*ANGA LA WASHENZI --- 45*
*Simulizi za series*
ILIPOISHIA
"Are you sure you've finished?" (Una uhakika umemaliza?)
"He doesn't breath anymore," (Ahemi tena) Alphonce akasema kwa uhakika.
"And about the police?" (Na kuhusu polisi?)
"Told you before. I am the only police whom you should worry about." (Nishakuambia hapo kabla. Mimi ndiye polisi pekee wa kumhofia.) Kisha akauliza:
"Where my money at?" (Pesa yangu ipo wapi?)
"Where are you rushing at?" (Unakimbilia wapi?) Foang akauliza.
"Let me inspect the phone first!" (Acha niikague simu kwanza!)
Kabla hajaifungua simu, Alphonce akamdaka mkono wake na kumwambia:
"Till I see my money first!" (Mpaka nione pesa yangu kwanza!)
ENDELEA
Macho ya Alphonce yalikuwa hayana utani hata kidogo. Hakuwahi na utani kwenye pesa tangu azaliwe. Kwake pesa ndiyo kitu cha thamani maishani. Amezaliwa atafute pesa! Na kutumia pesa!
Kuhusu kiapo cha kazi ya upolisi, uzalendo na mambo ya ujamaa, hayo unaweza ukabaki nayo. Yeye mpe pesa! Kama unataka uendelee kuvuta pumzi ama kuishi kwa amani.
Foang akamtazama mwanaume huyo machoni. Akajifunza kweli hana utani. Hata akaogopa. Akatabasamu na kupandisha mabega yake:
"I still depend on you, Alphonce. I can not cheat on you." (Bado nakutegemea, Alphonce. Siwezi kukulaghai.)
Alphonce hakusema kitu, akaendelea kumtazama na macho yaliyotoa ujumbe tosha. Foang akanyanyuka na kwendaze chumbani, muda si mrefu akarejea na bahasha ya kaki aliyomkabidhi Alphonce.
Alphonce akatupia macho yake ndani ya bahasha, akatabasamu na kunyanyuka akimpatia mkono Foang.
"I think I should go." (Nadhani napaswa kwenda.)
"But I have not yet inspected the phone!" (Lakini bado sijaipekua simu!) Akalalama Foang.
"Just do it then you will inform me. You know my contacts, right?" (We fanya alafu utanitaarifu. Unajua namba zangu, sio?)
Hakungoja Foang aseme neno, akaenda zake Foang akimsindikiza kwa macho. Mchina huyo hakuwa anajua cha kufanya, akaishia kumtazama Alphonce akiyoyoma.
Alphonce akaweka bahasha yake kwenye kiti cha pembeni, akatekenya funguo na kutoka ndani ya nyumba ya Foang kwa kasi. Haikupita punde, simu yake ikaita. Ilikuwa ndani ya mfuko wa koti, akaichomoa na kuitazama kwa kuibia. Alikuwa ni kamanda.
"Ndio, mkuu ... muda si mrefu sana n'takuwa hapo ... serious? ... sijatazama na wala sijasikia kabisa! ... sawa! ... sawa."
Simu ikamuacha ameachama mdomo. Alikuwa amekunja sura, macho yake yakiwa yametambaliwa na utashi wa fikra. Habari alizozipokea zilimshangaza, na kumpatia mawazo. Zilimfanya kwa muda asahau kwamba alikuwa ameweka 'manoti' kadhaa kwenye kiti cha pembeni yake akiwa ameziingiza kwa 'kazi ndogo'.
Akashusha pumzi ndefu. Akasonya na kutikisa kichwa. Lakini ajabu, ghafla akasikia kitu cha baridi shingoni kwake! Akatazama kupitia 'sight mirror' akamwona mchina akiwa amemuwekea 'chuma', macho ameyakaza wakitazamana kiooni.
Alikiwa ni Lee!
"Habari za muda mrefu, Alphonce."
"Hivyo ndiyo namna ya kumsalimu rafiki yako ambaye hamjaonana kwa muda mrefu?"
"Si hivi, bali kwa kutoboa shingo yake na risasi! Rafiki hawi tena rafiki anapouarua mgongo wa rafiki yake aliyemkabidhi aukune."
"Una maanisha nini Lee?"
"Unajua ninachomaanisha. Peleka gari makaoni kabla sijakugeuza nyakati iliyopita ... na unafahamu vizuri kwamba sitanii."
Alphonce akamtazama Lee kiooni. Lee akamtazama Alphonce kiooni. Macho yao yalikuwa yanasema mengi zaidi ya maneno waliyoyatamka na vinywa. Macho haya yalikuwa ya janja janja! Macho ya kizandiki!
