Anga la washenzi na Joana anaona kitu usiku

Anga la washenzi na Joana anaona kitu usiku

*ANGA LA WASHENZI – 13*

*Simulizi za series inc.*


ILIPOISHIA...

Kabla Jona hajaanza kuwaza kuhusu lile gari, alikuwa anawaza kuhusu miwani yake kwanza. Alijua fika yeye pasipo miwani ni nusura kipofu. Miwani yake ndiyo macho yake, sasa itakuwaje pasipo nayo?

Ataweza pambana kwenye hii vita akiwa haoni? Alijikuta anajiuliza.

ENDELEA...

Hakutaka kukaa tena hapo kazini, akaondoka zake. Bila shaka safari hii ilikuwa ni kwenda kutafuta miwani ya macho.

Kwa muda kidogo ni kama kichwa chake kilikuwa kimechina. Hakutaka kukifikirisha zaidi. Alikua anatazamia tu ni wapi atapata miwani nzuri kwa ajili ya macho yake mabovu.

Alikuwa anahitaji miwani haraka iwezekanavyo alafu ndiyo mengine yafuatie. Akanyookea duka moja la mwarabu mzee katikati ya jiji, Kariakoo.

Ilikuwa ni ajabu kwa namna alivyoliteua duka hilo ingali alikuwa mhafifu wa kuona. Aliposhuka tu kwenye gari alijikuta mwili wake ukielekea uelekeo huo ambao haukuwa mgeni kwake.

Ni wazi huko nyuma alishawahi kuja kwenye duka hili kununua miwani.

Muuzaji wake alikuwa mzee wa kiindi mwenye ndevu nyingi rangi ya kahawia na baghalasia nyeupe ya nyavunyavu akivalia kanzu fupi rangi ya maziwa, pamoja na viatu vya wazi.

“Umewezaje kufika hapa pasi na miwani?” muuzaji alimuuliza akiinamisha mgongo wake na kunyoosha mkono kutwaa miwani fulani iliyokuwa imekingwa na zingine, ikipakana na kioo.

“Naenda kwa hisia kama jongoo!” Jona akatania, wakacheka. Alikabidhiwa miwani akaijaribisha kwa kujivesha.

Alikuwa anaona sawia! Bahati kwake alikuwa anajua vipimo vya macho yake na hata aina ya miwani anayotakiwa kuivaa hivyo hakujisumbua wala kumsumbua muuzaji.

Akailipia, ila kabla hajaondoka muuzaji akateka kidogo muda wake. Alikuwa mjawa wa simulizi mwenye maneno mengi japokuwa Kiswahili kilikuwa kinamtatiza hapa na pale.

Wakati Jona anapiga soga na muuzaji huyo, alikuwa anaangaza angaza huku na kule akifurahia uwezo wake wa kuona uliorejea.

Akiwa anaangaza angaza huko, akamuona mtu fulani aliyemtilia shaka. Alikuwa ni mwanamke mrefu aliyekuwa amevalia blauzi nyeupe, suruali nyeusi ya kumbana na viatu vyenye kisigino msawazo.

Hakufanikiwa kuona sura ya mwanamke huyu, ila aliamini kabisa alikuwa anamtazama yeye kwani aliukwepesha uso wake upesi punde tu alipotazama upande alipo – upande wa mashariki.

Alikuwa amevalia nywele ndefu feki ambazo ziliziba shepu ya kichwa chake na masikio. Pengine Jona angeviona hivyo vitu vingemsaidia kumng’amua mwanamke huyo.

Ni nani? Jona akajiuliza. Alipata tu hamu ya kuona sura ya mwanamke japo haikuwa kubwa. Hakuwa na mashaka kiasi cha kumfanya achukue hatua nzito.

“Nilisahau kukupatia risiti bwana Jona,” muuzaji alimgutua, akamtazama.

“Ahsante,” alijibu upesi akiikwapua risiti kisha akarudisha macho yake kwa yule mwanamke.

Hakumuona! Alikuwa amepotea.

Alitazama huku na huko lakini hakufanikiwa kumpata. Aliamua kupuuzia, akaaga na kwenda zake kujipaki kwenye gari. Akiwa sasa njiani akaanza kudadavua tukio lile la gari mark 2 kutaka kumgonga.

Akili yake yote iliamini tukio lile lilikuwa la kupangwa na si bahati mbaya, lakini ni nani analifanya? Nani yupo nyuma ya tukio hilo? Kwanini anataka kumfanyia hivyo?

Aliamini watakuwa ni wale watu waliokuwa wanamfuatilia mpaka nyumbani kwake, yani Miranda na Kinoo, japokuwa shaka lake lilikuwa sehemu moja – mbona hawakutumia gari lao, Range Rover sport?

Ila hiyo ilikuwa sababu ndogo sana kutia dosari kwenye ubashiri wake. Pengine gari limebadilishwa kuvunja ushahidi, ama basi wana magari mengi. Akili yake iliwaza.

“Nitajua leo,” akajikuta anafanya maamuzi.

Aliona sasa ni wasaa wa kukutana na adui yake uso kwa uso, macho kwa macho. Akashuka na kukwea gari jingine lililompeleka mpaka maeneo ya Kawe alipoteka bodaboda na kwenda moja kwa moja mpaka getini mwa makazi ya Miranda.

Akagonga geti mara tatu.

Mlinzi akafungua na kumtazama. Alikuwa ni mwanaume mrefu mweusi aliyekuwa amevalia sare zenye rangi nyekundu na nyeusi, pamoja na kofia iliyochoka, mkononi akibebelea kirungu.

Mwanaume huyu mlinzi alikuwa mgeni maeneo haya, bila shaka kama si jana yake basi ni juzi ndiyo aliwasili.

