Bwana Henry akafadhaika akasema, ‘Nafikiri amejeruhiwa.’
Na hapo aliposema hayo, Yule tuliyefikiri kuwa ni maiti Mkukuana akaruka akampiga Bwana Good kichwani akamwangusha chini, akaanza kumchoma mikuki, Tulimkimbilia Bwana Good, na tulipomkaribia tulimwona Yule Mkukuana anampiga na kumpiga tena kwa mkuki, na kila alipopiga mikono na miguu ya Bwana Good ikaruka juu.
Yule Mkukuana alipotuona tunakuja, akazidi kumpiga kwa nguvu, akapiga kelele, ‘Haya, wewe mchawi nimekuua.’ Akakimbia. Bwana Good akalala kimya wala hakuweza kujimudu hata kidogo, tukafikiri kuwa rafiki yetu tayari amekufa.
Tulimkaribia kwa huzuni, tukashangaa tulipoona anacheka ingawa amegeuka rangi kwa maumivu, akacheka na miwani bado ipo katika jicho lake, akasema, ‘Hizi nguo za chuma ni nzuri sana, naona kuwa Yule Mkukuana amestaajabu.’
Na mara akazimia. Tulipomtazama tuliona kuwa amejeruhiwa vibaya mguu mmoja kwa pigo la kisu kikubwa, lakini nguo zile za chuma zimemlinda asiumizwe zaidi na Yule Mkukuana. Ikawa ameokoka kwa rehema ya Mungu.
Hatukuweza kumtibu wakati ule basi tukamweka juu ya ngao akachukuliwa pamoja nasi. Tulipofika penye lango la Loo tukaona kikosi cha askari wa upande wetu wamesimama kulinda zamu kwa amri za Ignosi.
Vikosi vingine viliwekwa penye milango mingine ya mji.
Yule mkubwa wa kikosi alipomwona Ignosi, alimwamkia kwa amkio la kifalme, akamwambia kuwa askari wa Twala wamejificha katika mji, na Twala mwenyewe vile vile yumo mjini, lakini alifikiri kuwa watu watajitoa, maana wame fadhaika kabisa.
Basi aliposikia hayo Ignosi alituma tarishi kwa kila mlango wa mji kuwaamuru walio ndani wafungue milango, naye aliahidi kuwa wote watakaojitoa na kutoa silaha zao watapata msamaha.
Basi habari hii ikapokewa, na mara tulisikia makelele na milango ikafunguliwa. Tukaingia katika mji, lakini tuliangalia sana tusije tukaghafilika.
Katika njia zote tulikuta askari wamesimama na vichwa kuinamia chini, na silala na ngao zao zimewekwa chini miguuni pao, na Ignosi alipokuwa akipita walimwamkia kwa amkio la kifalme.
Tukaenda mbele mpaka jumba la Twala, Tulipofika kwenye kiwanja kile tulichokwenda juzi juzi kutazama ngoma, tulikiona kipo wazi kabisa, lakini si wazi, maana pale mbele ya mlango wa jumba lake, Twala mwenyewe alikaa, pamoja na mtu mmoja tu, naye alikuwa Gagula.
Ilisikitisha kumwona vile alivyokaa, na shoka lake na ngao yake vimewekwa chini ubavuni pake, na kichwa chake kainamisha kifuani, na mtu mmoja tu amekaa kumfariji.
Na ingawa tulikumbuka ukatili wake, hatukuweza kujizuia kuto kumsikitikia.
Hapana hata askari mmoja katika maelfu ya askari wake; hapana hata mfuasi mmoja katika wale wengi walionyenyekea mbele yake, hapana hata mke mmoja aliyesalia kumfariji katika uchungu wa yaliyomfika. Masikini!
Tulipita mlango wa kiwanja tukaenda mpaka mbele ya Twala, na huku Gagula anatutukana vibaya.
Tulipokaribia, Twala akafanya kutuona, akainua kichwa chake kilichovikwa manyoya marefu, akamtazama Ignosi kwa jicho moja lake, likang’aa kama ile almasi iliyofungwa katika kipaji chake cha uso, akasema kwa sauti yenye uchungu na dharau, ‘Hujambo, Ewe mfalme, wewe uliyekula chakula changu, na sasa kwa msaada wa uchawi wa watu weupe umewashawishi askari wangu kuniasi!
Niambie, ajali yangu ni nini, Ewe mfalme?’
Ignosi akajibu kwa ukali, ‘Ajali yako ni ile ile uliyompa baba yangu, ambaye kiti chake umekikalia kwa miaka hii yote.’ Twala akasema, ‘Vema, nimekubali. Nitakuonyesha njia ya kufia, ili nawe ukumbuke wakati wako utakapowadia.
