Uhusiano wangu kimapenzi na "Hamida"

Uhusiano wangu kimapenzi na "Hamida"

SEHEMU YA SITA
******************

Nilikaa kwa mzee Katibu Kata hadi saa tatu usiku, hakuwa katika afya nzuri, malaria ilikuwa inamsumbua na alikuwa amemeza klorokwin (Chloroquine), dawa chungu kama muarobaini lakini pia zilikuwa zinamuwasha...

Tuliongea mambo mengi, lakini suala langu la kumchumbia Hamida lilichukuwa nafasi kubwa.

Aliniambia kuwa siwezi kufanikiwa kumpata binti Burhani, na sababu zake niliona zina mashiko. Kwamba, kwanza mimi ni mkristo, siwezi kufunga ndoa na binti Burhani ambaye baba yake ni mtu wa msimamo katika dini yake. Pia aliniambia kuwa Waarabu wana utaratibu wa kuoana wao kwa wao kama ilivyo kwa Wahindi. Ni nadra sana kukuta ndoa iliyo tofauti na hivyo, aliniambia.

Pia alinishauri kama kweli nimedhamiria basi kwanza kabisa nianze kumteka kimapenzi Hamida; Hamida ambaye hata hajui kwamba James 'amemzimikia'

Yaani nijitahidi nipate nafasi ya kuongea naye ili ajue nia yangu, nijue kama atanikubali ama la. Kisha ndio nianze mashambulizi kupitia Mshenga. Lakini pia alinishauri nijiweke sawa kisaikolojia na kuanza kufikiria kubadili dini.

Nilirudi home nikiwa na ahueni ya fikra, nilala vizuri usiku huo huku nikiwaza mambo mengi hususani pa kuanzia 'kumteka' Hamida kimapenzi.

Kwa wakati huo tayari nilikuwa mbobezi katika kufanya ngono na suala zima la mahaba, nikawaza sijui nitumie mbinu kama ya kwenye kitabu cha "Captive Bride"? Mwandishi Johanna Lindesy alisimulia kisa cha kusisimua sana katika kitabu hicho na harakati za kumteka umpendaye kisha atakupenda baadaye... [emoji23]

Wakati huo tayari nilikuwa nimeshasoma vitabu vingi vya falsafa ya mapenzi nk, nilikuwa najuwa nama ya kummiliki nimpendaye ipasavyo, sikuwa na hofu juu ya namna ya kuonesha mahaba yangu kwa Hamida, bali hofu ilikuwa namna ya kupata wasaa naye na kuanza kueleza 'neno la mapenzi'

Nilijimwagia maji (kuoga) na kulala huku nikiwa na ahueni.
*******

Kulipokucha kama kawaida ya siku za kazi huwa nawahi kazini kwa ajili ya kulisukuma gurudumu la maendeleo...

Nilifanya kazi nikiwa mwenye furaha sana kuliko mwanzo wa mwisho wa juma lililopita.

Baada ya kutoka kazini nilienda moja kwa moja hadi Magomeni Mwembe chai ambapo kulikuwa na kinyozi mzuri chini ya mwembe. (Alikuwa anatumia mikasi misafi, vitambaa vyake ni visafi na pia ananijulia kuninyoa)

Wakati huo nilikuwa nafuga nywele nyingi (afro / mchicha), hivyo nilienda kuziweka vizuri.

Baada ya kutoka hapo nilienda nyumbani kuoga na kubadili mavazi, chini nilivaa raba mtoni (raba toka Ulaya), nikavaa jeans ya bluu iliyokolea ya Levi Straus 501, mkanda mweusi wenye backle kubwa, nikavaa shati langu la picha ya ndege (a.k.a. Juliana), ndani nilikuwa nimetanguliza vest ya matobo matobo madogo (ilikiwa fasheni), mkonono nikavaa saa yangu Motima, nywele zangu afro nikazichana baada ya kuzipaka mafuta safi (hairtonic) Nilijipulizia pafyumu pendwa 'YU for Men', kisha nikatoka kuelekea Magomeni mapipa, pale yanapogeuzia Ikarus kwa pembeni kulikuwa na studio ya kupigia picha iitwayo Africa Studio.

Nilipiga picha tatu matata sana, moja nikiwa nimekaa kwenye kiti, nyingine nimesimama pembeni ya stuli ndefu ya studio na ya mwisho ilikuwa ni passport size. "Kwa hizi picha, Hamida hachomoi", niliwaza.

Wakati huo ilibidi kusubiri picha kwa siku nne ama tano hivi ili ziwe tayari. Hivyo sikukaa sana pale nikaelekea Shibam kwenye kijiwe cha Keram.

Niliwakuta watu wengi kama kawaida, niliwasalimia (vizuri safari hii), nikakaribishwa, kawaida yangu nikifika pale lazima niwapige round moja kwanza huku burudani zinaendelea...

Walikuwa wananipenda sana kwa hilo lakini pia kwa nafasi yangu RTC.

Wakati burudani, mabishano / mijadala inaendelea, nikaenda jirani na mzee Burhan (alikuwa hakosi hapo kila baada ya swala ya alasir) na kuanza kumdodosa...

" Mzee, nimeyafikiria maneno yako ya siku ile nimeona leo nije unipe muongozo" nilimuambia.

"Maneno gani tena?" Aliuliza.

Nikamkumbusha jinsi nilivyokosea kusalimia na kusema "salama leko" badala ya assalaam aleikum"

Akasemaa "ahaaaaa", kisha akacheka...

"Sasa mzee nafanyaje ili niwe mwislamu?" Nilimuuliza.

"Hebu twende nyumbani tukaongee vizuri" alisema huku akiwa amefurahi na kuanza kuinuka"

Moyoni nikasema "yes!, mwanzo huoo!

Kwakuwa hapakuwa mbali na hapo, batavuz yangu niliiacha nimeifunga vizuri, tukaanza kuelekea kwa nyumbani kwa mzee Burhan taratiib huku tukiongea mawili matatu.

Tukiwa njiani alinifundisha maana ya assalaam aleikum. Akaniambia kuwa maana yake ni 'amani iwe nanyi', na wa aleikum salaam maana yake ni ' nanyi iwe kwenu' yani hiyo amani. Nilifurahi sana kufahamu maana ya salamu hiyo na majibu yake.

Nikamwambia kuwa sisi waroma tunasalimiana 'tumsifu Yesu kristu' na tunajibu kwa kusema milele amina. Akaniambia kuwa anajuwa kwa kuwa kuna wakati aliwahi kwenda pale Moroco Hotel, Kanisani na kuwasikia waumini wakisalimiana hivyo mara kwa mara.

Tukafika kwake, akausukuma mlango kwa ndani bila hodi, ila akaniambia karibu sana kijana. Nikasema starehe.

"Karibu varandani" alisema huku akivua sandals zake na kutambuka (kuruka) kizingiti kuingia sebuleni.