Macho ya njama!
Akilini mwa Alphonce kulikuwa kuna mafikirio, kama ilivyokuwa kwenye bongo ya Lee. Alphonce hakuwa tayari kwenda popote pale akiongozana na Lee. Mosi, kamanda anamngojea ofisini. Pili, ilikuwa ni ombwe kwake juu ya anachoenda kukutana nacho huko apelekwapo.
Akili yake ikabidi ifikirie namna ya kujinasua. Hakuwa na budi kumzidi akili Lee kisha atokomee zake! Basi akakaza mkono kwenye usukani wa gari. Akiwa katika mwendo wake wa kasi, akaanza kuhesabu kimoyomoyo, mdomo wake ukiwa unachezacheza kwa mbali.
1 ... 2 ... 3 ... 4 ...
... 5!
Akakanyaga breki kwanguvu! Lakini asifahamu kilichotokea, akajikuta hana fahamu baada ya kuhisi amegongwa kwanguvu chini ya kisogo.
Akazama kizani!
---
Robo saa mbele ...
Gazeti linatupiwa juu ya meza ya kioo, Kamanda akasonya na kunyanyuka akifuata kabati. Anatazama saa yake alafu anasonya tena. Anachukua faili rangi ya samawati, nalo analirushia mezani.
Anasimama na kufikiri jambo. Akajirejesha kwenye kiti chake na kunyakua simu yake nyeusi, SONY toleo jipya, akapiga. Simu ikaita pasipo kupokelewa. Akapiga tena, haikupokelewa!
Akaweka simu mezani na kulaza kichwa chake kwenye kiti. Akazunguka kwenda kushoto na kulia, kulia na kushoto akitazama feni yake darini.
Lile faili alilolitoa kabatini, hakuonekana kuligusa wala kuwa na mpango nalo. Mezani, kwa mbele yake, ungeweza kuliona gazeti la Habari Leo likiwa na picha ya wanaume wawili waliokuwa wamelala chini, wamejeruhiwa na kutapakazwa damu.
Kwa juu ya picha hiyo ikisomeka kichwa cha habari chenye maneno meusi:
*"WATU WAWILI WAMEUAWA KINYAMA NA MTU ASIYEJULIKANA."*
Chini ya maneno hayo, kwa mtu mwenye macho 'mepesi' angelisoma tena maneno yenye ukubwa wa saizi ya kati yaliyoandikwa kwa wino wa kijani:
"Watu hao watuhumiwa kuwa majambazi, na wameuawa kwa mkono wa siri."
Chini ya kichwa hicho, kulikuwa na habari kamili sasa ikiwa imeandikwa kwa maneno madogomadogo, ngumu kuonekana kwa macho ya wazi yaliyo mbali. Na mbele kidogo ya taarifa hiyo ikalekezwa kuendelea ukurasa wa tatu.
***
Usiku wa saa mbili ...
Baada ya sauti ya vishindo vya miguu, inafuata ya mlio wa mlango kisha Jona anaingia ndani ya makazi yake akiwa anachechemea.
Anawasha taa na kujitupia kwenye kochi kama mzigo. Akahema kwa mafundo makubwa makubwa mara tano kabla hajavua nguo yake ya juu na kubaki na kaushi ya kuzuilia risasi.
Akafungua kaushi hiyo kwa nyuma kisha akaiweka mezani. Kifuani kwake kulikuwa kuna majeraha, kwa mbali kulikuwa kuna rangi nyekundu ya kuvilia damu.
Kabla hajafanya kitu kingine chochote, akanyanyuka na kwenda chumbani akiwa anapepesuka. Alipofika mlangoni, akadondoka chini kama mzigo, akapoteza fahamu!
Baada ya kama dakika tano akiwa hapo chini, taratibu, kwa mbali akaanza kupata taswira ambazo hakuzielewa. Taswira hizi zilikuwa zinakatiza upesi kichwani kwake mithili ya mwanga wa radi!
Kulikuwa na sauti ambazo hazikueleweka. Mayowe na nderemo za kifo. Na mara sauti za watu waliomezwa na giza wakiwa wamebebelea maginga ya moto!
"Amepita wapi?" Sauti moja ya mwanaume ikauliza. Giza lilikuwa pana kiasi cha ginga la moto kutofua dafu!
"Huku! ... Amepita huku!" Akasema mwanaume mwingine upesi!
Mara tih! Tih! Tih! Vishindo vikaenda huko na kupotelea gizani.
Jona hakutikisika. Na hakuonyesha dalili ya kuamka karibuni. Masikioni hakusikia tena kitu, na machoni akawa mpofu.
***
Saa sita usiku.