“Naweza nikakusaidia?” mlinzi aliuliza kwa sauti ya amri.

“Naomba kuonana na mwenye nyumba.”

“Una miadi naye?”

“Hapana. Ni dharura tu, kuna jambo muhimu nataka kuongea naye.”

“Kama hauna miadi naye siwezi kukuruhusu.”

“Nimekwambia ni dha …”

“Nimekusikia, na bila shaka nawe umenisikia. Siwezi nikakuruhusu kama hauna miadi!” mlinzi akasema akitoa macho yake mekundu.

Jona akasonya. Sasa alilazimishwa kufanya kitu ambacho hakikuwapo kwenye mipango kwakua hakuwa tayari kuona muda wake alioutumia kuja hapo unaenda bure.

Alidaka kichwa cha mlinzi kwa kutumia mkono wake wa kuume, akakizungushia upande wa kisogo na kukikita, mlinzi akazirai. Akamsukumia ndani kabla hajaingia na kufunga mlango mdogo wa geti.

Akagonga sasa mlango wa sebuleni na kusubiria majibu.

Miranda alikuwa chumbani ila aliisikia hodi hiyo. Kabla hajanyanyuka kwenda kuipokea, akafungua dirisha la chumbani na kutazama nje.

Chumba chake kilikuwa kimekaa mahali ambapo alikuwa na uwezo wa kutazama na kuona kibarazani.

Akamuona Jona.

Alishangazwa haswa. Amepajuaje hapa? Hilo ndilo lilikuwa swali la kwanza kuja kichwani. Hodi iliita tena, akanyanyuka na kwenda sebuleni.

Alikuwa amevalia suruali pana ya malighafi laini, kaushi nyeusi pasipo sidiria, miguuni akiwa peku. Nywele zake zilikuwa timu, kinyumbaninyumbani. Nyuma ya kiuno alikuwa amechomeka bunduki ndogo.

Japokuwa alishangazwa na Jona kujua makazi yake, ila hakuwa na wasiwasi sana. ni ‘mchora picha tu, alijiambia moyoni akisogelea mlango.

“Karibu.”

Jona akazama ndani pasipo kusema lolote. Akaketi na kukunja nne. Miranda naye akafuatia nyuma, akaketi kwenye kiti kilichowafanya watizamane vema.

“Najua ujio wangu umekustaajabisha, pengine ulitegemea nisingekuwa hai wakati huu ama basi ni mlemavu, samahani sana,” alisema Jona kwa kujiamini. Miranda akakunja ndita za kukanganyikwa.

Hakupewa muda wa kuuliza, Jona aliendelea kuongea.

“ … Anyway, I am tired of your bullshit. Mnataka nini kwangu? Ile picha? Ni picha ndiyo inawafanya mtake kunitoa roho? Mmeona picha haitoshi sasa mnawinda roho yangu?”

“Jona, please calm down. Sielewi unachokizungumza. Nani anataka kukutoa roho? Embu twende taratibu taratibu, umepajuaje hapa?”

Jona akatabasamu.

“Usitegemee kama nitajibu swali lolote toka kwako. Sijaja hapa kufanyiwa mahojiano bali kutoa tamko na angalizo. Mosi, hamtapata picha yoyote toka kwangu. Pili, acheni mara moja kunifuatilia, la sivyo …” Hakumalizia, ila macho yake yalisema kila kitu.

Akanyanyuka na kuondoka zake akimwacha Miranda kwenye bumbuwazi.

Mwanamke huyo akamtazama Jona akifungua mlango wa geti na kuufunga kwa kuubamiza. Akagundua mlinzi hayupo. Haraka akanyanyuka na kwenda kutazama.

Akamkuta mlinzi akiwa hana fahamu.

Akampigia simu Kinoo na kumtaka aje nyumbani upesi. Baada ya muda mfupi Kinoo akatia miguu yake eneoni akitumia Range Rover sport nyeupe. Alikuwa amevalia ‘ki body’ cheusi na suruali ya jeans aliyoifunga na mkanda kiunoni, miguuni akila moka nyeusi.

Miranda akamweleza yale yote yaliyotukia kuhusu Jona.

“Si unaona sasa?” Kinoo akatahamaki. “Mi’ ndo’ mana n’likuambia tummalize tu, we ukawa unavunga vunga. Ona sasa!”

“Kinoo, embu uwe unatumia akili hata mara moja moja. Yani we umeona hilo ndo’ la kukimbilia kuropoka?”

“Haya, we endelea kun’zarau.”

“Si kwamba nakudharau, nakwambia ukweli. Kuna maswali ya kuanza kujiuliza na kuyatafutia majibu, na si kuanza kurusha risasi za lawama.”

Kinoo akashusha pumzi ndefu puani na kubinua mdomo wake.

“Haya sema nakus’kiza.”

“Kinoo, huyu mchora picha si tu mchora picha. Nimeshangazwa kwa namna alivyopajua hapa na hata kujiamini kwake.

Kama haitoshi, namna alivyomkabili mlinzi, kunazidi kunifanya nihofie. Pengine mtu huyu anahitaji jicho la pili, ni mtu mwenye ujuzi binafsi ama mafunzo.

Zaidi ya hapo, kwa necha ya maongezi yake kuna watu wanamfuatilia, na hawa watu wanataka kumuua japo hajaweka wazi ni wakina nani na wametumia njia gani. Ila wapo, na ajabu sio sisi! Kwani kwa muda kidogo hatujasumbuka naye, na hatujawahi pia kutishia uhai wake.

Unadhani nini kinaendelea? Ina maana mchora picha huyu naye anataka kumalizwa kama Bite?”

