WANASHERIA MNATUVURUGA HUYU KAANDIKA
TLS wamepotosha umma
Mwongozo wa TLS uliotolewa Machi 19, 2021 nimeusoma kwa umakini, ila una sehemu zifuatazo zinazofanya baadhi ya wanasheria kushindwa kesi Mahakamani na katika hili wamejielekeza vibaya kama ifuatavyo:-
1. TLS wanazungumzia cheo cha Raisi, Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania haina cheo cha aina hii hivyo ushauri huu ni batili tangu mwanzo (null and void abi initio). Cheo kilichopo kwenye Katiba ni Rais .
2. Ningekuwa mahakamani kesi ingeishia hapo baada ya hoja ya kwanza, ila kwa kuwa nalenga kuielimisha jamii, najielekeza katika hoja ya pili. Ibara ya 37 (5) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania (1977) katika maneno msingi inasema: "Basi Makamu wa Rais ataapishwa na atakuwa Rais katika muda uliobaki katika kipindi cha miaka mitano na kwa masharti yaliyoelekezwa katika Ibara ya 40" Mzizi wa sentensi hii ni muda uliobaki (kumalizia) kipindi alichokuwa anatumikia chini ya Rais aliyepoteza madaraka ikabidi yeye ashike madaraka kumalizia. Hii ina maana anaendeleza aliyoyakuta si kuanzisha mapya (ingawa hakuna kifungu kinachomzuia kufanya manadiliko kwa utashi wake).
3. Kwamba alipopanda wadhifa kuwa Rais ameapa hakuendelea na kiapo cha awali cha Makamu wa Rais, hii ni hoja dhaifu kwani hizi ni nafasi mbili tofauti, hivyo kuapa ni lazima kwani anashika wadhifa mpya.
4. Kwamba Waziri Mkuu na mawaziri waliapa mbele ya Rais aliyepoteza madaraka, pia ni hoja dhaifu. Hawa hawakuapa kwa mtu (Dr. Magufuli), bali waliapa kwa taasisi (Rais). Hoja ya TLS ilikuwa sahihi mpaka mwaka 1995 mawaziri walipokuwa wanaapa kumtii Rais wa Jamhuri ya Muungano, lakini baada ya Dr. Masumbuko Lamwai kuipiga ngwala Serikali bungeni, tangu wakati huo viapo vyote wakiwamo mawaziri wanaapa "kuitii Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na kumshauri kwa uadilifu Rais (taasisi) wa JMT". Hivyo, hoja ya kula kiapo mbele ya Rais inafia hapo kwani taasisi ya urais inaendelea kuwa ileile baada ya Makamu wa Rais kuapa kuwa Rais. Kwa hoja hii ibara ya 51(2) Kuteua Waziri Mkuu ndani ya siku 14, Ibara ya 55(1) ya kuteua mawaziri, Ibara ya 56 ya Waziri na Naibu Waziri kuapa mbele ya Rais... kwa ufafanuzi huu zinapoteza sifa ya kurejewa. Si hoja tena.
6. Hoja nyingine iliyojengwa kwenye hoja ya nguvu, badala ya nguvu ya hoja ni ile TLS waliyoiegemeza kwenye dhana ya Baraza kuvunjika baada ya Waziri Mkuu kupoteza madaraka, ambapo wametumia maneno: "kwa sababu nyingine yoyote ile." Maneno haya naamini labda yapo kwenye Katiba yao, ila Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania moja ya sababu ilizozitaja za Waziri Mkuu kupoteza madaraka inayoelekea kufanana na hiyo wanayotaka kulazimisha iwe sehemu ya Katiba yetu, ipo katika Ibara ya 51(3)(e), inayosema: "Atakapoacha kushika kiti cha Waziri Mkuu kwa mujibu wa masharti mengineyo ya Katiba hii." Nimesoma Ibara zote 152 za Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania (1977), sikuona sehemu ya kifo cha Rais kilipotajwa kama sharti la Waziri Mkuu kupoteza madaraka yake. Pia nitafurahi TLS wakinionyesha ibara yenye maneno "kwa sababu yoyote ile" wanayoyatumia kuhalalisha hoja ya nguvu ya Waziri Mkuu kupoteza madaraka na hivyo Baraza kuvunjika.
Kimsingi, sitaki kuamini kwamba TLS hawakupata muda wa kuisoma Katiba au wana nia ya ziada dhidi ya baadhi ya wateule ndani ya Baraza la sasa au wamejielekeza vibaya, ila kuna jambo.
Kabla sijatoa ufafanuzi kupitia TBC juu ya utaratibu kwamba hakuna uchaguzi bali Makamu wa Rais anaapishwa kuwa Rais, wapo watu waliokuwa wameanza kupiga jaramba wakiamini miezi 3 ijayo tungeingia katika uchaguzi. Sitashangaa kuwa inawezekana kuna wanufaika wa ushauri kama huu wa TLS wanaoamini Baraza likivunjwa, basi wao watapata fursa.
Mwisho, baada ya ufafanuzi huo nasema Katiba haiweki sharti la kuteua upya Waziri Mkuu au Mawaziri, japo Katiba hii hii haimfungi mikono Rais Samia Suluhu Hassan kufanya uteuzi kadri atakavyoona inafaa.
Nasubiri majibu kutoka TLS yenye nguvu ya hoja kama wanayo.
Deodatus Balile
Mhariri Mtendaji,
Gazeti la Uchunguzi JAMHURI
19/03/2021