SEHEMU YA SABA
*******************
Alarm ya saa ya mezani iliniamsha saa kumi na mbili asubuhi, ndio nikajuwa kuwa nilikunywa kupita kiasi, turntable ilijizima yenyewe (changer), taa sikuzima, na nilishtuka nikiwa sebuleni kwenye kochi.
Kumbe niligigida mzinga wote wa Cognac Brandy. Kichwa kilikuwa kizito, na ilikuwa Jumanne.
Niliamka kujiandaa kwenda kazini.
=
"Habari za asubuhi Marry?" Nilimsalimia mhudumu ofisini kwangu .
"Nzuri boss, karibu" alinijibu huku akipokea mkoba wangu mdogo.
"Leo najisikia vibaya kidogo, hivyo napumzika ofisini kwangu hadi saa nne, baada ya hapo utaruhusu watu kuonana nami" nilimwambia.
"Sawa boss" alijibu huku akiendelea na usafi.
Niliingia ofisini na kukaa kwenye dawati langu huku nimeinama.
"Karibu chai boss" Marry alinistua...
"Oh, ahsante, eeeeh hebu nenda pale mgahawani kaniletee supu maridadi" nilisema huku nikijiweka sawa.
Nikaiangalia ile chai, nikaona haipandi kabisa asubuhi ile. Hivyo nikaanza kupekua mafaili yangu wakati nikisubiri supu, huku nawaza mambo mawili makuu, kusilimu na kuanza kumtongoza Hamida.
******
Haikupita muda mrefu nikaletewa supu ya ng'ombe ya moto safi kabisa, nikainywa na kula nyama, nikaanza kujisikia ahueni.
Niliendelea kufanya kazi kivivu vivu huku nikiwaza mengi kichwani...
Niliwaza jinsi harusi za kwetu utaturuni zinavyokuwa, niliwaza jinsi wanawake wa kitaturu wanavyojuwa kuwanyenyekea wanaume, niliwaza kuhusu sherehe zinavyokuwa, niliwaza msisimko wa nyimbo na hamasa zenye kuamsha hisia kali... Ilimradi niliwaza mambo mengi kuhusiana na mambo ya harusi.
"Kweli sasa nimekua" nilijikuta nasema kwa sauti.
"Vipi boss, leo mbona uko hivyo? siyo kawaida yako!" Marry aliniuliza alipokuja kuchukuwa vyombo pamoja na kuleta mafaili mengine ya kuyapitia...
"Eeeeh, nafikiri muda wangu wa kuoa sasa umewadia" nilimjibu huku nikitabasamu
"Heheeee!" Alicheka kiumbea
"Vipi, huamini?" Nilimuuliza huku natabasamu
"Hapana, naamini ila najiuliza ni nani huyo aliyekukamata hadi umetangaza ndoa" alisema.
"Hapana, sijatangaza ndoa, wala mchumba mwenyewe hajui kama atatongozwa..." Nikasita kidogo kisha nikaendelea...
"Nataka nioe Mwarabu" nilimalizia.
"He!" Alishangaa na kuondoka.
**********
Marry ni mfanyakazi hodari sana, ni Katibu muhtasi wa siku nyingi (nilimkuta kazini) na anapenda sana utendaji wangu.
Huwa namshirikisha mambo yangu mengi, na huwa ananishauri vizuri.
=
Jioni baada ya kutoka kazini moja kwa moja nilielekea kwa Alimaua kumtembelea mzee Katibu Kata.
Nilimkuta ana nafuu sana kuliko juzi yake. Nikamweleza maamuzi niliyofanya ya kuanza kubadili dini na kisha kuanza kumpa maneno ya mapenzi mchumba mtarajiwa.
Alifurahia uamuzi wangu wa kuamua kuingia katika 'dini yake', lakini hakuwa na matumaini kama nitafanikiwa kumuoa Hamida kwa jinsi alivyokuwa anazifahamu familia za Kiarabu.
*****
Mzee Burhani ana asili ya Oman, Babu yake alikuja miaka mingi kabla ya uhuru, alikuwa anaishi kisiwani Unguja. Baba yake mzee Burhan marehemu alhaj Ahmed Said alihamia Dar es Salaam katika harakati za kibiashara na yeye mzee Burhani alizaliwa hapo Dar.
