Familia tata

Familia tata

SEHEMU YA 28

Sasa watu walishajaa, walijitahidi kuuzima kwa mchanga na maji kwenye ndoo, lakini walionekana kama watu wanaofanya mchezo, moto ulizidi kuteketeza vitu, vilivyosikika vikipasuka kila mara!
Sasa endelea...

“Maskini mzee Linus na familia yake wanateketea hivihivi, lakini mbona hatujasikia hata kelele,” majirani wenye majonzi walikuwa wanazungumza nje ya nyumba hiyo wakiwa hawaamini kinachotokea.
Akina Beka walikosea, hawakuichoma nyumba ya akina Stone, bali waliiwasha moto nyumba ya mtu wao. Akilini mwao walijua wamefanya kazi waliyotumwa kikamilifu, walisubiri kukuche wakachukue mshiko wao. Mtu mmoja miongoni mwa watu waliofurika nje ya nyumba, akapata wazo na kubonyeza namba za simu ya mzee Linus.

Aliisikia ikiita hadi ikakatika. Akapiga tena, ikaita hadi kukatika.
“Haiwezekani, simu ya mzee Linus inaita, atakuwa hayupo nyumbani, masikini sijui kama anajua,” mtu huyo alisema kwa sauti iliyowashitua watu wengine, akina mama wakajaribu kupiga namba ya mkewe, nayo ikawa inaita, lakini haikupokelewa, vijana wakapiga namba ya Brown, haikuita hata mara tatu ikapokelewa..

“Hellow mwana uko wapi?” Jaffari, jirani yao mtaani alimuuliza bila hata kumsalimia.
“Dah, afu una bahati kweli, ningekuwa ndani nisingesikia simu yako maana kelele ni nyingi kweli, nipo Club mwana, vipi?” alijibu Brown muda huo ukielekea saa nane na nusu usiku.

Brown hakushangaa kupigiwa simu muda ule na Jaffari kwa sababu walikuwa ni marafiki na wote walipenda kujirusha. Alipoambiwa kuhusu nyumba yao kuungua alishangaa sana!Alianza kuwatafuta wazazi wake kwenye simu, lakini hata hivyo hawakusikia kwa vile kila mmoja alikuwa ametoa mlio kuepuka usumbufu. Brown hata hivyo, hakuwa na wasiwasi wa kuwepo kwa vifo kwa vile alijua hakukuwa na mtu aliyelala humo kwa vile nyumba ilikuwa inapigwa dawa!

Saa kumi na moja alfajiri mzee Linus alishtuka kutoka usingizini, alikuwa anaota ndoto mbaya. Aliposhtuka simu yake ilikuwa inaita, lakini kabla hajaifikia, ikakata. Alipoichukua na kuangalia aliyempigia, akagundua simu nyingi kupigwa katika simu yake, nyingi zikiwa za majirani, akajua kimenuka!

Akamchagua jirani mmoja, akampigia kumuuliza kulikoni.
“Mzee Linus? Siamini kama ni wewe kweli, uko wapi? Nyumba yako imeteketea kwa moto na sijui kama kuna mtu alilala ndani,” jirani huyo alisema kwa pupa mara tu mzee huyo alipomsalimia na kujua kulikoni kumpigia simu usiku wa manane!

***
Wakiwa bado hawajalala, mzee Komba na mkewe ghafla wakaona mwanga mkubwa ukimulika nyumba yao kutoka upande wa mzee Linus, kwa haraka wakaamka na kuchungulia. Walishangaa sana kuona moto mkubwa kwa jirani yao, lakini wasisikie sauti yoyote ikiita, angalau kuomba msaada.
Haraka wakawafuata watoto vyumbani mwao na kuwaamsha kwa nguvu, walikuwa ni watu wa kwanza kuamka miongoni mwa nyumba zote za jirani na ndiyo waliopiga kelele za kwanza kuashiria kulipuka kwa moto huo.

Waliungana na wengine katika harakati za kuuzima lakini bila mafanikio. Wengi walijaribu kuwauliza chanzo cha moto huo, lakini walisema hawaelewi, wakihisi huenda kulikuwa na hitilafu za umeme.
Maneno yalikuwa ni mengi wakati watu wakiangalia na kusubiri moto huo umalizike kuwaka. Hadi wakati huo, walishakuwa na uhakika kuwa hakukuwa na mtu yeyote ndani ya nyumba hiyo, kwani wote walikuwa wametoka.

“Lakini, hebu tujiulize jamani, kwa nini moto uwake leo kukiwa hakuna mtu ndani, wote kwa pamoja walikwenda wapi,” mtu mmoja, ambaye mtaani hapo alijulikana kama Ndocha, aliuliza huku akiwakazia wenzake macho, kuonyesha kuhitaji majibu.
“Lakini kweli eti jamani?” mtu mwingine naye akadakia na mara moja, mjadala mpya juu ya tukio hilo ukaanza.

Hisia za kuwepo kwa mpango maalum wa kuichoma nyumba hiyo kutoka kwa mzee Linus mwenyewe ukaanza kusemwa taratibu.

Inaendelea
 
SEJHEMU YA 29

“Lakini kweli eti jamani?” mtu mwingine naye akadakia na mara moja, mjadala mpya juu ya tukio hilo ukaanza.
Hisia za kuwepo kwa mpango maalum wa kuichoma nyumba hiyo kutoka kwa mzee Linus mwenyewe ukaanza kusemwa taratibu.
Sasa endelea...

Mzee Linus akachanganyikiwa. Ghafla mwili wake wote ukaloa jasho ndani ya sekunde kumi tu, akili yake haikujua nini cha kufanya na wala hakuelewa ataanza vipi kumfahamisha mkewe juu ya tukio hilo.
Wakati akihangaika kichwani mwake kujiuliza jinsi gani atafanya, mara mkewe naye akaamka, simu yake ambayo ilikuwa chini ya mto aliolalia, ikawa inaita, akaichukua na kuipeleka sikioni huku akimshangaa mumewe alivyoloa jasho chapachapa!

“Whaaaat,” mke wa mzee Linus aliruka ghafla kitandani huku simu yake ikianguka chini, mara tu baada ya kupewa taarifa ya kuteketea kwa nyumba yao.“Baba Brown, usitaka kunitania kabisa, niambie kwa nini umechoma nyumba yetu moto, niambie sasa hivi kabla sijaenda Polisi, huwezi kuturudisha kwenye umasikini kirahisi namna hii,” alifoka mama huyo, sasa akiwa amesimama chini, akihema kwa sauti kubwa.

Mzee Linus hakujua aseme nini, akajilaumu kwa kitendo chake cha kufanya siri mpango ule, maana kama angemweleza, wangeweza kujua ni bahati mbaya. Na sasa, baada ya tukio kutokea, hakukuwa na jinsi yoyote ya kumweleza maneno akayaelewa!
“Lakini ni ya kwetu kweli? isije ikawa ni ya jirani yetu,” mzee huyo alijaribu kujifariji, akiamini huenda wamekosea kumpigia.

“Watu wawili hawawezi kukosea kukupigia wewe na mimi kutuambia juu ya kuungua kwa nyumba, hilo jasho la nini, si wamekupigia wao? Au unatoka jasho kwa ajili ya nini, nyumba iliyoungua ni yetu na wewe ndiye uliyeichoma, kwa nini?” aliendelea kufoka mama wa watu.
Mzee Linus akainamisha kichwa chake chini, lakini sekunde chache baadaye, kama aliyekumbuka kitu, akainua uso wake na kumwambia mke wake.

“Tulia, kuna kitu kinaanza kunipa picha kuhusu hili tukio, tulia usiwe na haraka kwanza, ngoja nifanye utafiti kidogo nitakujuza,” maneno hayo hata hivyo hayakusaidia lolote, mama huyo alivaa nguo zake na kutoka nje, alikochukua gari na kuliwasha kuelekea eneo la tukio!

“Chuga, nini kimetokea, mbona umenigeuzia kibao,” mzee Linus alimwambia Dayani, mara tu mkewe alipotoka nje na kuhakikisha akiliwasha gari lao na kuondoka. Kauli hiyo ilimshangaza rafiki yake, ambaye alikuwa akijiandaa kukutana na vijana wake wa kazi kwa ajili ya kuwapongeza kwa kazi nzuri!
“Vipi, mbona sikuelewi?” naye alimjibu mwenzake ambaye alimwelezea kuhusu simu alizopigiwa kuwa ni nyumba yake ndiyo iliyoungua badala ya mtu waliyekusudia.

Dayani akaomba azungumze na vijana wake, ambao baada ya kuwauliza kuhusu nyumba waliyoichoma, walimhakikishia kuwa ni ileile waliyoikagua mchana wake.

“Nataka kuwaambia hivi, mmezingua, mmeifanyia nyumba ya mshkaji wangu na mnanijua vizuri nilivyo sitaki ujinga, kazi zenu zote huwa nawalipa vizuri kwa sababu mnazifanya vizuri, sasa mnapokosea kama hivi ni lazima muwajibike, chagueni adhabu inayofanana na ile nyumba,” Dayani aliongea kwa ukali, hali iliyomtisha Beka, aliyekuwa na simu.
Simu ikakatika, lakini iliendelea kubaki sikioni mwa Beka kwa sekunde kadhaa mbele, kisha akamwambia Shosi;

“Tumekwisha babaake”
“Kivipi,” Shosi akasema huku akihema, tena akiwa ameshamsogelea karibu, alimfahamu vyema Dayani, hakuwa na masihara kwenye kazi.
“Anadai nyumba tuliyoichoma siyo yenyewe, tuliyoifanyia ni ya rafiki yake,” Beka alisema huku sura yake ikionyesha hofu ya dhahiri.

Inaendelea
 
SEHEMU YA 31


“Mimi nafikiri mngezungumza na baba maana mimi hapa nilipo nitadondoka wakati wowote, sina nguvu kabisa,” alisema mama huyo huku akikaa chini pembeni ya gari lake. Wale askari walimwelewa, wakamwomba ampigie simu mumewe, wakimtaka kufika kituo kidogo cha Polisi Wazo kwa mahojiano mafupi.
Sasa endelea.....

Mke wa mzee Linus akachukua simu yake na kubonyeza namba za mumewe, alipopokea akamweleza kuhusu wito wa Polisi. Akakata na kuirudisha kwenye mfuko wake wa kwapani.

Mzee Linus alijua kimenuka, hakuelewa atasema nini kwa Polisi. Lakini baada ya kutafakari na kujijibu maswali aliyojiuliza, aliamua kwenda, lakini kwanza baada ya kuwa amefika nyumbani kwake.

Akachukua bodaboda iliyomfikisha hadi nyumbani kwake. Alishangaa kuona umati wa watu ukiongezeka, licha ya kwamba kulishakucha. Watu wote walimwangalia yeye. Alionekana kusikitika sana kwa tukio hilo, lakini baadhi ya watu walimtilia shaka, walimuona kama anayefahamu kilicho nyuma ya pazia.

Mzee huyo alizunguka zunguka kuitazama nyumba yake huku akizungumza peke yake, kichwani mwake alikuwa anawaogopa zaidi polisi kuliko hasara aliyoipata. Alimuomba Mungu ampe nguvu aweze kuwajibu vizuri maswali yao!
***
Wakiwa chumbani kwao, simu ya mama Juddy iliita, alipoangalia katika kioo, jina la mpigaji lilimshangaza, kabla ya kupokea, akamuonyesha mumewe, ambaye naye alionyesha mshangao.
“Haloo,” aliita baada ya kuipokea.

“Habari za leo mama,” upande wa pili ulijibu.
“Tunashukuru Mungu tumeamka salama, sijui wewe huko baba,” mama Juddy alijibu akiwa na hamu ya kutaka kujua sababu ya kupigiwa simu.

“Huku wazima. Vipi, kuna kitu gani kimetokea huko kwenu?” mpigaji aliuliza.
“Huku kwetu? Huku kuko shwari tu baba,” alijibu mama.
“Kweli?”

“Eeeh, kwani vipi baba,”
“Kama ni hivyo sawa, tutawasiliana wakati mwingine.”
“Haya asante, kukiwa na lolote tutakuambia,” alisema mama na kukata simu.
Ni mganga wao!

