saa tatu usiku hivi, alikuja mtu mmoja hapa getini nami nikamwambia kuwa haukuwa muda wa kazi hivyo aje asubuhi. Yeye akasema ana shida na mimi, ya kwamba alitaka nimjulishe iwapo kuna mtu yeyote hapa ofisini anayeitwa Jaka, unaona bwana?" Yule mlinzi alimwambia, na Jaka akauhisi moyo ukimpiga chogo chemba ndani ya kifua chake, lakini alijitahidi kuendelea kusikiliza.
"...Sa' mi' nikamwambia kuwa wafanyakazi wote wa humu ndani nawajua, na hakuna hata mmoja mwenye jina hilo, au vipi bwana? Jamaa akaondoka zake akidai kuwa labda alikuwa amepotea." Chonya akaweka kituo.
Jaka alianza kufikiri haraka haraka. Ni kweli kwamba pale ofisini yeye alijulikana kwa jina la Brown Madega, lakini hakuna mtu yeyote zaidi ya Clara aliyelijua jina la Jaka. Alishakubaliana na Clara kuwa jina hilo lisitumike kabisa pale ofisini, kwa sababu za kiusalama. Maswali mengi yalipita kichwani mwake katika muda ule mfupi aliobaki kimya akitafakari maelezo yale. Ni nani huyo aliyekwenda kumuulizia pale ofisini, akimtaja kwa jina la Jaka? Kwa nini aende usiku wakati akijua fika kuwa yeye hatokuwepo? Ofisi ya RPC ilikuwa ina taarifa na kuwepo kwake pale Zaza Cargo Movers, naye alikuwa ana ruhusa maalum kutoka kwa mzee Januari Mwakaja ya kufanya kazi pale, kwa hivyo haiwezekani huyu mtu awe ametoka polisi...
"Uliweza kumuona sura yake huyo mtu?" Hatimaye alimuuliza yule mlinzi.
"Enhee.. sasa hilo ndilo jambo jingine la ajabu kuhusu yule mtu, kwa sababu alikuwa amevaa kofia kubwa ya pama iliyoficha uso wake, halafu alikuwa amevaa koti refu jeusi lililofika mpaka magotini...unajua mi' nilimuona kama jambazi tu..." Chonya alimjibu, na kumchanganya zaidi.
"Hakutaja jina lake au sehemu anayotokea...? "
"Hapana...hakunipa nafasi ya kumuuliza maswali mengi. Nilipomjibu vile tu, akadai kuwa amepotea njia, akaondoka."
Jaka aliyatafakari kwa muda maelezo yale kabla ya kuuliza, "Hebu subiri kidogo, we' si umesema alikuja usiku? Sasa ulijuaje kuwa koti lake lilikuwa jeusi? Lingeweza kuwa la buluu au kahawia!"
"Sawa kabisa, ila unajua kwa nini? Kwa sababu leo asubuhi amekuja tena na nguo zile zile kama za siku ile."
Hapo Jaka alizidi kupata wasiwasi.
"Sasa...Dah! Sasa kwa nini unadhani mimi napaswa kujua juu ya hilo? Si ulishamwambia kuwa hapa hakuna mtu anayeitwa Jaka...?"
Yule mlinzi alimtazama Jaka kwa macho makavu na taratibu alimwambia huku akiendelea kumtazama
"Kwa sababu leo asubuhi ameniuliza kama kuna mtu aitwaye Brown Madega...Jaka Brown Madega.
“Eeenh?"
“Ndiyo bosi!" Chonya alithibitisha habari ile, na kuendelea, “Sasa mi' najua kuwa wewe unaitwa Brown Madega....sasa aliposema Jaka Brown Madega moja kwa moja nikahisi kuwa ni wewe!"
Ingawa sasa moyo wa Jaka ulikuwa anaenda mchaka-mchaka ndani ya kifua chake, alifyatua tabasamu la ghafla usoni kwake.
"Ah! Basi lazima huyo atakuwa ni mmoja kati ya jamaa niliosoma nao sekondari....hilo jina niliacha kulitumia zamani sana baada ya kumaliza sekondari..." Alijikausha na kumjibu yule mlinzi huku akitabasamu. Aliona uso wa yile mlinzi ukisajili mshangao tu. Hakumpa muda wa kufikiri wala kuongea zaidi.
"Ahsante sana Chonya kwa taarifa hii. Basi akija tena usisite kunieleza...na nitahitaji kuonana naye, sawa?" Alimwambia.
"Bila shaka mzee...!" Chonya alijibu na Jaka akaondoka haraka kuelekea ofisini kwake huku akimwachia noti ya shilingi elfu mbili yule mlinzi ambaye alifurahi sana na kuahidi kuwa pindi yule jamaa akitokea tena atampa taarifa.
Ni kitu gani tena kinataka kujitokeza sasa?
Alikuwa akijiuliza huku akifungua mlango wa ofisi yake iliyokuwa ghorofa ya pili ya jengo lile la ghorofa tatu.
Sasa kichwabi mwake kulikuwa kuna mgongani wa mawazo.
Kwanza kuna swala la Clara ambalo bado alikuwa hajalipatia ufumbuzi, sasa tena anatokea na huyu mtu mwenye makoti marefu na kuanza kuulizia habari zake...
Ni nani huyu mwenye kuvaa koti refu jeusi na kofia kubwa ya pama?
Na kikubwa zaidi...anamtakia nini?
Alijikuta anarudi pale pale. Hakuna jibu.
Na bado kuna tatizo la Clara.
Clara...ina maana amemfanyia mambo yote haya....wema wote huu...kwa vile alikuwa na matakwa yake binafsi?
Jaka aliliona hilo ni gumu kuamini, kwani kadiri alivyokuwa akilitafakari, alishindwa kujiridhisha kuwa halikuwa hivyo.
Kwanza yule binti alijihatarishia maisha yake alipojitolea kumuokota pale alipopigwa na kutupwa barabarani usiku ule alipoonana tena na yule mshenzi wa tabia, Tony. Zaidi ya hapo alijitolea kumtibu na kumhudumia ndani ya nyumba yake, bila ya kujali kuwa angeweza kuwa mwizi au muuaji na kumdhuru. Asiishie hapo yule binti, akajitolea kumkaribisha ahamie nyumbani kwake, ampe chumba ndani ya nyumba yake aishi, bure....!
Kama hiyo haitoshi, bado binti yule alimfanyia wema wa kumpatia kazi kwenye kampuni ya baba yake, kazi iliyompatia kipato kizuri, na gari la kuendea kazini na kutembelea kampa!
Haya yote hayawezi kuwa bure...na ingawa Clara mwenyewe alisisitiza kuwa hayo yote hayawezi kufikia wema ambao Jaka alimfanyia kwa kujitolea kuokoa maisha yake usiku ule wa mvua kubwa kule Dar es Salaam zaidi ya mwaka mmoja uliopita, bado Jaka hakuamini kuwa hiyo ndio sababu pekee.
Na sasa mashaka yake hayo yalikuwa yamethibitishwa. Ni kweli kulikuwa na sababu nyingine zaidi ya hiyo. Aliingia kwenye ofisi yake ndogo na nzuri, akaketi nyuma ya meza ya mninga iliyokuwa ikiutazama mlango. Mbele ya meza ile kulikuwa kuna viti vingine viwili ambavyo viliwekwa kuitazama ile meza. Baada ya muda mfupi aliinuka na kutembea taratibu juu ya zulia zito la rangi ya zambarau lililonakshiwa kwa maua mekundu na kwenda kusimama nyuma ya dirisha kubwa lililokuwa nyuma ya kiti chake likitazamana na mlango. Alifungua pazia zito la rangi ya zambarau lililokuwa limefunika dirisha lile. Lilikuwa ni dirisha la kioo kitupu ambacho aliweza kukifungua na kukifunga pindi atakapo. Hakutaka kukifungua.
Kutokea pale dirishani aliweza kuiona Jeep Cherokee ya Clara ikiwa imeegeshwa kule chini, kando ya gari alilokwenda nalo yeye pale ofisini. Alielewa kuwa Clara alikuwa ameshafika pale ofisini. Ilikuwa ni kawaida kuwa ingawa walikuwa wakiishi pamoja, siku zote Jaka alikuwa akitangulia kuondoka na kumwacha Clara akiwa bado amelala au ndio anaamka. Ilibidi iwe hivyo kwa sababu wote walielewa kuwa Jaka alilazimika kupitia kituo cha polisi kuripoti kabla ya kufika ofisini. Vilevile hawakupenda kwenda pamoja ofisini ili kuepusha kupandikiza mawazo potofu kwa wafanyakazi wa pale ofisini zaidi ya yale ambayo tayari yalishapandikizwa kutokana na wao kuishi nyumba moja, kwani ingawa walilala vyumba tofauti, watu wa nje hawakujua hilo.
Aliaendelea kusimama pale dirishani akiangalia kule nje huku akiwa katika lindi la mawazo, kisha alishusha pumzi ndefu na kurudi kuketi pale kwenye kiti chake nyuma ya ile meza na kuendelea na mawazo yake huku akiwa amejishika tama na uso ameukunja kwa uzito wa mawazo aliyokuwa nayo.

__________________

Tangu akutane tena na Clara pale dodoma, wamekuwa marafiki wakubwa sana. Kitu ambacho Jaka alikitilia mkazo sana akilini mwake siku zote ni kwamba urafiki ule usivuke mipaka na kuingia kwenye hatua ya mapenzi. Kwanza Clara alikuwa tajiri sana na hivyo aliamini kuwa asingekuwa na haja ya kutaka kujihusisha na mtu kama yeye kimapenzi; kwa hiyo vile Clara kuweza kuwa na urafiki wa heshima tu na yeye ni jambo lililomfanya Jaka amheshimu sana. Angekuwa ni mtu asiye na heshima wala shukurani iwapo pamoja na yote yale ambayo Clara amemfanyia, na heshima yote ambayo Clara amemuonesha, bado tena angemtaka binti yule kimapenzi. Hilo halingewezekana asilani, na Jaka hakuwa na wasiwasi hata kidogo kuwa angeweza kumvunjia Clara heshima hata siku moja.
Ni kweli Clara alikuwa ni msichana mwenye sura ya kuvutia na umbo la nzuri, lakini pia Jaka hakutaka kujidanganya kuwa atakuwa amekaa miaka yote hiyo aliyokaa na uzuri ule asipate mtu yeyote wa kumpenda mpaka aje atokee yeye ndio ampende...kwani yeye ni nani? Katika watu wote Dodoma ile, akae bila mpenzi hata mmoja mpaka atokee Jaka, mtuhumiwa na hatimaye mhukumiwa wa kosa la mauaji, ndio aje apendane naye?
Hapana, hiyo halikuwezekana, na Jaka alikuwa na akili timamu kuelewa hivyo.
Sasa cha ajabu ni kwamba, ni Clara mwenyewe ndiye ambaye anaonesha kumtaka Jaka kimapenzi! Alishafanya visa kadhaa wa kadhaa vya kumuonesha Jaka kuwa alikuwa tayari kumridhia kwa lolote atakalo...
Kuna siku alimuuliza iwapo Jaka alikuwa na mpenzi kabla ya kuja kwake Dodoma.
"Ni ajabu mtu handsome kama wewe kukosa girlfriend...." Clara alijibu baada ya Jaka kumueleza kuwa hakuwa na mpenzi kabla ya kuja Dodoma. Hakutaka kumueleza ukweli juu ya maisha yake yaliyopita, kwani alikuwa ana nia ya kufunua ukurasa mpya katika maisha yake na hakutaka kujikumbusha yale yaliyopita. Walikuwa wamekaa sebuleni kwa Clara usiku ule wakiangalia video. Clara alikuwa amevaa suruali ya mazoezi na fulana kubwa, wakati Jaka alikuwa amevaa suruali yake ya Jeans na sweta zito, miongoni mwa nguo nyingi alizoweza kununua kutokana na fadhila za ajira aliyopatiwa na Clara.
Kwa hiyo wewe unadhani mimi ni handsome.
Jaka alijiwazia kichwani siku ile lakini hakusema kitu, alibaki kimya.
Taratibu Jaka alianza kujishughulisha na kazi za pale ofisini huku mawazo yale yakimrudia mara kwa mara.
Siku nyingine wakati Jaka akiwa amekaa kwenye kochi refu pale sebuleni akiangalia runinga, Clara alikuja na kujilaza kwenye kochi lile huku akilaza kichwa chake mapajani kwa Jaka. Kwa mshangao Jaka aliinamisha uso wake na kumtazama. Kwa kweli ilikuwa ni picha ya kuhamasisha hisia za mapenzi kwa kiasi kikubwa, kwani nywele zake ndefu na laini alikuwa amezitimua kivivu na gauni lake la jioni la kitambaa chekundu cha hariri, liliongezea mvuto wa hisia zile za mapenzi na Jaka alihisi moyo wake ukibadili mapigo.