Mke wake ni half-cast wa kingazija na kihindi, yaani baba yake alikuwa mgazija na mama yake alikuwa ana asili ya kihindi waliolowea Comoro.
Mchangachiko huo ulitoa matunda mazuri ya watoto wa kike ambaye kitinda mimba wao ndio nafikiria jinsi ya kumuingia na kumtongoza.
Kaka yake Hamida aitwaye Yasir pamoja na rafikiye Abdul wote ni madereva wanaendesha malori (Scania 81). Wiki hiyo magari yao yalikuwa Kibaha (Sub-Scania) kwa ajili ya service kubwa, ndiyo maana walikuwa wanaonekana mjini muda mwingi.
Warda ameolewa na mtoto wa baba yake mdogo, yupo Mwanza, Sabra ameolewa pia na ndugu yao wapo Oman, Yasir bado hajaoa.
********
Tuliongea mengi na mzee Katibu Kata, akanitia moyo japo alikuwa anahisi 'nitagonga mwamba' katika harakati zangu za kumchumbia Hamida.
Nilivyotoka Mwananyamala moja kwa moja nilielekea nyumbani, baada ya kupumzika nilielekea Butiama Restaurant, tayari ilikuwa jioni, nilienda kwa mzee Burahan kurudisha 'coolbox' yao, na kuchukuwa juisi nzuri ya mikomamanga iliyochanganywa na embe ng'ong'o.
Aliyenipokea alikuwa Yasir, kaka yake Hamida, alipokea lile boksi kisha akamwita Hamida apeleke jikoni.
Hamida alivyokuja alinikuta bado nimesimama ukumbini (koridoni)...
"Huingii varandani leo" Hamida aliuliza huku anakuja
"Hapana, leo nina haraka..." Kabla sijaendelea alinikatisha...
"Basi subiri nikuletee juisi" alisema.
"Sawa" nilimjibu.
Punde si punde alirejea dumu la lita 3 lililojaa juisi. Nilipokea na kumlipa, nilijifanya sina stori siku hiyo, nikaaga na kuelekea home.
*******
=
Siku tatu baadaye jioni nilipotoka kazini, ilikuwa siku ijumaa, nilitoka mapema kuliko kawaida yangu...
"Naenda kwenye mawindo ya binti mwarabu" nilisema baada ya kumuaga Marry.
"Haya boss, usinisahau kwenye kamati ya maandalizi..." Alijibu kuhu akitabasamu.
Nikaenda nyumbani moja kwa moja, nikaoga na kubadili nguo, (nilivaa 'bora shoes', suruali ya kitambaa, tshirt nyeupe) nikatoka nikaenda moja kwa moja hadi Africa Studio, nikakuta picha zipo tayari (black & white), zilikuwa zimetoka vizuri mno. Wakaziweka kwenye bahasha (B5) nyeupe, nikamalizia malipo nikaelekea Shibam.
Pale Shibam sikumkuta mzee Burhani, niliwapiga round moja ya kahawa kisha nikaelekea nyumbani kwa mzee Burhani.
Nilikaribishwa vizuri na yule mama wa kiafrika na kuingia sebuleni. Sebule yote nikaibadilisha harufu na kuanza kunukia uturi (perfume) ya Gift of Zanzibar. Ilikuwa inanukia vizuri sana, kama udi hivi lakini siyo, kama asmini hivi lakini siyo, ilimradi ni harufu isiyochosha wala kukera.
Baada ya kusalimiana, nikamkabidhi lile dumu la juisi, halafu nikamwambia kuwa nina shida na mzee.
Akanijibu mzee yupo chumbani kwa Hamida wana mazungumzo na wanawe.
"Kuna posa (ya maneno) imeletwa ndio wanajadili mzee, mama Warda, Hamida na Yasir." Alisema.
Ghafla moyo ukaanza kunidunda kwa nguvu, nadhani hata yule mama aligundua.
"Sawa mama, nasubiri wakimaliza watanikuta" nikamjibu.
