Riwaya: Senyenge

Riwaya: Senyenge

SEHEMU YA TISA
Kwenye maktaba ya jiji kulikuwa na taarifa nzuri na mbaya. Kwenye kitabu cha namba za simu watu walioitwa Jacob walikuwa wengi. Wengine kutoka Manhattan, Bronx, Brooklyn, Queens na kila sehemu. Hiyo ilikuwa taarifa nzuri.

Taarifa mbaya ni kwamba hakukuwa na namba wala jina la mpelelezi wa kujitegemea anayeitwa Costello. Reacher aliguna, lakini hakushangaa. Ingeshangaza sana kama angekuta Costello Investigation: Tunashughulika na kutafuta watu waliopotea.

Namba nyingi za wapelelezi zilikuwa na majina yanayofanana huku wengi wao wakishindania herufi A ili wakae juu zaidi kwenye kitabu. Reacher alikivuta kitabu karibu na kuanza kunakili namba kumi na tano za askari wa idara ya polisi New York. Alikaa muda kidogo kutafakari kama ndiyo uamuzi sahihi. Aliporidhika alianza safari kutafuta sanduku la kupiga simu. Alitoa pesa na kidaftari kilichokuwa na namba na kuanza kupiga simu moja baada ya nyingine.

Bahati yake ilikuwa kwa mtu wa nne. Watu watatu wa mwanzo hawakuwa watu wake. Simu ya nne ilianza kama simu zingine zote. Mlio wa kuita halafu sauti za mtu kuishikashika na kupokelewa.

"Namtafuta mtu anaitwa Costello," Reacher alisema. "Amestaafu na sasa anafanya kazi ya upelelezi. Umri wake ni kati ya miaka 60."

"Sawa, Wewe ni nani?" Sauti ya upande wa pili ilihoji. Ilikuwa inafanana sana na sauti ya Costello. Reacher alihisi ni Costello mwenyewe.

"Naitwa Carter," Reacher alidanganya. "Kama jina la Rais tu."

"Unataka nini kwa Costello, bwana Carter.?"

"Nina kazi nataka tufanye, lakini nimetafuta namba yake bila mafanikio."

"Hiyo ni kwasababu namba zake hazipo kwenye hivyo vitabu."

"Kwahivyo unamfahamu?"

"Namfahamu? Mimi ninamjua."

"Ofisi yake ipo wapi kwani?"

"Ipo Greenwich avenue kama nakumbuka vizuri."

"Namba ya mtaa?"

"Sina."

"Namba ya simu?"

"Sina."

Reacher alishangaa kwanini watu wanasema wanawajua watu ilihali hawamjui. Lakini hakutia neno.

"Kuna mwanamke anaitwa Jacob, unamjua?"

"Hapana, sijawahi kusikia hilo jina."

"OK, Ahsante kwa msaada wako." Reacher alisema.

"Poa."

Reacher alikata simu na kurudi tena maktaba ambako alichukua kitabu kumtafuta mtu wa jina la Costello kwenye orodha ya namba za watu wa Greenwich Avenue. Hilo jina halikuwepo. Aliingia mtaani tena.

Greenwich Avenue ni mtaa mdogo uliopo kusini mashariki mwa Fourteenth street. Unazungukwa na ofisi ndogondogo nyingi. Reacher alifika barabara kuu na kuanzia ofisi za kaskazini. Hakupata kitu. Aliporudi majengo ya kusini aliona alichokuwa anakitafuta. Ulikuwa ni mlango wenye kibao kilichoandikwa Costello kwa juu. Mlango ulikuwa umepakwa rangi nyeusi na ulikuwa wazi.

Ndani kulikuwa na korido ndefu ambayo ukuta wake ulikuwa umeandikwa kila jina la ofisi na kazi yake. Reacher alisoma na chumba namba tano ndicho kilikuwa ofisi ya Costello.

Reacher alianza kupanda ngazi kuelekea kilipokuwa chumba. Mlango ulikuwa umepakwa rangi ya kung'aa na ulikuwa wazi. Haukuwa umefunguka sana, ila ulikuwa wazi. Reacher aliusukuma kwa mguu wake na wenyewe ukafunguka. Kilichokuwa mbele yake kilikuwa chumba cha mapokezi. Kilikuwa kimepakwa rangi ya kijivu mpauko. Meza ya katibu muhtasi ilikuwa hapo ikiwa na simu pamoja na kompyuta juu yake.

