Anga la washenzi na Joana anaona kitu usiku

Anga la washenzi na Joana anaona kitu usiku

*ANGA LA WASHENZI --- 41*

*Simulizi za series*


ILIPOISHIA

Lakini kwa mara hii haikumuwia vigumu Jona. Alijua adui yake hakuwa sawa, na basi akamruhusu arushe shambulizi lake yeye awe wa mwisho. Roba akaingia mkenge. Aliruhusu hasira zikamtawala. Akairusha ngumi yake kwa pupa, Jona akaiyeya kama amefungiwa ‘springi’, Roba akakatiza hatua mbili mbele, Jona akamrusiha nyuma kwa teke la kukunjuka lililomkita kifuani. Roba akalala tuli asionekane mwenye dalili ya kuamka!

Jona akamuweka Nade mgongoni, wakaendelea na safari. Wakatembea kwa hatua kumi na tano, mara wakamulikwa na kurunzi!

Watatoboa?

ENDELEA

Jona akageuka na kuangaza mwanga huo watokea wapi na kwa nani, hakuona! Mwanga ulimpiga usoni na kumuumiza macho. Hakuwa na cha kufanya zaidi ya kukazana kukimbia. Alidhani aliyemnyoshea kurunzi ni adui, na yupo karibu.

Alikimbia kwa muda mrefu pasipo kusikia ama kuona chochote. Alifanikiwa kuchoropoka ndani ya ngome ya Nyokaa salama, mgongoni akiwa amembebelea Nade aliyekuwa hajiwezi kwa lolote.

Alikuja kugundua mbeleni ya kuwa kurunzi ile iliyommulika, ilikuwa ni ya Roba aliyemlaza chini, akifanya hivyo kuwapa ishara wenzake baada ya yeye kunoa nanga.

Baada ya nusu saa wafuasi wote wa Nyokaa wanakutana na kutoa taarifa kwamba hawajafanikiwa kumtia mikononi mvamizi wala mateka. Nyokaa ananghafirika, anapasua chupa alikuwa ameibebelea mkononi kisha alaani kwa matusi.

“Yani himaya hii ilivyo kubwa, mtu anatokaje kirahisi namna hiyo? Ni uzembe mkubwa kiasi gani? … Roba!” akaita. Roba akampatia macho na masikio. Alikuwa ameumia mdomo na upande wake mmoja wa uso ukiwa taabani.

“Unaweza ukaniambia ni kwa namna gani huyo ms** ametoka humu?!” Nyokaa akafoka. Akaongea na kuongea lakini hakuna hata mtu mmoja aliyesema neno. Wote walibakia kusikiliza kana kwamba mwalimu mkuu yupo ‘asembo’.

Nyokaa alikuwa ameudhika sana. aliona ni kama vile amevuliwa nguo mbele ya umati. Aliona amedharauliwa na kushushwa kiwango haswa. Inakuaje mtu azame ndani ya nyumba yake na kutawala meza?

Akachojoa sigara kubwa ndani ya mfuko wake, alafu akaiwasha akipepesuka. Akavuta pafu moja zito kabla hajautema moshi nje kana kwamba treni ya makaa. Akanyamaza kwa muda akiwaza kwa kutumia kichwa chake cha pombe, watu wote wakimtazama na kumngojea atasema nini.

“Robaa!” Nyokaa akaita. Roba akaitikia kiukakamavu.

“Nataka kichwa cha Eliakimu hapa. Namtaka na Miriam hapa … Utajua mwenyewe cha kufanya. Anayelikoroga sharti alinywe.”

Aliposema hayo akaondoka zake kwenda kujipumzisha, akimwachia jukumu zito Roba, ambaye alishusha pumzi ndefu na kuketi chini kwanza kabla hajafungua kinywa.


***


Saa tatu asubuhi …

Baada ya usingizi kukoma, Nade anaunguzwa na mwanga wa jua usoni. Alikuwa juu ya kitanda kidogo kilichotandikwa vema, ndani ya chumba cha ukubwa wa kati. Pembeni ya kitanda hicho kulikuwa kuna taa ya mwamvuli, na bado ilikuwa inawaka.