"Basi ngoja nikuletee kinywaji chako ukipendacho" alisema huku akiinuka
"Sawa mama" nilijibu.
Aliniletea bilauli iliyojaa togwa baridi, akavuta stuli na kuniwekea.
"Karibu" alinikaribisha.
"Ahsante mama" nilisema kisha nikaweka bahasha yangu kwenye stuli.
Nikaanza kunywa mdogo mdogo huku nikiwa na mawazo.
Akatoa ukimya kwa kuniuliza, imekuwaje nalipenda togwa, nilimjibu nilijifunzia kunywa Iramba ambako ni kinywaji cha kawaida.
Akahoji "wewe ni mnyiramba"
Nikamjibu "hapana"
"Mnyaturu?"
"Hapana"
"Ishi, sasa wewe ni kabila gani?" Aliuliza.
"Mimi ni Mtaturu" nilimjibu
"Ahaaaa, nyie ndio Mang'ati eee" alisema kwa kutania
"Hapana, ila tunashabihiana sana, wote asili yetu ni Ethiopia, lakini mababu zetu walihamia miaka mingi sana maeneo ya Arusha - Manyara (wakati huo Manyara ilikuwa sehemu ya Arusha)
" Ahaaa, ndio mkaanza kuwaibia wamasai ng'ombe zao eeee!" Alitania
Nikacheka kisha nimasema "Hapana, sisi ndiyo tulikuja na mifugo kutoka Ethiopia, babu zetu walikuwa wakibadilishana mifugo na wenyeji kupata ruhusa ya kukaa sehemu kabla ya kufika ardhi waliyoipenda ambapo ni kandokando ya ziwa Eyas. Hivyo zote hizo ni ng'ombe zetu...." Nikacheka tena kisha nikaendelea, "Hata zile za Usukumani ni za kwetu pia" nilitania...
Nilikuwa nadhani yeye ni msukuma kwa lafudhi yake wakati anaongea.
"Unafikiri mie msukuma, mie ni Mnyamwezi" alisema na kucheka kiasi
Nami nikacheka. Hakika aliniondoa kwenye mawazo yaliyotaka kuniteka ghafla.
"Basi togwa hilo ni la Tabora" alisema,
"Mie ndio nimewafundisha humu ndani kulitengeneza, niko nao hawa tangia usichana wangu hadi sasa, kuna wakati niliondoka nikaolewa nikazaa watoto 7, lakini ndoa haikuwa ya furaha sana, nikaomba talaka, ndipo niliporudi hapa hadi sasa." Alisema huku akionesha huzuni kiasi.
"Du, pole sana", nilimwambia, na kumuuliza watoto wake wako wapi.
Alinijibu kuwa wote wapo Tabora kwa baba yao.
Mazungumzo yetu yalikatishwa pale Yasir alipoingia sebuleni, alisalimia na kuketi. Haikupita muda mama Warda naye akaingia, tukasalimiana, kisha akatania "umefuata ice cream na leo?", nikamwambia hapana, leo nina shida nyingine na mzee, mara mzee naye akaingia. Tukasalimiana kisha akasema "samahani, nimekusikia umekuja muda kidogo, lakini tulikuwa tuna mazungumzo ndani, binti yangu ameposwa, lakini hataki kuolewa ndiyo tulikuwa tunayajenga..."
Da! Kimoyomoyo nilifurahi sana, nikaona hii ni dalili njema kwangu, hofu na wasiwasi juu ya kumkosa Hamida ikaniondoka.
"Ahaa, haina neno, mie nilikuwa na mama huyu sikuwa mpweke" nilijibu.
"Naam, twaib, nakusikiliza, au ni faragha niwaombe hawa watuachie nafasi?" Mzee Burhani alisema.
"Hapana, siyo siri, nimekuja naomba unisilimishe, nimeshakata shauri" nilisema.
"Allahu akbar" alisema mzee Burhani.
"Hamidaaaa" mzee Burhani alimuita binti yake.
Mara Hamida akaingia, kimyakimya, macho mekundu, sura imemvimba kama alikuwa analia. Akaketi jirani na yule mama wa kiafrika.
Pakawa na ukimya fulani hivi wa sekunde chache, kisha mzee Burhani akakata ukimya kwa kusema...
