HabariLeo; Tuesday,May 29, 2007 @00:01
HATIMAYE Serikali imetoa tamko kuhusiana na hatima ya wanafunzi 29 waliosimamishwa masomo katika vyuo vya elimu ya juu Ukraine kutokana na kushindwa kulipa ada. Katika tamko lililotolewa na Kaimu Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu ya Juu, Sayansi na Teknolojia, Celestin Gesimba, Serikali imewataka wanafunzi hao kurejea nyumbani mara moja.
Alisema katika mwaka wa masomo wa 2005/06, wanafunzi 130 walipata udahili katika vyuo vikuu mbalimbali nchini Ukraine na kati yao ni wanafunzi 84 ndio waliokamilisha taratibu za kupata mkopo kutoka Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu na walijiunga na vyuo hivyo.
Kaimu Katibu Mkuu huyo aliendelea kueleza kwamba wanafunzi wengine 46 hawakuweza kukamilisha taratibu hizo na walishauriwa wajiunge na vyuo vya elimu ya juu vya hapa nchini, kwa vile serikali haikuwa na uwezo wa fedha.
Alisema wanafunzi 17 kati ya wanafunzi hao 46 walikubali kutafuta udahili kwa vyuo vya elimu ya juu nchini na wanafunzi 29 ambao ndiyo waliofikwa na matatizo ya ada nchini Ukraine hivi sasa, hawakukubaliana na ushauri huo wa serikali wa kusoma nchini.
Alisema wanafunzi hao wamekwama kulipa ada na sasa wamesimamishwa masomo na wanaulazimisha ubalozi wa Tanzania ulioko Moscow, uiombe Serikali iwasaidie. Wakati Serikali ikitoa tamko hilo, imeripotiwa kwamba wanafunzi hao sasa wamekwenda kuweka kambi katika Ubalozi wa Uingereza mjini Moscow wakiomba Serikali ya Uingereza iwasaidie, kwa vile Serikali ya Tanzania imeshindwa kuwasaidia.
Hatua hiyo imekuja siku chache tangu wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na matawi yake walipogoma na kusimamishwa masomo na baadaye kurejeshwa vyuoni kutokana na kuibana Serikali kuwakopesha asilimia 100 ya ada na fedha za matibabu. Pamoja na kuibana kwa kila hali ili Serikali itimize azma yao hiyo, bado Serikali ilisisitiza kwamba haikuwa na fedha za kutosha za kuwakopesha kwa asilimia 100, wanafunzi wote wa vyuo vya elimu ya juu, hatua ambayo iliwafanya wanafunzi hao kugomea masomo na baadaye kusimamishwa masomo.
Tamko hilo la serikali dhidi ya wanafunzi hawa wa Ukraine, halina ubishi kwamba limetokana na kosa lililofanywa na wanafunzi hao la kudharau ushauri wa serikali yao. Ni wazi kwamba Serikali haikuwa na fedha za kuwakopesha wanafunzi hao ili waende kusoma nje ya nchi na ndiyo maana iliwashauri kutafuta vyuo vya ndani ikiamini kwamba ulipaji wake ni nafuu zaidi.
Ukweli huu unathibitishwa na kitendo cha kushindwa kuwapa asilimia 100 ya mkopo hata kwa wanafunzi wa vyuo vya elimu ya juu vya hapa nchini, hatua iliyowafanya waone kama serikali yao inawanyanyasa na kugomea masomo.
Kwa vile hili limekwisha kutokea ni vizuri kwa wanafunzi hawa wakajifunza kutoka kwa wenzao wa vyuo vya juu nchini ambao pamoja na kuishinikiza serikali kuwapa fedha walizotaka, shindwa kufanya hivyo na wakajikuta wakiingia katika mgogoro uliosababisha kusimamishwa
masomo.