Anga la washenzi na Joana anaona kitu usiku

Anga la washenzi na Joana anaona kitu usiku

*ANGA LA WASHENZI --- 11*


*Simulizi za series*



“Karibu sana, Miranda,” Nade alisema kwa bashasha la tabasamu, akiutanua mlango zaidi na kunyooshea mkono wake ndani.

“Ahsante, nimekaribia. Mnaendeleaje?”

“Tupo poa. Kitambo kweli umetususa!”

“Sema tumesusana, Nade. Hata nanyi mmekaa kimya kama maji ya mtungini.”

“Bila shaka kuna jambo kubwa limekuleta!”

Miranda akatabasamu pasipo majibu. Aliketi akamtazama mheshimiwa, wakapeana salamu.

“Najua umeshatambua nini kimenileta mheshimiwa.”

“Hapana. Pengine unikumbushe si unajua mambo mengi, Miranda.”

“Ni kuhusu ile ishu tuliyojadili siku ile kule Mango garden.”

“Hivi tuliongelea kitu gaaa …” Mheshimiwa alikuna kichwa kwa kidole akijaribu kukumbuka pasipo mafanikio. Alimtazama Miranda, Miranda akampa ishara ya macho kwa kumtazama Nade. Basi Mheshimiwa akamtoa Nade sebuleni kwa ishara ya kumtikisia kichwa.

Sasa wakawa wamebakia wenyewe sebuleni.

“Ni kuhusu yale madawa tuliyokuwa tumeyagiza toka Uswizi.”

“Oooh! Sasa nimekumbuka!” Mheshimiwa akaliza vidole vyake. “Enhee vipi kwani mzigo umeshakamilika?”

“Ndio, upo tayari kabisa na umeshapakiwa kwenye makontena kwa ajili ya usafirishaji.”

“Makontena? – mmepanga kutumia njia ya maji?”

“Ndio. Ndiyo njia ya kubeba mzigo mingi zaidi.”

“Ni sawa, pia ndiyo salama zaidi ukilinganisha na njia ya anga. Kwahiyo jumla kuna makontena mangapi?”

“Hamsini na mbili.”

“Ni mengi mno. Haiwezekani yakasafirishwa yote kwa siku moja.”

“Una mpango gani, mheshimiwa?”

“Kuna mwanya wa kusafirisha manne tu kwa sasa, na ni juma lijalo. Mnaweza mkafanya hivyo?”

Miranda akasita kwanza kujibu apate kutafakari.

“Siwezi nikatoa jibu la moja kwa moja mheshimiwa, kama unavyojua ni lazima nipeleke taarifa hizi kwa mkuu wa kitengo kisha yeye ndiyo anipe maagizo.”

“Basi mtaarifu hivyo. Juma lijalo kuna mpango wa kuleta kontena ishirini zilizobebelea vifaa vya kujengea uwanja wa kisasa kama ule wa taifa. Kama unavyojua vifaa hivi havitozwi kodi, na hata upekuzi wake unakuwa hafifu kwakuwa ni vya serikali.”

“Ni kweli mheshimiwa. Ila vipi na kuhusu hiyo mzigo mingine itakayokuwa imebakia? – nayo inabidi ije kwa namna yoyote ile ili kukamilisha pakeji nzima.”

Mheshimiwa akafichama mdomo wake kwa kiganja akitafakari. Aliangazia mianya anayoweza kuenenda afanikishe zoezi hilo. Wazo likamjia.

“Ok, tutafanya hivi. Kadhaa zitabebwa kama nilivyokuambia – kwa kutumia makontena ya vifaa vya uwanja wa mpira. Na hayo mengine, yote, tutapitishia kwa kutumia mgongo wa shirika la madawa nchini.

Tutafanya kama malighafi za kutengenezea madawa ya kutulizia maumivu na nusu kaputi. Unaonaje?”

Miranda akatikisa kichwa kuafki.

“Ni sawa, ila napata shaka kidogo.”

“Gani hilo?”