Kinoo akaguna na kubinua lips zake nyeusi.

“Hilo halina shaka. Ina maana tayari wanajua kuhusu mchora picha huyu, na sasa wanataka wamalize ushahidi kabisa kisibakie hata punje. Hii ina maana wanajua kulikuwa kuna mahusiano kati ya Bite na huyu mchora picha.”

“Ndiyo maana yake. Na naona msisitizo ni kumuua mchora picha kuliko kuipata picha yenyewe. Wanataka kummaliza. Ina maana kilichomo kwenye picha hawakihitaji, wanakijua?”

Kinoo akapandisha mabega juu.

“Leo inabidi tupate picha hiyo, Kinoo,” Miranda akasema kwa msisitizo. “Tusipoipata leo, kuna hatihati tukaikosa daima.”


**


Wakati huo upande huu ukiwa unateta, upande mwingine kwenye laini mojawapo ya simu maongezi ya Nade na mheshimiwa waziri, Eliakimu Mtaja, nayo yakawa yanachukua nafasi.

Nade alikuwa amejikobeka mahali fulani alipoegemea ukuta.

Kumbe alikuwa ndiye mwanamke yule Jona aliyemuona kule Kariakoo. Nguoze zilisema hivyo.

Eneo hili alilokuwepo halikujulikana kwa urahisi.

“Nimemshuhudia kwa macho yangu akiingia na kutoka kwa Miranda.”

“Una uhakika?”

“Ndio, mheshimiwa.”

“Ina maana wanajuana na Miranda?”

“Itakuwa wanajuana. Hakukaa kwa muda mrefu ndani.”

“Watakuwa wanafanya ishu gani na Miranda?”

“Sijajua mkuu. Sijajua pia nani aliyejaribu kumuua kwa kumgonga na gari. Inaonekana kuna mambo kadhaa tusiyoyafahamu kuhusu Jona.”


*NINI KITAKACHOTUKIA?*
 
*ANGA LA WASHENZI --- 14*

*Simulizi za series*

ILIPOISHIA…

“Ina maana wanajuana na Miranda?”

“Itakuwa wanajuana. Hakukaa kwa muda mrefu ndani.”

“Watakuwa wanafanya ishu gani na Miranda?”

“Sijajua mkuu. Sijajua pia nani aliyejaribu kumuua kwa kumgonga na gari. Inaonekana kuna mambo kadhaa tusiyoyafahamu kuhusu Jona.”

ENDELEA…

“Mfuatilie kila nyendo,” mheshimiwa akanguruma. “Hakikisha kama anayoyafanya yanahusiana na Mariam, kama ndiyo unipashe habari upesi. Kama sio basi fanya ujue ni jambo gani.”

“Sawa, mkuu,” Nade akajibu na kukata simu.



***



“He’s promised, so very soon things gonna be ok,” (Ameahidi, kwahiyo karibuni vitu vitakuwa sawa) Miranda alisema kwa sura ya uhakika. Alikuwa anaongea na mwanaume mzungu, makadirio ya miaka hamsini na mambo hivi, mwenye ndevu nyeupe zilizochongwa vema, na nywele za wastani kichwani.

Mwanaume huyu alikuwa amevalia shati jeupe lililoziba mikono yake, suruali nyeusi na moka rangi ya kahawia, iking’aa mithili ya kioo. Shingoni alikuwa amejinyonga na tai rangi ya chinikiwiti.

Mkono wake wa kushoto alikuwa ameuvika saa kubwa rangi ya dhahabu, huku mkono wake wa kuume ukiwa umekamatia sigara kubwa ya kaki iliyokuwa inafuka kama gari moshi.

Mkono huu ulikuwa na kazi mbili, moja kupeleka sigara mdomoni, na pili kukung’utia sigara kwenye kisosi kilichokuwapo mezani.

Miranda alikuwa amevalia gauni jeusi linalombana na kumsadifu umbo. Nywele zake zilikuwa zimetengenezwa na kuundwa vema kama nyasi za msonge. Shingoni alikuwa na mkufu wa dhahabu, masikioni hereni za ghali.

Mezani alikuwa ameweka pochi yake ndogo nyekundu yenye zipu kubwa. Alikuwa ananukia kana kwamba ametoka kuoga kwenyee dimbwi la marashi ya Uajemi.

Waliendana na makazi waliyopo – nyumba kubwa ya kisasa iliyozungukwa na bustani ya majani na maua. Mlinzi getini mwenye bunduki na mbwa mkubwa mchanganyiko wa mbegu za Ulaya.

Lakini kwa mujibu wa mavazi yao, usingekosea kubashiri kuwa watu hawa wana safari muda si mrefu ya kwenda mahali fulani. Tena penye taadhima. Haingii akilini kusema wamejikobeka vile kwa ajili ya makutano tu.

Mwanaume huyu mzungu anafahamika kwa jina la Brown Curtis, Ama kwa kifupi BC kama watu wake wa karibu na yeye pia anavyopenda kuitwa. Sauti yake ni nyembamba na ya chini, macho yake ni makali rangi ya bluu.

“But his price goes higher every now and then. It becomes very expensive to afford him,” (Lakini bei yake hupanda kila sasa na baadae. Inakuwa gharama kubwa kummudu,” alisema BC kabla hajapeleka sigara mdomoni na kuinyonya mithili ya mtoto anyonyavyo titi la mama yake.

"But we have no choice. We depend on him so much. Or have you got someone else?" (Lakini hatuna chaguo. Tunamtegemea mno. Au umeshampata mtu mwingine?" Miranda aliuliza.

BC akatikisa kichwa.

"No! And that's the real problem. I must find a way out." (Hapana! Na hilo ndilo tatizo haswa. Ni lazima nitafute namna.)

