Simulizi ya kusisimua: Kaburi la Mwanamuziki

Simulizi ya kusisimua: Kaburi la Mwanamuziki

KABURI LA MWANAMUZIKI EP 10
Mtunzi; Robert Heriel
0693322300

ILIPOISHIA

“ Nimefikaje hapa” Nikawaza, simu bado ikiendelea kuita, sikutaka kuipokea nikawa nakikagua kile chumba kwa macho, kilikuwa chumba kikubwa kilichotosha kitanda cha ukubwa wa sita kwa sita, kulikuwepo na sofa na kimeza cha kioo, chini likiwepo zulia zuri la manyoya, pembeni kabisa lilikuwepo kabati la nguo lenye milango miwili, mlango mmoja ukiwa na kioo, mlango mwingine ukiwa umefunguka nusu, ndani yake niliweza kuona nguo za kike, juu ya kabati ilikuwepo midoli mikubwa miwili yenye kuvutia, mpaka hapo niliamini chumba kile kilikuwa cha mwanamke, macho yangu yalihama upande huo wakati yakizunguka yaliona mapazia mawili maridadi ya kisasa, yaliyofunika madirisha ambayo sikuweza kuyaona, mwisho macho yangu yalikuwa juu ya mlango ambapo kulikuwa na saa kubwa ya ukutani, na kabla sijaona ni saa ngapi mlango ukafunguliwa, nilishtuka kumuona Alice akiwa kabeba sinia lenye vikorombwezo vya kifungua kinywa, alivyoniona nimeamka akatabasamu.

ENDELEA
“ Rise and shine Baby!” Akasema, nikawa namtazama na wala sikumjibu lolote, akaweka lile sinia kwenye Ile meza ya Kioo, kisha akanifuata pale kwenye kitanda, nikainuka na kuketi, akanibusu lakini nikawa namzuia,

“ Mbona unanizuia Mpenzi” akasema, kisha akanitazama,

“ Naomba unipishe nahitaji kwenda nyumbani Mama yangu atakuwa na wasiwasi” Nikasema nikiwa naamka pale kitandani,

“ Gibson! Mbona hivyo lakini, tayari nimeshaongea na mama yako, anajua upo kwangu” akasema, maneno hayo yalinifanya nimtazame vizuri, alikuwa amenishtua,

“Mbona unaniangalia hivyo, mimi sio mgeni kwako, wala sio mgeni kwa mama yako, ninafahamika mpaka na ndugu zako achilia mama, unavyoshangaa sijui unamaanisha nini? Embu kaa chini acha mambo ya kitoto” Alice akasema huku akiniketisha kwa nguvu ungedhani ni Dada yangu, nikaketi tena kwenye kitanda, hapo nikakumbuka maneno ya Neema, “Mbwa koko ni Alice na sio huyu kipenzi changu” nikamtazama Alice, ungedhani namfananisha na mbwa koko, Alice alikuwa akimimina chai ya maziwa kwenye kikombe akanitazama,

“ Tatizo lako unavamia wanawake hovyohovyo usiowajua, ona sasa” Alice akasema, akaketi kwenye sofa na kunikaribisha chai, nilikataa katakata, wakati tukibishana mara simu ikaita tena, kuchungulia alikuwa ni Mama anapiga, “pokea” Alice akanieletea simu nikaipokea na kuiweka sikioni, mama alinambia nirudi nyumbani, wala sikuweza kujibu chochote, nikakata simu, nikaondoka nikimuacha Alice akinilazimisha kubaki..

*********

“ Kuna mstari mwembamba kati ya mapenzi na chuki, pia kuna mstari mwembamba kati ya uaminifu na usaliti, alichokifanya Neema huwezi ukamlaumu, hayo ndio maisha, huwezi ukajifunza vizuri na ukawa mwanafunzi mzuri katika maisha kama hujapitia maumivu makali, kwenye mapenzi huwezi yajua mapenzi yakoje kama hujawahi kusalitiwa, kama ukipendwa tuu siku zote pasipo kusalitiwa huwezi ijua thamani ya upendo, upendo wa kweli ni ule unaobakia baada ya mtu kuumizwa, kama hujaumizwa kwenye mapenzi huwezi sema unaupendo wa kweli. SIjui unanielewa mwanangu” Mama alisema, lakini sikuwa namuelewa anazungumzia nini,

“ Mama, hata sikuelewi, naona unanichanganya tuu” Nikasema,

“ Utanielewa polepole mwanangu, kama hutanielewa leo basi utanielewa kesho, kama hutanielewa nikiwepo basi utanielewa siku nikiwa sipo” Akasema,

“ Lakini Mama nampenda Sana Neema, kwa nini anifanyie hivi lakini?” Nikasema,

“ Huna haja ya kumlaumu Neema, Maisha hayahitaji umuamini mtu, hilo litakuwa ni kosa kubwa litakalouumiza nafsi yako, maisha yanahitaji upendo lakini upendo wa kutokuaminiana, unajua ni kwa nini?” Akaniuliza,

“ Mimi sijui mama” Nikajibu,

“ Unajua nini ninakiwaza sasa hivi?” Akasema, nikawa namtazama tuu alafu akaendelea kusema

“ Kwa sababu moyo wa ni msitu, na kichwa chake ni bahari, kama tungekuwa tunauwezo wa kujua mawazo ya watu wengine watuwaziayo basi ningekuambia uwaamini binadamu, lakini kwa vile hatujui mawazo ya wengine ndio maana haupaswi kumuamini mtu mwingine”

“ Sasa kama mtu haumuamini kwa nini umpende? Nikauliza nikiwa nimemkatisha.

“ Gibson, upendo ndio maisha, upendo ni dawa ya moyo, upendo utakufanya uishi maisha mema yenye furaha, hatuwapendi watu kwa sababu wanatutendea wema, hapana, tunawapenda watu ili maisha yawe ya furaha, utampenda mtu ili usimuumize na kuingia katika matata ya sheria, ukimpenda mtu huwezi mtendea mabaya” Akasema,

“ Kwa hiyo Neema alinitendea haya kwa sababu hanipendi, Mnafiki mkubwa yule, kumbe alijigeuza kondoo kumbe ni fisi” Nikasema kwa hasira,

“ Hapana Gibson, Kuna upendo na tamaa, kuna hasira na chuki, mtu anaweza akawa anakupenda sana lakini tamaa ikamponza, tamaa wakati mwingine huweza kuutikisa upendo wa kweli, hasira haimaanishi chuki, kwa mfano wewe sasa hivi unahasira na Neema lakini humchukii, kama utairuhusu hasira yako izae uchungu moyoni mwako itazaa chuki ambayo ni kinyume na upendo” Akasema

“ Nimpende nani sasa, kila ninayempenda ananiumiza, wanawake ni wabaya sana”

“ Gibson, usijali mwanangu utampata akupendaye, unachoweza kukifanya kwa sasa ni kujipenda mwenyewe na kujikita kwenye ndoto yako” Mama akasema, kisha tulimaliza kuongea akaniaga akiniacha chumbani.

Nikiwa chumbani nilikumbuka maneno ya Rais aliyoninong’oneza siku ile ya Tamasha, niliangalia kwenye kalenda iliyokuwa mule ndani ambayo niliiwekea alama tarehe aliyoniambia nikutane naye, “ Kumbe siku yenyewe ni kesho tuu” Nikawaza, nikiwa naangalia tarehe kuhakiki kama ni kweli ni kesho au nimeangalia vibaya, lakini wala sikuwa nimeangalia vibaya, tarehe ya kukutana na Rais ni kweli ilikuwa kesho, nikawa nawaza ni jambo gani Rais anataka kuzungumza na mimi, kwa kweli sikupata majibu ya moja kwa moja, unajua kuitwa na Rais sio jambo dogo ndugu msomaji, embu fikiria Rais anayeongoza mamilioni ya watu akuite wewe Ikulu, lazima utakuwa na wasiwasi uliochanganyika na furaha,

Kwenye bahati kuna mtego, kwenye mazuri kuna gharama, na kadiri unavyoikaribia pesa ndivyo unavyokaribia kuvunja sheria, sisemi kuwa na pesa ni kuwa mhalifu isipokuwa nawatahadharisha watu kuwa pesa ipo kwenye mlango wa gereza, kadiri unavyoisogelea na kuichota nyingi ndivyo unavyojiingiza gerezani. Sasa hapo itategemea kama mahakamani kuna haki au rushwa imetamalaki, hiyo ndio itaamua utambe mtaani au ujikute korokoni.

