JF Photo Library: Mada maalum ya Picha za Zamani

BANZA STONE 'ALIVYOMCHAMBA' MUUMIN NA ELIMU YA MJINGA.
_________________
Na Kado Cool
Wakati muziki wa dansi ukiwa umeshika chati katikati mwa miaka ya 2000, kulitokea vita kali ya maneno kati ya Wanamuziki nyota wawili, Prince Mwinjuma Muumini na mwanamuziki mwenye sauti tamu ya kuvutia Waziri Sonyo.

Chanzo cha vita hiyo iliyofikia hatua mbaya ni kitendo cha mwanamuziki Waziri Sonyo kujiengua ndani ya bendi maarufu ya Double M Sound wana 'Mshike Mshike' iliyokuwa ikiongozwa na Prince Mwinjuma Muumini 'Kocha wa dunia'.

Malumbano yao yalifikia hatua mbaya mpaka wanamuziki wote wawili kuanza kutuhumiana kujihusisha na vitendo vya Ushoga huku kila mmoja akimpiga dongo mwenzie kuwa na tabia hiyo ovu isiyofaa kwenye jamii.

Wakati Muumini akimpiga vijembe Waziri Sonyo kuwa ni shoga kutokana tabia za kupenda kusuka nywele, Sonyo naye alidai Muumini ndiye mwenye tabia hizo kwani alipokuwa jijini Mombasa nchini Kenya aliwahi kusikia akituhumiwa kujihusisha na vitendo hivyo.

Hatua hiyo ilipelekea gazeti maarufu la Udaku la wakati huo liitwalo 'Ijumaa' kuingilia kati kuwapatanisha wanamuziki hao lakini kila mmoja aliendelea kumtuhumu mwenzie Ushoga, hivyo suluhu iliyoamuliwa wote wawili kwenda hospitali ya Taifa Muhimbili kufanyiwa vipimo ili kuthibitisha ukweli huo dhidi yao.

Wakati hayo yakiendelea kutokea, aliyekuwa Mkurugenzi wa bendi ya TOT, Marehemu Kapteni John Damian Komba akautumia mwanya huo kuwapeleka wanamuziki wa bendi yake Chuo cha Sanaa Bagamoyo ili kusoma Kozi fupi ya muziki huo.

Hatua hiyo ya ghafla ilipelekea Waandishi wa habari kumuhoji Kapteni Komba, kwanini ameamua kuwapeleka wanamuziki wa bendi yake ya TOT kupata Kozi fupi ya muziki wakati huu na si wakati mwingine.?

Kapteni Komba aliwajibu waandishi kuwa hapendi wanamuziki wake waje wapate aibu inayowakumba sasa wanamuziki Sonyo na Muumini kwa sababu yote yanayowatokea sasa ni tabia ya kubweteka na kutoongeza elimu ya taaluma yao.

Lilikuwa ni jibu lililoonekana kumkera zaidi mwanamuziki Muumini, kwani kama ilivyo kawaida yake ya kutopenda kubaki kimya pale anapohisi kushambuliwa, akaamua kurusha kombola kwa Kapteni Komba kuhusu tuhuma za 'kubweteka' kimuziki.

Muumini alimshambulia Kapteni Komba na bendi yake ya TOT kuwa, kilichowapeleka TOT Bagamoyo si kujifunza muziki, bali kujifunza Ushirikina kwenye muziki, maelezo yaliyoonekana kuwastaajabisha wengi.

Akisisitiza maelezo hayo bila hofu, Muumin alisema kuwa Bagamoyo ni kwao na anazijua kona zote, hivyo tayari anayo taarifa ya wanamuziki hao kupiga kambi kwa Mganga fulani kwa miezi kadhaa ili kufundishwa mambo ya Ushirikina kupitia muziki.

Baada ya bendi ya TOT kumaliza Kozi yao fupi chuoni hapo na wanamuziki wote kuweza kutunukiwa vyeti, bendi hiyo ikaamua kuboresha jina lao kwa kuongeza neno 'Plus' mbele ya TOT na kuanza kutambulika rasmi kama TOT Plus badala ya TOT Band kama ilivyokuwa mwanzo.