Nami nikavua raba zangu kisha nikaingia. Mle ndani tuliwakuta watu watano wakiongea, alikuwepo yule mama Mwarabu, mama wa kiafrika, kijana wa makamo wa kiarabu, kijana mwingine wa kiafrika na mtoto mdogo (wa umri wa miaka mitano hivi)

Mzee Burhan alianza...

"Karibu sana James, huyu hapa ni mke wangu, maarufu kama mama Warda, yule pale ni mdogo wake (nilikuja kujuwa baadaye kuwa alikuwa msaidizi wa kazi waliyeishinaye kwa miaka mingi sana), yule pale ni mwanangu anaitwa Yasir na rafiki yake..."

"Anaitwa Abdul" alidakia Yasir.

"Nashukuru kuwafahamu" nilijibu

"Eeee na huyu anaitwa James..." Mzee Burhani alimalizia akinioneshea mimi kidole....

"Tunamfahamu" walijibu wale vijana (Yasir na Abdul) kwa pamoja.

"Samahani, naomba mtupishe tuna maongezi nyeti kidogo" alisema mzee Burahani.
Yasir na Abdul walitoka nje kabisa ya nyumba, mama Warda na mdogo wake wakaenda chumba kingine...

Mzee akachukuwa Radio cassete recorder (Memory Q), akasogeza nilipokaa akaweka juu ya stuli kisha akaniambia kuwa atarikodi mazungumzo yetu ili awe na ushahidi...

"Hamidaaa" aliita yule mzee Burhani

"Abee baba" nilisikia sauti hafifu kisha nikasikia mlango unafunguliwa na hatua za kivivu zikawa zinasikika kuja upande wa sebuleni.

"Abee baba" alirudia kuitikia, safari hii sauti ilikuwa kama ile ya siku ya kwanza kumuona.

"Katuletee soda" Mzee Burhani alimuambia...

Kabla hajaondoka nikaijikuta nasema "Mie niletee togwa kama lipo"

Hamida hakusena neno, akaondoka...

"Huyu ni binti yangu wa mwisho, anaitwa Hamida, ndio ametoka college juzi juzi, alikuwa akisomea mambo ya upishi." Aliendelea mzee Burhani.

"Nilikuwa watoto watano, Watatu wakike na wawili wakiume, dada yao mkubwa anaitwa Warda, kisha amefuatia Sabra halafu Yasir na Hamida ndio kitinda mimba. Mmoja alifariki. Huyo mtoto mdogo unayemuona ni mjukuu, mtoto wa binti yangu wa kwanza Warda" alinifahamisha.

Mara Hamida akaingia na chupa moja ya fanta na bilauli tatu.

Akaifungua ile soda na kumimina kwenye bilauli ndogo ambayo alimpa yule mtoto.

"Nadya, usimwage mwage eee!" Sauti nyororo ya Hamida ilisikika.

Kisha akamimina soda iliyobakia kwenye bilauli ya baba yake. "Karibu baba" alisema kisha akatoka tena.

Aliporudi alikuja na magi yenye togwa baridiii!, akasogeza redio pembeni kidogo, akachukua ile bilauli iliyosalia akaiweka kisha akamimina... " Karibu kaka" alisema na kuondoka.

Mie hapo moyo wangu burdani, nilikuwa nafurahia kila sekunde aliyokuwepo Hamida.

"Karibu James..." Mzee alisisitiza na kunitoa kwenye mawazo yaliyonijia ghafla.

"Enhe, umesema unataka muongozo kuhusu kubadili dini!" Alisema huku akibofya kitufe cha kuchezea kaseti sanjari na kitufe chekundu cha kurekodia.

"Ndio mzee, nipe muongozo" nilijibu baada ya kugida (kunywa) fundo (puff) moja ya togwa.

Akasema, sasa nitakuhoji maswali ambayo utakavyojibu itanipa mwelekeo...

"Je umelazimishwa ama kushawishiwa na mtu kubadili dini na kuwa mwislamu?" aliuliza

"Hapana mzee" nilijibu.

"Je huogopi kutengwa na jamii yako wakigundua kuwa umewahama?" Aliendelea kuuliza...

Niliinua bilauli ya togwa na kunywa tena, kisha nikamjibu, hapana, nimeshafikisha umri wa kuamua nitakalo, hivyo sina hofu yoyote.

Mzee Burhani akaniangalia kwa makini kisha akaniuliza kama najuwa uwepo wa mtu aliyeitwa Muhammad (s.a.w), nikamjibu, ndiyo nasikia alikuwepo mtu huyo.

Mzee aliendelea kunihoji imani yangu kuhusu Mungu. Nikamjibu "Sisi tunaamini Mungu ni mmoja na yupo katika nafsi tatu, yani Mungu Baba, Mungu Mwana na Mungu Roho mtakatifu"

Akaniambia wao waislamu wanaamini kwamba Mungu ni mmoja tu na hakuna Mungu mwana wala Mungu Roho mtakatifu...

Kwa kuwa nilishayavulia maji ilibidi nikubaliane naye katika kila alilozungumza, nilikuwa naona kama ananichelewesha...

"Sasa ili uwe mwislamu inabidi ukiri kwa moyo na kutamka kwa ulimi kwamba hapana Mola apasaye kuabudiwa kwa haki ila Allah na Muhammad ni mjumbe wake" alisema.

Aliniambia mengi ya awali kuhusu imani ya kiislamu ikiwemo kutosulubiwa kwa Yesu ambapo wao wanamuita Nabii Issa na mambo mengine kadha wa kadha.

Nikapata ugumu wa kiimani, kwani kusulubiwa kwa Yesu ndiyo msingi wa imani yetu ilipolala, lakini nikapiga moyo konde.

Akaniambia, nikajifikirie, kama nitakuwa tayari basi nimtafute ili anisilimishe rasmi na kunipeleka msikitini kwa ajili ya utambulisho.

Nikamjibu, sawa. Kisha nikamalizia togwa iliyobakia kwenye bilauli.

Alisisitiza kuwa, kuwa muislamu ni rahisi sana, unatamka shahada mbili basi tayari unakuwa mwislamu.

Kwa kuwa jua lilizama tukiwa bado tunaongea, akaniambia anaenda kuswali (ndani) hivyo nimsubiri, kisha akatoka mle sebuleni.

Mara sauti za miguu ikitembea nikasikia ikija upande wa sebuleni.

Waooo! Hamida huyo! Nikijisemea kimoyomoyo, akakusanya zile bilauli na magi iliyobakia togwa shinda (kiasi) na kutaka kuondoka...

"Angalia usiangushe bilauli kama siku ile..." Maneno yalinitoka mdomoni...

Akatabasamu kisha akasema "hizi chafu hazitoanguka kwakuwa nimezibebanisha... Halafu siku ile ule mtandio ulikuwa unateleza sana ndio maana..." Alijibu huku akimfuta Nadya alipojimwagia soda.

"Pole" nilimwambia kisha nikamuuliza "Eti malai (icecream) zipo?"

Akajibu kuwa zimebakia chache. Nikamwambia, nikitaka kuondoka naomba uniletee zote.

Akashangaa na kuuliza "sasa utazibebaje?"