“Kuhusu usalama wa hiyo mizigo na pia ka …”

“Miranda, hilo ni jukumu langu. Nimeshawahi kuwaangusha?”

“Hapana, mheshimiwa.”

“Basi unaweza kwenda kumfikishia taarifa mkuu wako. Mashaka yangu yapo kwenye muda wa shirika la madawa maana bado sijaongea na mtu wa huko nikajua. Ila … n’tawataarifu kesho I think.”

“Sawa. Ada?”

“Miranda, sasa mnaniangusha. Ndiyo tumeanza kufanya hii kazi leo kiasi cha kutokujua ada?”

“Hapana, mheshimiwa. Kusema ukweli kwa sasa hali yetu imetetereka kiuchumi haswa baada ya sera za mambo ya nje za baadhi ya nchi kubadilika. Tuwiane radhi mheshimiwa na utuzingatie.”

“Nenda, nitaongea na mkuu wako.”

Miranda akanyanyuka na kwenda. Mheshimiwa akamuita Nade aliyekuja sebuleni upesi na kuketi.

“Sorry kwa kukutoa hapa, Nade.”

“Usijali, mheshimiwa. I understand.”

“Thanks. Sasa kuna kazi imeibuka hapa na inabidi ifanywe haraka. Kesho, asubuhi na mapema, nitakuagiza kwenda kuonana na Maxwell Ndoja. Unamkumbuka?”

“Ndio.”

“Kuna mambo machache nataka umfikishie mdomo kwa mdomo. Hak…”

“Hakikisha hamtumii simu, mtandao wala njia yoyote itakayoacha ushahidi!” Nade alimalizia kauli ya Mheshimiwa.

Mheshimiwa akajikuta anatabasamu.

“Sitakuambia tena hayo maneno kumbe umeyashika kiasi hicho. Anyway, baada ya Ndoja itabidi uonane pia na Nassoro Mauje.”

Baada ya kusema hayo, akafunguka kumwambia Nade mambo gani ya kwenda kujadiliana na hao watu. Alipomaliza akafungia mjadala kwa kusema:

“Kuwa makini. Hakikisha unatumia kila njia kuhakikisha hili jambo linafanikiwa, sina haja ya kukueleza ni kiasi gani cha pesa tutakivuna endapo dili hii ikitiki, unajua mwenyewe.”

“Ndio,” Nade akajibu kwa kutikisa kichwa.


***


Saa 04:35 asubuhi, ndani ya nyumba ya marehemu Bite.


Sebuleni kuna watu watano, wanne wageni machoni, mmoja bwana Kinoo. Katika hao wanne ambao ni wageni mbele ya mboni, mmoja alikuwa mwanaume mzee kuliko wote akiwa amevalia suti rangi ya nyekundu na tai nyeusi yenye vidotidoti vyeupe. Aitwa Brokoli.

Mwingine alikuwa mwanaume mwenye makamo ya miaka thelathini mpaka na tano. Alikuwa mweusi mwenye kichwa cha duara, uso mtulivu na macho ya kistaarabu. Alivalia ‘body’ nyeusi na suruali ya jeans. Aitwa Mudy.

Wengine wawili walikuwa mapacha wa kike, Sara na Sasha. Wasichana warembo warefu wenye nywele nyekundu, macho makali makubwa na ‘lips’ pana nyekundu.

Sara alikuwa amevalia gauni jeupe lenye madoa madoa ya maua, Sasha akivalia blauzi ya kijani na suruali pana nyeusi inayobana juu na kumwaga chini. Kwa makadirio, warembo hawa wana miaka isiyozidi ishirini na nane, wala kupungua ishirini na tano.

Mzee Brokoli ndiye aliyekuwa anaongoza kikao hichi ambacho kiliita wajumbe wanaohusika na kampuni ya magari ya marehemu Bite. Lengo lilikuwa ni kujadili mustakabali wa kampuni hiyo lakini pia kumwongelea marehemu Bite kwa ujumla.