Alipepesa macho yake kukagua chumba kizima kabla hajafanya lolote. Mpaka muda huo hakuwa anajua chumba hicho ni cha nani na amefikaje hapo. Alichokuwa anajua ni kwamba yeye ni mateka, na mara ya mwisho akiwa fahamuni alikuwa amefungiwa kwenye kiti na amegoma kula wala kunywa.

Mbona yupo kitandani?

Akatupia shuka lake kando na kujaribu kuketi kitako. Mwili ulikuwa unamuuma sana. uso wake ulikuwa mwekundu, maungio ya mikono yake yalikuwa mekundu. Mgongo wake ulikuwa unatoa jasho la damu.

Kwa maumivu hayo lakini akamudu kusimama na kutembea kwa hatua chache kwenda ukutani. Aliona picha ya mwanamke hapo na mtoto mdogo wa kiume. Akaitazama picha hiyo kwa umakini akijaribu kushirikisha akili yake. Lakini hakupata kitu!

Akiwa anachechemea kwa maumivu, akauendea mlango na kuusukuma. Ulikuwa wazi, usifungwe na komeo. Hakuusukuma kwanguvu, akiwa na lengo la kuchungulia, ili basi kama ni adui ajue ni namna gani atakabiliana naye.

Alivyotupa macho, akaona taswira ya Jona. Mwanaume huyo alikuwa amekaa kwenye kiti akipitia karatasi ya mchoro, ule ambao aliletewa na Panky toka kwa Marwa. Macho yake nyuma ya miwani yalikuwa yanaenda huku na huko. Juu ya meza kulikuwa kuna kikombe cha chai, karatasi tatu nyeupe, kalamu ya risasi na rula ndefu.

Nade akasimama kwa sekunde kumi na tano akimkagua mwanaume huyo aliyekuwa kifua wazi, ndani ya bukta fupi ‘timberland’.

“Karibu na pole,” Jona akasema akiwa anaendelea kutazama karatasi yake. Nade akajikuta anatabasamu baada ya kugundua ameonekana, akiwa anajivuta kwa maumivu, akasonga na kuketi kwenye kiti.

“Kumbe ni wewe,” Nade akasema akimtazama Jona.

“Nikupatie chai?” Jona akamkarimu Nade.

“Hapana, nashukuru. Nipo sawa.”

“Haupo sawa. Najua haujala kwa muda wa siku tatu. kila chakula ulicholetewa ulikuwa unafanya kukimwaga kwa kukipiga teke. Tumbo lako linahitaji kinywaji cha moto kwa sasa kabla ya chakula ... unajua kwanini? Kwasababu unaweza ukajikunja na kukusababishia matatizo.”

“Umejuaje kama nilikuwa sili?”

“Sidhani kama ni siri hiyo, Nade.”

Jona akaamka na kuifuata chupa ya chai akamimina kiasi kwenye kikombe na kumkabidhi Nade. Alafu kwa ukimya, akaendelea kufanya kazi yake ya kupekua ile karatasi, na muda mwingine akiwa anachorachora vitu vyake ambavyo Nade hakuwa anavielewa.

“Ile picha ni ya mkeo na mtoto wako?”

Jona akamtazama Nade kama mtu ambaye hakuamini kusikia swali hilo.

“Picha ipi?”

“Kule chumbani ukutani.”

“Ndio,” akajibu kwa ufupi.

“Wako wapi? Sijawahi kuwaona.”

“Chai itapoa, hakikisha unamaliza upesi,” Jona akasisitiza. Nade akatabasamu na kupiga mafundo mawili ya chai. Macho yake hayakukoma kuendelea kutazama huku na huko.

“Umempatia masharti gani mheshimiwa?” Mwanamke huyo akauliza.

“Masharti? Kivipi?”

“Najua mpaka umekuja kuniokoa kuna makubaliano mliyoyaweka. Unaweza ukanishirikisha?”

Jona hakujibu kitu, akaendelea kufanya kazi yake. Nade naye akalipuuzia hilo swali, akaendelea kunywa chai lakini sasa hivi akiwa anazingatia kile ambacho Jona alikuwa anafanya. Kukawa kimya kwa muda.

Kama dakika kumi na tano hivi mbele, Jona akapokea simu yake. Akaongea maneno machache tu akiahidi kufika ndani ya muda. Akanyanyuka toka sebuleni na kwenda chumbani.