Chumba hiki hakikuwa na mtu. Lakini pia kilikuwa na ukimya usio wa kawaida. Reacher aliingia ndani na kuufunga mlango nyuma yake kwa kutumia mguu wake tena. Aliingia na kuufuata mlango wa kuingia ofisi ya ndani. Hapo akalivuta shati lake na kufunika kiganja cha mkono wake ndipo akashika kitasa kufungua. Kama askari watatafuta alama za vidole!

Kilikuwa chumba cha Costello. Hilo lilithibitishwa na picha zilizokuwa zimening'inizwa ukutani. Zilimuonesha Costello akiwa mwembamba alipokuwa mdogo na kadri alivyokuwa ndivyo alivyozidi kunenepa. Mpangilio wa zile picha ilikuwa kama tangazo la mtu aliyeenda Gym kupunguza mwili likiwa limegeuzwa - Kutoka wembamba kwenda unene.

Reacher alitoka nje kurudi chumba cha mapokezi. Kulikuwa na harufu ya utuli iliyoning'inia angani. Alienda hadi kwenye meza na kukuta mkoba ukiwa umefunguliwa zipu. Alichukua penseli yake na kupekenyua. Kulikuwa na mkusanyiko wa vitu ambavyo wanawake hubeba kwenye pochi zao.

Kioo cha kompyta kilikuwa kinawaka. Reacher alibonyeza kielekezi kwa penseli yake. Hapo kioo kikafunguka na kuonesha maneno yakiwa hayajamaliza kuandikwa - kama mtu alikuwa anaandika halafu akapata dharura akaachia njiani. Ghafla picha ya mwili wa Costello kule Key West ikamuijia Reacher kichwani, halafu mkoba wa mwanamke ukiwa wazi ilihali wanawake huwa hawaachi mikoba yao wazi, milango iliyokuwa wazi hapo ofisini na zaidi maneno ambayo hayakuwa yamemaliza kuandikwa. Mwili ukamtetemeka.

Aliitumia penseli yake kukata faili lililokuwa linaandikwa. Kompyuta ikamuuliza kama anataka kulihifadhi au la. Alibonyeza 'no'. Alifungua file manager kutafuta taarifa za malipo. Alijua Costello ni mtu makini aliyeendesha biashara kwa umakini hivyo lazima angekuwa na taarifa za malipo humu. Alianza kukadiria ingekuwa zimepita siku ngapi kabla ya Costello kujua yupo West Key. Jibu lilikuwa rahisi - Siku ya kwanza ya kupigiwa simu na kupewa maelekezo na kulipwa hela ya kuanzia. Siku ya pili kufikiria. Siku tatu baadae kutafuta taarifa. Taarifa za mwanajeshi mstaafu zingechukua muda hadi kupatikana na benki lazima zingemsubirisha Costello kwa siku kadhaa kabla ya kumpatia taarifa za mteja wao. Hivyo ingekuwa ni kati ya siku kumi zilizopita. Hivyo mtu wake alikuwa kwenye orodha ya watu wa siku kumi zilizopita, aliwaza.

Alifungua faili na kuanza kuanza kutafuta jina la Jacob kwanza. Halikuwepo. Majina mengi ya Costello yalikuwa yanaandikwa kwa ufupisho tu. Akaamua kuangalia tarehe. Aliona taarifa moja ya siku tisa zilizopita. Ilikuwa imeandikwa Sgr&t-09.

Hii ilimaanisha Costello alikuwa anafanya mambo kwa kasi kuliko Reacher alivyomchukulia au ni katibu muhtasi wake alikuwa mzembe. Aliibonyeza hiyo taarifa ya malipo likafunguka jedwali dogo linaloonesha dola elfu moja zimelipwa kwaajili ya kutafuta mtu anayeaminika amepotea. Anuani iliyotuma pesa ilikuwepo, lakini hakukuwa na namba za simu.

