*ANGA LA WASHENZI -- 57*
*Simulizi za series*
ILIPOISHIA
"Najua BC anakuamini sana. Endapo ukiuweka ulimi wako vizuri, hawezi akakataa."
"Lakini, Kinoo," Miranda akatia shaka. "Mbona ni haraka hivyo? Mbona ghafla ghafla hivyo? Kuna nini?"
Kinoo akashusha pumzi ndefu na kutazama chini. Akarudisha macho yake kwa Miranda na kumwambia:
"Sarah ana mimba yangu."
Miranda akakodoa. "Wasema?"
ENDELEA
"Sarah ana mimba yangu," Kinoo akasisitizia. Miranda akashusha pumzi ndefu na kuulaza mgongo wake kitini.
Akatikisa kichwa chake akimtazama Kinoo. Akamlaumu kwa jambo hilo la kipumbavu, kamwe hakulitegemea kwa mtu kama yeye.
"Unajua wazi situation yetu. And blindly you are about to make a family!" Miranda akalalama. Hawakuongea sana na Kinoo, akamtaka mwanaume huyo aende, amwache peke yake.
Kinoo akaendaze akiongozana na wanawake wake aliokuja nao. Walijipaki kwenye gari, Escudo ya grey, wakatimka.
"Umefanikiwa?" Sasha akamuuliza Kinoo baada ya kuacha makazi ya Miranda kwa hatua kadhaa. Kinoo akashusha pumzi ndefu. Macho yake yalikuwa yanatazama mbele lakini akiwa amezama fikirani.
"Ni jambo la kuchukua muda," Kinoo akajibu. "Lakini litakuwa sawa tu," akawatoa hofu.
Hawakuongea tena kwa muda. Sauti ya gari tu ndiyo ikawa inavuma na kuita.
**
Jona akatazama saa yake mkononi. Muda ulikuwa umeenda sasa. Alishamaliza kula na sasa akaona ni vema akienda kumwona Nade kama vile daktari alivyomwambia kwamba atakuwa macho kipindi cha kula chakula cha mchana.
Akanyanyuka na kulipia bili yake ya chakula, na kwa hatua nzito akajongea mpaka kwa daktari moja kwa moja. Yeye hakuwa anangojea msururu wa wagonjwa kwa kutumia kofia yake ya kazi.
Akiongozana na nesi, akaenda mpaka alipolazwa Nade, akamkuta mwanamke huyo akiwa anakula.
Nade akatabasamu kwa mbali kumtia Jona machoni. Ni kama vile alikuwa anataraji ujio wa mwanaume huyo. Alionekana bado hana nguvu, ila ilikuwa kheri. Akamkaribisha Jona kula.
"Nashukuru," Jona akasema kwa tabasamu la bati. Kisha "Nimefurahi kukuona," akasema akimtazama Nade machoni.
Nade akatabasamu kimaumivu. Jona hakumwongelesha tena, akamwacha amalize kwanza kula.
"Daktari kaniambia umekuwa na mawazo sana hapa karibuni, nini shida?" lilikuwa swali la kwanza Jona kuuliza.
Nade akajilaza kwanza kitandani. Akawa kimya kwa muda. Mara macho yake yakaanza kulowana na hatimaye kuvujisha machozi.
Kuna kitu kilikuwa kinamsumbua kifuani. Jona aliliona hilo. Hakutaka kumlazimisha kuongea, akamngojea kwa wakati wake sahihi.
"Nisamehe sana, Jona," Nade akasema akitazama dari. Macho yake bado yakiendelea kuvuja kama mto.
"Nimekukosea sana, najua hilo. Umekuwa ukinipa mkono wakati mimi nikikukabidhi kisu. Umetetea uhai wangu lakini mimi nikifanya jitihada kuupokonya wa kwako. Nisamehe sana. Sistahili hata msaada wako."
Uso wake ukawa mwekundu. Mafua yakaanza kumtambalia, na kwikwi za kilio zikampalia.
Akamwomba sana Jona msamaha. Jona akamsihi hana haja ya kufanya hivyo kwani alishamsamehe, hata hivyo alifanya hayo kwasababu za ushawishi wa bosi wake, marehemu Eliakimu.
"Nataka tu uniweke bayana kile ambacho bosi wako alikuwa ananificha. Naomba unisadie kwenye hilo," Jona akampendekezea, lakini hakutaka kumpa presha mwanamke huyo kutokana na hali yake, akamtaka apumzike, na utakapofika muda basi wataongea kwa urefu na mapana.
Lakini Nade akakataa.
"Tuongee tu hata sasa," akateta kwa sauti ya chini ya msisitizo. Uso wake ulikuwa mzito ukizongwa na majuto ya kujiona mkosefu. "Huna haja ya kungoja, Jona, ntakwambia hata sasa."
Kisha akakaa kimya. Bado macho yake yakimwaga machozi.