Hakukukawia kukucha, asubuhi nilikuta missed call ya Aunt, nikampigia akasema yupo Zanzibar atakaa huko wiki moja ili arudi Dar, nikiwa navuta vuta muda nikingojea muda wa kwenda kuonana na Rais niliingia mtandaoni kujivinjari, nikijibu baadhi ya maoni ya wafuasi na wapenzi wa kazi zangu za muziki, wapo waliokuwa wakinisifu na kupongeza kwa kazi nzuri huku wakinitakia kila lenye kheri katika kazi zangu, nilikuwa najisikia fahari kuona maelfu elfu ya watu wakiparangana kwenye ukurasa wangu mtandaoni, nilivutiwa na wafuasi waliokuwa wakinikingia kifua kwa wale waliokuwa maadui zangu wasiopenda kazi zangu, nilikumbuka siku zile kabla sijawa maarufu jinsi akaunti yangu ilivyokuwa imechacha bila watu ku-like wala kutoa maoni yao, lakini wakati huu nikiweka tuu kitu mtandaoni haizidi dakika maelfu ya watu wanajitokeza kuonyesha hisia zao.

Sehemu ya Inbox zilijaa jumbe nyingi za watu mbalimbali, wadada warembo waliotaka niwachumbie walijaa pomoni, vijana wakike na wakiume waliokuwa wanaomba msaada niwashike shati kimuziki nao walikuwa katika msafara, sikuwa na uwezo wa kusoma jumbe zote, hiyo kwangu ingekuwa sehemu ya biashara, ningeweza kutumia akaunti zangu mtandaoni kama jukwaa matangazo kujiingizia mapato, baadhi ya makampuni yaliingia ubia na mimi niyatangazie bidhaa zao, na kila bidhaa niliyoitangaza katika ukurasa wangu ilifanya vizuri sokoni, hiyo ilizidi kuongeza thamani ya jina langu na kuongeza pato langu, ingawaje sio sana kivile kutokana na sababu ya kielimu. Laiti ningekuwa na elimu walau shahada moja huenda mambo yangekuwa tofauti, kila mara wazo la kujiendeleza lilikuwa likija lakini majukumu mengi yalifanya nishindwe.

Jioni ilifika, tofauti na nilivyotarajia kuwa nitaenda kwa Rais kwa kutumia gari langu nikashangaa Mama akiniita, kufika sebuleni nikakuta wanaume wawili waliojitambulisha kama maafisa wa Ikulu waliotumwa na Rais, baada ya kujiandaa nikachukuliwa na wale maafisa, walikuwa wameligesha gari lao nje ya Geti, ilikuwa VX ya damu yam zee yenye vioo vya tinted, nikaingia ndani ya gari, safari ikaanza, hatukuzingatia sana sheria za barabarani na gari lilikuwa kasi kiasi, Giza lilikuwa limeingia, tukaingia kwenye Hotel kubwa ya kimataifa, kisha tukatoka ndani ya gari, eneo lote lilikuwa limepoa sana, huku mazingira ya hotel ile yakizidi uzuri wa kipimo cha macho yangu, sikuwahi kudhani hapa Dar kuna Hoteli yenye uzuri wa namna ile, kuna wakati nilidhani nipo nchi zilizoendelea, lakini kila nilipokumbuka nilikuja na Gari imani yangu ikabaki kuwa thabiti kuwa bado nipo Dar. Tukapanda ngazi huku tukipokelewa na lango kubwa pana kama hatua kumi na tano hivi lenye vioo ambavyo vilikuwa na sensor, tulipolikaribia likateleza kwa kutawanyika kutupisha tupite katikati, mbele tulilakiwa na ukumbi mkubwa ambao kwa mbele kulikuwa na mapokezi ya kisasa yenye vijana wawili wakiume waliovalia kitanashati, kila kitu kilikuwa kwa mpangilio wa kipekee, sakafu ya hoteli ile ilikuwa kama rangi ya bahari huku kitu mfano wa maji yakipita chini ya ile sakafu, kulia kama hatu kumi zilikuwepo vizuizi vinavyohitaji alama za vidole au kadi maalumu ili mtu apite, kushoto kama hatu kumi zilikuwepo vijito vya maji vinavyorusha maji juu na kuunda maumbo mbalimbali ya kushangaza, kwa mbele kabisa kulikuwa na sehemu ya mgahawa ambao watu wachache wenye asili ya bara la Ulaya walikuwa wakiendelea kujivinjari, hayo yote yaliendelea kuyashibisha macho yangu, tofauti na watu wengine ambao tuliwakuta pale ambao ni mpaka watoe kitambulisho Fulani au passport alafu wapewe kikadi Fulani ambacho wangekitumia Kupitia kwenye vile vizuizi, sisi tulifika yule mwanaume akachukua kadi tatu, kisha akawaaga wale watu wa mapokezi, moja kwa moja tukapita vile vizuizi na kusonga mpaka kwenye Lifti, akabonyeza Floor ya 40, lifti ikaanza kupanda,

Hofu ikaanza tena kung’otang’ota moyo wangu, sijui nilikuwa naogopa jambo gani, lakini nilihisi magoti kukosa nguvu, kitambo kidogo tulifika, tulipokelewa na Kibao kilichoandikwa 40 FLOOR, VIP., Hapo tukatembea kuukabili mlango wa vioo vitupu vinavyoonyesha taswira zetu, tulikuwa tukijiona tukiukabili ule mlango, kwa pembeni kilikuwepo kifaa kinachowaka taa nyekundu alafu chini yake kuna alama ya kuweka dole gumba, kamaera za CCTV kamera zilikuwa tatu, moja ilikuwa kwenye mlango, nyingine juu ya dari, nyingine kule kwenye lifti tulipokuwa tumetokea, Mmoja wa wale wanaume akasogelea ule mlango akaweka Dole gumba, kukatokea kioo mfano wa flat screen na maandishi yalioyoandika Please wait, baada ya sekunde kumi kwenye kile kioo kama cha Luninga tukajiona wote watatu kama vile video call za WhatsApp au Zoom App, kisha iile video ikagawanyika vipande viwili, sisi tukiwa upande wa chini alafu nikashtuka kumuona Rais kwenye video upande wa juu wa ile Screen ya luninga, alikuwa ameketi kwenye kiti mbele yake kukiwa na meza kubwa yenye lapatop, ni kama kuna kazi alikuwa akiifanya, kisha baada ya yeye kutuona akatuashiria tuingie, nikamuona akibonyeza simu yake, nikshangaa mlango unafunguka, nikajua ule mlango umeunganishwa wireless na simu ya Mhe. Rais.

Tukapokelewa na korido fupi ambapo mbele kidogo kulikuwa na mlango wa vioo ambavyo havionyeshi taswira zetu, ule mlango ukatawanyika tukapita katikati, hapo tukaingia kwenye ukumbi wa mkutano wenye meza ndefu zenye viti vingi, alafu mbele kuna Ubao na Luninga yenye kioo cha nchi kama hamsini na tano hivi, tukasonga, mpaka tukatokea kwenye ukumbi mwingine ambao kulikuwa na bustani ya maua na bwawa la kuogelea, pamoja na sehemu ya viti na meza za kupumzikia, wale wanaume wakaniacha huko, kisha wao wakarudi, wakiniambia nimsubirie Mhe. Rais hapo.

