Sarah Baartman: Mwanamke mweusi kutoka Afrika Kusini aliyesafirishwa Ulaya kwa maonesho ya makalio makubwa

Sarah Baartman: Mwanamke mweusi kutoka Afrika Kusini aliyesafirishwa Ulaya kwa maonesho ya makalio makubwa

UBIDHAISHAJI MAUMBILE YA BINADAMU - KUTOKA SARAH BAARTMAN HADI AGNES 'MASOGANGE'

TUNAISHI katika zama mpya. Zama za ubepari uliochukua sura ya uliberali mamboleo. Ipo tofauti kati ya ubepari halisi na uliberali-mamboleo. Ubepari halisi ulijikita katika kuzalisha bidhaa viwandani. Uliberali mamboleo ni ubepari wa kikasino.

Ubepari wa kikasino ni ule wa kutengeneza pesa bila kujihusisha katika uzalishaji-mali. Uzalishaji-mali hufanyika mashambani na viwandani.

Katika ubepari wa kikasino na kiporaji, mtu hutengeneza pesa kwa biashara za udalali, ununuaji na uuzaji hisa, ukopeshaji, kamari au upaishaji wa bei za vitu.

Katika uliberali mamboleo, ambao ni awamu ya ubepari uliofilisika, kila kitu hugeuzwa bidhaa na kuuzwa au kununulika sokoni.

Huduma za jamii (afya, elimu) hugeuzwa bidhaa na kuuzwa sokoni kama inavyotokea kwa manukato, nguo au magari. Ubidhaishaji umevuka mipaka, kiasi kwamba hata viumbe vinabidhaishwa.

Katika makala haya nitazungumzia ubidhaifishaji wa muoneko wa viungo vya binadamu, hususun akinamama unaofanyika katika mfumo wa uliberali mamboleo.

AGNES MASOGANGE
Jina la Agnes Gerald “Masogange” sio geni katika masikio ya Watanzania. Ni mwanadada mrembo. Lakini warembo wapo wengi. Masogange ni maarufu. Akina dada warembo na maarufu wapo wengi pia. Lakini umaarufu wa Masogange ni tofauti.

Umaarufu wake umepatikana kutokana na anavyoonekana katika video za wanamuziki, na sehemu ya mwili wake inayompatia umaarufu ni makalio yake.
Mara kadhaa amekwishahojiwa naye akajisifia kuwa anajisikia raha kuwa na makalio makubwa: “Hakuna sehemu ninayoipenda kama makalio, yamekaa vizuri, nayapenda, najidai kupitia sehemu hiyo niliyojaaliwa na Mwenyezi Mungu,” alisema Agnes katika moja ya mahojiano yake yaliyochapishwa Machi 29, 2014 katika blogu ya Global Publishers.

Ukiingia katika mtandao utaona picha na video za Masogange. Nyingi ya hizo zinaonyesha “sehemu hiyo aliyojaaliwa na Mwenyezi Mungu”. Ameenda mbali hata kuweka picha na video zinazoonyesha utupu wake. Huko mtandaoni kuna wanaomlaani. Lakini hawa ni wachache. Wengi, hasa vijana, wanamsifia.

Lakini ole wako ewe msomaji mwema. Kama ulidhani kuwa makala haya yamelenga kumlaani ama kumsifia Masogange basi umekosea. Makala haya hayamzungumzii Masongange kama mtu bali yanazungumzia mfumo. Nitatumia pia mfano wa “Masogange wa Kenya” aitwaye Vera Sidika.

Afrika nzima kuna “akina Vera” wanaoibuka na kujizolea umaarufu na pesa. Huko Ulaya na Marekani ndio zaidi. Katika kona mbalimbali za dunia, wapo mabinti wanaotamani kuwa na umbile kama la Vera Sidika ili wawe maarufu na kujizolea pesa. Je, ni nini chanzo cha wimbi hili? Nani mwenye maslahi katika wimbi hili? Makala haya yamelenga kujibu maswali hayo.

SARAH BAARTMAN
Kwa kuanzia, ningependa kujadili kisa cha Sarah Baartman. Sarah alizaliwa nchini Afrika Kusini mwaka 1789. Alifariki mwaka 1815, jijini Paris, Ufaransa, akiwa na umri wa miaka 26. Je, alifikaje Paris?