ITAENDELEA
 
SEHEMU YA KUMI

Matunda ya makutano yao hayo ya mara kwa mara yalikuwa ni Clara kufanikiwa kumshawishi baba yake kumpatia Jaka ajira kwenye kampuni yao ya ZazaCargo Movers kama msaidizi wa afisa ugavi wa kampuni ile. Alipatiwa mshahara mzuri na hivyo katika muda wa miezi miwili tangu apatiwe ajira ile, Jaka aliweza kurudia muonekano ule ule aliokuwa nao kabla ya kukutana na masahibu yaliyomkutanisha na yule binti kwa mara ya kwanza kule jijini Dar.
Lakini Clara hakuishia hapo. Baada ya Jaka kumtambulisha kwa mzee Mnyaga, Clara alimpatia yule mzee ajira katika ile kampuni yao kama utingo kwenye magari yao yaliyokuwa yakisafiri kuelekea nchi mbali mbali barani Afrika. Hivyo na maisha ya mzee Mnyaga pia yalibadilika na kuwa bora zaidi, kwani mshahara aliokuwa akilipwa na posho za safari za nje ya nchi vilikuwa ni vikubwa kuliko alivyowahi kutarajia. Nyumba yake ilibadilika na kuwa nzuri na imara zaidi, ingawa mwenyewe alikuwa safarini muda mwingi.
Ingawa Jaka alikuwa na uwezo wa kupanga chumba na kuishi mwenyewe, au hata kuishi nyumbani kwa Mnyaga, Clara alimuomba sana aendelee kukaa naye ndani ya nyumba yake, jambo ambalo lilipingwa vikali na Jaka pamoja na mzee Wilfred Mashauri Zaza, baba yake Clara, lakini lilitetewa kwa nguvu na Clara mwenyewe pamoja na mzee Mnyaga. Hatimaye Clara alifanikiwa na Jaka akaendelea kuishi mle nyumbani kwake kwenye chumba kile kile alichokuwa amelazwa baada ya kuokolewa na Clara kutoka kwenye kipigo kikali.
Jaka alipewa ruhusa ya kutumia magari ya kampuni kwa kazi za kiofisi na hata kwa safari zake binafsi. Hali hii ilimfanya ajisikie vizuri sana, kwamba ingawa hakuwa nyumbani kwao kama ambavyo angetaka, angalau alikuwa akiishi kama binadamu wengine. Hata hivyo, bado hakusahau sababu za kuwepo kwake pale Dodoma na bado alikuwa akihesabu siku zilizobaki kabla hajarudi tena kwenye maisha yake ya hapo awali, ingawa sasa alianza kupata mashaka kama alitaka tena kurudi huko.
Lakini asubuhi ya siku hii, ikiwa ni miezi mitatu tangu akutane tena na Clara pale Dodoma, Jaka hakuwa akijisikia vizuri hata kidogo. Alikuwa akiendesha gari la Zaza Cargo Movers aina ya Suzuki Vitara kuelekea kazini akitokea kuripoti kituo cha polisi kama kawaida huku kichwani akiwa amezongwa na mawazo mazito. Mawazo yaliyomzonga yalitokana na ukweli kwamba jambo alilokuwa akilihofia siku zote tangu akubali kuhamia nyumbani kwa Clara, sasa kilikuwa linajitokeza.
Clara alikuwa akimtaka kimapenzi.
Hilo aliligundua mapema mno na hilo ndilo jambo alichokuwa akilihofia siku zote. Yeye hakuwa tayari kabisa kujihusisha kimapenzi sio tu na Clara, bali na msichana yeyote maishani mwake. Alishajihusisha na mapenzi hapo nyuma, tena mapenzi mazito kabisa, lakini yaliyompata...!
Alikata kona na katika mtaa mfupi ambao ndio ofisi za Zaza Cargo Movers zilikuwepo. Baada ya kufunguliwa geti kubwa na kuingia ndani ya uzio mpana wa eneo la ofisi zile, aliegesha gari na kuelekea moja kwa moja kwenye jengo kubwa ambamo ofisi yake ilikuwamo. Kabla hajalifikia lango kuu la kuingilia ndani ya jengo lile, yule mlinzi aliyemfungulia geti alimwita huku akimkimbilia. Jaka alisimama na kumsubiri.
"Samahani sana mista Brown..." Alisema huku akitweta yule mlinzi, kwa lafudhi ya kigogo.
"Bila samahani Chonya, unasemaje?" Jaka alimjibu. Pale ofisini watu wote walimjua kwa jina la Brown Madega.
"Hapana mzee...ila kuna jambo tu nilitaka nikueleze. Juzi usiku nilikuwa zamu hapa. Kiasi cha saa tatu usiku hivi, alikuja mtu mmoja hapa getini nami nikamwambia kuwa haukuwa muda wa kazi hivyo aje asubuhi. Yeye akasema ana shida na mimi, ya kwamba alitaka nimjulishe iwapo kuna mtu yeyote hapa ofisini anayeitwa Jaka, unaona bwana?" Yule mlinzi alimwambia, na Jaka akauhisi moyo ukimpiga chogo chemba ndani ya kifua chake, lakini alijitahidi kuendelea kusikiliza.
"...Sa' mi' nikamwambia kuwa wafanyakazi wote wa humu ndani nawajua, na hakuna hata mmoja mwenye jina hilo, au vipi bwana? Jamaa akaondoka zake akidai kuwa labda alikuwa amepotea." Chonya akaweka kituo.
Jaka alianza kufikiri haraka haraka. Ni kweli kwamba pale ofisini yeye alijulikana kwa jina la Brown Madega, lakini hakuna mtu yeyote zaidi ya Clara aliyelijua jina la Jaka. Alishakubaliana na Clara kuwa jina hilo lisitumike kabisa pale ofisini, kwa sababu za kiusalama. Maswali mengi yalipita kichwani mwake katika muda ule mfupi aliobaki kimya akitafakari maelezo yale. Ni nani huyo aliyekwenda kumuulizia pale ofisini, akimtaja kwa jina la Jaka? Kwa nini aende usiku wakati akijua fika kuwa yeye hatokuwepo? Ofisi ya RPC ilikuwa ina taarifa na kuwepo kwake pale Zaza Cargo Movers, naye alikuwa ana ruhusa maalum kutoka kwa mzee Januari Mwakaja ya kufanya kazi pale, kwa hivyo haiwezekani huyu mtu awe ametoka polisi...
"Uliweza kumuona sura yake huyo mtu?" Hatimaye alimuuliza yule mlinzi.
"Enhee.. sasa hilo ndilo jambo jingine la ajabu kuhusu yule mtu, kwa sababu alikuwa amevaa kofia kubwa ya pama iliyoficha uso wake, halafu alikuwa amevaa koti refu jeusi lililofika mpaka magotini...unajua mi' nilimuona kama jambazi tu..." Chonya alimjibu, na kumchanganya zaidi.
"Hakutaja jina lake au sehemu anayotokea...? "
"Hapana...hakunipa nafasi ya kumuuliza maswali mengi. Nilipomjibu vile tu, akadai kuwa amepotea njia, akaondoka."
Jaka aliyatafakari kwa muda maelezo yale kabla ya kuuliza, "Hebu subiri kidogo, we' si umesema alikuja usiku? Sasa ulijuaje kuwa koti lake lilikuwa jeusi? Lingeweza kuwa la buluu au kahawia!"
"Sawa kabisa, ila unajua kwa nini? Kwa sababu leo asubuhi amekuja tena na nguo zile zile kama za siku ile."
Hapo Jaka alizidi kupata wasiwasi.
"Sasa...Dah! Sasa kwa nini unadhani mimi napaswa kujua juu ya hilo? Si ulishamwambia kuwa hapa hakuna mtu anayeitwa Jaka...?"
Yule mlinzi alimtazama Jaka kwa macho makavu na taratibu alimwambia huku akiendelea kumtazama
"Kwa sababu leo asubuhi ameniuliza kama kuna mtu aitwaye Brown Madega...Jaka Brown Madega.
“Eeenh?"
“Ndiyo bosi!" Chonya alithibitisha habari ile, na kuendelea, “Sasa mi' najua kuwa wewe unaitwa Brown Madega....sasa aliposema Jaka Brown Madega moja kwa moja nikahisi kuwa ni wewe!"
Ingawa sasa moyo wa Jaka ulikuwa anaenda mchaka-mchaka ndani ya kifua chake, alifyatua tabasamu la ghafla usoni kwake.
"Ah! Basi lazima huyo atakuwa ni mmoja kati ya jamaa niliosoma nao sekondari....hilo jina niliacha kulitumia zamani sana baada ya kumaliza sekondari..." Alijikausha na kumjibu yule mlinzi huku akitabasamu. Aliona uso wa yile mlinzi ukisajili mshangao tu. Hakumpa muda wa kufikiri wala kuongea zaidi.
"Ahsante sana Chonya kwa taarifa hii. Basi akija tena usisite kunieleza...na nitahitaji kuonana naye, sawa?" Alimwambia.
"Bila shaka mzee...!" Chonya alijibu na Jaka akaondoka haraka kuelekea ofisini kwake huku akimwachia noti ya shilingi elfu mbili yule mlinzi ambaye alifurahi sana na kuahidi kuwa pindi yule jamaa akitokea tena atampa taarifa.
Ni kitu gani tena kinataka kujitokeza sasa?
Alikuwa akijiuliza huku akifungua mlango wa ofisi yake iliyokuwa ghorofa ya pili ya jengo lile la ghorofa tatu.
Sasa kichwabi mwake kulikuwa kuna mgongani wa mawazo.
Kwanza kuna swala la Clara ambalo bado alikuwa hajalipatia ufumbuzi, sasa tena anatokea na huyu mtu mwenye makoti marefu na kuanza kuulizia habari zake...
Ni nani huyu mwenye kuvaa koti refu jeusi na kofia kubwa ya pama?
Na kikubwa zaidi...anamtakia nini?
Alijikuta anarudi pale pale. Hakuna jibu.
Na bado kuna tatizo la Clara.
Clara...ina maana amemfanyia mambo yote haya....wema wote huu...kwa vile alikuwa na matakwa yake binafsi?
Jaka aliliona hilo ni gumu kuamini, kwani kadiri alivyokuwa akilitafakari, alishindwa kujiridhisha kuwa halikuwa hivyo.
Kwanza yule binti alijihatarishia maisha yake alipojitolea kumuokota pale alipopigwa na kutupwa barabarani usiku ule alipoonana tena na yule mshenzi wa tabia, Tony. Zaidi ya hapo alijitolea kumtibu na kumhudumia ndani ya nyumba yake, bila ya kujali kuwa angeweza kuwa mwizi au muuaji na kumdhuru. Asiishie hapo yule binti, akajitolea kumkaribisha ahamie nyumbani kwake, ampe chumba ndani ya nyumba yake aishi, bure....!
Kama hiyo haitoshi, bado binti yule alimfanyia wema wa kumpatia kazi kwenye kampuni ya baba yake, kazi iliyompatia kipato kizuri, na gari la kuendea kazini na kutembelea kampa!
Haya yote hayawezi kuwa bure...na ingawa Clara mwenyewe alisisitiza kuwa hayo yote hayawezi kufikia wema ambao Jaka alimfanyia kwa kujitolea kuokoa maisha yake usiku ule wa mvua kubwa kule Dar es Salaam zaidi ya mwaka mmoja uliopita, bado Jaka hakuamini kuwa hiyo ndio sababu pekee.
Na sasa mashaka yake hayo yalikuwa yamethibitishwa. Ni kweli kulikuwa na sababu nyingine zaidi ya hiyo. Aliingia kwenye ofisi yake ndogo na nzuri, akaketi nyuma ya meza ya mninga iliyokuwa ikiutazama mlango. Mbele ya meza ile kulikuwa kuna viti vingine viwili ambavyo viliwekwa kuitazama ile meza. Baada ya muda mfupi aliinuka na kutembea taratibu juu ya zulia zito la rangi ya zambarau lililonakshiwa kwa maua mekundu na kwenda kusimama nyuma ya dirisha kubwa lililokuwa nyuma ya kiti chake likitazamana na mlango. Alifungua pazia zito la rangi ya zambarau lililokuwa limefunika dirisha lile. Lilikuwa ni dirisha la kioo kitupu ambacho aliweza kukifungua na kukifunga pindi atakapo. Hakutaka kukifungua.
Kutokea pale dirishani aliweza kuiona Jeep Cherokee ya Clara ikiwa imeegeshwa kule chini, kando ya gari alilokwenda nalo yeye pale ofisini. Alielewa kuwa Clara alikuwa ameshafika pale ofisini. Ilikuwa ni kawaida kuwa ingawa walikuwa wakiishi pamoja, siku zote Jaka alikuwa akitangulia kuondoka na kumwacha Clara akiwa bado amelala au ndio anaamka. Ilibidi iwe hivyo kwa sababu wote walielewa kuwa Jaka alilazimika kupitia kituo cha polisi kuripoti kabla ya kufika ofisini. Vilevile hawakupenda kwenda pamoja ofisini ili kuepusha kupandikiza mawazo potofu kwa wafanyakazi wa pale ofisini zaidi ya yale ambayo tayari yalishapandikizwa kutokana na wao kuishi nyumba moja, kwani ingawa walilala vyumba tofauti, watu wa nje hawakujua hilo.
Aliaendelea kusimama pale dirishani akiangalia kule nje huku akiwa katika lindi la mawazo, kisha alishusha pumzi ndefu na kurudi kuketi pale kwenye kiti chake nyuma ya ile meza na kuendelea na mawazo yake huku akiwa amejishika tama na uso ameukunja kwa uzito wa mawazo aliyokuwa nayo.

__________________

Tangu akutane tena na Clara pale dodoma, wamekuwa marafiki wakubwa sana. Kitu ambacho Jaka alikitilia mkazo sana akilini mwake siku zote ni kwamba urafiki ule usivuke mipaka na kuingia kwenye hatua ya mapenzi. Kwanza Clara alikuwa tajiri sana na hivyo aliamini kuwa asingekuwa na haja ya kutaka kujihusisha na mtu kama yeye kimapenzi; kwa hiyo vile Clara kuweza kuwa na urafiki wa heshima tu na yeye ni jambo lililomfanya Jaka amheshimu sana. Angekuwa ni mtu asiye na heshima wala shukurani iwapo pamoja na yote yale ambayo Clara amemfanyia, na heshima yote ambayo Clara amemuonesha, bado tena angemtaka binti yule kimapenzi. Hilo halingewezekana asilani, na Jaka hakuwa na wasiwasi hata kidogo kuwa angeweza kumvunjia Clara heshima hata siku moja.
Ni kweli Clara alikuwa ni msichana mwenye sura ya kuvutia na umbo la nzuri, lakini pia Jaka hakutaka kujidanganya kuwa atakuwa amekaa miaka yote hiyo aliyokaa na uzuri ule asipate mtu yeyote wa kumpenda mpaka aje atokee yeye ndio ampende...kwani yeye ni nani? Katika watu wote Dodoma ile, akae bila mpenzi hata mmoja mpaka atokee Jaka, mtuhumiwa na hatimaye mhukumiwa wa kosa la mauaji, ndio aje apendane naye?
Hapana, hiyo halikuwezekana, na Jaka alikuwa na akili timamu kuelewa hivyo.
Sasa cha ajabu ni kwamba, ni Clara mwenyewe ndiye ambaye anaonesha kumtaka Jaka kimapenzi! Alishafanya visa kadhaa wa kadhaa vya kumuonesha Jaka kuwa alikuwa tayari kumridhia kwa lolote atakalo...
Kuna siku alimuuliza iwapo Jaka alikuwa na mpenzi kabla ya kuja kwake Dodoma.
"Ni ajabu mtu handsome kama wewe kukosa girlfriend...." Clara alijibu baada ya Jaka kumueleza kuwa hakuwa na mpenzi kabla ya kuja Dodoma. Hakutaka kumueleza ukweli juu ya maisha yake yaliyopita, kwani alikuwa ana nia ya kufunua ukurasa mpya katika maisha yake na hakutaka kujikumbusha yale yaliyopita. Walikuwa wamekaa sebuleni kwa Clara usiku ule wakiangalia video. Clara alikuwa amevaa suruali ya mazoezi na fulana kubwa, wakati Jaka alikuwa amevaa suruali yake ya Jeans na sweta zito, miongoni mwa nguo nyingi alizoweza kununua kutokana na fadhila za ajira aliyopatiwa na Clara.
Kwa hiyo wewe unadhani mimi ni handsome.
Jaka alijiwazia kichwani siku ile lakini hakusema kitu, alibaki kimya.
Taratibu Jaka alianza kujishughulisha na kazi za pale ofisini huku mawazo yale yakimrudia mara kwa mara.
Siku nyingine wakati Jaka akiwa amekaa kwenye kochi refu pale sebuleni akiangalia runinga, Clara alikuja na kujilaza kwenye kochi lile huku akilaza kichwa chake mapajani kwa Jaka. Kwa mshangao Jaka aliinamisha uso wake na kumtazama. Kwa kweli ilikuwa ni picha ya kuhamasisha hisia za mapenzi kwa kiasi kikubwa, kwani nywele zake ndefu na laini alikuwa amezitimua kivivu na gauni lake la jioni la kitambaa chekundu cha hariri, liliongezea mvuto wa hisia zile za mapenzi na Jaka alihisi moyo wake ukibadili mapigo.

ITAENDELEA
Story nzuri sana.