Reacher alilifunga hilo faili akafungua databezi. Akaandika Sgr&t halafu akabofya enter. Hapo likafunguka jedwali lingine. Hili lilionesha anuani ya mlipaji, namba za simu, faksi na barua pepe.

Alilizungusha tena shati lake kuziba viganja vyake na kunyanyua simu ya mezani iliyokuwepo hapo. Simu ilianza kuita halafu ikapokelewa.

"Spencer Gutman," Sauti ya upande wa pili wa simu ilisema. "Sijui nikusaidie nini?"

"Naomba kuongea na Mrs. Jacob tafadhali." Reacher alijibu.

"Nipe dakika moja," Yule mtu alijibu.

Ukaja mziki kwenye spika za simu halafu ghafla sauti ya yule mtu ikarudi tena.

"Mrs. Jacob, tafadhali." Reacher alisema.

"Ametoka kuelekea Garrison na sifahamu atarudi saa ngapi."

"Mwanamke inaonekana anatoka asubuhi sana nyumbani kwake, sio?"

"Mwanamke?" Yule mtu aliuliza na kuongeza, "Ni mwanaume sio mwanamke."

Reacher alitulia kidogo na ili asishtukiwe alikuwa hamjui Mrs. Jacob aliendelea kuongea, "Namaanisha huyo mwanaume. Nimechanganya tu kuo...."

"Usijali," Ile sauti ilisema. "Mimi ndiye nililichapa jina hivyo kwa maksudi."

Alipomaliza alimsomea anuani ya kumpata Mrs. Jacob huko Garrison.

"Ningekushauri uwahi," Yule mwanaume alisema.

"Sawa! Nitawahi." Reacher alijibu na kuishusha simu chini.

Alinyanyuka kutoka kwenye kiti na kufunga lile jedwali lililokuwa kwenye kioo cha kompyuta. Alitoka nje kuingia mtaani kumfuata Mrs. Jacob ambaye hakuwa mwanamke bali mwanaume!

SEHEMU YA KUMI
 
SEHEMU YA KUMI
Katibu muhtasi wa Costello alikufa dakika tano baadaye baada ya kusema utambulisho wa Mrs. Jacob. Hii ilikuwa ni baada ya Hobie kumshughulikia kwa chuma lake kwa dakika tano pia. Walikuwa kwenye bafu ya ndani ya ofisi ya Hobie ghorofa namba themanini na nane. Ilikuwa ni sehemu maalumu kwa kazi hiyo. Bafu yenyewe ilikuwa ni kubwa kuliko ilivyopaswa kuwa. Kulikuwa na bomba la kuogea na mapazia ya plastiki. Bomba lilikuwa ni muundo wa Italia. Hobie aligundua lilikuwa na uwezo wa kumning'iniza binadamu kwa kumfunga bila kuvunjika. Katika nyakati tofautitofauti watu wa uzito tofautitofauti walikuwa wamening'inizwa kwenye bomba hilohilo huku Hobie akiwahoji maswali ya hapa na pale.

Tatizo pekee lilikuwa ni mfumo wa kuzuia sauti. Hata hivyo Hobie aliamini hilo sio tatizo kubwa sana. TWC ni jengo kubwa lenye kuta nene. Na yeye hakuwa na majirani wa kumhoji chochote. Hivyo ilikuwa ni sawa tu, lakini Hobie alikuwa mtu makini ambaye kama ilimlazimu kufanya jambo flani kuepusha hatari basi alilifanya. Na ndiyo maana watu aliowaingiza kwenye bafu hilo aliwaziba midomo yao kwa gundi ya karatasi "cello tape". Angewasurubu huku akiangalia macho yao kwa umakini kuona kama yatasema wapo tayari kujibu maswali yake. Hapo angewafungulia waongee. Kama wangejifanya kupiga kelele, basi angeirudishia gundi na kuanza kuwasurubu kwa ukali kuliko mwanzo. Kwa kawaida majibu yake aliyapata mara tu alipowatolea gundi kwa mara ya pili.

Halafu sakafu ingehitaji kufanyiwa usafi kuondoa damu. Lingefunguliwa bomba kuruhusu maji yatoke huku fagio likitumika kuyasukuma. Hobie hakuwahi kufanya usafi - ilikuwa inahitaji mtu mwenye mikono miwili. Na hii ilimaanisha mwanaume mmoja kati ya wale walioenda Key West ndiye aliyefanya hiyo kazi. Na leo alikuwa amekunja suruali yake huku soksi na viatu akiwa kaviweka pembeni.

