Anga la washenzi na Joana anaona kitu usiku

Anga la washenzi na Joana anaona kitu usiku

vitu vya usiku bado tu havijaanza kuonekana?basi tuputishe kwenye anga za washenzi
 
*JOANA ANAONA KITU USIKU ---- 09*

*Simulizi za series*


ILIPOISHIA

Aliufunga mlango akarudi kitandani.

Hakulala sasa mpaka jua linachomoza. Asubuhi ndiyo akapata usingizi, ambao ulikuja kukatishwa na hodi.

Alikuwa ni inspekta Westgate ndani ya suti yake rangi ya udongo na briefcase nyeusi mkono wake wa kulia.

ENDELEA…

“Karibu,” Joana alimkarimu inspekta kwa mshangao. Alijawa na hofu sana, moyo wake ulianza kukimbia kwa kasi. Alijikuta anaanza kutetemeka viungo kwa kuhofia mkono wa dola.

“Bila shaka wewe ni Joana …”

Joana akasita kwanza kabla hajapandisha kichwa chake juu taratibu, akajibu kwa sauti ya chini:

“Ndio.”

Inspekta akajitambulisha na kuonyesha kitambulisho chake, kisha akasafisha koo lake na kumtazama Joana machoni.

“Joana, unaongeleaje mauaji yanayotukia hapa chuoni?”

Joana akameza kwanza mate.

“Yanatisha … yanatisha kwakweli,” akajibu, kwa sauti yake ya chini ileile.

Inspekta akafungua briefcase yake na kutoa picha kadhaa. Zilikuwa ni picha za watu wote waliouawa hapo chuoni, kumi na kitu. Akaishika picha ya kwanza ya mwanamke yule marehemu, mnaijeria, akamwonyesha Joana.

“Unamjua huyu?”

Joana akatikisa kichwa kuafiki.

“Anaitwa nani?”

“Anaitwa Judith.”

“Alikuwa anaishi wapi?”

“Alikuwa jirani yangu, chumba kinachofuata.”

“Unadhani aliuawa na nani?”

“Sijui!”

Inspekta alifanya hivyo kwa picha zote akizionyesha na kumuuliza maswali Joana juu ya ufahamu wake kwa marehemu, na kisha nani aliyemuua. Majibu yake yakawa sijui … sijui.

Lakini Inspekta alipofikia kwenye picha ya mwisho, ya marehemu wa mwisho kabisa kuuawa, mlinzi aitwaye bwana Rodney Windows, Joana akasita kutoa jibu kwa wepesi.

Inspekta akamkazia macho na kurudia swali:

“Unadhani nani aliyemuua?”

“Sijui,” akajibu akitikisa kichwa.

“Unadhani muuaji ni jinsia gani?”

“Ya kiume.”

“Umejuaje?”

“Nimebuni tu,” Joana akajibu akipandisha mabega juu.

“Joana,” inspekta akaita. “Muuaji alikuwa amevaa shati la njano kwa mujibu wa kamera, na alielekea upande huu wa kipande cha bweni lenu, unadhani alielekea wapi?”
Joana akatikisa kichwa.

“Sijui.”

Mpaka hapo alikuwa anahisi haja zote zinambana. Alihisi baridi vidoleni na kichwa kikimgonga mno. Kila sekunde iliyokuwa inaenda mbele, kwake ilikuwa ngumu zaidi ya nyuma.

“Haukusikia chochote, aidha vishindo vya miguu?”

“Sikusikia, nilikuwa nimelala.”

“Ulizima taa?”

Joana akababaika kidogo. Akawaza, akaona akisema taa ilikuwa inawaka, basi ataulizwa na itabatilisha hoja yake kwamba alikuwa amelala. Na hivyo kama hakuwa amelala basi lazima atakuwa amesikia vishindo vya miguu.

Basi akasema:

“Nilikuwa nimezima, ndio.”

“Kwa mujibu wa kamera za nje, haukuwa umezima taa.”

“Sidhani, pengine mmechanganya vyumba.”

Inspekta akatoa picha fulani hafifu toka kwenye briefcase. Akampatia Joana. Ilikuwa ni picha iliyochukuliwa toka kwenye kamera za cctv zikionyesha muda kwa chini.

Kwa mujibu wa muda huo, ilikuwa ni saa nane na nusu usiku.

“Hicho si chumba chako?”

“Labda mwenzangu aliamka usiku, siwezi jua!”

Inspekta akanyaka picha yake na kurejesha ndani ya briefcase. Hakuuliza kuhusu chumba, akafunga mkoba wake na kumtazama Joana.