"Be keen. He knows most of our moves, he may spoil the car if we deny him the fare." (Kuwa makini. Anajua harakati zetu nyingi, anaweza kuharibu gari akijua tumemnyima nauli.)

"Don't worry, I will be the first one to take action after getting an exit door. He cannot do anything stupid unless I am dead," (Usijali, nitakuwa wa kwanza kufanya jambo nikishapata mlango wa kutokea. Hawezi akafanya jambo lolote la kijinga labda niwe mfu,) alisema BC uso wake ukiwa umezibwa na moshi wa sigara

Mara akatokea dada wa kazi. Alikuwa amevalia sare rangi nyeusi na nyeupe akibebelea trey yenye glasi kubwa ya sharubati ya Strawberry.

Akaitua mezani na kumkaribisha Miranda, kisha akaenda zake.

"Any suggestion?" (Wazo lolote?) BC aliuliza akimtazama Miranda. Alijua mwanamke huyo hatokosa cha kusema.

Miranda akapandisha mabega juu.

"It's just ok if you believe things won't go out of your hands." (Ni sawa tu kama unaamini vitu vitakuwa poa.)

"Yes. We gat to do something, he takes almost half of the profit. It is dangerous ... let us see what will happen." (Ndio. Inabidi tufanye kitu, anachukua karibia nusu ya faida. Ni hatari ... acha tuone nini kitatokea.)

Kukawa kimya kidogo. BC alikuwa anavuta pafu za sigara, Miranda akipiga mafundo ya sharubati yake tamu.

"What about the report I sent? Have you gone through it?" (Vipi kuhusu ripoti niliyokutumia, umeipitia?) Miranda alivunja ukimya. BC akakohoa kwanza mara moja kabla hajajibu.

"I have done so. It's already sent ... and thanks for reminding me, the results are nothing but perfect! You can’t imagine even some governments have already booked them secretly." (Nimeipitia. Tayari imeshatumwa ... na shukrani kwa kunikumbusha, matokeo ni mazuri sana! Huwezi amini hadi baadhi ya serikali wameshaweka oda zao kwa siri.)

"That's nice! Then we have to produce more!" (Hilo ni jema! Basi inabidi tuzalishe zaidi!)

"Exactly, men are in the laboratories, as we are talking, working day and night. In fact more of it will be here soon special for our enemies." (Kabisa, watu wapo maabara, hapa tunavyoongea, wakifanya kazi usiku na mchana. Vile vile itatumwa hapa zaidi kwa ajili ya maadui zetu.)

"It's better! Enemies now are closer than before." (Ni bora! Maadui sasa wapo karibu kuliko awali.)

"All for the sake of business! Competition is stiff. Chemical and biological weapons are marketable for its effectiveness though they are prohibited in most places. I think it’s time now to put emphasis on this." (Yote kwasababu ya biashara! Ushindani ni mkubwa. Silaha za kemikali na baiolojia zina soko kwasababu ya ufanisi wake japo zinakatazwa mahali pengi. Nadhani ni muda sasa wa kuweka msisitizo kwenye hili.)

BC alitazama saa yake ya mkononi, kisha akamwambia Miranda.

"It's time. Let's go!" (Muda huu. Tuondoke.)

Miranda akamalizia kinywaji chake, BC akaminyia sigara yake kwenye kisosi kuizima. Wakanyanyuka na kwenda kwenye gari, Jeep nyeusi aina ya Cherokee. Wakakwea na kutoka ndani ya jengo.

Mwanaume ndiye alikuwa akiendesha, mwanamke akiwa amekaa pembezoni yake.

Walipoacha tu geti kwa umbali mdogo, Miranda akatoa simu yake kwenye pochi na kumtumia ujumbe Kinoo:

“Naweza nikakawia. Hakikisha unapata ile picha leo hii kama tulivyokubaliana.”

Ujumbe ulipofika, akarejesha simu yake ndani ya pochi.

“I don’t have to tell you about this, you know how important it is. We have to expand our network tonight. We must look for another hand. You are an expert in that and that’s why I go with you.” (Sina haja ya kukuambia kuhusu hili, unajua namna gani lilivyo muhimu. Inabidi tutanue mtandao wetu. Ni lazima tutafute mkono mwingine. Wewe ni mtaalamu kwenye hilo na ndiyo maana naenda nawe.)

“I will do my best,” (Nitajitahidi,) Miranda akasema kwa ufupi, kukawa kimya.


***



“Naomba maji makubwa ya Kilimanjaro, ya moto. Na waambie jikoni waniandalie ndizi tano na nyama rosti,” Jona alitoa oda kwa mhudumu. Mhudumu akatikisa kichwa chake na kwenda.

Mwanaume huyu alikuwa ndani ya bar akatizayo kabla ya kwenda nyumbani kwake. Majira yalikuwa ya giza sasa. Alikuwa amechoshwa na uchovu, na mgongo wake ulikuwa unamuuma kwa mbali kutokana na purukushani ile ya ajali.

Akiwa anangojea huduma, akatoa simu yake na kuiangaza. Hakukuwa na ujumbe wala missed call. Akatahamaki Mheshimiwa hajamtafuta mpaka muda ule.

“Hajaona missed calls zangu?”

Alikumbuka maagizo ya Mheshimiwa kwamba akiwa amebanwa basi amtafute Nade na kumwambia shida yake, ila hakutaka kufanya hivyo, akaamua kuachana na jambo hilo.

Kulikuwa kuna jumbe kadhaa toka Facebook ila hakutaka kusumbuka nazo, akazipuuza.