Hobie alikuwa kwenye meza yake akijadili na yule mwanaume wa pili.

"Nitakupatia anuani ya Mrs. Jacob. Hakikisha unamleta hadi kwangu, sawa?"

"Sawa." Yule mwanaume alijibu na kuongeza, "Na vipi kuhusu huu mwili?"

"Subirini mpaka usiku," Hobie alianza kueleza. "Utamvalisha nguo zake na kwenda kumtupa kwenye maji."

"Mwili wake unaweza kurudishwa nchi kavu siku sio nyingi, mkuu."

"Sijali," Hobie alisema. "Mpaka anapatikana atakuwa tayari kaharibika na hakuna polisi atapoteza muda kufuatilia. Sanasana watasema ni ajali ya kwenye maji."


Tabia ya Reacher kutotaka kujulikana ilikuwa na faida pamoja na changamoto. Njia ya haraka kufika Garrison ilikuwa ni kukodi gari. Lakini kwa mtu ambaye hana hata leseni kukodishwa gari isingewezekana. Kwahivyo Reacher alipanda Taxi kuelekea ilipokuwa stesheni ya treni. Aliposhuka alimlipa dereva na kuingia kwenye kundi kubwa la wasafiri wengine waliokuwepo stesheni hapo. Aliinua kichwa kuangalia ratiba ya treni zilizokuwa zinaingia na kuondoka kwenda Garrison. Alianzia juu mpaka chini. Chini mpaka juu. Treni iliyokuwa ya mapema ilikuwa inaondoka baada ya lisaa limoja na nusu.


Walifanya kama walivyokuwa wakifanya siku zingine. Mmoja wao alishuka hadi ghorofa ya mwisho chini na kuchukua boksi kubwa tu kwenye pipa la uchafu. Alitegemea kupata boksi la friji, lakini usipokuta unachotaka unatumia ulichokikuta. Aliliweka lile boksi kwenye toroli la kubebea mizigo na kwenda nalo hadi kwenye lifti. Huko alipandisha na mzigo wake hadi ghorofa ya themanini na nane.

Mwenzake alikuwa anafunga zipu ya mfuko alimoweka mwili wa katibu muhtasi wa Costello. Walipomaliza waliuingiza ule mwili kwenye boksi na kuzungushia gundi ya karatasi kwa usalama zaidi. Halafu wakashuka na lifti hadi kwenye maegesho ya magari ya ndani. Waliuweka mwili kwenye buti ya gari moja kubwa jeusi na kufunga kwa funguo. Walipomaliza wakatembea hatua kadhaa na kuangalia kulia na kushoto. Hakuna mtu aliyekuwa anatazama.

"Nina wazo," Yule mwanaume wa kwanza alisema. "Unaonaje tukianza kumfuta Mrs. Jacob ili tutakapokuja kwenda kumtupa huyu tukawatupe kwa pamoja. Hakuna kitu kinanikera kama kuingia kwenye maji kila siku."

"Poa," Mwanaume wa pili alijibu na kuongeza, "Boksi ziliisha kwani?"

"Hilo ndilo lilikuwa linafaa, lakini yaliyobaki yanaweza kufaa pia. Itategemeana kama Mrs. Jacob ana mwili mkubwa au mwili mdogo."

"Sema itategemeana kama tutamaliza habari yake leo."

"Unahisi atapona? Nadhani haujaona munkari alionao Hobie leo." Mwanaume wa kwanza alisema.

Walitembea na kuingia kwenye gari lingine lililokuwepo hapo. Lilikuwa jeusi pia. Muundo kama wa lile walimouweka mwili wa katibu muhtasi wa Costello, lakini dogo kwa umbo.

"Kwahivyo huyu mwanamke Mrs. Jacob yupo wapi?"

"Mtaa mmoja unaitwa Garrison," Yule mwanaume wa pili alijibu. "Umbali wa lisaa limoja na nusu kutoka hapa."