Niwekee kwenye chombo kesho nitakuletea, naenda kuzihamishia kwenye chombo kingine ili niziponde ponde nitengeneze juisi.

Akacheka kisha akasema "si bora ungesema tu tukutengenezee juisi"

"Ewaaaaa (aiwaa) hilo pia ni wazo zuri, lakini leo nifungie, halafu naomba unitengenezee juisi nzuri ili nikinywa niwe nakukumbuka muangusha bilauli" nikasema.

"Mmh" akaguna na kuondoka.

Baada kama ya dakika kumi hivi nikamsikia mzee Burhani akikohoa huku akija uelekeo wa sebuleni.

"Samahani nilikuacha peke yako" alisema huku akiingia.

"Bila samahani, sikuwa peke yangu, Hamida alikuwepo na huyu Nadya pia..." Nilisema huku nikikaa vizuri kwenye kochi.

Hatukuongea sana baada ya pale, nikaaga na kutaka kuondoka, nikamuambia nimeagiza niletewe malai...

"Hamidaaaa" Mzee Burhani aliita.

"Mgeni anataka kuondoka"

Mara akaja na kiboksi kidogo cha kuhifadhi joto (ama baridi), akanipatia.

"Shilingi ngapi?" Nikamuuliza kwa sauti ya chini.

"Shilingi nne, zipo nane humo" alijibu.

Nikatoa gwala (dala/ shilingi tano) nikampatia, nikamwambia chenji nitachukuwa kesho.

Akasema "in shaa Allah."

Tukasimama na mzee Burhani kwa pamoja, nikachukuwa kiboksi chenye malai na kutoka sebuleni, nikavaa ndaba (raba mtoni) zangu na mzee Burhani akanifungulia mlango, akanisindikiza hadi Shibam (siyo mbali), nikamwacha hapo, nikachukuwa batavuz yangu huyoo hadi Butiama restaurant kisha nyumbani.
*******

Nilikuwa na furaha kubwa sana, kupata wasaa wa kuongea na mzee Burhani na kubadilishana maneno na Hamida.

Ghafla tafakari za imani ya dini yangu ikanijia, nikaanza kuwaza mabadiliko yatakayojitokeza kama nikisilimu.

Kupoteza mawazo nikachukuwa zile ice-cream na kuzipondaponda kisha nikaweka kwenye friji. Nikachukuwa sehemu ya ile juisi (vibarafu vidogo vidogo) na kuweka kwenye glasi kisha nikachukuwa brandy kabatini na kumiminia kwa wingi hadi glasi ikajaa.

Kiukweli wala sikuwa nahitaji ice-cream, nilitaka tu nipate wasaa wa kubadilishana maneno ya Hamida, "nimefanikiwa hivyo ngoja nishangilie ushindi wa awali." Nikijisemea kisha nikaanza kunywa taratiibu huku nikisikiliza santuri ya Kool and the Gang, wimbo wa 'Celebration'
************

Itaendelea...
IMG-20200129-WA0016.jpeg
IMG-20200129-WA0008.jpeg


James Jason
 
SEHEMU YA SABA
*******************

Alarm ya saa ya mezani iliniamsha saa kumi na mbili asubuhi, ndio nikajuwa kuwa nilikunywa kupita kiasi, turntable ilijizima yenyewe (changer), taa sikuzima, na nilishtuka nikiwa sebuleni kwenye kochi.

Kumbe niligigida mzinga wote wa Cognac Brandy. Kichwa kilikuwa kizito, na ilikuwa Jumanne.

Niliamka kujiandaa kwenda kazini.

=

"Habari za asubuhi Marry?" Nilimsalimia mhudumu ofisini kwangu .

"Nzuri boss, karibu" alinijibu huku akipokea mkoba wangu mdogo.

"Leo najisikia vibaya kidogo, hivyo napumzika ofisini kwangu hadi saa nne, baada ya hapo utaruhusu watu kuonana nami" nilimwambia.

"Sawa boss" alijibu huku akiendelea na usafi.

Niliingia ofisini na kukaa kwenye dawati langu huku nimeinama.

"Karibu chai boss" Marry alinistua...

"Oh, ahsante, eeeeh hebu nenda pale mgahawani kaniletee supu maridadi" nilisema huku nikijiweka sawa.

Nikaiangalia ile chai, nikaona haipandi kabisa asubuhi ile. Hivyo nikaanza kupekua mafaili yangu wakati nikisubiri supu, huku nawaza mambo mawili makuu, kusilimu na kuanza kumtongoza Hamida.
******

Haikupita muda mrefu nikaletewa supu ya ng'ombe ya moto safi kabisa, nikainywa na kula nyama, nikaanza kujisikia ahueni.

Niliendelea kufanya kazi kivivu vivu huku nikiwaza mengi kichwani...

Niliwaza jinsi harusi za kwetu utaturuni zinavyokuwa, niliwaza jinsi wanawake wa kitaturu wanavyojuwa kuwanyenyekea wanaume, niliwaza kuhusu sherehe zinavyokuwa, niliwaza msisimko wa nyimbo na hamasa zenye kuamsha hisia kali... Ilimradi niliwaza mambo mengi kuhusiana na mambo ya harusi.

"Kweli sasa nimekua" nilijikuta nasema kwa sauti.

"Vipi boss, leo mbona uko hivyo? siyo kawaida yako!" Marry aliniuliza alipokuja kuchukuwa vyombo pamoja na kuleta mafaili mengine ya kuyapitia...

"Eeeeh, nafikiri muda wangu wa kuoa sasa umewadia" nilimjibu huku nikitabasamu

"Heheeee!" Alicheka kiumbea

"Vipi, huamini?" Nilimuuliza huku natabasamu

"Hapana, naamini ila najiuliza ni nani huyo aliyekukamata hadi umetangaza ndoa" alisema.

"Hapana, sijatangaza ndoa, wala mchumba mwenyewe hajui kama atatongozwa..." Nikasita kidogo kisha nikaendelea...

"Nataka nioe Mwarabu" nilimalizia.

"He!" Alishangaa na kuondoka.
**********

Marry ni mfanyakazi hodari sana, ni Katibu muhtasi wa siku nyingi (nilimkuta kazini) na anapenda sana utendaji wangu.

Huwa namshirikisha mambo yangu mengi, na huwa ananishauri vizuri.

=

Jioni baada ya kutoka kazini moja kwa moja nilielekea kwa Alimaua kumtembelea mzee Katibu Kata.

Nilimkuta ana nafuu sana kuliko juzi yake. Nikamweleza maamuzi niliyofanya ya kuanza kubadili dini na kisha kuanza kumpa maneno ya mapenzi mchumba mtarajiwa.

Alifurahia uamuzi wangu wa kuamua kuingia katika 'dini yake', lakini hakuwa na matumaini kama nitafanikiwa kumuoa Hamida kwa jinsi alivyokuwa anazifahamu familia za Kiarabu.
*****

Mzee Burhani ana asili ya Oman, Babu yake alikuja miaka mingi kabla ya uhuru, alikuwa anaishi kisiwani Unguja. Baba yake mzee Burhan marehemu alhaj Ahmed Said alihamia Dar es Salaam katika harakati za kibiashara na yeye mzee Burhani alizaliwa hapo Dar.

