Simulizi ya Kijasusi: Mikononi Mwa Nunda

Simulizi ya Kijasusi: Mikononi Mwa Nunda

SEHEMU YA 79

aliyofikia kwa kukosa pesa za kulipia.”
“Ndipo alipofikia hatua ya kufanya kile ambacho kamwe hakupenda kukifanya, kujikabidhi mikononi mwa wanaume ambao waliuchezea mwili wake kama mzoga kwa malipo hafifu ambayo yaliandamana na kashfa. Ulikuwa wakati mgumu kuliko nyakati zote alizowahi kupitia, kulazimika kumkumbatia mwanaume yeyote; mbaya kwa mzuri; anayetisha kwa anayechekesha; anayetesa kwa anayesimanga; anayependeka kwa asiyependeka. Yeyote, mradi ana chochote ambacho kingemwezesha kuishi. Wote waliomfikia ingawa aliwalaki kwa tabasamu, lakini moyoni aliwachukia zaidi ya sumu. Alijua ni mbwa mwitu katika ngozi ya kondoo, haja yao si zaidi ya kuburudisha nafsi zao zenye kiu isiyokatika. Na alimchukia zaidi yeyote ambaye alijitia kumpenda na kusisitiza ndoa. Mtu wa aina hiyo alimwona kama chui ambaye alitaka kuwa na zizi la mbuzi mwituni. Aliona kheri aendelee kuwa jamvi la wote badala ya kigoda cha mmoja wao.”
“Wakati ulipotimu alijifungua mtoto mzuri wa kiume. Usiku uleule ambao alimzaa akafanya kile ambacho wasichana wote waliopotoka hufanya mara wapatapo mtoto asiyehitajika. Alimnyonga na kuutumbukiza mzoga chooni.”
“Hakumtupa mtoto huyo kwa ajili ya upotovu kama wasichana wengine ili aendelee kuitwa msichana badala ya mama, la. Wala haikuwa kwa hofu ya kushindwa kumlea ipasavyo. Kilichomfanya amtupe hasa ilikuwa kule kuona kuwa kazaa kiumbe mwingine wa kiume, kiumbe mwingine ambaye angeendeleza kanuni ileile ya kuwafanya wanawake watwana au vyombo ambavyo vililetwa duniani kumstarehesha mwanaume. Yeye ambaye anahitaji kuiondoa kanuni hiyo, yeye ambaye ameteseka kwa ajili ya kanuni hiyo, vipi akubali kutunza kiumbe mwingine wa kiume? Ni hilo ambalo lilimshawishi kuangamiza damu yake mwenyewe.”
“Kitendo chake kilifahamika kwa jirani ambao waliiarifu polisi. Msichana huyo alikamatwa na kufikishwa mahakamani ambako alikiri kosa lake lakini hakuruhusiwa kueleza hoja zake. Akahukumiwa kifungo cha miaka mitatu na kazi ngumu. Huko gerezani aliteseka sana. Alipofunguliwa alirejea mtaani, katika vichochoro vilevile vya Buguruni, Magomeni, Kariakoo na kwingineko. Hali ikiwa ngumu kiuchumi, wanaume waliadimika mno. Ikawa vigumu kuwaona wakimfuata kama awali. Hivyo, akawajibika kuomba kazi ya kuuza pombe kwenye mabaa mengi, akikutana na watu wengi. Kati yao alifahamiana na majambazi, wafanya magendo na wagongaji, kama ambavyo alikutana na mahakimu, walimu na wakulima. Wote hao walimshirikisha katika harakati zao za maisha na siri zao bila ya kujijua. Ndipo akapata fursa ya kuwafahamu majambazi wengi na mienendo yao.”
“Ni wakati ambao alikuwa ameajiriwa West Bar alipokutana na mtu ambaye kamwe asingeweza kumsahau, mtu ambaye alikuwa kisa hasa cha kuanguka kwake kimaisha, adui yake mkubwa, Ukeke Maulana. Hasira zikampanda ghafla na njaa ya kulipiza kisasi kumteka hata akamwendea na kumshawishi mapenzi. Alipolaghaika badala ya kupokea mahaba aliyoyategemea alijikuta akipokea pigo la kisu, pigo lililomtoa duniani.”
***
Joram aliisikiliza hadithi hiyo kwa makini sana, macho yake yakimtazama Suzana hali mikono yake ikishughulikia sigara moja baada ya nyingine. Msichana huyo aliposita na kuvuta pumzi kwa nguvu, Joram alijirekebisha juu ya kiti na kunong’ona jambo ambalo halikumfikia Suzana.
“Msichana huyo ni mimi, Joram. Mimi hapa. Na hiyo ni hadithi ya kweli inayohusu maisha yangu.” Baadaye alisema kwa sauti ndogo, iliyotofautiana na ile aliyotumia kueleza habari nzima.
 