ITAENDELEA.
jipatie nakala ya kitabu cha WAKALA WA SIRI kwa Tsh 15,000/=

Namba ya muamala
0693322300
Robert Heriel
Airtelmoney
 
KABURI LA MWANAMUZIKI EP 11
Mtunzi: Robert Heriel
0693322300

Ilipoishia

Tukapokelewa na korido fupi ambapo mbele kidogo kulikuwa na mlango wa vioo ambavyo havionyeshi taswira zetu, ule mlango ukatawanyika tulipouksribia tukapita katikati, hapo tukaingia kwenye ukumbi wa mkutano wenye meza ndefu zenye viti vingi, alafu mbele kuna Ubao na Luninga yenye kioo cha nchi kama hamsini na tano hivi, tukasonga, mpaka tukatokea kwenye ukumbi mwingine ambao kulikuwa na bustani ya maua na bwawa la kuogelea, pamoja na sehemu ya viti na meza za kupumzikia, wale wanaume wakaniacha huko, kisha wao wakarudi, wakiniambia nimsubirie Mhe. Rais hapo.

ENDELEA
Kitambo kidogo hata kabla macho yangu hayajazoea eneo lile, Mhe. Rais akafika;

“ Aah! Habari yako Gstar, Karibu sana, Nimefurahi kuona umeitikia wito wangu” Rais akasema, uso wake ukifunikwa na tabasamu nzito.

“ Kama nisipoitikia Wito wa Rais wa nchi yangu, mchapakazi, mzalendo kama wewe, Sidhani kama yupo mwingine nitakayeitikia wito wake” Nikasema,

“ Hahahaha! Gstar unamaneno ya kisanii sana” Akasema,

“ Hapana Mhe. Huo ndio ukweli, nchi yetu inayobahati kubwa kuongozwa na Rais mwenye akili na uchu wa maendeleo kama ulivyowewe” nikasema, kisha nikameza mate, nikiwa nimesimama tangu nilipomuona Mhe. Rais, Nikaendelea,

“ Shikamoo Mhe. Rais”

“ Marhaba kijana wangu, Napata moyo kusikia maneno ya faraja kutoka kwa mtu kama wewe, wewe ni jembe, muziki wako ni mkubwa mno, nakuona mbali sana” Rais akasema, hapo nikawa nimenyamaza nikiwa natazamana naye.

“ Tunaweza Kuketi sana” Akasema, tukakaa na punde wakatokea wahudumu wakike wawili wakiwa wamebeba visinia vyenye vinywaji kadhaa, wakaviweka vile vinywaji pale mezani kwa adabu. Kisha Rais akasema;

“ Msikilizeni Mgeni wangu anahitaji nini”

Nikaagiza, kisha wakaondoka na kutuacha pale, Rais akawa anafungua vile vinywaji na kujimiminia kwenye Bilauri, kisha akafungua moja ya Hotpot la kisasa ambalo ndani yake kulikuwa na Nyama iliyokaushwa vizuri, akaitoa ndani ya Hotpot na kuiweka kwenye sahani, akachukua kisu na kuanza kuikatakata, kitambo kidogo akasimama moja ya wale wahudumu akiwa na vinywaji na chakula nilichokuwa nimeagiza, akaviweka mezani na kunikaribisha kisha akaondoka. Tukawa tunakula huku tunazungumza;

“ Nchi hii inahitaji vijana kama wewe” Rais akasema huku akitafuna nyama, nywa!nywa!Nywa! Huku akinitazama usoni akiwa na uso wa kunitathmini. Sikumjibu neno lolote zaidi ya kuendelea kula huku mara mojamoja nikimtazama usoni.

“ Kila mtu anatamani kufanikiwa, lakini ni wachache wenye kutamani maendeleo ya nchi yetu. Wengi husema tuu midomoni kuwa wanataka nchi hii iendelee, kila anayetaka kuongoza nchi hii huimba wimbo huo, lakini hata wakichaguliwa matatizo ni yaleyale miaka nenda rudi. Ubinafsi wa kutisha umekuwa saratani katika nchi hii. Unaelewa nazungumzia nini Bwana mdogo?” Akaniuliza akiwa anaweka pembeni fupa alilokuwa amelishika,

“ Bado sijaelewa unazungumzia nini Mheshimiwa Rais, Pia nashangaa ni kwa nini unanieleza mambo haya” Nikasema,

“ Wewe sio mwanamuziki?” Akaniuliza,

“ Mimi ndiye”

“ Sasa iweje usijue kwa nini nakueleza wewe mambo haya? Nataka mguso wa kihisia uliopo kwenye muziki unaouimba uupachike katika nafsi za watu, nataka vile unavyowaimbia watu wakasisimka vivyohivyo wasisimuke wakisikia habari za maendeleo ya nchi yao, nataka uifanye kazi hiyo kwa kiwango cha ajabu kitakacholeta mapinduzi ya kifikra katika jamii yetu, hiyo ndio kazi yako” Rais Akasema, akachukua maji yaliyokuwa kwenye chupa akayafungua na kujinawisha mikono, kisha akachukua Tishu akajifuta, alafu akachukua moja ya chupa za pombe zilizokuwa pale juu ya meza na kubugia kwa mkupuo kisha akaiweka chupa mezani, akawa anaisikilizia pombe aliyoinywa jinsi inavyoshuka tumboni. Akaendelea…

“ Kuna kazi nataka nikupe”

“ Kazi gani Mheshimiwa” Nikamuuliza nikiwa nashauku,

“ Kama utaiweza kuifanya kazi hii utakuwa sehemu muhimu ya nchi hii, hautapata tuu zawadi kubwa bali utawekwa katika kumbukumbu ya historia ya nchi” Akasema huku akinitazama, nami maneno hayo yakanichukua na kunipeleka mbali sana, niliona fursa muhimu ya kuwa miongoni mwa watu wenye bahati watakaokumbukwa katika nchi hii, wakati maneno hayo yakiwa yamenichukua mbali licha ya kuwa nilikuwa tumetazamana uso kwa uso lakini macho yangu hayakuweza kumuona Mheshimiwa Rais, hii ilimaanisha nilikuwa mbali kimawazo, niliporejea nikamuona Rais akiwa ananiangalia, kisha alivyoona akili yangu imerudi eneo lile, akatabasamu, nikasema nikiwa namtazama;

“ Unamaanisha jina langu litasomwa na watu vitabuni na kwenye historia?”

Akatingisha kichwa chake huku akiwa anatabasamu, alafu akasema;

“ Ni endapo utanifanyia kazi yangu nitakayokupa”

“ Nipo tayari Mkuu, naomba uniambie ni kazi gani?” Nikasema, nami nikiwa nimemaliza kula, nikachukua maji nikajinawisha mikono alafu nikajifuta mikono kwa kutumia tishu, nilipomaliza, punde wakaja wale wahudumu wakatoa vile vyombo na kusafisha ile meza huku wakiacha chupa zenye vinywaji.

“ Miezi sita ijayo ni uchaguzi, nipo katika maandalizi ya kugombea awamu ya pili, Gstar; Siasa ni vita inayohitaji wapiganaji, silaha, mipango na mikakati itakayotufanya tubaki katika Dola. Nimejiandaa kwa muda sasa kukabiliana na washindani na mahasimu wangu na ninaendelea kufanya hivyo, ndio maana nimekuita hapa kwaajili ya kukusajili katika timu yangu ya ushindi, tunapoelekea katika uchaguzi miezi michache ijayo. Usajili huu utakuwa muhimu wenye kugusa vijana hasa wa miaka hii wanaopenda mambo ya burudani na muziki” Akanyanyua Bilauri yenye kinywaji alafu akanywa fumba mbili, kisha akabehua,

“ Mheshimiwa unajua mpaka sasa siamini unayoyazungumza, tazama mimi ni kijana kutoka familia masikini, sina uzoefu na mambo ya siasa, na wala sikuwahi kutamani kujiingiza katika mambo ya siasa…” Nikasema, lakini Rais akanikatisha akasema;

“ Gstar, hauna sababu ya kuwa na mashaka, siasa ndio maisha, huwezi sema kwamba hukuwahi kufikiri kujiingiza katika siasa, Hata muziki wenyewe ni Siasa…”

“ Muziki ni Siasa! Kivipi?” Nikajikuta niking’aka.

