*ANGA LA WASHENZI --- 42*
*Simulizi za series*
ILIPOISHIA
Akiwa humo fikirani, anashtuliwa na sauti kubwa! Gari lao linayumba vibaya mno! Dereva anajitahidi sana kulimudu na kuliweka sawa. Jona anakuja kusoma mchezo, walikuwa wamepushiwa na gari moja kubwa jeusi, Toyota Prado. Na halikuwa mbali.
Bado dereva akihangaika kuweka matairi sawa, prado ikashusha vioo, mkono mweupe uliobebelea bunduki aina ya SMG unatoka. Haraka Jona akapiga kelele:
“Lala chini!”
Mara risasi zikaanza kumwagwa kama njugu kushambulia taksi waliyomo Jona na wenzake. Dereva anakula risasi nne na kufa papo hapo. Taksi inaacha njia na kufuata fremu za maduka kwa kasi.
ENDELEA
Sasa hakukuwa na namna la sivyo wanaenda kufa wote. Jona akajirusha upesi toka kwenye viti vya nyuma na kuudaka usukani tena huku akipambana na mwili mfu wa dereva. Akajitahidi kuwakwepa watu na mali zao japo hakufanikiwa kwa kiasi kikubwa, akapasua na kubinua nyungo za karanga na kadhalika.
Lakini hatimaye akafanikiwa kurejesha gari barabarani. Taharuki na makelele yakiwa yametamalaki, magari mengine yakiwa yamesimama ama kuhepa kujiepusha na hasara ama vifo!
Akiwa mtulivu, macho yake yakatazama gari lile lililokuwa linawashambulia, Prado nyeusi, basi akadhamiria kufanya jambo. Taratibu akaanza kuutafuta mwanya wa kuisogelea gari hilo ambalo kwa muda huo tayari yule mshambuliaji alikuwa ameurejesha mkono wake wenye silaha ndani.
Akayekwepa magari ya mbele na pembeni yake kwa ustadi. Kufanikisha adhma yake ikamlazimu atumie barabara ya wanaokuja, si wanaoenda kama yeye. Na hivyo basi ikamlazimu tena awe makini kupitiliza. Akifanya hayo Nade akajawa na hofu kubwa, hata akapiga kelele kumtaka Jona asitishe zoezi.
“Jona, are you crazy!” (Jona, umewehuka!) akawaka akiwa amejishikiza kwenye viti. “Stop the car! Simamisha gari!”
Lakini Jona hakujali, akaendelea kusaka lengo lake. Si kuwaua wale waliokuwa wanamshambulia, lah! Hakuwa na silaha pamoja naye ila alitaka kulitambua gari hilo vema na hata wale waliomo ndani.
Akajitengenezea vema kwenye kiti cha dereva baada ya kumsukumia dereva yule mfu kando. Akakanyaga mafuta na kuendesha atakavyo. Lakini bado muda ukawa haupo upande wake, chombo chake hakikuweza kufua dafu kupambana mwendokasi na Prado, akaachwa.
“Damn it!” akalaani akisaga meno. Akabadili mwelekeo akirejea nyuma kidogo na kisha akachukua njia ya kushoto. Mwendo ukabadilika, akawa anasukuma magurudumu kwa mwendo kati.
“Watakuwa ni wale watu! – wakina Nyokaa!” Akasema Nade. Bado moyo wake ulikuwa unaenda mbio asiamini kama ametoka salama kwenye yale mashindano.
“Hapana!” Jona akatikisa kichwa. “Sio hao unaowadhani.”
“Ni wakina nani basi kama si wao ambao wangefuata roho yetu?” Nade akauliza.
“Sijajua ni wakina nani ila sio hao unawafikiri. Mosi, hakuna mtu anayenijua kama mimi ndiye nahusika na kukuokoa isipokuwa mheshimiwa peke yake. Niliyatenda yote sura yangu ikiwa nyuma ya kinyago.