Kwenye meza ya kioo, hapo sebuleni, palikuwa pamejazwa vinywaji vilaini; sharubati takribani tatu; ya embe, pasheni na machungwa zikiwa zimetapakazwa kwenye glasi kubwa tano kulingana na idadi ya wajumbe.

Watu hawa walikuwa tayari wameshaanza kikao, na walikuwa katikati ya maongezi ambayo yalikuwa yanapokelewa kwa umakini na utulivu mkubwa.

Brokoli alikuwa ananguruma.

“Hatuelewi nini chanzo cha mauaji haya. Mpaka sasa polisi hawajampata wala kumshikilia mtuhumiwa yeyote yule, inashangaza kwakweli lakini pia inatia hofu. Inatuweka kwenye njia panda kujua kama mauaji haya yanahusiana na kampuni ama la!

Lakini kampuni inabidi iendelee. Si kwamba kifo cha Bite basi ndiyo kiwe kifo cha kampuni. Ni mapema sana kuamua hivyo. Ila kama nilivyosema hapo awali, ni lazima sasa kampuni hii ibadilike. Tufanye mambo mengine mbali na haya mambo ya magari.”

Hoja hii ikachukua muda kujadiliwa. Muda wote huo Kinoo alikuwa kimya kwani hili halikuwa linamhusu. Yeye alihudhuria hichi kikao kama mdau tu wa mbali, mwakilishi wa kampuni moja mteja wa kampuni ya magari ya Bite.

Hapa kikaoni yeye alikuwepo kwa lengo la kupata taarifa tu, kama kutakuwa kuna mpya, kumhusu Bite. Pengine akapata jambo likamjuza aliyehusika na kifo cha mwanamke huyo.

Hilo lilikuwa muhimu sana kwao. Kumjua aliyehusika na mauaji kungewafanya wachukue hatua kujilinda na kufuatilia kwanini mwanamke huyo ambaye alikuwa amebebelea siri kubwa, siri ya mafanikio, akapata kadhia kama hiyo.

Basi hitaji lake hili likamvuta mpaka ukingoni mwa kikao hichi, ambapo huko kuna kauli ya Mudy ilimshtua na kumfanya afikirishe zaidi akili yake.

“Kuna taarifa niliiwasilisha kwa mpelelezi wa kesi hii ya Bite, ni muda mrefu sasa, nikitegemea ingesaidia kwa namna moja kubwa kumpata muuaji. Ila ajabu haikufuatiliwa, ikapuuzwa!

Hata pale nilipokuwa nampigia simu mpelelezi na kumkumbushia, sikuwa Napata majibu ya maana. Kwakweli nikakata tamaa.”

Kiu ya Kinoo ikakua. Alitaka kujua zaidi kuhusu taarifa hiyo, basi akawahi kuuliza:

“Ni taarifa gani hiyo?”

“Sidhani kama kuna haja ya kujadili tena mambo hayo!” Brokoli akaingilia kati. “Hayo yameshapita, na hata tukiyateta hapa hayatabadili chochote. Tuendelee na mengine.”

“Mkuu Brokoli, huoni tukilitilia mkazo linaweza kuleta angalau haki kwa dada yetu aliyeuawa kinyama?” Mudy akauliza.

Brokoli akamkazia macho na ndita. Akamuuliza:

“Mudy, wewe ni nani kwenye kampuni?”

“Accountant,” Mudy akajibu akitazama chini.

“Na mimi ni nani?”

“Mkurugenzi.”

“Basi sina haja ya kuongea tena. Tugange yajayo, si ya nyuma. Ina maana kuna kitu haukuelewa huko nyuma tulivyokuwa tunaongea?”

“Nilielewa, mkuu. Samahani.”

Kikao kikaendelea na kukoma punde fupi. Watu wakanyanyuka na kuondoka zao.

Lakini kifuani mwa Kinoo mulikuwa mna jambo. Jambo mtambuka kumhusu Brokoli. Alimtazama mzee huyo katika namna ya pekee, namna ya tofauti na alivyokuwa anamtazama mwanzoni.