“ Hakuna jambo lisilo na siasa, sehemu yoyote yenye maslahi lazima siasa iwepo, Mimi nilikuwa nafuatilia sana shindano la Tanzania Got Talent, TGT. Siku ambayo umetolewa kwenye nusu fainali ile nilijua kabisa kuna njama za kisiasa zimejiingiza katika shindano lile. Wewe sio wa kutoka nusu fainali, kwa uzoefu wangu ninaweza kubashiri kuwa kuna mchezo mchafu uliosababisha wewe kujifelisha kwa makusudi ili wengine waendelee” Rais akasema, Nikajikuta nimeshikwa na butwaa nisijue niseme nini. Maneno ya Rais yalikuwa ni kweli kabisa, ingawaje hakujua kilichotokea lakini aliweza kukisia kwa karibu mchezo mchafu niliofanyiwa. Hii ilinifanya nimuone anauzoefu na michezo michafu ya hila, njama na fitna kama inayofanyika katika siasa.

“ Sikiliza nikuambie Bwana mdogo, nitakuacha uende ukatafakari, alafu utanipa jibu langu, kama ni ndio au hapana” Akasema huku akijaribu kufungasha baadhi ya vitu vyake kama vile simu vilivyokuwa pale juu ya meza.

“ Endapo nitakubali ombi lako nini kitatokea?” Nikauliza, hapo akanyanyua uso wake uliokuwa unashughulishwa na simu, akanitazama, alafu akasema;

“ Ushindi wako” Alafu akatabasamu, akaongeza,

“ Utakuwa mshindi, kwa sababu utakuwa umejiunga na timu ya ushindi”

“ Vipi nisipokubali, nini kitatokea?” Nikauliza, nikaona tabasamu lake likiyeyuka, sura yake ikawa sio yakufurahisha hata kidogo, akasema;

“ Anguko kuu!” Akanisogezea uso wake na kunikazia macho yake, kisha akanong’ona,

“ Utaanguka kama yule Lusifa uliyeimba wimbo wake siku ile ya fainali, mbona huniulizi kwa nini?”

“ Kwa sababu gani?” Nikauliza, tayari mapigo yangu ya moyo yalikuwa yameanza kupiga kwa hofu huku mwili wangu ukipata moto.

“ Kwa sababu umechagua kuanguka kwa kuwa na timu iliyoshindwa tangu zamani” Akasema kwa sauti, akaiangalia simu yake iliyokuwa imewaka kutokana na ujumbe uliokuwa umeingia.

“ Gstar, Sifikirii kijana mwerevu kama wewe utashindwa kufanya uchaguzi sahihi kwa manufaa ya taifa na nchi yako, natamani ningekuwa na muda nikueleze vile ambavyo tunahitaji muda wa kuitengeneza nchi yetu, lakini kwa sasa muda umekuwa mdogo, nafikiri tutazungumza wakati mwingine pale utakaponipa majibu yangu” Rais akasema, kisha tukaagana, wale watu walionileta wakaja kunichukua, tukapanda katika gari lilelile tulilokuja nalo, wakanirudisha nyumbani.

ITAENDELEA

Lipia Tsh 15,000/= kupata kitabu cha Kaburi la mwanamuziki Namba ya muamala 0693322300 Airtelmoney
 
KABURI LA MWANAMUZIKI EP 12
Mtunzi: Robert Heriel
0693322300


Nilifanikiwa kuingia ndani ya ile Boti pasipo kushtukiwa, nikazama upande wa ndani kimyakimya mithili ya chui awindaye. Nikajibanza kwenye moja ya kona mule ndani, nikipima utulivu wa eneo lile, palikuwa kimya taa ya rangi nyekundu ikitoa nuru hafifu katika kona ile, nikaifuata korido fupi ambayo mbele yake ulikuwepo mlango uliokuwa umefungwa, nikashika kitasa cha ule mlango kisha nikapeleka sikio mlangoni, bado kulikuwa tuli, nikaingiwa na wasiwasi isijekuwa ni mtego, nikafikiri huenda wameshaniona hivyo wameniwekea mtego, lakini nikajipa ujasiri na kupuuzia wazo hilo. Nikakitekenya kitasa cha mlango polepole, mlango ukafunguka pasipokutoa sauti, nikapokelewa na chumba kingine ambacho kilikuwa na samani kama masofa, meza ya kioo, luninga kubwa, Jokofu la milango miwili, chini palikuwa na vigae vya mbao, Luninga ilikuwa ikionyesha muziki uliokuwa ukiendelea. Nikapiga hatua kwa tahadhari huku nikiendelea kusahili chumba kile. Sikuona jambo la maana nikaufikia mlango mwingine ambao ulikuwa umefungwa, hapo nikachungulia Kupitia tundu lililokuwa usawa wa macho yangu kwenye ule mlango, nikashtuka kumuona Dora na wanaume watatu, mwanaume mmoja alikuwa anaasili ya Kiarabu, pamoja na vijana wawili, walikuwa wamekaa wakiwa wameizunguka meza fupi ya kioo Dora na yule mwanaume wa kiarabu walikuwa wamekaa upande mmoja, huku wale vijanaa wawili wakiwa wamekaa upande wa pili wa ile meza ambayo juu yake kulikuwa na begi mfano wa Briefcase,

Nilipokaza jicho langu vizuri, nikamtambua moja wa wale vijana alikuwa ni Stelini Kaboga, nilimkumbuka kwa sababu alikuwa miongoni mwa washindi wa shindano la Tanzania Got Talent tena ndiye aliyeshika nafasi ya pili, Nikawa najiuliza, Stelin anafanya nini kwenye hii Boti, anamahusiano gani na Dora, vipi huyu muarabu ni nani, sikutaka kumfahamu sana yule kijana mwingine, hata hivyo macho yangu yakatua katika lile begi, “ Kuna nini ndani ya lile begi” Nikawaza, nikaingiza mkono mfukoni nikatoa Kalamu maalumu yenye kamera kisha, nikaiweka kwenye kile kitundu na kuanza kurekodi matukio nikiwachukua wahusika bila ya wao kujua. Baada ya kuridhika kurekodi kilichokuwa kinaendelea, nikairudisha ile kalamu mfukoni. Nikachungulia tena, hapo nikawaona wakicheka, kisha yule muarabu akaweka simu sikioni wengine wakakaa kimya, akaongea kwa dakika moja kisha akakata simu. Sikuwa nawasikia walichokuwa wanazungumza.

Nikawa nakisahili kile chumba walichokuwamo, kilikuwa chumba kikubwa cha wastani, chenye dirisha moja, alafu mbele kabisa kulikuwa na mlango niliokuwa natazamana nao. Punde mlango wa kile chumba nikaona ukifunguka, alafu akatokea mwanaume ambaye nilimkumbuka ndiye aliyembeba Dora mgongoni kumpandisha kwenye Boti kule Bwejuu.. Wakanyanyuka wale vijana, Stelini akabeba lile Begi kisha wakamfuata yule Mwanaume, Mlango ukafungwa, akabaki Dora na yule mwanaume wa Kiarabu. Wakawa wanazungumza lakini sikuweza kusikia chochote. Punde nikahisi kama Boti imesimama, nikaangalia huku na huku kwenye kile chumba nilichokuwepo, nikaona dirisha lenye pazia, nikalisogelea dirisha na kuchungulia kwa nje, kulikuwa na giza, tayari usiku ulikuwa umeingia, nikaangalia saa yangu ya mkononi, ilikuwa saa nne kasoro ya usiku, eneo lile lilikuwa kama kuna kisiwa, nikatoa hadubini”binocular” mfano wa bomba la makapeni, nikaiweka kwenye jicho moja, natazama nikaona kwa mbali nyumba nzuri yenye mfano wa Hoteli hivi, ikiwa inawaka mataa yenye kupendeza, alafu kulikuwa na vijumba vizuri vya msonge visivyo na kuta vyenye mapaa ya makuti kama Uyoga, chini yake kulikuwa na vitanda vya fukweni ambavyo juu yake walikuwa wamelala watu jamii ya kizungu, wake kwa waume wakila raha na kustarehe. Nikahamisha macho yangu upande mwingine nikaona majiko ya nyama choma yakiwa na nyama zilizotengenezwa vizuri pamoja na mishikaki, wakiwepo wapishi watatu waliokuwa wamevaa Aproni nyeupe na makofia meupe ya upishi. “ Kisiwa hiki kitakuwa kinaitwaje?” Nikawa najiuliza, niliamini kuwa pale sio Zanzibar ila ni moja ya vijisiwa vilivyopo karibu na Zanzibar.