Mzee Komba alikuwa na hamu kubwa ya kusikia kilichosemwa na mganga wao, lakini aliposimuliwa, hakuona kama kulikuwa na chochote cha kutilia shaka…
***
Mzee Linus baada ya kuiangalia nyumba yake ilivyoungua, alimfuata mkewe na kumtaka kuingia ndani ya gari ampeleke Polisi. Yeye alienda upande wa dereva, akashika usukani na kuondoa gari taratibu.
“Sikiliza mke wangu, mimi ni mumeo, tuna watoto, hiki kilichotokea ni kikubwa sana, kitatugharimu, lakini nadhani mimi ni muhimu zaidi ya nyumba,” alisema taratibu huku akiendesha kwa mwendo wa taratibu sana.

“Kwa hiyo,” mkewe alimjibu huku sura yake ikiwa imejikunja.
“Nataka unisaidie, vinginevyo ninaweza kuangamia na kuizidishia familia yetu matatizo,” alisema huku akionyesha huzuni kubwa.

“Nikusaidie nini, kuichoma tena moto nyumba?” mama alizidi kufoka.
Mzee Linus akaamua kunyamaza. Aliendesha gari kama mita hamsini, akalisogeza pembeni na kuliegesha. Kichwa chake akakiinamisha kwenye usukani, akionekana kuwa na mawazo mengi.

Mkewe alibakia ameegemea kiti chake, naye akili yake ikiwa mbali kabisa kimawazo. Watu waliokuwa wakipita ambao waliwafahamu, waliwaonea huruma, walijua kwa nini ni lazima wawe kama walivyokuwa!

Baada ya kama nusu saa ya kukaa pale pembeni, hatimaye mzee Linus aliliwasha gari na kabla ya kuondoka, akamuita mkewe, alipoitika akaanza tena kumsemesha akisisitiza amsaidie katika tatizo lililo mbele yake. Mkewe akaamua kumsikiliza anachotaka kusema, ili aone kama anaweza kumsaidiaje.

“Kule Polisi, nataka nikadanganye, sitasema kama tulitoka wote kwa sababu ya nyumba kupigwa dawa, nikisema hivyo nitajikamatisha,” alisema mzee Linus, macho yake yakiwa usoni mwa mkewe, moyo wake ukimdunda!

Mkewe akamtupia macho kwa mshangao, kitu kama hakumwelewa vile. Akili yake ikampeleka kuamini moja kwa moja kuwa mumewe ndiye aliyechoma moto nyumba yao. Lakini akajiuliza, kwa nini?

Inaendelea.
 
SEHEMU YA 32

Mkewe akamtupia macho kwa mshangao, kitu kama hakumwelewa vile. Akili yake ikampeleka kuamini moja kwa moja kuwa mumewe ndiye alichoma moto nyumba yao. Lakini akajiuliza, kwa nini?
Sasa endelea...

“Unataka uende ukasemaje,” mkewe alimuuliza.
“Kila mtu awe na sababu yake, zungumza na watoto waambie unachoweza kuwaambia ili wasiseme kama waliondoka kwa sababu ya nyumba kupigwa dawa, mimi nitasema tulitoka kulala hoteli kama moja ya taratibu zetu, kwamba mara kwa mara tunatoka kubadilisha mazingira,” mzee Linus alizungumza huku macho yake yakiwa bado kwa mkewe.

“Unafikiri maelezo hayo yatawaridhisha Polisi?” alimuuliza.
“Wewe nisaidie kwa hilo, hayo mambo mengine niachie mimi,” mumewe alijibu.
“Ni hilo tu ndilo unalotaka nikusaidie?” mkewe alimuuliza.
“Ndiyo”

“Nitakusaidia kwa hilo, lakini kwa masharti,” mkewe alisema.
“Masharti gani?”
“Niambie sababu ya wewe kuichoma moto nyumba yetu.”

***Beka na Shosi walikuwa wamekaa mbele ya Dayani, katika mojawapo ya vibanda ndani ya baa kubwa ya Zanzi. Mwenyeji wao alionekana kuwa na hasira za dhahiri, alitaka maelezo kutoka kwa vijana wake ili aweze kujua nini cha kuwafanya.

Vijana wale walijitahidi kujieleza kadiri walivyoweza, wakisema kuwa walifanya mahesabu ya kutosha na walishalifahamu eneo lile kwa kadiri walivyoweza, lakini wakashangaa kwa kilichotokea.

“Unajua mnanishangaza sana, itawezekanaje iwe hivyo mnavyosema? Yaani kwa mfano unajua kabisa unanipiga ngumi mimi, halafu eti umpige huyu, itawezekanaje?” Dayani aliwauliza uso wake ukiwa umezidi kufura kwa hasira.

Kwa jinsi walivyomtambua Dayani, vijana wale wawili wakajikuta wakianza kulia, walifahamu mwisho wao ulikuwa umefika, kwa sababu moja ya sifa kubwa za bosi wao, ni kutotaka masihara kwenye kazi.
“Sikilizeni, mimi nimefanya kazi hii kwa miaka mingi sana, nimenusurika mara nyingi sana kuuawa, nilichojifunza ni kwamba dawa pekee ya kuepuka kuuawa ni kuua, mmesikia?”

“Tunaomba utusamehe bosi, usituue, tunaomba tukafanye tena ile kazi, hata ikibidi leo,” Beka, huku akitoa machozi, alimuomba Dayani, aliyekuwa anavuta sigara.
“Sasa niwasamehe na hii nyumba ya rafiki yangu mliyochoma?”

“Tutatafuta hela tumlipe bosi, tuambie tu ni shilingi ngapi tutatafuta, wajinga wengi tu wana hela, tutaipata,” Shosi alisema, huku akili yake ikifikiria vituo vya mafuta, maduka makubwa na wafanyabiashara wanaoweza kuwa na hela.

“Sawa, nitataka mfanye jambo moja la msingi, tena kwa haraka kabisa, nataka mumlipe fedha za nyumba hiyo, ngoja niongee naye, hela hizi zipatikane leoleo,” alisema Dayani na kuchukua simu yake, akabonyeza namba za rafiki yake.
***
Mzee Linus alikuwa ametumbua macho baada ya kuulizwa swali lile, hakujua aseme nini, baada ya kutafakari sana kwa haraka, akaamua aseme ukweli ili mkewe ajue, potelea mbali kama atamwelewa au la.

Alipokohoa kama ishara ya kutaka kuanza kuzungumza, simu yake ikaita, jina la rafiki yake Dayani likajitokeza, akasita, ikaita kwa muda lakini baadaye akapokea.
“Niambie Chuga,” alijibu mara tu alipopokea.

“Poa, aisee, sasa nimeongea na vijana, watakulipa leoleo, sema ni shilingi ngapi thamani ya nyumba yako?” Dayani aliongea kwa kujiamini. Masikioni mwa mzee Linus, zilikuwa ni habari njema ambazo hakuzitegemea.

“Kwa thamani ya sasa, nadhani siyo chini ya milioni 150,” alisema kwa utulivu.
“Basi, leo hiihii utapata mzigo, usiwe na wasiwasi,” alisema Dayani na kukata simu.

Mzee Linus akaonyesha tabasamu usoni mwake, hali ambayo iliendelea kumshangaza mkewe. Anafurahi wakati nyumba yetu imeungua? Huyu ana nini? Alijiuliza mara mbilimbili mke wake, alijua kuna siri kubwa nyuma ya pazia, akakohoa kumpa ishara mumewe kwamba anahitaji kujibiwa swali lake.

Itaendelea.
 
SEHEMU YA 33

“Kwa thamani ya sasa, nadhani siyo chini ya milioni 150,” alisema kwa utulivu.
“Basi, leo hiihii utapata mzigo, usiwe na wasiwasi,” alisema Dayani na kukata simu.

Mzee Linus akaonyesha tabasamu usoni mwake, hali ambayo iliendelea kumshangaza mkewe.
Endelea...



Mzee Linus akamueleza kila kitu mkewe, kama kilivyokuwa kuanzia mwanzo hadi mwisho. Alipomaliza, akavuta pumzi ndefu, mzigo mkubwa sasa ukawa kwa mke wake ambaye naye alipumua kwa nguvu, moyoni akiwa na wasiwasi mwingi.

Wakati mumewe akiwa anataka kumsikia atakavyosema, mama Tonny alibakia kimya kwa muda mwingi, akitafakari kile alichokisikia. Hatimaye akafunguka.

“Hivi tumefikia kiwango cha kutaka kuangamizana kweli baba Tonny?” alimuuliza mumewe.
“Kama Stone alitaka kumuua mwanetu, sisi tuna sababu gani ya kuwaonea huruma, kama mbwai mbwai tu,” alisema mumewe.

“Dah, ni hatari kwelikweli, haya sasa wameunguza nyumba yetu, itakuwaje?” aliuliza.
Ndipo mzee Linus akamuelezea habari nzuri alizopata hivi punde kutoka kwa Dayani, kwani siku hiyohiyo walikuwa na uhakika wa kuzipata shilingi milioni mia moja na hamsini.

Baada ya kuridhishana kwa maelezo hayo, safari ya kuelekea polisi ikaendelea na hata walipofika, walichukua muda mfupi kumaliza mahojiano, kwani hakukuwa na lolote ambalo polisi walilikomalia na wote waliona kama ni ajali ya bahati mbaya.

Baada ya kutoka hapo, walielekea kwenye hoteli waliyolala jana yake na kuendelea kulipia chumba chao, kwa vile hawakuwa na sehemu ya kwenda kwa muda huo. Walikaa na kutafakari jinsi watakavyozitumia fedha walizokuwa wakizitegemea kutoka kwa vijana wa Dayani.

Wakakubaliana kutafuta kiwanja na kujenga sehemu nyingine mbali na pale, ili pamoja na mambo mengine, kuwaepuka kabisa majirani zao, kwani uhasama wao sasa ulizidi kipimo, kwani wakati wowote wanaweza kuuana.
***Wakiwa bado chumbani kwao wakiendelea na mazungumzo yao, simu ya mama Juddy iliita tena na kwa mara nyingine, mganga wao ndiye aliyekuwa akipiga. Kabla ya kupokea, akamuonyesha mume wake na baadaye akaipeleka sikioni.

Alisikiliza kwa muda wa kama dakika mbili hivi, lakini sura yake ilibadilika haraka na jasho likaanza kumtoka. Hadi alipomaliza kusikiliza, mikono yake ilibakia kifuani kwake, akihema alimwambia mumewe.
“Huwezi kuamini alichoniambia mganga, eti nyumba yetu ndiyo ililengwa ichomwe moto na hawa majirani zetu, lakini kibao kikawageukia,”

“Unasema?” aliuliza mzee Komba huku akihema.
Mkewe akarudia kumwelezea. Wakashindwa kuamini, wakalazimika kufunga safari hadi Salasala kusikia vizuri ana kwa ana.

Mganga hakuwaficha, akawaeleza kila kitu kilivyokuwa na baada ya hapo akamalizia kwa kuwaambia.
“Na muda wowote kuanzia hivi sasa, watakamatwa kwa sababu wataunganishwa kwenye kesi ya mauaji ambayo inaelekea kutokea hivi sasa.”

“Kivipi, kwani kuna mtu aliyekufa mle ndani?” mzee Komba alimuuliza mganga.
“Hapana, kuna mauaji yanaelekea kutokea muda siyo mrefu ujao, wao ndiyo chanzo, kabla ya jua kuzama, watakuwa polisi,” mganga aliongea, lakini hawakuweza kabisa kuelewa maana yake.

Baada ya mazungumzo kadhaa, baadaye wateja hao wawili waliaga na kuondoka kuelekea kwao, wakiwa na mawazo mengi sana vichwani mwao, maelezo waliyopata kutoka kwa mganga yaliwachanganya kabisa.

Hata hivyo, walijikuta wakishindwa kufanya lolote kwa sababu hawakuwa na ushahidi wowote wa kuwakamata majirani zao. Hata hivyo, wakaambizana kuongeza umakini katika kujilinda.
***
Beka na Shosi walikuwa wamesimama nje ya kituo cha mafuta cha Afrikana, wakimsoma meneja ambaye walipewa mchongo kwamba angechukua fedha za makusanyo ya wiki ili azipeleke benki. Nyendo za Meneja huyo zilionyesha kuwa wakati wowote angekabidhiwa mzigo aupeleke.