Tazama, jua linazama, ni vizuri na jua langu lizame pamoja nalo. Na sasa, ewe mfalme, mimi tayari kufa, lakini nataka haki ya mfalme wa Wakukuana, yaani nife nikipigana. Huwezi kunikatalia; ukikataa hata wale waoga waliokimbia leo, hata na wao watakwita mwoga.’
Ignosi akajibu , ‘Nimekubali. Chagua, utapigana na nani? Mimi mwenyewe siwezi kupigana nawe, maana mfalme hupigana katika vita tu.’
Jicho la Twala likatutazama, na kwa dakika moja nilimwona ananitaza mimi tu, na baadaye akasema, ‘Ndovu, wasemaje, tumalize yale tuliyoanza leo, au nikwite kwa jina la mwoga?’
Ignosi akasema kwa haraka, ‘La, huna ruhusa kupigana na Ndovu.’ Twala akajibu, ‘Vema, kama anaogopa, sipigani naye.’ Basi Bwana Henry alifahamu maneno hayo, na uso ulimwiiva akasema, ‘Nitapigana naye, naye ataona kuwa siogopi.’
Nikamsihi, ‘Nakuomba usipigane naye, usijitie katika hatari ya bure, maana huyu anajua lazima afe. Kila mtu aliyekuona leo anajua kuwa wewe ni shujaa, si muoga.’
Akajibu, ‘Lazima nipigane naye. Hapana mtu atakayeniita muoga na kuishi. Sasa mimi ni tayari.’ Akashika shoka lake akasimama mbele. Nilipoona kuwa amekwisha azimia, wasiwasi uliniingia, lakini sikuweza kumzuia asipigane.
Ignosi akaweka mkono juu ya bega lake kwa upole, akamwambia, ‘Rafiki, ndugu yangu mweupe, usipigane naye. Vita uliyopigana leo inatosha kabisa, na ukidhurika, moyo wangu utakuwa mzito sana.’
Bwana Henry akasema, ‘Ignosi, lazima nitapigana naye .’ Akaijibu, ‘vema, Ndovu, wewe ni shujaa kweli kweli. Tazama, Twala, Ndovu yu tayari kupigana nawe.’
Twala akacheka kicheko kikubwa, akasimama akamtazama Bwana Henry. Kwa muda kidogo wakasimama hivi na mwangaza wa jua lililokuwa likishuka ukawaangaza ukaonyesha maungo yao namna yalivyokuwa mazuri.
Kisha wakaangaza kuzungukiana, na mashoka yao juu.
Mara Bwana Henry akaruka mbele akajaribu kumpiga Twala kwa nguvu zake zote, lakini Twala aliepa.
Nguvu za pigo zilikuwa nyingi hata alitaka kuanguka, basi adui yake akawa tayari akapungu shoka lake kichwani, akapiga kwa nguvu nyingi kabisa. Moyo wangu ulisita, nikafikiri kuwa yamekwisha. Lakini sivyo;
Bwana Henry akaweka mkono wake juu kwa upesi akalikinga shoka. Mara Bwana Henry akapata nafasi kupiga mara ya pili, lakini Twala akakinga kwa ngao yake.
Basi ikaendelea hivyo, pigo kwa pigo, na kila pigo lilikingwa. Sasa watu wote waliokuwako wakaanza kusongana katika mshangao wao, wakapiga kelele au kuguna kwa kila pigo.
Hapo Bwana Good aliye kuwa amezimia, akapata fahamu tena, na mara akasimama akaanza kurukaruka huku akimtia moyo Bwana Henry.
Basi hivyo hivyo wakapigana, hata kwa bahati mbaya Twala akapata nafasi ya kulipiga shoga la Bwana Henry likamtoka mkononi, likaanguka chini.
Sasa wote waliugua kwa mashaka na huzuni, na Twala akainua shoka lake juu akamrukia huku akipiga kelele. Nikafumba macho.
Nilipofumbua macho tena, niliona ngao ya Bwana Henry imelala chini, naye amemkumbatia Twala kiunoni.
Huku na huku waliminyana, huku wamekamatana kwa nguvu zao zote. Twala akajitahidi sana, akamwinua Bwana Henry juu, wakaanguka chini wote pamoja, na Twala alijaribu kumpiga shoka la kichwa, na Bwana Henry akajaribu kumpiga Twala kisu.
Ikawa shindano kuu kabisa, na hapo Bwana Good alipiga ukulele, ‘Shika shoka lake!’ Na labda Bwana Henry alisikia, maana alitupa kisu chake akashika shoka la Twala wakaanza kupinduana chini wakipigana kama paka wa mwitu wanavyopigana, huku wakitweta kwa nguvu.