Punde nikashangaa kuona boti ndogo ikiwasili katika kile kisiwa, nikashtuka kumuona Stelini na yule kijana wakishuka kutoka kwenye ile Boti wakiwa na lile Begi, kabla sijafikiri zaidi, nikashtuka Boti niliyoipanda ikianza kuondoka. Nikajua kuwa ilisimama ili wale kina Stelini na yule kijana washuke. Nikarudi kwenye ule Mlango, nikashtuka nilipochungulia, Dora na Yule Mwarabu hawakuwepo, akili yangu ilikosa utulivu, nikafikiri huenda nao walishuka. “ Nimefanya uzembe” Nikawaaza. Nikafungua mlango kisha nikatokea kwenye kile chumba walichokuwepo Dora na Yule Muarabu, hapakuwa na jambo lolote la maana, nikasonga kwenye mlango uliokuwa ukinitazama, nikaufungua kwa tahadhari huku nikipima utulivu wa upande wa pili, kulikuwa kimya, nikafungua mlango na kupokelewa na chumba mfano wa chumba nilichotoka, lakini chumba hiki kilikuwa na milango miwili, Mlango wa kwanza ulikuwa mbele yangu ukinikabili, Mlango wa pili ulikuwa upande wa kushoto; huu ulikuwa karibu zaidi kama hatua moja kutoka pale nilipokuwa nimesimama, kabla sijaamua nini nifanye, nikasikia miguno ya mahaba ikitokea katika ule mlango wa kushoto, ilikuwa sauti ya yule muarabu pamoja na Dora, nikaufungua kwa tahadhari pasipo ya wao kujua, macho yangu yaliingiwa na haya yalipotuama kwenye miili iliyokuwa uchi ikiwa inafinyangana kwa mahaba mazito, walikuwa katika sayari nyingine, sikutaka kuangalia yasiyo nihusu, pale chini nikaona nguo zao walizokuwa wamezitelekeza ungedhani hawatozihitaji tena, Lilikuwa gauni, chupi na brazia ya Dora, pamoja na suruali, boxer na Tsheti ya yule muarabu. Akili yangu ikaniamuru nikaipekue ile Suruali, Nikainama na kuanza kutambaa kama nyoka kuzifuata zile nguo pale chini, nilipokaribia nikamsikia Dora akizidisha sauti ya miguno hali hiyo ikanifanya moyo wangu kupiga sana,nikaifikie ile Suruali, nikaishika lakini kabla sijaipekua, macho yangu yakauona mguu wa Dora ukishuka chini, nikajiviringisha upesiupesi pembeni kuelekea chini ya uvungu wa kitanda bado nikiwa na ile suruali ya Muarabu.

Nikiwa mwanzoni mwa uvungu wa kitanda, Nikauona mguu wa dora ukikanyaga chini, kisha mguu wake mwingine ukafuata, nikabinya pumzi yangu huku nikiituliza akili yangu. Dora alikuwa akilalamika kuwa amechoka, lakini yule muarabu akawa anambembeleza waendelee. Nikaipekua mifukoni, nikapata simujanja ya yule Muarabu, upesiupesi nikaipigia simu yangu iliyokuwepo nyumbani kwa kutumia namba ya muarabu, baada ya simu kuita nikakata, kisha nikaenda sehemu kwenye setting ya simu, nikachukua Imei namba ya ile simu ya muarabu, nikajitumia ujumbe wenye Imei namba, kisha nikafuta ile meseji, kisha nikafuta pia kumbukumbu ya nilivyojipigia, kabla sijairudisha simu kwenye suruali nikashangaa kuona suruali ikivutwa, upesi nikajisogeza zaidi chini ya uvungu, huku tayari nikiwa nimeshaitoa bastola yangu na kuishika mkononi.

“ Leo umenikatili sana Dora” Yule Muarabu akasema, akiwa anavaa nguo zake. Dora hakumjibu, naye alikuwa akivaa nguo.

“ Tumeshakaribia Kufika Dar, Hakikisha mipango yetu inaenda kama tulivyopanga, unafahamu tupo nje ya wakati?” Muarabu akasema,

“ Nitakujulisha kila kitu kitakachoendelea, mipango yetu inaenda sawasawa, sioni sababu ya wewe kuwa na hofu” Dora akajibu akiwa anamalizia kufunga brazia yake.

“ Simu yangu iko wapi?” Muarabu akasema, huku akijaribu kuhangaika huku na huku kuitafuta. Maneno hayo yaliamsha mapigo yangu ya moyo, nikaishika vizuri bastola tayari kwa kupambana, nilidhamiria kuwa yeyote atakayeinama kuchungulia chini ya uvungu wa kitanda; nitakipasua kichwa chake kwa risasi.

“ Labda umeiacha kwenye kile chumba cha kikao” Dora akasema akiwa tayari amevaa gauni lake. Muarabu akatoka akamuacha Dora mule chumbani, mimi nikiwa bado chini ya uvungu, nilijua kuwa endapo ataikosa simu kule kwenye chumba cha kikao kitakachofuata ni kuipigia, kwa upesi nikasogea polepole mpaka mwanzoni mwa uvungu nikamchungulia Dora, nikamuona akijitazama kwenye kioo akiwa anajiweka sawa, kabla sijafanya jambo lolote nilishtuliwa na sauti ya mlango ukifunguliwa na Muarabu akatokea huku akisema;

“ Hata kule haipo”

“ Haipo! Ngoja niipigie” Dora akasema huku akichukua simu yake kutoka kwenye Mkoba wake, akabonyeza bonyeza, kisha akaweka Louderspeaker, punde simu ya Muarabu ikawa inaita, macho yao kwa pamoja yakaangalia chini, wakaiona ikiwa karibu na nguzo ya kitanda ikiwa inaita. Nilikuwa nimeiweka pale kisha nikarudi mbali zaidi chini ya uvungu, Muarabu akaichukua simu yake pasipokujua kilichotokea.

Tayari Boti ilikuwa imefika Dar es Salaam kwenye bandari Bubu majira ya saa nane Usiku, wakatoka, nami nikatoka pasipo ya wao kuniona, nikajirusha baharini nikaanza kuogelea mpaka ufukweni. Nikayaona magari mawili meusi yakiwa yamepaki kwa mbali karibu na usawa wa ile boti, Dora akapanda gari ya mbele, huku Muarabu akipanda Gari lililokuwa nyuma, Yale magari yakaondoka yakiacha eneo lile likiwa kimya, hapo sikuwa na ujanja zaidi ya kuyasindikiza magari yale kwa macho mpaka yalipopotea katika macho yangu.

