Baada ya Diamond kusaini mkataba na record label ya Universal Music Group (UMG), baadhi ya mambo yameshaanza kubadilika, na baadhi ya mashabiki, hususan wale wa Tanzania hawana furaha.
Of course, kuna mjadala mwingi kuhusiana na ‘kusainishwa kwake’ hasa kwasababu aliwahi kudai kuwa hawezi kuwa chini ya label, labda kama itakuwa ni partnership.
Hata hivyo kwenye mahojiano yake na Clouds FM, Novemba mwaka jana, Diamond alisema Universal Music Group walitoa dola milioni 1 (takriban shilingi bilioni 2.2 za Tanzania) kumsainisha mkataba wa kusambaza nyimbo za wasanii wa label ya Diamond Platnumz, WCB. Naye meneja wake, Sallam aliiambia Bongo5 kuwa mkataba huo ulisainiwa tangu July mwaka jana, lakini tangazo rasmi limetolewa, Alhamis hii, Feb 2.
Kwakuwa sasa UMG imechukua usukani rasmi kwa kusambaza nyimbo za Diamond, mashabiki wake wanapaswa kutambua kuwa, baadhi ya mambo yatabadilika. Kwa sasa nyimbo zake zitakuwa na mlolongo mrefu kutoka na sio kama zamani ‘click link kwenye bio kuona video yangu Youtube.’ Mfano sasa, Marry You aliyomshirikisha Ne-Yo, ilianza kwa kuchezwa Trace TV, ambayo tunajua kuwa inapatikana DSTV pekee, hiyo ina maana kuwa hadi sasa ni Watanzania wachache wamekwishaiona.
Kwasababu lengo la UMG ni kumpeleka Diamond mbali zaidi kimataifa, Marry You unakuwa wimbo wake wa kwanza kuwekwa kwenye platform za kustream muziki kwa kulipia, ambako shabiki wa kawaida wa Masasi au Njombe, nyingi hawajawahi kuzisikia, lakini yule wa Stockholm, Sweden ndio maeneo yao ya kujidai, tayari anaufurahia wimbo huo.
Bila shaka, lengo la UMG sasa ni kumpatia Diamond mashabiki wapya wa kimataifa kumuongezea wigo wa kupata fedha za kigeni na hivyo kukuza mapato yake ambayo yataisaidia pia UMG kurudisha gharama zake za uwekezaji kwa kumsainisha, sababu hii ni biashara, sio charity. Kwa mtazamo huo, kipaumbele cha UMG kwa kazi za Diamond, sasa kitakuwa si Tanzania tu, bali kimataifa zaidi, huo ni ukweli ambao mashabiki wanapaswa kuutambua.