Jina Guinea lilitokana na nini kwanini nchi 5 zijikute zina Guinea kwenye majina yao?
Kijiografia Guinea ni eneo la Afrika Magharibi, Ghuba ya Guinea.
Makoloni mengi ya Ulaya katika eneo hilo yalijipa majina kama Guinea ya Ufaransa, Guinea ya Ureno, Guinea ya Uhispania, na Guinea ya Ujerumani.
Nchi hizo zilipopata uhuru wao kila mmoja alibakiza jina la Guinea kwa namna moja au nyingine. Guinea ya Ufaransa ikawa Guinea. Guinea ya Ureno ikawa Guinea-Bissau. Guinea ya Uhispania ikawa Equatorial Guinea.
Kihistoria inasemekana neno Guinea linatokana na neno la Kireno Guiné ambalo liliibuka katikati ya karne ya 15 kurejelea nchi zinazokaliwa na Guineus. Pia, Wareno walitumia neno na msemo wa watu kutoka Afrika Kaskazini (Berber) "aginaw" na "Akal n-Iguinawen" wakimaanisha "mweusi" na "ardhi ya watu weusi". Msemo huu waliutumia kuwatambua watu wa Guinea. Kuna maneno mengine ya kibaguzi kama "Ghinawen" wakimaanisha "watu walioungua" walitumia neno hili kutokana na ngozi nyeusi waliyokuwa nayo watu wa Guinea.
Wareno walifika Guinea katika karne ya 15, ndiyo ukawa mwanzo wa kufanya biashara na Ulaya kwenye pwani ya Guinea. Dhahabu, pembe za ndovu na watumwa walibadilishana kwa bunduki na bidhaa nyingine za Ulaya.
Lakini pia, Guinea lilikuwa ni jina la sarafu ya Uingereza. Ni sarafu ambayo ilitengenezwa kati ya 1663 na 1813. Dhahabu iliyotumika kutengenezea guineas za kwanza ilichimbwa katika eneo la Guinea.
Ajabu ni Papua New Guinea. Kisiwa hicho kiliitwa Papua mwanzoni, baada ya jina lake la asili. Wamagharibi wa kwanza kufika huko walianza kukiita kisiwa hicho "Guinea Mpya" kwa sababu walidhani wenyeji wa huko walitokea Guinea kwakuwa walikuwa wakifanana na Waafrika weusi.
Nahodha na mwanajiografia wa Ureno António Galvão aliandika kwamba: "Watu wa visiwa hivi vyote ni weusi, na wana nywele zilizojikunja, ambao watu wa Maluco huwaita Papuas." Maluco (Maluku Islands) ni visiwa vilivyopo huko Indonesia.
Papuwah (Papua) ni neno kutoka lugha ya Malay likiwa na maana "nywele zilizojikunja" (curly hair) na ndiyo lilitumika kuwatambua watu wa Papua ila baada ya Wamagharibi kufika huko wakawafananisha na watu weusi wa Guinea, ndiyo likapatikana jina New Guinea.
"Guinea Mpya" lilikuwa jina lililoundwa na Mhispania Yñigo Ortiz de Retez. Mnamo 1545, alibainisha kufanana kwa watu hao na wale aliokuwa amewaona hapo awali kwenye pwani ya Guinea ya Afrika.
Kwa maana hiyo majina yote Papua na New Guinea yanatumika kuitambulisha nchi ya Papua New Guinea.