Kwa uchungu mkubwa, akaanza kufunguka kinagaubaga. Akamweleza Jona ni kwa namna gani Eliakimu alivyokuwa anacheza mchezo wa damu kwa kutumia mkono wa serikali.
Namna gani alivyokuwa anashiriki magendo na biashara haramu na vitu hivyo vikamvunisha pesa nyingi mno. Namna alivyokuwa akishirikiana na magenge ya wauaji, madawa ya kulevya, utakatishaji wa fedha na kadhalika na kadhalika nyuma ya pazia.
Na ni kivipi alivyokuwa anatumkika kama mkono wa kushoto wa bwana Eliakimu akitumwa kuwamaliza maadui zake, na hata wale washirika wake waliomzulumu baada ya kupiga dili.
Akamweleza Jona yote kumhusu BC na Sheng. Namna anavyowafahamu, na jinsi walivyoshirikiana na hao watu kutimiza kazi kadhaa za kimagendo, ikiwamo kuingiza nchini makemikali yaliyokatazwa, pia hata madawa ya kulevya.
"Tulifanya hivyo kwa siri sana tukitambua wazi BC na Sheng walikuwa ni maadui wakubwa kibiashara, lakini tukafanikiwa kula na vipofu."
Akamwambia pia Jona ni kwasababu gani walikuwa wanamuwinda Miriam, na kwanini basi mwanamke huyo alikuwa anatakiwa kuuawa japokuwa ni mke wa Eliakimu.
"Kwanza Miriam hakuwa anampenda Eliakimu hata kidogo. Eliakimu alikuwa analijua hilo, lengo la mkewe lilikuwa ni kurithi tu mali zake pindi atakapofariki ama kumuua. Ilifikia kipindi Miriam akawa anatembea na mshirika mmoja wa kibiashara wa Eliakimu, mwanaume huyu akiitwa Nyokaa, mfanyabiashara wa madini Arusha.
Nyokaa alikuwa amekorofishana na Eliakimu kwasababu za kibiashara. Kila mmoja akawa anataka kulipa kisasi kwa mwenzake kwa kutuhumiana kurudishana nyuma, lakini kiuhalisia ni Eliakimu ndiye alikuwa na makosa. Aliingia dili na Nyokaa, mwisho wa siku akamsaliti kwa kuchukua kiasi fulani cha mzigo wake na kumdanganya ulipotelea njiani kwasababu za kiusalama.
Kulipiza kisasi na kurejesha fedha yake nyingi, akafanikiwa kumlaghai Miriam ili amtumie kunyooshea biashara zake kwa mtandao wa Eliakimu."
Jona akakuna kidevu chake. Akajikuta anapata kiu ya kutaka kujua zaidi na zaidi kadiri alivyokuwa anaelezwa.
Akataka kujua kwanini Nade hakutumwa kummaliza Nyokaa baada ya kuyatambua hayo. Nade akamwambia asingeliweza hilo kwani Nyokaa ana jeshi kubwa la watu.
Si rahisi kumkamata kama kutamka.
"Tulikuwa tunataka kumrejesha tu Miriam kwani alikuwa anajua mengi kumhusu Eliakimu, kwahiyo kuwa mikononi mwa adui, ilikuwa ni hatari sana."
Lakini zaidi, Eliakimu asingeweza kutekeleza mipango na mambo yake yote haya akiwa peke yake. Hilo lilikuwa bayana.
Ni lazima kuna watu vitengo na maeneo mbalimbali aliokuwa anasaidiana nao.
"Ni watu wengi mno," akasema Miranda. "Kila mtu na eneo lake, kila mtu na kitengo chake. Kila mtu akicheza nafasi yake kutimiza maagizo ya Eliakimu. Na kwasababu alikuwa anatoa pesa nono, haikumuwia vigumu kuwakamata."
Sasa Jona akaona kuna haja ya kutia nguvuni watu hao wote, lakini ushahidi ni muhimu sana kwenye hili. Ataupataje? Na atawapatia wapi watu wote hawa waliokuwa wanashirikiana na Eliakimu?
"Usijali," Nade akamtoa hofu. "Eliakimu alikuwa ana orodha ya watu wake wote aliokuwa anafanya nao kazi, pamoja pia na mawasiliano yao."
Akamwelekeza Jona wapi atavipata.
"Chumbani kwake, kwenye droo za kitanda, utakuta nyaraka zake zote humo. Ufunguo wa droo hizo huwa anauweka ndani ya moka zake ndefu nyeusi kwenye stendi ya viatu."
Jona akashukuru kwa taarifa hizo. Lakini kabla hajaondoka, akamsihi mwanamke huyo asimweleze mtu mwingine yoyote juu ya habari alizoongea naye. Nade akamhakikishia hilo kwa kuapia na maisha yake.
"Sitakusailiti tena kwa sasa."
Jona akaenda zake.
***