Mke wake ni half-cast wa kingazija na kihindi, yaani baba yake alikuwa mgazija na mama yake alikuwa ana asili ya kihindi waliolowea Comoro.

Mchangachiko huo ulitoa matunda mazuri ya watoto wa kike ambaye kitinda mimba wao ndio nafikiria jinsi ya kumuingia na kumtongoza.

Kaka yake Hamida aitwaye Yasir pamoja na rafikiye Abdul wote ni madereva wanaendesha malori (Scania 81). Wiki hiyo magari yao yalikuwa Kibaha (Sub-Scania) kwa ajili ya service kubwa, ndiyo maana walikuwa wanaonekana mjini muda mwingi.

Warda ameolewa na mtoto wa baba yake mdogo, yupo Mwanza, Sabra ameolewa pia na ndugu yao wapo Oman, Yasir bado hajaoa.
********

Tuliongea mengi na mzee Katibu Kata, akanitia moyo japo alikuwa anahisi 'nitagonga mwamba' katika harakati zangu za kumchumbia Hamida.

Nilivyotoka Mwananyamala moja kwa moja nilielekea nyumbani, baada ya kupumzika nilielekea Butiama Restaurant, tayari ilikuwa jioni, nilienda kwa mzee Burahan kurudisha 'coolbox' yao, na kuchukuwa juisi nzuri ya mikomamanga iliyochanganywa na embe ng'ong'o.

Aliyenipokea alikuwa Yasir, kaka yake Hamida, alipokea lile boksi kisha akamwita Hamida apeleke jikoni.

Hamida alivyokuja alinikuta bado nimesimama ukumbini (koridoni)...

"Huingii varandani leo" Hamida aliuliza huku anakuja

"Hapana, leo nina haraka..." Kabla sijaendelea alinikatisha...

"Basi subiri nikuletee juisi" alisema.

"Sawa" nilimjibu.

Punde si punde alirejea dumu la lita 3 lililojaa juisi. Nilipokea na kumlipa, nilijifanya sina stori siku hiyo, nikaaga na kuelekea home.
*******

=

Siku tatu baadaye jioni nilipotoka kazini, ilikuwa siku ijumaa, nilitoka mapema kuliko kawaida yangu...

"Naenda kwenye mawindo ya binti mwarabu" nilisema baada ya kumuaga Marry.

"Haya boss, usinisahau kwenye kamati ya maandalizi..." Alijibu kuhu akitabasamu.

Nikaenda nyumbani moja kwa moja, nikaoga na kubadili nguo, (nilivaa 'bora shoes', suruali ya kitambaa, tshirt nyeupe) nikatoka nikaenda moja kwa moja hadi Africa Studio, nikakuta picha zipo tayari (black & white), zilikuwa zimetoka vizuri mno. Wakaziweka kwenye bahasha (B5) nyeupe, nikamalizia malipo nikaelekea Shibam.

Pale Shibam sikumkuta mzee Burhani, niliwapiga round moja ya kahawa kisha nikaelekea nyumbani kwa mzee Burhani.

Nilikaribishwa vizuri na yule mama wa kiafrika na kuingia sebuleni. Sebule yote nikaibadilisha harufu na kuanza kunukia uturi (perfume) ya Gift of Zanzibar. Ilikuwa inanukia vizuri sana, kama udi hivi lakini siyo, kama asmini hivi lakini siyo, ilimradi ni harufu isiyochosha wala kukera.

Baada ya kusalimiana, nikamkabidhi lile dumu la juisi, halafu nikamwambia kuwa nina shida na mzee.

Akanijibu mzee yupo chumbani kwa Hamida wana mazungumzo na wanawe.

"Kuna posa (ya maneno) imeletwa ndio wanajadili mzee, mama Warda, Hamida na Yasir." Alisema.

Ghafla moyo ukaanza kunidunda kwa nguvu, nadhani hata yule mama aligundua.

"Sawa mama, nasubiri wakimaliza watanikuta" nikamjibu.

"Basi ngoja nikuletee kinywaji chako ukipendacho" alisema huku akiinuka

"Sawa mama" nilijibu.

Aliniletea bilauli iliyojaa togwa baridi, akavuta stuli na kuniwekea.

"Karibu" alinikaribisha.

"Ahsante mama" nilisema kisha nikaweka bahasha yangu kwenye stuli.

Nikaanza kunywa mdogo mdogo huku nikiwa na mawazo.

Akatoa ukimya kwa kuniuliza, imekuwaje nalipenda togwa, nilimjibu nilijifunzia kunywa Iramba ambako ni kinywaji cha kawaida.

Akahoji "wewe ni mnyiramba"
Nikamjibu "hapana"

"Mnyaturu?"
"Hapana"

"Ishi, sasa wewe ni kabila gani?" Aliuliza.

"Mimi ni Mtaturu" nilimjibu

"Ahaaaa, nyie ndio Mang'ati eee" alisema kwa kutania

"Hapana, ila tunashabihiana sana, wote asili yetu ni Ethiopia, lakini mababu zetu walihamia miaka mingi sana maeneo ya Arusha - Manyara (wakati huo Manyara ilikuwa sehemu ya Arusha)

" Ahaaa, ndio mkaanza kuwaibia wamasai ng'ombe zao eeee!" Alitania

Nikacheka kisha nimasema "Hapana, sisi ndiyo tulikuja na mifugo kutoka Ethiopia, babu zetu walikuwa wakibadilishana mifugo na wenyeji kupata ruhusa ya kukaa sehemu kabla ya kufika ardhi waliyoipenda ambapo ni kandokando ya ziwa Eyas. Hivyo zote hizo ni ng'ombe zetu...." Nikacheka tena kisha nikaendelea, "Hata zile za Usukumani ni za kwetu pia" nilitania...

Nilikuwa nadhani yeye ni msukuma kwa lafudhi yake wakati anaongea.

"Unafikiri mie msukuma, mie ni Mnyamwezi" alisema na kucheka kiasi

Nami nikacheka. Hakika aliniondoa kwenye mawazo yaliyotaka kuniteka ghafla.

"Basi togwa hilo ni la Tabora" alisema,

"Mie ndio nimewafundisha humu ndani kulitengeneza, niko nao hawa tangia usichana wangu hadi sasa, kuna wakati niliondoka nikaolewa nikazaa watoto 7, lakini ndoa haikuwa ya furaha sana, nikaomba talaka, ndipo niliporudi hapa hadi sasa." Alisema huku akionesha huzuni kiasi.

"Du, pole sana", nilimwambia, na kumuuliza watoto wake wako wapi.

Alinijibu kuwa wote wapo Tabora kwa baba yao.

