Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan alifanya uteuzi wa mabalozi 23, miongoni mwa mabalozi wateule hao wamo Hoyce Temu( 43) aliyewahi kuwa Miss Tanzania mwaka 1999, Togolani Mavura ambaye ni msaidizi wa Rais wa Awamu ya Nne Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, Macocha Tembele aliyewahi kuwa Msaidizi wa Hayati Benjamin William Mkapa na Kaimu Idara ya Ushirikiano wa Kikanda, Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki na Luteni Jenerali Yakub Hassan Mohammed ambaye ni Mnadhimu Mkuu wa Jeshi la Wananchi wa Tanzania JWTZ.
Kati ya wateule hao 23 wa Rais Samia Suluhu Hassan wateule wawili wameonekana kugusa akili za watu wengi sana katika mitandao ya kijamii, hawa ni Hoyce Temu na Luteni Jenerali Yakub Mohammed.
Kwa lengo la kufahamu kuhusu uteuzi wa Hoyce Temu na Lt. Jen Yakub Mohammed katika jicho la kidiplomasia ni vema tukafahamu tafsiri ya Balozi.
Balozi ni "mwakilishi anaetumwa na Mkuu wa nchi, Serikali ama taasisi ya kimataifa kwenda kumuwakilisha Rais, mkuu wa serikali au taasisi au nchi inayomtuma katika nchi inayompokea."
Mabalozi hufanya kazi zao kwa mujibu wa Mkataba wa Vienna wa mwaka 1961 unaohusu Mahusiano ya Kidiplomasia (Vienna Convention on Diplomatic Relations of 1961) ambapo kazi za ubalozi zimeelezwa katika Ibara ya 3.
Wanapokuwa katika nchi walizotumwa mabalozi huwa na kazi za kukusanya taarifa mbalimbali na kuzituma nyumbani sambamba na kulinda maslahi ya Tanzania na watanzania katika nchi wanazowakilisha.
Lakini si mabalozi wote huteuliwa na kutumwa katika nchi mbalimbali duniani, wapo ambao huteuliwa na Mheshimiwa Rais na kuendelea kufanya shughuli zao hapa nchini.
Ili kufahamu hili ni vema kwanza tuangalie uteuzi wa mabalozi, huwaje?
Mabalozi kama walivyo wateule wengine huteuliwa kwa mujibu wa katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 sambamba na marebisho yake yote. Ibara ya 36 (2) ya Katiba inasomeka kama ifuatavyo:
"Rais atakuwa na madaraka ya kuteua watu wa kushika nafasi za madaraka ya viongozi wanaowajibika kuweka sera za idara na taasisi za Serikali, na watendaji wakuu wanaowajibika kusimamia utekelezaji wa sera za idara na taasisi hizo katika utumishi wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano, nafasi ambazo zimetajwa katika Katiba hii au katika sheria mbalimbalizilizotungwa na Bunge kwamba zitajazwa kwa uteuziunaofanywa na Rais."
Katika muktadha wa uteuzi wa mabalozi unatokana na katiba na Rais huweza kumteua yeyote kuwa balozi itakavyompendeza kwa kuzingatia vigezo mahsudi. Kwa kawaida huwa kuna mabalozi wa aina mbili:
(1) Wanaoteuliwa kutokana na utashi wa kisiasa (Political Appointees/Diplomats)
(2) Wanaoteuliwa kutokana na weledi wao (Career Diplomats).
Katika teuzi za aina zote hizo mbili hufanyika kwa siri kubwa mno ambapo kama mteule anatokana na weledi wake kwenye diplomasia yaani kutokana na kuwa Afisa wa Wizara ya Mambo ya Nje (FSO), jina lake hupelekwa kwa siri na Wizara Ikulu na pia kama hatokani na kuwa Afisa wa Wizara ya Mambo ya Nje jina hupelekwa kwa siri na idara ya Usalama wa Taifa kwa ajili ya kuchunguzwa ama kufanyiwa vetting.
Hawa wanaoteuliwa kutokana na utashi wa kisiasa huwa ni pendekezo la Mheshimiwa Rais moja kwa moja kutokana na atakavyoona inafaa kwa kuzingatia wakati, mahitaji, taaluma katika eneo fulani, malengo na mazingira yanayozunguka hali ya halisi ya dunia kwa wakati huo.
Kwa mfano Rais huweza kuteua Balozi mwenye taaluma katika eneo la Ulinzi na Usalama hapa mara nyingi utakuta Rais akiwateua maafisa wa wa juu wa Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) au Jeshi la Polisi kuhudumu nchi ambazo zina changamoto za kiusalama kama vile Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), Burundi n.k, lakini pia maafisa hao wa jeshi huweza kutumwa katika nchi zilizo kimkakati kama Urusi, Misri, Afrika Kusini na Rwanda.
Si rahisi kwa mtu ambaye si mwanajeshi kuhudumu katika nchi zenye migogoro au vita au zilizo kimkakati zaidi ambapo kunahitaji utaalamu wa masuala ya vita, migogoro na stratejia ili aweze kumsaidia Mheshimiwa Rais kwa urahisi. Ndiyo maana tunaona Balozi wetu kule Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo ama DRC ni Afisa wa Juu wa Jeshi Luteni Jenerali Meela.