[SIZE=+2]Pambano Kati ya Nyerere, Tewa na Bibi Titi, 1968[/SIZE] HII ni sehemu ya saba ya mfululizo wa makala ambazo ni sehemu ya muswada wa kitabu "Mwalimu Julius K. Nyerere, Kanisa Katoliki na Uislamu: Dola na tatizo la Udini Tanzania" kitakachotoka hivi karibuni. Kitabu hicho kimeandikwa na mwandishi maarufu wa masuala ya historia hasa ya Tanganyika BWANA MOHAMMED SAID.
Waislamu iweze kufanya kazi yake vyema na bila upendeleo, ilikuwa lazima ile tume ya Waislamu iiombe serikali izuie propaganda iliyokuwa ikiendeshwa na wale waliokuwa wamejitenga na EAMWS, wakitumia jukwaa la radio ya serikali na magazeti ya TANU. Tume ya Waislamu ilikutana na Waziri wa Habari na Utangazaji, Hasnu Makame, ofisini kwake tarehe 20 Novemba, 1968, kujadili tatizo lile. [SUP]50[/SUP] Hii haukusaidia kitu. Propaganda dhidi ya uongozi wa EAMWS iliendelea kwa nguvu zote. Mashambulizi kutoka pande tatu yaliyopangwa vyema yalikuwa kazini. Benjamini Mkapa akitumia gazeti la Nationalist ataandika habari yoyote ya Adam Nasibu, Martin Kiama akitumia Radio Tanzania atatumia habari ile kama habari muhimu katika radio na habari hiyo itatangazwa kutwa nzima huku ofisi ya rais ikiwa kimya kwa fitna ile. Lile kundi la waliojitenga na umma wa Waislam Adam Nasibu akiwa kama msemaji wao mkuu wakawa wakati mwingine kwa mastaajabu makubwa wakawa wanakiuka hata misingi ya akida ya Tanzania, wakitoa madai ya ubaguzi a rangi, wakikazania lazima EAMWS ivunjwe. Adam Nasibu alinukuliwa na The Nationalist akisema kuwa:
Waislam lazima wafahamishwe kwa nini East African Muslim Welfare Society iwe na katiba ambayo inaendana na mwelekeo wa nchi. Hatujui nafasi ya Aga Khan katika nchi yetu na ndiyo maana tunamkataa. [SUP]51[/SUP]
Lakini cha kushangaza zaidi ilikuwa ule ukimya wa serikali kuhusu matakwa ya kundi la Adam Nasibu lililokuwa likidai kuwa Waislam wachanganye dini na siasa katika suala hili, wakati ilikuwa ikijulikana wazi kuwa kufanya hivyo ni mwiko mkubwa katika siasa za Tanzania. Haya yote mbali, lile la kushangaza hasa na kitu ambacho kilikuwa kigeni katika Tanzania ilikuwa yale madai ya kuingiza ubaguzi wa rangi katika siasa za Tanzania. Ilikuwa inastaajabisha kuona magazeti ya TANU yaliyokuwa na sifa ya kuheshima haki za binadamu yakichapisha na kuzipa uzito wa hali ya juu habari za kundi dogo la Waislam waliokuwa wanawalaumu Waislam wenzao wa Kiismailia kwa kutozaliwa weusi. Miaka kumi iliyopita watu wa Tanganyika, Waislam wenyewe waliokuwa ndiyo walioanzisha na kuijenga TANU, walipambana vikali dhidi ya siasa za kibaguzi za Zuberi Mtemvu na chama chake cha African National Congress. Mtemvu alishindwa na matokeo yake ikawa Tanganyika kuwa na serikali ya watu wote isiyobagua rangi na ikitawala raia wa rangi zote kwa misingi ya haki. Kwa ajili hii nchi ikawa haina msuguano kwa ajili ya ubaguzi wa rangi. Haya matokeo mapya yalikuwa hayaendani na misingi ya TANU.
Ilipofikia hali hii, rais wa EAMWS, Tewa Said Tewa na makamo wake Bibi Titi Mohamed, waliamua kulipeleka suala hili kwa Julius Nyerere, Rais wa Tanzania na mwenyekiti wa TANU, chama tawala. Watu hawa walikuwa wakichekeana jino pembe. Lakini ili tuelewa chanzo cha uadui huu inatulazimu turudi nyuma hadi mwaka wa 1963, katika siku za mwanzo za uhuru, katika mkutano wa Halmashauri Kuu ya TANU [SUP]52[/SUP] uliofanyika Ukumbi wa Karimjee.