Wakati Muumini akiendelea kutamba na vijembe vyake kwa bendi ya TOT Plus kuwa wameenda kujifunza uchawi badala ya muziki, Kiongozi wa TOT Plus, Jenerali Banza Stone 'Mwalimu wa Walimu' akaamua kumjibu Muumini kupitia wimbo badala kuongea na vyombo vya habari kama Muumini anavyofanya.

Banza akakaa chini na kuandika kibao cha 'Elimu ya Mjinga' huku akionekana kumpiga madongo kisawasawa Muumini ndani ya kibao hicho kuwa "ikiwa anaona elimu ni ghali, basi aendelee tu kujaribu ujinga wake wa kuitukana TOT" aone kama utamsaidia.

[emoji443][emoji445][emoji445][emoji445][emoji445][emoji445][emoji445][emoji445]

Ni usemi wa siku nyingi, mamaa..
Na leo hii nakubali miye, ooh ooh
Elimu ya Mjinga ni Majungu..
Elimu ya Mjinga ni Majungu...
Ni Bora ukose Mali, Upate Akili..
Kwani Elimu ni Bahari na Haina mwisho... (X2)

Majungu si Mtaji
Useme ufanye Utajirike..
Majungu si Biashara
Useme uuze Inunuliwe..
Ikiwa unaona elimu ni ghali
Basi jaribu, Ujinga aaah.. (X2)

Mjinga upenda Majivuno..
Upenda Majisifu..
Asichokijua.. Hujifanya anajua..
Mazuri ya kwake..
Mabaya ya wenzake..
Anaweza akateketeza...
Misingi na Malengo..
Ya Jamii... Yoyote eeeh..!!

[emoji443][emoji445][emoji445][emoji445][emoji445][emoji445][emoji445][emoji445]

Lilikuwa ni shuti kali mno ambalo lilimshinda kabisa Prince Muumin Mwinjuma 'Mwana Buguza' na kuzama nyavuni, hivyo kumaliza kabisa vita vya maneno vilivyokuwa kati yake kupitia bendi anayoimiliki ya Double M Sound Wana 'Mshike Mshike' na TOT Plus ya Kamarade Banza Stone

'Elimu ya Mjinga' ikawa Hit Song bora kabisa mpaka sasa kupitia muziki wa dansi. Inaelezwa kuwa wimbo huu ndiyo wimbo bora kabisa wa muda wote wa mwanamuziki Banza Stone pamoja na kuwa na tungo nyingi mahiri.

Solo ya Elly Chinyama, mtoto wa kiongozi wa zamani "Mchumi" wa bendi ya Ochestra Maquis Original marehemu Chinyama Chiyaza (Chi-Chi) kwangu binafsi ndiyo solo Bora zaidi kupigwa naye katika nyimbo zake nyingi alizoshiriki.

Elliiiiiiii....
Chinyamaaaaa..
Le Side Babaaa....
Mwana Sinzaa... [emoji445][emoji445][emoji445]
Mfunulieeee..
Mfunulieeee..
Mfunulieeee.. Aone.!![emoji445][emoji445][emoji445]

Achana kabisa na hii kitu aisee.! [emoji4]
Endelea kupumzika kwa amani Jenerali Ramadhani Masanja Banza Stone, Mwalimu wa Walimu.

Mungu akupe umri mrefu na afya njema, Prince Muumin Mwinjuma Kocha wa Dunia. Hakika mlijua kuupaisha muziki wa dansi kupitia tungo zenu mahiri.

Acha tuendelee kutoa ushuhuda wa yale tuliyoyashuhudia kwa macho na masikio yetu enzi za muziki wa dansi ulipokuwa mahiri miaka ya 2000
 