".... Eeeh bila shaka nyote mnamfahamu James, wiki iliyopita tulikuwa hapa tunazungumza, alikuja kuomba muongozo akitaka kusilimu. Nilimpa mawili matatu na leo amekata shauri na kutaka kusilimu."
Alitulia kidogo kisha akaendelea...
"Binadamu wote kwa asili tunazaliwa waislamu, lakini wazazi wetu ndio hutubadili dini na kufuata dini nyingine ama kubaki katika dini ya asili ambayo ni uislamu..."
Aliendelea na hotuba isiyo rasmi...
"Uislamu ni Amani, kama lilivyo neno lenyewe, ni kujisalimisha kwa Mola Muumba wa mbingu na nchi na kunyenyekea kwake, hivyo basi umefanya uamuzi sahihi kurejea katika dini ya asili ambayo ina mfumo mzima wa maisha ya mwanadamu wa namna ya kuyaendea mambo yake hapa duniani, kaburini, siku ya ufufuo na hukumu na baada ya hukumu." Alisimama kidogo kumeza mate kisha akaendelea...
"Shahada mbili ni mkusanyiko wa matamko mawili ya ahadi anayoichukua kiumbe (mwanadamu) mbele ya Muumba wake na viumbe wenzake; mbapo mtamkaji hula kiapo cha utii kwa Mwenyezi Mungu (Allah) na Mtume wake katika maisha yake yote kwa kufuata maamrisho na makatazo yake."
"Shahada ya kwanza ni tamko la utii kwa Allah, na shahada ya pili ni tamko la utii wa mtume wa Allah..."
"Sasa nitasema maneno nawe utafuatisha..."
Nikaitikia sawa.
"Nitaanza kusema kwa kiarabu kisha tutarudia kwa kiswahili ili uelewe maana yake" alisema, kisha akaanza kutamka...
Wakati huo wote sebuleni palikuwa kimya, nami namsikiliza mzee Burhani kwa makini huku nikiibia kumuangalia Hamida, alikuwa amejitanda uso wote kwa mtandio kasoro macho tu ambayo yalionekana kuwa mekundu kuliko kawaida.
“ASH-HADU"
Nikafuatisha,
(Ash-hadu)
"AN LAA"
(An-laa)
"ILAAHA"
(Ilaaha)
"ILLAL-LAAHU”
(Illal-laahu)
“WA ASH-HADU"
(Wa ash-hadu)
"ANNA MUHAMMADAN"
(Anna Muhammadan)
"RASUULU LLAH”
(Rasuulu llah)
"NASHUHUDIA KWA MOYO NA KUTAMKA KWA ULIMI KWAMBA"
Nikaendelea kufuatisha...
(Nashuhudia kwa moyo na kutamka kwa ulimi kwamba)
"HAKUNA MOLA APASWAYE KUABUDIWA KWA HAKI ISIPOKUWA ALLAH"
(Hakuna Mola apaswaye kuabudiwa kwa haki isipokuwa Allah)
"PIA NASHUHUDIA KWA MOYO NA KUTAMKA KWA ULIMI KWAMBA"
(Pia nashuhudia kwa moyo na kutamka kwa ulimi kwamba"
"MUHAMMADI NI MJUMBE WA ALLAH"
(Muhammad ni mjumbe wa Allah)
"kama alivyo Yesu, Mussa, Ibrahimu" alimalizia kisha wote mle ndani wakasikika wakisema, Allahu akbaru, Allahu akbaru, Mungu ni Mkubwa, Mungu ni Mkubwa.
Walisema maneno hayo (Allahu akbaru) hata kabla sijayafuatisha maneno ya mwisho ya mzee Burhani.
Kisha nikamuona Hamida, Yasir na mama Warda wanalia kwa kutokwa na machozi bila kutoa sauti...
Pakawa na ukimya kidogo...
Nikawa nawaza, hivi hawa wanaolia, wanalia kwa sababu nimesilimu ama kuna jambo jingine!
Nilikuja kujuwa baadaye sana wakati mtu mwingine aliposilimu nikishuhudia, kuna hali fulani ya utii na unyenyekevu wa imani (emotions) hujaa...