Nade akanyakua makaratasi ya mwanaume huyo upesi na kuyatazama. Jona aliporejea, akawa tayari ameshamaliza haja yake.

“Twende kwa bosi wako,” Jona alisema akimwonyeshea Nade mlango. Nade akanyanyuka kwa taabu kabla ya Jona hajamshika mkono na kutoka naye ndani, Huko nje taksi ilikuwa tayari inawangoja, wakajiweka ndani na safari ya kwenda kwa Mheshimiwa ikaanza.

Ndani ya gari kulikuwa kimya. Jona alikuwa anatazama nje ya dirisha lililokuwa limezibwa na kioo. Pembeni yake Nade alikuwa ametulia tuli kama maji ya mtungi. Mbali na mlio wa gari, kwa mbali sana ndiyo ungeweza kusikia sauti ya redio.

Redio hii ilikuwa inaimba nyimbo za zamani, miaka ya themanini huko, na kwa uchache miaka ya tisini kipindi hicho muziki ukiwa muziki. Nyimbo hizi zilikuwa zinaendana na dereva wa taksi hii: mwanaume mweusi aliyepambwa na mvi kadha kwa kadha kichwani.

Derava huyu ndiye pekee anayeaminika na mheshimiwa Eliakimu kwenye mambo ya usafiri, ukimtoa dereva wake anayempeleka ofisini na kumrudisha nyumbani.

“Jona,” Nade akaita na kumshtua Jona. Jona akamtazama pasipo kusema jambo.

“Ule mchoro uliokuwa unautazama pale sebuleni, umeutoa wapi?” akauliza. Jona akampuuza, akaendelea kutazama nje.

“Naujua … naujua ule mchoro,” Nade akasema. Jona akurudisha upesi uso wake kumtazama.

“Umeujulia wapi?”

Hapo Nade akawa amekamata atensheni yote ya Jona. Mwanaume huyo alimtazama akiwa na kiu kubwa ya kujua.

“Nilishawahi kuuona mahali kama sijakosea. Kwenye mojawapo ya vipeperushi ama barua ya mheshimiwa.”

Jona akashangazwa. Mchoro huo ulikuwa na mahusiano gani na mheshimiwa? Alitaka kujua zaidi lakini hakupata majibu kwani Nade naye alikuwa mtupu asiyefahamu kwa kina.

“Nakumbuka siku moja niliuona. Sikuuliza kwa kuwa sikuona kama una maana ya kufanya hivyo,” alisema Nade. Akamuuliza Jona kama ana lolote la kumwambia kuhusu mchoro huo, Jona akamwambia pengine majibu yao watapewa na Mheshimiwa.

Baada ya hapo kukawa kimya tena. Lakini kichwani mwa Jona kukiwa na vurugu kwasababu ya mawazo mapya aliyopewa na Nade. Alijiona ana maswali mengi ya kujibiwa na mheshimiwa. Alijiuliza Eliakimu ni nani haswa asipate jibu.

Akiwa humo fikirani, anashtuliwa na sauti kubwa! Gari lao linayumba vibaya mno! Dereva anajitahidi sana kulimudu na kuliweka sawa. Jona anakuja kusoma mchezo, walikuwa wamepushiwa na gari moja kubwa jeusi, Toyota Prado. Na halikuwa mbali.

Bado dereva akihangaika kuweka matairi sawa, prado inashusha vioo, mkono mweupe uliobebelea bunduki aina ya SMG unatoka. Haraka Jona akapiga kelele:

“Lala chini!”

Mara risasi zinaanza kumwagwa kama njugu kushambulia taksi waliyomo Jona na wenzake. Dereva anakula risasi nne na kufa papo hapo. Taksi inaacha njia na kufuata fremu za maduka kwa kasi.


WAKINA JONA WANASHAMBULIWA NA NANI? NINI ROBA ATAFANYA KUTIMIZA AGIZO LA KUMUUA MHESHIMIWA? LEE NA GLADY WAMEISHIA WAPI? MIRANDA ATAYAMALIZA MAMBO NA BOKA? MHESHIMIWA ANA KIPI CHA KUSEMA JUU YA MCHORO? ALPHONCE ATATIMIZA AGIZO LA KAMANDA?
 