Sarah alikuwa mtumwa huko Afrika Kusini. Mmiliki wake mwenye asili ya kikaburu aliamua kumuuza kwa daktari wa kiingereza aliyeitwa Alexander Dunlop.

Dunlop alikuwa ameona fursa katika umbile la Sarah, na hasa makalio yake makubwa. Hivyo akamshawishi mmiliki wa Sarah amuuzie “bidhaa” hiyo ili akaitumie kutengeneza pesa huko Ulaya.

Sarah alipelekwa katika nchi kadhaa za Ulaya, hasa Uingereza na Ufaransa. Huko alipelekwa katika kumbi za maonyesho akiwa utupu, na wazungu wakawa wanalipa viingilio kuja kushuhudia weusi wa ngozi yake na ukubwa wa makalio yake na sehemu zake za siri.

Ili kutengeneza pesa zaidi, mmiliki wa Sarah akawa akimuuza kwa wanaume wa kizungu waliotaka “kumvumbua” zaidi mwanadada huyo wa Kiafrika. Sarah akafariki kwa ugonjwa wa zinaa. Hata baada ya kufariki viungo vya mwili wake vilikatwa na kuwekwa katika makumbusho huko Paris ili wazungu wakajionee. Sarah aliendelea kuwa bidhaa na kivutio cha utalii hata baada ya kufa.

TOFAUTI YA SARAH NA “MA-MODO” WA SASA
Je, kuna tofauti kati ya Sarah na “mamodo” wa sasa? Sarah aliishi katika kipindi ambacho biashara ya utumwa ilikuwa imeshika hatamu.

Waafrika waligeuzwa bidhaa, wakauzwa na kununuliwa sokoni, kama vile mtu anunuavyo nyanya, nguo au kuku. Wakapelekwa huko Amerika kuzalisha mashambani na migodini.

Nguvu-jasho ya Waafrika hawa ndiyo iliyozijenga na kuzistawisha nchi za Ulaya na Marekani ambazo leo tunakwenda kuomba misaada ya hali na mali.

Kwa hiyo, kama ilivyokuwa kwa babu na bibi zetu wengine waliopelekwa utumwani, Sarah hakwenda Ulaya kwa hiari yake. Alilazimishwa. Alikuwa ni bidhaa.

Usipofanya uchambuzi wa kina, unaweza kusema kuwa “ma-modo” wetu wa leo wanaotumia maumbo yao kama vivutio hufanya hivyo kwa hiyari yao. Lakini ukweli ni kwamba kuna nguvu ya kimfumo inayowalazimisha kufanya hivyo wafanyavyo. Nitajadili.

Maumbile ya Sarah yalikuwa ni ya asili. Mwili wake ni ule aliojaaliwa na Muumba. Katika zama zetu, wapo ‘mamodo’ wenye maumbile ya asili. Lakini wapo wengi pia ambao wamelazimika kubadili maumbile yao.

Ukuzaji wa makalio na matiti, uchubuaji wa ngozi na hata ubadilishaji wa jinsia yamekuwa ni mambo ya kawaida.
KIINI MACHO NA NGUVU YA SOKO
Ukiingia mtandaoni, utakuta kampuni kadhaa zikitangaza bidhaa za kukuza makalio na matiti.

Kwa wanaume, zipo dawa za kunenepesha na kurefusha uume, kukuza misuli, n.k. Kampuni hizi za kibepari ndizo kiini hasa cha ubidhaishaji wa viungo vya binadamu, na hasa makalio na matiti. Ili bidhaa zao zikubalike, kampuni hizi sharti zitengeneze soko la bidhaa zao.

Soko lenyewe hutengenezwa kwa kubadili mtazamo na fikra za watu, na hasa vijana, juu ya dhana ya urembo, mapenzi na uhusiano wa kimwili. Kwa hiyo, kwa kushirikiana na kampuni za utengenezaji wa filamu za ngono, kampuni za kurekodi video za muziki, wamiliki wa vilabu na makasino, magazeti na televisheni za udaku, hospitali za binafsi za upasuaji wa plastiki, kampuni za uzalishaji wa dawa hizi zimewezesha kukubalika kwamba makalio na matiti makubwa ni urembo, lakini pia ni hazina.

