Shikamooo baba,
Ninaamini unalihisi joto japo kuwa huelewi linatokea wapi kutoka pale ulipo.
Joto hili linatokana na moshi,moshi unaofuka kutoka kwenye mto.
Mto huo ndiyo unaoutegemea ukupatie pumuziko nyakati zako hizi za mwisho kwenye maisha yako ya hapo nyumbani.
Nyumbani wameungana,wameshikamana na kukubaliana wauchome ili usilale wala kupumzika ili ukiweza kuishi uhame chumba na mtaa.
Nyumbani wanalalamika,wageni unawajali kuliko wanao,kwa faida ya nani?
Nyumbani umewatelekeza,hata ndani kwao umewazuia wasifanye chochote zaidi ya kuimba mapambio na ngoma za sifa.
Umeanza pia kuwapiga makofi ya machoni kisa tu wameimba taarabu na wengine kila kukicha unawatisha utawafukuza na bibi zao utawachapa bakora.
Mimi ni mwanao,nina marafiki,wamezama katika roho mpaka kule ambako kila mtu anapatamani afike,umechumbia wasio na vyeti,unawaacha wenye vyeti wasote mtaani kwao kwa kuwatenga mara ooh hawajasoma 'uchawi wa kizungu',roho inaniuma sana tena sana.
Hivi baba,wewe si ndiye ulisema ukishasafisha chumba chako ukawatoa buibui utaleta wasaidizi wapya,utapandisha neti chumbani kwetu? Imekuwaje?!
Miezi 36 inakatika,bado wewe unahangaika kutafuta mchawi,utaagua lini? Ugonjwa wako ni kuamini waganga wa kienyeji kuliko sisi uliotupeleka maabara za kileo,hatujui tukusaidie vipi?
Nyumba imechafuka,magodoro uliyoleta eti ni mapya....ha ha ha! Yana kunguni kibaaao.
Mzee wangu,zama zimebadilika,siyo kila homa ni maralia.
Kapime tu uhakikishe.Mto amechoma mjomba na ndugu zake akiwemo mama mdogo na yule mjomba mkubwa tena mkuuubwa kuliko wewe mara mia nne na themanini.
Kesho na keshokutwa hautalala maana hata nyumba wamekubaliana wauze baada ya kutalakiana na mama.
Lala baba,lala tu ......