Kama ilivyokwishaelezwa hapo mwanzoni kuwa mwaka 1963 ulikuwa mwaka wa mambo mazito. Ilikuwa ndiyo mwaka ambao Kanisa Katoliki liliteua wagombea wake wapambane na wagombea wa TANU waliokuwa Waislam katika uchaguzi wa serikali za mitaa kule Kigoma na Bukoba. Ulikuwa ndiyo mwaka ambao Rais wa TANU, Nyerere alipombana na EAMWS kupitia Bilali Rehani Waikela. Mwaka wa 1963 ndiyo ulikuwa mwaka ambao Halmashauri Kuu ya TANU ilivunja Baraza la Wazee wa TANU lililokuwa limetawaliwa na Waislam kwa madai kuwa baraza hilo lilikuwa 'likichanganya dini na siasa'. Mwaka 1963 ulikuwa mwaka muhimu kwa Halmashauri Kuu ya TANU kwa sababu ilikuwa mwaka ambao ilifanya maamuzi nyeti ya kidini. Mwaka ule Bibi Titi na Nyerere walishambuliana kwa maneno ndani ya Halmashauri Kuu yA TANU kuhusu jambo jingine tena la dini lililokuwa likihusu EAMWS.
Wanakamati wawili wa Halmashauri Kuu ya TANU, Selemani Kitundu na Rajab Diwani, waliiomba Halmashauri Kuu ya TANU imjadili Aga Khan na nafasi yake kama patroni wa EAMWS. Kitundu na Diwani walidai kuwa wana habari Aga Khan anataka kuitawala Tanganyika kupitia Waislam na EAMWS. Kwa ajili hii basi wakapendekeza EAMWS ifungiwe. Nyerere aliwaunga mkono Selemani Kitundu na Rajab Diwani. Bibi Titi akasimama kishujaa dhidi ya Diwani, Kitundu na Nyerere, akasema hakuna kati yao aliyekuwa na haki ya kuifungia jumuiya yoyote ya Waislam. Kama walikuwepo watu ndani ya EAMWS ambao walikuwa wanakwenda kinyume na sheria basi watu hao wapelekwe mahakamani na sheria ichukue mkondo wake. Bibi Titi akaendelea na kusema kuwa EAMWS imekuwepo kabla ya TANU na siku zote imekuwa ikitoa huduma kwa Uislam. Inasemekana hasira zilipanda na kukawa na kutoleana maneno kati ya Bibi Titi na Nyerere. Bibi Titi akamwambia Nyerere yeye hamuogopi yeyote ila Allah.
Tuhuma zile dhidi ya Aga Khan na EAMWS hazikuweza kuthibitishwa na Halmashauri Kuu ya TANU ikaliacha jambo lile kwa wakati ule. Lakini Nyerere alikuwa amefedheheka. Kuanzia hapo akajenga chuki dhidi ya Bibi Titi na kumweka Rajab Diwani na Selemani Kitundu karibu yake. Katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 1965 Bibi Titi na Tewa wakapoteza viti vyao kwa watu ambao walikuwa hata hawafahamiki * A.M. Mtanga na Ramadhani Dollah. Iliaminika kuwa Nyerere alikuwa anahusika na kuanguka kwa Bibi Titi na Tewa. Kuanzia hapo mambo yakawa dhahiri. Nyerere alikuwa amewatangazia vita wote wawili, Bibi Titi na Tewa. Nyerere alikuwa sasa ana imani kuwa wale maadui zake wawili walikuwa wamekwisha kisiasa. Lakini kilichokuwa kikimuudhi Nyerere zaidi ilikuwa taarifa ambazo alikuwa akizipata kuwa Tewa alikuwa akipewa mapokezi makubwa sana na Waislam katika ziara zake huko mikoani kama rais wa EAMWS. [SUP]53[/SUP]
Sasa mwaka wa 1968, Bibi Titi na Tewa walipokwenda kumuona Nyerere kuhusu jambo lililokuwa linawahusu Waislam, Nyerere alikuwa amejitayarisha vyema. Kiwanuka ameueleza mkutano huu vizuri sana:
Viongozi hawa wawili wa Waislam walimueleza Mwalimu masikitiko yao jinsi radio ya serikali na magazeti ya TANU yalivyokuwa yakiandika habari kuhusu matatizo yale ya Waislam. Walidai kuwa TANU ilikuwa ikichanganya dini na siasa. Waliokuwa wakimtahadharisha kuhusu jambo hilo hawakuwa wengine ila marafiki zake wa zamani na wa kutumainiwa, Tewa na Bibi Titi. Marafiki wa kutumainiwa kwa sababu ilikuwa Titi aliyemuunga mkono Nyerere katika siku za mwanzo za TANU, pale Suleiman Takadir * mmoja wa wazee wa TANU * aliposema kuwa TANU ilikuwa na Ukristo kama Mwalimu na Rupia, rais na makamo wake walivyokuwa Wakristo. Yeye mwenyewe akiwa Muislam hasa, aliipatia TANU ushindi kwa kuthibitisha kuwa Tanzania, Tanganyika kama ilivyokuwa ikijulikana wakati ule, ilikuwa mbele, na Uislam unafuata nyuma. Leo, alikuwa anazungumzia jambo ambalo yeye mwenyewe alilishinda katika miaka ya 1950. Jibu walilopata kutoka kwa Mwalimu lilikuwa la kusisimua. Mpashaji wangu habari anasema lilikuwa jibu la mkato. 'Mmeamua kunipiga vita, jiandaeni.' [SUP]54[/SUP]
Mwalimu Nyerere alikuwa anawaambia Tewa Said Tewa na Bibi Titi Mohamed uso kwa macho wajiandae kwa kile kilichokuwa dhahiri: vita ya msalaba dhidi ya umoja wa Waislam. Sheikh Suleiman Takadir aliyaona haya na aliiomba TANU toka mwaka wa 1958 pawepo na uhakika kuwa Wakristo hawatakuja kuwafanyia uadui Waislam pale Waislam watakapokuwa sasa wanataka kugawana madaraka ya kuongoza nchi sawa na Wakristo baada ya uhuru. Tewa Said Tewa, muasisi wa TANU, waziri katika serikali ya kwanza ya uhuru, balozi katika Jamuhuri ya watu wa China na Rais wa baraza la Tanzania la EAMWS, pamoja na Bibi Titi, mwanamke aliowakusanya wanawake wote nyuma ya Mwalimu Nyerere na TANU, walikuwa wakisemwa na Nyerere kama vile watoto wadogo wa shule waliokuwa watukutu kwa sababu tu, walikuja kumfahamisha Rais kuhusu kukiukwa kwa maadili ambayo ilihitaji yeye ashughulikie mara moja na kutoa uamuzi.
Ulipofika mwezi Oktoba, 'mgogoro' ukachukua mwelekeo mpya pale Makamo wa Rais wa Tanzania, Abeid Amani Karume, alipoishambulia EAMWS kuwa ni chombo cha unyonyaji. [SUP]55[/SUP] Kutokea hapo Karume akawa anafanya mashambulizi na kutoa shutuma kwa EAMWS, wakati mwingine akijaribu kufananisha uhusiano wa EAMWS na Waislam katika mtazamo wa Ki-Marxist, akidai kuwa jumuiya ile kilikuwa 'chombo cha makabaila wakubwa na kilikuwa chini yao kikiwanyonya watu wa chini'. [SUP]56[/SUP] Mgogoro ulipozidi kukua mashambulizi yakahama sasa kutoka EAMWS na kuhamia kwenye mafunzo ya msingi katika Qur'an Tukufu. Katika mkutano wa hadhara Zanzibar, Karume alitoa changamoto kwa Muislam yeyote ajitokeze bila ya woga kupinga kauli zake mbili kuwa 'Hakuna tofauti kati ya Uislam na Ukristo', na 'Kufunga siyo lazima'.
Lakini juu ya mashambulizi dhidi ya uongozi wa Waislam kutoka serikalini, Nyerere alikuwa hana uwezo wa kumgusa Mufti Sheikh Hassan bin Amir. [SUP]57[/SUP] Sheikh Hassan bin Amir alikuwa na nguvu sana kiasi cha kwamba si Nyerere au yeyote yule kuweza kumgusa kwa wakati ule. Sheikh Hassan alikuwa kwenye siasa kabla ya vijana waliokuwa katika TANU na nafasi yake katika umma wa Kiislam na uzalendo wake ulikuwa hauna shaka. Sheikh Hassan bin Amir aliingizwa TAA kwa mara ya kwanza mwaka 1950 na Abdulwahid Sykes akiwa mwanakamati katika Kamati ndogo ya siasa ya TAA. Kwa ajili hii basi, akawa mmoja wa wale waliotia sahihi ile memorandam iliyotayarishwa na TAA kwenda kwa Gavana wa Tanganyika, Edward Twining kuhusu mabadiliko ya katiba ya Tanganyika.
Courtesy: Mohamed Said