Aliridhia na akili yake mzee huyu anahitaji kufanyiwa upembuzi zaidi, tena wa kina. Kuna jambo analijua kuhusu Bite.

Kwanza, alitaka kujua kwanini alikuwa anasimamia sana hoja yake ya kubadili biashara, akikataa abadani kuendelea na biashara ya magari. Pili, kwanini hakutaka kugusia swala la taarifa ya Mudy juu ya Bite, ilhali mwanzoni alisema amefadhaishwa na ukimya wa polisi.

Aliamini kabisa endapo akiyapata majibu ya maswali hayo, basi hatotoka mtupu. Kuna kitu atapata, muhimu, chenye faida.

Taratibu akiwa ndani ya gari lake akatazama uelekeo wa gari la Mudy ambalo ndani yake lilikuwa pia limewabebelea Sara na Sasha. Gari hilo lilipotoka ndani ya eneo la nyumba, Kinoo akatia moto injini na kulifuatilia taratibu.

Alikuwa yupo ndani ya Range Rover sport wanayoitumia kwenye kazi zao.

Lengo lake lilikuwa ni kujua makazi ya Mudy, kwani watamuhitaji mtu huyo muda si mrefu. Kama taarifa yake ilipuuzwa na Brokoli, basi wao walikuwa wanaitaka. Tena kwa udi na uvumba!



*WATAPATA TAARIFA GANI KWA MUDY?*

*BROKOLI NI NANI? KWANINI ANAZALISHA SHAKA KIKAONI?*

*SIKU INAENDA HIVYO, JE BIGO ANA MPANGO GANI WA KUKAMILISHA AGIZO LA KUMMALIZA JONA?*

*NADE ATAFANIKIWA?*
 
*ANGA LA WASHENZI – 12*

*Simulizi za series inc.*


“Pole sana, Mudy, ndiyo boss huyo!” alisema Sara akitikisa kichwa na kutabasamu. Mudy akasonya. Alikuwa anatazama mbele aelekeapo. Mkono wake wa kushoto akiwa ameketi Sara, na Sasha amekaa nyuma peke yake. Ni ndani ya Rav4 nyeupe.

Mudy akatikisa kichwa na kutahamaki:

“Mpumbavu kweli yule. Sasa alikuwa analalamika nini kuhusu polisi kama hataki tuchangie mawazo?”

Sara na Sasha wakaangua kicheko.

“Sasa na hivi Bite amefariki, yule mzee si ndo’ atatupelekesha mpaka basi!” Sasha akapayuka.

“Nakwambia!” Sara akadakia. “Tutapelekwa kama gari bovu maana mzee yule hataki kushauriwa wala nini!”

“Tatizo mkoloni sana!” Mudy akaunga mkono hoja. “Sijui ametuitia nini kwenye hicho kikao chake kama kila kitu tayari ana majibu nacho. Si angetutumia tu ujumbe!”

“Kwakweli. Lakini Mudy, ulikuwa na taarifa gani kuhusu Bite? Mbona hujawahi hata kun’tonya siku zote hizo?” Sara aliuliza.

“Tatizo mambo mengi,” Mudy akajibu. “Huwezi kuamini nilikuwa nimesahau kabisa mpaka pale niliposikia tena kuhusu Bite pale kwenye kikao.”

“Tuambie basi nasi tujue,” Sasha akashupaza masikio, Mudy akatabasamu.

“Mnapenda sana umbea na nyie.”

“Tuambie bana, Mudy,” Sara naye akashadadia. “We hujui umbea kwa mwanamke ni sunna!”

Kabla Mudy hajasema neno, hamaki dereva bodaboda akakatiza upesi mbele yake! Alijitahidi kukwepa bodaboda kwa kupeleka gari kando ambapo napo huko kulikuwa kuna gari iliyokuwa inakuja nyuma kwa kasi, hivyo akaishia kubamizwa ubavuni na kusababisha tafrani barabarani!