Mara tuliona kuwa ngozi iliyofungiwa shoka kwenye mkono wa Twala imekatika, na Bwana Henry ametengwa naye na amepata shoka hilo. Mara akaruka juu, na damu inamtoka usoni pale alipojeruhiwa na Twala, na mara ile Twala naye akaruka juu.
Basi sasa ikawa kupigana tena, mpaka Bwana Henry akajitahidi akapiga shoka kwa nguvu zote, akampiga la shingo.
Hapo watu waliokuwapo waliguna kwa pamoja maana kichwa cha Twala kikaanguka kikabiringika mpaka kikafika kwenye mguu wa Ignosi kikasita.
Kwa dakika hivi kiwiliwili chake kilisimama wima, kisha kikaanguka kwa kishindo, na pale pale Bwana Henry alizimia, naye akaanguka juu ya maiti ya Twala.
Basi tulimwinua tukammwagia maji akafumbua macho yake. Hakufa, nami, jua lilipokuwa likishuka, nikasimama mbele, nikafungua ile almasi iliyofungwa juu ya kipaji cha uso wa Twala, nikampa Ignosi, nikasema, ‘Itwae Ignosi, mfalme wa haki wa Wakukuana, mfalme kwa ‘kuzaliwa, na mfalme kwa kushinda.’
Ignosi akaifunga juu ya kipaji chake, akaja mbele akaweka mguu wake juu ya kiwiliwili cha Twala, akaanza kuimba wimbo wa ushindi, hivi:
Sasa uasi wetu umemezwa katika ushindi, na vitendo vyetu viovu vimegeuka kuwa haki kwa nguvu. Asubuhi wadhalimu waliamka wakajitikisa; walijifungia manyoya wakajiweka tayari kwa vita. Waliamka wakashika mikuki yao: askari waliwaita wakubwa wao, ‘Njooni mtuongoze.’
Na wakubwa walimwita mfalme, ‘Utuongoze vitani.’ Wakaondoka na kiburi chao, watu ishirini elfu na tena ishirini elfu.
Manyoya yao yalifunika nchi kama manyoya ya ndege yanavyofunika tundu lake; walitikisa mikuki yao kwa vigelegele.
Ndiyo, walirusha mikuki yao katika mwangaza wa jua; wakatamani vita wakafurahi.
Wakanishambulia; wenye nguvu wao eakanijia mbio waniue, wakipiga kelele,’ Hal Ha! Ni kama aliyekwisha kufa.’ Ndipo nilipovuma juu yao, na pumzi zangu zikawa kama upepo wa tufani, na tazama! Wakatawanyika .
Umeme wangu uliwachoma; nililamba nguvu zao kwa umeme wa mikuki yangu; niliwapeperusha kwa ngurumo ya kulia kwangu.
Walivunjika, walitawanyika, walitoweka kama ukungu wa asubuhi.
Sasa wamekuwa chakula cha kunguru na fisi, na mahali pa vita pamenona kwa damu yao.
Wa wapi wale walioamka asubuhi na nguvu zao?
Wa wapi wale wenye kiburi waliotikisa manyoya yao wakasema ‘Ni kama aliyekwisha kufa:’
Wameinamisha vichwa lakini si katika kusinzia; wamejinyosha, lakini si katika usingizi.
Wamesahauliwa; wametoweka gizani nao hawatarudi; ndiyo, watu wengine watawachukua wake zao, na watoto wao hawatawakumbuka tena.
Na mimi, mimi? Mimi ni mfalme. Kama tai nimeona tundu langu.
Tazama! Nilitembea mbali wakati wa usiku, lakini nimewarudika makinda yangu wakati wa mapambazuko.
Ingieni nyinyi kwenye kivuli cha mabawa yangu, ee nyinyi watu, nami nitawafariji, nanyi hamtafadhaika tena.
Huu ndiyo wakati wa neema, huu ndio wakati wa kuteka. Ng’ombe walio bondeni ni wangu, wanawali pia walio mjumbani ni wangu.
Taabu imepita, neema imefika. Sasa uovo utafunikwa uso wake, na Huruma na Furaha watakaa katika nchi.
Furahini, furahini, watu wangu!
Dunia yote ifurahi kwa kuwa jeuri imekanyagwa, na mimi ndiye mfalme.
Ignosi akanyamaza, na kutoka katika giza lililokuwa limeingia, jibu likaja kama ngurumo kutoka milimani, ‘Wewe ndiye mfalme!’
Hivyo yale niliyombashiria Yule tarishi yalitimia, na katika muda wa saa arubaini na nane, kiwiliwili cha Twala kimelala kikavu mbele ya mlango wa jumba lake.