Sent using Jamii Forums mobile app
 
Riwaya nzuri sana, naomba utuwekee muendelezo wake!
 
SEHEMU YA KUMI NA MOJA

Kwa hiyo wewe unadhani mimi ni handsome.
Jaka alijiwazia kichwani siku ile lakini hakusema kitu, alibaki kimya.
Taratibu Jaka alianza kujishughulisha na kazi za pale ofisini huku mawazo yale yakimrudia mara kwa mara.
Siku nyingine wakati Jaka akiwa amekaa kwenye kochi refu pale sebuleni akiangalia runinga, Clara alikuja na kujilaza kwenye kochi lile huku akilaza kichwa chake mapajani kwa Jaka. Kwa mshangao Jaka aliinamisha uso wake na kumtazama. Kwa kweli ilikuwa ni picha ya kuhamasisha hisia za mapenzi kwa kiasi kikubwa, kwani nywele zake ndefu na laini alikuwa amezitimua kivivu na gauni lake la jioni la kitambaa chekundu cha hariri, liliongezea mvuto wa hisia zile za mapenzi na Jaka alihisi moyo wake ukibadili mapigo.
Wakati Jaka alipoinamisha uso wake kumtazama kwa mshangao namna ile, Clara naye aliinua uso wake na kumtazama huku akitabasamu, na ilimchukua Jaka sekunde kadhaa kabla hajakumbuka kuwa alitakiwa ashangazwe na kitendo kile.
"Vipi...nikupishe ulale vizuri nini...?" Hatimaye alimuuliza huku akijaribu kujisogeza ili kumpa Clara nafasi ya kujilaza vizuri pale kwenye kochi.
"Kwa nini...mi' napenda tukae hivi hivi tu..." Clara alijibu huku akijilaza vizuri zaidi mapajani kwake.
Usiku ule Jaka hakulala kwa mawazo. Jambo ambalo aliazimia kutolianzisha baina yake na Clara lilikuwa linaanza kujitokeza, na siyo yeye aliyekuwa analianzisha.
Ataweza kulizuia?
Baada ya kutafakari hali ile kwa muda mrefu, alipitisha uamuzi usiku ule kuwa ifikapo asubuhi, angefungasha virago vyake na kuihama nyumba ile, na ikibidi kufukuzwa kazi kwa kufanya hivyo potelea mbali...
Kumbukumbu zake hizo zilikatishwa na hodi iliyobishwa kwenye mlango wa ofisi yake. Alipaza sauti kumkaribisha mgongaji, na Clara akaingia na kumsalimia kwa uchangamfu.
"Hey! Mambo ?"
Jaka alimtazama yule binti. Kwa hakika alikuwa amependeza sana.
"Ah, safi tu Clara..." AliMjibu, lakini si kwa uchangamfu kama jinsi Clara alivyomsalimia. Hali hiyo ilimfanya Clara asimame mbele ya meza yake pale ofisini kwa muda huku akimtazama kwa macho ya wasiwasi.
"Hey, what's the matter with you? Mbona umechukia?" Alimuuliza kwa mashaka, akimaanisha kutaka kujua alikuwa ana tatizo gani.
"Eeenh? No!...sijachukia...niko sawa..." Jaka alimjibu, ingawa ilionekana wazi kuwa hali haikuwa sawa.
Clara alimwangalia kwa sekunde kadhaa.
"Samahani, nilikuwa nimekuja kukusalimia tu." Hatimaye alimwambia kwa kisirani, kisha akageuka na kutoka nje ya ofisi ile.
"Clara..." Jaka alijaribu kumuita kabla hajatoka nje, lakini Clara hakusimama wala hakugeuka.
Hakuweza kufanya kazi vizuri siku yote ile kutokana na kutawaliwa na mawazo mengi. Ilikuwa ni kawaida pale ofisini kuwa kila ifikapo saa nne asubuhi, wafanyakazi wanaelekea kantini pale pale ofisini kupata chai. Alitegemea kuwa angemkuta Clara kantini, kwani walikuwa na mazoea ya kukaa meza moja kila siku na kunywa chai huku wakiongea, na baada ya hapo kila mmoja alielekea ofisini kwake.
Siku ile hakumkuta.
Alitembeza macho huku na kule ndani ya ile kantini bila kufanikiwa kumuona. Aliagiza chai na kuanza kunywa taratibu akitarajia kuwa Clara angefika na kumkuta pale kantini. Wakati akinywa chai ile taratibu, mawazo yake yalirudia tena kwenye matukio mbalimbali yaliyotokea baina yake na Clara...
____________________

Alikumbuka kuwa baada ya tukio la usiku ule ambao Clara aliamua kujilaza mapajani mwake, asubuhi yake aliamka akiwa na wazo la kuhama upesi sana kutoka kwenye nyumba ile kabla mambo hayajaharibika. Na asubuhi ile Clara aliamka akiwa na homa kali sana. Hakuwa na namna, akalazimika kuahirisha mpango wake ule kwa muda mpaka Clara atakapopona.
Ikawa anamhudumia kwa kumkorogea chai, kumtengenezea juisi na kumhimiza kunywa dawa, kwani Clara alikuwa mwoga sana wa kumeza dawa.
Katika wiki moja ile aliyougua, ukaribu wao ukaongezeka maradufu. Na Clara alivyojua kujidekeza sasa! Ikawa halali usingizi mpaka alale mapajani mwa Jaka, ambaye alilazimika kukaa naye hivyo hivyo mpaka alale, ndipo alipomlaza kitandani taratibu na kutoka kwenda kulala chumbani kwake.
Jaka alijiuliza ingekuwaje iwapo akiondoka halafu binti yule akapata ugonjwa wa ghafla wakati yuko peke yake mle ndani. Alijipa moyo kuwa kabla ya ujio wake si alikuwa akiishi peke yake?
Alikumbuka jinsi alivyolijadili swala la Clara na mjomba wake Mnyaga.
"Kwani we' wasiwasi wako nini mjomba?" Mnyaga alimuuliza.
"Aakh! Anko...mi' siwezi kujihusisha naye kimapenzi..."
"Kwa nini?"
“Kwanza sijui kama hana au hakuwa na mpenzi mwingine kabla yangu.
“Si umuulize? Si uulize watu wanaomjua kabla yako? Si uchunguze? Acha hizo anko!”
“Akh, sasa yote hayo ya nini na mi’ sina nia naye? Isitoshe, iwapo anaweza kufanya hivi kwangu, ni watu wangapi kabla yangu ambao amewahi kuwanasa kwa kutumia utajiri wake?” Jaka alimjibu. Mnyaga alimcheka sana kwa jibu lile kiasi cha kumkera.
“Sasa Anko we’ unaona hili ni jambo la kuchekesha?”
“Hapana. Hili si jambo la kuchekesha, ila wewe ndio kichekesho.”
“Khaa!”
“Ndio.”
“Sasa ndio majibu gani hayo mjomba!”
“Mimi nimeanza kumuona yule binti kabla yako, Jaka. Na kama angekuwa ana tabia kama hizo ambazo wewe unamdhania kuwa anazo, basi mimi ndio ningekuwa wa kwanza kukueleza kuwa huyo binti si mwema...”
“We’ ungejuaje Anko? Wanawake hawatabiriki hata kidogo mjomba! Niulize mimi bwana...achana nao kabisa!”
Jibu hilo lilimfanya Mnyaga acheke kwa mara nyingine. Kwa mara nyingine Jaka alikereka kuchekwa namna ile.
“You think this is funny? We’ Anko hili jambo lote unaliona mzaha tu, eenh?”
“Sio hivyo msomi wangu...lakini kama ungekuwa umekaa hapa duniani kwa muda mrefu kama mimi ungeelewa...lakini wewe bado mgeni na mambo mengi sana hapa duniani anko; bado kijana sana wewe, na ndio maana hutakiwi kukimbia mambo kama haya,unatakiwa uyaelewe halafu uyapeleke jinsi utakavyo...utajificha mpaka lini?”
Jaka alibaki akimkodolea macho tu. Mnyaga akaendelea, “Jaka yule msichana anakupenda! Tena anakupenda kwa nia nzuri tu. Na hili sio swala la ajabu au geni hapa duniani, kwa mtu mmoja kutokea kumpenda mwingine...sasa wewe badala ya kuchangamkia nafasi hiyo unachukia? Au umesahau?"
Jaka aliendelea kumtazama Mnyaga kwa mshangao.
"Nimesahau...? nimesahau nini tena!"
Mnyaga alimkazia macho na kumwangalia Jaka moja kwa moja machoni kwa muda kabla ya kumjibu.
"Ndoto Jaka....ile ndoto uliyokuwa ukiiota tena na tena...huoni kuwa ndio maana yake inazidi kujidhihirisha? Haya mambo yalishajionesha kwako kwa njia ya ile ndoto. Sasa wewe unataka kushindana na ukweli, unataka kubadili hali ambayo tayari historia imeshaamua kuiweka...utashindwa tu!"
Jaka alibaki mdomo wazi wakati ukweli wa maneno yale ulivyokuwa ukiingia kichwani mwake.
"Kwa hiyo...?"
"Kwa hiyo wewe huna haja ya kuhama kwa sababu hizo ulizozitoa, labda utafute sababu nyingine. Endelea kukaa naye tu pale nyumbani. Iwapo mwenyewe amekuamini kiasi hicho, na baba yake anajua juu ya uwepo wako pale nyumbani, sioni sababu ya wewe kujitia wasiwasi wa bure..."
"Tatizo sio kukaa tu pale nyumbani kwa Clara Anko, tatizo ni kwamba, nikiendelea kukaa pale ndio itabidi nikubaliane na matakwa yake..."
"Ndivyo alivyokwambia?"
"Hapana...ila..."
"Ila hayo ni mawazo yako! Ambayo sio lazima kila wakati yawe sahihi. Sikiliza anko, mi' nakushauri usifanye papara ya kuondoka pale nyumbani, kwani muda ukiwadia mtapata ufumbuzi wa swala hilo. Mbona tangu mwanzo mambo yote yalivyokuwa yakitokea hukuweza kuyazuia? Iweje uanze sasa?"
Ni baada ya mjadala ule ndipo Jaka akaendelea kuishi na Clara ndani ya ile nyumba.
Aligeuka na kuangaza tena mle kantini. Clara hakuwepo. Alikumbuka kuwa alikuwa hajamaliza kunywa chai aliyoagiza. Alichovya kidole kwenye ile chai na kugundua kuwa ilikuwa imeshapoa sana. Alishusha pumzi ndefu huku akiinuka na kurejea ofisini kwake. Kabla hajafika ofisi kwake aliamua kupitia ofisi kwa Clara ili kujua kulikoni, ingawa alijua kuwa Clara alikuwa amekasirishwa na hali aliyomkuta nayo pale ofisini kwake asubuhi ile.
Sasa yeye alitegemea nini!
Sekretari wa Clara alimjulisha kuwa Clara alikuwa ameenda nyumbani kujipumzisha kutokana na maumivu ya kichwa. Taratibu Jaka aligeuza na kuelekea ofisini kwake.
Kitu kilichomkosesha raha asubuhi ile ni kwamba usiku wa kuamkia siku ile Clara alitupa mipaka katika vituko alivyokuwa akimfanyia pale nyumbani.
Jioni ya siku ile kama kawaida yake Jaka aliingia nyumbani baada ya Clara kuwa amesharudi. Yeye siku zote huchelewa kutoka ofisini kwani hulazimika kubaki mpaka saa kumi na moja na nusu ili kufunga mahesabu ya ugavi ya siku. Na akitoka kazini hupitia kituo cha polisi kusaini kama kawaida, ndipo huelekea nyumbani.
Alipoingia chumbani kwake alishangaa kusikia harufu uturi ghali sana ambayo mara moja aliitambua kuwa ni harufu ya uturi ambao Clara hupenda kujipulizia. Na ndio harufu aliyokumbuka kuinusa mara ya mwisho kabla hajapoteza fahamu siku ile aliyoambulia kipigo kizito pale nje ya ukumbi wa disko wa NK kabla ya kuokolewa na Clara. Alizungusha macho mle ndani ili kuona iwapo kuna kitu chochote kilichobadilishwa, kwani Clara hakuwa na mazoea ya kuingia chumbani kwake kabisa.
Kila kitu kilikuwa kama alivyokiacha.
Alivua shati na kulitupia juu ya kiti kilichokuwa nyuma ya meza ya kusomea mle chumbani, na alikuwa analiendea kabati dogo lililokuwa kando ya ile meza ili achukue taulo ndipo alipoiona.
Katikati ya kitanda chake kulikuwa kuna kadi nzuri na kubwa iliyonakshiwa kwa michoro ya maua mazuri kwa rangi ya dhahabu. Akiwa amemakinika aliichukua na kuitazama kwa karibu zaidi, na hapo alihisi mlipuko fulani moyoni mwake, kisha ubaridi akamtambaa mwilini. Hali hiyo ilimpitia kwa kama nusu sekunde hivi halafu joto la mwili wake likarudi kama kawaida na akahisi kijasho kikimtiririka kufuata uti wake wa mgongo.
Juu ya ile kadi kulikuwa kuna maandishi makubwa yaliyocharangwa kwa rangi ya dhahabu.
I Love You With All My Heart.
Heh!
Nakupenda kwa moyo wangu wote.
Ni maneno yaliyomtoa kijasho Jaka. Kama mwenye kutaka kuhakikisha, aliifungua ile kadi na hapo kipande cha karatasi kilichokunjwa vizuri kilidondoka kutoka ndani ya ile kadi. Hakufanya haraka kukiokota,bali alibaki akikodolea macho kile kilichokuwa kimeandikwa ndani ya kadi ile.
“Dear Jaka,” ilikuwa imeandikwa kwenye kona ya kushoto kwa juu ndani ya ile kadi. Halafu katikati yake kuliandikwa maneno kwa lugha ya kiingereza yaliyotafsirika kama:
Pokea ujumbe wa dhati kutoka ndani kabisa ya moyo wangu.
Na kwenye kona ya kulia kwa chini, kadi ile ilikuwa imeandikwa kwa lugha ile ile ya kiingereza:
Ni mimi, pamoja na upendo wa dhati, Clara.
Alishusha pumzi ndefu na kuketi taratibu pale kitandani. Naam, ama kweli sasa mambo yalikuwa yameanza. Hakujua afanye au aseme nini. Alibaki akiwa amepigwa na butwaa tu. Kabla hajajua ni hatua gani ifuate, akakiona kile kijikaratasi kilichoanguka pale sakafuni kutoka kwenye ile kadi. Alikiokota na kukifungua. Kwa lugha ile ile iliyotumika kwenye kadi, kilikuwa kimeandikwa maneno yaliyotafsirika:

Nimekuonesha kila kinachohitajika,
Nimekufungulia kila kilichofungwa,
Lakini wewe, wewe hutaki kuangalia,
Na mimi sasa, sasa nakupasulia,
Moyo wangu uko radhi,kwako kutulia,
Iwapo utaridhia, kwangu kutulia.

Akupendaye, Clara.