***********************************

Nikachukua Laptop yangu kisha moja kwa moja nikaingia upande wa Email, nikakuta ujumbe wa Dr. Miranda akitaka kujua nini kinaendelea na nimefikia hatua ipi katika kazi aliyokuwa amenipa, nikaijibu ile Mail, kisha nikaondoka upande wa mail, na kufungua Programu maalumu ya kudukua mawasiliano ya simu, nilipoiwasha program ile, nikachukua simu yangu ambayo ni simu ya ya kazi, nikakuta missed call moja na ujumbe wenye Imei namba, nikachukua namba ya muarabu na Imei namba yake kisha nikaiingiza kwenye ile programu maalumu ya udukuzi, alafu mfumo ukawa unajiseti, baada ya dakika tatu zilikuja taarifa za ile simu aliyokuwa anaitumia Muarabu, kisha chini yake kulikuwa na taarifa za mawasiliano yote yaliyofanyika kwa siku tisini, Simu alizopiga, simu alizopigiwa, jumbe alizotuma na alizotumiwa. Jambo moja lililonishangaza ni kuiona namba ya Osman Midevu katika mawasiliano ya yule Muarabu. Nikafungua meseji walizokuwa wametumiana. Hapo nikahisi mapigo yangu yamoyo yakiniacha, sikuamini nilichokuwa nakiona. Kwanza nilishangaa kuona kwenye zile meseji jina langu likiwepo, Niliona baadhi ya movements zangu zikiwa zinajulikana na watu hawa wabaya, mbaya zaidi Osman Midevu alikuwa anafahamu mimi ndiye niliyemtorosha Mr. Kibadeni lakini hawakujua wapi nilimpeleka,

“ Jukumu la kumtafuta Peter Mirambo linapaswa kushughulikiwa mapema zaidi kabla hajatuharibia Mipango yetu, Tumejaribu kutafuta Cv yake lakini mpaka sasa hatujaipata, hata hivyo tayari tumemuandaa Mtu maalumu wa kushughulika na Peter Mirambo, atuambie ni nani, Yupo wapi, na wapi alipompeleka Mr. Kibadeni” Ujumbe huo uliokuwa umetumwa na Osman midevu kwenda kwa Ashraf ulitingisha mishipa ya moyo wangu, akili yangu ikapoteza mhimili wake, sasa nikawa nafikiri; “ Watu hawa wanamipango gani ambayo hawataki niivuruge” Nikameza mate, “ Huyo mtu maalumu aliyepewa jukumu la kunishughulikia ni nani” Nikawaza. Jambo moja la kushukuru nimejua mambo haya mapema, “Hii kazi nilijua itakuwa ngumu sana, lakini naona mambo yanajiseti yenyewe bila kutumia nguvu kubwa”

“ Hapa kuna Osman Midevu” Nikasema, huku nikiichapisha picha ya Osman Midevu, picha ikawa inatoka kwenye Printer polepole, ilipomalizika, nikaichukua na kuitazama nikiwa nimeiweka mbele ya uso wangu. Ilikuwa picha inayomuonyesha Osman akiwa na ndevu nyingi nyeusi, kichwani akiwa na upaa, alafu mdomoni akiwa na sigara iliyokuwa inatoa moshi. Nikachukua Gundi alafu nikaigundisha kwenye Ubao uliokuwa mule chumbani kama ubao wa matangazo. Alafu nikaiseti tena Printer, ikawa inanguruma “kraa! Kraa! Kraa!” kisha ikawa inatoa picha nyingine iliyokuwa inamuonyesha Ashraf, ndiye yule muarabu, nikaitoa ile picha kwenye Printer baada ya kuchapishwa, nikaishika mkononi nikiiweka usawa wa uso. “ Kuna huyu Ashraf” Picha ilimuonnyesha Ashraf akiwa na bonge la kitambi akiwa kifuaa wazi, akiwa amevaa miwani, nywele zake zikiwa zimeanguka kwenye mabega, mashavuni akiwa na timberland, akiwa kanyoa ndevu. Alikuwa kashika mkononi Bilauri yenye Pombe. Lakini picha hii ilikuwa na mtu mwingine kwa nyuma, ambaye alikuwa msichana akiwa kavaa nguo za kuogelea akiwa kajilaza kifudifudi kwa mapozi, wote walikuwa juu ya Boti. Nikajikuta natamani kumjua binti huyu lakini ningemjuaje ikiwa ndio mara ya kwanza kumuona tena kwenye picha.

Picha ya Tatu ilikuwa inamuonyesha Dora akiwa kavaa gauni refu jekundu linaloburuzika akiwa kwenye bustani yenye maua yenye kuvutia, alikuwa naye kavaa miwani. Nikazichukua zile picha kisha nikazibandika kwa gundi kwenye ule ubao kwa kufuata picha ile ya kwanza ya Osman Midevu.

Nikatoka katika chumba cha siri ambacho ndicho nilikuwa nahifadhia vifaa na nyaraka zangu za kazi za kijasusi, chumba hiki kipo chini kabisa ya ardhi, hakuna ambaye anajua kilipochumba hiki zaidi yangu. Moja kwa moja nikaenda kuoga ili kuupa mwili nguvu mpya, na kuifanya akili yangu ipate mng’ao. Baada ya kutoka kuoga, niliamua kwenda kumtazama Mr. Kibadeni katika ile nyumba ya chini. Huko nilimkuta Mr. Kibadeni akiwa anasoma kitabu licha ya kuwa ilikuwa ni saa kumi na moja alfajiri.

“ Bwana Mkubwa, hujalala tuu” Nikasema, nikiwa nafungua mlango baada ya kubisha hodi na Mr. Kibadeni kuniruhusu kuingia ndani. Akanitazama, kisha akatoa miwani yake usoni.

“ Sikutegemea ningekukuta upo macho” Nikasema, hapo nikakaa kwenye kiti kilichokuwa mule ndani.

“ Ratiba yangu huanza alfajiri na mapema, ninaanza kwa kusali na kumshukuru Mungu kwa kuniamsha salama, kisha ninakunywa maji, alafu ratiba ya mazoezi ingefuata, lakini kutokana na hali yangu ya ugonjwa nimesitisha ratiba ya mazoezi, nimerukia ratiba ya kusoma kitabu… hii imenisaidia sana..” Mr. Kibadeni ambaye ni Wakili, na aliyewahi kuwa Jaji, lakini pia Jasusi wa kitaifa yaani ndani ya mipaka ya nchi yetu. Sumu aliyokuwa amenyweshwa ilikuwa imemchakaza vibaya mno, nywele na ngozi yake vilionekana kama vya mtu mzee lakini usingeamini kama umri wake ni miaka hamsini,

“ Nimeipenda Ratiba yako” Nikasema, huku nikijaribu kuangalia picha zilizopo katika jalada la kile kitabu.

“ Vipi kazi zinaendaje huko?” Akaniuliza,

“ Bado kugumu, ila tumepiga hatua Fulani, ingawaje ni hatua ndogo ukilinganisha na muda uliobakia” Nikasema, Hapo nikamuona Mr. Kibadeni akiingiwa na fadhaa, taarifa ile haikumfurahisha,

“ Itakuwa mimi ndiye nimekuwa sehemu ya kufeli kwa misheni hii” Akasema kwa masikitiko yaliyonifanya nimuonee huruma.

“ Hapana! Usiseme hivyo. Hatujashindwa bado, iweje useme kuwa wewe ndiye sehemu ya kufeli kwa misheni hii?” Nikazungumza kama mtu niliyekasirishwa na maneno yake.

“ Nisikie Kibadeni, tayari ninamajina mengine mawili yaliyoongezeka katika chain tunayotakiwa kuifuata mpaka kuukuta mzizi wa jambo hili, watu hawa ni muhimu na ninaamini wataifanya kazi yetu iwe rahisi” Nikasema, taarifa hiyo ikamfanya Mr. Kibadeni anitazame, nikaona angalau sura yake imepata faraja. Nikamuona kama kuna kitu anataka kukisema, lakini akasita,

“ Vipi mbona kama unataka kuzungumza jambo Fulani alafu unasita?” Nikasema nikimtazama,

“ Unakumbuka shindano la Tanzania Got Talent?” Akaniuliza, nikamtingishia kichwa kuwa ninakumbuka.

“ Unaweza kuniambia nini kilitokea mpaka Gstar hajashinda katika shindano Lile?” Akasema, nikajikuta namtazama Mr. Kibadeni kwa macho ya kutafakari, kitambo kidogo nikiwa natafakari swali lake nikamuuliza;

“ Unafikiri kuna uhusiano wowote na misheni yetu?”