“Ulikuwa na mgeni yoyote usiku mzito wa kuamkia leo?”

“Hapana, sikuwa na mgeni.”

“Ila ulikuwa macho na taa ilikuwa inawaka.”

Joana akasita. Akahofia kudanganya.

“Ndio, taa ilikuwa inawaka.”

“Na ulikuwa macho.”

“Yah … n’likuwa macho.”

“Mlinzi aliona alama za viatu katika korido yenu, na mtu aliyekuwa na viatu hivyo alikatiza wakati wa usiku, muda si mrefu sana baada ya mlinzi kukatiza kuwaonya na kuwakataza juu ya ugeni. Mtu huyo hakuja kwako?”

“Hapana, hakuja kwangu.”

“Alielekea wapi?”

“Sijui.”

“Ulimsikia anaenda wapi?”

“Sikumsikia.”

“Na ulikuwa macho!”

“Ndio. Labda kwasababu nilikuwa natazama tamthilia.”

“Nyayo za mtu huyo zilikuwa zinaonekana vema, kumaanisha hakuwa ananyata bali anatembea kawaida. Una uhakika hukusikia kitu?”

Joana alihisi joto kali. Aliona kama vile inspekta amemuweka kwenye uwanja kisha akaketi kumtazama namna anavyohangaika huku na kule. Alitamani ayeyuke. Aliona kama anakabwa.

“Sikusikia kitu.”

Inspekta akashusha pumzi ndefu. Akanyakua mkoba wake na kuukumbatia.

“Mtuhumiwa wa kwanza wa mauaji ya mlinzi, ni mwanaume mwenye viatu vyenye alama hizo kwani alama hizo hizo za viatu ndizo zimebainika kwenye eneo la tukio la mauaji ya mlinzi.”

Inspekta akaweka kituo. Akamkazia macho Joana, Joana akatazama chini.

“Naweza nikaona mguu wako?”

Joana akatahamaki. Mguu wangu wa nini? Akajiuliza kifuani. Ina maana anaufananisha na wa muuaji wa mlinzi? Akaendelea kujiuliza akiunyanyua mguu wake na kumkabidhi inspekta.

Inspekta akafungua mkoba wake, akatoa kipima urefu, akaupima mguu wa Joana, urefu na upana kisha akarudisha kifaa chake ndani.

“Ahsante sana,” Inspekta akasema akinyanyuka. “Naweza nikakutembelea kama nikiona kuna hitaji hilo,” inspekta akaaga kwa hayo maneno, akaenda zake akimwacha Joana hali si muhali.

Joana alishusha pumzi ndefu akajilaza kitandani. Akaamka upesi na kwenda kwanza kupata maji kupooza kifua. Alikunywa glasi mbili kabla hajarejea kitandani na kujilaza tena.

Alishangaa ilikuwaje inspekta akamuacha huru. Alijikuta anapata mawazo mengi sana kichwani ambayo yalizidi kumuumiza kichwa.

Aliona kuna haja ya kuonana na Moa, tena upesi kumpasha habari. Hata hakungoja avae wala kuoga, akaenda zake kama alivyokuwa amelala na kuamka.

Alimtafuta sana Moa, tafuta na tafuta pasipo mafanikio yoyote yale. Alizunguka chuo kizima, kwa gari na miguu, lakini hola! Hakuona wala kumsikia Moa.

Alichoka akarudi ndani.

“Moa, ana matatizo gani? Yupo wapi?”

Siku nzima hakuwa na amani wala raha. Hakula wala kunywa. Alijaribu kumpigia Moa lakini hakupatikana. Alihisi kuchanganyikiwa. Hata Lisa aliporejea hakutaka kuongea naye.

Usiku usingizi haukuja, aliwaza, je atoroke? Ajiue? Au afanye nini?

Usiku ukazidi kusonga na kusonga. Kwenye majira ya saa nane, mlango ukagongwa. Akashtuka na kutazama.



JE, NI NANI HUYO MLANGONI?

NINI INSPEKTA AMEKIPATA TOKA KWENYE MAHOJIANO NA JOANA?

Usikose sehemu ijayo.







Sent from my SM-J110F using JamiiForums mobile app
 
*JOANA ANAONA KITU USIKU --- 10*

*Simulizi za series*


ILIPOISHIA

Usiku usingizi haukuja, aliwaza, je atoroke? Ajiue? Au afanye nini?

Usiku ukazidi kusonga na kusonga. Kwenye majira ya saa nane, mlango ukagongwa. Akashtuka na kutazama.

ENDELEA...

