Nahisi Manara na wanaomuunga mkono wana tatizo la kujua tofauti baina ya Msemaji wa Klabu, Mhamasishaji na Afisa Habari. Pengine hata wanaomlaumu nao wanafanya kosa hilohilo. Kwanza tunapaswa kutofautisha, kwa sababu Manara mwenyewe ameshindwa kutofautisha, baina ya Haji Manara na Msemaji/Afisa Habari wa Simba. Haji Manara hafungiki kutoa maoni yake binafsi kwenye swala lolote lile, lakini anapaswa kutoa angalizo mapema kabla ya kutoa kauli kama hiyo. Lakini anapaswa pia kuchunga kauli zake kama Manara, kwa kujua kwamba hata akitoa angalizo mapema, kauli yake yoyote tata lazima itaishia kuhusishwa na Simba kwa sababu yeye ni kiongozi wa Simba. Na Bado inatuwia vigumu kumhukumu dhidi ya matendo na maneno yake viwanjani na kwenye vyombo vya habari kwa sababu hatuelewi maelezo ya kazi (job description) yake. Msemaji wa klabu, mathalan anategemewa kutumia zaidi kalamu a mdogo waku kuliko kiuno chake, kwa hivyo hategemewi kuonekana ‘anamwaga radhi’ uwanjani mbele ya washabiki wa timu yake. Lakini mhamasishaji anakubalika kufanya hayo. Kadhalika Afisa habari, anategemewa zaidi kuwa msimamizi wa vyombo vya habari vya klabu (radio, TV, mitandao ya kijamii, n.k. na si kuwa ndiye mwenye mitandao hiyo ya kijamii au kuwa ndiye mtangazaji kwenye vyombo hivyo vya habari.