Dakika kumi baadaye, gari la Night Support, lilifika katika kituo hicho, likageuka na kuelekeza upande wake wa nyuma katika mlango wa chumba cha meneja. Watu waliovalia mavazi ya walinzi binafsi walikuwa imara na bunduki zao, wakiwa wanaangalia huku na huku.

Zoezi la kupakia fedha lilifanyika kama dakika kumi hivi, mlango wa gari ukafungwa, walinzi wawili wakapanda nyuma, meneja akapanda mbele na taratibu gari likaanza kuondoka kuifuata barabara ya lami kuelekea mjini..!

Je nini kitatokea?
 
SEHEMU YA 34

Zoezi la kupakia fedha lilifanyika kama dakika kumi hivi, mlango wa gari ukafungwa, walinzi wawili wakapanda nyuma, meneja akapanda mbele na taratibu gari likaanza kuondoka kuifuata barabara ya lami kuelekea mjini..!
Sasa endelea...

BEKA na Shosi waliliacha gari hilo hadi lilipofika katika kituo cha daladala, wakapeana ishara na wenzao waliokuwa wamekaa kwenye gari lililoegeshwa njia panda ya kuelekea Mbezi juu. Wakaifuata pikipiki yao aina ya Boxer na kuanza kuondoka taratibu kuingia barabarani.

Gari lililokuwa mbele, ambalo walipeana ishara na kina Beka, lilikuwa na watu wanne, wote wakiwa na bunduki zilizokatwa vitako. Waliliona lile gari likienda mwendo wa kasi, walitaka shughuli ile ifanyike kwa haraka, hapohapo barabarani eneo la Makonde.

Mpango ulikuwa ni kwamba baada ya kulivamia, wangevunja mlango wa gari kwa risasi kisha makasha ya fedha yangepewa akina Beka ili wakimbie nayo njia za vichochoroni na nyingine waondoke nazo.
Katika kikosi hicho kulikuwa na takriban watu sita, wale waliokuwa kwenye gari, walikuwa ni vijana wa Kinyarwanda ambao muda mwingi katika maisha yao wametumia katika vita katika misitu ya Kongo wanakotumikia vikundi vya kijeshi kwa malipo maalum.

Mara ya mwisho, walikitumikia kikundi cha M23 kabla ya kuamua kukimbia baada ya kusikia majeshi ya Tanzania yamekwenda huko kuisaidia serikali ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC). Walipoondoka walifikia Mwanza, ambako daima walikutana na bosi wao, Ntumba, ambaye ndiye kiunganishi kikubwa cha askari walioasi Rwanda, wanaotumika katika matukio mbalimbali ya ujambazi nchini.

Ntumba alipata simu ya Dayani asubuhi kuhusu kazi inayotakiwa kufanywa siku inayofuata naye akawapandisha ndege vijana wale wanne, ambao wanafahamu vizuri lugha ya Kiswahili.

Walilifuata gari lile lililobeba fedha wakitaka wakafanye tukio katikati ya barabara, lakini ghafla bila wao kutarajia, wakashangaa kuliona linapinda kona kuingia kushoto. Kwao, huko ndiko kulikuwa sehemu nzuri zaidi kwa kazi yao.

Walipoliona linakata kona, Beka na Shosi nao wakajikuta wakitabasamu, zoezi lingekuwa rahisi kuliko walivyoliona jinsi ambavyo lilitakiwa kufanywa pale barabarani.
***
Moyo wa dereva ulikuwa unadunda wakati alipoanza kumwambia meneja wa kituo kile cha mafuta.
“Inabidi tupite njia hii kuepuka foleni, ukiwa umebeba hela nyingi kama hii kupita njia kubwa, ukikwama kwenye foleni ni rahisi watu kutuvamia,” alisema huku mapigo ya moyo wake yakiongezeka.

Akili ya meneja ikajikuta imepata maswali mara moja, mbona kila siku tunapita njia hii na hakuna kinachotokea? Hata hivyo, aliamua kunyamaza, akashika sehemu aliyoweka bastola yake, akakuta ipo imetulia, akajiweka sawa kwa lolote, maana machale yalishaanza kumcheza.

Simu ya dereva ikaita, alipoitoa na kuitazama kwenye kioo chake, jina lililojitokeza likamtisha, lakini hakutaka kuonyesha hofu yake. Akaipokea na kusema neno moja tu “Yes”.

Jibu hilo lilimtosha mpigaji aliyekuwa ameegesha gari katika njia ambayo gari lile lilikuwa linapita. Ndani ya gari lile kulikuwa na watu wanne, wote wakiwa na bunduki. Walishajiandaa kwa mauaji na uporaji fedha!
Walikuwa wamesimama eneo ambalo ndilo lilipangwa kwa ajili ya shambulizi la kushtukiza, ambalo kwa mujibu wa mipango ya awali, lingetakiwa kumwacha hai dereva tu, ikibidi akiwa na majeraha kidogo kwa sababu yeye ndiye mkuu wa mipango!

Ilikuwa ni kwenye kona, ambapo hata hivyo kulikuwa na eneo pana la kuweza kupishana magari hata matatu. Ni kona ambayo hakukuwa na nyumba ambayo mlango wake wa kutokea au kuingilia uliiangalia barabara. Lilikuwa ni eneo zuri kwa wapanga mashambulizi, kwani kama lingeweza kuchukua muda mfupi, wahalifu wangeweza kutoweka bila kipingamizi.

Kundi la akina Beka na Shosi walijaribu mara kadhaa kulipita gari lile ili walikinge kwa mbele, lakini ilishindikana, ama sababu ya magari mengine kupishana au wembamba wa barabara.

Ghafla wote wakakumbuka kama kuna eneo lile la kona, wakawapigia simu vijana wa Kinyarwanda ili wafanye kila wanachoweza kumpita na kwenda kulisubiri eneo lile.

Walipokubaliana, nao wakakanyaga mafuta na kuwahi eneo la tukio. Bila kujua, wakawa wameegesha wakiwa wameangaliana uso kwa uso na gari lililokuwa mbele yao. Wote hawakujua walilisubiri gari moja, lenye fedha..!!

Inaendelea.
 
SEHEMU YA 35

Ghafla wote wakakumbuka kama kuna eneo lile la kona, wakawapigia simu vijana wa Kinyarwanda ili wafanye kila wanachoweza kumpita na kwenda kulisubiri eneo lile. Walipokubaliana, nao wakakanyaga mafuta na kuwahi eneo la tukio. Bila kujua, wakawa wameegesha wakiwa wameangaliana uso kwa uso na gari lililokuwa mbele yao. Wote hawakujua wanalisubiri gari moja, lenye fedha.
Sasa endelea..

Sean Jackson, askari wa kikosi maalum cha kupambana na ujambazi, alikuwa ameegesha pikipiki yake yenye namba za kiraia pembeni ya kituo cha daladala cha Afrikana, kisha yeye mwenyewe akaenda kukaa katika mbao za kituo hicho, macho yake yakiwa yanaangaza kila kona ya eneo hilo, kuangalia mambo yanavyokwenda.

Ulikuwa ni mpango maalum wa jeshi la Polisi kuweka askari karibu kila kwenye mkusanyiko, ili angalau kuweza kuwahi au kuhisi matukio yanayotokea. Katika kila umbali wa mita 200 kulikuwa na vijana maalum wasio na sare. Tokea mfumo huu ubuniwe, umeonyesha mafanikio makubwa kwani ujambazi wowote uliofanyika katika maeneo waliyokuwepo, watuhumiwa wote walikamatwa.

Akiwa kituoni hapo, aliliona gari la Night Support likitoka katika kituo cha mafuta, alielewa utaratibu wa usafirishaji wa fedha na alijua lilikuwa na fedha ndani yake. Alilitupia macho wakati likimpita pale alipokuwa na aliendelea kuwa nalo likienda.

Wakati akitaka macho yake yaachane na gari hilo, akapata mshtuko mkubwa baada ya kuliona likikata kona na kupita njia ya uchochoroni. Haikuwa kawaida.Haraka akaifuata pikipiki yake, lakini kabla ya kuwasha, akapiga namba za kampuni ile ya ulinzi, kwani alikuwa na simu za kampuni zote za ulinzi jijini, kwani majukumu yao kuna wakati yaliingiliana.

“Kuna gari lenu limekuja huku Afrikana, lina ratiba gani leo,” Sean alisema kwenye simu mara baada ya kujitambulisha.“Sean vipi kaka, hapa wanaonekana wamefuata hela pale petrol station kupeleka benki kaka,” alijibiwa upande wa pili.

Akakata simu, akawasha pikipiki yake, lakini simu yake ya mkononi ikaendelea kupiga huku na kule, akakanyaga mafuta kiasi hadi alipokuwa umbali wa mita hamsini kutoka lilipo gari lile lenye fedha, katikati yake kukiwa na magari manne.

Akawasiliana na Polisi Kawe, ambako baada ya kuwaelezea hali hiyo, gari tatu zenye polisi waliovalia kiraia zikatayarishwa. Kwa kuwa waliifahamu njia hiyo, walijua maeneo ambayo yangeweza kutumika kwa ujambazi wa kupora fedha kama kulikuwa na mpango huo.

Gari la kwanza likaenda kuegeshwa katika kona inayotokeza barabara ya Mbezi chini kutokea barabara ya Bagamoyo, palepale ambako gari lenye fedha litatokezea. Pikipiki za polisi, maarufu kama Tigo nazo zikawa tayari, zikiwa karibu kabisa na eneo la tukio.
***
Mle ndani ya gari, Meneja akaanza kuhisi hali ya hatari, jinsi magari yalivyokuwa yakimpita na macho yao kwake, yakampa mashaka, akapeleka mkono wake kwenye mfuko alioweka bastola yake, ilikuwepo.
Akaichomoa na kumwambia dereva; “Nahisi kama kuna hatari, kuwa makini.”

Kauli ile ilimpa mshtuko mkubwa sana dereva, lakini akajikaza. Akajiuliza amejuaje, lakini hata hivyo akamdharau, kwa sababu alikuwa na uhakika ana dakika chache tu za kuishi. Akakanyaga mwendo na mara akaingia eneo la kazi!

Watu waliokuwa katika mpango mmoja na dereva walikuwa wa kwanza kulianzisha, mtu aliyekuwa amekaa upande wa abiria kwenye gari hilo dogo, akatokeza na bunduki na kumlenga Meneja ambaye alishamuona na akalala chini haraka. Risasi zilikichakaza kioo cha mbele cha gari lile na kuwashtua askari wawili waliokuwa siti za nyuma.

Wakafungua milango na kutoka nje, lakini wakakutana na risasi zilizowaua palepale. Jamaa wakawa wanakimbia kulielekea gari lile. Kundi la akina Beka likapatwa na mshangao mkubwa kuona mchezo ule, wakausoma haraka na wale vijana wa Kinyarwanda wakatoa ishara ya kuwataka akina Beka kutulia.

Ni mpaka waliposhambulia sehemu ya kuhifadhia fedha kwa ajili ya kulifungua, ndipo na wao walipoanza kurusha risasi zilizowaua watu watatu kati ya wanne waliokuwepo, kisha wakakimbilia na kwenda kutoa mifuko ya fedha.

Mfuko wa kwanza mkubwa ulioshushwa ukarushwa kwa akina Beka waliosogea na pikipiki yao, wakakanyaga mafuta kuondoka kwa kasi eneo lile, Shosi akiwa dereva, Beka amekamatia fuko katikati, mkono mmoja ameinua juu bastola, akipiga risasi ovyo.

Je, nini kitatokea?
 
SEHEMU YA 36

Shosi akawasha pikipiki, wakitaka wapitie katika vichochoro vya upande wa pili wa njia. Ghafla akahisi kama kitu kimemuingia begani, alipojitazama, akaona damu zinatoka. Alipomtazama Beka, akamuona akianguka na fuko lake la hela mtaroni, macho yake yakaanza kuhisi giza, taratibu akapoteza fahamu!
Endelea...

DAYANI, mzee Linus na mkewe walikuwa wamekaa nje ya hoteli waliyofikia, wakibadilishana mawazo kuhusiana na tukio lililotokea, huku akiwahakikishia kuwa vijana wa kazi walikuwa wamekwenda kurekebisha mambo na muda wowote kuanzia wakati huo watachukua kilicho chao.
Mama alionekana mwenye mawazo mengi yaliyotoa ishara kwa Dayani kama wasiwasi, akazidi kumtaka shemeji yake huyo kuamini alichokuwa akikisema.