Alipoweka simu yake mezani, macho yake yakatekwa kumtazama mwanaume fulani aliyekuwa anaingia ndani ya eneo ya bar. Mwanaume huyu alikuwa amevaa suti nyeusi na tai nyekundu.

Aliketi karibia na eneo kubwa la kutokea.

Alikuwa ni Bigo! Mwanaume aliyeagizwa kummaliza Jona.

Jona alimtazama mwanaume huyu kwa muda kidogo. Atensheni yake ikaja kuharibiwa na mhudumu akileta maji makubwa aliyoagizwa, akayapokea na kumiminia kiasi ndani ya glasi.

Mhudumu akamfuata Bigo, mwanaume huyo naye akaagiza maji makubwa kama yale ya Jona. Mhudumu akamskiza na kwenda zake.

Mara tatu Jona akakutana macho kwa macho na Bigo. Alikunywa glasi mbili za maji kisha akanyanyuka kabla hajakutana na mhudumu akimletea chakula chake alichoagiza jikoni.

“Kiweke tu hapa mezani, naenda maliwato nakuja,” alisema Jona, kisha akaenda uani kwa ajili ya haja ndogo.

Bigo alitaka kumfuata ila akasita. Hakuwa analijua eneo hilo vizuri, ilimradi alikuwa na uhakika kwamba Jona atarudi kwasababu ameacha mizigo yake mezani, basi akatuama asiwe na mashaka.

“Acha nikamuulie kwake,” alisemea kifuani, akaendelea kunywa maji yake taratibu.

Upande wa pili Jona akamaliza haja yake, akafunga zipu ya suruali na kuanza safari ya kurudi alipokuwepo.

Lakini kabla hajamaliza safari yake, hatua chache tu toka chooni, macho yake yakaona gari Mark 2 nyeusi kwenye kauwanja kadogo ka maegesho ya magari hapo bar. Haraka kumbukumbu yake ikamjuza gari hilo ndilo lile lililotaka kumgonga.

Akataka kuhakikisha.

Kwa tahadhari akalisogelea na kulitazama mbele juu ya bodi, akaona limebonyea. Akaligusa kwa nyuma na mgongo wa kiganja, kama haitoshi akainama na kusogeza kichwa chake uvunguni mwa gari.

Akagundua gari hilo lilikuwa limefika hapo muda si mrefu. Nani ameingia bar muda si mrefu? Hakuna mwingine mbali na mwanaume yule aliyevalia suti, akili yake ikampa majibu haraka.

Basi akajikuta akitabasamu.

“Naona amenifuata kumaliza kazi yake,” alisema kisha akajirudisha kwenye kiti chake. Akaketi na kumtazama Bigo.


*NINI KITATOKEA?*

*MIRANDA AMEENDA WAPI NA BC? MIPANGO YA BC ITAKAMILIKA?*

*KINOO ATAFANIKIWA KUPATA PICHA USIKU HUU KAMA ALIVYOAGIZWA?*

*JONA ATATOKA SALAMA USIKU HUU?*
 
*JOANA ANAONA KITU USIKU --- 11*

*Simulizi za series*


ILIPOISHIA

Lisa alikuwa peke yake chumbani wakati alipokuja kuchukuliwa. Ila alipotiwa ndani ya gari la polisi, Joana alijitokeza na kushuhudia tukio hilo.

Alipata mashaka sana. Hakuna yeyote anayejua siri yake na Moa zaidi ya Lisa. Je, ataenda kusema?

ENDELEA…

Alikosa amani kabisa na akajihisi tumbo limemvuruga. Ndani hakukukalika, akaamua kuketi nje alipojichanganya na wengine waliokuwa wamesimama kwenye vikundi vikundi wakiteta na kuongelea swala lile la mlinzi.

Kila mtu alikuwa anaongea lake, na yote Joana alitaka kuyasikia kwa wakati mmoja.

“Ni jini!” mwanafunzi mmoja alisikika akiropoka. Wenzake sita walikuwa wamesimama wakimsikiliza kwa umakini. “Anayemaliza watu ni jini na anaishi msituni. Anapitapita koridoni mwa bweni la wasichana kila nyakati za usiku!”

Maelezo hayo yakamfanya Joana ajisikia vibaya, moja kwa moja alimfikiria Moa. Ina maana Moa ni jini au? Inawezekanaje hili?

“Alibadilika mbele ya mlinzi na kuwa jitu la ajabu!” msimuliaji yule aliyezingirwa na wenzake aliendelea kunena. “Alipomulikwa usoni akakimbilia msituni, la sivyo alikuwa anamuua mlinzi mwingine! Unaambiwa alikuwa jitu kuuubwa jeusi lenye mikono kibao.”

Joana akaona inatosha sasa, akaondoka zake na kwenda mbali alipojitenga na watu. Alijikunja akiwaza kumhusu Moa. Kwa namna moja akili yake ikakiri kuna jambo halipo sawa na Moa.

Hakuwa Moa wa kawaida. Ila ndiyo tuseme amekuwa jini!

Aliutazama mkufu ambayo Moa amempatia, akahisi dunguli kubwa linamkaba koo. Machozi yalikuja upesi machoni, yakatiririka kama mto.

Alijitahidi kuyafuta, lakini hayakukoma. Aliona maisha yake yameharibika na furaha imepotea. Mtu pekee aliyekuwa anamtegemea, nawe amekengeuka. Kwa muda akajihisi mtupu na ulimwengu wote unamcheka.

Kutafuta ahueni, akampigia mama yake na kumweleza. Alihisi akimwambia mtu mambo yanayomsibu basi angalau atapata ahueni kwa kutoa jambo kifuani.

“Rudi nyumbani, mwanangu. Upesi kesho asubuhi uwepo nyumbani,” sauti ya mama iliita simuni. Alishikwa na uchungu kumsikia mwanae analia.

