RAIS Samia Suluhu Hassan leo ataongoza waombolezaji kumzika Rais wa Serikali ya Awamu ya Tano, John Magufuli.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Uratibu, Bunge, Vijana na Wenye Ulemavu, Jenista Mhagama atamkaribisha Mwenyekiti wa Kamati ya Mazishi ya Kitaifa, Waziri Mkuu Kassim Majaliwa atoe neno la utangulizi likifuatiwa na salamu.
Salamu hizo zitatolewa wawakilishi wa makundi wakiwemo wazee wa Chato, vyama vya siasa, na viongozi wa nchi za nje. Salamu nyingine ni kutoka kwa vyombo vya ulinzi na usalama, Mahakama ya Tanzania, Bunge la Jamhuri ya Muungano, Rais mstaafu Jakaya Kikwete, Rais mstaafu Ali Hassan Mwinyi, na Rais wa Zanzibar, Dk Hussein Mwinyi.
Baada ya salamu, Rais Samia atahutubia waombolezaji na kisha ataongoza wananchi na wageni kutoka nje ya nchi kutoa heshima za mwisho kumuaga Rais Magufuli.
Baada ya tukio hilo, familia ya Magufuli ikiongozwa na mkewe Janet Magufuli, Rais Samia na viongozi watakwenda eneo la maziko nyumbani kwa Magufuli.
Saa 8:00 mchana mwili wa Rais Magufuli utaondolewa uwanjani na kupelekwa mazikoni ambako itafanyika ibada itakayoongozwa na Askofu wa Jimbo la Rulenge wilayani Ngara Mkoa wa Kagera, Severine Niwemugizi na kisha yatafanyika mazishi ya kijeshi.
Mazishi hayo ya kijeshi yatahusisha gwaride la mazishi na upigwaji wa mizinga 21 kutoa heshima kwa aliyekuwa Amiri Jeshi Mkuu wa majeshi ya ulinzi na usalama.
Tukio hilo litahitimisha safari ya mwisho ya maisha ya Rais Magufuli aliyefariki dunia Machi 17, katika Hospitali ya Mzena, Dar es Salaam alikokuwa akitibiwa ugonjwa wa umeme wa moyo uliomsumbua kwa zaidi ya miaka 10.
Pia soma>> Askofu Niwemugizi: Rais Magufuli aliagiza nirejeshewe Passport yangu na alisema 'Wewe ni Askofu wangu utanizika'