“Kwa hiyo sasa hawa jamaa zetu ndiyo inakuwaje, tunawaacha?” Dayani aliuliza huku macho yake yakiwa zaidi kwa shemeji yake.

“Hatuwezi kuwaacha, lakini nadhani tubadili mbinu, maana hii ya moto tunaweza kushtukiwa, nyumba mbili mtaa mmoja lazima jamii itashtuka, hii tu yenyewe naona watu wanaanza kunitilia wasiwasi,” alisema mzee Linus, mkewe akitingisha kichwa kukubaliana naye.

“Lakini pia ningependa jambo hili nalo lisichukue muda mrefu, ikibidi misiba iambatane,” Dayani alisema kwa sauti yenye msisitizo. Linus na mkewe walitingisha vichwa kuonyesha kukubaliana naye.
Baada ya kuzungumza kuhusu suala hilo, waliendelea na mambo mengine hadi ilipofika mchana, wakati Dayani alipoaga kurejea nyumbani kwake, akiahidi kuwapigia simu na kuwaeleza kuhusu mzigo wao kabla jua halijazama.

***
Katika chumba maalum kwenye hospitali ya Mwananyamala, watu wawili walikuwa wamelazwa huku miguu yao ikiwa imefungwa pingu, chupa za dripu zikiwa zimefungwa mikononi mwao huku madaktari wawili wakiwashughulikia. Pembeni yao, askari kanzu wasiopungua wanne nao walikuwa wakiangalia kila hatua inayoendelea.

“Hawana majereha makubwa, baada ya kuwatoa hizi risasi, ni majeraha ambayo wanaweza kwenda kuponea nyumbani, kwa hiyo tunaweza kuwaruhusu watoke kesho,” Dr Editha, mwanamama shupavu kwa upasuaji, aliyekuwa daktari kiongozi katika shughuli hiyo, aliwaambia askari waliokuwepo chumbani.

“Vizuri, fanya hivyo, na nafikiri usiwaongeze tena hiyo nusu kaputi, kama majeraha siyo makubwa, basi tunaweza kuongea nao baadaye kidogo,” Inspekta Jonas, mpelelezi kutoka Makao Makuu ya Jeshi la Polisi alimwambia dokta Editha.

Vitandani, walikuwa ni Beka na Shosi, ambao walipigwa risasi wakati wakijiandaa kutoroka na fuko la fedha baada ya kunusurika ajali. Walikamatwa na fedha zote zikaokolewa. Wale vijana wa Kinyarwanda nao hawakufika mbali, kwani baada ya mmoja wao kupigwa risasi na Sean, wenzake walipojaribu kukimbia kimyakimya, wananchi walianza kuwakimbiza huku wakiwazomea.

Kuona vile wakaanza kupiga risasi ovyo, lakini kadiri walivyokuwa wakipiga na wananchi kukimbia, ndivyo walivyozidi kuwazonga kiasi kwamba wakajikuta wameishiwa risasi, wananchi wakawasogelea na kuwafikia, waliwaangushia kipigo na kuwachoma moto wote watatu.
Askari walijitahidi kuwafikia na kuwatawanya kwa mabomu ya kutoa machozi, lakini hadi walipotawanyika, vijana wale walibakia majivu!!

***
Beka na Shosi wote walirudiwa na fahamu kiasi cha saa kumi jioni, walishangaa kujikuta wakiwa vitandani, miguuni wakiwa na pingu mikononi na chupa za dripu. Wakatazamana na walipogeuza zaidi shingo zao, wakakutana na macho ya watu wasiowafahamu.

“Vipi wazee, salama?” walisalimiwa na jamaa aliyekuwa akitabasamu, mbele yao.
“Salama tu kaka, vipi?” Beka alikuwa wa kwanza kujibu.

“Poa, vipi mnajua hapa ni wapi,” aliwauliza huku vijana wale wakiendelea kushangaa.
Wakatingisha vichwa kuonyesha kutotambua lolote, lakini wakiendelea kujikumbusha. Baada ya kama dakika kumi hivi, Yule mtu aliyekuwa chumbani akawaambia kuwa pale walikuwa hospitalini, na kwamba waliokotwa wakiwa wamejeruhiwa kwa risasi na majambazi..!!!

Beka na Shosi wakatazamana, kwa mbali kila mmoja akaanza kupata picha.

Je, nini kitaendelea?
 
SEHEMU YA 37


Wakatingisha vichwa kuonyesha kutotambua lolote, lakini wakiendelea kujikumbusha. Baada ya kama dakika kumi hivi, Yule mtu aliyekuwa chumbani akawaambia kuwa pale walikuwa hospitalini, na kwamba waliokotwa wakiwa wamejeruhiwa kwa risasi na majambazi..!!!
Beka na Shosi wakatazamana, kwa mbali kila mmoja akaanza kupata picha.
Sasa endelea...

Inspekta Jonas aliwaangalia wale vijana pale kitandani sura yake ikiwa imejaza tabasamu, kiasi kwamba kadiri Beka na Shosi walivyokuwa wakirejewa na fahamu zao, walishindwa kumwelewa kama alikuwa ni askari au daktari.

“Samahani Bro, sasa wewe ni askari au daktari na tuliokotewa wapi,” Shosi alimwuliza baada ya kuwa ameshakumbuka mchezo mzima ulivyokuwa.

“Mimi ni daktari tu, sielewi lolote, wamewaleta tu hapa na kutuzuia kuuliza kitu chochote, walituambia tu tuwatibu,” Inspekta Jonas aliongopa na wakati huohuo akawaomba udhuru kuwa anatoka kidogo, lakini akawatahadharisha kuwa wasijitingishe sana, maana pingu walizofungwa zinabana kadiri wanavyojitingisha.

Inspekta Jonas akatoka, akiwa ameacha vinasa sauti vilivyofungwa chini ya vitanda vya wawili hao, akaenda nje kuungana na vijana wake waliokuwa wanacheza drafti. Akawaambia kwamba jamaa wamezinduka na amezungumza nao kidogo.

***
Baada ya kutolewa hospitalini kesho yake, Beka na Shosi walipelekwa katika eneo moja lililo katikati ya jiji la Dar es Salaam, lakini lililokuwa kimya sana. Ndani ya nyumba moja kubwa, iliyokuwa haina dalili za kuishi watu, waliwakuta watu kama sita hivi, wakiwa na miili iliyojazia, wenyewe wakisema mabaunsa.

Wakati wakitoka Mwananyamala hospitalini na kuelekea mjini, walijua wanakwenda Kituo kikuu cha Polisi, lakini walipoona wanaingia mjini zaidi, wakaamini wanapelekwa makao makuu ya Polisi, sasa wakajikuta wanachanganyikiwa walipopita makao makuu hayo na kuendelea kuelekea hospitali ya Ocean Road.

Katika kiuchochoro kisafi, wakashangaa zaidi walipoona mlango wa geti kubwa jeusi ukifunguka na gari kwenda moja kwa moja. Gari likasimama ndani na geti likarejeshwa, milango ikafunguliwa na vijana wale wakatolewa mikononi wakiwa na pingu zao. Zikafunguliwa nao wakaelekezwa kukaa kwenye benchi lililokuwa pembeni.

Katika gari waliyokuja nayo, Prado yenye rangi nyeusi, kulikuwa na askari kanzu wanne akiwemo Inspekta Jonas na Sean. Kwenye nyumba hiyo, licha ya wale mabaunsa sita, pia kulikuwa na watu wengine wawili wenye umri wa makamu.

Beka na Shosi waliwatambua watu wawili miongoni mwa wale mabaunsa, ni askari ambao walishawahi kuwaponyoka katika matukio mawili siku za nyuma. Walipotazamana, wale askari walitabasamu, lakini kwa vijana wale, wakasinyaa, ujasiri waliobaki nao ukazidi kutoweka.

“Nadhani mnafahamu kwa nini mpo hapa vijana au nimekosea,” aliuliza mmoja kati ya wale watu wazima wawili baada ya kuwa wamewazunguka pale walipokuwa wamekaa. Beka na Shosi wakatazamana kabla ya kujibu, walionekana kutegeana.

“Nataka kuamini kuwa mnajua. Hawa vijana wenzenu waliojazia, kazi yao ni kuwakumbusha watu kama nyinyi wajibu wa kutambua kilichowaleta hapa, kwa hiyo kama hamjui kilichowaleta hapa niwaruhusu wawakumbushe,” alisema tena yule mzee kwa sauti ya upole sana.

“Lakini kabla sijawaambia wawakumbushe, nataka kuwapa tahadhari, ni watu wachache sana waliowahi kutoka hapa wakiwa hai baada ya kukumbushwa, kwa hiyo ni juu yenu sasa kucheza kamari,” alisema.

“Tunajua mzee,” wote kwa pamoja walijibu, majibu ambayo yalimfurahisha sana yule mzee, ambaye aliwaambia;

“Kitu kimoja cha faida kwenu, tunafahamu nyinyi ni watu wa kutumwa, tunamtaka aliyewatuma na sisi tutawalinda, vinginevyo tutawapoteza na mnayemficha pia tutamfikia, haya nani atatupa mkanda, wewe hapo elezea, nadhani unajua kuwa tunajua ukweli, ole wako utamponza na mwenzio,” alisema mzee huyo akimuonyesha sura ya kutisha Beka aliyeteuliwa kuongea.

Beka akakohoa, kuonyesha kujiandaa kwa ajili ya kutoa maelezo. Yule mzee alimpa kitu kama simu, akimwambia wakati anazungumza akiweke mdomoni mwake, ambacho dhahiri kilikuwa ni kipaza sauti. Macho ya vijana wote wawili yalionyesha woga, kitu kilichowapa nguvu wale watu waliowazunguka…
 
SEHEMU YA 38

Beka akakohoa, kuonyesha kujiandaa kwa ajili ya kutoa maelezo. Yule mzee alimpa kitu kama simu, akimwambia wakati anazungumza akiweke mdomoni mwake, ambacho dhahiri kilikuwa ni kipaza sauti. Macho ya vijana wote wawili yalionyesha woga, kitu kilichowapa nguvu wale watu waliowazunguka…
Sasa endelea...

Mzee Komba na mkewe walikuwa wamekaa sebuleni kwao, wakijadiliana hili na lile kuhusu maisha yao baada ya matukio yale ya kushangaza. Jirani na rafiki yao wa muda mrefu aligeuka adui mkubwa na wakati wowote maafa zaidi yangeweza kutokea.

Waliwaita watoto wao na kuwaeleza jinsi ambavyo familia yao ilivyokuwa vitani na majirani, na kuwataka kuwa makini kwani lolote baya linaweza kuwatokea endapo hawatakuwa waangalifu.

***
Dayani alikuwa amekaa katika moja ya vibanda vilivyomo ndani ya baa yake ya Zanzi wakati simu yake ya mkononi ilipoita na mara moja mapigo ya moyo wake yakapiga. Akaipokea kwa hamasa na baada ya sekunde chache za kusikiliza, akaiondoa sikioni na kuikata.

Baada ya sekunde chache, naye akaichukua tena simu yake na kubonyeza namba kadhaa, kisha akaipeleka sikioni kwake. Ikaita kwa muda mrefu bila kupokelewa. Akakata na kusubiri, baada ya dakika mbili akaichukua na kuirudia tena ile namba ambayo sasa ilipokelewa.
“Chuga” upande wa pili wa simu uliita.
“Uko wapi?”
“Hotelini”

“Nakuja”
Dayani aliliendea gari lake, akaingia na kuwasha, kisha akaelekea kwanza nyumbani kwake, akakaa muda wa dakika kama ishirini akizungumza na mkewe, kisha akatoka akiwa na begi dogo mkononi mwake.
Akaingia tena kwenye gari lake na kuliwasha. Dakika ishirini baadaye alikuwa nje ya hoteli aliyofikia rafiki yake mzee Linus. Akaegesha na kuingia ndani moja kwa moja hadi chumbani kwake.