Halafu gari ikaanza kuteleza kuelekea nje kulikamata barabara. Safari ikaiva kuelekea kaskazini mwa New York.

SEHEMU YA KUMI NA MOJA
 
SEHEMU YA KUMI NA MOJA
West Street huwa inakuwa Eleventh avenue ambako kuna foleni kubwa ya magari. Ile gari aina ya Tahoe ya wale wanaume wawili ilijikuta imekwama katikati ya foleni hiyo kubwa. Waliamua kukata njia nyingine lakini jitihada zao hazikuzaa matunda. Walijikuta wamerudi kwenye foleni ileile hata walipofika Javits Convention Center iliyopo Twelfth Street. Hapo wangeingia barabara kuu ya Miller halafu wangetokea Hudson. Ambapo Hudson ilikuwa inaenda mpaka barabara namba 9A na ingewapeleka hadi Garrison. Lakini walikuwa bado wapo Manhattan wakiwa wamekwama kwenye foleni kwa zaidi ya lisaa limoja na nusu tangu watoke kwenye jengo la WTC.


Kilichomshangaza Reacher ilikuwa ni yale maneno yaliyokuwa yameandikwa kwenye kompyuta.

Mlango kuachwa wazi pamoja na mkoba viliongeza tu mashaka, lakini havikuwa na maana kubwa sana. Ni kweli wafanyakazi wengi wa maofisini huwa wanabeba vitu vyao na kufunga milango kila wanapotoka, lakini muda mwingine huwa hawafanyi hivyo. Pengine yule katibu muhtasi wa Costello alitoka nje kwenda kufuata kahawa au sharubati tu. Mtu akiwa anatoka ofisini kwake kwa dakika mbili anaweza akaacha mlango wazi na akaishia kujikuta ametoka kwa zaidi ya nusu saa. Lakini hakuna mtu huwa anatoka na kuacha kazi yake kwenye kompyuta bila kui-save. Hata kama ni kwa dakika moja tu. Lakini huyu katibu muhtasi hakuwa ame-save kazi yake. Reacher alilijua hilo kwa sababu kompyuta ilikuwa imemuuliza unataka kuhifadhi kazi yako? Ambayo ilimaanisha katibu muhtasi yule alikuwa amenyanyuka kutoka kwenye kiti bila kubonyeza kitufe cha ku-save ambayo ni sawa na abane pua ili asipumue kwa maksudi - Jambo ambalo lilimshtua Reacher.

Yeye mwenyewe alikuwa bado yupo stesheni ya treni akiwa anamalizia kikombe chake cha pili cha kahawa. Alikuwa amekwisha kata tiketi yake ya treni ambayo ndiyo ilikuwa imefika inapakia watu tayari kwa kuondoka. Treni aliyopanda Reacher ilikuwa ni ile ya kawaida tu. Kichwa chake alikuwa amekiegesha kwenye dirisha la sehemu aliyokuwa amekaa akiwaza ni nini kilichokuwa kinaendelea, na ni wapi alipokuwa anaenda na kama atafika huko atafanya nini? Na je atawahi au atawahiwa tena?


Barabara ya 9A ikawa ya 9. Walilichochea gari moto hadi wakajikuta Garrison na kuanza kutafuta anuani waliyokuwa wamepewa na Hobie. Haikuwa kazi rahisi. Nyumba zilikuwa zimeachanaachana. Mtu angeweza kuwa na Zipu namba ya Garrison lakini anaishi mtaa wa nyuma kabisa. Hilo lilikuwa wazi. Baada ya mwendo kidogo walilipata barabara sahihi na mtaa sahihi. Walipunguza mwendo wa gari na kuanza kuitafuta nyumba. Haikuwachukua muda wakawa wameiona mbele yao. Walipunguza mwendo na kuegesha gari.


Reacher alishuka kwenye treni alipofika Coton. Alikuwa ametumia dakika sabini na saba hadi kufika hapa. Alizipanda ngazi kuelekea yalipokuwa maegesho ya Taxi. Kulikuwa na madereva wanne - watatu wa kiume na mmoja mwanamke. Reacher alimchagua mwanamke.

"Unapafahamu Garrison," Reacher aliuliza.

"Garrison, ndiyo. Ni mbali sana kutokea hapa." Yule dereve alijibu.