Nguvu zilimwisha.
Hivi huyu msichana ana akili sawasawa kweli...? Hajui chochote kuhusu maisha yangu, hajui iwapo naweza kuwa mtu hatari kwake au la, halafu ana...
Alishindwa kumalizia mawazo yake na akaishia kusonya. Alisikia vishindo laini vya Clara akipita nje ya chumba chake. Alitamani amtokee na ampe mawazo mawili matatu kuhusu swala la mapenzi baina yao na jinsi lilivyokuwa ni wazo la kipuuzi kuliko yote aliyowahi kuyasikia maishani mwake, lakini aliamua kutulia kwanza.
Baada ya kuoga Jaka alienda kukaa sebuleni akiwa tayari ameamua kumueleza kwa utaratibu kuwa hawawezi kuwa wapenzi. Clara alikuwa akijishughulisha na mapishi jikoni, jambo ambalo si la kawaida kwani kila siku msichana wa kazi huwa anakuwa amewapikia kabla ya kuondoka na kurudi tena asubuhi ya siku iliyofuata.
Aliamua kumfuata kule kule jikoni ili ajaribu kuongea naye juu ya swala lile.
"Yap! Mambo?" Clara alianza kumsalimia kwa uchangamfu alipoingia mle jikoni.
"Safi..." Jaka alijibu kwa mashaka kidogo, lakini kabla hajasema lolote zaidi,Clara aliongezea, "Umekuja kunisaidia kupika nini?" Alikuwa katika hatua ya kugeuza vipande vya kuku alivyokuwa akikaanga. Pembeni Jaka aliona viazi vilivyokaangwa, hivyo akajua kuwa Clara alikuwa anatayarishwa mlo wa chipsi kwa kuku. Pia aligundua kuwa Clara alikuwa anajitahidi kukwepa kumtazama usoni. Kabla Jaka hajajibu lile swali aliloulizwa Clara akamtuma.
"Naomba ukaniletee sahani pale kabatini."
Shit!
Jaka alilaani kimoyo moyo huku akitekeleza.
"Naona leo uliamua kutembelea chumbani kwangu" Alimwambia huku akimkabidhi sahani. Clara aliipokea sahani ile na kuendelea na upishi wake kama kwamba hakumsikia. Jaka aliendelea kumtazama, akisubiri jibu.
"Hukupendezewa?" Hatimaye Clara alimjibu kwa swali.
Aan-haa, kumbe ulisikia swali langu.
"Si hivyo, ila tu nilikuwa..."
"Ah, jamani! Basi Jaka naomba unisaidie kukata vitunguu ili tupate kachumbari, mi' n'takata nyanya na karoti." Alimkatiza kabla hajapata fursa ya kujieleza.
Jaka akajikuta anakata kachumbari na Clara jikoni badala ya kumwelezea ukweli aliodhamiria kumweleza. Wakati Jaka akiwa amekereka na hali ile, Clara alionekana kuifurahia sana. Jaka alijaribu tena kuuanzisha ule mjadala wakati wakiwa mezani wanakula.

MAMBO YANASOGEA ZAIDI. NINI KITAENDELEA?!
 
SEHEMU YA KUMI NA MBILI

Aan-haa, kumbe ulisikia swali langu.
"Si hivyo, ila tu nilikuwa..."
"Ah, jamani! Basi Jaka naomba unisaidie kukata vitunguu ili tupate kachumbari, mi' n'takata nyanya na karoti." Alimkatiza kabla hajapata fursa ya kujieleza.
Jaka akajikuta anakata kachumbari na Clara jikoni badala ya kumwelezea ukweli aliodhamiria kumweleza. Wakati Jaka akiwa amekereka na hali ile, Clara alionekana kuifurahia sana. Jaka alijaribu tena kuuanzisha ule mjadala wakati wakiwa mezani wanakula.
"Clara...nilikuwa naomba tuongee kidogo kuhusu jambo ambalo nadhani linatuhusu sote..."
"Mmmnh! Sasa si tunakula jamani Jaka? Huwezi kusubiri hadi tukamaliza?" Clara alimkatisha huku akitabasamu, na kuendelea, "kwanza mbona husifii upishi wangu, au sijui kupika ?"
"Ah, chakula kizuri sana..."
"Na kadi yangu?" Aliuliza kwa sauti ya chini huku akiinamisha uso wake. Jaka hakusikia vizuri, akamwomba arudie tena. Clara akauliza tena huku ameinamisha uso, bila shaka kwa aibu.
Ilitakiwa uone aibu kabla ya kuniandikia kadi ile bibie...sio baada!
"Ni nzuri...asante...na nilikuwa nataka kuongelea juu ya swala hilo hilo Clara..."
"Tule kwanza basi."
Waliendelea kula wakiwa kimya. Baada ya kula na kuondoa vyombo, Clara aliaga kuwa anaenda kulala kutokana na uchovu. Jaka alishangaa, kwani walikubaliana kuongea baada ya kula.
"Hey! Tuna maongezi mimi na wewe Clara, umesahau?"
"Ah! Bwana mi' nimechoka...tuongee kesho basi, eeenh?" Clara alimjibu kivivu huku akijinyoosha. Kisha aligeuka na kuelekea chumbani kwake bila kumwangalia wala kusubiri mjadala zaidi.
Jaka alifura kwa hasira. Alitamani amrukie na amtikise kwa nguvu sana mpaka akili yake ikae sawa ndani ya bichwa lake, na kisha amueleweshe kuwa iwapo alikuwa anampenda, basi yeye alikuwa hampendi na hivyo hawawezi kuwa wapenzi na pia ni kinyume cha uungwana.
Lakini alibaki akiwa ameduwaa tu pale mezani, akiikodolea macho sehemu ambayo yule binti alikuwa amesimama sekunde chache zilizopita.
Hiyo ilikuwa jana usiku.
Na sasa akiwa amekaa nyuma ya meza yake pale ofisini alikuwa akijiuliza maswali mengi.
Ni kweli alikuwa hampendi yule msichana?
Alikumbuka siku ile alipojikuta chumbani kwa yule binti baada ya kupoteza fahamu kutokana na kipigo ambacho kilikuwa kinampeleka moja kwa moja kwenye himaya ya ziraili. Yule binti alimtoa nguo zote na kumsafisha mwili wake uliotapakaa damu na petroli.
Ni kweli kuwa yule binti haujui undani wake?
Alikumbuka maneno ya mzee Mnyaga.
Jaka, yule msichana anakupenda! Tena anakupenda kwa nia nzuri tu...
Ni kweli?
Je, hii itakuwa heshima kweli kwa mzee Zaza, baba yake Clara?
Isitoshe, kwa tabia iliyojengeka ya vijana wengi kupenda kulelewa na akina mama au akina dada wenye pesa, ni dhahiri kuwa ataonekana kuwa ni yeye ndiye aliyemshawishi yule binti kimapenzi ili apate kufaidi matunda ya utajiri wake.
Jaka hakupenda kabisa kunasinishwa na tabia hiyo chafu.
Lakini ni nani atakayeamini kuwa ni Clara, na sio yeye, ndiye amekuwa chanzo cha penzi hilo?
Roho ilimuuma. Alijiona kuwa amenswa kwenye mtanziko mkubwa sana.
Kwa nini kila linapokuja swala la uhusiano wa kimapenzi baina ya mvulana na msichana, ni mvulana ndiye ambaye siku zote anabebeshwa lawama iwapo penzi hilo litaingia vipingamizi fulani?
Sasa kabla hajajua hatima ya swala lile tete baina yake na Clara, limezuka swala jingine ambalo bila shaka ni tete zaidi!
Ni nani huyu anayevaa koti refu na kofia pana anayepita akiulizia habari zake? Anataka nini?
Mawazo haya yalimsakama siku nzima pale ofisini pasina kuyapatia ufumbuzi wowote.

__________________

Jioni ile aliporudi nyumbani alimkuta Clara akiwa amejiinamia pale sebuleni. Ingawa runinga ilikuwa imewashwa, Clara hakuwa na habari nayo kabisa. Alikuwa amekaa kwenye kochi refu huku miguu yake yote miwili akiwa ameipandisha juu ya kochi lile na kufanya magoti yake kuwa sawa na kidevu chake. Alikuwa amevaa gauni jepesi la usiku lililokuwa limemkaa vyema sana. Weupe wa gauni lile ulimkumbusha Jaka ile ndoto aliyokuwa akiiota mara kwa mara huko nyuma, na moyo wake ukapiga mshindo.
Hakuwa ameifikiria ile ndoto kwa muda mrefu, sasa kwa nini ameikumbuka wakati ule?
Clara aliinua uso wake na kumtazama, na Jaka akaona kuwa yule binti hakuwa mwenye furaha kabisa. Walitazamana kwa sekunde kadhaa kisha Clara alirudia kujiinamia bila ya kumsemesha. Akajua kuwa Clara bado alikuwa amekasirika kutokana na yale yaliyotokea baina yao asubuhi ile kule ofisini.
Sasa kwani ye’ alitegemea nini? Alitaka nishangilie kwa kuniletea ile kadi?
"Clara, vipi...niliambiwa uliondoka mapema ofisini kutokana na maumivu ya kichwa..." Alimsemesha.
"Kwani we' unajali chochote hata kama nikiumwa?" Baada ya kimya kifupi Clara alimjibu kwa swali.
"Come on, Clara, unajua kuwa mi' n'najali..." Alianza kumjibu, lakini hapo Clara aliinua uso na kumtazama kwa macho ya hasira na yenye kukata tamaa. Yalikuwa yamejaa machozi ingawa bado yalikuwa hayajaanza kutiririka kutoka kwenye macho yale ya kuvutia. Jaka alijikuta akipiga hatua tatu za haraka kumsogelea pale kochini akitaka amshike, amfute yale machozi ambayo hakuwa na uhakika kuwa yalitokana na maumivu ya kichwa au hasira. Kabla hajamgusa Clara alimnyooshea mikono yake yote miwili kumwashiria kuwa asisogee zaidi.
"Usiniguse, Jaka!"
Jaka alisimama na kuduwaa.
Sasa yale machozi yalianza kumtiririka Clara.
"Clara...kwani vipi...?"
Akiwa amekaa vile vile pale kwenye kochi, Clara aliikumbatia miguu yake kwa mikono yake huku akimtazama Jaka kwa macho makali.
"Hivi we' unanionaje mimi?" Clara alimuuliza taratibu.
Kabla Jaka hajajua cha kujibu, binti aliendelea, "Leo nimekuja ofisini kwako ukajitia kuninunia...kisa nini? Eti nimekuandikia kijibarua na kadi vilivyokuwa na ujumbe kuwa nakupenda..!"
Jaka bado aliendelea kuduwaa, akijaribu kuitathmini ile hali.
"Kwa hiyo umeniona kuwa mimi najipendekeza na najirahisi mno kwako, sio? Siku zote nikikuonesha kuwa nakupenda wewe unajifanya huelewi, au unajitia huoni. Kwa vile umeshajua kuwa nakupenda basi ndio unaamua kunidharau na kunitesa...mimi nilidhani kuwa wewe ni mtu muwazi na mwenye kuelewa, kumbe nilidhani vibaya!" Clara aliendelea kumtupia maneno yaliyomkaa moyoni.
"Sio hivyo Clara...wewe ndio huelewi..." Jaka alijaribu kujitetea, lakini hapo Clara aliinuka kutoka pale kwenye kochi na kupiga hatua mpaka pale alipokuwa amesimama. Alimuinulia uso wake na kumuuliza huku machozi yakiendelea kumtiririka, “Sielewi nini Jaka...hebu nieleze ni nini nisichokielewa mimi, eenh? Au unataka nikueleze ninachoelewa? Unataka kujua ni nini ninachoelewa ambacho wewe unadhani sikielewi....?” Sasa Clara alikuwa anaongea huku akisaidiwa na kichwa pamoja na mikono yake yote miwili, hali sauti yake bado ikiwa kali lakini ya chini.
Jaka alibaki amebutwaika. Hajawahi kumuona Clara katika hali kama ile na wala hakutegemea kuwa angeweza kumuona katika hali kama ile.
“No! Nilichotaka kukuelewesha ni…”Jaka alijaribu kuongea, lakini Clara hakutaka kumsikiliza.
"Huna lolote la kunielewesha Jaka! Mimi naelewa kuwa unanipenda! Unanipenda, na unanitaka. ila unaogopa...!"
Khah!
"We' una wazimu nini?" Hii ilikuwa kali kuliko, na Jaka alijikuta akifoka bila kuelewa kwa nini alikuwa anafoka.
"Ndio! Mimi n’na wazimu, tena n’na wazimu sana...!" Clara naye alianza kufoka.
"Mimi jana nilitaka niongee na wewe juu ya mambo haya, lakini we’ ukajitia kunikwepa ukaenda kulala...ulitegemea mimi niichekelee hali hiyo?"
"Eti kuongea na mimi! Mimi nilishaongea na wewe kabla ya hiyo jana Jaka...na niliongea kwa sauti ambayo wewe ulishindwa kuielewa, na ndio maana ikabidi nikuandikie...!”
"Hatujawahi kuongea juu ya swala hili mimi na wewe hata siku moja Clara, na we' unajua hilo!”
"Mimi nimeongea nawe kwa sauti ya moyoni! Na nimelisikia penzi lako kwangu kutoka moyoni mwako, na si kinywani mwako. Sauti ya moyoni husikiwa na moyo, sio na masikio, na huwa inatoka moyoni na sio mdomoni...sauti ya moyoni huhitaji kueleweka zaidi kuliko kusikiwa; ni wewe ndiye huelewi Jaka, sio miye!”
Heh!
Jaka alibaki kinywa wazi. Hakutegemea kusikia maneno kama yale kutoka kwa Clara. Mshangao huo ulipita upesi sana, kisha nae akajibu huku akitikisa kichwa.
“Usitegemee kuwa moyo uliokwisha kufa unaweza kufufuka tena ili kuja kusikia sauti iliyochelewa Clara...”
“There is never too late for love Jaka and you should know that!” Clara alimfokea kwa jazba, akimaanisha kuwa kwenye penzi hakuna kuchelewa, na kwamba Jaka alitakiwa awe analijua hilo.
“Hiyo dhana ya moyo uliokufa ni njia yako ya kujidanganya tu juu ya swala hili...inaweza kuwa uliumizwa kimapenzi huko nyuma but so what? You can always love again, and I am giving you that chance, god damn it! Nipe nafasi uone!” Clara aliendelea kwa ukali, akimaanisha kuwa si hoja iwapo alishawahi kuumizwa katika penzi huko nyuma, kwani anaweza kupenda upya tu wakati wowote, na kwamba yeye alikuwa anampa nafasi ya kupenda upya…basi na aichukue hiyo nafasi ajionee.
Duh!
Kwa mara nyingine tena Jaka alipigwa na butwaa kwa maneno yale makali kutoka kwa Clara. Ilikuwa wazi kwamba alikuwa anaelekea kushindwa kwenye malumbano yale makali.
“Ni wewe ndiye unayejidanganya kuwa tunaweza kuwa wapenzi...sisi ni watu tulio pande mbili tofauti Clara. Sijui kwa nini hulioni hilo..maana halihitaji digrii...liko wazi kabisa!" Alimjibu kisha akageuka kuelekea chumbani kwake bila hata ya kujua alikuwa anaenda kufanya nini.
"Siwezi kuliona hilo kwa sababu moyo unapozidiwa hutoa sauti yake kwa njia yoyote ile ili usikike...mimi nakupenda Jaka...nakupenda wewe kama ulivyo....sijali kuwa umehukumiwa kwa kosa la mauaji kwa sababu najua kuwa wewe si muuaji na wala hukuua..." Clara alimjibu kwa sauti ya chini akiwa amesimama pale pale alipokuwa.
Jaka alisita kwenye hatua zake. Kisha akageuka taratibu na kumtazama kwa kutoamini yule msichana. Clara alikuwa amesimama pale sebuleni, shingo yake ameilaza upande na mikono yake ameiacha ikining'inia kila upande wa mwili wake. Uzito wake wote alikuwa ameuegemeza kwenye mguu wake wa kushoto ilhali mguu wake wa kulia akiwa ameukunja kwenye goti na umesogea mbele kidogo. Machozi yalikuwa yakimtiririka naye wala hakuonesha kujua kuwa alikuwa akitokwa na machozi.
Ilikuwa ni picha mtu aliyekata tamaa na mwenye huzuni kubwa kabisa, na kwa hakika alimtia simanzi kubwa sana Jaka.
Na alipokuwa akimtazama yule binti akiwa amesima kwa simanzi isiyosemeka huku akibubujikwa machozi namna ile, taswira ya yule binti kama alivyokuwa akimlilia kwenye ile ndoto ikamrudia, na sanjari na mlipuko wa kumbukumbu ya ndoto ile, ukweli aliokuwa akipingana nao ukamshukia na kumvaa kama joho fahamuni mwake.
Ni kweli alikuwa akimpenda yule binti!
Huo ni ukweli ambao siku zote amekuwa akishindana nao. Siku zote amekuwa akihisi kuwa kuuruhusu ukweli ule umtawale kungekuwa ni kosa kubwa sana kwake kwani kusingemletea isipokuwa majuto tu...
Lakini sasa mtoto ndio ananililia huyu jamani…sio kwenye ndoto tena, bali wazi wazi mbele ya macho yangu! Ameridhia mwenyewe huyu! Kanitamkia kwa maandishi na kwa kinywa bloody hell…nafanyaje sasa?
"We’ unajaribu kuukimbia ukweliJaka...hutaki kukubali kuwa mambo yaliyokutokea yamekutokea wewe na kwamba una nafasi ya kuikubali hali iliyopo na kuishi nayo..." Clara aliendelea kumweleza taratibu huku machozi yakimtoka.
Akilini mwake Jaka alikumbuka maneno ya mzee Mnyaga.
...wewe unataka kushindana na ukweli, unataka kubadili hali ambayo tayari historia imeshaamua kuiweka...
Akili ilimzunguka.
Sauti ya Clara ilizidi kumfikia masikioni mwake.
“...yule Jaka wa zamani ni wewe, na huyu wa sasa pia ni wewe Jaka, huo ni ukweli ambao huwezi kuufuta. Unapojaribu kuukimbia ukweli huu Jaka, unakuwa ni sawa na unayejaribu kujikimbia wewe mwenyewe, na hivyo unakuwa hujijui wewe ni nani na unataka nini hapa duniani! Amini usiamini Jaka, huwezi kufika huko unapokimbilia mpaka kwanza ukubali kujitambua na kujikubali...”
“Dah, Clara…”
“…mimi nakupenda kama ulivyo sasa Jaka. Sijui huko nyuma ulikuwaje au ulifanya nini, hilo kwangu si tatizo, na nipo tayari kuwa na wewe mwanzo-mwisho katika matatizo yote unayohofia kuwa yatatokea huko mbeleni..."
Sasa hii ilikuwa imezidi.Jaka hakuweza kuvumilia zaidi. Aliziba masikio yake kwa viganja vya mikono yake huku akimaka kwa kelele.
"Basi! Basi! Basi....inatosha....!"
Clara aligutuka na kumshangaa pale alipomuona akatoa mikono yake masikioni na kupiga ngumi ndani ya kiganja chake kwa hasira.
"We' unataka nini kwangu lakini mimi, eenh? Nimeshakwambia kuwa mimi siwezi...siwezi, tena siwezi kabisa!" Alifoka kwa hasira na kuchanganyikiwa.
Clara nae akamjibu, sasa machozi yakiwa yanambubujika kama maji na akiongea kwa uchungu mkubwa.
"Hivi wewe unafikiri mimi napenda sana wanaume...? Au unadhani ni kwa nini najidhalilisha na kujiangusha kwako kiasi hiki, eeenh...?"
"Hayo yote yako Clara...mimi ninachosema ni kwamba sitaki hicho kitu unachotaka wewe, na sitaki kwa vile moyo wangu hauko tayari...mi' niko tayari kuondoka hapa nyumbani kwako Clara, na hata kufukuzwa kule kazini, lakini heshima yangu kwako na kwa mzee Zaza kwangu ni kitu cha maana sana..."
"Ndio! Moyo wako hauko tayari kwa sababu hutaki kutembea na janamke malaya, huni...lenye kupapatikia kila mwanaume limuonaye, sio? Laiti ungejua...!" Clara alipandisha sauti kwa jazba.
“Hayo yote yako Clara, mimi sijasema hivyo! Ninachosema ni kwamba…”
"Kwa taarifa yako mimi pia nina heshima zangu na ninaujali sana usichana wangu! Hii kukupenda wewe ni moyo wangu tu ndio umeamua kunishusha chini na kunidhalilisha kiasi hiki..lakini nilifanya hivyo nikijua na nikiamini kuwa na wewe unanipenda na ni mtu mwenye kuelewa...Ni mara ngapi nimekufuma ukinitazama kwa matamanio? Sa’ sijui unaogopa nini! Hujui maana ya kupendwa masikini...!" Hapo Clara hakuweza kuendelea kwani kwikwi zilimzidi. Uchungu wa maneno yake ulimkaba na alianza kuangua kilio. Kama kwamba alikuwa ameelemewa na uchungu ule, alidondokea magoti huku akiendelea kulia akiwa amekalia visigino hali kiwiliwili chake amekiegemeza nyuma. Alijiziba mdomo kwa viganja vya mikono yake miwili akijaribu kila mafanikio kuzuia sauti ya kilio chake

