WANAFUNZI WA TANZANIA KUJISALIMISHA UBALOZI WA UINGEREZA, UKRAINE
Balozi wa Uingereza nchini Ukraine, Bw. Tim Barrow
Wanafunzi wa kitanzania wapatao 29 waliotelekezwa na serikali ya Rais Jakaya Kikwete kwenye vyuo vya nchini Ukraine hatimaye wameamua kufanya kile walichotishia miezi michache iliyopita, nacho ni kujisalimisha na kuomba hifadhi kwenye Ubalozi wa Uingereza jijini Kiev, nchini Ukraine. Ubalozi huo tayari umeshakubali kuwapokea vijana hao mapema asubuhi. Uamuzi huo umefikiwa baada ya serikali ya Tanzania chini ya Wizara ya Sayansi na Elimu ya juu kuwakana wanafunzi hao na kutowatambua licha ya kuwaahidi mikopo ya masomo tangu mwezi wa tisa mwaka jana.
Kwa mujibu wa wanafunzi hao waliozungumza na KLH News ambao tayari wako njiani kuelekea Jijini Kiev kwa treni toka vyuo mbalimbali sababu kubwa ya uamuzi huo ni kuwa:
- a. Wanaishi katika maisha magumu ambayo yanatishia siyo tu usalama wao bali pia afya zao. Mara moja tayari wameshaitiwa vyombo vya usalama kuwachunguza.
- b. Vyuo vyao vikuu vimewapa tarehe 20 ya mwezi huu kama tarehe ya kufutwa chuoni na hapo kuwa wahalifu na kuweza kukamatwa na kufungwa
- c. Mmoja wa wanafunzi alishanganyikiwa kutokana na msukumo wa matatizo hadi kuitiwa madaktari wa magonjwa ya akili. Hali yake licha ya kutengemaa lakini bado yuko nusu nusu.
- d. Jitihada za wanafunzi hawa kuwasiliana na viongozi wa wizara zimekwama baada ya kuzunguzwa zungushwa na viongozi wa wizara hiyo akiwemo Waziri wa Wizara hiyo Prof. Msolla ambaye amefikia kukata simu kila vijana hao wanapojitambulisha. Wizara hiyo hiyo imeshindwa kushughulikia matatizo ya wanafunzi wengine walioko nje ya nchi wanaokabiliwa na matatizo yanayolingana au kukaribiana na yale ya Ukraine. Miongoni mwa wanafunzi walioko katika hali mbaya ni wale wa Cuba, na wale Urusi.
- e. Jitihada za wazazi wa vijana hao kuwasiliana na viongozi wa Bodi ya Mikopo na wizara imeshindikana baada ya serikali kusema kuwa "haiwatambui" vijana hao na hivyo kuwafanya wazee hao kushindwa kujua wafanye nini isipokuwa kuanza hatua za kisheria dhidi ya wizara na wahusika wengine. Madai haya ya kutowatambua yalithibitishwa na Prof. Msolla mwenyewe alipozungumza nami mapema leo. Na nilipomuuliza kama wizara au bodi ya mikopo haikutoa ahadi yoyote kwa vijana hao alikataa kujibu na kukata simu na kuizima kabisa. Sehemu ya mahojiano yangu na Prof. Msolla yatasikika kesho.
- f. Ubalozi wa Uingereza Ukraine uliipa serikali ya Tanzania ofa ya kuwasaidia kuwalipia vijana hao na kuwapa misaada mingine ya kibinadamu endapo tu serikali ya Tanzania itaandika barua ya kurudisha fedha hizo kwa serikali ya Uingereza. Serikali ya Tanzania haikuwapa jibu hadi leo.
- g. Balozi wa Tanzania Urusi ambaye pia anatuwakilisha Ukraine amejitahidi kufanya mambo mengi ambayo yangefanywa na wizara hadi amefikia mahali pa kuwaambia wanafunzi hao hana jingine la kufanya na kuwataka "waombe Mungu".
- h. Ahadi ya serikali ya kutuma ujumbe kwenda nchi hizo (usiniulize pesa za ujumbe huo zitatoka wapi) kwenda kuangalia matatizo hayo mwanzoni mwa mwezi huu imefutwa na hakuna ahadi nyingine au mpango unaoeleweka wa kufanya ziara hiyo.
- i. Bodi ya mikopo ya elimu ya juu imekuwa ikibadili badili taratibu na kushindwa kabisa kuja na utaratibu wa haki, unaoeleweka na wenye mantiki katika kushughulikia tatizo la elimu ya Juu Tanzania. Matatizo yanayotokea kwenye vyuo vikuu nyumbani na yaliyosababisha wanafunzi kugoma ni matokeo ya bodi goigoi, isiyo makini, isiyojua inachofanya, na isiyo na uwezo wa kushughulikia suala zima la elimu ya juu. Bodi hii ni aibu kwa Taifa, ni kashfa iliyochosha, na ni mfano wa ukiritimba uliokithiri. Ni lazima ivunjwe.
Ni kutokana na mambo hayo yote, vijana wetu, watoto wetu na wa Watanzania wenzetu wamefikia kikomo cha ustahimilivu wao na uungwana wao. Majaribio yote ya kutatua tatizo hili kimya kimya yameshindikana. Wakati wa kumwajibisha Prof. Msolla, Mama Katunzi, na wakuu wa Bodi ya Mikopo umefika. KLH News inasimama upande mmoja na vijana hawa kwa kitendo chao ambacho kingeweza kuepukika lakini kutokana na kiburi na ubabe wa serikali (ambao umeendelezwa) imebidi wakichukue. Hisia ya viongozi wa serikali kudhani wanaimiliki Tanzania na wana maamuzi ya mwisho ni lazima ioneshwe kuwa ni hisia iliyopotoka na isiyo na nafasi tena katika jamii yetu. Viongozi ni watumishi na wanatakiwa kuongoza. Katika hili wameshindwa kabisa kuongoza na badala yake wamebakia kupiga kelele za "ukuu wa serikali" wakionesha wazi kutojali hatima ya watoto wa wenzao!! Unganeni nami, na kwa mlio mmoja kuitisha kujiuzulu kwa Prof. Msolla na Mama Katunzi, na kuvunjwa kwa bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu.
M. M. Mwanakijiji