Mazungumzo yetu yalikatishwa pale Yasir alipoingia sebuleni, alisalimia na kuketi. Haikupita muda mama Warda naye akaingia, tukasalimiana, kisha akatania "umefuata ice cream na leo?", nikamwambia hapana, leo nina shida nyingine na mzee, mara mzee naye akaingia. Tukasalimiana kisha akasema "samahani, nimekusikia umekuja muda kidogo, lakini tulikuwa tuna mazungumzo ndani, binti yangu ameposwa, lakini hataki kuolewa ndiyo tulikuwa tunayajenga..."

Da! Kimoyomoyo nilifurahi sana, nikaona hii ni dalili njema kwangu, hofu na wasiwasi juu ya kumkosa Hamida ikaniondoka.

"Ahaa, haina neno, mie nilikuwa na mama huyu sikuwa mpweke" nilijibu.

"Naam, twaib, nakusikiliza, au ni faragha niwaombe hawa watuachie nafasi?" Mzee Burhani alisema.

"Hapana, siyo siri, nimekuja naomba unisilimishe, nimeshakata shauri" nilisema.

"Allahu akbar" alisema mzee Burhani.

"Hamidaaaa" mzee Burhani alimuita binti yake.

Mara Hamida akaingia, kimyakimya, macho mekundu, sura imemvimba kama alikuwa analia. Akaketi jirani na yule mama wa kiafrika.

Pakawa na ukimya fulani hivi wa sekunde chache, kisha mzee Burhani akakata ukimya kwa kusema...

".... Eeeh bila shaka nyote mnamfahamu James, wiki iliyopita tulikuwa hapa tunazungumza, alikuja kuomba muongozo akitaka kusilimu. Nilimpa mawili matatu na leo amekata shauri na kutaka kusilimu."

Alitulia kidogo kisha akaendelea...

"Binadamu wote kwa asili tunazaliwa waislamu, lakini wazazi wetu ndio hutubadili dini na kufuata dini nyingine ama kubaki katika dini ya asili ambayo ni uislamu..."

Aliendelea na hotuba isiyo rasmi...

"Uislamu ni Amani, kama lilivyo neno lenyewe, ni kujisalimisha kwa Mola Muumba wa mbingu na nchi na kunyenyekea kwake, hivyo basi umefanya uamuzi sahihi kurejea katika dini ya asili ambayo ina mfumo mzima wa maisha ya mwanadamu wa namna ya kuyaendea mambo yake hapa duniani, kaburini, siku ya ufufuo na hukumu na baada ya hukumu." Alisimama kidogo kumeza mate kisha akaendelea...

"Shahada mbili ni mkusanyiko wa matamko mawili ya ahadi anayoichukua kiumbe (mwanadamu) mbele ya Muumba wake na viumbe wenzake; mbapo mtamkaji hula kiapo cha utii kwa Mwenyezi Mungu (Allah) na Mtume wake katika maisha yake yote kwa kufuata maamrisho na makatazo yake."

"Shahada ya kwanza ni tamko la utii kwa Allah, na shahada ya pili ni tamko la utii wa mtume wa Allah..."

"Sasa nitasema maneno nawe utafuatisha..."

Nikaitikia sawa.

"Nitaanza kusema kwa kiarabu kisha tutarudia kwa kiswahili ili uelewe maana yake" alisema, kisha akaanza kutamka...

Wakati huo wote sebuleni palikuwa kimya, nami namsikiliza mzee Burhani kwa makini huku nikiibia kumuangalia Hamida, alikuwa amejitanda uso wote kwa mtandio kasoro macho tu ambayo yalionekana kuwa mekundu kuliko kawaida.


“ASH-HADU"
Nikafuatisha,
(Ash-hadu)

"AN LAA"
(An-laa)

"ILAAHA"
(Ilaaha)

"ILLAL-LAAHU”
(Illal-laahu)

“WA ASH-HADU"
(Wa ash-hadu)

"ANNA MUHAMMADAN"
(Anna Muhammadan)

"RASUULU LLAH”
(Rasuulu llah)

"NASHUHUDIA KWA MOYO NA KUTAMKA KWA ULIMI KWAMBA"

Nikaendelea kufuatisha...
(Nashuhudia kwa moyo na kutamka kwa ulimi kwamba)

"HAKUNA MOLA APASWAYE KUABUDIWA KWA HAKI ISIPOKUWA ALLAH"
(Hakuna Mola apaswaye kuabudiwa kwa haki isipokuwa Allah)

"PIA NASHUHUDIA KWA MOYO NA KUTAMKA KWA ULIMI KWAMBA"
(Pia nashuhudia kwa moyo na kutamka kwa ulimi kwamba"

"MUHAMMADI NI MJUMBE WA ALLAH"
(Muhammad ni mjumbe wa Allah)

"kama alivyo Yesu, Mussa, Ibrahimu" alimalizia kisha wote mle ndani wakasikika wakisema, Allahu akbaru, Allahu akbaru, Mungu ni Mkubwa, Mungu ni Mkubwa.

Walisema maneno hayo (Allahu akbaru) hata kabla sijayafuatisha maneno ya mwisho ya mzee Burhani.

Kisha nikamuona Hamida, Yasir na mama Warda wanalia kwa kutokwa na machozi bila kutoa sauti...

Pakawa na ukimya kidogo...

Nikawa nawaza, hivi hawa wanaolia, wanalia kwa sababu nimesilimu ama kuna jambo jingine!

Nilikuja kujuwa baadaye sana wakati mtu mwingine aliposilimu nikishuhudia, kuna hali fulani ya utii na unyenyekevu wa imani (emotions) hujaa...

"Sasa James umeshakuwa mwislamu, inabidi uchague jina zuri ulipendalo ili uitwe kwa jina hilo" mzee Burhani alitoa ukimya uliokiwepo.

Tayari kichwani nilikuwa nina jina nililolipenda ambalo lilianzia na herufi J kama jina langu.

"Jamaal" nilitamka

"Maa shaa Allah, Jamaal maana yake ni mzuri, wa kupendeza yaani handsome..." Alidakia mzee Burhani.

"Kuanzia sasa tutakuwa tunakuita Jamaal" aliendelea...

"Sasa kuna mambo muhimu ambayo unapaswa kujifunza ili uyajuwe ukishakuwa mwislamu, nitakupatia vitabu ili uweze kujisomea mambo muhimu, yameandikwa kwa kiswahili pia vipo vitabu vya kwa lugha ya kiingereza..." Aliendelea

"Kwakuwa wewe ni mtu mzima, inabidi upate mafunzo ya dini kwa njia tofauti siyo kama watoto wanavyofundishwa, chaguwa siku za kujifunza nami nitakutafutia mwalimu"

Nikamjibu

"Mie nipo tayari siku nne kwa wiki, yaani Jumatatu hadi Alhamis baada ya kutoka kazini nakuwa huru, hivyo nakusikiliza wewe mzee"

"Yasir hebu kalete kile kitabu cha swala na mafundisho / maamrisho yake" mzee Burhani alimwambia kaka yake Hamida

"Naona muda wa swala umewadia, sasa twende wote msikitini" alisema mzee Burhani huku akiwa mwenye furaha.