ITAENDELEA
 
SEHEMU YA KUMI NA TATU

"Kwa taarifa yako mimi pia nina heshima zangu na ninaujali sana usichana wangu! Hii kukupenda wewe ni moyo wangu tu ndio umeamua kunishusha chini na kunidhalilisha kiasi hiki..lakini nilifanya hivyo nikijua na nikiamini kuwa na wewe unanipenda na ni mtu mwenye kuelewa...Ni mara ngapi nimekufuma ukinitazama kwa matamanio? Sa’ sijui unaogopa nini! Hujui maana ya kupendwa masikini...!" Hapo Clara hakuweza kuendelea kwani kwikwi zilimzidi. Uchungu wa maneno yake ulimkaba na alianza kuangua kilio. Kama kwamba alikuwa ameelemewa na uchungu ule, alidondokea magoti huku akiendelea kulia akiwa amekalia visigino hali kiwiliwili chake amekiegemeza nyuma. Alijiziba mdomo kwa viganja vya mikono yake miwili akijaribu kila mafanikio kuzuia sauti ya kilio chake.
Alilia kwa uchungu sana, na kilio kile kilisababisha mabega na kichwa chake kutikisika kwa kila kwikwi aliyopiga. Katika zile sekunde chache kabla hajadondoka na kupiga magoti pale sakafuni, Jaka alimkumbuka tena yule msichana kama alivyomuona kwenye ndoto ile iliyokuwa ikimjia mara kwa mara. Na katika sekunde zile Jaka alipata wasiwasi iwapo na ile pia haikuwa ndoto. Hakika aliomba sana iwe ndoto, lakini alijua kuwa haikuwa ndoto. Alitafuta maneno ya kusema, hakuyapata. Aliendelea kumtazama yule binti tajiri akilia pale chini na lile joho la ukweli aliokuwa akishindana nao lilizidi kumbana kila kona ya mwili, hisia na fahamu zake.
Nampenda huyu msichana jamani...haki ya Mungu nampenda!
Sasa mateso yote haya ni ya nini?
Alipiga hatua mpaka pale Clara alipokuwa na kumwinamia huku akimshika mabega.
"Clara...Clara..." Alianza kuongea lakini alishinndwa kuendelea. Clara aliikung’uta mikono yake kutoka mabegani mwake huku akitupa mikono na kutikisa kichwa chake kwa nguvu.
"Don't touch me! Don't touch me at all Jaka! Just leave alone damn it!" Alibwata kwa hasira huku akilia, akimaanisha kuwa hakutaka Jaka amguse kabisa, amuache tu kama alivyo.
"Hapana Clara, hapana. Naomba unisikilize tafadhali...tafadhali sana hebu tulia kwanza!" Jaka alijitahidi kumshika mikono ile ambayo sasa ilikuwa ikimpiga kila sehemu.Usoni, kifuani, mabegani…kila mahali kwani sasa Jaka nae alikuwa amepiga magoti mbele ya yule binti. Lakini Clara aliendelea tu kutupa mikono na kutikisa kichwa huku akilalamika.
"Sitaki! Niachie..don't you dare touch me goddamn it! Just Don't! "
Jaka alijitahidi kumzuia hatimaye alifanikiwa kumkamata mabega na na kumvutia kwake, na hivyo kuibana mikono ya yule mwanadada baina ya vifua vyao viwili. Clara aliendelea kufurukuta lakini Jaka alikuwa amembana kwa nguvu huku akimuongelesha kwa kubembeleza.
"Clara naomba unisikilize basi..."
"Leave me alone Jaka..." Clara alimbishia huku akizidi kufurukuta. Hapo Jaka alimtikisa kwa nguvu sana huku akifoka, "Clara tulia basi unisikilize!”
“Sitaki!”
“Sikia basi kwanza wewe!”
“Niache nimesema na umalaya wangu, fala we!”
“Nakubali nilikuwa mjinga...tena fala kweli kweli! Lakini sasa...lakini...Oh, I love you! Clara, I love you...!"
Kimya!
Ilichukua kama sekunde tatu hivi kwa maneno yale kuzama akilini mwa Clara. Alitulia kimya na kubaki akimkodolea macho ya kutoelewa au kutoamini yule rijali aliyemkumbatia pale sakafuni, kama kwamba ndio anamuona kwa mara ya kwanza. Alishangaa kuona kuwa na Jaka naye alikuwa akitiririkwa machozi. Jaka aliyaangalia macho ya Clara yaliyokuwa yamemkodolea na aliona jinsi yalivyokuwa yanajitahidi kuamini maneno yake. Walibaki wakitazamana kwa muda kabla Jaka hajauvunja ukimya ule.
"Ndio Clara, nakupenda, nakupenda sana, Clara. Tafadhali nyamaza kulia...hakika nilikuwa bonge la fala!"Alimwambia kwa sauti ya upole sana huku akimtazama moja kwa moja machoni.
Loh!
Clara alimtazama Jaka kwa mshangao mkubwa kabisa. Hakika alikuwa haamini aliyokuwa akiyasikia. Jaka alimtikisia kichwa chake taratibu kumuashiria kuwa aliyoyasikia ni haki kabisa. Hapo midomo ilianza kumcheza huku kwa mikono iliyotetemeka akianza kumfuta Jaka machozi.
“Oh, Clara…” Jaka naye alianza kumfuta machozi.Clara aliangua kilio kipya.
"Sikukuona malaya wala muhuni Clara...nakubali kuwa nilipata mawazo mabaya juu yako, lakini ukweli ni kwamba wewe ni msichana mzuri sana. Kwa sura na tabia. Sikupenda nije nikuharibie maisha yako...kwa sababu mimi ya kwangu yalishaharibika zamani na sina uhakika na maisha yangu ya baadaye! Wewe una kila sababu ya kujitengenezea maisha bora zaidi ..."
Kilio kilizidi kuongezeka kwa Clara.
"...lakini vile vile lazima nikiri kuwa ni kweli nilikuwa nashindana na ukweli Clara, na ukweli wenyewe ni kwamba nakupenda sana Clara...nakupenda na sitaki nikuache kwa hata dakika moja..."
Hapo ndio ilikuwa kama ametoa idhini rasmi, kwani Clara aliachia kilio cha sauti huku akimzungushia mikono yake shingoni na kumkumbatia kwa nguvu.
"Oh! Jaka...Jaka...jamani…." Alibwabwaja huku akilia kwa furaha yule mwanadada. Jaka nae alimkumbatia kwa upendo yule huku akitiririkwa machozi, donge kubwa likiwa limemkaba kooni. Alijihisi kama aliyetua mzigo mzito uliokuwa ukimuelemea kwa muda mrefu.
Wakiwa wamekumbatiana huku wamepiga magoti pale chini namna ile, wote wawili walijua kuwa ule ulikuwa ni mwanzo wa penzi lililokuja baada ya vikwazo kadhaa.
Na kwa wakati ule hakuna aliyejali ni nini kingetokea baadaye.
6
Mapenzi baina yao yalishamiri upesi sana. Jaka alijiona kama mtu aliyezaliwa upya katika ulimwengu wa wapendanao. Katika muda huo aliokuwa na Clara kama mpenzi, rafiki na mshirika wake wa karibu, Jaka aliweza kumeelezea Clara mambo yote yaliyomtokea wakati akiwa Dar es Salaam mpaka alipojikuta pale Dodoma; ingawa bado kulikuwa kuna mambo machache ambayo alidhani haikuwa lazima kwa Clara kuyajua.
Siku kadhaa baada ya lile tukio lililoishia kwenye ahadi ya mapenzi mazito baina yake na Clara pale sebuleni Jaka alikuwa akiendesha gari la kampuni ya Zaza Cargo Movers kuelekea ofisini huku akikumbukia matukio ya siku ile, matukio ambayo yaliishia kwa wao kuamka asubuhi iliyofuata wakiwa kitandani kwa Clara. Na baada ya usiku ule hakika aliazimia kumpenda kwa moyo wake wote yule binti, kwa kadiri atakavyojaaliwa.
Tangu mapenzi yao yaanze, walikuwa wametembelea sehemu mbali mbali za starehe pale mjini na mara nyingi wamekuwa wakienda picnic nje ya mji, kwenye vilima tulivu vya pale Dodoma. Ilikuwa ni furaha sana kuwa pamoja, na hili Jaka alilithamini sana.
Aliegesha gari nje ya kituo cha polisi na kuingia mle ndani ili kusaini kama ilivyo ada. Alimkuta Osman Mgunya pale ofisini naye alisaini bila ya kumsemesha neno na kuanza kuondoka.
“Naona sasa umesahau kabisa kuwa unatumikia adhabu kwa kosa la mauaji, eeenh?” Osman alimtupia kauli ya kichokozi. Hakumjibu wala hakusimama. Alitoka nje na kufungua mlango wa gari lake kwa nia ya kuondoka eneo lile, lakini akajikuta akisita na kukunja uso huku mguu mmoja tayari ukiwa ndani ya gari. Upande wa pili wa barabara kulikuwa kuna mtu mmoja aliyesimama chini ya mti kama anayesubiri kuvuka barabara. Alitoa miwani yake ya jua usoni, kisha akatoa kitambaa kwa mkono mmoja huku ule mwingine bado ukiwa umeshikilia ile miwani. Alianza kuifuta ile miwani taratibu. Muda wote aliokuwa akifanya matendo hayo, macho yake yalikuwa yakimtazama yule mtu aliyekuwa upande wa pili wa barabara, kwani kuna kitu kilimvutia kuhusu yule mtu.
Jamaa alikuwa amesimama upande wa pili wa barabara akiangalia kule kule ambako Jaka alikuwepo, na kwa muda wa dakika kama tatu hivi barabara ilikuwa tupu kiasi cha kutosha mtu yeyote kuvuka, lakini yule mtu hakufanya bidii yoyote ya kuvuka barabara ile. Hapo Jaka akajua kuwa yule jamaa alikuwa akimtazama yeye. Naye aliendelea kumtazama.
Alijitahidi japo kupata muundo tu wa sura ya yule mtu kwa umbali ule lakini alishindwa, kwani sehemu kubwa ya sura ya yule mtu ilikuwa imefunikwa kwa kofia pana kama zile uzionazo kwenye filamu za kimarekani za Cowboys au Westerns.
Chini ya uzio wa kofia ile Jaka aliweza tu kuona sehemu ya mdomo na kidevu chake kilichozungukwa na ndevu zilizochongwa vizuri katika umbo la herufi “O”.
Chini, yule mtu alikuwa amevaa koti refu lililoteremka mpaka chini ya magoti yake, ambapo Jaka aliweza kuona suruali ya rangi ya kahawia ikitokeza chini ya koti lile na viatu vyeusi vilivyopanda juu kidogo kama vya jeshi. Kola za koti lile jeusi alikuwa amezisimamisha kama vile aliyetaka kujikinga na baridi na mikono yake yote miwili alikuwa ameizamisha kwenye mifuko ya koti lile.
Jaka alirudisha miwani yake usoni taratibu kisha akaingia garini nakufunga mlango. Yule mtu alikuwa amesimama pale pale alipokuwa, akiendelea kuangalia upande ule lilipokuwa gari lake. Jaka alipata wazo la kumfuata yule mtu pale alipo na kumuuliza kwa nini alikuwa akimfuata-fuata, kwani alikuwa na hakika kabisa kuwa huyu ndiye yule mtu aliyekuwa akiulizia habari zake kwa mlinzi kule ofisini kwake. Lakini aliamua kutofanya hivyo, kwani aliamini kuwa iwapo yule mtu alikuwa ana haja ya kuonana naye, basi ni yeye na sio Jaka ndiye anayepaswa kufanya jitihada ya kukutana naye uso kwa uso. Aling’oa gari na kuondoka eneo lile, akimuacha yule mtu alikuwa amesimama pale pale.
Jioni ya siku ile alimuelezea Clara kuhusu yule mtu, na wote walikuwa na mawazo kuwa mtu yule, ambaye waliamua kumpachika jina la John Doe, angeweza kuwa ni kibaraka wa Osman Mgunya aliyetumwa kumfuatilia Jaka ili kuhakikisha kuwa Jaka anapata balaa pale Dodoma. Jambo lile liliwakera sana.
“Kwa nini usimshitaki kwa mkuu wake wa kazi?” Clara aliuliza.
“Nimshitaki nani?”
“Osman Mgunya.”
“Aaah, bado hatuna ushahidi wowote kuwa ni kweli yule mtu ametumwa na Osman....” Jaka alijibu kwa kukata tamaa.
“Mnh! Ila kweli. Sasa...?” Clara aliafiki na kuhoji.
“Hebu tusuiri tuone kama ataendelea kunifuatilia...na iwapo ataamua kuweka wazi dhamira yake kwangu.” Jaka alimwambia.
John Doe alikuja kuonekana tena siku mbili baadaye.
Ilikuwa ni siku ya Jumamosi nao waliamua kwenda kwenye ukumbi wa disko kujiburudisha. Ni Clara ndiye aliyetoa wazo hilo baada ya kuona kuwa Jaka alikoseshwa raha sana na swala la John Doe.
Kwa siku mbili Jaka alikuwa na mawazo mengi kuhusu yule jamaa. Alijiuliza sana kuwa iwapo John Doe hakuwa ametumwa na Mgunya, atakuwa ametokea wapi? Na anataka nini? Alijaribu kukumbuka matukio yote yaliyomtokea kule Dar kabla ya kuletwa kwake pale Dodoma na kadiri alivyotafakari ndivyo alivyozidi kuamini kuwa John Doe atakuwa ametokea Dar es Salaam japo hakuwahi kabisa kukutana naye huko. Hili lilizidi kumkera, kwani alijua matukio yaliyotokea Dar hayakufikia mwisho na siku zote alikuwa akihofia kuwa yangemrudia tena tu, kwa namna moja au nyingine.
Je, sasa ndio yalikuwa yanamrudia?
Hili jambo lilimfanya aanze kujutia uamuzi wake wa kuingia kwenye mapenzi na Clara, kwani sasa na Clara atakuwa ameingizwa rasmi kwenye matatizo yanayomuandama.
Kitu kingine kilichomkosesha raha ni ukweli kwamba John Doe aliweza kumpata Jaka wakati wowote atakao, wakati yeye hakuwa na namna yoyote ya kumpata iwapo angehitaji kufanya hivyo. Mawazo haya yalimsumbua sana kiasi Clara akaona ni bora waende disko jumamosi ile ili kidogo apumzishe akili yake. Na kwa kweli hilo lilisaidia, na Jaka alifurahi sana.
Walikuwa wanarudi nyumbani kwao kiasi cha saa saba za usiku ule ndipo alipomuona.
Wakiwa kiasi cha kama mita kumi hivi kutoka kwenye geti la nyumba yao huku Clara akiwa nyuma ya usukani, taa za gari lao zilimmulika mtu akiwa amesimama upande wa pili wa barabara akitazama kule ilipokuwa nyumba ya Clara. Mara moja Jaka aliyagundua mavazi ya mtu yule.
“Simamisha gari!” Alimaka huku akiangalia kule alipokuwa amesimama yule mtu.
“Kuna nini...?” Clara aliuliza huku akipunguza mwendo na kusimamisha gari kama alivyoambiwa, lakini Jaka alikwisha ruka nje ya gari kabla hata halijasimama sawasawa. Yule mtu alipoona vile aligeuka na kuanza kuondoka taratibu. Jaka alianza kumfuata kwa hatua za haraka.
“Hey, Jaka vipi? Unaenda wapi...” Clara alimsemesha kwa hamaniko huku akimfuata kwa gari kwa mwendo mdogo.
“Tangulia nyumbani!” Jaka alimjibu huku akianza kumkimbilia yule mtu. John Doe naye akaanza kutimua mbio.
“Simama wewe! Simama laa sivyo nakupigia kelele za mwizi!” Jaka alimpigia kelele huku akizidisha kasi kumfuata. John Doe akaongeza kasi akishika njia ya kuelekea kituo cha kurushia matangazo ya redio cha TBC kanda ya kati, Jaka akimfuata kasi nyuma yake huku Clara naye akiongeza mwendo wa gari kuwafuata. Mbele kidogo John Doe akakunja upenuni mwa ukuta wa kituo cha redio kanda ya kati na kukata kulia kuelekea kwa kasi sana kwenye kichochoro kingine kilichotokezea kwenye uwanja ambao kwa nyakati maalumu huwa unatumika kwa sherehe za mbali mbali za kimkoa, maarufu kama uwanja wa sabasaba. Jaka nae akakunja kona ile kwa kasi huku akiwa hatua chache sana nyuma yake kiasi aliweza kuzisikia pumzi za yule mtu akihema kwa nguvu.
Alipofika usawa wa jengo la ofisi ndogo ya posta tawi la uwanja wa sabasaba, John Doe alitaka kukata kushoto ili apotelee kwenye uchochoro mwingine mdogo. Jaka alijua kuwa akifanikiwa tukuingia kwenye uchochoro ule hatoweza tena kumpata. Pia alihisi kuwa huenda John Doe akawa ana wenzake kule upande wa pili wa uchochoro ule ambao wangeweza kumdhuru.
Hakumpa nafasi hiyo.
Alijirusha mzima mzima na kumdaka kiunoni kwa mikono yake yote miwili. John Doe aliachia yowe la hamaniko huku akipepesukia mbele, na kwa sekunde kadhaa aliendelea kukimbia kwa kuyumba yumba huku akimburura Jaka nyuma y
 
