JanguKamaJangu
JF-Expert Member
- Feb 7, 2022
- 2,780
- 6,607
Tukio la Said Oswayo kumuua mkewe, Swalha Salum kisha na yeye kuuawa ikidaiwa amejiua bado ni gumzo Nchini Tanzania.
Wivu wa mapenzi ndio unatajwa na wengi kuhusu matukio hayo yaliyotokea ndani ya mwezi huu Mei 2022, lakini hoja yangu hapa siyo kuhusu walivyouawa, nina kitu tofauti kabisa.
Tayari kumeanza kelele kuhusu urithi wa mali, upande wa mwanamke inadaiwa wanaamini wao wana haki ya msingi, wakati huo ndugu wa mume nao wameanza kuonesha ishara kuwa wanataka kuwa sehemu ya mali hizo.
Marehemu walifunga ndoa Desemba 2021, ikiwa na maana kuwa ndoa yao ilikuwa na miezi mitano tu lakini mwanaume alikuwa vizuri kiuchumi na wadau wengi wa Mwanza wanaamini hicho ndicho kilichompeleka kwa mwanaume huyo, inasemekana lakini, hatuwezi kuusemea moyo wa mtu.
Inadaiwa mwanaume ana mtoto ambaye alimpata kabla hajamuoa huyo bibie.
Nimezungumza na wataalam wawili wa sheria na haya ndio yalikuwa maelezo yao:
MDAU WA KWANZA WA SHERIA:
Cha kwanza kabisa itaangalia kama marehemu aliacha wosia ambao unaweza kutaja mgawanyo wa mali zake na mengine yote.
Kama hakuna wosia, na wawili hao hawakuwa wamefanikiwa kupata mtoto, hapo mrithi halali ni mtoto wa huyo mwanaume hata kama alimpata nje ya ndoa.
Kinachotakiwa kufanyika ni kikao cha familia ambacho kitamchagua msimamii wa mirathi. Kama mtoto ana miaka chini ya 18 basi huyo msimamizi wa mirathi atatakiwa kusimamia mali za marehemu hadi mtoto atakapofikisha miaka 18.
Lakini kabla ya kufika huko msimamizi wa mali akishateuliwa na familia, anatakiwa kwenda Mahakamani kuapa, baada ya hapo ndani ya siku 14 atatakiwa kutafuta mali zote za marehemu ziwe kwenye orodha yake na zijulikane.
Nikirudi nyuma kama hivyo wawili hao hawakuwa na mtoto, kwenye urithi kawaida sheria inasema mtoto au watoto wanatakiwa kupata 80%, wazazi wa mume 10% na wazazi wa mke ni 10%
Mtoto akifikisha miaka 18 anatakiwa kwenda Mahakamani kuapa kuwa ametimiza umri huo na yuko tayari kuchukua mali kutoka kwa msimamizi na kuziendesha mwenyewe, au anaweza kuandika barua ya kutaka msimamizi aendelee kusimamia kwa muda atakaopendekeza yeye.
MDAU WA PILI WA SHERIA
Hapo baada ya taratibu za vikao vya familia na kumteua msimamizi wa mirathi, mali zote zitakuwa mali ya mtoto au watoto, kama hawana basi mali zitaenda kwa wazazi wa mwanaume.
Hiyo itafanyika kama marehemu hakuacha urithi wowote, mfano hao wanandoa (Swalha na Said) ndoa yao ilikuwa changa, hawakuwa na mtoto, hapo mwenye haki ya mali ni mtoto.
Mali ambazo walizipata ndani ya ndoa hizo wanaweza kugawana na upande wa mwanamke, mfano nimeona familia ya mwanamke inataka kung’ang’ania nyumba, ile siyo mali yao, labda kama wakati wanajenga walikuwa pamoja na nyaraka zipo wakati wa ujenzi kuwa mwanamke alishiriki.
Pia mali ambazo zitakuwa na jina la mwanamke pia zinaweza kuchukuliwa na upande wa familia ya mwanamke
HITIMISHO
Baada ya wadau hao, kuna yeyote ambaye anaona kisheria imekaaje kuhusu mali za marehemu Said? Kwani najua mgogoro mkubwa utaibuka muda si mrefu.... Mwenye uelewa atuelezee