Kwa hiyo, katika zama zetu hizi binti mrembo anasemekana kuwa ni yule aliye na makalio makubwa, matiti makubwa, na ngozi nyeupe. Ikitokea hukuzaliwa na vitu hivi basi usikonde: utavipata kwa kutumia dawa au kwa kufanyiwa upasuaji wa plastiki.

Binti mwenye sifa hizi anaaminishwa kuwa ana “rasilimali” ambayo anaweza kuitumia kutengeneza pesa iwe ni kwa kujiuza sokoni ama kwa kuwa na mpenzi mwenye pesa.

Hivyo basi, wapo wanenepeshao kuwaridhisha wapenzi wao. Wapo wafanyao hivyo ili “kwenda na wakati”. Lakini wengi pia hufanya hivyo ikiwa ni sehemu ya soko.

Soko lenyewe sio lazima liwe la kujiuza kimwili. Ni soko la kuuza “makalio”, watu wakayaona iwe ni katika klabu za usiku, magazeti ya udaku au video za muziki, na mwenye nayo akatengeneza pesa.

Februari 10 2011, gazeti la MailOnline la nchini Uingereza liliripoti kifo cha Claudia Aderotimi, mwanafunzi wa nchini Uingereza, aliyefariki huko Marekani akiwa ameenda kufanyiwa upasuaji wa kuongeza makalio. Claudia, ambaye alikuwa na ndoto ya kuwa mnenguaji katika video za wanamuziki wakubwa, aliwahi kukosa tenda kwa kutokuwa na makalio makubwa.

Aliambiwa kuwa ili afanikiwe ni lazima awe na makalio yaliyobinuka kama ya mwanamuziki Beyonce. Hivyo, mfumo tulio nao unawatengenezea mabinti kiini-macho (illusion) cha “kuwa na umbo kama la Beyonce ili ufanikiwe”.

VERA SIDIKA: “MWILI WANGU NI DILI”
Katika kipindi cha The Trend kirushwacho na kituo cha NTV nchini Kenya, Vera Sidika, ambaye amejizolea umaarufu nchini Kenya kutokana na umbile la makalio yake, alisema kuwa huenda kufanya “shopping” ya kati ya dola 10,000 hadi 50,000 (yaani kati ya shilingi milioni 16 hadi milioni 80).

Viatu alivyokuwa amevaa siku hiyo vinagharimu shilingi milioni tano na laki sita, na nywele zake za bandia ni shilingi milioni tatu na laki saba.

Ngozi ya Vera sio ya asili. Ilichubuliwa kitaalamu na akawa mweupe. Vera anajitapa kuwa ubadilishaji wa rangi ya ngozi yake ulitumia zaidi ya shilingi milioni 15 za Kenya (takribani shilingi milioni 300 za Tanzania).

Vera anasisitiza kuwa tangu apate ngozi nyeupe, kwake imekuwa “baraka”. Anatengeneza pesa zaidi, na anaalikwa nchi mbalimbali kwenda kusherehesha vilabu vya usiku (club hosting).

Vera anasema kwamba ukimwona klabu ujue amekwenda kutengeneza pesa. Hufanyaje hasa? “Huwa nasimama pale, na kutabasamu, na kupiga picha na mashabiki,” alifafanua. “Mwili wangu ni biashara yangu na ninautumia kutengeneza pesa,” Veera alijitapa.

Nyuma ya Vera, zipo kampuni za kurekodi video za muziki, wanamuziki, magazeti, redio, vituo vya televisheni, vilabu vya usiku, kampuni za kuzalisha kemikali za kubadili rangi ya ngozi, hospitali za binafsi zifanyazo uchubuaji wa ngozi, kampuni za vipodozi na mavazi ya kisasa bila kusahau hoteli za kifahari. Wote hawa humtumia Vera kutengeneza faida.

Lakini tusisahau watu wa msingi wamfanyao binti huyu ajivune: hawa ni wale anaowaita “my fans”, yaani mashabiki wake. Kila siku Vera huweka picha za nusu uchi, zionyeshazo makalio yake, katika mtandao ili kukonga nyoyo za mashabiki wake. Aendapo klabu hujiachia na kupiga nao picha za “ajabu” ili waendelee kumshabikia.

Mashabiki hawa pia tayari wamekwishatekwa na mfumo wa uliberali mamboleo, nao wakaamini juu ya urembo utokanao na umbo kama la Vera.
MTANDAO WA KIBIASHARA
Zipo nchi nyingi, mathalani Venezuela na Ufaransa, ambako ukuzaji-makalio na matiti vimetia fora kiasi cha wananchi kuzipigia serikali zao kelele ili zidhibiti vitendo hivyo.