SEHEMU YA KUMI NA NNE

Alipofika usawa wa jengo la ofisi ndogo ya posta tawi la uwanja wa sabasaba, John Doe alitaka kukata kushoto ili apotelee kwenye uchochoro mwingine mdogo. Jaka alijua kuwa akifanikiwa tukuingia kwenye uchochoro ule hatoweza tena kumpata. Pia alihisi kuwa huenda John Doe akawa ana wenzake kule upande wa pili wa uchochoro ule ambao wangeweza kumdhuru.
Hakumpa nafasi hiyo.
Alijirusha mzima mzima na kumdaka kiunoni kwa mikono yake yote miwili. John Doe aliachia yowe la hamaniko huku akipepesukia mbele, na kwa sekunde kadhaa aliendelea kukimbia kwa kuyumba yumba huku akimburura Jaka nyuma yake.
Huku akigumia, Jaka alihisi mikono yake ikianza kuteleza. Akawa amemng’ang’ania koti yule jamaa huku miguu yake ikiendelea kubururwa kwenye ardhi ile iliyojaa kokoto. John Doe akazidi kupepesuka, kasi yake ikaanza kupungua, naye akijitahidi kujitikisa na kujikung’uta ili Jaka amwachie. Akafanikiwa kumchomoa mkono mmoja, na Jaka akabaki akiwa amemng’ang’ania kwa mkono mmoja huku akibururwa vibaya.
“Sim…ma…ma we…wweee!” Alikuwa akimshinikiza yule mtu mwenye koti refu huku akisota vibaya ardhini akiwa amemng’ang’ania kwa mkono mmoja ilhali kwa ule mwingine akijitahidi kujiinua bila ya kupunguza mwendo.
Ilikuwa ni tafrani ya aina yake.
Ghafla John Doe alimgeukia na kofi kali lililomkosa Jaka na kupitia inchi chache juu ya kichwa chake. Kitendo kile kilisababisha lile koti lichanike ule upande ambao Jaka alikuwa ameung’ang’ania kwa mkono wake wa kulia huku John Doe akizidi kukukuruka kwa nguvu ili ajinasue kutoka mikononi mwake. Jaka akamng’ang’ania mguu kwa nguvu na hapo wote wawili wakapiga mweleka mzito. Jaka hakuuachia ule mguu hata kidogo. Sasa John Doe alikuwa anagaragara pale chini huku akijaribu kuunasua mguu wake, wakati Jaka akizidi kuung’ang’ania huku akiutumia kama nyenzo ya kujivutia juu ili amlalie yule jamaa pale chini na kumdhibiti kikamilifu.
Katikati ya rabsha ile John Doe alimfyatulia teke kali sana la uso kwa mguu wake uliokuwa huru. Yowe la maumivu lilimtoka Jaka huku akisukumwa pembeni na mikono ikamlegea. John Doe akajichomoa na kumshindilia kwa soli ya kiatu chake kifuani akiwa bado amelala pale chini, na Jaka akagaragazwa hovyo pale chini huku akigumia kwa maumivu na hasira.
John Doe alikurupuka kutoka pale chini na kutaka kukimbia, lakini Jaka nae alikuwa ameshainuka na aliwahi kumdaka ukosi wa koti lake kwa nyuma kabla hajafika mbali.
“Tulia weweee! Unan’natakia nini mim...” Alianza kumfokea, lakini hapo John Doe alimgeukia kwa konde zito lilitua sawia kwenye “solar plexus”, sehemu nyeti sana iliyopo baina ya pale kifua kinapoishia na tumbo linapoanzia. Jaka alienda chini bila kupenda na kupiga goti moja ardhini huku akipatatapa kutafuta pumzi bila mafanikio. Lilikuwa ni konde zito sana lililomlegeza maungo yote na hakuelewa kwa nini pigo lile lilimfanya vile.
Kwa mbali aliweza kumsikia Clara akiita jina lake huku akikimbilia pale walipokuwa. Aliinua uso wake kumtazama yule jamaa, na kuona kuwa John Doe alikuwa amemsimamia katika ile “honor stance” ya kibondia, kama kwamba alikuwa akimsubiri ainuke ili waendelee na pambano iwapo Jaka angekuwa tayari kuendelea. Lakini ile ngumi ilikuwa kali sana na Jaka hakuwa na nguvu kabisa ya kujiinua kutoka pale chini. Alibaki akiwa amejikunja kwa maumivu huku akimtumbulia macho ya kukata tamaa yule jamaa.
“Wew…we nin…nah…nahh…nannii?” Alimbwabwajia kwa taabu yule mtu huku bado akiwa amejikunja pale chini.
“Jaka! Jak…Ni nini tena hiki lakini? Umekuwaje?” Sasa Clara aliwafikia pale walipokuwa na alikuwa akisaili kwa sauti iliyojaa hamaniko.
“Uh…usingekuja huku Clar…” Jaka aligumia kwa taabu, lakini Clara hakumtilia maanani.
“Who are you, mwanaharamu mkubwa wewe? Umemfanya nini huyu wewe, Eeenh?” Clara alimfokea yule jamaa kwa ukali huku akijitahidi kumuinua Jaka kutoka pale chini.
“No, Clara…ondoka ha…hapa! Ni hatari!” Jaka alijilazimisha kuongea huku akishindana na pumzi zilizoonekana kumbana kwa namna ya ajabu kutokana na pigo alilopokea.
John Doe alimtupia macho yule dada, kisha akamtazama Jaka aliyekuwa akihangaika kuinuka kutoka pale chini huku akisaidiwa na Clara, kisha bila ya kujibu akaruka nyuma hatua tatu, akageuka na kutokomea kichochoroni.
Clara akamtupia tusi la nguoni kwa hasira, kisha akamgeukia mpenziwe.
“Jaka! Jaka...vipi, uko salama...? Ni nani yule?” Alimuuliza huku akitweta.
“Yeah! Niko fiti....” Jaka alijibu kwa kujikakamua huku akiyumba. Mate yalimpalia na akakohoa kwanguvu sana, Clara akimpa pole kwa mashaka makubwa. Alitikisa kichwakwa nguvu kamamtu atakaye kuiweka akili yake sawa.
“Pole mpenzi…lakini…ilikuwaje kwani?”
“Ni John Doe yule!” Jaka alimjibukwa taabu huku wakiwa wameshikana mabega wakirudi kule ambako Clara alikuwa ameliacha gari lao, mbele ya jengo la TBC kanda ya kati.
“John Doe?”
“Yeah, ndiye yeye…mshenzi ana ngumi nzito sijapata kuona, bloody fool!”
Hakuwa na namna ya kujua kuwa yule mtu waliyempachika jina la John Doe alikuwa amempiga ile ngumi mahala pale makusudi, akijua kuwa ingemfanya ashindwe kabisa kumbughudhi. Ilikuwa ni ngumi iliyopigwa kwa uzito uliokusudiwa na ikatua mahala ilipokusudiwa.
Clara aliguna.
Hatua chache mbele yao Jaka aliiona kofia ya John Doe ikiwa imeanguka pale chini. Aliiokota na kuikumbatia kwapani kwake huku akiyumba kuelekea nje ya ule uwanja akisaidiwa na Clara.
Kwa nini umekimbia John Doe…?
Unataka nini kwangu wewe lakini…?