*ANGA LA WASHENZI --- 42*

*Simulizi za series*


ILIPOISHIA

Akiwa humo fikirani, anashtuliwa na sauti kubwa! Gari lao linayumba vibaya mno! Dereva anajitahidi sana kulimudu na kuliweka sawa. Jona anakuja kusoma mchezo, walikuwa wamepushiwa na gari moja kubwa jeusi, Toyota Prado. Na halikuwa mbali.

Bado dereva akihangaika kuweka matairi sawa, prado ikashusha vioo, mkono mweupe uliobebelea bunduki aina ya SMG unatoka. Haraka Jona akapiga kelele:

“Lala chini!”

Mara risasi zikaanza kumwagwa kama njugu kushambulia taksi waliyomo Jona na wenzake. Dereva anakula risasi nne na kufa papo hapo. Taksi inaacha njia na kufuata fremu za maduka kwa kasi.

ENDELEA

Sasa hakukuwa na namna la sivyo wanaenda kufa wote. Jona akajirusha upesi toka kwenye viti vya nyuma na kuudaka usukani tena huku akipambana na mwili mfu wa dereva. Akajitahidi kuwakwepa watu na mali zao japo hakufanikiwa kwa kiasi kikubwa, akapasua na kubinua nyungo za karanga na kadhalika.

Lakini hatimaye akafanikiwa kurejesha gari barabarani. Taharuki na makelele yakiwa yametamalaki, magari mengine yakiwa yamesimama ama kuhepa kujiepusha na hasara ama vifo!

Akiwa mtulivu, macho yake yakatazama gari lile lililokuwa linawashambulia, Prado nyeusi, basi akadhamiria kufanya jambo. Taratibu akaanza kuutafuta mwanya wa kuisogelea gari hilo ambalo kwa muda huo tayari yule mshambuliaji alikuwa ameurejesha mkono wake wenye silaha ndani.

Akayekwepa magari ya mbele na pembeni yake kwa ustadi. Kufanikisha adhma yake ikamlazimu atumie barabara ya wanaokuja, si wanaoenda kama yeye. Na hivyo basi ikamlazimu tena awe makini kupitiliza. Akifanya hayo Nade akajawa na hofu kubwa, hata akapiga kelele kumtaka Jona asitishe zoezi.

“Jona, are you crazy!” (Jona, umewehuka!) akawaka akiwa amejishikiza kwenye viti. “Stop the car! Simamisha gari!”

Lakini Jona hakujali, akaendelea kusaka lengo lake. Si kuwaua wale waliokuwa wanamshambulia, lah! Hakuwa na silaha pamoja naye ila alitaka kulitambua gari hilo vema na hata wale waliomo ndani.

Akajitengenezea vema kwenye kiti cha dereva baada ya kumsukumia dereva yule mfu kando. Akakanyaga mafuta na kuendesha atakavyo. Lakini bado muda ukawa haupo upande wake, chombo chake hakikuweza kufua dafu kupambana mwendokasi na Prado, akaachwa.

“Damn it!” akalaani akisaga meno. Akabadili mwelekeo akirejea nyuma kidogo na kisha akachukua njia ya kushoto. Mwendo ukabadilika, akawa anasukuma magurudumu kwa mwendo kati.

“Watakuwa ni wale watu! – wakina Nyokaa!” Akasema Nade. Bado moyo wake ulikuwa unaenda mbio asiamini kama ametoka salama kwenye yale mashindano.

“Hapana!” Jona akatikisa kichwa. “Sio hao unaowadhani.”

“Ni wakina nani basi kama si wao ambao wangefuata roho yetu?” Nade akauliza.

“Sijajua ni wakina nani ila sio hao unawafikiri. Mosi, hakuna mtu anayenijua kama mimi ndiye nahusika na kukuokoa isipokuwa mheshimiwa peke yake. Niliyatenda yote sura yangu ikiwa nyuma ya kinyago.

Pili, kabla sijafanya zoezi la kukuokoa nilifanya upekuzi wa mazingira yote, hamna mahali niliona lile gari. Haitaleta maana kusema wao wanahusika, labda tu kama tungekuwa tumetokea nyumbani kwa mheshimiwa, hapo tungesema walianza kutufuatilia tokea huko, maana makazi yake watakuwa wanayajua.”