“ Peter, Kwenye upelelezikitu chochote kinaweza kuhusika, mimi ni Jaji mbali na upelelezi, nimefanya kazi ya ujaji kwa miaka kadhaa, ninajua visa na mikasa mingi kuhusiana na matukio ya uhalifu. Uzoefu wangu katika fani ya Ujaji unanionyesha kuwa matukio mazuri yanayoendelea mchana yameficha ubaya, ukatili, ushenzi na mambo ya kutisha yanayoendelea usiku. Peter Mirambo najua wewe ni Kijana Msomi, tena jasusi wa kimataifa, uliyebobea katika fani ya ukachero. Fuatilia nini kilitokea mpaka Gstar akashindwa katika shindano la Tanzania Got Talent” Mr. Kibadeni akasema, maneno yake yalivuta kumbukumbu ya siku ya fainali ya Tanzania Got Talent ambapo nilimuona Gstar akiwa na mwanamke mmoja chobingo ambaye mwanamke yule nilimtambua kama Dora. Akili yangu ikanipeleka Zanzibar nilipokuwa namfukuzia Dora kule Bweju, kisha akili yangu ikasafiri miaka mingi nyuma nikikumbuka yule mwanamke ndiye Dora akimuambia Baba yangu kuwa aachane kufuatilia jambo Fulani ambalo sikufanikiwa kulijua moja kwa moja. Ni kama Mr. Kibadeni kuna kitu anakisema ambacho akili yangu inataka kukubaliana naye lakini bado sikuwa nauhakika.

“ Peter Mirambo, panga mipango yako vizuri, mchunguze Gstar mpaka ujue nini kilitokea, kwa bahati nzuri Neema Mdogo wako yupo karibu na Gstar. Unaweza anzia hapo, wakati ukiendelea na hao watu wengine waliojitokeza” Mr. Kibadeni Akasema, nikamkubalia kwa kutingisha kichwa. Kisha nikamuaga, ratiba yangu kwa siku hii ilikuwa ni kumfuatilia Dora. Akili yangu ilimuona Dora kuwa sehemu ya wale niliopewa kazi ya kuwafuatilia katika Mpango wa Operation Tonardo, uwepo wa jina la Osman Midevu kwenye simu ya Muarabu Ashraf Amur uliniongezea imani ya kuwa Dora ni miongoni mwa wahusika hatari wanaohitajika kukamatwa na kupewa adhabu kali.

ITAENDELEA

Lipia Tsh 15,000/= kupata kitabu cha Kaburi la mwanamuziki Namba ya muamala 0693322300 Airtelmoney
 
KABURI LA MWANAMUZIKI EP 13
Mtunzi: Robert Heriel
0693322300

ILIPOISHIA

Dora kuwa sehemu ya wale niliopewa kazi ya kuwafuatilia katika Mpango wa Operation Tonardo, uwepo wa jina la Osman Midevu kwenye simu ya Muarabu Ashraf Amur uliniongezea imani ya kuwa Dora ni miongoni mwa wahusika hatari wanaohitajika kukamatwa na kupewa adhabu kali.

ENDELEA
Nikarudi chumbani kwangu, nikafungua ile programu ya udukuzi iliyokuwa kwenye Laptop yangu, nikapekua mpaka nilipoipata namba ya Dora, Nikaidukua kujua yupo maeneo gani, mtandao ulikuwa unasumbua lakini hatimaye mfumo ukaleta ramani ambayo ilikuwa na kitufe chekundu kilichokua kinamwakuamwakua kwa kung’aa na kupunguza mng’ao wake, nikakuza ile ramani ili eneo lile niweze kujua lipo mtaa gani, ramani ile ilikuwa mfano wa Google map, nikashtuka kuona mfumo unaniambia simu ya Dora ipo Mbezi Beach, karibu na Little Star Medium School, “ Hii si ni nyumba ya Osman Midevu?” Nikajikuta nikiropoka kwa sauti huku nikitazama kioo cha Laptop kwa umakini na jinsi kile kitufe chekundu kwenye laptop kinavyomwakuamwakua. Sasa nilijihakikishia kuwa Dora na Osman midevu ni washirika, sikutaka kupoteza muda nikaenda kwenye kabati langu, nikachukua bastola mbili, moja nikaiweka kwenye kiuno, nyingine nikaiweka kwenye viatu. Kisha nikachukua Kamera nne ndogo sana, nikazitia kwenye mifuko ya koti nililokuwa nimelivaa, nikachukua simu maalumu ambayo niliiunganisha na mfumo wa ile laptop, baada ya kuchukua yale yote niliyoona yananifaa, nikaingia ndani ya gari langu, nikaondoka.

Nikiwa njiani nikakumbuka kuwa nina wiki mbili sijaongea wala kuonana na Neema, nikachukua simu kisha nikampigia Neema, simu haikuita sana ikapokelewa na neema akazungumza;

“ Shikamoo Kaka”

“ Marhaba Ney mwanamuziki, hujambo” Nikasema,

“ Hahah! Niko pouwa kabisa! Umeona mdogo wako kimya..”

“Nakuambia we acha tuu! Nikasema huyu Gibson kamteka Mdogo wangu, sijui kampa nini?” Nikasema, hapo pakatokea ukimya kidogo jambo ambalo likanifanya nishangae, nikawa naita;

“ Neema! Neema! Heello! Nee..” Nikasikita sauti kwa mbali kama yamajibishano baina ya Neema na mwanaume mwingine hivi, lakini sikuweza kusikia vizuri, kisha simu ikakatika. “Heeh! Ajabu hii” Nikasema huku nikiwa natazama kioo cha simu, bado naendesha gari nikitokea nyumbani Goba kuelekea Mbezi Beach. Nilikuwa naendesha gari kwa mwendo mdogo, nikaipigia tena namba ya Neema. “ Namba unayoipigia kwa sasa haipatikani tafadhali jaribu tena Baadaye” taarifa hiyo ilikaribisha hofu moyoni mwangu, “Neema yupo wapi? Haikuwa sauti ya Gibson. Naifahamu sauti yake, Neema atakuwa yupo na nani? Kwa nini simu ikatike, alafu aizime. Tangu namchukua Neema Kumlea, haijawahi kutokea jambo kama hili” Nikawa nawaza tayari nikiwa nimefika Mbezi shule. Akili yangu iliniambia kuwa kuna jambo haliko sawa, “Neema na Gibson wamegombana?” Nikawaza, lakini sikutaka kuingilia mambo ya mahusiano ya Mdogo wangu Neema.

Baada ya kufika Bagamoyo Road nikakatisha upande wa Kulia, ulipo muelekeo wa Mjini, hapo nikatembea kwa dakika moja nikaikuta ile njia iendayo Little Star Medium School ambayo ipo mkono wa kushoto, nikakatisha kuifuata. Ilikuwa majira ya saa mojamoja za asubuhi, pilikapilika za watu ndio zilikuwa zinachanganya watu wakikimbia kwenda makazini. Nikaegesha gari langu Mita arobaini kabla ya kuifikia nyumba ya Osman Midevu ambapo Geti la nyumba yake nilikuwa naliona kwa mbele. Nikiwa ndani ya gari, nikaitoa ile simu maalumu niliyoiunganisha na mfumo wa Laptop kule nyumbani, nikaona kwenye ile simu bado kitufe chekundu kilikuwa kinamwekua kwenye nyumba ya Osman Midevu, jambo hili likanipa moyo. Nilikuwa makini kuangalia wapitanjia waliokuwa wanatumia ile barabara ambao wengi walikuwa Wasaidizi wa kazi za ndani wakiwa wanawasindikiza watoto wadogo wenye sare kwenda shuleni, mara chache yalipita magari ya watu binafsi ambao bila shaka walikuwa wakienda katika shughuli zao. Lisaa limoja liliisha, utulivu ukaongezeka eneo lile, hapakuwa tena na watoto waliokuwa wakienda au kupelekwa shule, utulivu ule ulinivutia kufanya jambo, nikataka nishuke ili niende katika ile nyumba ya Osman, nikaiseti Saa yangu ya mkononi, kisha nikaiunganisha na kifaa maalumu kilichokuwa ndani ya gari. Kabla sijashuka, nikashtuka kuona geti la nyumba ya Osman likifunguliwa. Nikaitoa upesiupesi bastola yangu mafichoni na kuiweka juu ya mapaja, nikamuona kijana mmoja hivi mrefu wa kati mwenye, maji ya kunde aliyevaa kapero akitoka mule ndani, akasimama mbele ya lile geti akatazama upande wa ile shule ya Little Star, kisha akageuka upande nilipokuwa nimeegesha gari, hapo nikajirudisha chini polepole kwa kuteleza na mgongo, nikamuona akilitazama gari langu kana kwamba anashangaa uwepo wake eneo lile. Kitambo kidogo akalipuuzia, akageuka na kutembea upande wa ile shule, nikamuona akiingia kwenye kiduka Fulani kilichokuwa eneo la ile shule, “Hii ni nafasi” Nikawaza huku nikichukua upesiupesi Kofia iliyokuwa Viti vya nyuma vya gari, nikavaa alafu nikachukua Gloves nyeusi za mikononi nikazivaa, Kisha nikashuka upesiupesi, bastola yangu nikiwa nimeificha kiuoni, shati nikiwa nimelichomoa likiwa linaning’inia. Macho yangu yalikuwa makini kumtazama yule kijana aliyekuwa anahudumiwa kule dukani, kwa bahati Yule Kijana hakuwa amefunga Geti dogo alipotoka, nikalikagua lile Geti upesiupesi, nikaona Kamera, lakini sikuijali sana, Kofia niliyokuwa nimeivaa ilizuia kwa kiasi kikubwa uso wangu. Nikachungulia ndani, hapakuwa na mtu isipokuwa uwanja mkubwa wenye vigae, upande wa kulia kulikuwa na kijumba cha mlinzi ambacho nacho hakikuwa na mtu ila mlango wake ulikuwa wazi, nje pakiwa na kiti pamoja na Radio iliyokuwa inaongea. Nikajua yule kijana ndiye alikuwa pale.