Pili, kabla sijafanya zoezi la kukuokoa nilifanya upekuzi wa mazingira yote, hamna mahali niliona lile gari. Haitaleta maana kusema wao wanahusika, labda tu kama tungekuwa tumetokea nyumbani kwa mheshimiwa, hapo tungesema walianza kutufuatilia tokea huko, maana makazi yake watakuwa wanayajua.”
“Sasa atakuwa ni nani?” Nade akashupaa kuuliza.
“Sijui ni nani,” akajibu Jona. “Ila atakuwa anawinda roho yangu, si yako!”
Baada ya nusu saa …
“Kwahiyo mwili wake upo wapi?” akauliza Mheshimiwa akiwa ameshikilia kiuno. Alikuwa amevalia kaushi nyeupe nyepesi na bukta iliyokomea juu ya magoti. Usoni akiwa amevalia miwani ya kusomea. Mkono wake wa kuume umebebelea gazeti.
“Upo ndani ya gari!” akajibu Jona.
“Kwahiyo hamjafanikiwa kabisa kugundua hao watu? Kabisa yani!”
“Sijafanikiwa, ila najua muda si mrefu ukweli utajiweka bayana.”
“Ebu twendeni kwanza ndani … tuingie ndani …” mheshimiwa aliwasukumizia Jona na Nade ndani huku akiperuzi macho yake huku na kule. Baada ya muda mfupi mezani kwao kukawa kumependezeshwa na vinywaji vilaini. Nade alikuwa ameketi kando ya Mheshimiwa, Jona akiwa amejitenga kwa umbali mdogo akiketi kwenye kiti cha kuwatazama.
“Hapa hapatakuwa mahali salama tena, ni kheri ukachukua tahadhari mapema,” Jona akashauri.
“Najua hilo na bila shaka umeshaliona. Nimeongeza walinzi sasa maradufu!”
“Sidhani kama watatosha, bado ni wachache. Adui yako ana jeshi kubwa, kwa idadi na hata nyenzo,” Jona akanguruma. “Nakushauri uwe makini zaidi.”
“Sasa Jona na ndiyo hapo sasa nami ninapokuja kwenye ombi langu. Najua endapo nikiwa na wewe basi nitakuwa salama salmini, mkishirikiana na Nade hapa. Walionaje hilo?” Mheshimiwa akatia nadhiri.
Kukawa kimya kidogo.
“Miriam yupo wapi?” Jona akauliza. Mheshimiwa akamtazama Nade kwanza kisha akaurejesha uso wake kwa Jona na kujibu:
“Yupo ndani.”
“Naweza nikamwona?”
“Ya .. yah! Unaweza ukamwona,” Mheshimiwa akajibu. Kukawa kimya kidogo.
“Ila si kwa sasa, Jona,” Mheshimiwa akapendekeza.
“Kwanini si sasa?” Jona akauliza. Mheshimiwa akawa kimya kidogo. Kisha akanyanyuka na kwenda ndani, baada ya dakika mbili akarejea akiongozana na Miriam aliyekuwa mchovu na mwenye huzuni. Alikuwa amevalia dera akitembea kama mwanamke aliyetoka leba.
Jona akamsalimu, hakuitikia. Akamrushia macho yake makali akiwa ameuvuta mdomo. Hakujalisha Jona ameongea kitu gani, yeye hakutia neno hata moja. Macho yake ndiyo yalibadilika rangi kuwa mekundu, na ndani ya kinywa chake akisaga meno.
Baada ya muda huo usiokuwa na matunda, mheshimiwa akamnyanyua mwanamke huyo kumrejesha ndani. Hapo sasa akaufungua mdomo wake akimtazama Jona. Akamlaani vikali akimrushia matusi.
“Sitakusamehe maisha yangu yote kwa kunileta jehanamu!”
Mheshimiwa akampeleka ndani ya chumba na kumfungia.
“Naweza nikaambiwa sasa nini kinaendelea hapa?” Jona akauliza akimtazama Mheshimiwa ndani ya mboni zake. Mheshimiwa akashusha pumzi, kisha akashushia na juisi yake ya komamanga.