Kabla hata Joana hajaongea neno la ziada, mama akasema:

“Au nakuja huko. Ningoje!”

“Hamna mama, nitakuja!” Joana akawahi.

“Kweli Joana?”

“Ndio, mama. N’takuja,” Joana akasema kwa sauti tumbuizi kabla hajakata simu. Angalau akahisi kifua kinapitisha hewa.

Alirejea chumbani, na baada ya kama lisaa limoja Lisa naye akaingia. Alikuwa na uso mchovu wenye mchanganyiko na mawazo. Aliketi juu ya kitanda akajilaza kana kwamba mtu aliyechoka mno.

“Vipi Lisa?” Joana akamuuliza akimsogelea rafikiye karibu.

“Safi tu,” Lisa akajibu kifupi akichochea hamu ya Joana.

“Wamekuambiaje huko?”

Kabla Lisa hajajibu hilo swali, akavuta kwanza kamasi.

“Joana, hakuna siku nimeongopa kama leo. Nimefanya kwasababu tu wewe ni rafiki yangu, la sivyo nisingeliweza!”

Lisa akaeleza yale yote aliyoulizwa huko kituoni mwa polisi. Na namna alivyoongopa kwamba hamjui Moa na hajawahi kumsikia akija chumbani kwao wala kumtilia mashaka rafiki yake.

“Ahsante sana, Lisa. Sina cha kukulipa.”

“Usijali, Joana. Lakini upo hatarini sana, na inaelekea polisi wanangoja kitu kidogo sana ili wapate kukutia nguvuni.”

“Kitu kidogo?”

“Ndio, kitu kidogo sana. chunnga mienendo yako Joana. Sitaki kukupoteza.”

Joana akakosa cha kusema, alitazama chini akitekwa na mawazo.

“Naamini si wewe uliyeua. Nakuamini Joana. Nitakuwa wa mwisho kuamini kama wewe ni muuaji.”

“Ahsante sana, Lisa.”

“Lakini Moa ni muuaji. Kuwa naye makini sana,” Lisa akatoa nasaha kabla hajageukia kando na kupitiwa na usingizi. Joana alikosa hata cha kusema akabaki akiwa amefumba mdomo kwa kiganja.

Siku ikasonga mpaka majira ya saa nne usiku. Si Joana wala Lisa aliyekuwa ametia kitu tumboni. Japokuwa Joana alifuata chakula kantini, kilibakia tu kwenye vyombo.

“Kesho naondoka kurudi nyumbani,” Joana alivunja ukimya.

“Na vipi kuhusu masomo?” Lisa akauliza.

“Nimechoka, Lisa, sitaweza hata kusoma. Nahisi nahitaji mapumziko, tena marefu. Nataka kutoka mazingira haya kabisa.”

“Unaniacha mpweke?” Lisa akauliza.

“Naomba twende wote,” Joana akashauri. “Naomba twende, Lisa. Twende hata chuo kingine, hilo siyo tatizo.”

“Si rahisi kihivyo, Joana … nitawaelezaje nyumbani?”

Mara wakasikia hodi ikiambatana na sauti ya kike mlangoni, wakatazamana kabla hawajasikia sauti:

“Cecilia!”

Joana akanyanyuka kwenda mlangoni. Cecilia ni kiongozi wao wa bweni. Ni mwanamke mnene machachari anayependa sana kuzungumza. Anafahamika sana kwa mwendo wake wa kibabe na sauti yake nyembamba.

“Hello Joana, tafadhali naweza nikaongea na wewe kidogo?”

Joana akaufunga mlango na kusogea kando kidogo.

“Kumekuwa na sintofahamu ndani ya bweni letu kwa muda sasa. Watu wamekuwa wakiishi kwa taharuki sana, hivyo basi mie kama kiongozi wa bweni nimeona nije kutoa tahadhari,” alisema Cecilia, mpaka hapo Joana hakuonekana kushtushwa.

Alichukulia taarifa hiyo kama zilivyo nyingine. Hakujiuliza kwanini aliitwa pembeni yeye mwenyewe.

“Kuna mwenzetu amekiri kumuona Moa akiwa anakuja kwako nyakati za usiku.” Hapo Joana akashtushwa. Moyo ulikita!

“Joana huwa unampokea Moa wakati wa usiku?”

Joana akakataa katakata, alimbishia kabisa Cecilia. Cecilia akaenda zake akimwachia tahadhari:

“Njia ya mwongo ni fupi.”

Joana akaenda kumweleza Lisa juu ya Cecilia. Alihisi kuchanganyikiwa na akazidi kupata sababu ya kuondoka eneoni hapo haraka iwezekanavyo.

Alilia Lisa akambembeleza sana mpaka kwenye majira ya saa saba usiku. Lisa akalala na kumwacha Joana macho.

Kwenye majira ya saa nane usiku, akiwa mwenyewe macho, akasikia hodi mlangoni. Na mara sauti:

“Moa!”

Joana akajikuta amepandwa na hasira. Alihisi kichwa kimekua cha moto na mwili umenyanyuka pasipo kujitambua.

Alielekea kabatini akatoa rungu moja kubwa, kisha akaenda mlangoni na kufungua. Moa akaingia, lakini akakutana na rungu kubwa kichwani – pam! Akadondoka kama kiroba akivuja damu kichwani.



JOANA AMEUA? NINI KITAMKUTA?