Mie sikuwa na hofu wala kipingamizi, nilishayavulia nguo maji inabidi niyaoge.

Yasir alirudi na kitabu kidogo kiitwacho Sala na maamrisho yake na kunipatia.

Kwakuwa kilikuwa kidogo sana, nilikiingiza mfukoni mwa suruali.

Mzee Burhani akasimama, nami nikasimama tukatoka tukawa tunaelekea msikitini. Tulielekea msikiti wa Mkauni, siyo mbali kutoka kwa mzee Burhani.

Nyuma yetu Yasir alitufuata, tukawa tunaambatana naye, tulivyofika msikitini, tukavua viatu kama kawaida, tukavihifadhi sehemu ya kuhifadhia, kisha mzee Burhani akamwambia Yasir anifunidishe namna ya kuchukuwa udhu ili niwe tayari kwa ibada ya swala.

Yasir alinielekeza msalani, baada ya kutoka msalani akanipeleka sehemu maalum ya kutawadhia (kuchukuwa udhu), yaani kuosha viganja vya mikono, kusukutua, kusafisha pua, uso, mikono yenyewe hadi viwikoni, kupaka maji kwenye kichwa na masikio kisha kumalizia na kuosha miguu.

Nilifanya kwa kumuigiza afanyavyo, tulipokuwa tayari tuliingia ndani tayari kwa ibada...

Baada ya kuswali (inachukuwa dakika tano hivi) nikasikia tangazo...

"Kuna kijana amesilimu, alikuwa akiitwa James Jasson na sasa ataitwa Jamaal Jason, alikuwa dhehebu la Roman Catholic, tunamuomba asimame ili waislamu tumuone tumjue kuwa ni ndugu yetu katika imani"

Ni imamu (kiongozi wa ibada) alikuwa akitangaza.

Wakati nainuka nilisikia Allahu akaru nyingi hadi nilisisimkwa mwili, nikaombewa dua, kishwa waumini wakaambia wawe wananisaidia katika mambo ya ibada na kadha wa kadha.

Baada ya tasbihi (kama kusoma rozali vile) na dua, watu walianza kutoka, mzee Burhani alikuwa anaongea na Imamu, bila shaka ndiye aliyempa taarifa za kusilimu kwangu.

Kisha nikaona mzee Burhani amesimama tena peke yake akawa anaswali.

Mie na Yasir tukatoka nje tukawa tunamsubiri.

"Eti, mbona nilimuona Hamida akilia, kulikoni" niliuliza kiuchokozi

"Aaaa ni stori ndefu nitakuhadithia kesho in shaa Allah" alijibu kifupi namna hiyo, na mara mzee Burhani akawa anatoka nje.

Tulirudi wote hadi nyumbani kwa mzee Burhani, lakini sikuingia ndani, bali niliagana nao nikapanda batavuz yangu huyooo hadi Butiama restaurant, kisha nyumbani.
**********

Nilivyofika nyumbani nilikipitia kile kitabu na kuona yaliyoandikwa, ni kitabu kidogo sana unachoweza kusoma kwa saa chache tu.

Nilikuta misamiati mingi ambayo sikujuwa maana yake mara moja, lakini kilikuwa kinaeleweka vizuri tu.

Baada ya kujimwagia maji na kujifuta, nikajilaza kitandani chalichali nikiwa nimevaa bukta huku nikitafakari safari ambayo nimeianza.

Nikawa nawaza, hapa pombe tena basi, kuzini tena basi nk hadi nikapitiwa na usingizi.
********

Sikwenda sinema ijumaa hiyo kama ilivyo kawaida yangu. Kesho yake mapema sana nikaenda kwa mzee Katibu Kata, niliwahi ili asije kuondoka nyumbani kabla.

Nilimueleza habari yote ya kusilimu kwangu, akafurahi sana, tukabadilishana maneno mawili matatu kisha nikamuaga huyooo hadi nyumbani.

Niliendelea na shughuli ya usafi hadi niliposikia adhana, nikaacha, nikajitayarisha kwenda msikitini. Kutoka nyumbani hadi msikiti wa mkauni ni mbali kidogo kwa kutembea kwa miguu, hivyo niliwasha batavuz nikaenda.

Nikifuata utaratibu kama wa jana usiku hadi ibada ilipoisha nikatoka na kuelekea Butiama. Hakika Butiama Restaurant nimewachangia sana!

Baada ya hapo nilirudi nyumbani kumalizia usafi na mambo mengine.
****

Saa kumi baada ya swala ya alasiri nilienda Shibamu, siku za Jumamosi watu huwa wengi wakijiburudisha kwa michezo mbalimbali.

Mara mzee Burhani akawasili...

"Ahaaaa sheikh Jamaal, upo?" Alisema baada ya kusalimia watu waliokuwepo pale...

"Jamani eee, kuanzia jana huyu James sasa tumuite Jamaal, amesilimu." Alisema

Allahu akbaru, watu waliokiwepo pale walisema maneno hayo kwa kurudia mara tatu.

"Karibu sana Jamaal" mzee mmoja maarufu sana kijiweni hapo alisema.

Mzee Burhani akaniambia, mwalimu wako wa awali atakuwa mwanangu Yasir, wiki hizi mbili yupo tu anasubiri gari iwe tayari, iko service kubwa.

Sasa basi Jumatatu utaanza naye hadi atakapoondoka kisha nitakuwa nimeshapata mwalimu utakaye endana naye kukusomesha mambo muhimu.

Tuliongea palee hadi magharibi ilipofika, baada ya swala akanikaribisha kwake kwa chakula cha usiku.

"Umri wako unaruhusu kuoa, utakula hotelini mpaka lini" alitania

"Bado natafuta mke muafaka" nilijibu...

Tuliendelea na mazungumzo ya dini hadi ilipowadia muda wa swala ya isha. (Swala ya saa mbili usiku)

Baada ya kuswali, tulirudi nyumbani kwa ajili ya chakula cha usiku.
*****

Sebuleni kuliandaliwa chakula kizuri sana, kulikuwepo viazi mbatata (viazi mviringo), sijui hata wamevifanyaje, maana ni vilaini pia vina kama mbogamboga (nilijuwa baadaye kuwa ni kachori), mchuzi wa nyama ya ng'ombe pamoja na nyama yenyewe, chapati maridadi sana, sikuwahi kuziona kama hizo kabla, wali uliopikwa kwa nazi, mchuzi shatashata wa kamba / kaji (prowns), chai ya maziwa na ya mkandaa (black tea), kisamvu kilichokolea nazi.... Bila kusahau pembeni kulikuwa na jagi la maji ya kunywa.

Mtihani ukawa namna ya kukunja miguu wakati wa kula maana pameandaliwa kwenye busati juu yake paliwekwa mkeka.