“Sasa atakuwa ni nani?” Nade akashupaa kuuliza.

“Sijui ni nani,” akajibu Jona. “Ila atakuwa anawinda roho yangu, si yako!”


Baada ya nusu saa …


“Kwahiyo mwili wake upo wapi?” akauliza Mheshimiwa akiwa ameshikilia kiuno. Alikuwa amevalia kaushi nyeupe nyepesi na bukta iliyokomea juu ya magoti. Usoni akiwa amevalia miwani ya kusomea. Mkono wake wa kuume umebebelea gazeti.

“Upo ndani ya gari!” akajibu Jona.

“Kwahiyo hamjafanikiwa kabisa kugundua hao watu? Kabisa yani!”

“Sijafanikiwa, ila najua muda si mrefu ukweli utajiweka bayana.”

“Ebu twendeni kwanza ndani … tuingie ndani …” mheshimiwa aliwasukumizia Jona na Nade ndani huku akiperuzi macho yake huku na kule. Baada ya muda mfupi mezani kwao kukawa kumependezeshwa na vinywaji vilaini. Nade alikuwa ameketi kando ya Mheshimiwa, Jona akiwa amejitenga kwa umbali mdogo akiketi kwenye kiti cha kuwatazama.

“Hapa hapatakuwa mahali salama tena, ni kheri ukachukua tahadhari mapema,” Jona akashauri.

“Najua hilo na bila shaka umeshaliona. Nimeongeza walinzi sasa maradufu!”

“Sidhani kama watatosha, bado ni wachache. Adui yako ana jeshi kubwa, kwa idadi na hata nyenzo,” Jona akanguruma. “Nakushauri uwe makini zaidi.”

“Sasa Jona na ndiyo hapo sasa nami ninapokuja kwenye ombi langu. Najua endapo nikiwa na wewe basi nitakuwa salama salmini, mkishirikiana na Nade hapa. Walionaje hilo?” Mheshimiwa akatia nadhiri.

Kukawa kimya kidogo.

“Miriam yupo wapi?” Jona akauliza. Mheshimiwa akamtazama Nade kwanza kisha akaurejesha uso wake kwa Jona na kujibu:

“Yupo ndani.”

“Naweza nikamwona?”

“Ya .. yah! Unaweza ukamwona,” Mheshimiwa akajibu. Kukawa kimya kidogo.

“Ila si kwa sasa, Jona,” Mheshimiwa akapendekeza.

“Kwanini si sasa?” Jona akauliza. Mheshimiwa akawa kimya kidogo. Kisha akanyanyuka na kwenda ndani, baada ya dakika mbili akarejea akiongozana na Miriam aliyekuwa mchovu na mwenye huzuni. Alikuwa amevalia dera akitembea kama mwanamke aliyetoka leba.

Jona akamsalimu, hakuitikia. Akamrushia macho yake makali akiwa ameuvuta mdomo. Hakujalisha Jona ameongea kitu gani, yeye hakutia neno hata moja. Macho yake ndiyo yalibadilika rangi kuwa mekundu, na ndani ya kinywa chake akisaga meno.

Baada ya muda huo usiokuwa na matunda, mheshimiwa akamnyanyua mwanamke huyo kumrejesha ndani. Hapo sasa akaufungua mdomo wake akimtazama Jona. Akamlaani vikali akimrushia matusi.

“Sitakusamehe maisha yangu yote kwa kunileta jehanamu!”

Mheshimiwa akampeleka ndani ya chumba na kumfungia.

“Naweza nikaambiwa sasa nini kinaendelea hapa?” Jona akauliza akimtazama Mheshimiwa ndani ya mboni zake. Mheshimiwa akashusha pumzi, kisha akashushia na juisi yake ya komamanga.

“Jona, ni simulizi ndefu sana hii. Ni simulizi ambayo isingependeza kabisa kusikika kwenye masikio ya yeyote yule, haswa mtanzania. Ni simulizi ya kutisha ambayo yaweza kukufanya ukashindwa kulala kwa ndoto za jinamizi!”

