Roving Journalist
JF Roving Journalist
- Apr 18, 2017
- 3,984
- 13,760
Dar es Salaam, Tarehe 02 Julai, 2024
Shirika la Reli Tanzania - TRC linautaarifu umma kuwa Seti mbili (2) za treni ya kisasa inayotumia nishati ya umeme EMU (Electric Multiple Unit) na vichwa nane (8) vya treni vya umeme vimewasili Tanzania kutoka nchini Korea ya Kusini.
Serikali kupitia TRC ilifanya manunuzi ya Seti kumi (10) za treni za EMU zinazotengenezwa na kampuni ya Hyundai Rotem ya nchini Korea Kusini, Seti moja ya EMU ina jumla ya mabehewa nane yakijumuisha kichwa kimoja mbele na kingine nyuma ikiwa na uwezo wa kubeba abiria 589 na kutembea kwa kasi ya kilomita 160 kwa saa.
Seti mbili (2) za EMU zinafikisha idadi ya seti tatu zilizowasili nchini mpaka sasa, seti ya kwanza iliyowasili mwezi Aprili 2024 inaendelea na majaribio.
Shirika la Reli Tanzania limeshapokea jumla ya mabehewa 65 ya abiria, vichwa 17 vya umeme na Seti tatu za EMU. Upokeaji wa vifaa vya uendeshaji vya reli ya kiwango cha SGR unaendelea kwa awamu tofauti, vifaa vipya vilivyowasili vitaendelea kufanyiwa majaribio kwaajili ya kujiridhisha kabla ya kuanza kutoa huduma.
Shirika linaendelea na uendeshaji wa awali na utoaji huduma ya usafiri wa treni za umeme kupitia reli ya kiwango cha kimataifa kati ya Dar es Salaam na Morogoro, uendeshaji rasmi kati ya Dar es Salaam hadi Dodoma unatarajiwa kuanza Julai 25, 2024.
Jamila Mbarouk Mkuu wa Kitengo cha Uhusiano