Roving Journalist
JF Roving Journalist
- Apr 18, 2017
- 3,984
- 13,760
Akizungumza Oktoba 29, 2024 jijini Dar es Salaam, katika Mkutano wa Tano wa Mwaka wa Bodi ya Usajili wa Wabunifu Majengo na Wakadiriaji Majenzi (AQRB) Mkuu wa Wilaya ya Ilala, Edward Mpogolo amesema kuwa Serikali inaendelea kutoa hamasa kwa wataalam hao kuchangamkia fursa za kazi katika miradi mikubwa inayondelea hivi sasa nchini.
“Niipongeze Serikali ya Awamu ya Sita kwa kutoa fursa kwa wazawa kushiriki miradi mikubwa nchini, sasa ni muhimu kwa wataalamu wetu wa ndani kufanya juhudi za makusudi za kujifunza uendelezaji wa nchi yetu kwa kutumia na Teknolojia ya kisasa ili kupata miradi mingi kama wataalamu wa nje”, amesema Mpogolo.
Mpogolo amesisitiza wataalamu hao kushirikiana na kufanya kazi kwa pamoja ili kuhakikisha mkakati wa kuinua wazawa kupitia fani hiyo unafanikiwa kutokana na kupata fursa za kushiriki katika utekelezaji wa miradi mikubwa nchini.
Ametoa rai kwa Bodi ya AQRB kuendelea kusimamia wataalam hao, kuendelea kutoa ushauri wa kitaalam kwa miradi mbalimbali inayotekelezwa nchini ili kusaidia kupunguza malalamiko ya weledi na ujuzi na utekezaji wa miradi nchini”, amesisitiza Mpogolo.
Kwa upande wake, Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Majengo Tanzania (TBA), Arch. Daud Kondoro akimwakilisha Katibu Mkuu Wizara ya Ujenzi amesema kuwa Serikali kupitia Wizara ya Ujenzi imefanikisha kufanyika kwa marekebisho ya Sheria ya Usajili wa Wabunifu Majengo na Wakadiriaji Majenzi ya mwaka 2023 ambayo yamelenga kuongeza ushiriki wa wataalam wa fani za Ubunifu Majengo na Ukadiriaji Majenzi katika usimamizi na utekelezaji wa miradi ya Ujenzi nchini.
Sambamba na hilo, ameongeza kuwa Wizara ya Ujenzi, ipo katika mchakato wa kuhuisha Sera ya Ujenzi ya mwaka 2003 pamoja na kuandika Sheria ya Majengo ambapo amefafanua kuwa mchakato wa uandaaji wa Sheria ya Majengo utakapokamilika utakuwa umejibu matamanio na shauku ya watalaam hao.
Naye, Mwenyekiti wa Bodi ya Usajili wa Wabunifu Majengo na Wakadiriaji Majenzi (AQRB) Dkt, Ludigija Bulamile amesema kuwa Bodi imesajili wahitimu 873 waliomaliza masomo yao kutoka Vyuo Vikuu mbalimbali nchini lengo ni kuhakikisha wahitimu wote wanasajiliwa ndani ya kipindi cha miaka miwili baada ya kuhitimu masomo yao.