Sent from my SM-J110F using JamiiForums mobile app
 
*JOANA ANAONA KITU USIKU --- 12*

*Simulizi za series*


ILIPOISHIA

Joana akajikuta amepandwa na hasira. Alihisi kichwa kimekuwa cha moto na mwili umenyanyuka pasipo kujitambua.

alielekea kabatini akatoa rungu moja kubwa, kisha akaenda mlangoni na kufungua. Moa akaingia, lakini akakutana na rungu kubwa kichwani - pam! akadondoka kama kiroba akivuja damu kichwani.

ENDELEA...

Joana akatahamaki kwa mshangao. Ni kama vile si yeye aliyefanya hilo tukio.

"Mungu wangu, nimeua!" alisema akishika kichwa. Lisa alikuwa ameachana mdomo macho yakimtoka.

"Lisa tunafanyaje sasa?" Joana akauliza akikung'uta viganja vyake. Jasho lilikuwa tayari limeshamvuja.

Lisa akanyanyuka upesi toka kitandani na kwenda kuweka mgongo wa kiganja chake mbele ya pua ya Moa. Akasikilizia kwa sekunde kadhaa.

Loh! Moa hakuwa anahema!

"Ina maana amekufa?" Joana akawahi kuuliza. Uso wake ulifinyangwa na hofu kubwa. Hajawahi kuua akiwa na akili zake timamu.

"Inawezekana akawa amekufa," Lisa akajibu kwa sauti ya chini.

"Sasa tunafanyaje jamani! Lisa tunafanyaje?"

"Sijui, Joana! Hii ni kesi kubwa, tutaenda kufia jela."

Joana akazidi kuchanganyikiwa. Lisa alijaribu kumtuliza na kumwambia:

"Usijali, Joana. Hakuna mtu anayejua kama Moa amekuja humu."

"Una maanisha nini, Lisa? Hata kama hakuna mtu anayejua, tutaupeleka wapi mwili wa Moa?"

"Joana, inabidi ufikirie mara tatu zaidi. Upo radhi tukamatwe na kufia jela?"

Joana akajibu kwa chozi.

"Basi ndiyo tutafute namna ya kufanya. Tatizo tayari limeshatokea, na kulia kwetu hakutasaidia."

Wakakaa kama dakika tano, bado mwili wa Moa ulikuwepo chini ila umeacha kumwaga damu.

"Tukautupie mwili wake huko mbali," akashauri Joana aliyekuwa anatetemeka.

"Tutapitia wapi?" Lisa akauliza.

"Tutapitia hii njia ya huku uani. Hamna kamera, na ni fupi zaidi."

Wakatazama saa, ilikuwa saa tisa usiku na dakika za mapema. Wakakubaliana kupiga moyo konde na kufanya hivyo ili kujiepusha na kadhia ya mkono wa dola.

Ila wakati wanahangaika na kumnyanyua Moa, wakasikia vishindo vya miguu nje ya mlango. Miili yao ikapoa ghafla kwa baridi la hofu. Walijikuta wanatetemeka kama wametoka kuogea maji ya barafu.

Wakaona ni hatari tena kwenda nje, hivyo wakakubaliana kuutia mwili wa Moa ndani ya kabati na watafanya tukio la kwenda kuutupa kesho usiku wakiona shwari.

"Huyo atakuwa ni mlinzi anazunguka huko nje!" Alisema Joana.

Mara mlango unagongwa. Tambalizi la uwoga linakamata chumba. wanatazamana kama mizimu.

Damu ilikuwa chini kwenye zulia, na mwili wa Moa ulikuwa bado haujanyanyuliwa kupelekwa kabatini.

Bahati kwao, mgonga mlango hakungoja afunguliwe, akapaza sauti:

"Ni muda wa kulala, tafadhali zimeni taa."

Kisha vishindo vya miguu vikasikika vikienda mbali. Wakashusha pumzi ndefu. Haraka wakaubeba mwili wa Moa na kuutia kabatini.

Wakafunga.

Wakaligeuza na zulia chini juu, juu chini, kisha wakaketi kitandani. Usingizi ulikuwa hauji kila mtu akibanwa na maswali kichwani. Kulala na maiti ndani ya kabati si kitu kirahisi.

Kila mmoja alikuwa anahofia na kujiuliza kuhusu kesho yake. Joana akajutia alichokifanya akishangaa na kujiuliza ilikuwaje akajitia matatizoni kiasi hicho. Basi wakajikuta hawana raha wala amani.

Muda ukasonga zaidi mpaka saa kumi na moja. Lisa alikuwa amebanwa na usingizi vibaya mno akaegesha kichwa chake kitandani akilala kana kwamba yupo vitani.

Joana yeye alikuwa ameketi vilevile ila akiwa anapiga 'magoli ya vichwa', macho yalikuwa yanafumba kwa lazima, kichwa kikidondoka na kusimama.

Katika muda huo huo, Joana akashtuliwa kwa kusikia sauti kabatini! Mlango wa kabati ulikuwa unagongwa na sauti ya mtu akinguruma.

Haraka akamshtua Lisa na kumwonyeshea kidole kabatini.

"Moa mzima!"

Kabla Lisa hajasema jambo, Joana akakimbilia kabatini na kufungua. Moa akatoka akiwa hoi. Alikuwa ameshikilia kichwa akikunja sura kwa kulalama maumivu.

"Moa, mzima!" Joana alimpapasa papasa Moa akiwa haamini. Moa hakusema jambo, akaketi kitandani bado akishikilia kichwa chake na kulalama.

Alikuwa anasikia maumivu makali.

"Nisamehe Moa, haikuwa dhamira yangu," Joana akajitetea.

"Haikuwa dhamira yako nini?" Moa akauliza. Hakuonekana kama anajua kilichotokea. Lisa akambinya mkono Joana kumwashiria anyamaze.

"Ni saa ngapi sasa?" Moa akauliza.

"Saa kumi na moja na robo," Lisa akajibu. Moa akakurupuka kusimama.