“Jona, ni simulizi ndefu sana hii. Ni simulizi ambayo isingependeza kabisa kusikika kwenye masikio ya yeyote yule, haswa mtanzania. Ni simulizi ya kutisha ambayo yaweza kukufanya ukashindwa kulala kwa ndoto za jinamizi!”
“Nipo tayari kuisikia simulizi hiyo,” akasema Jona. Basi Mheshimiwa akamtazama Nade na kumpandishia kichwa pasipo kutia neno. Nade akanyanyuka, na kwa mwendo wake wa majeruhi, akasonga kuondoka zake.
“Jona,” Mheshimiwa akaita. “Mimi si kiongozi mzuri, si mfano wa kuigwa wala sistahili kuwepo kwenye kiti hiki. Ni mambo mengi nimefanya, na yote hayo ni kwa ajili yangu si kwa taifa wala wananchi. Kuna muda nafsi yangu inanisuta sana, lakini sina namna maana yaliyopita hayawezi tena kubadilika.
Nimeshaingia kwenye anga la wenyewe, nikavinjari ninavyotaka, kutua chini ni ngumu …”
Nade akarejea akiwa amebebelea kiboksi kidogo cha chuma. Akamkabidhi Mheshimiwa aliyekipokea kwa mikono miwili na kisha akakiweka mapajani. Akaendelea kunena akiwa anafungua kiboksi hicho.
“… maana nimeshazoea hewa ya huko juu kiasi kwamba naona nikitoa naweza nikafa kwa kukosa pumzi. Kutua chini kutaninyima uhuru niliozoea kwenye anga hilo … kwahiyo siwezi, siwezi tena kutua. Siwezi kurudi tena ardhini.”
Alipomaliza kusema hivyo, mara mkono wake ukatoka ndani ya kiboksi ukiwa umebebelea bunduki ndogo nyeusi. Akamnyooshea Jona.
“Na hivyo basi, haitakiwi mtu yeyote kujua kama nami ni rubani kwenye anga hilo. Ni siri inayotakiwa kudumu milele, na milele, amin,”
Akafyatua risasi mbili kutoboa kifua cha Jona. Kisha akaangua kicheko akirejesha bunduki yake ndani ya kiboksi.
“Kwaheri Jona, kwaheri katuandalie makao.”
Akamuita mmoja wa walinzi wake waliokuwepo nje, akaunyooshea mkono mwili wa Jona.
“Beba hiyo na nyingine ndani ya taksi, kaitupie mbali!”
“Sawa mkuu!”
“Hakikisha hakuna mtu anayekuona, wala anayekufuatilia. Sawa?”
“Sawa!”
Mwanaume huyo mpana na mrefu, akaubeba mwili wa Jona na kutoka nao nje, akautupia ndani ya gari kisha akaubeba na ule wa dereva taksi, alafu akatimka akienda anapopajua yeye kichwani. Kwenda kuitupa miili hiyo isiwahi kuja kujulikana!
Huko nje ya jiji la Dar akaishusha na kuitelekeza baada ya kuhakikisha yupo mwenyewe, na kweli alikuwa mwenyewe. Akajipaki kwenye chombo na upesi akatimka.
“Ndio, mkuu. Kazi imeshakwisha!” akaongea mtumishi huyo mwadilifu.
Baada ya lisaa limoja …
Mtumishi huyo akafungua mlango wa sebuleni na kuangaza macho. Sura yake imebeba hofu na mazingira yalikuwa tulivu mno. Mkononi mwake alikuwa amebebelea bunduki ndogo. Haikuchukua muda, akaona mwili wa mheshimiwa pamoja na wa Nade ukiwa umelala kwenye kochi, damu zinawatiririka vichwani!
Akatahamaki. Akawatazama watu hao kwa macho ya bumbuwazi. Akakimbilia napo chumbani kutazama, Miriam hakuwapo! Chumba kilikuwa kitupu, mlango upo wazi.
NI NINI KIMEJIRI?