Baada ya kujikunja vizuri nikifanikiwa kukaa ipasavyo, ni mkao unaoweza kukaa hivyo kwa muda mrefu bila kuchoka (miguu inakunjwa kwa kupishana kama unaikalia lakini huikalii)

Kwa kuwa sebule ilikuwa kubwa sana, kuliandaliwa sehemu mbili, jirani na pazia la mlango walikaa mama wa Kiafrika, Hamida, Nadya na mama Warda, na upande mwingine tulikuwa mimi, Yasir na mzee Burhani.

Mie nilikaa kwa namna ambayo nilikuwa naangaliana uso kwa uso na Hamida japo kuna ka-umbali hivi.

Nilishazoea kula kwa kijiko, leo najifunza kula kwa mikono, nilisema hivyo wakati Yasir akinimwagilia maji ya kunawa...

"Utaweza tu Jamaal" alijibu.

Sikutaka kuanza kula wali kwa kuwa nimeshauzoea, nilianza kula chapati kwa mchuzi na chai, [emoji39] Hakika kuna watu wanajuwa kupika jamani... Nilijikuta nasema tu kwa sauti...

Nilivyomaliza chapati moja nikahamia kwenye kachori, dah, tamu sana, zina pilipili kwa mbaali, mwisho nikapakuwa 'tuwali' kiduchu ili nimalizie, loh salaleh, kumbe bwana ule wali ndio funga kazi, nikaongeza mwingine mwingi...

Mchuzi wake sasa na prouwns waliokaangwa na kumenywa kisha kuungwa kwa nazi nzito, acha kabisa..., utamu wa kisamvu sijawahi kula popote pale... (Kilitwangwa jana yake na kuchemshwa kwa viungo muafaka, leo ndio kimeungwa vizuri kwa nazi, hii aliniambia Hamida siku nyingine kabisa nilivyomuuliza)
*****

Baada ya kula, tukawa tunazungumza mambo ya kawaida, hali ya uchumi wa nchi, kupungua kwa bidhaa muhimu nk

Wakati huo Hamida alikuwa bize akiondosha vyombo...

Aliporudi alikuja na bahasha yangu niliyoishau jana (kwa makusudi)

"Jana ulisahau mzigo wako" Hamida alisema huku akinipatia bahasha ambayo tangia awali sikuwa nimeifunga kwa lengo maalum.

"Ooh, ahsante, nilishasahau kama zipo hapa" nilijibu

Lengo langu lilikuwa Hamida anione vizuri kwakuwa mara zote niwapo hapo huniangalia kwa kuibia ibia tu.
*******

Niliaga, Yasir akaniambia ngoja nikusindikize....

Nilikokota batavuz huku tukielekea maeneo ya Shabam kutokea nyumbani kwa akina Hamida...

Njiani wakati tunaongea mawili matatu ndipo nikachomekea kuhusu kulia kwa Hamida...

Akanieleza kuhusu posa iliyokuja kutoka Oman, na kwamba muoaji alikuwa mtu mzima sana lakini tajiri... Hamida alikuwa hataki kuolewa na mtu mzima hivyo walikuwa wanajaribu kumsihi akubali kwani ndiyo posa ya kwanza na umri wake ulikuwa umewadia kuolewa...

Hamida alimaliza kidato cha nne miaka miwili iliyopita kisha akaenda Kenya kusomea stashahada ya domestic science na catering (Kenya Utalii College - Campas ya Mombasa).

"Du" nilisema
"Lakini yafaa apewe uhuru wa kuchaguwa ampendaye, kama hamtaki msimlazimishe, asije akachukuwa maamuzi mabaya" nilisema

Kipindi hicho mabinti kusaga chupa na kumeza kwa ajili ya kujiua ilikuwa tabia iliyoshamiri sana.

Tuliagana yeye akarudi na mie nikapanda batavuz yangu hadi home nikiwa na furaha sana kwa kupiga hatua nyingine kwenda 'mbele'.
*******

Itaendelea
IMG-20200129-WA0035.jpeg
IMG-20200129-WA0036.jpeg
IMG-20200129-WA0022.jpeg


James Jason
 
SEHEMU YA NANE
*******************

Siku ya Jumapili nilitulia nyumbani kwa ajili ya kunyoosha nguo na kujisomea.

Baadaye nilianza kufikiria jinsi ya kuanza kumtongoza Hamida.
******

Enzi hizo kupata mpenzi wa kudumu naye unasotea haswa, hasa katika mazingira magumu kama haya ya geti kali na msimamo wa kidini.

Kwakuwa tayari nimepata tiketi ya kuwa na Yasir siku nne kwa wiki japo kwa saa chache, niliona ni nafasi nzuri ya kutimiza azma yangu...

Siku ya Jumatatu niliwahi afisini kama kawaida yangu, niliingia huku napiga mluzi

"Karibu boss, habari za asubuhi? Marry alinisalimu wakati naingia afisini kwangu...

" Njema sana bibie, ukimaliza kazi zako uje afisini" nilimuambia.

Nilifanya kazi baadaye nikaletewa chai, nikamwambia Marry aketi niongee naye huku nakunywa chai...

"Zoezi la kumnasa mwarabu limeanza, Ijumaa nimesilimu" kikanyanyua kikombe nikanywa chai kidogo

"Enhe!" Alishabikia

"Ndiyo hivyo, sasa naitwa Jamaal, japo sinto badili kwenye makaratasi kiserikali, ila wewe tambua mimi ni Muislamu na jina langu ni Jamaal" niliendelea

"Huyo bibie kweli amekuweza, yani ulivyokuwa hushikiki leo umetulizwa, kweli hakuna mkate mgumu kwenye chai" aliongea huku akicheka.

Mary tunaelewana sana, wakati mwingine nilikuwa namshirikisha kufanikisha kupata warembo wa kustarehe nao, yaani kifupi nilikuwa kiwembe balaa!

Lakini tangia nimuone Hamida mara ya kwanza, nikawa kama pepo la uzinzi limenitoka vile, maana sikutamani tena wanawake. Nilikuwa namtaka yeye tu, hadi nimpate tena kwa kumuoa kabisa.

Tuliendelea kuongea na Mary hadi walipoingia wageni, mie nikaendelea na kazi zangu naye akawahudumia wageni (wateja)
****

Muda wa kutoka kazini ulipowadia nilienda nyumbani, nikabadili nguo kisha nikaelekea kwa mzee Burhani kwa mwalimu wangu Yasir.

Tulianza masomo ya Qur'an, alianza kunifundisha herufi za kiarabu, (abt... Aliif, bee tee..) Hadi mwisho na kuniambia nizidurusu hadi nizikariri hadi mpangilio wake. Alinifundisha herufi 30 japo aliniambia zipo zingine lakini kwa mpangilio wa kuzichanganya.

Aliporidhika ninazitamka vizuri, alitoka akaniacha na kuniambia niendelee kuzisoma zote kwa sauti (siyo ya juu bali ya kusikia) hadi atakaporudi.

Sehemu niliyokuwa nasomea ilikuwa chumba kinginge ambacho huwa wanakitumia kuswalia wanaoswalia nyumbani.

Chumba si kikubwa kama pale sebuleni, kuna zulia zuri la kijani, kuna miswala iliyokunjwa mitano, hakuna vitu vingine bali misahafu.

