Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mbeya, Kamishina Msaidizi wa Polisi Benjamin Kuzaga ametoa elimu kwa Wanafunzi wa Darasa la Nne wa Shule ya Msingi Azimio iliyopo Jijini Mbeya ambao wapo katika maandalizi ya mwisho kuelekea mitihani ya upimaji ya Taifa inayotarajia kuanza kesho Oktoba 25, 2023 nchini.
Akizungumza na wanafunzi shuleni hapo, Kamanda Kuzaga amesisitiza na kuwataka wanafunzi kuzingatia yale yote wanayofundishwa pamoja na kutojihusisha na vitendo vya kihalifu ikiwemo wizi, ulawiti pamoja na vitendo vyote vinavyopelekea mmomonyoko wa maadili.
Aidha, Kamanda Kuzaga amewataka wanafunzi hao kutokaa kimya na kufumbia macho vitendo vya ukatili wa kijinsia dhidi yao na kuwataka kutoa taarifa mapema kwa walimu, wazazi na Jeshi la Polisi ili hatua stahiki ziweze kuchukuliwa dhidi ya watuhumiwa.
Sambamba na hilo, amewapongeza walimu kwa juhudi wanazoendelea kuzifanya kwa kuwafundisha wanafunzi hao licha ya kuwa walimu lakini pia wao ni wazazi hivyo wanatakiwa kuwa karibu na kuwasikiliza wanafunzi ili kubaini changamoto wanazopitia wakiwa shuleni.
Jeshi la Polisi Mkoa wa Mbeya linaendelea kutoa elimu mbalimbali kwa wanafunzi na Jamii kwa ujumla kupitia vituo vya redio, mashuleni pamoja na mikutano ya hadhara ili kuzuia matukio ya uhalifu ndani ya Jiji la Mbeya.