Lakini hii ni kazi bure kama tusipoelewa kiini cha tatizo lenyewe.
Gazeti la mtandaoni liitwalo “The Revolution” linalomilikiwa na cha Chama cha Kikomunisti cha Marekani liliwahi kufanya uchambuzi wa biashara ya upachikaji wa matiti ya bandia kwa wanawake.

Nchini Uingereza pekee kati ya wanawake 20,000 hadi 30,000 hukuza matiti kwa njia hiyo kila mwaka, na biashara hiyo huingiza pato la zaidi ya dola milioni 150 (takribani shilingi bilioni 240 za Tanzania) kwa mwaka.

Kwa mujibu wa taarifa ya chama cha madaktari bingwa wa upasuaji wa plastiki nchini Marekani, idadi ya watu wanaojihusisha na upasuaji wa plastiki iwe ni katika kukuza au kupunguza makalio, matiti, nyusi, nywele, kubadili sura au ngozi, imeongezeka kutoka watu milioni 7.5 mwaka 2000 na kufikia watu milioni 14 mwaka 2011.

Jarida la “The Revolution” linaripoti kuwa kampuni za utengenezaji kemikali za ukuzaji matiti hutumia kemikali bandia ili kutengeneza faida zaidi. Moja ya kampuni hizo ni Poly Implant Prothese (PIP) ya nchini Ufaransa. Kutokana na madhara makubwa ya kiafya yasababishwayo na kemikali za PIP, baadhi ya nchi zimejaribu kuzipiga marufuku bidhaa za kampuni hizo bila mafanikio.

Maslahi ya kibiashara hayaishii katika kampuni tu. Ubidhaishaji wa huduma za afya umezifanya hospitali nyingi za binafsi zijiingize katika kazi ya upasuaji wa plastiki ili kukuza au kupunguza viungo vya mwili. Wateja waliopata madhara ya kiafya kutokana na kemikali za kukuza matiti na makalio wamekataliwa na hospitali zilizowapa huduma hizo.

Wamiliki wa hospitali hizo, kwa mujibu wa jarida la The Revolution, “wanadai kuwa hawapashwi kuwajibishwa kutokana na kununua bidhaa zilizokuwa sokoni.”

UBEPARI: KUTOKA UZALISHAJI HADI UBIDHAISHAJI
Pengine cha kufikirisha ni kauli ya Vera kuwa “mwili wangu ni biashara yangu na ninautumia kutengeneza pesa”. Suala la kujiuliza ni kuwa, je, tangu lini mwili wa binadamu uligeuka kuwa bidhaa, hata ukatumika kutengeneza pesa?

Katika kitabu chake cha Das Kapital (Capital au Mtaji) kilichochapishwa mwaka 1867, Karl Marx aliubainisha ubepari kama mfumo unaojitambulisha kupitia bidhaa. Lakini bidhaa hizo ni zile zinazozalishwa na nguvu ya binadamu na kupelekwa sokoni kwa ajili ya kuuzwa.

Cha kushangaza ni kuwa watu hushikwa na wazimu wa bidhaa, wakazipenda na kuzithamini, lakini wasione kiini ndani ya bidhaa hizo. Kiini hicho ni nguvu-kazi ya binadamu iliyotumika kuzitengeneza.

Marx alifariki mwaka 1883, yapata miongo saba baada ya Sarah kufariki. Kipindi alichoishi Marx kilikuwa ni kipindi cha ubepari wa uzalishaji bidhaa, viwandani na mashambani.

Takribani karne moja na nusu baada ya kuchapishwa kwa Das Kapital, Prof. Issa Shivji, mmoja wa wanazuoni wa Kimaksi, ameandika kuhusu ubepari wa karne ya 21, ambao umechukua sura ya uliberali mamboleo.

Mfumo huu hautegemei tena uzalishaji, bali ubidhaishaji wa kila kitu.
Vitu ambavyo kwa asili yake haviwezi kuuzwa, hugeuzwa bidhaa na kuuzwa sokoni. “Utengenezaji wa bidhaa-sesere na zisizo za asili hauna mipaka katika mfumo wa uliberali-mamboleo,” anaandika Shivji katika kitabu chake kiitwacho Accumulation in an African Periphery.