Kabla ya jua kuzama, nikaona mtu anaingia, kumbe Hamida, mkononi ameshika bilauli...

"Pumzika kidogo, nimekuletea togwa..." Alisema

Nikaacha kusoma, nikapokea na kumuuliza

"Na hili umelitengeneza wewe?!

"Hapana leo sijaliandaa mimi, ma-mkubwa ndiyo ameandaa" alijibu.

"Ahaa, basi kesho niandalie kinywaji utakachotengeneza wewe" nilimuambia

"Unafikiri mie sijui, ndiyo fani yangu ati" alisema kwa kulegeza ulimi ile lafudhi ya kimombasa

"Haya basi nione ufundi wako hiyo kesho" nilimjibu. Kisha akatoka.

Mara Yasir akaingia na adhana ya magharibi ikaanza.

"Twende zetu masjid" Yasir alisema

Bila kujibu kitu nikainuka, tukatoka nje na kuelekea msikitini.

Njiani aliniuliza kama nimehifadhi herufi zote, nikamwambia tukitoka msikitini nitamsomea ili ahakiki.

Baada ya ibada tulirudi kwao na kuingia chumba kile kile cha kusomea na akaanza kunisikiliza.

Kuna herufi chache nilikuwa nakosea kuzitamka ipasavyo, akanirekebisha kisha akaniambia ngoja akanunue daftari ili niziandike.

Kumbe wakati nasoma, walikuja akina Hamida, mama yake na mama mkubwa kwa nje (koridoni)/walikuwa wananisikiliza...

Hamida akaingia na kuniambia...

"Ma shaa Allah hodari kumbe, mara hii umehifadhi!..."

"Kwani umenisikia?" Nilihoji

"Eeee, wote tumekusikia kasoro baba tu yeye hajarudi, tulijibanza kwenye korido"

"Namshukuru Mungu, lakini naamini ukinifundisha wewe, nitahifadhi kwa haraka zaidi" nilichombeza kwa sauti ya chini kidogo

"Mmh, makubwa" alisema huku akaondoka kwa kuwa mlango mkuu ulikuwa unasukumwa.

Aliyeingia alikuwa mzee Burhani.

"Assalaam aleikum yaa Jamaal" alinisalimu huku akiingia mle chumbani

"Wa aleikum salaam" nilimjibu.

"Sasa leo tujifunze namna ya kusalimia kwa kirefu" mzee alianza somo lake lisilo rasmi...

"Assalaam aleikum wa rahmatullah wa barakatu, hii ndiyo salamu bora kwa waja kusalimiana" aliendelea

"Maana yake ni kwamba, amani ya iwe kwenu na rehema za Allah na baraka zake" aliendelea

"Kujibu kwake ni, wa aleikum salaam wa rahmatullah wa barakatu, na maana yake ni kwamba, nanyi iwe kwenu hiyo amani, na rehema za Allah pamoja na baraka zake" kisha akaendelea.

"Kusalimia ni sunna, yaani ni jambo tulilohimizwa kufanya na ambalo Mtume (rehema na amani zimwendee) alikuwa akifanya" kisha akaendelea...

"Kujibu salamu ni fardhi, fardhi maana yake ni wajibu, hivyo ukisalimiwa ni wajibu kurudisha salaam. Usiporudisha unapata dhambi. Lakini usiposalimia hupati dhambi japo utakosa faida nyinginezo kama utakavyofundishwa siku za usoni" alimaliza na Yasir akawa anaingia...

"Haya, andika herufi zote kwa kufuatisha kama zilivyo kwenye kitabu, hakikisha unaziumba vizuri" Yasir aliniambia baada ya kusalimia.

Wakaniacha nikaendelea na uandishi, haikunichukuwa muda kumaliza, maana na herufi 30 tu. Nikawa tayari.

Muda wa swala ya isha tukaenda kuswali, tukarudi, pia siku hiyo nilikula hapo vyakula vizuri laini laini, ilikiwa tambi za nazi, mikate ya boflo na mchuzi wa samaki (koana) na vidubwashika vingine vidogo vidogo.

Mazungumzo yaliendelea, nikajiona ni kama sehemu ya familia ya mzee Burhani.

Saa nne kasoro niliaga na kuelekea nyumbani.

Kidogo kidogo ratiba zangu zilianza kubadilika.

'Maggot' ziendi tena, 'Tazara' siendi, 'Mboye' siendi, Sikinde tu tena Kariakoo ndio mara moja moja nilikuwa nahudhuria nikiwa kijana mwenye utulivu, ratiba za sinema zikapungua pia.
*********

Nilisomeshwa na Yasir kwa siku tatu tu, taarifa zilikija kuwa lori lake lipo tayari hivyo Alhamisi waliondoka yeye na Abdul kuelekea Kahama.

Siku hiyo ya alhamis nilifika kama kawaida kwa mzee Burhani majira ya saa kumi na nusu hivi, nilikaribishwa vizuri na mama mkubwa, kisha nikaingia chumba cha kusomea.

Mara mama Warda (mama yake Hamida pia) akaingia na kuniambia kuwa Yasir amesafiri leo, hivyo durusu aliyokufundisha, mzee akirudi atakufanyia utaratibu upate maalim wa kukuendeleza.

Nilimjibu kuwa hakuna neno, nitajitahidi kusoma kwa bidii.

Da, nakumbuka siku hii nilisoma kwa sauti ya juu kidogo ili walio vyumba vingine wasikie kama kuna sehemu nakosea basi wanisahihishe.

Nilisoma mara kadhaa na kumaliza nilipoishia na kurudia tena na tena, baadaye Hamida akaja na bilauli...

"Nimekuletea kinywaji kingine leo, ni juisi ya furusadi" alisema Hamida huku akinipatia...

"Bila shaka umeiandaa wewe" nilisema huku naipokea

"Hapana, hii aliandaa mama, mie leo nilitoka kidogo, nimerudi muda mchache kabla hujafika" alijibu

Kisha akaendelea...

"Halafu nimekusikiliza kuna sehemu unakosea kutamka..., siyo zwadi, ni dhwad, tamka kwa kujaza ulimi mdomoni..."

"Dhwad" nikajaribu,

"Enheee, hivyo umepatia" akaendelea

"Sasa rekebisha matamshi kwenye fatha'a, na fatha'a ten an, yaani kwenye dhwad."

Nikajaribu, nikaweza, akanipongeza kisha akaketi pembeni yangu kwa nyuma kidogo wote tukiangalia uelekeo mmoja na kuniamuru nisome kuanzia mwanzo...

Nikawa nasoma, na kila nilipokosea ananirekebisha papohapo...

Hali iliendelea hivyo hadi baba yake akaja na kukuta ananisomesha vizuri, akaingia akatuangalia kisha akatoka kwenda sebuleni.

Naye hakukaa muda mrefu akaenda sebuleni, mie nikawa naandika ili yakae vizuri kichwani.
IMG-20200125-WA0001.jpeg


James Jason
 
Back
Top Bottom