The Sheriff
JF-Expert Member
- Oct 10, 2019
- 747
- 2,112
Marehemu mzee Morris Nyunyusa
Nina jambo moja ambalo huwa linanitatiza kidogo. Majina ya viongozi wa kisiasa ndiyo yametanda kila kona ya nchi yetu. Kuanzia majengo, mitaa, barabara, taasisi za elimu na nyinginezo. Hili sina shida nalo na wala sina dhamira ya kulifanya kuwa shida akilini mwangu ama kwa mwingine.
Hata hivyo, ninachotaka kujua ni kama kuna, ama hakuna, uwezekano wa kuwa na utaratibu pia wa kuwaenzi (kwa wingi stahiki) hata watu mashuhuri wa hapa nchini ambao wana mchango mkubwa katika michezo na sanaa kwa ujumla. Kwa mfano akina Morris Nyunyusa, Mbaraka Mwishehe, Remmy Ongala, Bi. Kidude, Siti Bint Saad, Suleiman Nyambui, Hasheem Thabeet, Juma Ikangaa, Mbwana Samatta, Gidamis Shahanga, Alfredo Shahanga, Filbert Bayi, John Stephen Akwari n.k.
Naamini orodha ya watu wanaopaswa kuenziwa ni ndefu sana. Kuna Watanzania wengi ambao wanastahili kuenziwa kutokana na mambo makubwa waliyoyafanya na kuiweka Tanzania katika ramani ya dunia kimichezo na kisanaa. Ni ajabu sana kwamba majina ya watu hawa wa muhimu katika taifa letu yanazikwa na historia zao kufutika.
Sasa basi, ili kuepusha kujirudia kwa majina yale yale (ya wanasiasa na vizazi vyao), nadhani ni vyema tukiwapa nafasi watu wengine kutambulika na vizazi vijavyo ili kulinda historia ya nchi yetu. Watoto wetu wanapaswa kufahamu historia ya nchi yao tofauti na ya kisiasa pekee.
Mwenye mawazo na orodha za Watanzania au chochote cha Kitanzania kinachopaswa kuenziwa kwa mtindo huo unakaribishwa.
Nawasilisha