“Chuga..nina wasiwasi mambo yameharibika, nimeongea na Beka kwa simu, ananiambia niende sehemu akanipe mzigo, sauti yake haikuwa huru, ninamjua yule dogo, kwa uzoefu wangu, wamekamatwa,” Dayani alisema huku akionyesha sura ya mashaka, maneno yaliyomshtua sana Linus na mkewe.
“Dah, kwani walikuwa wameenda wapi,” aliuliza.

“Hakuna muda wa maswali, wale watakuwa wamebanwa na wamesema kila kitu, wameniita ili wakanikamate, cha kufanya hapa ni mimi na wewe kutoweka haraka sana kabla hatujakamatwa,” alisema huku akisimama, ishara kwamba waondoke.

“Mke wangu naye tunaenda naye?” aliuliza huku akijifuta jasho.
“Hapana, yeye anaweza kwenda kukaa sehemu yoyote, hata akikamatwa ni rahisi kwake kukataa kuwa hajui lolote,” akatoka nje akiwaacha ndani mzee Linus akijadiliana na mke wake.
“Sasa mume wangu itakuwaje, maana naona hasara juu ya hasara,” alisema mama Tony.
“Hata sielewi, nimechanganyikiwa kabisa, hebu ngoja kwanza nitoke eneo hili nisikilizie. Halafu mimi sitaki wewe uondoke, kaa hapahapa, ili ujue kinachoendelea upate kunifahamisha,”

“Kwani nyie mnaenda wapi?” aliuliza mkewe
“Sijui, nitakufahamisha,” alisema huku naye akitoka, baada ya kuwa amempa fedha kidogo. Benki walikuwa na akiba ya kutosha ambayo angeweza kuitumia wakati huu wa matatizo.
Akatoka nje akiwa hana hata mfuko wa Rambo, kwa sababu nguo zake zote ziliteketea na hakuwa amenunua tena. Akaungana na Dayani garini, likawashwa na likaelekezwa njia ya Bagamoyo.

***
Beka na Shosi walikuwa ndani ya gari jeusi lililochokachoka kidogo, nje ya baa ya Jilipue, mitaa ya ndanindani Mwananyamala jijini Dar es Salaam. Wakati wanazungumza na Dayani, askari mmoja alikuwa pembeni yao akiwasikiliza. Walipomaliza wakanyang’anywa simu na kuelekezwa kutulia ndani ya gari.
Zaidi ya askari kanzu kumi walikuwa wamezunguka eneo hilo wakimsubiri Dayani.

Kwa jinsi walivyokuwa wamejipanga, walikuwa na uhakika hataweza kuponyoka hata akiwa mahiri vipi. Baadhi yao walikuwa kaunta, wengine kazi yao ilikuwa ni kuangalia nyendo za wale vijana garini.
Saa moja ilipita bila Dayani kutokea, askari mmoja akawaendea mle garini na kuwauliza mbona bosi wao hajatokea hadi muda ule, nao wakamwambia hawaelewi. Yule askari akawapa ishara wenzake na watatu kati yao wakalisogelea lile gari.

“Jamaa hajatokea, tufanyaje?” aliwauliza wenzake.
“Hebu wamcheki tena kumuuliza amefika wapi,” mwingine alishauri. Wakakubaliana, wakatoa simu ya Beka na kumpa ili apige tena simu kwa Dayani.
 
SEHEMU YA 39


“Jamaa hajatokea, tufanyeje?” aliwauliza wenzake.
“Hebu wamcheki tena kumuuliza amefika wapi,” mwingine alishauri. Wakakubaliana, wakatoa simu ya Beka na kumpa ili apige tena simu kwa Dayani.
Sasa endelea..

Moyoni, Beka alijua bosi wake ameshashtukia mchezo na kwa jinsi alivyokuwa akimfahamu, hivi sasa atakuwa njiani kuelekea chimbo. Akaichukua simu hiyo na kupiga namba ya Dayani, huku akiwa ameweka laudi spika.

Kule alikokuwa, Dayani aliiona simu ya Beka ikiingia, wakati huo, alikuwa anaingia barabara ya kuelekea Morogoro, inayotokea katika eneo la Tamco, mbele kidogo ya Kibaha mkoani Pwani.
“Hao, wanataka kujua nimefika wapi, ngoja niwasubirishe,” Dayani alimwambia Mzee Linus kabla ya kuichukua simu na kuipokea.

“Yes Beka, niko njiani, hapa Lugalo kuna kafoleni kidogo, nadhani kuna ajali hapo mbele, nisubiri tu nadhani muda si mrefu natia timu hapo, si unajua tena leo bia hadi majogoo..” Dayani alizungumza kwa kujiamini huku akimbinyia jicho mzee Linus aliyekaa pembeni yake.

“Okee bro, maana naona umechelewa sana na si unajua tumeshaleta noma sasa hofu tupu kuwa na huu mzigo,” Beka alizungumza upande wa pili huku wale askari wakitingisha vichwa kuonyesha kukubaliana naye.

Beka na Dayani wakaagana. Akiwa sasa ameshatulia katika barabara hiyo, Dayani alipunguza mwendo pale tu aliposubiri gari la mbele yake kabla ya kulipita na kwenye matuta. Kama watasubiri nusu saa kuanzia muda ule, atakuwa ameshapita Chalinze.

Baada ya kusikiliza mazungumzo ya Beka na Dayani, wale askari wakakutana tena kujipanga upya na majadiliano zaidi. Kiongozi wao, Inspekta Jonas, akiwa ameliegemea Prado, lenye namba za kiraia aliwaambia wenzake.
“Uzoefu wangu wa miaka 15 katika kazi hii, unaniambia kwamba huyu jamaa tunayemsubiri hawezi kufika, ameshashtuka. Huyu jamaa ni jambazi mzoefu, ninamfahamu na tumeshamkosa kosa kwenye matukio mengi sana. Kila siku tunakosa ushahidi ili kumkamata, sasa tujipange kwa ajili ya kumtafuta, siyo kumsubiri tena,” alisema na kuwatazama wenzake, ambao nao walikubaliana naye kwa kutikisa vichwa vyao.
Wakaingia kwenye magari yao, lile la akina Beka likiwa mbele. Beka nyuma ya usukani na Shosi pembeni yake, askari wawili wenye miili mikubwa walikuwa nyuma yao wakiwaelekeza cha kufanya.
“Huwa mnakutana wapi kwa ajili ya kupanga mipango yenu ya uporaji,” askari mmoja aliwauliza wale vijana.

“Mara nyingi huwa ni pale kwenye baa yake ya Zanzi,” Shosi alijibu. Alipowauliza kama kulikuwa na watu wengine zaidi walikuwa viongozi wao zaidi ya Dayani, walikataa na kusema yeye ndiye kila kitu.
***
Dayani alijua wapi anakwenda. Mzee Linus akili yake ilishahama, alijiona mwenye mikosi baada ya jaribio lake la kumdhuru jirani yake, sasa kuonekana kama litamaliza kabisa. Hakuwa na furaha kabisa moyoni mwake, kitu ambacho Dayani alikiona dhahiri.

“Chuga siku hizi umekuwa mlokole sana, yale makeke yako yamepotea kabisa, yaani hapa ni kama niko na mzoga endapo jamaa watatokea na kuanzisha mapambano,” Dayani alimwambia mzee Linus.“Siwezi kuwa na ushujaa na ujasiri kama wa kipindi kile, mimi nimeishi uraiani miaka zaidi ya ishirini bila kumtoa mtu utumbo, sasa wewe kila siku unatoa roho za watu, hatuwezi kufanana,” alisema mzee Linus.

“Ni kweli najua, lakini sasa katika ishu kama hii lazima ukomae, jivalishe ujasiri wa enzi zile za hatari ili tuvuke salama, hili jambo litaisha tu na dhamira yetu itatimia,” alisema Dayani na kupapasa sehemu ya mbele, akafunua eneo moja hivi na kutoa sigara, akaiwasha.

Saa moja na nusu baadaye waliingia mjini Morogoro, katika mzunguko wa Msamvu, Dayani akakizunguka na kulielekeza gari njia ya Dodoma.

Kilometa kama kumi, katika eneo linaloitwa Mkundi, akawasha indiketa kuonyesha kwamba anakata kulia, akaingia katika njia ya vumbi na baada ya kama dakika tano, akasimama nje ya nyumba moja kubwa, iliyozungushiwa ukuta mkubwa, mbele ya geti kubwa, akapiga honi!Je, hapo ni kwa nani? Hekaheka za kutafutana zitafikia wapi? Usikose
 
SEHEMU YA 40

Saa moja na nusu baadaye waliingia mjini Morogoro, katika mzunguko wa Msamvu, Dayani akakizunguka na kulielekeza gari njia ya Dodoma.

Kilometa kama kumi, katika eneo linaloitwa Mkundi, akawasha indiketa kuonyesha kwamba anakata kulia, akaingia katika njia ya vumbi na baada ya kama dakika tano, akasimama nje ya nyumba moja kubwa, iliyozungushiwa ukuta mkubwa, mbele ya geti kubwa, akapiga honi!

GETI lilifunguliwa na kijana mmoja mwenye umri upatao miaka kama 16 hivi, lakini aliyeonekana mkakamavu, kutokana na misuli ya mikono yake kutuna. Akaliacha wazi na Dayani akaliingiza gari lake hadi ndani na nyuma yake, geti lile likafungwa.

Akalisimamisha gari hilo katikati ya magari mengine kama sita hivi yaliyokuwa yameegeshwa mle ndani. Nyumba ilikuwa kubwa iliyomshangaza mzee Linus, akamtazama kwa mshangao kidogo na kwa uzoefu wake, akatambua kuwa ile ilikuwa ni maficho yake mambo yanapochafuka.

Dayani akampa ishara ya kushuka, wakateremka na kuufuata mlango mkubwa mbele yao. Akionekana kuwa mwenyeji, aliufungua mlango na kuingia sebuleni. Ilikuwa sebule kubwa pia, ya kisasa ambayo ilikuwa imepangiliwa vizuri sana.

“Karibu Chuga, hapa ndipo yatakuwa makazi yetu kwa muda tukisikilizia kinachoendelea Dar es Salaam, humu ndani kuna kila kitu, tunaweza kukaa mwezi mzima bila kutoka nje,” Dayani alimweleza rafiki yake.
“Nani anaishi humu?” mzee Linus alimuuliza.

“Hii ni nyumba yangu, lakini ni chimbo letu kila linapotokea tatizo. Wanaweza kututafuta dunia nzima lakini wasijue kama tupo hapa. Kama umekaona kale kakijana kalikofungua mlango, wako wenzake kama wanne hivi, ndiyo walinzi na ni vijana wa kazi vilevile, usiwaone vile, wanaweza kuangusha mbuyu wale,” alisema Dayani, maneno yaliyomsisimua mzee Linus.

Dayani alibonyeza kengele moja iliyokuwepo pale sebuleni na baada ya dakika moja, vijana watano wa kiume walikuwa wamesimama mbele yake, wakionyesha nidhamu ya hali ya juu.

“Chuga, kama nilivyosema, hawa ni vijana wetu wa kazi ambao wanaishi hapa. Wanasoma shule moja ipo hapo mbele, lakini pia wanaweza kufanya jaribio lolote la hatari ambalo unaweza kufikiria. Vijana, ni rafiki yangu wa muda mrefu na ni mchapakazi, tumekinukisha Dar, tutakuwa hapa kwa muda,” alisema na kuwatazama vijana wake kwa zamu.
***
Beka alisimamisha gari hatua chache kabla ya kufika nyumbani kwa Dayani, nyuma yake kulikuwa na magari mawili ambayo yalimpita na kwenda moja kwa moja hadi kwenye geti la nyumba yake. Lililokuwa limetangulia lilipiga honi, lakini mlango haukuonekana kufunguliwa.

Mtu mmoja akashuka na kutoa ishara kwa Beka kuteremka, akashuka garini na kumfuata na alipomfikia, akaambiwa agonge mlango.“Najua kuna namna zenu za kuwasiliana, hebu gonga ili ajue kuwa ni wewe,” Yule askari alimweleza.