Alimtazama Lisa akamuona amelala hajitambui. Akautazama mlango akijiuliza maswali kifuani. Ni nani huyo? Moa?

Akaamua kunyamaza. Hakutaka kuitikia hodi hiyo.

"Kama ni Moa nilishamwambia asije tena muda huu!"

Hodi ikaendelea kugonga pasipo kukoma, mwishowe Lisa akaamka.

"Joana, nani huyo muda huu?" Akauliza kwa sauti yenye ulevi wa usingizi.

"Sijui!" Joana akajibu, bado alikuwa anatazama mlangoni.

"Umeuliza lakini?"

"Sijataka hata kuuliza."

"Sasa atapiga hodi mpaka lini?"

Joana kimya. Lisa akapaza sauti yake:

"Nanii?"

"Moa!" Sauti ikajibu huko nje.

"Ni Moa!" Lisa akatahamaki akimtazama Joana. Joana alikuwa ametulia kana kwamba hajasikia.

"Kamfungulie, la sivyo atakamatwa hapo nje na wewe utakuwa matatani!" Akasihi Lisa. Basi Joana akanyanyuka na kwenda mlangoni.

Akafungua mlango, Moa akazama ndani upesi.

"Unataka nini muda huu?" Lilikuwa swali la kwanza la Joana.

Hakutaka kabisa kumuelewa Moa pasipo kujali namna gani alivyokuwa anajitetea. Alikuwa ameghafirika na kumchoka Moa kwa matendo yake yasiyoeleweka.

"Unaishi wapi? - kwanini unanijia saa nane za usiku?" Yalikuwa maswali ambayo Moa alishindwa kuyajibu.

Pasipo kujali ilikuwa ni majira ya usiku, Joana alijikuta anapaza sauti kufoka na kufoka. Lisa akajaribu kumtuliza pasipo mafanikio.

"Moa, nimechoka. Na tafadhali naomba kila mtu aende na njia yake!"

Kabla Moa hajasema jambo wakasikia hodi mlangoni.

"Mlinzi hapa, kuna shida gani humo ndani?" Ilikuwa sauti ya kike.

Joana na wenzake wakatahamaki. Moa akikutwa humo ndani itakuwa kazi si kidogo, haraka wakashauriana wamfiche ndani ya kabati.

Wakafanya hivyo kisha mlango ukafunguliwa.

"Kuna nini humo ndani?"

"Samahani, tulikwaruzana kidogo," akajibu Joana akijitahidi kutabasamu.
Mlinzi akatazama ndani, akamuona Lisa akiwa ameketi kitandani.

"Kama vile nilisikia sauti ya kiume."

"Hapana! Itakuwa umesikia vibaya tu."

Mlinzi akaingia ndani kuhakikisha. Kwakuwa alikuwa mwanamke basi hakuwa na pingamizi kuwandawanda chumbani humo.

Aliangaza asione lolote la kutilia mashaka.

"Bweni zima lilikuwa limetawaliwa na kelele zenu, hamjui muda huu ni usiku sana?" Mlinzi aliwaka.

"Samahani, tunaahidi haitajirudia tena," akasema Joana.

Mlinzi akawatazama tena kabla hajaondoka zake.

Wakamtoa Moa kabatini.

"Sasa tunafanyaje Joana?" Akauliza Lisa.
"Huoni tukimtoa Moa sasa hivi atakamatwa huko nje?"

Joana hakujibu kitu. Akamtazama Moa na kumwambia:

"Toka chumbani kwangu, usirudi tena hapa!" Kisha akaufungua mlango na kusontea nje.

"Nakupenda, Joana. Na sitaacha ku ..."

"Nenda nje!" Joana hakutaka maelezo. Macho yake yalikuwa mekundu, na pua pia.

Moa akautazama mkufu wa Joana kifuani. Akatabasamu na kwenda zake.

"Ilimradi una huo mkufu kifuani, basi daima utakuwa nami," Moa alisema kifuani akiyoyoma.

Ingali walinzi walikuwa wametapakaa huko nje tangu mauaji yatokee, hakuna hata mmoja aliyemuona Moa.

Alikatiza kwa amani akielekea misituni. Alikwepa taa zote akienenda kwenye njia ya giza.

Kadiri alivyokuwa anazama ndani ya msitu akawa anabadilika umbo, sura na mwendo. Alikuwa anatisha asieleweke kama ni binadamu, kigagula ama kibwengo.

Hakuwa kiumbe chenye taswira ya Moa tena, bali mnyama ama jitu!