“Mazingira, ikolojia, na viumbe vingine wa asili (wanyama na mimea), viini vya kibaiolojia (ute wa mimea na viini-tete vya binadamu) hugeuzwa kuwa bidhaa, hali ambayo hutokea pia katika hisia na raha zihusishazo mahusiano ya kimwili. Juu ya vitu na mahusiano halisi hutengenezwa vitu-pepe na mahusiano-pepe, ambavyo pia hubidhaishwa.

Katika ulimwengu wa mahusiano utaona mambo kama mabinti wa mtandaoni, vyumba vya faragha, na ufanyaji-mapenzi katika mtandao” (tafsiri yangu).

Kwa hiyo, tujifunzacho hapa ni kuwa mtandao wa watumiao miili ya vijana, na hasa wa kike, kutengeneza pesa ni mpana: vituo vya televisheni huwaalika katika mahojiano na kueneza udaku juu yao na kwa kufanya hivyo hutengeneza pesa, magazeti ya udaku hutengeneza pesa kwa kuchapisha picha na stori za mabinti hao, kampuni za utengenezaji wa kemikali za ukuzaji makalio/matiti na uchubuaji ngozi nazo hutengeza pesa, hospitali zijihusishazo na uchubuaji ngozi na upasuaji wa ukuzaji makalio hutengeneza pesa, na vilabu vya usiku viwaalikao mabinti hao navyo hutengeneza pesa, n.k. Huu ni mtandao mkubwa wa kutengeneza pesa katika zama hizi za utumwa mamboleo.

Kiini cha mtandao huu ni mfumo wa uliberali mamboleo, ambao ni aina ya ubepari uliofilisika na uliochukua sura ya kikatili ya ubidhaishaji wa kila kitu, yakiwemo maumbile ya binadamu! Mfumo huu hauwezi kuwekewa viraka kwa kuhubiri juu ya maadili kwa vijana. Ni ama tuubomoe, au tuuache uendelee kutubomoa kwa kugeuza hata miili yetu kuwa bidhaa.

Kama wapigania uhuru wa bara la Afrika walipambana dhidi ya ukoloni, sisi wajukuu wao hatupashwi kusalimu amri. Hatuna chaguo mbadala, ni jukumu letu sote kupambana dhidi ya uliberalimamboleo

MUHIMU: Mwandishi wa Makala haya ni SABATHO NYAMSENDA, Mwanafunzi wa Shahada ya Uzamivu (PhD) ya Stadi za Jamii katika Chuo Kikuu cha Makerere, Uganda.

Sent using Jamii Forums mobile app
Vera sidika

queenveebosset-20190121-0001.jpeg
queenveebosset-20190121-0002.jpeg


Sent using Jamii Forums mobile app
 
Mimi sijui hiyo Phd ameipata mwaka gani, nachojua kwenye Makala zake alikuwa anaandika tu "Na Sabatho Nyamsenda" huko ndiko nilikomjulia mkuu.

Inawezekana, kuna vile unafanya PHD Makerere kama ilivyoandikwa hapo lakini ukiwa Dar.

Maana dogo kipindi hicho 2012 yote nilikuwa nakaa naye jirani akiwa either Assistant Lecturer/Tutorial, sikumbuki vizuri.
 
Hakika umenifundisha jinsi msomi anavyo paswa kuandika..

Heko kwa makala bora kabisa yenye mifano inayoendana na hadhara.
 
Yaani nimesoma kwa taabu sana mpaka nimefika mwisho ni kwa neema tu 😂
 
We jamaa ni kilaz.a ungejua madini yaliyotemwa humo usingeandika hiz pumba zako.Sio kila uzi lazima ucoment,kujua haya ni madini kiasi soma comment za watu waliosoma makala.next time chunga vidole vyako sio kila kitu utype tu na kujificha nyuma ya keyboard.