"Sasa James umeshakuwa mwislamu, inabidi uchague jina zuri ulipendalo ili uitwe kwa jina hilo" mzee Burhani alitoa ukimya uliokiwepo.
Tayari kichwani nilikuwa nina jina nililolipenda ambalo lilianzia na herufi J kama jina langu.
"Jamaal" nilitamka
"Maa shaa Allah, Jamaal maana yake ni mzuri, wa kupendeza yaani handsome..." Alidakia mzee Burhani.
"Kuanzia sasa tutakuwa tunakuita Jamaal" aliendelea...
"Sasa kuna mambo muhimu ambayo unapaswa kujifunza ili uyajuwe ukishakuwa mwislamu, nitakupatia vitabu ili uweze kujisomea mambo muhimu, yameandikwa kwa kiswahili pia vipo vitabu vya kwa lugha ya kiingereza..." Aliendelea
"Kwakuwa wewe ni mtu mzima, inabidi upate mafunzo ya dini kwa njia tofauti siyo kama watoto wanavyofundishwa, chaguwa siku za kujifunza nami nitakutafutia mwalimu"
Nikamjibu
"Mie nipo tayari siku nne kwa wiki, yaani Jumatatu hadi Alhamis baada ya kutoka kazini nakuwa huru, hivyo nakusikiliza wewe mzee"
"Yasir hebu kalete kile kitabu cha swala na mafundisho / maamrisho yake" mzee Burhani alimwambia kaka yake Hamida
"Naona muda wa swala umewadia, sasa twende wote msikitini" alisema mzee Burhani huku akiwa mwenye furaha.
Mie sikuwa na hofu wala kipingamizi, nilishayavulia nguo maji inabidi niyaoge.
Yasir alirudi na kitabu kidogo kiitwacho Sala na maamrisho yake na kunipatia.
Kwakuwa kilikuwa kidogo sana, nilikiingiza mfukoni mwa suruali.
Mzee Burhani akasimama, nami nikasimama tukatoka tukawa tunaelekea msikitini. Tulielekea msikiti wa Mkauni, siyo mbali kutoka kwa mzee Burhani.
Nyuma yetu Yasir alitufuata, tukawa tunaambatana naye, tulivyofika msikitini, tukavua viatu kama kawaida, tukavihifadhi sehemu ya kuhifadhia, kisha mzee Burhani akamwambia Yasir anifunidishe namna ya kuchukuwa udhu ili niwe tayari kwa ibada ya swala.
Yasir alinielekeza msalani, baada ya kutoka msalani akanipeleka sehemu maalum ya kutawadhia (kuchukuwa udhu), yaani kuosha viganja vya mikono, kusukutua, kusafisha pua, uso, mikono yenyewe hadi viwikoni, kupaka maji kwenye kichwa na masikio kisha kumalizia na kuosha miguu.
Nilifanya kwa kumuigiza afanyavyo, tulipokuwa tayari tuliingia ndani tayari kwa ibada...
Baada ya kuswali (inachukuwa dakika tano hivi) nikasikia tangazo...
"Kuna kijana amesilimu, alikuwa akiitwa James Jasson na sasa ataitwa Jamaal Jason, alikuwa dhehebu la Roman Catholic, tunamuomba asimame ili waislamu tumuone tumjue kuwa ni ndugu yetu katika imani"
Ni imamu (kiongozi wa ibada) alikuwa akitangaza.
Wakati nainuka nilisikia Allahu akaru nyingi hadi nilisisimkwa mwili, nikaombewa dua, kishwa waumini wakaambia wawe wananisaidia katika mambo ya ibada na kadha wa kadha.
Baada ya tasbihi (kama kusoma rozali vile) na dua, watu walianza kutoka, mzee Burhani alikuwa anaongea na Imamu, bila shaka ndiye aliyempa taarifa za kusilimu kwangu.
Kisha nikaona mzee Burhani amesimama tena peke yake akawa anaswali.
Mie na Yasir tukatoka nje tukawa tunamsubiri.