“Nipo tayari kuisikia simulizi hiyo,” akasema Jona. Basi Mheshimiwa akamtazama Nade na kumpandishia kichwa pasipo kutia neno. Nade akanyanyuka, na kwa mwendo wake wa majeruhi, akasonga kuondoka zake.

“Jona,” Mheshimiwa akaita. “Mimi si kiongozi mzuri, si mfano wa kuigwa wala sistahili kuwepo kwenye kiti hiki. Ni mambo mengi nimefanya, na yote hayo ni kwa ajili yangu si kwa taifa wala wananchi. Kuna muda nafsi yangu inanisuta sana, lakini sina namna maana yaliyopita hayawezi tena kubadilika.

Nimeshaingia kwenye anga la wenyewe, nikavinjari ninavyotaka, kutua chini ni ngumu …”

Nade akarejea akiwa amebebelea kiboksi kidogo cha chuma. Akamkabidhi Mheshimiwa aliyekipokea kwa mikono miwili na kisha akakiweka mapajani. Akaendelea kunena akiwa anafungua kiboksi hicho.

“… maana nimeshazoea hewa ya huko juu kiasi kwamba naona nikitoa naweza nikafa kwa kukosa pumzi. Kutua chini kutaninyima uhuru niliozoea kwenye anga hilo … kwahiyo siwezi, siwezi tena kutua. Siwezi kurudi tena ardhini.”

Alipomaliza kusema hivyo, mara mkono wake ukatoka ndani ya kiboksi ukiwa umebebelea bunduki ndogo nyeusi. Akamnyooshea Jona.

“Na hivyo basi, haitakiwi mtu yeyote kujua kama nami ni rubani kwenye anga hilo. Ni siri inayotakiwa kudumu milele, na milele, amin,”

Akafyatua risasi mbili kutoboa kifua cha Jona. Kisha akaangua kicheko akirejesha bunduki yake ndani ya kiboksi.

“Kwaheri Jona, kwaheri katuandalie makao.”

Akamuita mmoja wa walinzi wake waliokuwepo nje, akaunyooshea mkono mwili wa Jona.

“Beba hiyo na nyingine ndani ya taksi, kaitupie mbali!”

“Sawa mkuu!”

“Hakikisha hakuna mtu anayekuona, wala anayekufuatilia. Sawa?”

“Sawa!”

Mwanaume huyo mpana na mrefu, akaubeba mwili wa Jona na kutoka nao nje, akautupia ndani ya gari kisha akaubeba na ule wa dereva taksi, alafu akatimka akienda anapopajua yeye kichwani. Kwenda kuitupa miili hiyo isiwahi kuja kujulikana!

Huko nje ya jiji la Dar akaishusha na kuitelekeza baada ya kuhakikisha yupo mwenyewe, na kweli alikuwa mwenyewe. Akajipaki kwenye chombo na upesi akatimka.

“Ndio, mkuu. Kazi imeshakwisha!” akaongea mtumishi huyo mwadilifu.


Baada ya lisaa limoja …


Mtumishi huyo akafungua mlango wa sebuleni na kuangaza macho. Sura yake imebeba hofu na mazingira yalikuwa tulivu mno. Mkononi mwake alikuwa amebebelea bunduki ndogo. Haikuchukua muda, akaona mwili wa mheshimiwa pamoja na wa Nade ukiwa umelala kwenye kochi, damu zinawatiririka vichwani!

Akatahamaki. Akawatazama watu hao kwa macho ya bumbuwazi. Akakimbilia napo chumbani kutazama, Miriam hakuwapo! Chumba kilikuwa kitupu, mlango upo wazi.

NI NINI KIMEJIRI?
 
Steve mdogo wangu, hiki unachokifanya kinakujengea heshima kubwa sana na kinakuweka katika kevels za juu sana? Hongera sana.. Kwa kweli unaweza na kipaji unacho. Kitendo cha kuahidi muda flan utatupia mzigo na kweli unatupia...!!!! We we in Khabari nyingine kabisa.. Tupo tunaofuatilia kimya2 wengi tu... Usibadilike ukawa kama watunzi wengine wababaishaji, nisiseme sana.. Keep it up..
 
Back
Top Bottom