Alikuwa msanii wa maigizo mkongwe hapa tanzania
Marehemu FUNDI SAIDI jina la usanii aliitwa KIPARA baadaye MZEE KIPARA
ALIZALIWA NZEGA MKOA WA TABORA mwaka 1922
Na alifariki 11-1-2012 akiwa na miaka 89
Alianza kuigiza miaka 60 kwenye michezo ya radio akiwa sehemu ya ukorofi na ubabe
Ameigiza michezo mingi sana
Vile vile alicheza kwenye magazeti ya FILM TANZANIA chini ya mwandishi mkongwe marehemu Faraji Katalambula
Vile vile alicheza kwenye sinema ya fimbo ya mnyonge maarufu kama yombayomba kwenye miaka 70
Kwenye mwaka 1990 alijiunga na kikundi cha splendid cha ilala bungoni ambacho michezo yake ilirushwa na chanel ya CTN
MWAKA 1999 yeye na wakongwe wenzake
Mzee pwagu,mama ambiliki,zena dilip na Russia makuka walijiunga na kaole
Amecheza tamthiliya nyingi sana akiwa na kaole
Vile vile amecheza movie nyingi sana za bongo movie
Mzee kipara aliugua sana
Alifariki 11-1-2012 na kuzikwa 12-1-2012 pale kigogo
 
Jagwa Music "Dege la Jeshi"

Moja kati ya Kundi Bora La Muziki Wa miondoko ya Mnanda, Likiwa na maskani yake Mwananyamala Kisiwani kama kumbukumbu zangu zipo sawa na Ngome yao kubwa ni Pale kwenye ukumbi wa CCM Mwinjuma (Sikiliza ule wimbo Wa Kifo Cha Oskar Mkoba aliyekatwakatwa mapanga kama mnyama).
Hapa Mnanda Ulipigwa Ukapigika.

Pichani ni Moja ya Album Yao iliyotikisa Enzi hizo "TUMECHOKA HOI" ikiwa na Nyimbo zifuatazo Kama pesa ni zako, Asha, UKIMWI Hauna Dawa, Usiwadharau Wazazi, Mapenzi pamoja na wimbo uliobeba jina la Album wa Tumechoka Hoi

Album hii imefuata baada ya Ile Album ya LIWALO NA LIWE [emoji91][emoji91]

[emoji119] Baba J (R.I.P) Akiwa Muimbaji Kiongozi,
Kwenye Kinanda Yupo Mtoto wa Tabora Kamongo Manjalino akisaidiana na Ally Tasha (Tasha Boy)
Msondo na Dumbak wapo Mazinge pamoja na Hossein Magoha na wengineo

Manager Bwana Jolijo
NB: Hawa jamaa hawana wimbo ambao hauna Ujumbe [emoji3][emoji3]
 
CHUCHU SOUND NDANI YA JIJI LA DAR ES SALAAM.
Kado Cool
Jiji la Dar es salaam lilipata kukumbwa na Joto kali la muziki wenye mahadhi ya 'Mduara' mwanzoni mwa miaka ya 2000 pale bendi kali ya Chuchu Sound ilipokuwa ikitoa burudani ya muziki kupitia kumbi mbalimbali za burudani.

Chuchu Sound maarufu kama wazee wa 'Kuzima Moto ndani ya Jiji', watakumbukwa na wadau wengi wa muziki wa dansi kutokana na namna walivyochochea burudani ya muziki wa 'Mduara', muziki ulioonekana kupendwa na vijana wengi wa Jiji la Dar.

Bendi hii iliyoanzishwa na Mfanyabiashara, Yusuph Alley Chuchu (RIP), ilileta ushindani kubwa kwa bendi nyingi za muziki wa dansi nchini zikizokuwa zimeshika kasi jijini Dar es salaam mwanzoni mwa miaka hiyo ya 2000.

Pamoja na kuwepo bendi kadhaa zilizokuwa zikipiga vibao vya miondoko ya 'Mduara' kama The Kilimanjaro Band (Njenje), InAfrika Band (Mgema), Beta Musica (Bana Beta), Chuchu Sound walikuwa ndiyo wakali zaidi katika miondoko hiyo.

Chuchu ambayo maskani yake ilikuwa maeneo ya Mwananyamala Komakoma, inakumbukwa na wengi kutokana na kujaza kumbi nyingi za burudani pale inapotumbuiza, hali iliyopelekea kuwa gumzo kubwa jijini Dar.

Ukumbi wa Vatican City uliopo Sinza jijini Dar, ilikuwa ndiyo 'Ngome Kuu' ya bendi hiyo, pale ilipokuwa ikitoa burudani kila mwishoni mwa wiki na kufanya wapenzi wengi "kuduarika" kwa raha na burudani kiasi ambacho ni vigumu kupimika.