Sara na Sasha walipiga kelele kali za hofu. Mudy alifanikiwa kulimudu gari akilipakia pembezoni mwa barabara.

“Shit!” Akalaani akisaga meno. Dereva bodaboda alitokomea asionekane wapi alipoelekea. Hakuna hata aliyenakili pleti namba yake.

“Ahsante, Mungu!” Sara alisema akihema kwanguvu. Vifua vyao vilikuwa vinapwita kwa hofu pana. Sasha yeye alikuwa ameishiwa nguvu kabisa.

Hawakuamini kama wametoka salama katika sekeseke hilo. Walikuwa wazima wa afya ila shepu ya mbele ya gari ikiwa imeharibika kiasi.

Punde alitokea dereva wa gari lile lililoparamiwa wakati Mudy anamkwepa bodaboda. Akaongea na Mudy kwa muda mchache kabla Mudy hajatoleshwa pesa, noti nyekundu kadhaa, dereva huyo akaondoka zake.

Hwakuhitaji trafiki polisi, waliona ni vema wakamalizana wenyewe.

“Pole sana, Mudy. Sasa?” Sara aliuliza.

“Siku yangu ishaharibika. Sina pesa yoyote hapa, yote nimetoa sababu ya yule bodaboda fala!”

“Pole sana, Mudy. Ila bora una uhai, hayo mengine ni ziada tu, na yanatafutwa.” Sasha alimfariji. Mudy akashusha pumzi ndefu.

“Tatizo gari yenyewe ilikuwa ina mafuta kiduchu, nilikuwa nimepanga nipitie sheli hapo mbele nitie mafuta, sasa pesa imeshaenda … anyway, nyie pandeni tu daladala muende, mie n’tajua cha kufanya.”

Sara na Sasha wakaondoka zao. Mudy akasema na yake kifuani: kweli wanawake si wa kuwategemea kwenye shida, hapa ningekuwa na wash’kaji zangu chap tatizo lingekuwa limeisha.

Akiwa hapo bado hajajua cha kufanya, mara Range Rover sport inatokea na kupaki kandokando yake, Kinoo anashuka na kumsalimu. Anamjulia hali na anapendekeza kumsaidia.

“Pole sana, ndiyo mambo ya barabarani hayo. Sasa inabidi uipeleke gereji ifanyiwe matengenezo.”

Mudy akaomba apelekwe kwanza ATM apate kutoa pesa kwa ajili ya mahitaji yake. Kinoo akambeba kumpeleka huko. Safari ikasindikizwa na soga ambazo Kinoo alikuwa amelenga kupatia majibu maswali yake.

“Nyumbani ni mbali sana?”

“Kiasi, naishi Mbweni.”

“Mmh … ni mbali!”

“Basi mie kwakuwa nimeshapazoea, naona si mbali sana. Ila kila mtu ninapomwambia naishi Mbweni husema ni mbali.”

Kinoo akatabasamu pasipo kuonyesha meno.

“In fact, ni mbali … Ila inabidi upunguze mawazo usije ukapata maswahibu mengine barabarani, Mudy. Mambo kama yale hutokea tu.”

Mudy hakuelewa, kabla hajapata mwanya wa kunena, Kinoo akaendelea kujazia nyama simulizi yake.

“Kiukweli Brokoli hakutakiwa kukukrash namna ile, alifanya makosa. Sikupendezwa naye kabisa. Na naanza kupata mashaka kama tutawezana naye kwenye biashara.”
Mudy akaguna na kutikisa kichwa pasipo kutia neno.

“Kama kuna watu ambao wamezaliwa kwa ajili ya biashara duniani, Bite alikuwa mmojawao. Mwanamke yule alikuwa smart sana. Anajua kuongea, kupanga na kusimamia. Alikuwa mhimili mkubwa wa kampuni yenu. Pengo lake gumu kulijaza.”