Sent using Jamii Forums mobile app
izo gazeti peleka Sani na Ijumaa uko
 
Sara Baartman alikuwa ni mwanamke mwenye makalio makubwa yalioshangaza ulimwengu kiasi cha kutumika kwenye maonyesho huko Ulaya. Pia mashavu ya uke(labia) wake yalikuwa marefu kwa kuwa ni tamaduni ya kabila lao, kitu ambacho siku hizi kinaonekana kama ni Female Genital Mutilation

Sara Baartman alizaliwa 1789 katika jamii ya kifugai ya Khoisan, alikulia kwenye mashamba ya kikoloni. Sara aliuzwa kwa kaburu piter willem ambaye alimpeka Cape town, na wakamuita Saartjie jina la kikaburu lenye maana sawa na Sara

Aliingia mkataba octoba 29, 1810 na dkt. William Dunlop, masharti ya kiwa kukubali kusafiri na dkt huyo kuwa mtumishi wake wa ndani na pia kutumika katika maonyesho na burudani. Ilikubaliwa kupata pesa kidogo katika maingizo ya fedha hizo ili arejee afrika kusini baada ya miaka mitano, swala la kusaini mkataba huo ni kizungumkuti kwa kuwa sara hakuwa anajua kusoma na kuandika.

Umbo la sara lililokuwa na makalio makubwa liliwashangaza wazungu ambao walikuwa wanajiona bora. Watu wakawa wanalipa kumuona sara akiwa uchi, kuyaangalia makalio yake na uke wake uliokuwa umerefushwa mashavu yake (Labia) kwa tamaduni za kabila lake

Stember 1814 awalienda ufaransa na akauzwa kwa mfanyabiashara Reaux, na akaendelea kutumika kwenye maonyesho huko Paris

March 1815 akachukuliwa kama kielelezo cha kisayansi, science specimen akitumika na wana anatomia, zoolojia, fiziolojia

Sara alikuwa akiwa na umri wa miaka 26, waliukata mwili wake na kuuweka katika makumbusho hadi mwa 1974, hadith ya sara ilifufuka mwaka 1981 Stephen Jay Gould alipoanza kuipinga sayansi ya kibaguzi.

Serikali ya Nelson mandela iliposhinda kupitia chama cha ANC ilianza mazungumzo na serikali ya ufaransa ili kuurudisha mabaki ya mwili wa Sara. Hatua hiyo ilichukua miaka nane, machi 6 2002, mwili wake ulirudishwa afrika kusini na akazikwa agosti 9, 2002.

1582094824840.png
1582094846626.png
 
images (39).jpeg
Katika miaka 1789-1815 palikuwepo na wanawake wawili wenye makalio makubwa, mmoja wapo aliitwa Sarah Baartman mwenye kutokea kabira la Khoi Khoi NCHINI Afrika Kusini. Wakoroni walivutiwa nae na kumchukua kwenye makumbusho NCHINI Ufaransa akitumika Kama kivutio. Kwa miaka hiyo biashara ya Human Zoo ilikuwa imetawala. Binadamu walikuwa wakiwekwa kwenye maonyesho Kama inavyofanyika kwa wanyama (animal zoo).

Sarah Baartman alifariki akiwa na miaka 29 mwaka 1815, hata alipofariki mwili wake uliwekwa makumbusho kwa malengo ya kisayanyasi atumike Kama specie sample ya kujifunzia. Hadi ilipofikia mwaka 1970 pale Muafrika Kusini aliyefahamika kwa jina Diana, aliandika shairi la kumhusu Sarah Baartman lenye tungo moja ikisisema "...nimekuja Kuirudisha nyumbani..." Utunzi wa shairi hili ukazua gumzo duniani na ukapata kasi zaidi mwaka 1980 lilipotungwa shairi lingine juu yake.

Mnamo 1994 baada Afrika Kusini kupata Uhuru wa kujitawala, Nelson Mandela aliomba kupitia serikali ya Ufaransa kuomba mabaki ya Sarah Baartman yarudi Afrika Kusini na yapate kuzikwa. Hadi mwaka 2002 masalia hayo yakarudi na kuzikwa na kufanyiwa sehemu ya maonyesho ya kihistoria.

images (40).jpeg

images (41).jpeg

images (42).jpeg
Mfahamu Pia Sarah Baartman aliweza kupewa majina mbali mbali Kama vile Venus n.k
 
unafahamu maana ya ya Female Genital Mutilation? I am not sure kama unafahamu.