“Sisi hatujawahi kufika hapa hata mara moja, mikutano yetu yote huwa pale baa au eneo lingine, lakini si hapa, alitukataza kabisa kusogelea nyumba hii,” Beka alimweleza.
Askari wengine wasio na sare walitoka nje ya magari na kusogelea pale mlangoni. Baada ya majadiliano ya muda mfupi, wakakubaliana kwenda kumchukua mjumbe wa mtaa ili aje kusaidia kugonga mlango.
***
Imelda, mke wa Dayani aliyaona magari yote matatu yaliyosimama nje ya geti la nyumba yake na kwa kuwaangalia, aliwatambua kuwa ni askari. Akakumbuka jinsi mume wake alivyomweleza, akaamua kutoroka kupitia handaki maalum lililojengwa ndani ya chumba chao cha kulala.

Dayani alitengeneza handaki ambalo lilitokeza kwa nje, umbali wa kama mita 100 kutoka kwenye uzio wa eneo lake. Sehemu ya kutokea eneo hilo, pia ilikuwa ni eneo lake ambalo alijenga nyumba ndogo iliyokuwa haikaliwi na mtu.

Imelda alivipanga vizuri vitu vyake, akatoa bastola na bunduki moja vilivyokuwemo chumbani, akaingia chini ya uvungu wa kitanda, akafunua mfuniko wa kuingia ndani ya handaki, akaurudishia vizuri, akaanza kuteremka na kutambaa kuelekea nje.
 
SEHEMU YA 41


Imelda alivipanga vizuri vitu vyake, akatoa bastola na bunduki moja vilivyokuwemo chumbani, akaingia chini ya uvungu wa kitanda, akafunua mfuniko wa kuingia ndani ya handaki, akaurudishia vizuri, akaanza kuteremka na kutambaa kuelekea nje!
Sasa endelea...

GARI dogo la rangi ya kahawia lilifunga breki nje ya nyumba ya mzee Komba, watu wawili wakatoka nje na kugonga geti. Mama Juddy alikuwa karibu, akachungulia katika tundu la ufunguo ili kuwatambua wagongaji, lakini hakufanikiwa, hata hivyo, kwa kuwa ilikuwa ni mchana wa jua kali, akafungua mlango na kuwakaribisha.

Wakauliza kama pale ni nyumbani kwa mzee Komba, mama huyo akakubali kwa kutingisha kichwa. Akawakaribisha sebuleni kisha akamfuata mumewe chumbani kumweleza juu ya ugeni huo ambao ulikuwa bado haujajitambulisha. Alipofika na kuwasalimia, mazungumzo yakaanza.

“Sisi ni Polisi, mimi naitwa Noel,” alisema askari mmoja huku akimpatia mzee Komba kitambulisho chake. Na yule mwingine naye akampa na baada ya kuviangalia na kujiridhisha, akatingisha kichwa na kuwataka waendelee na kilichowaleta.

“Huyu anaitwa Yona. Tumekuja hapa kwako ili utusaidie mambo machache unayoyajua kuhusu Linus Kingwande,” Noel alimweleza mzee Komba.“Mambo ninayoyajua? Kama yapi,” naye alijibu kwa kuuliza.
“Tuna taarifa kuwa ni rafiki yako wa muda mrefu, lakini uhusiano wenu katika siku za hivi karibuni ulidorora sana, ni kweli?”

“Ni kweli, sielewi hasa tatizo lilianzia wapi, lakini nafikiri ni mambo ya watoto yamesababisha hadi ikawa hivi.”“Kivipi labda, ungejaribu kutufafanulia kidogo,” Noel alisema.Mzee Komba akasimulia kila kitu alichokijua kuhusu uhusiano wao, urafiki wao na mwanzo wa mzozo na hadi walipofikia. Wale polisi wakatazamana huku wakionekana kuwa kwenye tafakuri nzito.

Baada ya kuuliza uliza tena maswali mawili matatu, waliaga na kuondoka huku wakiwaachia maswali mengi yaliyokosa majibu wanandoa hao wawili. Walipobaki peke yao, wakajadiliana tena na kwa mbali, wakaanza kuhisi huenda jirani yao alikuwa katika matatizo makubwa.
***
Imelda alitambaa kwenye mtaro huo polepole huku akiwa na ujasiri wa ajabu. Tokea alipotambua kuwa mume wake ni jambazi, akajikuta amejivika roho ngumu, isiyojali wala kuogopa na mara mbili alishajaribu bila mafanikio kumshawishi Dayani waende wote eneo la tukio.

Kitendo hicho kilimfanya Dayani ampende sana na alimweleza kila jambo alilolifanya, tofauti na majambazi wengine ambao huwaficha wake zao kazi wanazofanya. Alipofika kwenye nyumba ndogo ambayo mtaro huo unatokea, alisimama kwa muda kusikilizia kabla ya kuufunua mfuniko.

Akachungulia kupitia dirishani na kujiridhisha kuwa hakukuwa na mtu karibu, akachukua ufunguo mmoja kati ya mitatu iliyokuwepo kwenye msumari, akafungua mlango na kutoka nje akiwa katika muonekano wa hijab. Bunduki aliiacha ndani ya handaki, lakini bastola ilikuwa pamoja naye.

Akaanza kutembea kuelekea barabarani, simu yake ya mkononi ikiwa sikioni, aliwasiliana na mume wake kumwelezea kinachoendelea, habari ambazo zilianza kumtia presha Dayani. Katika siku zote za uhalifu wake, polisi hawakuwahi kufika nyumbani kwake!

Alipofika barabarani, akasogea kituo cha daladala ili apande basi aelekee Kitunda kwa shemeji yake, akakae huko hadi mumewe arudi. Akiwa kituoni hapo, akamuona mjumbe wa mtaa wao, akiwa kwenye gari na watu waliofika nyumbani kwake.

Akabonyeza tena namba za mumewe, akasogea pembeni mbali na watu kisha akamfahamisha juu ya jambo hilo. Mumewe akamweleza kuwa kwa vyovyote wanakwenda kuvunja mlango ili waingie ndani.
“Umeziondoa zile bunduki?” Dayani aliuliza akiwa na hofu kubwa.

“Ndiyo, ile shotgun nimeiacha kwenye mtaro ila ile ndogo ninayo naondoka nayo,” mkewe alimjibu akiwa anatazama huku na huko kuona kama watu wanaweza kumtambua!
 
SEHEMU YA 42

“Ndiyo, ile shotgun nimeiacha kwenye mtaro ila ile ndogo ninayo naondoka nayo,” mkewe alimjibu akiwa anatazama huku na huko kuona kama watu wanaweza kumtambua!
Endelea

Dayani alianza kuhisi hatari kufuatia mazungumzo yake na mkewe, lakini akaamua kukaa kimya bila kumfahamisha rafiki yake Linus juu ya kinachoendelea. Na mkewe Imelda naye ndiyo kwanza aliona kama sinema inaanza, alitamani apate kashikashi ili azidi kukomaa katika kazi za kijambazi.

Mzee Linus alihisi kama kitu usoni mwa rafiki yake, kwani alikuwa na uzoefu naye, ingawa hata hivyo naye hakutaka kumshtua, akabakia kumezea moyoni mwake. Hata hivyo, akataka kujua kuhusu kinachoendelea, akaamua kumpigia simu mkewe.

Simu ya mkewe haikupatikana. Kwa kuwa ilikuwa bado mapema, akaamini ilikuwa kwenye chaji na kwamba angeongea naye muda ukifika.
**
Mkuu wa kituo cha Polisi Wazo alikuwa anapekua pekua kitabu kikubwa cha ripoti na majalada mbalimbali, alikuwa anatafuta sehemu aliyoandika taarifa iliyomhusu mzee Linus, kumbukumbu ilikuwa bado kichwani mwake kuwa mtu huyo aliwahi kupeleka malalamiko yake kwake.

Mkuu huyo alikuwa pamoja na askari kanzu waliokuwa pamoja na Beka na Shosi, ambao walisharejeshwa kituo kikuu cha Polisi kati. Baada ya kupekuapekua, hatimaye akakuta sehemu palipoandikwa malalamiko ya mzee Linus, aliyekwenda kutoa taarifa ya hofu ya maisha ya mwanaye aliyedai kutishiwa maisha na mtoto wa jirani yao!

“Yaaa, huyu hapa bwana, unaona eeh, alikuja hapa kulalamika kuwa mtoto wake anaweza kudhuriwa na kijana wa jirani yao. Nafikiri ndiyo katika mwendelezo wa vita vyao vya chinichini, ngoja nichukue namba zao niwapigie,” alisema huku akiandika pembeni namba zake.

Akaichukua simu yake na kubonyeza namba za mzee Linus, ambaye baada ya kuziangalia na kutotambua ni simu ya nani, akaamua kutopokea, alishaanza kuhisi mambo kuanza kwenda kombo.
“Mbona hupokei Chuga,” Dayani alimuuliza alipoona anaitumbulia macho simu yake bila kupokea.
“Nahisi kama siyo simu nzuri Chuga,” mzee Lius alimjibu mwenzake.
“Tucheze kamari, hebu pokea,” alimwambia.

Mzee Linus akaipokea na kuipeleka sikioni na kuita Halooo..!
Baada ya kusalimiana, upande wa pili ukajitambulisha na kumweleza kuwa ulikuwa unamhitaji kituo cha polisi kwa mahojiano mafupi, alipouliza ni kituo gani na kutajiwa, akawaambia kuwa alikuwa safarini Dodoma.

“Kama uko Dodoma pia unaweza kwenda kuripoti pale, utaulizwa mambo machache halafu utaendelea na shughuli zako mzee wangu, ni muhimu kidogo,” askari alimwambia mzee Linus kwa sauti ya upole.
Simu ikakatwa na tayari mwili mzima wa mzee huyo ulikuwa umeloa jasho. Akamsimulia alichokisikia na Dayani akatoa tabasamu lisilo rafiki.

“Kimenuka rafiki yangu, wale watoto watakuwa wamebanwa, wametapika hadi utumbo,” alisema Dayani, dhahiri kumuonyesha kwamba mambo hayakuwa mazuri.
“Tunafanyaje sasa?” Mzee Linus alimuuliza Dayani ambaye alikuwa ameinua macho yake juu darini, akionyesha kutafakari sana.

Akilini mwake, alikuwa anajiuliza kama akina Beka walikuwa wanapajua pale Morogoro alipo. Hata hivyo, hakukumbuka kama wale vijana waliwahi kufika pale, ingawa walikuwa wanajua uwepo wa sehemu ya kujificha.

Wakakubaliana wawapigie simu wake zao na kuwaeleza hali halisi ilivyo na kwamba baada ya hapo watazima simu zao na hawatawasiliana kila baada ya saa sita. Dayani alimpata mkewe na kumwelezea walipofikia, lakini simu ya mkewe mzee Linus haikupatikana, kitendo kilichomtia wasiwasi!

Je, mke wa mzee Linus amepatwa na nini?
 
SEHEMU YA 43


Wakakubaliana wawapigie simu wake zao na kuwaeleza hali halisi ilivyo na kwamba baada ya hapo watazima simu zao na hawatawasiliana kila baada ya saa sita. Dayani alimpata mkewe na kumwelezea walipofikia, lakini simu ya mkewe mzee Linus haikupatikana, kitendo kilichomtia wasiwasi!
Sasa endelea..

Mzee Linus hakujua nini kilitokea kwa mkewe, kwani tokea alipoondoka ghafla pale hotelini na kumuacha, hakuwasiliana naye tena. Akajaribu kupiga tena na tena hakupatikana. Ingekuwa zamani, angepiga kwa mke wa mzee Komba na kuzungumza naye na kujua nini kimemsibu. Pia kwa wakati ule, angeweza kuwapigia watu kadhaa kule nyumbani kwake, lakini asingeweza kwa sababu mkewe hakuwa kule!

Baada ya kufikiria sana, akaamua kumpigia kijana mmoja aliyekuwa akielewana naye sana kule kwao Nakalekwa, alimzoea kwa jina la Jumba, kutokana na umbo lake kubwa.

“Shikamoo mzee Linus, dah umepotea kabisa,” Jumba alimsalimia mara baada ya kuona namba ya simu ya mzee huyo ikiingia kwenye simu yake, hawakuwa wamewasiliana kwa muda mrefu kidogo.
“Marahaba Jumba, mambo vipi? Bwana nipo si unajua tena haya matatizo niliyopata?” alisema mzee Linus baada ya kupata salamu kutoka kwa Jumba.