Kabla hajapotelea humo msituni, mjumbe mmoja wa ulinzi shirikishi alimuona, akapaza sauti:

"Hey! Unaenda wapi?"

Mlinzi huyo shirikishi alikuwa amebebelea kurunzi na bunduki kubwa.

Kile kiumbe kikamtazama. Mlinzi alipokimulika akastaajabu, hakukielewa! Kilikuwa ni kama kivuli kikubwa kilichoganda.

Ni macho tu ndiyo yalibakia wakati mwili mzima ukiwa mweusi ti na umbo la ujiuji.

La haula! Mlinzi akajikuta anaishiwa nguvu baada ya kuona kiumbe hicho chaja kwa kasi kumfuata.

Haraka alichukua filimbi iliyokuwa inaning'inia kifuani mwake, akapuliza kwanguvu akikimbia.

Hakupata hata wazo la kutumia silaha yake. Pengine aliona atachelewa ama basi haitasaidia lolote.

Alikimbia haraka mno, lakini kile kiumbe kikawa kinamkaribia kwa kasi mno hatua kwa hatua!

Ilikuwa bayana mlinzi asingefika kwenye makazi ya watu kabla hajatiwa nguvuni. Alishakaribiwa kiasi cha kutosha!

Akaanguka chini. Sasa mchezo kwake ukawa umekwisha. Alimtazama kiumbe kilichokuwa kinamkimbiza akahisi hofu kubwa ndani yake.

Haraka akateka bunduki yake na kuanza kufyatua kwa fujo. Hazikusaidia. Ajabu kile kiumbe kikaanza kummeza!

Si kwa mdomo la hasha bali kwa mwili. Kilikuwa kinamsogelea zaidi mlinzi, miguu ya mlinzi ikawa inapotelea ndani ya mwili wa kiumbe isijulikane wapi ilikuwa inaelekea.

Ni kana kwamba alikuwa anazama ndani ya maji!

Katika kuhangaika, mlinzi akateka kurunzi yake na kummulika kiumbe usoni. Kile kiumbe kikapagawa. Kikapiga kelele kali kikijitahidi kujikinga.

Hiyo ikawa salama ya mlinzi.

Alimmulika zaidi na zaidi akijitahidi kukwamua miguu yake toka kwenye tope la mwili wa kiumbe.

Akafanikiwa.

Kiumbe kikashindwa kustahimili zaidi mwanga wa kurunzi, haraka kikapotelea msituni kwa kasi! Punde walinzi wengine, watatu kwa idadi, wakatokea na kumkuta mwenzao akiwa chini.

Wakamuuliza nini kimemkumba, akawaelezea. Wakamnyanyua na kumpeleka mahali salama.

"Ulimuona ametokea wapi?"

"Hapana! Nilimuona tu akielekea msituni."

"Inawezekana akawa ndiye muuaji?"

"Sijui! Hakuwa hata na miguu, uso wala umbo la binadamu."

Taarifa zikafikishwa polisi, mapema ya saa kumi na moja polisi wakafika wakiongozwa na inspekta Westgate.

Wakapekua eneo zima la tukio.

"Inaweza ikawa ndiye muuaji," akasema inspekta. "Alama za viatu vilivyopatikana hapa ndivyo vilevile vilivyopatikana eneo la mauaji ya mlinzi."

Basi ikatolewa amri ya kusakwa pori zima. Polisi zaidi wakaongezeka wakiwa na kikosi cha mbwa.

Wakasaka pori lote, lilikuwa na ukubwa wa kilomita za mraba mia mbili hamsini. Walimaliza msako wakitumia muda wa masaa sita, hawakufanikiwa kupata mtu.

Ila wakakuta mifupa ya binaadamu. Waliikusanya mifupa hiyo kwa ajili ya upelelezi zaidi.

Mojawapo ya mifupa ilionyesha mhanga hakuwa ameuawa kwa muda mrefu. Bado mifupa yake ilikuwa na utelezi na mabaki ya damu.

Ila kabla ya polisi hao kuondoka, inspekta akamchukua Lisa, mkazi mwenza wa Joana. Alimwambia ana maswali kadhaa anayotaka kuyapata majibu toka kwake.

Lisa alikuwa peke yake chumbani wakati alipokuja kuchukuliwa. Ila alipotiwa ndani ya gari la polisi, Joana alijitokeza na kushuhudia tukio hilo.

Alipata mashaka sana. Hakuna yeyote anayejua siri yake na Moa zaidi ya Lisa. Je, ataenda kusema?



*Usikose sehemu ijayo.*

Sent from my SM-J110F using JamiiForums mobile app
 
Back
Top Bottom