“Ni kweli,” Mudy akaunga mkono hoja. “Zaidi ya yote alikuwa anaishi vizuri sana na wafanyakazi wake, kila mtu alikuwa anampenda. Kifo chake kilitushtua mno. Ametuacha kwenye mikono migumu.”

“Kwakweli. Ni jukumu letu kuhakikisha angalau kifo chake kinaheshimiwa kwa kupata haki na kuwatia nguvuni wauaji.”

“Kivipi sasa na wakati polisi na mkurugenzi hawaeleweki? Naona kama Bite ameenda na hamna lolote litakalokuja kufanyika.”

“Wewe unataka iwe hivyo?”

“Hapana, ila sina la kufanya sasa.”

“La kufanya halikosekani Mudy. Mimi pia sitaki iwe hivyo kama wewe, sasa watu wawili ni wachache kufanya jambo?”

Mudy akasita kujibu.

“Ulisema ni Barclays?” Kinoo aliuliza. Mbele yao umbali mfupi kulikuwa kuna ATM ya Barclays. Yalikuwa ni maeneo ya Sinza, Kijiweni.

“Yah! Ni Barclays,” Mudy akalipuka kujibu. Gari likatafuta mahali pa kuegeshwa, akashuka na kwenda kwenye ATM kutoa pesa. Kinoo akampeleka tena sheli alipochukua mafuta kwa kutumia kidumu kisha akamrejesha mpaka kwenye gari lake.

Wakaagana, Kinoo akahepa zake wakipeana miadi ya kukutana karibuni wapate kutazamia namna gani ya kujadili na kufufua kesi ya Bite. Walibadilishana namba za simu kwa ajili ya mawasiliano zaidi.


***


Majira ya saa nane mchana, maeneo ya Mwenge.


Kwa kiasi kikubwa sasa Jona alikuwa amesogeza kazi zake zilizokuwa zimemtinga. Mgongo ulikuwa unamuuma kwasababu ya kuukunja kwa muda mrefu. Alijinyanyua akaunyoosha akipiga mihayo.

Alimtazama Jumanne aliyekuwa amelala kitini, akamshtua na kumuuliza:

“Vipi, hatwendi kula?”

Jumanne akatikisa kichwa na kufumba macho yake mazito mekundu.

“Unaendekeza usingizi enh?”

“Hamna … sina njaa.”

“Njaa unayo sema usingizi kwako ndiyo bora zaidi. Haya mimi naenda.”

Jumanne akatikisa kichwa akiwa amefumba macho yake.

“Sasa ukiwa umelala, utaona wateja kweli Jumanne?”

“Nikisikia tu miguu, naamka,” Jumanne akajibu akiwa bado amefumba macho. Jona akatikisa kichwa na kwenda zake kwa mama K wa mgahawani.

Kama kawaida aliketi na kutoa simu yake wakati anangojea chakula na kuanza kuiperuzi. Alizama mtandaoni Facebook, akakuta jumbe tano, nne toka kwa mwanamke yule wa Afrika ya kusini.

Alikuwa anamjulia hali na pia amemtumia picha kadhaa za bidhaa zake, nguo na mikoba akiulizia kuhusu mrejesho wa fasheni. Jona akampuuzia. Akaenda moja kwa moja kwenye ujumbe mmoja uliosalia, ulikuwa pia wa mtu mgeni – mwanaume mmoja toka Uarabuni.

Nayo akapuuzia.

Hakuona kama kuna la maana huko mtandaoni. Akakagua akaunti ya Mariam – mke wa mheshimiwa, hakupata jambo. Basi akaamua kuacha simu na kufikiri mambo yake mengine.

Chakula kikaja, akala taratibu. Alimfikiria Nade kidogo, akaachana naye. Alimfikiria Mheshimiwa, hapo akakumbuka kwamba ana miadi naye siku hiyo. La haula! Alikuwa amesahau kabisa.

Alitazama saa yake mkononi. Aliwaza ni muda gani anaweza akaenda kumuona Mheshimiwa, akaona kuna haja ya kumuuliza. Akanyanyua simu na kumpigia. Simu ikaita pasipo majibu.