“Dah kweli mzee pole sana, umepotea kabisa, haupo mjini nini?” Jumba alimuuliza.
“Yaaa, nipo Dodoma mara moja. Sasa nina tatizo kidogo, najaribu kumpigia mama simpati kwa simu yake, sijui ana matatizo gani,” alisema.“Aisee, lakini na yeye simuoni huku, hata washkaji zangu nao hawapo, leo kama wiki sasa,” alisema Jumba.

“Yaa ni kweli, unajua baada ya tukio lile tulisambaratika kidogo, ila mama yupo kwenye ile gesti ya pale Tegeta, naomba ukimbie mara moja ukamtazame maana nina shida sana, nahitaji kuongea naye,” alisema mzee Linus.

Jumba alikuwa akimuheshimu sana mzee huyo, ingawa alikuwa na kazi zake, akaamua kuahirisha, akatafuta usafiri wa bodaboda, akaenda zake kumfuata mtu ambaye alimuita mama!
**
Stone ambaye bado alikuwa na hasira na familia ya jirani yao, alijiapiza kuwa ni lazima siku moja atalipiza kisasi kwa kifo cha kaka yake Festo, aliyefariki katika ajali pamoja na Asfat, walipokuwa wakirejea nyumbani kutoka kula maisha.

Kariakoo, majira ya saa nane hivi, katikati ya watu wengi katika mtaa wa Kongo, akamuona Maria, dada yake Tonny, msichana wa tatu kuzaliwa katika familia ya mzee Linus. Mapigo ya moyo wake yakasimama kwa muda, hakuamini macho yake.

Yalipoanza tena, akaanza kumfuatilia taratibu, alitaka kujua ni wapi anaishi, kwani sasa alikuwa na nafasi kubwa ya kulipiza kisasi, alijua huyu angemuongoza walipo ndugu zake, maana tokea kuungua kwa nyumba yao, hawakuonekana tena maeneo yale na hawakuwa na mawasiliano.

Maria akiwa hajui hili wala lile, alitembea kwa kukwepa watu na hatimaye akaifikia hoteli moja ya ghorofa iliyokuwa katikati ya mtaa huo. Akaingia na kwenda kukaa katika kiti, muda uleule mhudumu alimfuata na kumhudumia alichohitaji.

Stone alipomuona ameagiza chakula, akaongeza mwendo na kwenda katika mashine ya ATM, akatoa kadi yake na kuchukua kiasi kadhaa cha fedha, hakujua baada ya pale angetumia usafiri gani, kwani kama angepanda teksi, naye angelazimika kuwa na teksi, kama ni bodaboda vilevile na yeye angekuwa vile.

Alipochukua akageuza haraka na kwenda kumchungulia Maria pale alipokuwa, akamkuta ananawa tayari kwa kutoka, akasimama eneo flani hivi kisha macho yake akayakaza katika mlango wa ile hoteli.

Maria akatoka, akaangaza macho huku na kule, Stone akajificha kwenye mojawapo ya nguo zilizokuwa zimetundikwa nje ya duka moja la nguo. Kisha msichana huyo akaanza kuondoka taratibu akiufuata mtaa wa Msimbazi!
 
SEHEMU YA 44

Maria akatoka, akaangaza macho huku na kule, Stone akajificha kwenye mojawapo ya nguo zilizokuwa zimetundikwa nje ya duka moja la nguo. Kisha msichana huyo akaanza kuondoka taratibu akiufuata mtaa wa Msimbazi.
Sasa endelea...

STONE alitoka na kuanza kumfuatilia taratibu kwa nyuma. Maria, akiwa hana hili wala lile, alitoa simu yake ya mkononi kutoka katika mkoba aliokuwa ameubeba, akabonyeza namba kadhaa na kuanza kuzungumza na shoga yake.

Akaendelea kupiga stori huku akisonga mbele, akaufikia mtaa wa Msimbazi, akaelekea kushoto, akaenda huku akisimama mara kwa mara kuangalia vitu vilivyokuwa vikiuzwa na wamachinga waliokuwa wamevipanga kando ya barabara.

Akaupita mzunguko na kwenda mbele ambako aliingia katika moja kati ya Bajaj zilizokuwa zimesimama sehemu moja hivi. Baada ya sekunde chache za kuzungumza na dereva, ikaondoka sehemu hiyo huku Stone akiharakisha mwendo naye akisogelea kituo kile.

Akiwa anaifuata Bajaj, nyingine ikawa inapita, akaisimamisha na kumuuliza dereva.
“Una mafuta ya kutosha?”
“Full tank kaka, hata Mwanza tunafika non stop,” alijibiwa na kijana aliyekuwa anaendesha. Akaingia na kumwambia;

“Unaiona ile Bajaj?” alimuonyesha Bajaj aliyokuwa amepanda Maria na kumweleza kuwa alitaka aifuate kwa nyuma hadi atakaposhuka abiria aliyepanda. “Vipi, kuna tatizo lolote kaka,” kijana huyo aliuliza huku akiongeza mafuta kuiondoa Bajaj hiyo. Stone akamwambia kuwa msichana aliyepanda ni mpenzi wake na anahisi ana mchepuko kwa hiyo anataka kumfumania. Kijana akacheka na kuendelea na hamsini zake.

Kijana aliyempakia Stone akajikuta akimtilia mashaka, hata hivyo hakumuonyesha. Bajaj aliyokuwa anaifuatilia ilikuwa inaendeshwa na rafiki yake, hivyo wakiwa wamesimama kwenye foleni alimtumia ujumbe mfupi kwenye simu yake ya mkononi.

“Oyaa, kuna jamaa nimempakia anaifuatilia Bajaj yako, una abiria gani humo?”
“Kuna demu mmoja mkali kweli mwanangu, huyo jamaa anamfuatilia huyu au mimi,” mtu wa upande wa pili naye alijibu baada ya muda mfupi. Waliendelea kuwasiliana na kila mmoja alionyesha mashaka yake.

“Hebu mpige picha afu unitumie nimuone huyo jamaa,” ujumbe uliingia katika simu ya kijana aliyekuwa na Stone, ambaye akili yake yote ilikuwa katika Bajaj iliyokuwa mbele yao. Aliamini wakati huu wakiwa wanaishi mbalimbali, ulikuwa ndiyo muafaka zaidi kumaliza kazi aliyopania kuifanya.

Kumpiga picha Stone ilikuwa ni kazi ambayo asingeweza, kwanza kwa kuwa alikuwa amekaa nyuma ya Bajaj na hivyo kugeuka na kumfotoa ingekuwa ishu kubwa, lakini kikubwa zaidi ni kwamba umbo lake lilimtisha, akamtumia jamaa yake ujumbe na kumfahamisha kuhusu suala hilo.

Wakakubaliana kusubiri ili kuona kitakachoendelea. Bajaj iliyombeba Maria ilikata kona kuifuata barabara ya Nyerere, baadaye ikapinda kushoto na kuelekea Keko. Ilipofika katika maghorofa ya NHC, Bajaj hiyo ilisimama na Maria akateremka.

“Paki pembeni babu, itakuwa bei gani hadi hapa” Stone alimwambia dereva wake, ambaye aliisogeza pembeni na kusimama. Akalipa kiasi cha fedha alizotakiwa na akaanza kuondoka, kijana huyo alitumia muda huo kumpiga picha bila mwenyewe kujua.

Maria akiwa hana hili wala lile, alivuka upande wa pili wa barabara, akaingia katika uchochoro mmoja uliokuwa na watu wengi, akatokezea upande wa pili mtaani. Hakumuona Stone aliyekuwa nyuma yake, alimfuatilia hadi alipoingia katika nyumba moja nzuri.

Stone akaipita nyumba hiyo na kwenda mbele kidogo, katika duka moja, akasimama nje na kuagiza soda. Hakutaka kuamini mara moja kama hapo ndipo alikuwa anaishi. Alikaa saa nzima bila kumuona Maria wala ndugu yake yeyote akitoka wala kuingia.

**
Jumba alifika katika nyumba ya kulala wageni aliyoelekezwa na Mzee Linus, akiwa mapokezi alimkuta mhudumu ambaye alipomuuliza kuhusu mgeni wake, alimwelekeza chumba alichokuwa amefikia.
Mama yake Asfat alishangaa sana kumuona Jumba nje ya mlango baada ya kumgongea. Walisalimiana na ndipo alipomueleza chanzo cha yeye kufika pale alipokuwa. Ndipo mama huyo aliposhtuka na kubaini kwamba simu yake haikuwa hewani tokea alipoizima muda mrefu uliopita.

“Jamani pole sana, simu niliizima muda mrefu, sikutaka usumbufu, basi asante ntampigia baba nimsikie,” alisema na Jumba akatikisa kichwa huku akiondoka sehemu hiyo.

Je, nini kitaendelea?
 
SEHEMU YA 45


“Jamani pole sana, simu niliizima muda mrefu, sikutaka usumbufu, basi asante ntampigia baba nimsikie,” alisema na Jumba akatikisa kichwa huku akiondoka sehemu hiyo.
Sasa endelea...

Jumba alipotoka, mke wa mzee Linus alibonyeza namba za mume wake na haraka sana ikapokelewa. Mzee Linus hakuamini aliposikia sauti ya mke wake, alitambua kwa vyovyote angekuwa mikononi mwa dola. Swali la kwanza alilomuuliza ni kuhusu sehemu aliyokuwepo. Alipojibiwa kuwa alikuwa bado hotelini kwake, alipomua na kumwelezea mambo yote yalivyokwenda hadi pale walipo.

“Kwa hiyo sasa nifanye nini?” mama alimuuliza mumewe.
“Sina uhakika, lakini jaribu kuzima simu, uwe unawasha kila baada ya saa tatu au nne na unipigie nikupe maendeleo, sawa?” mzee Linus alimweleza mkewe ambaye alikubali.

Alipokata simu tu, namba asiyoijua ikaingia katika simu ya mama, akajiuliza maswali mengi kabla ya kupokea. Iliita hadi ikakata. Ilipokata akampigia mumewe kumweleza kuhusu simu hiyo, akamuuliza kama aipokee au la maana aliitilia mashaka. Mumewe akamshauri kupokea lakini kama itakuwa ni ya Polisi, basi adanganye kuwa yupo nje ya Dar.

Namba ileile ikaingia tena, akaipeleka simu sikioni huku akitetemeka. Sauti ya kike ya upande wa pili ilimpa unafuu, akarejesha ujasiri wake na kutulia. Baada ya kusalimiana, aliyepiga alijitambulisha kama mwalimu wa shule anayosoma mwanaye Tonny, kwani alikuwa na siku tano sasa hakuwa amekwenda na hawana taarifa zake.

“Jamani tulipatwa na matatizo, tukajikuta tumechanganyikiwa, nyumba yetu iliungua moto na kuteketea yote, hivyo watoto wote wanaishi kwa ndugu zao ambao wapo mbali na nyumbani,” alisema mama Tonny.

“Sasa kuna fomu zinatakiwa kujazwa na mzazi pia kuchukua ripoti yake ya mwisho wa mwaka, tutafanyaje mama?” Mwalimu alimuuliza.Wakakubaliana aende akachukue, akawaahidi kwenda kesho yake saa nne asubuhi!

Aliamka kiasi cha saa mbili asubuhi, akajinyoshanyosha mwili wake halafu akaingia bafuni kuoga, kisha akavaa nguo zake na kutoka nje, moja kwa moja kwenye mgahawa uliokuwa ng’ambo ya pili ya barabara, akaagiza chai na vitafunwa, alipomaliza kunywa, akachukua bajaj kuelekea shuleni kwa mtoto wake, Mother Of Mercy, Madale.

Alikaribishwa ofisini kwa mwalimu mkuu, ambako baada ya kujieleza, aliulizwa pia kuhusu sababu za mwanaye kutoonekana shule, akaelezea ilivyokuwa. Akapewa pole nyingi, kisha akakabidhiwa ripoti ya mtoto wake ya mwisho wa mwaka.

Aliwashukuru walimu, akajiinua kitini na kutoka nje ambako aliangaza macho na kuliona gari moja dogo jeupe limeegeshwa katika njia ya kutokea nje ya shule, gari hilo halikuwepo wakati akiingia. Hakujali, akaanza kutembea taratibu hadi alipolifikia, mlango wa gari ukafunguliwa na msichana wa umri wa miaka kama 28 hivi akatoka na kumsimamisha.