"Eti, mbona nilimuona Hamida akilia, kulikoni" niliuliza kiuchokozi
"Aaaa ni stori ndefu nitakuhadithia kesho in shaa Allah" alijibu kifupi namna hiyo, na mara mzee Burhani akawa anatoka nje.
Tulirudi wote hadi nyumbani kwa mzee Burhani, lakini sikuingia ndani, bali niliagana nao nikapanda batavuz yangu huyooo hadi Butiama restaurant, kisha nyumbani.
**********
Nilivyofika nyumbani nilikipitia kile kitabu na kuona yaliyoandikwa, ni kitabu kidogo sana unachoweza kusoma kwa saa chache tu.
Nilikuta misamiati mingi ambayo sikujuwa maana yake mara moja, lakini kilikuwa kinaeleweka vizuri tu.
Baada ya kujimwagia maji na kujifuta, nikajilaza kitandani chalichali nikiwa nimevaa bukta huku nikitafakari safari ambayo nimeianza.
Nikawa nawaza, hapa pombe tena basi, kuzini tena basi nk hadi nikapitiwa na usingizi.
********
Sikwenda sinema ijumaa hiyo kama ilivyo kawaida yangu. Kesho yake mapema sana nikaenda kwa mzee Katibu Kata, niliwahi ili asije kuondoka nyumbani kabla.
Nilimueleza habari yote ya kusilimu kwangu, akafurahi sana, tukabadilishana maneno mawili matatu kisha nikamuaga huyooo hadi nyumbani.
Niliendelea na shughuli ya usafi hadi niliposikia adhana, nikaacha, nikajitayarisha kwenda msikitini. Kutoka nyumbani hadi msikiti wa mkauni ni mbali kidogo kwa kutembea kwa miguu, hivyo niliwasha batavuz nikaenda.
Nikifuata utaratibu kama wa jana usiku hadi ibada ilipoisha nikatoka na kuelekea Butiama. Hakika Butiama Restaurant nimewachangia sana!
Baada ya hapo nilirudi nyumbani kumalizia usafi na mambo mengine.
****
Saa kumi baada ya swala ya alasiri nilienda Shibamu, siku za Jumamosi watu huwa wengi wakijiburudisha kwa michezo mbalimbali.
Mara mzee Burhani akawasili...
"Ahaaaa sheikh Jamaal, upo?" Alisema baada ya kusalimia watu waliokuwepo pale...
"Jamani eee, kuanzia jana huyu James sasa tumuite Jamaal, amesilimu." Alisema
Allahu akbaru, watu waliokiwepo pale walisema maneno hayo kwa kurudia mara tatu.
"Karibu sana Jamaal" mzee mmoja maarufu sana kijiweni hapo alisema.
Mzee Burhani akaniambia, mwalimu wako wa awali atakuwa mwanangu Yasir, wiki hizi mbili yupo tu anasubiri gari iwe tayari, iko service kubwa.
Sasa basi Jumatatu utaanza naye hadi atakapoondoka kisha nitakuwa nimeshapata mwalimu utakaye endana naye kukusomesha mambo muhimu.
Tuliongea palee hadi magharibi ilipofika, baada ya swala akanikaribisha kwake kwa chakula cha usiku.
"Umri wako unaruhusu kuoa, utakula hotelini mpaka lini" alitania
"Bado natafuta mke muafaka" nilijibu...
Tuliendelea na mazungumzo ya dini hadi ilipowadia muda wa swala ya isha. (Swala ya saa mbili usiku)
Baada ya kuswali, tulirudi nyumbani kwa ajili ya chakula cha usiku.
*****
Sebuleni kuliandaliwa chakula kizuri sana, kulikuwepo viazi mbatata (viazi mviringo), sijui hata wamevifanyaje, maana ni vilaini pia vina kama mbogamboga (nilijuwa baadaye kuwa ni kachori), mchuzi wa nyama ya ng'ombe pamoja na nyama yenyewe, chapati maridadi sana, sikuwahi kuziona kama hizo kabla, wali uliopikwa kwa nazi, mchuzi shatashata wa kamba / kaji (prowns), chai ya maziwa na ya mkandaa (black tea), kisamvu kilichokolea nazi.... Bila kusahau pembeni kulikuwa na jagi la maji ya kunywa.
