Ndugu gombe sugu; naomba uniite "mwanakijiji" tu au kama wengine wanavyoita "MM"; sistahili kuitwa uheshimiwa kwa sababu siamini katika "uheshimiwa" kama hadhi au sifa ambayo wengine wanayo na wengine hawana. Ni muumini wa "Kila binadamu anastahili heshima ya kutambuliwa na kuthaminiwa utu wake". Nashukuru.
Maswali yako uliyoanza nayo hapo juu kufikia hapa chini nimeyasoma na ninashukuru kwa kuniuliza. Majibu yangu bado yamebaki yale yale. Ila nitaangalia haya mambo kidogo hapa chini.
hivi ndugu yangu wewe binafsi kwa mtazamo wako unakubaliana na mawazo ya baadhi ya wanajamvi hapa,watanzania kadhaa pamoja na Serikali hapo kuwa Waislam wana matatizo na dhiki kadhaa za kihistoria na inalazim Serikali iwatengee sikio japo la upande mmoja kujua kinachowasibu?
Mimi sikubaliani na mawazo au nadharia kuwa Waislamu wana 'matatizo na dhiki kadhaa za kihistoria" hasa kama unamaanisha kuwa dhiki hizo za kihistoria zinaikumba jamii ya "kiislamu" peke yake. Hii ni tofauti yangu kubwa labda na baadhi ya watu; naamini matatizo ya kihistoria ambayo yalisababishwa na ukoloni yalikuta jamii nyingi za Watanganyika na hilo halikujali dini au imani zao. Matokeo yake utayaona ni yale yale. Ukifika Usafwa utakutana na matatizo yale yale ambayo unayaona Mkuranga; ukienda Ndala utakutana na matatizo yale yale unayoyaona Masasi; ukienda Bunda utakutana na matatizo yale yale ambayo unaweza kuyaona Mtwara. Matatizo ambayo wananchi wetu wanakabiliwa nayo hayana dini. Kudai kuwa matatizo haya yamejali sana dini kiasi kwamba kundi moja la watu (Waislamu) wadai upendeleo wa pekee ni kutokuwa wa kweli wa historia.
Nitakupa mfano mmoja mzuri ambao hatujaujadili sana hapa. Kabila kubwa Tanzania ni Wasukuma/Wanyamwezi. Wanaishi katika mikoa minne (Mwanza, Shinyanga, Geita na Tabora). Wasukuma peke yao wanakadiriwa kuwa karibu milioni 5.5 (sawa na kama asilimia 15 hivi ya Watanzania wote); ukijumlisha na Wanyamwezi (ambao ni milioni 1.5) utaona kuwa Wasukuma ni wengi kweli kweli.
Kulinganisha nao:
Wachagga - milioni 2 hivi
Nyakyusa - milioni 1 hivi (bila kuhesabu wale wa Malawi)
Haya - milioni 1.5 hivi
Utaona kwa haraka tu kuwa makabila ambayo yamepata nafasi kubwa zaidi (katika elimu, ajira n.k) katika Tanzania tangu ukoloni (haya matatu) hayafikii kwa ujumla wake idadi ya watu wa kabila moja - Wasukuma. Tulinganishe tena kidogo:
Wazaramo - 700,000 hivi
Ndengereko - 150,000
Zigua -580,000
(makabila haya matatu yamepokea Uislamu kwa wingi; karibu asilimia 90 ya watu wake ni Waislamu).
Wasukuma hata hivyo Wakristu ni asilimia kama 43 hivi na Imani za jadi asilimia 42 waliobakia ni Waislamu.
Lakini tuangalie makabila mengine ambayo yana Wakristu wengi na tuone nayo kama yako yanawakilishwa vizuri katika utawala na mafanikio ya nchi:
Wahehe wako kama milioni 1.2 na Wakristu ni kama asilimia 90 hivi
Wagogo milioni 2 hivi asilimia 70 Wakristu
Wamatengo 300,000 na asilimia 80 Wakristu.
Sasa namba hizi
(unaweza kuangalia makabila mengine hapa) ni lazima zikufanye ujiulize maswali:
a. Ni kweli Wakristu wanapendelewa? Hili lingeonekana kwa jamii zote za Kikristu kuwa na mafanikio kuliko zile za Kiislamu.
b. Je jamii za jadi (zenye waamini wengi wa jadi kuliko wa dini zetu mbili kubwa) zimefanikiwa kiasi gani kulinganisha na Waislamu (ni lazima uwe na sehemu ya kucompare)? Wasafwa wana tofauti gani na Wazaramo?
c. Wasukuma kwa kuwa ndio kabila kubwa nchini kwanini hawana elimu sana kama jamii na hawaonekani katika nafasi mbalimbali za uongozi nchini (underrepresented)?
Kusema Waislamu ndio pekee wenye matatizo na kuwa matatizo yao yamesababishwa na wao kuwa Waislamu SI KWELI.
Sijui kama unakubaliana na ile kauli ya Bwana W. Mkapa ya kuthibitisha na kuwa wengi kati ya Waislam wana matatizo na dhiki zilizosababishwa na kurithiwa toka kwa wakoloni?
Kama nilivyosema hapo juu sikubaliani na maono hayo kwani hayana msingi wa kihistoria tukichukulia all the other factors into consideration.
Unakubaliana na mimi kuwa Sheikh Mohammed Said alipoandika Historia ya Tanu/Tanganyika, hakuwa na madhumuni potofu au kukusudia uchochezi kama mnavyodai bali labda ni khitilafu kiduchu na dhahama tu za kitaaluma na kiuandishi na pia hakukusudia nia dhalili dhidi ya nchi yake na wananchi wenzie.
Sikubaliani na wewe kabisa. Nimemsoma Mohammed Said vya kutosha na ninaifahamu historia ya Tanzania vizuri tu. Mohammed Said aliandika kama Mwanaharakati wa Kiislamu; lengo lake (pamoja na wale wengine wa WARSHA) ilikuwa ni kuwapandikizia Waislamu hisia ya kuwa duni na kujihisi wanadhulumiwa. Hivyo kufikia lengo hilo ameandika historia upya, akipotosha matukio mbalimbali na akiweka hisia zake juu kuliko ukweli wa historia.
Nashukuru, na niwie radhi kama kuna masuala nimekuuliza tena. Najaribu kuangalia kama mpaka hapa mnakasha ulipofikia labda kuna majambo umeyaona na umepata kubadili fikra zako japo kiduchu.
Ahsanta.
Kwa kweli baada ya kusoma sana sijaona chochote ambacho Mohamme Said au mtu mwingine mwenye kutetea histohisia hii amesema kuweza kunishawishi fikra zangu. Nilichokiona ni kuwa tuna tatizo kubwa zaidi katika kufikiria, kutafuta ukweli, kupima ukweli na kuutetea. Kimsingi nimeamini kuwa wapo kati yetu ambao wanaogopa ukweli kwa sababu utawaondoa katika kile walichokiamini au kile ambacho wanaamini ni kweli. Kuogopa ukweli siyo sawasawa na kuujua ukweli. Ukweli unafungua. Mohammed Said ameficha historia, kapotosha matukio na kwa makusudi kabisa amechafua na kufunisha mchango wa Baba wa Taifa Mwalimu Nyerere kwa nchi yake kiasi kwamba wapo baadhi ya watu wakiamini simulizi la Mohammed Said wanamuona Nyerere kama adui wa Waislamu na wanamlaani huko kaburini aliko.