“Mama shikamoo, samahani..!”
“Marahaba, bila samahani mwanangu, unasemaje,” alimjibu huku akiangalia ndani ya gari, ambako kulikuwa pia na watu wawili, dereva na msichana mwingine aliyekuwa amekaa siti ya nyuma.

“Mimi ni askari polisi kutoka kituo cha Wazo, kuanzia sasa upo chini ya ulinzi na tunaomba tuongozane kituoni kwa mahojiano zaidi,” alisema msichana huyo huku akimtolea kitambulisho, kitendo kilichomfanya mama Tonny kupoteza mawasiliano kichwani mwake kwa sekunde kadhaa!

Akili yake ilipokaa sawa, akajaribu kuuliza sababu za yeye kutakiwa kituoni, askari akamshauri kuwa mtulivu kwani suala hilo angeweza kulifahamu mara tu baada ya kufika huko. Akakubali kwa shingo upande kuingia ndani ya gari. Wale watu wengine waliokuwa garini, ambao nao walikuwa bado vijana, walimsalimia kwa heshima na safari ya kuelekea kituoni ikaanza.
 
SEHEMU YA 46

Akili yake ilipokaa sawa, akajaribu kuuliza sababu za yeye kutakiwa kituoni, askari akamshauri kuwa mtulivu kwani suala hilo angeweza kulifahamu mara tu baada ya kufika huko. Akakubali kwa shingo upande kuingia ndani ya gari. Wale watu wengine waliokuwa garini, ambao nao walikuwa bado vijana, walimsalimia kwa heshima na safari ya kuelekea kituoni ikaanza.
Sasa endelea...

STONE aliondoka katika duka lile alilosimama na kunywa soda kwa muda mrefu, akasogea katika pub moja hivi iliyokuwa kwa mbali kidogo na nyumba aliyokuwa ameingia Maria, hata hivyo angeweza kumuona na kumtambua mtu yeyote ambaye angetoka au kuingia.

Pale alipokaa, akaagiza tena soda yake baridi, akaendelea kunywa taratibu huku macho yake yakiwa yameganda pale kwenye nyumba ile. Kwa muda aliokuwa ameshautumia kukaa pale, haukuweza kumshawishi kama ndipo wanapokaa wale majirani zao, kwa sababu hakumuona tena mtu mwingine akitoka wala kuingia anayemfahamu.

Muda wa saa kumi na moja na nusu hivi, macho ya Stone yaliona kitu alichokitaka, Maria, akiwa na nguo zilezile, alitoka akiwa ameongozana na jamaa mmoja hivi, ambaye kwa kuwatazama, walionekana kama wapenzi.

Ndiyo, Jimmy, kijana mmoja mkakamavu alikuwa ni mpenzi wa Maria kwa muda mrefu na pale ndipo alipokuwa amepanga. Kwa muda wote ambao wamekuwa na matatizo, msichana huyo alipata mwanya wa kuwa anakwenda pale mara kwa mara, lakini hakuwa akilala.

Stone akahisi hivyo pia na kwa kuwa walikuwa wanaondoka, akadhamiria kuwafuata tena nyuma, kuona ni wapi ambako Maria angemalizia safari yake. Akamaliza haraka soda yake, akainuka na kuwafuata wapenzi wale ambao baada ya kuingia katika uchochoro na kutokea upande wa pili wa barabara, wakaifuata Bajaj na kujipakiza.

Stone naye akaifuata Bajaj iliyokuwepo eneo lile, akaingia na kumwambia dereva aifuate ile iliyokuwa mbele yake.“Kwani vipi Bro na ile Bajaj?” dereva alimuuliza.

“Kuna jamaa kaingia na demu wangu, nataka kuwafuatilia nijue wanakoenda, sina shida na mwanaume, nataka ushahidi wa kumuacha demu,” Stone aliongopa tena, uongo ambao dereva wa Bajaj aliutilia shaka. Kwa kuwa aliyekuwa akiendesha ni watu wanaofahamiana, akaamua kumtumia ujumbe mfupi wa maneno na kumweleza kuhusu suala hilo.

Dereva wa ile Bajaj baada ya kusoma ujumbe ule, hakutaka kuremba, mara moja akawaambia abiria wake kuhusu kufuatiliwa na mtu nyuma yao.

Maria alishtuka sana kusikia vile, kwani kwa zaidi ya miaka mitatu aliyokuwa na Jimmy hakuwahi kutoka na mwanaume mwingine. Jimmy kwa upande wake, alikuwa mtulivu, akamwambia dereva wa Bajaj aendelee kuwasiliana na mwenzake ili kujua nyendo zake.

Waliuliza kuhusu umbo lake, muonekano wake na sauti yake kama angeweza. Ujumbe mmoja ulioingia ulianza kutoa mwanga kwa Maria na Jimmy, ambao dereva aliwasomea … “Jamaa kavaa tisheti kifuani imeandikwa Join Them.”

“Kuna sehemu nimeshawahi kuiona hii flana, wapi, wapi wapi vile jamani, aaaah kuna mtu namjua,” alilalama Maria aliyekuwa akijitahidi kukumbuka, lakini kabla hajamaliza, Jimmy akaja na wazo.

“Sikia dereva, wasiliana na mwendesha Bajaj mwingine mwambie aje resi amfuate mshkaji wako, akampige picha abiria wake alafu akurushie tumuone huyo jamaa, si inawezekana,” alisema na wote wakakubaliana naye.

Sasa walikuwa wanaingia eneo la Kigogo Sambusa, safari yao ilikuwa ni Kawe, ambako Maria ndipo alipokuwa anaishi.
**
Gari liliingia katika kituo cha Polisi Wazo kwa mwendo wa taratibu, likaenda na kuegeshwa sehemu yake, kisha mama Tonny akateremka na kuwafuata askari waliomsindikiza ndani ya kituo hicho. Akaongozwa moja kwa moja hadi katika chumba kimoja, ambacho hakikuwa na mtu. Akatakiwa kusubiri kwa muda.

Wale askari wakatoka na kumuacha peke yake. Moyoni mwake, alijawa na wasiwasi usio kifani, katika maisha yake yote, hii ilikuwa ni mara yake ya kwanza kukamatwa.Baada ya muda mchache askari aliyemkamata, aliingia akiwa ameandamana na mwanamke mwingine aliyekuwa amevalia kiraia, ambaye baada ya kukaa alijitambulisha kuwa ni askari, mkononi mwake akiwa na karatasi kadhaa.

“Sikia mama, tuna taarifa zote kuhusu kilichofanyika katika nyumba yenu, tunajua wewe pia unajua kilichotokea. Mumeo yuko wapi?” alimuuliza kwa sauti ya upole kabisa.

“Kwa kweli mimi sijui alipo, mara ya mwisho alinipigia simu akisema yupo Dodoma, lakini akaniambia anaelekea Mwanza,” alijibu.“Sasa sikia..” yule mwanamama askari akamwambia mama Tonny!
 
SEHEMU YA 47

“Sikia mama, tuna taarifa zote kuhusu kilichofanyika katika nyumba yenu, tunajua wewe pia unajua kilichotokea. Mumeo yuko wapi?” alimuuliza kwa sauti ya upole kabisa.
“Kwa kweli mimi sijui alipo, mara ya mwisho alinipigia simu akisema yupo Dodoma, lakini akaniambia anaelekea Mwanza,” alijibu.
“Sasa sikia..” yule mwanamama askari akamwambia mama Tonny!
Sasa endelea...

Mama Tonny alibakia kimya akimuangalia yule askari ambaye alikuwa akizichezea karatasi zilizokuwa mikononi mwake. Akatumia kiasi cha dakika 15 kumuelekeza jinsi ya kufanya kwa ufasaha kabisa bila kukosea, vinginevyo angekosa bahati ya kuondolewa katika shitaka kubwa linalomkabili mumewe pamoja na watu wengine.

“Nadhani umenielewa mwanamke mwenzangu?” askari alimuuliza mkewe mzee Linus, ambaye alitingisha kichwa kuonyesha kuelewa. “Haya sasa, piga,” askari mwanamama alimwambia.
Mama Tonny alibonyeza namba za mumewe, baada ya sekunde chache, mzee Linus aliipokea simu hiyo, kama kawaida akiwa na hofu flani moyoni mwake.

Mkewe alimsalimia na baadaye alimuuliza kama yupo sehemu ambayo anaweza kuongea bila wasiwasi. Akiwa sebuleni kwa Dayani, kule Morogoro, alimtoa wasiwasi mkewe na kumwambia anaweza kuendelea, lakini huku akimkonyeza rafiki yake Dayani.

“Nimepigiwa simu na Polisi, sijui wamepata wapi namba yangu, wanataka niende kituoni eti kuna jambo wanataka kuzungumza na mimi, nimewakubalia, lakini kabla sijaenda nikataka kwanza ushauri wako, niende nisiende?” mkewe aliongea huku askari aliyekuwa naye karibu, akirekodi kwa kuwa simu ilikuwa imewekwa ‘loud speaker’.

“Hebu ngoja kwanza nitakupigia baada ya dakika mbili, ngoja nishauriane na Dayani,” Mzee Linus alisema simuni na kukata. “Safi sana, ninakuhakikishia usalama wako, ni kufuata tu vile tunataka utusaidie,” mwanamama askari alimwambia mkewe mzee Linus.

Dakika mbili baadaye, mumewe alikuwa hewani akimtafuta kwenye simu yake.
“Sikiliza, hawa hawatakiwi kabisa kutupata muda huu, ngoja kwanza tupotee ili angalau tujipange tujue jinsi ya kujitetea. Kwani sasa hivi uko wapi,” alimwambia mkewe.

“Nimeamua kuondoka ile hotel, nimehamia nyingine kule chini kidogo,” mkewe alimjibu.
“Sasa sikiliza, sikiliza vizuri, nenda kachukue mizigo yako, halafu uende pale Kimara, kuna gereji moja bubu ipo mbele tu ya Resort Inn, muulizie mtu anaitwa Bob, jitambulishe, utapewa usafiri uje hapa tulipo,” alisema mumewe, akimsisitizia kufanya zoezi hilo haraka.

Baada ya kukata simu, askari alitoka chumbani, akaingia chumba kingine na baada ya dakika ishirini, kila kitu kikawa sawa. Gari moja nyekundu, yenye namba za kiraia ilimchukua mama Tonny na askari wengine wawili waliovalia kiraia.

Dereva aliendesha kasi hadi walipofika Kimara, katika gereji bubu iliyokuwa mbele ya Resort Inn. Mama huyo akashuka garini huku askari wa kike wakimtazama, alikwenda hadi kwa kijana mmoja na kuzungumza naye maneno machache. Kisha, mtu mmoja mwenye mwili mkakamavu akajitokeza na kwenda kuzungumza naye. Alipoanza kujitambulisha tu, akamkatiza.

“Ingia kwenye ile pale gari, kwani una mizigo zaidi ya huo mkoba? Hawa rafiki zako unaweza kuwaaga tu,” Bob akamwambia akimuonyesha gari moja nyeupe, lakini yenye vioo vya giza, aina ya Prado VX!
Mama Tonny alirejea kwenye gari alilokuja nalo, akawakonyeza askari na kuwaaga kwa kuwapa mikono, akalifuata Prado na kuingia. Gari la askari likageuza na kurejea zake mjini, wakati alilopanda mkewe mzee Linus, likaingia upande wa Morogoro, safari ikaanza!

Katika gari hilo, kulikuwa na watu wawili tu, yeye na dereva ambaye pia alikuwa mwanamke. Hakumsemesha jambo lolote hadi walipopita mizani Kibaha, tena baada ya kuwa ametoka kuwasiliana kwa simu.

“Mama nimependa tabia yako, kwa kawaida sisi kama tuko na mtu tusiyemfahamu, hatupendi awe anatumia simu yake, lakini wewe tokea tumepanda sijakuona uhangaike na simu yako,” sauti nyororo kutoka kwa mwanamke dereva ilipenya masikioni mwa dereva na kabla mkewe Linus hajajibu, simu yake ikaita.

“Ndiyo kama nimeiambia iite sasa, lol,” alisema na kusababisha wote kuangua kicheko, ilikuwa inatoka kwa mumewe.
“Mmefika wapi,” aliuliza mzee Linus, swali ambalo alijibiwa kuwa ndiyo kwanza wanatoka Kibaha, kabla ya kukata simu.
 
Back
Top Bottom