"Bosi nadhani kuna mtu getini," akasema mlinzi baada ya kugonga mara mbili mlangoni, Foang akatoka akiwa amevalia taulo.
"Who is it?" (Nani?) Foang akauliza. Macho yake madogo ya kichina yalikodoa, mkono wake wa kuume ulikuwa umeshikilia taulo lake lisianguke.
"Bwana mi sielewi! Spiki kiswahili" akalalama mlinzi.
"Nani? Nani huyo?" Foang akafoka kwa lafudhi ya puani.
"Sijui nani? Hauna appointment na mtu?"
"No! No! No appointment!" Foang akatikisa kichwa, kisha akamtaka mlinzi aende, akafunga zake mlango!
Akiwa ndani ya chumba akasimamisha masikio yake apate kusikia kila jambo linalotukia huko nje. Lakini hakusikia hata lepe. Zikapita mpaka dakika nne ... tano ... sita ...
Akaulaza mwili wake kwa amani. Akazima taa, na bunduki yake ndogo ambayo alikuwa ameshaisogeza karibu akaisokomezea chini ya mto.
Kabla hajabebwa na usingizi, akasikia hodi mlangoni. Akalalama na kutusi. Aliona sasa huyu mlinzi ameshindwa kazi, na akaapa kumfunda adabu huko mlangoni aendapo.
Akajikwamua kitandani na kupiga hatua tatu ndefu. Akafungua mlango kwa hasira na kuangaza. Uso kwa uso akakutana na bomba la bunduki!
Alikuwa ni Lee!
Akamwamuru atoke na kumpatia simu aliyopewa na Alphonce. Na akitumia lugha ya kichina, akamuuliza kama amefanya lolote na ile nyaraka. Foang akatikisa kichwa chake upesi, akakana katukatu!
Kuhakiki, Lee akapekua simu ile kwa haraka. Alipomaliza, akamuaga Foang na kisha akamzamishia chuma cha risasi kichwani! Akatoka zake ndani ya jengo kwa kuchumpa ukuta.
Dakika kumi na tatumbele ...
"Ndiyo hii?" Akauliza Lee akimwonyeshea simu Alphonce aliyekuwa amefungwa kamba kitini. Walikuwa ndani ya chumba kidogo ndani ya makazi ya Lee. Kulikuwa kimya sana, kama si maongezi haya ungeliweza dhani hapana mtu.
"Ndiyo yenyewe!" Alphonce akajibu kwa kiburi. "Nifungilie basi niende!"
"Bado sijamalizana na wewe," Lee akananga akitikisa kichwa. Akaketi na kumuuliza Alphonce:
"Niambie ni nani aliyekuwa anawasiliana naye?"
"Mzee!" Alphonce akaita. "Hilo mimi silijui. Kazi yangu ilikuwa ni kutafuta hiyo simu tu!"
Kabla Lee hajaongeza kauli ujumbe ukaingia kwenye ile simu, haraka akatazama. Ilikuwa ni barua pepe toka kwa mtu aliyetunzwa kwa jina la Chen Zi. Lee akalazimika kufungua barua hiyo na kuitazama.
Akajikuta moyo unapiga fundo kubwa! Gibum! Alafu ukaanza kukimbia mbio! Mbio! Mbio!
Asiamini macho yake, aliona nyaraka ile, anayoipambania iwe siri, ikiwa imeshatumwa kwenye historia ya maongezi. Na huyu bwana Chen Zi alikuwa yupo huko Hong Kong, China!
Akahisi kuishiwa nguvu. Akapiga moyo konde na kusoma maongezi ya barua pepe ile mwanzo mpaka mwisho. Alipomaliza, akaiweka simu chini akisaga meno. Alipandwa na hasira mno. Alikunja ngumi yake kubwa akifuma ndita.
Akamtazama Alphonce kwa hasira, na mara akanyanyuka na kuchomoa bunduki yake akamuwekea kwenye paji la uso. Hakusema kitu, macho yake yalikuwa tayari mekundu. Akabinua mdomo na kufyatua kitufe cha bunduki!
Klick! Hakuna kitu. Klick! Klick! Klick! Hamna kitu, risasi zilikuwa zimeisha. Kwa hasira akaitupia bunduki mbali Alphonce akishusha pumzi ndefu ya neema.
Akatoka ndani ya chumba na kwenda kuketi sebuleni akiwa ametingwa na mawazo lukuki. Aliwaza, je kuna haja ya kumshirikisha Sheng kwenye mkasa huu?
Vipi kama Sheng akijua hizi habari, ambazo amejitahidi kuziweka chini ya kapeti akashindwa, atafanya nini na atamfanya nini?
Akajikuta akitetemeka mikono.
***