SEHEMU YA 80 ....................... MWISHO




“Ndiyo,” Joram alimjibu. “Toka hapo naweza kueleza. Toka ulipotoka ufukoni ambako ulimwua Ukeke ndipo ulipomkuta Mohamed Matoke akibarizi nje ya nyumba yake, kama ilivyokuwa kawaida yake. Ukiwa bado na hamu ya kuua ukamwendea na kumshawishi mapenzi hata mkafuatana chumbani ambako ulimwangamiza. Siyo?”
“Kidogo umekosea,” Suzana akamwelekeza. “Kwa kweli, mara baada ya kumwua Ukeke nilichanganyikiwa nikiwa sijui la kufanya. Nilipokuwa nikienda zangu nisipokujua mzee huyo aliniita na kuanza kunitongoza. Hasira zilinipanda hasa nilipowaza kuwa huyu ni mwanaume mwingine ambaye alikuwa na njaa ileile ya kumfanya mwanamke kuwa chombo chake cha starehe. Anichezee kwa muda na kisha kunitupa! Ndipo nikaamua naye afe. Uoga wake pindi akifa ukamfanya aanze kunionyesha alikoficha fedha yake, fedha ambayo, kwa kweli, sikuhitaji wakati huo. Akawa amenipa wazo jipya. Wazo la kujipatia fedha nyingi. Hivyo, nilipomwacha nilifikiria namna ya kuipata fedha hiyo, ingawa sikujua namna ya kuitumia. Ndipo liliponijia wazo la kuyatumia majambazi yote niliyoyajua kuendelea kuua huku na huko hali mimi nikipita na kukusanya faida. Hakuna hata mmoja wao aliyenijua wala kunidhania kuwa ningeweza kuwa Nunda. Wote waliniona kama kila mwanaume amwonavyo mwanamke; mnyonge asiye na uwezo wa kufanya lolote.” Akacheka kidogo kabla hajasema, “Sijui ningeendelea mpaka lini kama usingetokea na kuharibu mkondo wangu wa kulipiza kisasi.”
Joram naye alicheka kidogo na kumjibu, “Ungeweza kuua jiji zima na bado usiibadili kanuni uliyokuwa ukipambana nayo. Kisasi siyo dawa ya kuondoa maradhi hayo ya ubinafsi ambayo yanaitesa jamii na dunia nzima. Sasa vaa vizuri, tupa kisu hicho tujadili hali yako ya baadaye.”
“Hapana. Bado nina kazi moja ya mwisho,” Suzana alimjibu akiinuka. “Nitakuua wewe, kisha nijiue na kuisahau dunia hii na maovu yake.”
“Usijidanganye, mpenzi wangu,” Joram alijibu akiwa amejituliza kitini, “Kuniua huwezi, wala sitapenda kukuona msichana mzuri kama wewe ukijiua. Hivyo, keti pale tuzungumze suala lako.”
“Joram!” sauti ya Suzana ilikuwa na mshangao. “Yaani hujanichukia kiasi cha kuniona mtu anayestahili kufa? Tuseme hukukusudia kunipeleka mahakamani nikanyongwe?”
Joram akatikisa kichwa kukataa. “Ndiyo, wewe ni mwuaji mkubwa, shetani mdogo ambaye amemwaga damu nyingi isiyo na hatia. Lakini bado u msichana mzuri kuliko wazuri wengi niwajuao.”
“Joram!” akafoka kwa mshangao uliochanganyika na hofu. “Sikujua kama wanipenda. Nilidhani haja yako ni kuniangamiza kama wanaume wenzako. Kumbe hatimaye ametokea mtu mmoja tu duniani ambaye ananipenda. Ni wewe peke yako,” akasita. “Kwa ajili hiyo sitakuua. Nitakufa peke yangu. Nife nikijua kuwa nimemwacha duniani mtu anipendaye,” alimaliza kusema akijiweka sawa na kukielekeza kisu ubavuni mwake.
Joram aliinuka hima akisema, “Usifanye hivyo Suzana!”
“Usiniguse mpenzi.”
Dakika hiyohiyo mlango ulifunguliwa na kuwaruhusu askari wanne wakiongozwa na Inspekta Mkwaju Kombora ambaye bastola yake ilimtangulia wazi mkononi.
“Usithubutu,” Kombora alifoka kwa sauti yake kali.
Haikusaidia. Dakika hiyohiyo kisu kilikuwa kikizama katika moyo wa Suzana. Kikamlainisha na kumfanya aanguke chali kitandani. Kombora alimkimbilia na kuambulia damu nyingi ambayo ilibubujika toka katika jeraha kubwa la jisu hilo. Juhudi zake za kuizuia damu hiyo isiendelee kutoka zilikuwa kazi bure kwani macho ya Suzana yalianza kuelekea katika dalili ya kifo. Baada ya muda akawa mzoga uliolala nusu uchi. Ilikuwa baada ya kuliita polepole jina la Joram na kushindwa kusema chochote alichokusudia kusema.
“Umechelewa sana Inspekta,” Joram alisema akiyatoa macho juu ya maiti na kumtazama Kombora.
“Nimechelewa! Ulijuaje kuwa nilikuwa nikija?”
“Nilijua wazi kuwa ungenifuata tangu nilipokugusia kumtia Nunda mikononi leo. Naamini ulikuwa nyuma ya mlango ukisikiliza maongezi yetu kwani nilisikia minong’ono yenu. Hivyo, sitakuwa na haja ya kueleza chochote zaidi.”

*MWISHO*****MWISHO****MWISHO








BURE SERIES
 
RIP Ben R Mtobwa.

Moja ya waandishi ninaowakubali sana.
Mwandishi bora zaidi kwa waliopo sasa na mshindani wa kweli kwa manguli waliopita
 
MWISHO*****MWISHO****MWISHO
Heshima kubwa Sana kwake mtunzi pamoja uliyefanikisha kuleta hapa
 
Back
Top Bottom