"Inabidi niende!"

"Uende wapi?" Joana akawahi kuuliza.

"Inabidi niende!" Moa akarudia kauli yake pasipo kujibu. hakumngoja tena mtu aongee, akaufuata mlango upesi, akaufungua na kutimka!

Joana akafunga mlango kwa ufunguo haraka, kisha akatulia kwanza hapo mlangoni kutega kama atasikia lolote huko. baada ya kama dakika mbili, akarejea kitandani kumkuta Lisa aliyekuwa ameketi kitako.

"Joana, Moa siyo binadamu," akasema Lisa kwa macho ya kujiamini.

"Kwanini wasema hivyo?"

"Moa hakuwa anapumua!" Lisa akalipuka.

"Kwa akili zangu nilipima pumzi zake, sikuhisi kitu!"

"Pengine alikuwa anapumua kwa mbali."

"Hapana! Hapana. Alikuwa hapumui kabisa. nimemtazama pia hata hapa alipokuwepo kitandani, sikuona kifua chake kikisinyaa na kutanuka. Naapa kwa Mungu wangu!"

Sasa ile hoja kwamba Moa ni jini ikaanza kuleta mashiko kichwani mwa Joana.

"Unajua Moa anakaa wapi?" Lisa akauliza.

"Sijui!" Moa akatikisa kichwa.

"Kuna kitu, Joana. Ni wazi kuna kitu hapa. We unahisi atakuwa anaishi wapi?"

"Msituni!" haraka likaja jibu kichwani mwa Joana.

Kama alihaha kutafuta makazi ya Moa akayakosa, basi Moa ndiye yule anayeishi msituni. Ndiye yeye muuaji. Ndiye yeye anayegeuka kuwa kiumbe cha ajabu! Aliyakumbuka maneno ya yule mwanafunzi aliyekuwa anawasimulia wenzake.

"Moa anakuja hapa saa nane za usiku tu. Anaonekana nyakati za usiku peke yake, tena akiwa mwenye nguvu. Si bure aliondoka haraka punde alipojua ni saa kumi na moja, maana jua linakaribia kuchomoza!"

Maneno hayo ya Lisa yalipenya vizuri masikioni mwa Joana na kujenga nyumba kuu ya hoja. yalikuwa na mantiki ndaniye. Yalimfumbua Joana macho ambayo alikuwa ameyafumba kwa kutokujua ama kwa kujua kwasababu tu ya upofu wa mapenzi.

"Naondoka, Lisa," akasema Joana. "Siwezi nikakaa tena hapa. Tafadhali naomba uniwie radhi nakuacha peke yako. Ila ni kwa mema."

"Naelewa, Joana. Nenda," akasema Lisa. Hakuona tena sababu ya kuzozana na Joana. Alimwonea huruma rafiki yake, akamshika bega na kumvuta kumkumbatia.

"Yote yatapita Joana, hata na hili."

Joana akaangua kilio. Alipanga vitu vyake ndani ya begi dogo tu la mgongoni maana hakutaka yeyote ajue kama anaondoka, akavalia nguoze na kumwaga Lisa.

"Tutaonana pale majira yatakapofika."

Uzuri alishakata tiketi jana yake kwa kupitia mtandao, hivyo hakupata shida. Alifika uwanja wa ndege akajipaki chomboni na kuondoka Ujerumani kwenda kwao Ubelgiji moja kwa moja.

Alijisema kifuani anataka kusahau yote ya huko alipotoka akaanze maisha mapya.

Lakini utaanzaje mapya ukiwa umeyabebelea ya zamani? Shingoni mwake bado alikuwa amebebelea mkufu aliomkabidhi Moa.

Mkufu huo alikuwa anarudi nao nyumbani. Alikuwa anaupeleka nyumbani, je utamwacha salama ilhali Moa alisema ilimradi ana mkufu huo na basi atakuwa naye?

Mama yake alimpokea kwa bashasha na kumpeleka mpaka nyumbani ambapo pasipo kuficha akamweleza mamaye yale aliyokumbana nayo huko chuoni.

Mama akampa moyo na kumsihi apige moyo konde, atafanya mpango apate chuo hapa hapa nyumbani awe anamuona na kumpatia nasaha.

Zikapita siku mbili akiwa nyumbani. Siku ya tatu Joana akapata habari kwa kupitia runinga. Lisa alikuwa ameuawa na mtu asiyejulikana!


NANI AMEMUUA LISA? NINI JOANA ATAFANYA? NINI MKUFU UTAFANYA?






Usikose sehemu ijayo.

Sent from my SM-J110F using JamiiForums mobile app
 
Asante Shunie. Naomba mkawe pia walinzi wako huko jamani.
Mkuu steve kama hizo hati miliki ni gharama kukata,Tafadhali tujulishe wadau tukuchangie japo elfu 5 kila mmoja wetu,maana kiukweli tunaosubscribe kwenye uzi wa simulizi zako ni wengi,sio vibaya tukafanya mpango wa mchango wa elfu 5 kila mtu kumsupport mtunzi wetu ili aendelee kutufurahisha na kutufariji kama hivi.
 
Mkuu steve kama hizo hati miliki ni gharama kukata,Tafadhali tujulishe wadau tukuchangie japo elfu 5 kila mmoja wetu,maana kiukweli tunaosubscribe kwenye uzi wa simulizi zako ni wengi,sio vibaya tukafanya mpango wa mchango wa elfu 5 kila mtu kumsupport mtunzi wetu ili aendelee kutufurahisha na kutufariji kama hivi.
Nashukuru Salito, nitawapa feedback juu ya kinachoendelea. Thanks!
 
Back
Top Bottom