Habari za kawaida
Posted Date::9/26/2007
Vigogo zaidi wajitokeza kwenda kortini kupinga kashfa ya ufisadi
Na John Stephen
KATIBU Mkuu wa Wizara ya Fedha, Gray Mgonja, jana alijitokeza na kusema kuwa hatajiuzulu wadhifa wake na kwamba anakusudia kumshtaki mahakamani Dk Willibrod Slaa na wenzake kwa kutoa tuhuma za uongo dhidi yake.
Akijibu tuhuma hizo katika mkutano wake na waandishi wa habari uliofanyika katika wizara hiyo, Mgonja alisema kutokana na tuhuma hizo atamshtaki Dk Slaa na wenzake kwa sababu walitoa shutuma za uongo ambazo zimemchafulia jina lake.
"Shutuma za Slaa na wenzake sio za kweli, bali ni uzushi na upotoshaji wa ukweli uliolenga kuchafua jina langu na kunishushia hadhi mbele ya umma wa Watanzania na watu wa nje, wakiwamo washirika wa Tanzania katika maendeleo ya nchi yetu," alisema Mgonja.
"Kwa kuzingatia uzito wa tuhuma zilizotolewa kwa nia mbaya ya kunipaka matope na hasa nikizingatia uadilifu wangu wa miaka 33 bila kuwa na shutuma au kashfa ya aina yoyote, ili haki itendeke nimeamua kutumia mkondo wa sheria kwa kufungua kesi mahakamani dhidi ya Dk Slaa, Gazeti la Mwana Halisi na Kiwanda cha Printech kilichochapisha matoleo hayo," alisema.
Katibu huyo alipoulizwa ni lini atafungua kesi hiyo, alisema ataifungua muda wowote kuanzia sasa baada ya kuwasiliana na wanasheria wake.
"Nitafungua kesi mapema iwezekanavyo na si lazima mjue kampuni itakayosimamia kesi yangu na wala siwezi kutaja kiasi cha fidia nitakachodai, nitasema mahakamani fidia nitakayodai," alisema Mgonja.
Pia alisema amechelewa kujibu tuhuma hizo kwa sababu alichelewa kupata nakala halisi ya tuhuma za ufisadi dhidi yake na kwamba mara baada ya kupata amejibu.
Akizungumzia kama kuna athari zilizojitokeza baada ya kuhusishwa katika ufisadi akiwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha, Mgonja alisema tuhuma hizo, hazijasababisha athari zozote za kukwamisha misaada kutoka kwa wafadhili.
Pia alisema hazungumzii ufisadi kutokana na shinikizo la mabalozi wa nje na kwamba yaliyosemwa na mabalozi ni maoni yao na kwamba tuhuma dhidi yake zingelikuwa za kweli basi Serikali ingelipata athari kubwa kutoka kwa wafadhili.
Juzi Jumuiya ya Umoja wa Ulaya (EU), iliitaka Serikali kutoa ufafanuzi wa kina kuhusu tuhuma za ufisadi dhidi ya viongozi wa Serikali na wafanyabiashara nchini ili kurejesha imani kwa wafadhili na wananchi.
Katika hatua nyingine, Mgonja alisema amejibu tuhuma hizo kama Gray Mgonja na wala si kwa niaba ya Serikali.
Hata hivyo, barua ya majibu ya shutuma hizo aliyoisambaza kwa vyombo vya habari, ilikuwa na nembo ya serikali na kusainiwa na yeye kama Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha.
Septemba 15, mwaka huu, Mbunge wa Karatu (Chadema), Dk. Slaa aliwatuhumu vigogo kumi na moja, wengi wao wakiwa ni viongozi wa serikali ya awamu ya nne kwamba walihusika na ubadhirifu wa mabilioni ya fedha za umma.
My take:
Hivi hawa watu kama hawataki kuzungumza kama maofisa wa serikali kwanini wasiwaite waandishi majumbani kwao, au kwenye hoteli binafsi. Tuhuma dhidi yao si kama watu binafsi bali kama maafisa wa serikali. HIvyo wanapojibu tuhuma hizo hata waseme mara ngapi kuwa wanafanya hivyo "kama wao" ukweli ni kuwa wanajibu tuhuma kama maafisa wa serikali. Na huyo aliyewaagiza wasema vinginevyo kawadanganya.