Alirudia kwa mara nne lakini hakukuwa na mabadiliko. Akapata mkanganyiko.

“Pengine akikuta missed calls zangu atan’tafuta,” alihitimisha kwa kusema hivyo kabla hajaweka simu chini, akamalizia chakula.

Akalipia na kutoka ndani.

Akiwa hana hili wala lile akashika barabara kufuata njia mbili kubwa za lami apate kuvuka na kwenda ofisini. Alivuka njia ya kwanza. Akiisogelea ya pili, kuna gari moja ndogo Mark 2 nyeusi, ikahamia upande wa pili wa barabara.

Upande huu ndiyo ambao Jona alikuwepo akiangaza avuke barabara.

Baada ya kuona kuna mwanya wa magari, Jona akashusha miguu yake juu ya lami na kupiga hatua za haraka haraka avuke salama.

Ajabu ile Mark 2, upesi nayo ikahama upande, ila sasa ikiwa imeongeza kasi maradufu! Mlio wake mkali uliokuwa unanguruma ulimshtua Jona, akarusha macho yake kutazama.

Hatua kama tano tu mbele yake, gari hilo, Mark 2, lilikuwa linakuja kwa kasi kubwa. Kwa mahesabu tu ya haraka ni kwamba asingeweza kumaliza barabara kwa kasi ya hatua zake.

Haraka aliwaza. Akarusha hatua zake kukimbia, ila napo hakuweza kumaliza kuvuka, gari lilikuwa tayari limeshamfikia karibu mno kumpindua na kumvunjavunja.

Hapo sasa ikabidia atumie ujuzi wake kujiokoa maisha. Kwa kutumia mguu wake mmoja akajirusha juu, kufumba na kufumbua, mgongo wake ukatua kwenye bodi la gari, akabiringita mara mbili kabla hajamwagikia kando gari likipita!

Alitua akiweka mkono wa kulia chini, mguu wa kushoto ukinyookea nyuma na wa kulia ukiwa umejisimika kwa kuukunja.

Ilikuwa ni ajabu! Walioshuhudia tukio hilo waliachwa kwenye bumbuwazi. Walichozoea kukiona kwenye tamthilia walikiona mbele ya macho yao, tena kamera zikiwa hazipo.

Upesi alisimama kana kwamba hakuna lililotokea, akatafuta miwani yake aliyoiona kando na kuiokota. Ilikuwa imevunjika kioo kimoja na fremu zake zikiwa legelege. Akaikunja na kuiweka mfukoni, akaenda zake ofisini.

Watu walikuwa wanamtazama, wengine wakidhani pengine ameumia pasipo yeye mwenyewe kujua. Aliwaambia yu salama akizidisha hatua apotee hapo.

“Upo sawa, Jona?” Jumanne alimpokea kwa maswali.

“Nipo sawa, usijali J,” Jona akajibu akiketi kitako kwenye kiti. Akachomoa miwani yake mfukoni na kuitazama.

Jumanne alikuwa anamkagua kwa kumuangaza huku na kule kama ataambulia kuona jeraha. Macho yake yalionyesha bado yupo kwenye bumbuwazi la kutoamini kilichotokea.

Kabla Jona hajaanza kuwaza kuhusu lile gari, alikuwa anawaza kuhusu miwani yake kwanza. Alijua fika yeye pasipo miwani ni nusura kipofu. Miwani yake ndiyo macho yake, sasa itakuwaje pasipo nayo?

Ataweza pambana kwenye hii vita akiwa haoni? Alijikuta anajiuliza.


*NANI ALIYEKUWA ANATAKA KUMGONGA JONA?*

*NINI JONA ATAFANYA NA NUSURA UPOFU WAKE?*

*KINOO ATAFANIKIWA KUPATA NINI KWA MUDY?*

*MWANAMKE WA AFRIKA YA KUSINI NI NANI?*
 
Back
Top Bottom