Alitekwa miaka ya 1780 ivi huko South Africa akapelekwa ulaya kwenye madanguro, akafa, hakuzikwa ila alifanyiwa upasuaji wa ubongo, makalio yake makubwa na sehemu za siri zikawekwa maabara uko ufaransa na uingereza. Then Mandela alienda kurudisha mabaki ya mwili wake (chini ya mabishano makali sana bungeni uko ufaransa) baada ya kwisha kwa utawala dhalili wa rangi. akazikwa uko kwa madiba kwa heshima kubwa.



Sara Baartman alikuwa ni mwanamke mwenye makalio makubwa yalioshangaza ulimwengu kiasi cha kutumika kwenye maonyesho huko Ulaya. Pia mashavu ya uke(labia) wake yalikuwa marefu kwa kuwa ni tamaduni ya kabila lao, kitu ambacho siku hizi kinaonekana kama ni Female Genital Mutilation

Sara Baartman alizaliwa 1789 katika jamii ya kifugai ya Khoisan, alikulia kwenye mashamba ya kikoloni. Sara aliuzwa kwa kaburu piter willem ambaye alimpeka Cape town, na wakamuita Saartjie jina la kikaburu lenye maana sawa na Sara

Aliingia mkataba octoba 29, 1810 na dkt. William Dunlop, masharti ya kiwa kukubali kusafiri na dkt huyo kuwa mtumishi wake wa ndani na pia kutumika katika maonyesho na burudani. Ilikubaliwa kupata pesa kidogo katika maingizo ya fedha hizo ili arejee afrika kusini baada ya miaka mitano, swala la kusaini mkataba huo ni kizungumkuti kwa kuwa sara hakuwa anajua kusoma na kuandika.

Umbo la sara lililokuwa na makalio makubwa liliwashangaza wazungu ambao walikuwa wanajiona bora. Watu wakawa wanalipa kumuona sara akiwa uchi, kuyaangalia makalio yake na uke wake uliokuwa umerefushwa mashavu yake (Labia) kwa tamaduni za kabila lake

Stember 1814 awalienda ufaransa na akauzwa kwa mfanyabiashara Reaux, na akaendelea kutumika kwenye maonyesho huko Paris

March 1815 akachukuliwa kama kielelezo cha kisayansi, science specimen akitumika na wana anatomia, zoolojia, fiziolojia

Sara alikuwa akiwa na umri wa miaka 26, waliukata mwili wake na kuuweka katika makumbusho hadi mwa 1974, hadith ya sara ilifufuka mwaka 1981 Stephen Jay Gould alipoanza kuipinga sayansi ya kibaguzi.

Serikali ya Nelson mandela iliposhinda kupitia chama cha ANC ilianza mazungumzo na serikali ya ufaransa ili kuurudisha mabaki ya mwili wa Sara. Hatua hiyo ilichukua miaka nane, machi 6 2002, mwili wake ulirudishwa afrika kusini na akazikwa agosti 9, 2002


Source:

APA - Sarah Baartman, at rest at last - SouthAfrica.info
 
Alijulikana Kama Sarah Baartman

.
_119878863_bbbb83d1-c0bb-4ceb-8b82-a4a881498162.jpg


Inadhaniwa kuwa alizaliwa katika jimbo la Afrika Kusini la Eastern Cape mwaka 1789, mama yake alifariki dunia alipokuwa na umri wa miaka miwili na baba yake, mfugaji, alifariki alipokuwa katika umri wa kubalehe.

Aliingia katika utoaji wa huduma za nyumbani mjini Cape Town baada ya mkoloni Mholanzi kumuua mwenza wake, ambaye alikuwa tayari amezaa naye mtoto ambaye alikufa

Aliletwa Ulaya kwa njia za madai ya uongo na daktari Muingereza , akiitwa kwa jina la jukwani "Hottentot Venus", ambapo alioneshwa katika kumbi za "maonyesho ya vituko" mbali mbali katika miji ya London na Paris, huku umati wa watu ukialikwa kuyaangalia makalio yake makubwa.

Haya yalimfanya asababishe mvuto wakati alipokuwa akifanya onyesho katika eneo la Piccadilly Circus jijini London baada ya kuwasil

Jukwaani alivaa nguo ya kubana mwili wake ( skin-tight) yenye rangi, pamoja na shanga na manyoya na alikuwa akivuta tumbaku. Wateja matajiri walikuwa wanalipa pesa zao kwa ajili ya kuburudishwa kibinafsi majumbani mwao, huku wageni wakiruhusiwa kumgusa
 
Back
Top Bottom