___________________

RPC Januari Mwakaja alishusha pumzi ndefu na kubaki akimtazama Jaka aliyekuwa ameketi kwenye kiti kilichokuwa upande wa pili wa meza yake pale ofisini huku akiigonga gonga meza ile taratibu kwa kalamu iliyokuwa mkononi mwake.
“I see...” Hatimaye alisema huku akiendelea kumtazama yule kijana, uso wake ukionesha kuwa bado alikuwa anajaribu kuyatafakari yale aliyokuwa ameambiwa na Jaka muda mfupi uliopita, kisha akaendelea, “...sasa wewe binafsi ulikuwa una mawazo gani hasa juu ya swala hili?”
Ikawa zamu ya Jaka kushusha pumzi ndefu kabla ya kuingea.
“Kitu ninachoomba kieleweke mzee ni kwamba, ingawa mimi nimeletwa hapa kama mhalifu niliyekuja kutumikia adhabu, bado kuna haki ninazopaswa nitendewe. Wakati nasomewa adhabu yangu sikusikia neno lolote kuhusu kuwekewa watu wa kufuatilia nyendo zangu kinyemela, halafu nikijaribu kuuliza kwa nini wananifuata wanipige...”
“Lakini mpaka sasa hakuna ushahidi wowote kuwa mtu huyo ametumwa na vyombo vya dola, kijana! Kama ingekuwa hivyo basi mimi ndiyo ningekuwa wa kwanza kujua...” January Mwakaja alimbishia.
“Sasa kama hivyo ndivyo, basi hiyo inathibitisha kauli yangu ya mwanzo kuwa maisha yangu yamo hatarini hapa Dodoma! Jambo lolote linaweza kunitokea hapa na wewe usiwe na habari mzee.” Jaka alizidi kuweka wazi mashaka yake.
Mzee Januari Mwakaja alimtazama kwa muda mrefu akiwa kimya. Hatimaye alimuuliza swali ambalo siku zote limekuwa likimsumbua kichwani mwake.
“Ni kweli uliua mtu huku ulipotoka?”
Ni swali ambalo Jaka hakulitegemea kabisa. Alipiga kimya kwa muda, akilini akitafakari iwapo lile swali halikuwa mtego.
“Unajua...kuna jaji mmoja huko Marekani aliwahi kusema kwamba, sisi sote tuko chini ya sheria, lakini sheria ni kile ambacho Jaji amesema kiwe...sasa kwa mtazamo huo mzee, iwapo bwana hakimu alisema kuwa mimi nastahili kifungo hiki kutokana na kuhusishwa na kifo cha mtu, kuna haja gani tena kutaka kujua iwapo ni kweli au si kweli niliua?” Hatimaye Jaka alimjibu kwa hisia kali.
Mzee Mwakaja alibaki akimtazama tu kwa muda.
“Oh! I see... Hivi ulifanya nini kule wewe...? Au uliona nini kule mpaka uwe mtu wa kufuatiliwa hivi?” Hatimaye alimuuliza kwa sauti yenye kukwaruza. Jaka aliachia tabasamu dogo la huzuni huku akiguna. Uso wake ulimbadilika na kuwa kama anayevuta kumbukumbu iliyomgusa sana, na ingawa alionekana kumuangalia yule mzee, hakika alikuwa hamuoni na badala yake alikuwa akiona mambo mbali mbali aliyokumbana nayo kabla ya kuletwa kwake pale Dodoma yakipita kwa kasi mno kichwani mwake.
“Ni mengi yametokea mzee...na mengi nimeyaona...tatizo ni kwamba waliotakiwa kuyasikia hawakutakana kufanya hivyo...”
Januari Mwakaja alizidi kumtazama. Tangu akutane na yule kijana, amekuwa akipata hisia kwamba kuna kitu hakikuwa sawa katika kuletwa kwake pale Dodoma. Aliwahi kuhisi kuwa pale alikuwa ameletwa ili apatwe na maafa ya kumtoa duniani, kwani kama ni kweli angekuwa amefanya kosa alilosemekana kuwa amelifanya, ile haikuwa hukumu sahihi.
“Unaweza kunieleza baadhi ya hayo uliyokutana nayo huko?”
Jaka alitikisa kichwa kwa masikitiko.
“Hapana mzee... ni hakika nimeona mengi sana, ila siwezi kukuelezea kwa sasa. Ni machungu sana...”
Mzee Mwakaja alimtazama kwa muda.
“Okay. Ila nina hakika kuwa katika hayo mengi uliyoona, kuna moja au mawili ambayo hukutakiwa kuyaona...” Hatimaye alihitimisha yule mzee.
Kimya kilipita kidogo, kisha Jaka akamuuliza yule mzee swali lililokuwa likimnanga kichwani mwake.
“Sasa baada ya kukuelezea mkasa ulionikuta jana usiku kutoka kwa huyu mtu mwenye koti refu na kofia pana...unaweza kunihakikishia vipi usalama wangu hapa mjini kwako?”
“Hilo swala niachie nilifanyie kazi kwanza kijana. Ninasikitika sana na yaliyokukuta hapa dodoma mpaka sasa ila elewa kuwa usalama wa raia wote wa hapa mjini uko chini yangu, hivyo na wewe pia uko katika himaya yangu. Nitalifanyia kazi kwa karibu sana hilo. Ila nawe saa upunguze kutembea tembea usiku na ujitahidi kuwa kwenye maeneo yenye majumuiko ya watu zaidi kuliko kuwa meneo pweke na peke yako...sawa?” Alimjibu.
Jaka aliafikiana naye kwa shingo upande, kisha akaaga na kuondoka.
Nyuma yake Mzee Januari Mwakaja aliinua mkono wa simu iliyokuwa pale mezani kwake na kumpigia mkuu wa polisi wa kanda maalum ya Dar es Salaam. Kuna mambo kadhaa ambayo alihitaji kufahamishwa.
Wakati ile simu ikiendelea kuita, Osman Mgunya aliingia mle ofisini nayeakairudisha ile simu mahala pake na kumtazama kwa macho ya kuuliza.
“Ulikuwa unahitaji kuniona afande ?” Osman aliuliza.
“Hapana...nikikuhitaji si nitakuita Osman?” Mwakaja alimjibu kwa mshangao.
“Ndio...nilikuwa nimetoka kidogo ofisini, na nilipokuwa narudi nikamuona Jaka akitoka ofisini kwako na simu ya ofisini kwangu ikawa inaita, lakini ilikatika kabla sijawahi kuipokea...hivyo nikadhani ni wewe ndiye uliyekuwa ukinipigia...” Mgunya amlijibu kwa kubabaika kidogo.
“Hapana, endelea na kazi zako.”
“Ndiyo Afande!” Osman alisaluti na kutoka.
Januari Mwakaja alikunja uso kwa mawazo huku akiendelea kukodolea macho pale mlangoni alipotokea Osman Mgunya sekunde kadhaa zilizopita.
Ni kweli alikuja kuulizia alichokuja kukiulizia pale ofisini, au alikuja kuhakikisha kitu...? Kwa nini ameamua kuja pale ofisini baada ya kumuona Jaka akitokea ofisini kwake?
Alikumbuka siku ile alipomkuta akimpiga Jaka kule ofisini kwake na akazidi kukunja uso kwa tafakuri. Alishusha pumzi taratibu, akainua tena mkono wa simu na kuanza kupiga namba za mkuu wa polisi wa kanda maalumu ya Dar es Salaam.

__________________

Dakika arobaini baadaye, Mzee Mwakaja alibaki akiwa ameduwaa na simu yake sikioni hata baada ya mtu aliyekuwa akiongea naye kule Dar kukata simu yake. Akiwa bado ameduwa na simu yake sikioni, aliweza kusikia mtu wa upande wa pili wa simu ile akiweka simu yake chini. Alikuwa anataka kuirudisha simu yake chini aliposikia tena mlio wa simu nyingine ikiwekwa chini. Alikunja uso na kuitoa haraka simu ile sikioni mwake na kuitazama, kisha akaiweka tena sikioni.
Kimya.
Aliurudusha mkono wa simu ile mahala pake huku sura yake ikisajili mikunjo mingi kwa mawazo. Alikuwa na hakika kabisa kuwa alisikia simu ya pili ikiwekwa chini baada ya simu ya RPC wa Dar kuwekwa chini...
Januari Mwakaja alikuwa mzoefu sana katika kazi kipelelezi, na ingawa alijua kuwa muda wake wa kustaafu ulikuwa unakaribia, bado alikuwa na imani kubwa sana katika uwezo wake wa kazi.
Kwa hali hiyo, mara moja alijua kuwa kuna mtu mwingine, mtu wa tatu, aliyekuwa akisikiliza mazungumzo kati yake na Kamanda wa Polisi wa kanda maalumu ya Dar es Salaam.
Kitu kingine alichojua ni kwamba ile simu ya tatu iliyotumika kusikiliza mazungumzo yale ilikuwa katika jengo lile lile ambamo ofisi yake ilikuwepo. Hiyo inamaanisha mtu aliyekuwa akisikiliza mazungumzo yale alikuwa ndani ya jengo lile lile alilokuwamo.
Ni nani?
Na kwa nini afanye vile?
Aliweza kujijibu swali la “nani” mara moja, au alidhani aliweza. Lakini swali la “kwa nini” bado lilihitaji uchunguzi wa kina.
Mawazo yake yalirudi kwenye maongezi yake na kamanda wa polisi wa kanda maalumu ya Dar es Salaam, ambapo alitaka ajulishwe mambo fulani kuhusiana na swala zima la mhalifu Jaka Brown Madega...
Tangu awali kesi ya huyu mtu aitwaye Jaka imekuwa ikimuachia maswali mengi kichwani, na alishindwa kuielewa. Cha ajabu ni kwamba baada ya kuongea kwa zaidi ya dakika arobaini na yule mwenzake wa Dar es Salaam, amejikuta ndio ameongezewa maswali zaidi kuliko majibu kuhusiana na kesi ya Jaka na hivyo kuzidi kutoielewa.
Samson Ramadhani, kamanda wa polisi wa kanda maalumu ya Dar es Salaam alimpa jibu ambalo hakulitegemea pale alipomuomba amtumie faili la kesi nambari 08/12582/94/800 inayomhusu mtu aitwaye Jaka Brown Madega.
“Faili hilo limetoweka katika mazingira ya kutatanisha kiasi cha miezi miwili iliyopita...”
Ndilo jibu lililomfanya abaki ameduwaa na simu sikioni...

_________________

Sehemu nyingine ya jengo lile lile, Osman Mgunya alirudisha taratibu mkono wa simu mahala pake baada ya kujihakikishia kuwa January Mwakaja na Kamanda wa kanda maalumu ya polisi ya mkoa wa Dar es Salaam, ambao yeye alikuwa akifuatilia mazungumzo yao ya simu bila ya wao kujua, walikuwa wameshaweka chini simu zao. Alibaki kimya kwa muda huku uso wake mbaya ukiwa umekunjamana kwa tafakuri.

ITAENDELEA KESHO MUDA ULE ULE, BILA KUPUNGUA HATA SEKUNDE MOJA.
 
SEHEMU YA KUMI NA TANO

Tangu awali kesi ya huyu mtu aitwaye Jaka imekuwa ikimuachia maswali mengi kichwani, na alishindwa kuielewa. Cha ajabu ni kwamba baada ya kuongea kwa zaidi ya dakika arobaini na yule mwenzake wa Dar es Salaam, amejikuta ndio ameongezewa maswali zaidi kuliko majibu kuhusiana na kesi ya Jaka na hivyo kuzidi kutoielewa.
Samson Ramadhani, kamanda wa polisi wa kanda maalumu ya Dar es Salaam alimpa jibu ambalo hakulitegemea pale alipomuomba amtumie faili la kesi nambari 08/12582/94/800 inayomhusu mtu aitwaye Jaka Brown Madega.
“Faili hilo limetoweka katika mazingira ya kutatanisha kiasi cha miezi miwili iliyopita...”
Ndilo jibu lililomfanya abaki ameduwaa na simu sikioni...

_________________

Sehemu nyingine ya jengo lile lile, Osman Mgunya alirudisha taratibu mkono wa simu mahala pake baada ya kujihakikishia kuwa January Mwakaja na Kamanda wa kanda maalumu ya polisi ya mkoa wa Dar es Salaam, ambao yeye alikuwa akifuatilia mazungumzo yao ya simu bila ya wao kujua, walikuwa wameshaweka chini simu zao. Alibaki kimya kwa muda huku uso wake mbaya ukiwa umekunjamana kwa tafakuri.
Aliyasikia yote yaliyoongewa baina ya January Mwakaja na yule mwenzake wa Dar es Salaam, na aliyoyasikia hayakumpa amani hata kidogo. Lakini kilichomnyima amani zaidi ni kukosa kujua kilichoongelewa baina ya Jaka na yule mkuu wake wa kazi wa pale Dodoma kule ofisini kwake asubuhi ile. Osman hakuwa mjinga. Aliweza kuunga moja na moja na akapata jibu sahihi kuwa ni mbili. Ilifunukia wazi kuwa ni kile kilichoongewa baina ya wawili wale mpe ofisini kwa Mzee Mwakaja ndicho kilimchochea yule mkuu wake wa kazi wa muda apige ile simu kule Dar.
Baada ya kusikia jinsi RPC January Mwakaja alivyokuwa akimhoji yule mwenzake wa Dar juu ya mazingira ya kupelekwa pale Dodoma kwa mtuhumiwa Jaka, na hususan alivyojaribu kuomba apelekewe faili zima la kesi iliyomhusisha yule kijana, alijua kuwa lolote aliloambiwa na Jaka kuhusu mazingira ya kupelekwa kwake pale Dodoma alikuwa ameliamini.
Alianza kumung’unya midomo kwa wasiwasi.
Ni nini Jaka amemwambia huyu mzee kilichomfanya apige ile simu na kuongea yale aliyomsikia akiongea na kamanada wa kanda maalumu ya Dar?

Hakupata jibu zuri. Na kwa kuwa hakupata jibu zuri alijua kuwa wakati wa kuomba msaada wa haraka kutoka kwa watu aliokuwa akishirikiana nao kule Dar ulikuwa umefika, vinginevyo angeweza kushindwa kumtia Jaka hatiani kwa kosa jingine pale Dodoma kama alivyokuwa ameagizwa. Yule mkuu wa polisi wa mkoa ule alionekana kumuamini sana yule kijana. Na hilo lingeifanya kazi iliyompeleka pale Dodoma kuwa ngumu sana.
Akiachana na ile simu ya mezani, alitoa simu yake ya kiganjani na kuanza kubofya tarakimu za namba ya simu ya mtu ambaye alijua kuwa muda ule alikuwa jijini Dar es Salaam...