Mtihani ukawa namna ya kukunja miguu wakati wa kula maana pameandaliwa kwenye busati juu yake paliwekwa mkeka.
Baada ya kujikunja vizuri nikifanikiwa kukaa ipasavyo, ni mkao unaoweza kukaa hivyo kwa muda mrefu bila kuchoka (miguu inakunjwa kwa kupishana kama unaikalia lakini huikalii)
Kwa kuwa sebule ilikuwa kubwa sana, kuliandaliwa sehemu mbili, jirani na pazia la mlango walikaa mama wa Kiafrika, Hamida, Nadya na mama Warda, na upande mwingine tulikuwa mimi, Yasir na mzee Burhani.
Mie nilikaa kwa namna ambayo nilikuwa naangaliana uso kwa uso na Hamida japo kuna ka-umbali hivi.
Nilishazoea kula kwa kijiko, leo najifunza kula kwa mikono, nilisema hivyo wakati Yasir akinimwagilia maji ya kunawa...
"Utaweza tu Jamaal" alijibu.
Sikutaka kuanza kula wali kwa kuwa nimeshauzoea, nilianza kula chapati kwa mchuzi na chai, [emoji39] Hakika kuna watu wanajuwa kupika jamani... Nilijikuta nasema tu kwa sauti...
Nilivyomaliza chapati moja nikahamia kwenye kachori, dah, tamu sana, zina pilipili kwa mbaali, mwisho nikapakuwa 'tuwali' kiduchu ili nimalizie, loh salaleh, kumbe bwana ule wali ndio funga kazi, nikaongeza mwingine mwingi...
Mchuzi wake sasa na prouwns waliokaangwa na kumenywa kisha kuungwa kwa nazi nzito, acha kabisa..., utamu wa kisamvu sijawahi kula popote pale... (Kilitwangwa jana yake na kuchemshwa kwa viungo muafaka, leo ndio kimeungwa vizuri kwa nazi, hii aliniambia Hamida siku nyingine kabisa nilivyomuuliza)
*****
Baada ya kula, tukawa tunazungumza mambo ya kawaida, hali ya uchumi wa nchi, kupungua kwa bidhaa muhimu nk
Wakati huo Hamida alikuwa bize akiondosha vyombo...
Aliporudi alikuja na bahasha yangu niliyoishau jana (kwa makusudi)
"Jana ulisahau mzigo wako" Hamida alisema huku akinipatia bahasha ambayo tangia awali sikuwa nimeifunga kwa lengo maalum.
"Ooh, ahsante, nilishasahau kama zipo hapa" nilijibu
Lengo langu lilikuwa Hamida anione vizuri kwakuwa mara zote niwapo hapo huniangalia kwa kuibia ibia tu.
*******
Niliaga, Yasir akaniambia ngoja nikusindikize....
Nilikokota batavuz huku tukielekea maeneo ya Shabam kutokea nyumbani kwa akina Hamida...
Njiani wakati tunaongea mawili matatu ndipo nikachomekea kuhusu kulia kwa Hamida...
Akanieleza kuhusu posa iliyokuja kutoka Oman, na kwamba muoaji alikuwa mtu mzima sana lakini tajiri... Hamida alikuwa hataki kuolewa na mtu mzima hivyo walikuwa wanajaribu kumsihi akubali kwani ndiyo posa ya kwanza na umri wake ulikuwa umewadia kuolewa...
Hamida alimaliza kidato cha nne miaka miwili iliyopita kisha akaenda Kenya kusomea stashahada ya domestic science na catering (Kenya Utalii College - Campas ya Mombasa).
"Du" nilisema
"Lakini yafaa apewe uhuru wa kuchaguwa ampendaye, kama hamtaki msimlazimishe, asije akachukuwa maamuzi mabaya" nilisema
Kipindi hicho mabinti kusaga chupa na kumeza kwa ajili ya kujiua ilikuwa tabia iliyoshamiri sana.
Tuliagana yeye akarudi na mie nikapanda batavuz yangu hadi home nikiwa na furaha sana kwa kupiga hatua nyingine kwenda 'mbele'.
*******
Itaendelea
James Jason