"Nafahamu ni mbali." Reacher alisema.

"Utanipa senti 40."

"Nitakupa 50," Reacher alijibu na kuongeza, "Ninachotaka unifikishe ninapoenda."

Alipanda kwenye Taxi na kukaa kiti cha mbele upande wa abiria. Yule dereva alikanyaga mafuta na kuishika barabara namba 9A kuelekea kaskazini.

"Unayo anuani ya sehemu unakoenda?" Aliuliza.

Reacher aliisema anuani aliyopewa kwenye simu.

"Hiyo sehemu inatazamana na mto." Yule dereva alisema. Ilionekana, kwa mtazamo wa Reacher, huyu mwanamke alikuwa anaifahamu vizuri Garrison.

Walikanyaga mafuta na kuziacha nyumba nyingi nyuma. Na kadri walivyosonga mbele ndivyo barabara ilivyozidi kuwa nyembamba.

"Nadhani tumefika, ni kati ya hizi nyumba unazoziona mbele hapo. Hauwezi kupotea kwa namba hiyo ya nyumba." Yule dereva alisema baada ya kusimamisha gari kwa kuwa njia ilikuwa haipitiki. Kulikuwa na gari nyingi zilizokuwa zimeegeshwa barabarani na ndiyo zilizowakwamisha. Reacher alikadiria zilikuwa zinafika arobaini.

Reacher alizitazama kwa umakini zile gari. Nyingi zilikuwa na rangi nyeusi au bluu mpauko, lakini kuna mbili ambazo zilikuwa zimepakwa rangi ya jeshi la marekani.

"Kila kitu kipo sawa," Yule dereva aliuliza.

"Nadhani," Reacher alijibu huku akishuka. Alimkabidhi yule dereva senti zake hamsini.

Ile Taxi ilipoondoka, Reacher alianza kutembea kuitafuta nyumba huku akiangalia sanduku za kuwekea barua. Aliona sanduku moja lenye anuani aliyopewa. Lilikuwa limeandikwa Garber A. Lilikuwa ni jina analolifahamu kama alivyokuwa analifahamu jina lake mwenyewe.

Nyumba yenyewe ilikuwa imejengwa kwenye uwanja mkubwa ikiwa katikati ya nyumba ya kisasa na ya kizamani.

Alitembea kuelekea upande wa nyuma ya nyumba ambako alisikia maongezi ya chinichini. Alianza kuzifuata sauti zilipotokea. Kulikuwa na watu takribani mia moja wakiwa wamesimama kwenye bustani ya nyuma ya nyumba. Walikuwa wamevaa suti nyeusi - wanawake na wanaume. Wote suti nyeusi, tai nyeusi, soksi na viatu vyeusi isipokuwa kwa baadhi ambao walikuwa wamevaa nguo za jeshi. Wote walikuwa wanaongea kwa sauti za chini.

Msiba. Alikuwa anaingilia katikati ya msiba. Alibaki amesimama ameduwaa. Mahali alipokuwa na mavazi aliyovaa havikuwa vikiendana. Alikuwa amevaa shati la njano na suruali ya kijivu aina ya Chinos. Alibaki amesimama akiwatazama wale waombolezaji halafu na wao wakageuka kumtazama kwa pamoja. Ni kama alikuwa amewashtua kwa kupiga makofi wamtazame ana tangazo muhimu. Wote walikuwa wakimshangaa. Na yeye alikuwa akiwaangalia. Ukapita ukimya. Utulivu kwa sekunde kadhaa halafu mwanamke mmoja akatoka kwenye umati ule kuelekea alipokuwa amesimama Reacher.

Alikuwa mwanamke mdogo mwenye umri kati ya miaka thelathini akiwa amevaa kama watu wengine waliokuwepo pale. Alionekana ana uchovu lakini uzuri wake usoni haukupotea. Alikuwa mzuri haswaa. Mwembamba mwenye miguu mirefu, nywele nzuri na macho yake yenye rangi ya kipekee. Alitembea na kuelekea kwa Reacher kumpokea. Ni kama alikuwa akimtarajia afike ili amwambie jambo fulani.

SEHEMU YA KUMI NA MBILI
 
Back
Top Bottom