Mbele kabisa kwenye ule uwanja wenye Vigae yalikuwepo magari mawili, Moja lilikuwa na rangi jeusi, Benzi. Jingine lilikuwa Ni landCrusser V8 yenye rangi kama udongo hivi. Bado nilikuwa nimesimama katikati ya lile Geti nikiwa nusu ndani nusu nje. Lilikuwa jumba kubwa sana la kifahari, lenye ghorofa mbili, ubavu wa kulia kutokea nilipokuwa nimesimama kulikuwa na miti mizuri ya maua, huku chini ya ile miti kukiwa na vibustani vya kupendeza, katika kingo za lile jumba kulikuwa na Mawe yaliyoundwa kiufundi yakiwa yanarusha maji kumwagilia bustani zilizokuwa pembezoni mwa kuta za lile jumba. Ubavu wa kushoto wa ile nyumba ambao uliangaliana na kijumba cha mlinzi, kulikuwa na nafasi kama mfano wa barabara inayoelekea upande wa nyuma wa lile jumba. Nilipotazama mbele kabisa kuifuata nafasi hiyo kama barabara macho yangu yakapokelewa na magari mengine mawili yaliyokuwa ndani ya kichanja maalum cha maegesho ya magari. Nikasonga upande wa Kulia, nikayapita yale magari mawili yaliyokuwa mbele ya lile jumba, kisha nikapita ubavu wa kushoto wa lile jumba wenye mitimiti na bustani za maua, nikapanda juu ya mti mmoja na kuipachika Kamera ya Siri ambayo ilikuwa inaangalia upande wa Getini, nikiwa juu ya mti nikamuona yule kijana akiwa amerudi akiwa kabeba Soda ya kopo “Takeaway” na maandazi, akaviweka kwenye kile kiti, kisha akaingia ndani ya kile kijumba cha mlinzi, baada ya kitambo akatoka akaenda kukaa kwenye kiti. Nikaachana naye.

Nikazunguka upande wa nyuma wa lile jumba, nikiwa natembea kwa tahadhari mkono mmoja ukiwa eneo la kiunoni ilipokuwa Bastola yangu, nikiufuata ukuta wa jumba lile. Upande wa nyuma nikapokelewa na Mandhari ya kuvurtia zaidi, kulikuwa na Bustani nzuri yenye kijani cha ajabu, Bwawa la kuogelea, pembeni ya lile bwawa kulikuwa na ndege wawili wazuri wenye rangi nyeupe. Nilipoona hali ipo shwari nikasonga upande wa kushoto kuufuata ukuta wa lile jumba, hapo nikakutana na Mlango, nikaweka sikio moja kwenye mlango kupima utulivu, kulikuwa kimya, nikakitekenya kitasa, mlango ulikuwa umefungwa, nikatoa funguo Malaya kisha nikafungua ule mlango polepole pasipokutoa sauti, nikapokelewa na korido ambayo kwenye kuta zake upande huu na upande huu kila baada ya hatua tano chini kabisa kulikuwa kumepachikwa taa zenye mvuto wa kipekee ambazo zilitoa nuru isiyong’aa sana na kufanya korido ile iwe na nuru hafifu, hapo nikaichomoa Bastola yangu, mazingira yale hayakuwa rafiki sana, na lolote linaweza kutokea. Bado kulikuwa kimya mno hali hiyo ilinifanya niingiwe na wasiwasi. Nikawa napiga hatua polepole kwa tahadhari, sasa pumzi yangu ilianza kuleta kiherehere na mapigo ya moyo yakawa yananisaliti, hata hivyo nilifundishwa kudhibiti pumzi na mapigo ya moyo niwapo katika mazingira kama yale.

“ Ukimya huu sio bure” Nikawaza, nikakumbuka jinsi yule kijana Mlinzi alivyokuwa ametoka nje ya Geti, nikahisi huenda ule ulikuwa ni mtego, Kabla akili yangu haijaenda mbali zaidi. Saa yangu ya mkononi ikawa inatetema, hii ilimaanisha kunamtu ameligusa gari langu kule nje. Akili yangu ikakosa utulivu, nikabonyeza ile Saa yangu, hapo nikaona Kupitia kioo cha Saa, mwanaume mmoja akiwa anajaribu kulifungua gari langu, nikiwa bado namtazama Mwanaume yule ambaye sikuweza kumuona uso wake kutokana na teknolojia ya saa yangu ya kijasusi, ambayo ilitumia zaidi Body Sensor, na wala sio kuwa ilikuwa imeunganishwa na Kamera za ndni ya gari. Natazama Mbele yangu akatokea mwanaume mmoja akiwa kanishikia Bunduki, nami nikawa nimemshikia bastola yangu tukiwa tunatazamana huku nuru ikiwa ni hafifu kutokana na taa za ile korido, nikiwa natafakari chakufanya, nikshtushwa na mwanaume mwingine akitokea nyuma ya yule mwanaume wa kwanza akiwa naye anabastola, akifuatana na Osman Midevu, Osman hakuwa na Silaha, aliponiona akatabasamu, na kabla tabasamu lake halijaisha nyuma yake akatokea mwanamke, ndiye Dora akiwa anakikombe cha kahawa, nikawa napiga hatua polepole kurudi nyuma nikiwa nimewanyooshea bastola, nikiwatazama kwa umakini kuchunga mienendo yao. Kabla sijapiga hatua ya nne nyuma nikashtuka kusikia sauti kutokea nyuma yangu ikaniambia “ Tulia hivyohivyo, ukijitingisha nitamwaga ubongo wako chini” Sauti ile ikanifanya ninyoshe mikono juu kujisalimisha.

“ Weka silaha yako chini, ujanja wowote utakuwa tiketi yako ya kuzimu” Sauti ileile isiyo na mzaha kutokea nyuma ikaniamrisha, nikatazamana na Dora, kisha Osman alafu nikaliona tabasamu la Kifedhuli likichanua katika uso wake. Nikaitupa silaha chini, hapohapo nikahisi kichwa kizito, nikaanguka chini, giza likafunika macho yangu, sikujua nini kiliendelea baada ya hapo.

*****************************************
ITAENDELEA

Lipia Tsh 15,000/= kupata kitabu cha Kaburi la mwanamuziki Namba ya muamala 0693322300 Airtelmoney
 
Back
Top Bottom