___________________

Jioni ya siku ile aliyokwenda kumshitakia Mzee January Mwakaja kuhusu tukiio la kushambuliwa na yule jamaa aliyempachika jina la John Doe, Jaka alikuwa amekaa sebuleni akiwa amezongwa na mawazo juu ya yale mambo yaliyokuwa yakimuandama. Alikuwa akifanya hivyo huku akiichezea chezea ile kofia ya yule mtu aliyoiokota kule uwanja wa sabasaba usiku uliopita baada ya kuambulia ile ngumi nzito sana ya chembe.
Clara alikuwa amezama kwenye kutazama tamthiliya aipendayo kwenye runinga, akijitahidi kutombughudhi kwani alijua kuwa Jaka alikuwa kwenye mawazo mazito na alihitaji kuachwa peke yake kwa muda.
Jaka alikuwa akiigeuzageuza ile kofia huku akiwa amezama kwenye lindi la mawazo, hususan namna atakavyoweza kumnusuru Clara na zahma ile ambayo sasa alikuwa ameshamtumbukiza rasmi.
Clara hakutakiwa kabisa aingizwe kwenye matatizo haya!
Alijiwazia huku akiigeuza ile kofia na kutazama ndani yake. Akamakinika. Kitu ndani ya kofia ile kilimvutia jicho lake, naye akamakinika maradufu huku akiisogeza ile kofia karibu zaidi na uso wake.
Mawazo yakatoka kwenye madhila yake na Clara na kuhamia ndani ya ile kofia.
Ukingo wa ndani wa kofia ile ulikuwa umeshonewa ufito wa kitambaa kwa ajili ya kumkinga mvaaji na jasho au mikwaruzo kutoka kwenye ngozi ya kofia ile. Kutoka kwenye ukingo wa ule ufito wa ndani ya ile kofia aliona kipande cha karatasi kikiwa kimechomoza kidogo. Alikichomoa kile kikaratasi na kukikunjua.
Kwa hati nzuri ya kiume aliona jina lake likiwa limeandikwa kwenye kile kipande cha karatasi, likifuatiwa na namba ambazo hakuzielewa, kisha maneno “Uhindini, DOM” yakafuatia. Chini ya maneno yote hayo kulikuwa kuna maneno yaliyopitisha ubaridi mwilini mwake.
MURDERER…OR FG…???
“Heh!” Alimaka kwa sauti huku akiinuka kutoka kwenye kochi akiwa amekishikilia kile kipande cha karatasi, ile kofia ikianguka kutoka mikononi mwake.
“Ni nini Jaka?” Clara alimuuliza huku akimgeukia.
“Mnh! Hata sielewi Clara!” Alimjibu huku akimpa kile kikaratasi. Clara alisoma yale maandishi na kumuinulia uso uliotatizika.
“Imetoka wapi hii karatasi Jaka?”
“Ilikuwa imechomekwa ndani ya kofia ya yule jamaa…John Doe!”
“Seriously?”
“Seriously…na zaidi ya hilo jina langu hapo, na hilo neno “murderer” linalomaanisha kuwa mimi ni muuaji, sielewi maana ya kitu kingine chochote kilichoandikwa hapo, mpenzi!” Jaka alilalama huku akiwa amejishika kiuno.
Clara alikunja uso.
“Subiri…hizi namba kando ya jina lako…ni namba za hii nyumba yetu tuliyomo hapa…” Alisema kwa hamasa.
“Ama?”
“Ndiyo! Ambayo iko hapa Uhindini, mjini Dodoma!” Clara alizidi kutanabahisha.
“Ah! Ndio maana ya hilo neno “Uhindini, DOM”, siyo?” Jaka naye alithibitisha uelewa wake juu ya ile hoja ya Clara.
“Ndiyo!”
Kimya kilipita kidogo.
“Kwa hiyo hii inathibitisha kabisa kuwa John Doe si mkaazi wa hapa Dodoma, ndio maana ameandika au ameandikiwa hiyo anuani ya mahala nyumba ninayoishi ilipo!” Jaka alisema huku akijiegemeza kwenye mgongo wa moja ya makochi ya pale sebuleni.
“Yah, inaonesha hivyo aisee!”
“Na amekuja hapa Dodoma kwa makusudi mazima ya kunifuatilia mimi!”
“Hilo tulishalijua Jaka…kilichobaki kuwa kitendawili ni haya maandishi ya mwisho hapa kwenye hii karatasi, mpenzi…” Clara alisema, na hapo Jaka akadakia.
“Yeah…murderer or FG…”
“Haswa! Muuaji, au FG…sasa hii FG ni nini?” Clara alithibitisha na kuanika hewani swali ambalo pia lilikuwa kichwani kwa Jaka wakati ule.
Kimya kilipita. Hakukuwa na jibu la aina yoyote juu ya swali lile.
“Nadhani hilo litajibiwa na John Doe pindi nitakapokutana naye tena. Hii sasa ni vita ya wazi kati yangu na yeye…!” Jaka alisema kwa sauti ya chini lakini yenye azma thabiti.
“No Jaka. Vita na yule jamaa huiwezi. Inabidi tutafute msaada katika hili!” Clara alimwambia kwa mashaka makubwa.
“Hakuna msaada kwangu katika hili Clara…naona lile jinamizi nililoliacha kule Dar limeamua kunifuata huku Dodoma. Sina jinsi wala namna sasa…ni kukabiliana nalo tu!”
“Kuna Polisi Jaka. Mzee Mwakaja anaonekana kuwa ni mwenye nia ya kukusaidia…mtake tena msaada!”
Jaka alimtupia jicho la pembeni, lakini hakusema kitu. Alijua kuwa asemayo kuhusu Mzee January Mwakaja ni kweli kabisa, lakini pia kuna mengi zaidi ambayo yeye alikuwa anayajua na Clara alikuwa hayajui. Na hayo ndiyo yaliyomfanya asiamini sana kuwa atapata msaada kutoka kwa jeshi la polisi, pamoja na uwepo wa Mzee Mwakaja.
“Nadhani nahitaji kwenda kulala sasa…” Alisema kwa upole huku akilelekea chumbani, akimuacha Clara akiwa amepigwa butwaa pale sebuleni ilhali bado amekishikilia kile kikaratasi.
Siku zilizofuata Jaka alijitahidi kuwa makini sana kila alipokwenda, na alimsisitizia Clara kufanya hivyo hivyo. Alijikuta akijaribu kumtafuta John Doe kila kona, akitaraji kuonana naye tena.
Lakini John Doe hakuonekana tena.
Alijaribu kuwauliza walinzi mbali mbali wa pale ofisini kwao iwapo kuna mtu yeyote aliyekuwa akimuulizia pale getini au ofisini.
Hakukuwa na mtu yeyote aliyekenda kumuulizia pale ofisini.
Hakumuona tena, lakini hakuweza kumtoa akilini mwake. Kitu kimoja alichokuwa na uhakika nacho ni kwamba John Doe hakuwa ametumwa na polisi wa mkoa ule wala wa Dar es Salaam. Hilo alilijua kutokana na maongezi yake na mzee Januari Mwakaja ambaye alishakutana naye mara mbili zaidi kuongelea juu ya jambo hilo. Sasa ilikuwa inakaribia wiki ya pili tangu vurumai ile ya uwanja wa sabasaba imtokee, na ingawa mwanzo RPC Januari Mwakaja alionesha dalili za kumshuku Osman Mgunya kuhusiana na tukio lile, baada ya muda huo kupita alianza kulipuuzia tukio lile na kuamini kuwa yule mtu alikuwa ni mwizi wa kawaida tu.
Wazo ambalo lilipingwa vikali na Jaka. Haikumuingia akilini kwa nini mwizi wa kawaida aanze kumuulizia habari zake ofisini kwanza kabla hajaamua kwenda kumwibia au kumvamia. Zaidi ya hapo, haikuwa rahisi kwake kulipuuzia tu swala lile. Kama John Doe alikuwa ni mwizi, basi kwa hakika hakuwa "mwizi wa kawaida tu".

___________________

Suzuki Vitara ya bluu ilikata kushoto na kuingia Mtaa wa Kuu(Kuu Street) ikitokea Uhindini. Moja kwa moja mwisho wa mtaa ule, jengo la ofisi za makao makuu ya Chama Cha Mapinduzi mkoa wa Dodoma lilionekana likiwa upande wa pili wa barabara ile. Ile Vitara ilipaki kiasi cha hatua kumi hivi za miguu nje ya wigo wa eneo maarufu na Nyerere Square pale Dodoma ambalo lilikuwa linatazama na jengo la Benki ya Taifa ya Biashara (NBC) ng'ambo ya pili ya barabara Kuu, upande ule ule ambao ofisi za CCM zilikuwapo. Eneo lile la Nyerere Square lilikuwa maarufu kwa migahawa mingi iliyoandaa maakuli mbali mbali kwa wakaaji wa pale mjini. Na pia kilikuwa ni kituo muhimu cha makutano kwa watu kutoka sehemu mbalimbali za mji wa Dodoma.
Jaka na Clara waliteremka kutoka kwenye gari lile na kuingia ndani ya eneo lile. Ikiwa ni asubuhi ya siku ya jumapili, eneo lile lilikuwa limefurika watu, wengi wao wakiwa ni waumini waliotoka kwenye nyumba za ibada na kuamua kwenda kujipatia staftahi au kujiburudisha kwa vinywaji mbali mbali ndani ya eneo lile. Wengine walienda eneo lile kwa lengo la kukutana tu na marafiki ambao hawakuweza kuonana nao kwa wiki nzima. Ilikuwa ni mazoea ya Jaka na Clara kwenda kupata kiamsha kinywa sehemu ile siku za jumapili badala ya kujipikia chai wenyewe nyumbani.
Pamoja na umakini aliojiwekea tangu siku ya mkabala wake wa mwisho na John Doe, Jaka hakumuona mtu mmoja aliyekuwa ameinama kwa msafisha viatu aliyekuwa pembeni ya mlango wa kuingilia ndani ya eneo lile. Yule mtu aliwaona wakipita mita chache tu kutoka pale alipokuwa amekaa akisafishiwa viatu vyake. Alikuwa amevaa koti refu jeusi lililoishia chini ya magoti yake. Suruali ya kahawia ilitokeza chini ya koti lile na kofia yake ya pama ya rangi ya kahawia alikuwa ameipakata mapajani mwake akiwa amekaa kwenye benchi la yule msafisha viatu...
Ambalo pia Jaka hakuliona ni kwamba dakika chache tu baada ya ile Vitara yao kuegeshwa pale nje ya eneo lile, gari jingine dogo aina ya Toyota Raum lenye rangi nyeupe lilifika na kuegeshwa nyuma ya gari la tatu kutoka pale ilipoegeshwa ile Vitara yao. Watu wawili waliokuwa ndani ya ile Raum hawakuteremka mara moja.Walitulia ndani ya lile gari wakiwaangalia akina Jaka wakiteremka na kuingia ndani ya lile eneo la Nyerere Square.
Kama Jaka na Clara wangekuwa makini zaidi, wangegundua kuwa ile Raum ilikuwa nyuma yao tangu walipotoka nyumbani kwao pale Uhindini kwenye kona ya Mbeya Avenue. Lakini umakini waliodhamiria kuwa nao ulikuwa umeshawatoka.
Yule bwana mwenye koti refu aliinuka kutoka kwenye benchi la mng'arisha viatu na kuondoka taratibu kuelekea kule lilipoegeshwa gari la akina Jaka. Alipofika usawa wa ile Vitara, alianza kuvuka barabara kuenda upande wa pili wa ile barabara ya Kuu, lakini ile Raum nyeupe nayo ikaanza kutoka na kuingia barabarani, hivyo alisimama ili ipite huku akiwa ameipa mgongo ile Vitara.
Ile Raum ilikuwa inakuja taratibu mno na yule mtu mrefu aliona kuwa mtu aliyekuwa kando ya dereva alikuwa akiiangalia sana ile Vitara. Jamaa alikuwa amevaa shati kubwa jeupe na tai pana yenye mchanganyiko wa madoa meusi na meupe. Usoni alikuwa amevaa miwani ya jua iliyoficha sehemu ya sura yake, na nywele zake zilikuwa zimekatwa na kuwa ndogo sana kiasi cha kukaribia kuwa upara. Hakuwa amepata kumuona kabla ya wakati ule yule jamaa. Raum ilipopita akavuka ile barabara na kwenda kusimama ng’ambo ya pili ya ile barabara, kando ya jengo la Benki, mahala ambapo kutokea pale aliweza kuona moja kwa moja kule ambapo ile Vitara ya akina Jaka ilikuwa imeegeshwa.
Dakika chache baadaye alimuona yule jamaa aliyekuwa kwenye ile Raum iliyompita muda mchache uliopita akirudi kwa miguu akiwa upande wa pili wa ile barabara, akielekea kule lilipokuwa gari la akina Jaka. Akamakinika naye huku akihisi msisimko ambao huwa unampata pale tu anapohisi hatari.
Alipofika usawa wa lile gari la Zaza Cargo Movers, yule jamaa aliinama kama anayefunga kamba za viatu zilizomfunguka ghafla. Alikuwa ameinama kando ya tairi la mbele la gari ile kwa upande wa barabarani. Hivyo hakuweza kuonekana na watu waliokuwa kule Nyerere Square. Mara ile yule mwenzake aliyekuwa akiendesha ile Raum nyeupe alipita na kuegesha lile gari upande ule ule aliokuwapo yule mtu mwenye koti refu, mita chache kutoka pale alipokuwa amesimama.
Mnh! Kuna mpango gani hapa?
Alimtazama kwa makini zaidi yule jamaa aliyechutama pale kando ya gari la akina Jaka.
Mbona kama anafunga kamba kwa mkono mmoja? Inawezekanaje?
Alimakinika zaidi na yule mtu, lakini gari lililopita pale barabarani lilimkinga kidogo. Akageuka na kumtazama yule dereva wa ile Raum, ambayo sasa ilikuwa upande ule aliokuwapo yeye. Huyu alikuwa kijana zaidi ya yule mwenzake na alikuwa amevaa kofia ya kepu, miwani myeusi na fulana nyeusi iliyoushika sana mwili wake mwembamba. Hakuwa na ndevu.
Alitupa tena macho upande wa pili wa ile barabara, na kuna gari jingine likawa linapita hivyo hakumuona yule jamaa mwenye tai mpaka lilipopita, ambapo alimuona yule jamaa akiinuka kutoka pale alipokuwa amechutama. Mara moja yule mtu mrefu mwenye koti refu aligundua kitu kisicho cha kawaida. Mkono wa kulia wa yule mtu mwenye tai ulikuwa unatokea nyuma ya bati linalofunika tairi la mbele la gari lile!
Ala!
Yule mtu mwenye tai alisimama kwa sekunde chache zaidi kama mtu anayetaka kuvuka barabara. Kisha taratibu alitumbukiza mikono yake kwenye mifuko ya suruali yake ya buluu, akageuka nyuma taratibu kuangalia upande ambao Jaka na Clara wangetokea, halafu aligeuka tena taratibu na kutazama kule ambapo ilipoegeshwa ile Raum nyeupe.

ITAENDELEA
 
Back
Top Bottom