Sauti tamu za waimbaji Omari Mkali, marehemu Waziri Sonyo, Joniko 'Flower' Maua, marehemu Ladislaus Manyama, na Rapa asiyepimika na kusahaulika kirahisi, marehemu Mao Santiago ziliifanya Chuchu kuwa Chuchu Sound kweli.

Albamu zao tatu, ya kwanza ikiitwa "Kusema sema", ya pili ikipewa jina la "Hodi Hodi" na ya Tatu ikiitwa "Mkataa Pema" zinakumbukwa na wengi kutokana na namna vilivyoipa bendi hiyo mafanikio makubwa.

Vibao kadhaa kama 'Kusema sema', 'Sitishiki', 'Usione vyaelea', 'Marafiki', na vinginevyo vingi, vilitosha kabisa kuifanya bendi hiyo kuzima moto wa burudani uliokuwa ukiwaka kupitia bendi nyingine za muziki wa dansi.

Hapa ndipo bendi ya Chuchu ilipobatizwa jina la "The Fire Brigadiers" (Wazee wa Zimamoto) na kupelekea bendi nyingi kulazimika kufanya 'Mduara' japo kidogo, ili kukidhi kiu za mashabiki wao walioanza kuielewa mizuka ya Chuchu.

Wengi tunakumbuka gitaa mahiri la Solo la King Giovanni (RIP), Rhythm gitaa ikipigwa na George Choka sambamba na Bass gitaa likipigwa na Mbwana Mponda, hivyo kukamilisha safu nzima ya wapiga 'Mipini' wa kikosi hicho.

Kwa upande wa Kinanda, Ababuu Mwana Zanzibar alikuwa mahiri mno kupapasa keyboard, Tumba zilijuta kumfahamu Mohamed Kachumbari huku marehemu Gabby Katanga 'Yero Masai' na Mohamed 'Muddy' Terminator (RIP) wakizicharaza kwa ufundi mkubwa drums.

Kama Waswahili wasemavyo kuwa "Ivumayo Haidumu", msemo huu ukajitokeza kwenye bendi ya Chuchu Sound baada ya wanamuziki wake kuanza kuchomoka mmoja hadi mwingine kwa sababu mbalimbali zikiwemo za kimaslahi.

Ndoano ya Kapteni John Komba, Mkurugenzi wa TOT ikawanasa wanamuziki Waziri Sonyo, na Gabby Katanga kuwafanya kuwa sehemu ya kikosi cha TOT na hivyo jinamizi la mikosi kuanza kuiandama Chuchu Sound.

Wakati Chuchu wakiendelea kujiuliza, mwimbaji Omari Mkali naye akajiondoa Chuchu na kwenda kuanzisha bendi ya Pamo Sound kitendo kilichoonekana dhairi kuifanya bendi hiyo kuchungulia kaburi.

Msumari wa mwisho ukapigiliwa na bendi ya Bambino Sound iliyokuwa ikiongozwa Banza Stone, baada ya kumnyakua 'keyboardist' Ababuu Mwana Zanzibar na Muddy Terminator na hivyo Chuchu Sound ikawa si Chuchu ile tena.

Tuna mengi ya kuzungumza yasiyokwisha pale tutakapoamua kuizungumzia Bendi ya Chuchu Sound tusimalize, lakini kwa leo itoshe tu kusema bendi hii ni moja kati ya bendi zitakazokumbukwa na mashabiki wengi.

Pamoja na maisha yake mafupi kwenye ulimwengu wa muziki wa dansi nchini, Chuchu Sound ilifanikiwa kuleta mapinduzi makubwa kupitia muziki wa 'Mduara'.

Hii imejionesha dhahiri baada ya bendi hiyo kufa kwa mtindo huo kushindwa kumpata mwingine aliyoumudu ikilinganishwa na enzi za Chuchu wazee wa "Zimamoto ndani ya Jiji".
 
Kusema sema,hodi hodi na marafiki ni mipini ninayoendelea kuburudika kwayo mpaka sasa.
 
1923 Jaray streamliner. The first car with covered headlights, a four seater and an airfoil on.
 
Cookies are required to use this site. You must accept them to continue using the site. Learn more…